Showing posts with label mahusuano. Show all posts
Showing posts with label mahusuano. Show all posts

Thursday, November 10, 2011

UTAPENDA HADI LINI?

Inasemwa siku zote kwamba, upendo ni kubadilishana, yaani mtu anampenda mwingine na huyo mwingine anampenda yeye. Hii ni kweli. Inapotokea kwamba, mpenzi mmoja anasahau wajibu wake, yaani kumpenda mwenzake na anasubiri kupendwa tu, tatizo hutokea.
Hali hii inapotokea, anayependa ambaye tunasema ndiye mtoaji pekee, hufikia mahali huingia kwenye hali ya hisia ambayo hufahamika kama resentment flu (Homa ya masikitiko). Hii ni hali ambayo, yule ambaye anatoa tu yaani anampenda mwenzake, lakini mwenzake hampendi, huihisi anapokuwa amechoka.
Kwa kawaida tunasema, mtu anapopenda asisubiri naye kupendwa, yaani anapotoa asijali kama mwenzake anatoa au hatoi. Lakini hufikia mahali kanuni za maumbile humfanya huyu anayetoa kuhisi kama amebeba mzigo mkubwa sana. Kama tunasema kupenda ni mtu kutoa bila kutarajia kupewa, inamaana kwamba, huyu anayeshindwa kutoa ameshindwa kupenda.
Kama ameshindwa kutoa ina maana kwamba, ameshindwa kutekeleza jukumu lake na hiyo ina maana kwamba, ameshindwa kupenda. Anaposhindwa kupenda anakuwa amevunja kanuni ya kimaumbile inayosimamia kupendana ambayo inasema ili kupendana kukamilike, pande zote ni lazima zitoe na kupokea.
Kumbuka nasema, kupendana, siyo kupenda. Kwenye kupenda tunatakiwa kutoa tu, kwenye kupendana tunatakaiwa kutoa na kupokea. Kama tunampenda mtu na mtu huyo hatupendi, yaani hatimizi majukumu na wajibu wake kwenye kutupenda sisi, hatimaye tunafikia mahali tunaingia kwenye hiyo hali niliyoitaja ya homa ya masikitiko.
Kumbuka ninaposema kutoa sina maana ya kutoa fedha, bali kumtendea na kumtolea kauli za wema mwenzako. Kwenye tatizo hili, wanawake wanaonekana kama wanaathirika zaidi.
Kama mwanamke akihisi kuwa yeye anatumikia upendo na mwenzake hajali tena, huumia kuliko ilivyo kwa mwanamume. Labda ni kwa sababu, wanawake huumia kihisia kirahisi zaidi kuliko wanaume na jambo hili linapotokea kuumiza zaidi hisia.
Mwanamke huanza kuingia kwenye hali hii polepole, pale anapobaini kwamba, mwenzake anapokea tu, badala ya kupokea na kutoa. Hii ina maana , mwanamume anaposubiri au kufurahia kutendewa mema na kutolewa kauli njema tu, wakati yeye hafanyi hivyo. hajali kuhusu mpenzi wake.
Mwanamke kwa kawaida huonyesha dalili kwamba, yuko kwenye hali hii kwa kuanza kuacha kufanya vile vitu ambavyo kwa kawaida huitwa au kuonekana vidogovidogo kwenye uhusiano.
Kwa mfano, anaweza akaacha kumtayarishia mumewe chakula anachokipenda sana ambacho alikuwa anamtayarishia kwa nyakati fulanifulani, anaweza asiwe anamchagulia tena nguo za kuvaa, anaweza asiwe anamkagua baada ya kuvaa, anaweza akaacha kumuuliza angependa kula nini na wakati mwingine anaweza kuchukua hatua mbaya zaidi kama kukataa kushiriki tendo la ndoa.
Mwanamume anapoona mke akiwa hivyo, naye huanza kumtendea mkewe kwa njia kama hiyo, yaani kuongeza kiwango chake cha kutojali. Anaweza kuanza kuchelewa kurudi nyumbani, anaweza hata kuscha Kukaa pamoja na mkewe hata akiwa nyumbani, anaweza hata kujitoa kabisa kwenye uhusiano, yaani kufanya mambo yake kama vile hana mke.
Inapotokea hali ambapo mwanamke anahisi kuingia kwenye homa hii, inabidi ajiulize haraka ni kwanini ameingia huko. Ni vizuri kujiuliza kwa sababu, akisubiri zaidi, mume naye ataanza kuwa mkorofi zaidi. Ikifikia hapo, njia ya kusuluhisha tatizo hili ambalo kwa kawaida, linaweza kuondolewa kwa mazungumzo, huwa ngumu zaidi.
Kwa hiyo, hakuna suala la “nitapenda hadi lini,” kwa sababu kupenda hakuumizi. Kunakoumiza ni kushindwa kutoa mapenzi. Ukitoa upendo wako kwa mtu ambaye yeye kazi yake ni kupokea tu, lakini hajui kutoa upendo, yeye ndiye atakayeumia. Yeye atakufanya uache kuendelea kutoa, hivyo yeye ndiye atakayekosa, siyo wewe.
Yeye atapata shida kwa sababu, kila mtu atakayeamua kuishi naye kama mpenzi, atahisi hali uliyoihisi wewe na ataamua kumkimbia. Ni hadi ajifunze kutoa, ndipo atakapoanza naye kuingia katika kupendana.
Hebu fikiria kwamba, unamtendea na kumtolea kauli nzuri mkeo au mumeo. Unahakikisha kwamba, unampa kila ambacho nawe ungependa kupewa, bila kujali kama naye anafanya hivyo kwako au hapana.Umemkubali kama alivyo na udhaifu wake na unazingatia zaidi ubora wake na siyo udhaifu huo. Hapa tunasema unampenda.
Lakini kwa bahati mbaya, huyo mwenzako ni mkosoaji, asiyejali, mchoyo, mlalamishi na mwenye ghubu. Huyu tunasema, hajui au hataki kupenda. Kwa maana hiyo, anaishi kwenye uhusiano usio na maana kwake. Hauna maana kwake kwa sababu, hana cha kutoa, ameshindwa wajibu wake katika uhusiano ambao ni kupenda. Kwa sababu hiyo, ni wazi hataweza kuendelea na uhusiano, ni lazima atasababisha uvunjike, kama tulivyoona.
Kama nawe hujui kupenda, utamuiga na utakuwa umeshindwa wajibu wako, kama yeye. Kwa hiyo, kwenye hali kama hiyo, hakuna kinachotolewa wala kupokelewa. Ni wazi uhusiano hauwezi kuwepo katika hali ya namna hiyo. Uzuri wa mmoja kuendelea kutoa bila kujali mwenzake anafanya nini ni kwamba, huyu mwenzake anaweza kungámua tatizo au kasoro yake na kubadilika.
Kwa hali hiyo, unaweza kuona jinsi upendo ulivyo kutoa na kupokea au njia mbili-kwenda na kurudi kama wengine wanavyosema. Unapokuwa wa kupokea tu bila kutoa au wa njia moja, hauwezi kuendelea kuwepo.
MAKALA HII NIMEISOMA MARA NGAPI SIJUI NA NIMEIPENDA NA NIMEONA SI VIBAYA NIKIWASHIRIKISHA NA WENZANGU ELIMU KUGAWANA …NIMEISOMA KWENYE KITABU CHA MAPENZI KUCHIPUA NA KUCHANUA KILICHOANDIKWA NA MAREHEMU MUNGA TEHENAN…PIA HABARI HII IMEWAHI KUTOKA KWENYE GAZETI LA MSHAURI WAKO.

Tuesday, March 3, 2009

MWANAUME NA MWANAMKE MAHITAJI YAO.SEHEMU YA II

a) Usalama: Ndiyo hali ya kujisikia kuwa huna hofu yoyote au wasiwasi. Wakati ambapo hakuna kitu cha kutisha au cha kuvuruga akili. Najisikia salama hatari ikiwa mbali, maadui hawapo nami nimeshinda matatizo.
Yapo mambo mengi ambayo yanaweza kutuondolea usalama katika mioyo yetu. Ajali yaweza kutokea, vita, magonjwa yaweza kutupata; watu pia wanaweza kutudhuru, kuiba mali yetu na hata kuhatarisha maisha yetu. Hofu ipo ndani yetu kwa namna nyingi. Hofu ya mambo tusiyoyajua, hasa katika kutafuta kazi, au tukiwa ugenini, tubadilishapo mtindo wa maisha.

Ingawa yote hayo yapo, bado tunajua usalama. Kuna usalama wa mtoto kifuani kwa mama yake. Usalama wa mtoto ashikapo mkono wa baba yake. Usalama wa rafiki ambaye anajua kwamba kwa vyo vyote rafiki yake yuko tayari kumsaidia. Usalama wa mwanamke aliye na hakika juu ya mapendo ya mumewe. Usalama huu ndio msingi wa haja zetu na usalama unatakiwa hasa katika ndoa. Haja hiyo ya usalama ikitoshelezwa, amani kubwa na utulivu wa moyo hupatikana.

b)Kukubalika: Haja yetu ya pili yaitwa kukubalika. Ni haja ambayo wewe na mimi tunaijua sana. Ni ile hali ya kukubalika na watu kama tulivyo, kueleweka nao, kpokewa jinsi tulivyo na tunavyojitahidi kuwa. Kila mmoja wetu anahitaji sana mtu mwingine wa kumsindikiza, kufurahi na kuhuzunika pamoja naye. Mtu ambaye anajua matatizo na matakwa yetu; pia mwenye kuelewa tunayohofia.
Jaribu kufikiri kidogo maisha yangalikuwa ya namna gani kama hatingalikuwa na mtu ye yote wa kumkimbilia wakati wa shida, au mtu wa kutupongeza na kututia moyo.

Katika ndoa mwezi wako Mume/mke, anatazamia kupata hayo kutoka kwako. Mume wako ama mkeo anataka kuhakikishiwa kwamba kwa upande wako hatapata masharti yo yote ya kumkubali; hii ina maana kwamba unamkubali na kumpokea kwa furaha jinsi alivyo nawe unamjulisha jambo hili.

Hii haina maana kwamba huwezi kuona kasoro na udhaifu alio nao mwenzako. Maana yake ni kwamba unakuwa tayari kumwambia: “Najua ya kwamba wewe si mkamilifu, lakini nakupenda jinsi ulivyo, na pia nakubali ujue kuwa wala mimi si mtu mkamilifu. Hata hivyo nina hakika kuwa unanipenda”. Unapokuwepo ukubaliano wa namna hii kila mmoja huwa na imani kubwa na mwnziye na kujiamini pia.

c) Kuthaminika: Ndilo hitaji la tatu ndani mwetu. Je, tulieleweje hitaji hilo? Unaweza kupata mwanga kidogo juu ya jambo hili kama ukikumbuka jinsi unavyojisikia wakati umekwisha fanya kila juhudi na kujisumbua ili upate kumfurahisha mwingine. Halafu mtu huyu unayetaka kumfurahisha hajali wala hatambui kwamba umefanya kitu kwa ajili yake. Katika hali hii utajisikia kama umekosa kitu fulani, na kitu chenyewe ni kuthaminika.

d) Kujikamilisha binafsi: Hiki ndicho kilele cha mahitaji yote ya hisi. Ni ile hali ya kujisikia kitu cha maana. Kujisikia kwamba nimetumia vipaji vyangu vyote kikamilifu. Nimetumia nguvu zangu zote za mwili, akili na moyo, na kweli nimefaulu kuwafurahisha wengine. Kwa kufanya hivi najiona mtu zaidi.
Si lazima kufanya mambo makubwa. Kwa mwanamke yaweza kuwa kazi ya kudarizi au kuremba kwa ushanga, kupamba nyumba kwa namna ya pekee, kutengeneza nguo za watoto zitakazomletea sifa ya wengine. Kwa mwanamume yaweza kuwa kuchukua kozi kwa njia ya posta ili kupata kazi nzuri zaidi au mshahara mkubwa zaidi.

Katika kufanya mambo haya kila mmoja anahitaji mwenzake, mume au mke. Kwa sababu kule kujikamilisha binafsi, mara nyingi, huhitaji msaada wa mwenzio. Mapendo yake yatakudhihirishia vipaji fulani ambavyo hukuvijua kwanza, na mapendo haya haya yatakupa nguvu ya kuviendeleza. Kwa pamoja utaweza kujijenga. Kwa pamoja pia mtayatosheleza mahitaji haya yaliyomo ndani ya moyo wa kila mwanamume na kila mwanamke.

Mahitaji ya kiroho
Aina ya mwisho ya mahitaji ni yale ya kiroho. Je, nina maana gani kusema hivi? Ninataka kusema, kuhitaji kitu kilicho kikubwa zaidi kuliko vile vya kibinadamu. Ni kuhitaji heri iliyo kubwa zaidi ya ile ya kibinadamu, kuhitaji amani iliyo kuu kupita moyo wa binadamu, kuhitaji Mungu Mwenyewe.