Tuesday, September 27, 2011

Makamu Wa Rais Dr Bilal Atoa Mhadhara Chuo Kikuu Cha Uppsala, Sweden!!!!

Pichani: Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohammed Gharib Bilal, akizungumza na Watanzania, waishio nchini Sweden wakati alipokutana nao katika mkutano Septemba 25, katika Ukumbi wa Hoteli ya Gillet Clarion iliyopo Uppsala Sweden. Kushoto ni kiongozi wa Jumuiya ya Watanzania wa Sweden, Prof. Lodhi. Picha: Muhidin Sufian.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano Wa Tanzania Dkt. Mohammed Gharib Bilal ametoa mhadhara kuhusu changamoto za kisayansi katika maadhimisho ya miaka 50 ya Idara ya Sayansi za Kimataifa kwa kifupi ISP ya Chuo Kikuu cha Uppsala kilichopo Uswidi ambapo amefafanua kuwa, mchango wa wanasayansi kutoka katika chuo hiki una manufaa makubwa katika kukuza teknolojia katika sayansi kwa nchi za Afrika.
Makamu wa Rais ambaye alikuwa mhadhiri wa somo la Fizikia katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kabla ya kuingia katika siasa, amealikwa na wanasayansi wa kariba yake katika maadhimisho haya yaliyo na lengo la kutanua uwanda wa tafiti katika nchi za Afrika na hasa Tanzania, ambayo kwa sasa imeanzisha chuo kikuu cha Sayansi na Teknolojia cha Nelson Mandela kilichopo Arusha.
Katika ziara hii ambayo Makamu wa Rais ameambatana na Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia Profesa Makame Mnyaa Mbarawa, Waziri wa nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira) Dkt. Telezya Huvisa, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mahadhi Juma Maalim pamoja na Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia cha Nelson Mandela Profesa Burton Mwamilwa.
Ujumbe wa Makamu wa Rais ulifika hapa na kupata nafasi ya kuzungumza na Watanzania waliopo Uppsala ambao wengi walitaka kujua kama Tanzania imejipanga vema kukabiliana na tatizo la umeme nchini. Makamu wa Rais ambaye katika ziara hii amekuwa akikutana na wanasayansi mbalimbali wa Sweden na hasa waliobobea katika sekta ya nishati aliwaeleza Watanzania waliokuwa katika mkutano naye kuwa; kama taifa tuna kila sababu ya kukubali kuwa tulifanya makosa huko nyuma kwa kutotambua utanuaji wa vyanzo vya umeme wa uhakika hali inayotuumiza sasa lakini pia akawaambia kuwa serikali imejipanga vema kuhakikisha kuwa tatizo la umeme linapata tiba katika kipindi kifupi na pia kuwa na umeme wa uhakika katika miaka miwili ijayo.
Maeneo makubwa ambayo Makamu wa Rais amekuwa akiwasikiliza kwa ukaribu wanasayansi wa Uppsala na Sweden ni kuhusu vyanzo mbalimbali vya uzalishaji wa umeme vikiwemo vile vya upepo na maji ya bahari huku pia ikiwa Tanzania imeshasaini mkataba wa uzalishaji wa umeme wa makaa yam awe na kampuni ya kutoka China, mkataba uliosainiwa wiki mbili zilizopita katika ya NDC na kampuni ya China ambazo zitashirikiana katika miradi mikubwa katika ukanda wa Mtwara.
Eneo jingine ambalo Makamu wa Rais amekuja kulihamasisha ni juu ya uhusiano wa chuo hiki kikongwe katika uwanja wa Sayansi na namna chuo hiki kitakavyozidisha ushirikiano wake katika kusomesha wataalamu wa Tanzania katika ngazi za Shahada za Uzamivu na mchango mkubwa ukiwa kukipatia uwezo Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia cha Nelson Mandela kilichopo Arusha.
Katika ziara hii ya kitaaluma aliyoalikwa Makamu wa Rais inayochukua siku mbili, Makamu wa Rais pia atakutana na Waziri wa Mambo ya Jamii wa Uswidi Ulf Kristersson na Waziri wa Mahusiano na Maendeleo Gunilla Carlsson. Katika ratiba hiyo pia Makamu wa Rais atatembelea Taasisi ya Mazingira ya Uswidi sambamba na kuzungumzia mafanikio ya Kilimo Kwanza kwa wadau wa maendeleo wa Uswidi.

4 comments:

emu-three said...

Tupo pamoa ndugu yangu, hata kwa shida shida, hivyo hivyo...! Twashukuru kwa taarifa hii!

ray njau said...

Nalazimika kuvunja ukimya na kupiga hodi kibarazani;wadau kwa nini hamsemi karibu!!
Wakati wa masomo yangu ya shule ya upili nakumbuka nilivyofanya vema kwenye somo la fizikia na hata siku nilipohudhuria siku ya Kiswahili pale Msimbazi Center na Mwalimu Omary Kiputiputi akaja na somo la Fizikia akiwa na wanafunzi wa shule ya sekondari ya Juu -Jitegemee chini ya mada ya mwendo aliniumbusha mbali sana japo kwa fizikia imehama kichwani.
Mheshimiwa makamu wetu wa Rais ni mwanzuoni mahiri na makini katika tasnia ya fizikia na ziara yake huko Sweden ni yenye manufaa kwa jamii yetu.
Tanzania ikiwa inapita kwenye shinikizo la mgawo wa umeme nahisi huu ni wakati ufaao wa kuwekeza katika uzalishaji umeme kupitia mawimbi ya bahari.Wadau naomba kuwasilisha hoja.

sam mbogo said...

Yasinta, nasubiri kukutia machoni katika ujio huu wa makamu wa rais,au wewe mikutano kama hii huipendi,mwanamke jitokeze waweza kuambulia chochote,penye wengi hapaharibiki neno. nimawazo yangu tu!! Kaka S.

Yasinta Ngonyani said...

em3 asante kwa mchango wako-

Raynjau! Nawe karibu tena na tena.

Kaka S. Bahati mbaya hutaiona picha yangu katika ziara hii ya makamu wa rais wetu kwani nilizidiwa na kubabe maboxi:-)