Wednesday, April 30, 2014

TUMALIZA MWEZI HUU WA NNE NA MOROGORO JAZZ BAND- DAR ES SALAAM...


MWEZI NDO UMEISHA NA KESHO TWAANZA MWEZI MPYA NA NI NI SIKUKUU YA WAFANYAKAZI MEI MOSI...TUPO PAMOJA....

Tuesday, April 29, 2014

JIONI NJEMA KWA WOTE!

Nimekaa hapa na mara naona natumiwa hii picha ya chakula kutoka kwa rafiki akinitamanisha...nami nikaona nisitamani peke yangu...

KATIKA MAISHA KILA KITU NI KUJIFUNZA!!

UJUMBE WA LEO:- Kitu muhimu katika maisha ni kujifunza jinsi ya kupenda/upendo, na kukaribisha/kuukaribisha ndani yako.

Monday, April 28, 2014

KUFUJWA KWENYE NDOA NI NINI?

Ni wiki nyingine na Jumatatu nyingine tena ya mwisho kwa mwizi huu wa nne! Nimeamka nikiwa na mawazo mawazo basi nikachukua kitabu hiki na kusoma. Kitabu chenyewe kinaitwa MAPENZI KUCHIPUA NA KUNYAUKA. Kilichoandikwa na Munga Tahenan... nikafananisha na wimbo ule wa Remmy Ongala usemao nilidhani nimepata kumbe nimepatikana.... bahati mbaya sijaupata wimbo wenyewe....Habari yenyewe inasomeka hivi:- Karibuni tujadili pamoja.

Ifuatayo ni habari ya mwanamke ambaye aliwahi kuja kwangu kwa ushauri kuhusu ndoa yake: Mama Kotilda Mkataha aliolewa mwaka 1980 na mume msomi aliyekuwa na wadhifa mkubwa kwenye taasisi moja ya fedha ya serikali.

Ndoa hii ilifungwa kwa sababu, Kotlida hakuwa na njia, lakini anasema, tangu wakiwa kwenye uchumba, alikuwa tayari na wasiwasi kama ndoa yao ingekuwa ni ya amani. Anasema, wakati bado wachumba, huyo bwana aliwahi kumpiga kibao kwenye kituo cha UDA kwa kosa la kuchelewa kufika kituoni kama walivyokuwa wamekubaliana.
Ndoa ilikuwa ni ya mateso makubwa hata kabla haijafungwa. Mwezi mmoja baada ya ndoa, Mume alimachisha mkewe kazi kwa kwenda kufanya fujo ofisini kwa bosi wake kwa madai kuwa bosi huyo alikuwa na uhusiano na mkewe. Kotlida alianza kuishi kwa mashrti. Hakuna kutoka, hata kwenda kwa jirani bila kuomba ruhusu na kutoa maelezo marefu kwa nini aende huko.
Kusimangwa, kukosolewa, kuitwa mjinga na mbumbumbu, ikaanza kuwa sehemu ya maisha ya mama huyu, Hali iliendelea hivi na Kotlida akawa anajiambia, kuna siku hali itabadilika. Lakini. kwa bahati mbaya, hali haikubadilika. Wakati anakuja kwangu, alikuwa ameshaanza kuamini kwamba, huenda ni kweli alikuwa anastahili kutendewa vile na mumewe.
Huku ndiko tunakoita kufujwa. Mpenzi mmoja anapomuumiza mwingine kwa kauli zake au limwili, mara kwa mara, tunasema hapo kuna kufujana.
Mpenzi mmoja anapokuwa na mamlaka aliyojipa dhidi ya uhuru na haki ya mwenzake, tunasema hapo imekuwa kufujana. Mara nyingi, wanaofuja ni wanaume. Miongoni mwa matatizo ya ndoa ambayo mtu hashauriwi kuendelea kuyavumulia ni kufujwa. Ndani ya kufujwa kuna maumivu makubwa ya hisia na mwili.
Ni vizuri hata hivyo, nikasema kwamba, neno kufuja ni jinsi ya kuelezea hali hii, ambapo mtu mwingine angeweza kuita matesa katika ndoa, kuonewa katika ndoa au kutumia istilahi yoyote.

Swali langu:- Kwanini alipoona mambo yanazidi hakuondoka?

Saturday, April 26, 2014

HAYA NI MAPISHI YA JIONI YA JUMAMOSI YA LEO.......KARIBUNI KUJUMUIKA NASI!!

 Maandalizi:- Muhogo, Kabichi/Kebichi, kiazi kitamu, nyanya, binzari, chumvi, limau, kitunguu saumu,  kitunguu cha kawaida, tui la nazi, nyanya kopo,  maharagwe, mchele na mafuta.
 Wali wa nazi, Kachumbali, Maharagwe yaliyoungwa kitunguu, nyanya moja, chumvi na kijiko kimoja cha chai cha binzari, Kabichi/Kabichi iliyoungwa kwa nyanya na kitunguu, na mihogo na viazi vitamu vilivyokaangwa (chips)
Na hapa ndivyo ilivyoonekana sahani ya Kapulya jioni hii  na cha kuteremshia si kingine tena bali ni maji. KARIBUNI SANA...MIJA UPO...NA WENGINE WOTEEEE....TWAWATAKIENI JUMAMOSI NJEMA SANA WOTE!

Friday, April 25, 2014

TUMALIZA WIKI NA SIKU HII IJUMAA YA MWISHO KWA MWEZI HUU KWA NGOMA HII YA ASILI:- MGANDA


Ni Ngoma ya asili ya wanyasa ichezwayo na wanaume katika ukanda wa ziwa Nyasa... IJUMAA IWE NJEMA SANA PIA MWISHO WA JUMA KWA WOTE!!!

Thursday, April 24, 2014

VAZI LILILOPENDWA NA KAPULYA WIKI HII!!!

 
NI DADA YETU NURU
Vazi hili limenivutia sana, kwanza ni nzuri  kwa rangi na lilivyoshonwa na pia la heshima. Nimelipenda sana. ....PICHA  nimeipata hapa.
MUWA NA SIKU NJEMA.



Tuesday, April 22, 2014

HALI YA USAFIRI VIJIJINI:- HII HALI MPAKA LINI?

Nimekaa hapa nikiwaza jinsi enzi zileee nilipokuwa msichana mdogo. Shule moja, Kanisa moja, Hospital moja, gari moja la kijiji. Na hapo gari hilo lilikuwa likisafiri  kwa wiki mara moja, na  ujue likiondoka kurudi majaliwa. Hii picha haihusiani na maelezo yangu ila tu inafanana sana. Hasa nilipokuwa nikienda shule kutoka kijijini kwetu Kingoli na Litumbandyosi kwa kuchapa mwendo mpaka Peramiho kwa muda wa siku mbili.  Alan Ntimba kama unasoma hapa najua nawe unakumbuka sana safari zetu za kwenda shule. Alan Ntimba ni rafiki yangu tulimaliza shule ya msingi pamoja.  Kama kuna mtu anajua habari zake TAFADHALI  nijuze au wewe mwenyewe Alan. Tulikuwa tukipata gari ambaloi  limejaa kiasi hicho bahati sana. Juzi tu nilikuwa nikienda kumsalimia baba mkubwa Litumbandyosi usafiri ni bado  yaani barabara si  za kuridhisha. Je? hii itakuwa hivi mpaka lini? Au je ule Ujamaa bado upo? Maana naamini ilikuwa vile kwa vile tuliishi sana kijamaa....Mmmmm nawaza tu kwa sauti...
TUPO PAMOJA!

Monday, April 21, 2014

BUSTANI YETU:- LEO MAMBO YAMEPAMBA MOTO MTU NA JEMBE....

 Ukiwa na shamba lazima uwe na jembe leo ni kukatua/kulima maana mikono imewasha kweli ...Kutoka tu mazoezini nikazamia bustanini  kama muonavyo:-)
 Hapo sasa jembe linainuka kwa "nguvu" kweli
 Kama muonavyo ukilima/katua lazima kutoa nyasi...na hapo kwa mbali unaona ni vitunguu saumu nilipanda mwaka jana na sasa ni vikubwa.  ....leo tayari nimepanda/atika mchicha, mboga maboga, figiri, vitunguu,  pilipili hoho  pia nyanya.
Kapulya ana alikuwa na msitu kwa hiyo sasa ni mavuno ..kuni hizo ..ukitaka kununua karibu:-)
Hivi ndivyo ilivyokuwa  siku yangu kwa leo na sasa napumzika kidogo kwa kikombe cha CHAI.  Majembe yapo mengi karibuni:-)

NI JUMATATU YA PASAKA:- NA TUSALI SALA HII YA FAMILIA KWA PAMOJA...MAANA SISI SOTE NI FAMILIA MOJA!!!

Milango imefungwa, Ee Bwana,
Yule mtoto mchanga amelala,tunajisikia salama,
Tuna raha ya ndani, kwani tumeshiba,chakula kilikuwa kizuri,
Kinatuletea faraja.

Huu ndio wakati wa kukugeukia, mwishoni mwa siku hii ya leo,
Kama familia - familia yako, ambapo Kristu anaishi.

Mwa ajili yetu, kila mmoja wetu, Bwana, tunakushukuru. Kwa ajili ya siku hii ya leo.
Iliyojaa mambo mengi, mema na yasiyo mema sana. Kwa yote tunakushukuru.

Tunapoangalia nyuma, mara ngingine, ni rahisi kuona kwamba ingewezekana kuwa vizuri zaidi.
Hapa na pale, tumeshindwa kukupendeza, kwa neno la hasira. Na lile ambalo hatukulitimiza.

Tunasikitika, Bwana tusamehe. Kwani tunahitaji upendo wako. Tunakuhitaji wewe, ukae nasi usiku  huu wa leo. Ili kutulinda, kutubariki, kwani wewe ndiwe kuta za kweli na paa za nyumba  zetu.
Utubariki tulalapo, utujalie ndoto zetu ziwe za furaha. Na utujalie tuamke kesho tukiwa na uzima mpya tele, nguvu mpya, na starehe mpya. Ili tuweze kuishi tena siku nyingine. Amina.

Sunday, April 20, 2014

SALAMU ZA PASAKA KUTOKA KWA KAPULYA WENU!!

Nawatakieni Kheri na Baraka tele  za Mwenyezi Mungu kwa Ufufuko wa Mkombozi wetu Yesu Kristo. Yasinta na Familia.

Naona tumalizia na wimbo huu kwa kumshangilia bwana Yesu!!

AU TUENDELEE KIDOGO NA HUU PIA

PASAKA NJEMA !!

Thursday, April 17, 2014

LUGHA NA MISEMO YAKE....

Mara nyingi nimekuwa mtu wa kupenda misemo ya lugha mbalimbali...KAPULYA..na hapa chini ni baadhi ya misemo niliyonasa. KARIBU

1. Mara nyingi anayetaka  zaidi ni tajiri kuliko hata anavyofikiria mwenyewe.
2. Hatuwezi kufanya kitu kizuri kwa haraka, kwa vile hatujui uharaka huo unaweza ukachelewa
3. Ndoto zetu hutimizwa kama kuna nia ya kutimiza.
4. Kucheka /kicheko ni dawa isiyoleta madhara
5. Tunazaliwa kama nakala halisi lakini tunakufa kama nakala
6. Kama una haraka kila mara, unalazimika kutulia na kusubiri  mpaka pale moyo wako utakapokuambia nini kufanya.
7. Kwenye matunda kuna mti.
8. Unapo wapa wengine furaha, na ndipo furaha huongezeka kwako pia.
9. Mimi ni mimi, lakini mimi ni mmmoja tu. Siwezi kufanya kila kitu, lakini naweza kufanya kitu fulani.
10.Unaweza kuwaza mambo mengi, lakini fanya kitu kimoja  kimoja.
ALHAMIS KUU IWE NJEMA KWA WOTE!!!!!

Wednesday, April 16, 2014

HII SIJUI IMEKAAJE? AU NDIYO MAANDALIZI YA PASAKA????

KITOWEO CHA PASAKA
Inaonekana mnyama/mbuzi beberu anakula mgumo hapo lakini akina baba hawakubali kushindwa. Je wewe nawe umejiandaa PASAKA hii na beberu? au labda kondoo....mmmmhhh,,, msije kujisahau IJUMAA KUU   hakuna kula nyama!...
Ila mimi nikipata mlo kama huu nitaridhika kabisa kabisa..Ugali, mlenda/bamia na samaki.
NAWATAKIENI SIKU NJEMA PANAPO MAJALIWA TUTAONANA TENA:-) KAPULYA.

Tuesday, April 15, 2014

KWA NINI URAIA WA NCHI MBILI?

Mara nyingi sana nimekuwa nikujiuliza hili swali na pia nimekuwa nikisikia ya kwamba itatokea na kwamba swala hili lipo jikoni yaani BUNGENI lakini hakuna kinachotokea. Sijui kama kuna Mtanzania ambaye anapenda kuwa raia wa nchi nyingine kuliko nchi aliyozaliwa. Naamini kabisa kama Mtanzania  ya kwamba HAKUNA MTANZANIA ASIYE  IPENDA TANZANIA NCHI YETU. KATIKA TEMBEA TEMBEA NIMEKUTANA NA HII EBU UNGANA  NAMI  KUMSOMA KAKA Peter H.A. Owino KARIBUNI PIA NAKUMBUKA NILIWAHI KUANDIKA/KUDODOSA  BONYEZA http://ruhuwiko.blogspot.se/2009/10/uraia-wa-nchi-mbili.htmlKUJIKUMBUSHA
Tanzania na Diaspora.

Wakati watanzania tunaendelea kushuhudia kikao cha marekebishia ya Katiba kikiendelea napenda kujumuika na baadhi ya waliopata nafasi kuchangia kuhusu swala la uwezekano wa uraia wa nchi mbili (Due citizenship).
Katika ya nchi yetu tuipendayo kwa sasa haitambui uraia wa nchi mbili, kwa maana kuwa ukichukua uraia wa nchi nyingine unapoteza haki ya kama raia wa Tanzania, Swala hili linapaswa kuangaliwa kwa makini wakati huu wa marekebisho ya katiba, Kwa maoni yangu iwe ruksa kwa Mtanzania kuwa na uraia wa Tanzania hata kama utakuwa umechukua uraia wan chi nyingine, swala hili lisipoangaliwa makani ama likiangaliwa haraka haraka linaweza tafsiriwa kuwa watanzania hao wanatamaa ya kutaka huku na kule, si sahii kulitafsiri namna lightly namna hiyo, wengi wa watanzania waliokwenda kuishi kasha kuombauraia kuishi nchi nyingine hawakuwa na maana wa kuukana Utanzania na ukiangalia mpaka sasa hakuna anayetamba ama kuupondda U-Tanzania popote alipo.
Wengi wa watanzania wanaoishi ughaibuni ama nchi yoyote nje ya Tanzania na kupata uraia wa nchi hiyo bado wanajitambulisha kama watanzania, uraia wanaopewa ni haki ambayo wengi wao wameifanyia kazi muda mrefu sana katika nchi waliyopo, na ili kupata baadhi ya haki muhimu inabidi watambulike kama raia, kwa maana hiyo inabidi kuomba uraia wan chi waliyopo, lakini hii haimaanishi hata kidogo kuwa sasa Tanzania basi. Hata watanzania waliokuwa wakubwa kisiasa waliishi nje lakini inafika wakati wanarudi nyumbani kama kina Abrahaman Babu na Mzee Kambona nyumbani ni nyumbani huna ujanja.
Watanzania hao amabao baada ya kupata uraia wa nchi wanayoishi sasa wanatakiwa kuomba visa kuingia Tanzania, yani Mswahili wa Tarime au Ndanda sasa wanakuja Tanzania kama mgeni!, wanalipishwa kiingilio kwa dola katika mipaka yote ya Tanzania. Kuwapa haki katika nchi yao mama (Tanzania) ni swala muhimu katika kuendeleza Tanzania pia, maana yangu ni kuwa wengi wanafanya kazi nje ya nchi lakini mawazo yao ni Tanzania wengi ama wote wanandugu ambao bado wanawasiliana nao kila mara, katika kuwasiliana huko wengi wanawekeza Tanzania sababu ndio kwao na ndipo siku wakikata kauli wengi watarudishwa na kulazwa walipolala ndugu zao wengine.
Raia wengi tunajua ugumu wa Maisha yaliyopo Tanzania tuna wahitimu wengi ambao wanamaliza na kufaulu vizuri bila kupata ajira, wapo wenye bahati ambao humaliza na kuanza kazi moja kwa moja lakini wengi hawana bahati hiyo. Mtanzania ambaye amekwenda kujiendeleza nje analiona hili swala na anajua labda hayupo kwenye kundi la wenye bahati kwa maana kuwa atarudi nyumbani na hakuna ajira na wanaopata ajira wengi kama walimu wanaanzia mshahara wa shilingi 277,00=, kiasi ambacho ambacho ukijiuliza mwalimu huyu ambaye amepanga na kutumia public transport anafikaje mwisho wa mwezi hupati jibu, ukipata bahati unaweza anzia taasisi zinazolipa 750,000= kwa mwezi, lakini ni watanzania wangapi wanabahati hiyo?.
Nchi kama Uholanzi mshahara wa mwezi unaanzia Euro 1440 sawa Tsh 3,240,000 Norway wanaanzia euro 2000 na Uingereza ni zaidi ya hapo, kwa haraka haraka watu hawa wanaweza kuishi kwa amani huko walipo nabado wakasaidia ndugu zao ambao wapo Tanzania.
 
Nchi kama uingereza ukiwa raia una haki kuishi kwa kutegemea Serekali kwa chakula malazi ,matibabu yaani hata kama hufanyi kazi, kwa maana hiyo Mtanzania huyu akipata kazi na anaishi nchi ambayo kwa kawaida huwezi kujinunulia kiwanja na kujenga unless uwe Millionea siku zote atakuwa na mawazo ya kuja kuijenga nyumba yake nyumbani na ya kisasa kama anayoiona huko nje, na kwa vile anaishi nje basi hii nyumba yake wataishi watanzania ambao kama walivyo wengi wetu hawana uwezo wa kujenga kwa haraka na kwa mishahara halali. Tutakaporuhusu Mtanzania anayepata uraia nje kuendelea na uraia wake wa Tanzania kama atapenda basi ataendelea kulala na kuwaza Tanzania.
Mimi nimeishi nje ya Tanzania kwa muda sasa kwahiyo naelewa umuhimu wa kuendelea kuwa raia wa Tanzania, naelewa umuhimu wa siku moja kuja zikwa pale walipozikwa ndugu zangu.
Wajumbe wa Bunge wa katiba watumie busara katika kujadili hili swala bila kusahau kuwa watanzania wanaoishi je na wamepewa uraia huko wanapenda kuendelea kuwa watanzania, wajumbe watakuwa wametenda jema kuruhusu uraia wa nchi mbili hasa kwa watanzania waliobahatika kupata uraia wa nchi nyingine katika njia ya kutafuta maisha kwa ajili yao wenyewe na ndugu zao.
Sababu nchi nyingi wanazoishi Wazanzania nje ya Tanzania system yao ya kufanya kazi ni 100% kazi hivyo watanzania wengi wanajifunza na kunakili mifumo hiyo ili siku wakirudi nyumbani wawaambukize watanzania wenzao maana nchi nyingi za nje unaposema kazi unamaaninisha kazi na si kazi ya kuingia saa unayotaka na kusign na kuondoka, unakula kwa jasho lako kihalali na ukijituma unapata, Japo ni kidogo lakini watanzania walio nje wanaweza na wamekuwa wakichangia kihalali kidogo walicho nacho katika kuendeleza uchumi wa Tanzania wengi wakati wa mapumziko huja Tanzania na wengi wao hawaji mikono mitupo ama hawaji kutengemea ndugu za walioko Tanzania badala yake huja wamekamilika na vitu ambayo wengi huvituma bandarini na kulipia ushuru, siku wakiwa wanaondoka kurudi makazini wengi wao huondoka watupu na kuanza upya katika arakati za kukusanya ili akirudi tena Tanzania aendelee pale alipoachia mara ya mwisho.
Mtanzania anayeishi nje hana sehemu ya kuishi kwa furaha zaidi ya Tanzania, hana sehemu anayoishi kwa amani zaidi ya Tazania, Mtanzani huyu hana sehemu aliyo na marafiki wengi zaidi ya Tanzania, Mtanzania huyo ambaye wazazi na ndugu zake wote wako Tanzania leo anaadhibiwa kwa kitendo cha kwenda kutafuta kipato ambacho hakipereki popote bali Tanzania.
 
Miaka ya sabini ilikuwa inaeleweka pale alipoadhibiwa mtanzania aliyekwenda kusoma Urusi, Denmak, Hungary na akakataa kurudi, sababu tuliitaji wataalam wetu ambao hatukuwa nao wa kutosha na wengi wao waliperekwa na gharama za serekali, Zanzibar tulikuwa na chuo kimoja tu tena cha ualimu pekee na sasa kuna vyuo zaidi ya vitatu vikubwa,bara kulikuwa na
chuo kikuu kimoja tukilicho kuwa kinahitimisha wanafunzi 15 tu na sasa tunavyuo zaidi ya 30 wanaohitimu ni zaidi ya 110,000 kwa mwaka, kwa miaka hii wengi wako nje kwa gharama zao katika kutafuta kilicho bora kwa ajili ya watanzania wenzao na sasa akifanikiwa kupewa uraia na nchi husika ili aishi kwa amani na haki zote za kufanya kazi kusoma nk Tanzania inamwambia sasa hapa ni wewe ni mgeni ukija kumuona mama ama baba yako ama kuendeleza nyumba yako unayojenga kijijini kwenu kule Butiama basi lipa kiingilio (visa)!!.
Watanzania walioko nje hawako nje sababu hawaipendi Tanzania na anafikiria hiyo atakuwa anajidanganya, Tanzania iko miyoni mwetu na hata serikali ingeweza hata ingeruhusu tukatengeneza system ya kupiga kura wakati chaguzi kuu zinapowadia. Wawakilishi wa vyama vya siasa katika bunge hili lililopewa heshima ya kurekebisha katiba tunawaomba kuingiza swala hili katka katiba mpya, Mheshimiwa Membe amekuwa akisikiliza na kwa makini kilio hiki cha watanzania walioko nje, pia mheshimiwa Kikwete amekuwa akikumbana na hili ombi kila wakati akikutana na watanzania waishio nje, katika kikao chake cha mwisho na watanzania Uingereza pale Wembley Mheshimiwa Raisi alisema swala hili limeingizwa kwenye rasimu kwahiyo liko ndani ya bunge kujadiliwa, napenda kumpongeza Mh Dr Kikwete kwa kutambua kilio hicho mpaka kumteua Singo kuwakilisha diaspora (thank you Mr President) katika kikao hicho.
Lakini sababu kwa walio wengi swala hili si muhimu kwao huko bungeni tunaomba mfungue macho na kulipa umuhimu. mnapojadili mjue mnamuongelea Masatu, Juma, Asha, Owino, Yasunta na wengi ambao huko waliko japo wamepewa uraia lakini wanahesabiwa kama wageni hawatakubalika kama wenyeji unless wameishi zaidi ya miaka 30, mjue mnamjadili mtu ambaye anakuja Tanzania sio kuchuma ama kujifunza Kiswahili na mila za Tanzania la hasha mnajadili maisha ya mtu amabaye amewaachia watanzania wenzake nafasi za ajira Dar , Mwanza ama Ndada na kwenda kutafuta huko nje ya nchi na anachopata japo kidogo lakini anakula na wakwao –WA-TANZANIA.
 
Mungu bariki Tanzania yetu.
Peter H.A. Owino
Rorya
Tanzania.
Live in UK
Nami nasema tena na tena MUNGU IBARIKI SANA TANZANIA YETU. PAMOJA DAIMA!!!

Monday, April 14, 2014

TUANZE WIKI NA MDADA HUYU NA MIKANDA YAKE /HILI LILIKUWA VAZI LANGU LA JANA JUMAPILI !!

Kwa kukumbuka vizuri ebu fungua hapa kuona huyu mdada/kapulya anayopenda mikando tangu enzi hizo za ujana wake:-) http://ruhuwiko.blogspot.se/2013/02/mwanadada-na-mikanda-yakemwanamtindo-wa.htmlKama umeangalia vizuri katika hiyo picha ya juu ...Je? Umegundua kitu gani kinakosekana?
NAWATAKIENI MWANZO MWEMA WA JUMA/JUMATATU

Sunday, April 13, 2014

MVUA NI NZURI LAKINI SASA JIJI LA DAR ER SALAAM LIMECHAFUKA KABISAPIA MIKOANI/MAFURIKO MAKUBWA

 Hapa ni ni Dar na hilo ni basi la shule linavyozolewa na maji ya mvua
Halafu sasa sio Jijini tu hata huko Mikoani nako si kuzuri angalia hapa kwa kujikomboa ameamua kukwea mti...Mungu ibariki Tanzania

NAWATAKIENI WOTEJUMAPILI HII YA MATAWI IWE NJEMA !!!

Mwenyezi Mungu, wewe ni kimbilio langu na ngome yangu. Mungu wangu ninayekutumaini. Zab: 91:2.
Mnajua ya kwamba bado kama wiki moja tu na itakuwa PASAKA....BWANA WETU YESY KRISTU ATAKUWA AMEFUFUKA.  Mpaka hapo TUWE NA AMANI PIA UPENDO. JUMAPILI YA MATAWI IWE NJEMA NDUGU ZANGUNI.

Saturday, April 12, 2014

MAUA MAZURI YAPENDEZA...NAPENDA SANA MAUA NIMEPATA HILI KAMA ZAWADI NA....:-)

NIKAONA NILIIMBIE NA HUU WIMBO TULIOKUWA TUKIIMBA ENZI ZILEEEE je nawe unakumbuka kama hukumbuki basi ni hivi kuimba!!!
1. Maua mazuri yapendeza x 2
    Ukiyatazama utachekelea
    Hakuna mmoja asiyeyapenda x 2

Kwa kutaka kuimba bila kukosea basi fuata hii hapa:-)
 Au pia tusiwasahau na watoto, si mnakumbuka na huu wimbo  haya wazazi waimbieni watoto wenu  kwa raha zote ni kama vile umsomeapo/msimuliapo hadithi :-
2.Mtoto msafi apendeza x 2
Ukimtazama utachekelea
Hakuna mmoja asiyependeza x 2
 
3. Mtoto mtii apendeza x 2
Ukimtazama utachekelea
Hakuna mmoja asiyempenda x 2

JUMAMOSI IWE YENYE UPENDO, FURAHA  JUU YA KICHEKO. SI MNAJUA KUCHEKA/KICHEKO NI DAWA ISIYOLETA MADHARA.
KUMBUKENI TUPO PAMOJA!!


Friday, April 11, 2014

MAMBO YA BUSTANI YANANUKIA NUKIA :-) TUMALIZE JIONI HII YA LEO KIHIVI UKULIMA!!!

Hii ni ile BUSTANI yetu, nilikuwa kimyaaaa, nilikuwa natifuatifua. Karibuni tu kutakuwa na zile mbogamboga na viungo. Hivyo vionekanavyo hapo ni vitunguu saumu. Nilipata ushauri kuwa ukipata mwezi wa kumi mapema mwanzoni mwa mwaka au kama baridi imepungua huchipua kwa haraka:-) Nimekwisha atika atika baadhi ya mbegu ndani kwenye makopo kama kawaida:-) ZAIDI MAENDELEO YA BUSTANI YATAKUJA....JIONI NJEMA NDUGU ZANGU!!

NAPENDA KWATAKIENI MWISHO WA JUMA KWA USEMI HUU KWENYE KANGA HII!!

Muwe na mwisho wa juma mwema sana wote. Pia kama ulimkosea rafiki, jirani, ndugu, au mtu yoyote sasa ndiyo wakati mwafaka wa kumsamehe maana wikiendi ijayo ni PASAKA. IJUMAA NJEMA!!!

Wednesday, April 9, 2014

HIVI HII IMEKAJE HAPA ...EBU SOMA! ETI NI KWELI HII au NDIYO MISEMO TU??

Hii nimetumiwa nimejiuliza mwenyewe kama kweli na jibu lake likabaki ni kuguna tu na mwisho nikaona niweke hapa labda naweza kupata jibu...Msaada jamani hapa!!!
-------------------------------------------------------------------------------------------------------
Ukitaka majungu oa Mhaya,
Ukitaka mapenzi ya ujanja ujanja na uwizi wa mfukoni oa Mchaga,
Ukitaka uchawi oa Mfipa,
Ukitaka maneno oa Mzenji,
Ukitaka mapishi oa Mtanga,
Ukitaka mume mwenza oa Mzaramo,
Ukiwa na shamba oa Msukuma,
Ukitaka mapenzi ya kuona aibu oa Mhehe,
Ukitaka kubana matumizi oa Mpare,
Ukitaka kisukari oa Mwarabu mara tende mara halua,
Ukitaka kujichanganya oa Mkerewe au Mjita,
Na kama unataka kuwachanganya mtu na dada yake oa Mrangi,
Ukitaka kubishana oa Mnyirmba
Ukitaka kupigana oa Mkuryaa,
Ukitaka kuzaa sana oa Muha,
Ukitaka kubembelezwa na kudanganywa oa Mnyamwezi
MMMMMHHH! PANA UKWELI HAPA KWELI ...NAONA WANGONI HATUPO KWENYE ORODHA:-)

Tuesday, April 8, 2014

TUDUMISHE UTAMADUNI WETU...HAPA NI BAADHI YA VIFAA VILIVYOTUMIKA SANA HAPO KALE NA PIA BADO VYATUMIKA

Kama mila na desturi zisemavyo usisahau ulikotoka na uendapo sehemu chukua na vile vyombo ambavyo ni asili yako. Hata kama hutatumia lakini unaweza kuwaelezea wanao wapi unatoka. Fuatana nami kuona baadhi ya vyombo asili nilivyochagua leo....Pia naomba msaada kama kuna anayejua majina ya kiswahili baadhi ya hivi vifaa.
 
 Hapa ni vifaa ambavyo huitwa VISONJO (ungonini tunaita VIJOMELA) hutengenezwa kwa majani ambayo huota ovyo ovyo tu (kingoni tunasema MALULU) anayejua kiswahili naomba msaada. Kifaa hiki ni maalumu kwa kunywea pombe hasa pombe ya kienyeji kama myakaya, komoni pia hata togwa badala ya kikombe;glasi au hizi waitazo dumla/robo nk.
 Hapa ni kifaa ambacho ni kwa kuhifadhia nafaka, kuwekea pombe nk..ni aina ya kikapu na miguu minne. Sisi wangoni huita (LINDANDALI). Kimetengenezwa kwa miazi na miti.
 Kwa nini kutumia chujio za kisasa ambapo zipo kama hizi. Mimi natumia hizi zinachunja sana kabisa nazi, na karibu kila kitu nitakacho kuchunja....ila nimekosa ya kuchujia chai.:-(.
Na hapa ni ungo mdogo ambao  hutumika sana katika nyumba nyingi sana Afrika/Tanzania. Ila sisi wangoni tuna jina letu tunaita (CHIHENEKO). Hiki waweza pia kupakulia/kuwekea ugali yaani kama sahani.

Sunday, April 6, 2014

NAPENDA KUWATAKIENI JIONI/JUMAPILI NJEMA SANA WOTE...ZILIPENDWA/NA MITINDO YAKE!!!

 zilipendwa 27/4/2009
Nimependa sana mkoba huu maana unamechisha na nguo yangu hapo juu. Ilikuwa ni hivi tu kwa JIONI HII YA JUMAPILI HII na NINAPENDA KUWATAKIENI WOTE JIONI /MCHANA/ASUBUHI NJEMA YA SIKU/JUMAPILI HII.

Friday, April 4, 2014

Thursday, April 3, 2014

UKIFIKA/PITA SONGEA USIKOSE KUPITIA HAPA ILI KUPATA CHAKULA CHA HARAKA NA KINYWAJI KIDOGO....SONGEA/LIZABONI!!!

Sehemu hii ipo Songea katika mtaa wa LIZABONI kwa wale wasio wenyeji wa Songea...Mara nyingi sana hapa huwa ni kituo chetu kupata nyama ya Nguruwe/kitimoto..mtanisamehe kwa wale waiotumia/kula mnyama huyu.
Kitu kingine kilichonifanya kuweka hii picha ni kwamba nimekumbuka enzi zileeee mtu unaweza kuwa safarini na usione sehemu ya kula kunywa ndo kabisa kama usipokuwa na chakula  mwenyewe au kupita kwa ndugu na kupata chakula kidogo. Nakumbuka nilipokuwa nasafiri  enzi hizo mama na baba walikuwa wananiandalia karanga zilizopondwa na chumvi(wangoni tunaita CHIMBONDI) Basi ukila hii inabidi uwe karibu na mto ili kupata maji ya kutelemshia. Leo vyakula vya haraka kila mji(Fasta food) Sijui ipi ni bora? Je nawe unakumbuka  kitu kama hiki au tofauti? 

Wednesday, April 2, 2014

MAMA MJASIRIAMALI..ANAPIKA POMBE

 Mama huyo hayupo nyumba katika kutaka kuitunza familia hapa anapika pombe. Kupika pombe ni kazi kubwa kwa kweli kwanza maandalizi yake ni makubwa halafu kuungua moto. Pia kupata kipato inategemea hiyo pombe "inoge" iwe nzuri. Nimewahi kutazamia jinsi inavyopikwa hii pombe wakati mama akipika hasa ile ya mihogo MYAKAYA si mnajua kila pombe huwa na jina lake baadhi ni kama vile kindi /komoni pombe ya mahindi Mbege pombe ya ndizi. Na pia pombe  si ni kinywaji tu cha kujifurahisha au kupata uchumi, kwa kifupi hasa sisi WANGONI kwa asili hupenda sana kunywa maji wakati akila chakula ila baada ya chakula hupenda kupata pombe/ugimbi kidogo kushushia ugali/chakula. Pia pombe huweza kuwashirikisha watu kwa kufanya kazi pamoja, kama vile kulima/kuvuna, kwenda kilabuni,  pombe ya harusi, na pombe ya sadaka. Na kwa kawaida huwa mtu/watu maalumu ambao huja mapema alfajiri kuonja kama pombe ipo safi "imenoga" kabla haijachunjwa na kwenda kilabuni au kunywewa.
Hapa naona ni ile POMBE ya kilabuni. Huyu baba kaona anachelewa kaamua kuchukua ndoa nzima  ameona "dumla" au kisonjo wangoni wanaita KIJOMELA. Nitawaonyesha siku yake. Kwa leo tuishia hapa. ANGALIZO:- TUSISAHAU SASA NI KWARESMA TUSINYWE KUPITA KIASI POMBE SI MAJI. Kapulya.

Tuesday, April 1, 2014

MWEZI MPYA NDIYO UMEANZA...HABARI ZA ASUBUHI AFRIKA/GODMORNING AFRICA....

Mwezi huu wa nne tuanze na hii picha ya mapozi ya watoto kutoka sehemu fulani Tanzania...Swali dogo tu je unajua hapa ni wapi?.... KILA LA KHERI.