Wednesday, June 30, 2010

Kinamama Kilindi wakiri kuwakeketa watoto wa kike

WANAWAKE wa jamii ya wamasai wilayani Kilindi mkoani Tanga wameeleza waziwazi kuwa wimbi la ukeketaji wasichana bado linaendelea katika jamii hiyo ya wafugaji, licha ya kampeni mbalimbali zinazofanywa na mashirika mbalimbali kukomesha shughuli hiyo.
Kina mama hao, walisema pamoja na kuendelea na vitendo hivyo vya ukeketaji kwa usiri mkubwa, pia wameeleza wamekuwa wakiwauguza mabinti zao nyumbani wanapopata madhara sehemu za siri kutokana na majeraha baada ya kukeketwa na wakati mwingine kupoteza maisha.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti wakati wa mkutano wa hadhara ulioshirikisha marika na jinsia zote katika eneo la Shule ya Msingi Mbogoi Kata ya Mkindi wilayani hapa juzi,kina mama hao, walisema wanaendelea na ukeketaji kwa madai kuwa hawajapata elimu ya kujua madhara yake.
Mimi tangu nianze kuwazalisha wazazi tangu miaka mingi iliyopita sijawahi kuona mwanamke ambaye hajakeketwa. Sisi tulifikiri kuwa duniani hakuna mwanamke ambaye hakeketwi na tuliona ni muhimu kwa kuwa ni kudumisha mila zetu. Lakini pia tukielimishwa zaidi tutaacha ukeketaji,†alisema Yosephat Taringo.
Naye Wiliam Tangoro (65) katika mkutano huo, alisema wanashukuru Shirika la AMREF kuchukua jukumu la kuwaelimisha wafugaji ili kuepuka mila hizo, ambazo sasa zimepitwa na wakati.
“Sisi tunalishukuru shirika hili la AMREF kwa kutujali na kutuelimisha ili tuachane na mila hii ambayo sasa elimu hiyo, imeanza kuenea sehemu mbalimbali za makazi yetu wafugaji,†alisema Tangono.
Mafunzo hayo, yanayofanyika usiku kwa njia ya mijadala na sinema na kushirikisha watu wa rika zote na jinsia zote ikiongozwa na Afisa Utamaduni wa wilaya hiyo, Adelina Ndumbaro na yamekuwa yakivutia watu wengi huku wachangiaji wakielezea undani wa maisha yao kwa uwazi zaidi.

Habari hii imeandikwa na Hussein Semdoe,Kilindi iliandikwa 25/3/2010 nimeona si vibaya kama wengi tukiisoma kupitia kibaraza hiki cha Maisha na Mafanikio.

Tuesday, June 29, 2010

Maliasili zetu!!!!

Hakuna mnyama ninayempenda kama twiga. Mama na mtoto hapo !!!

Monday, June 28, 2010

KUSHIKWA KWENYE MAPENZI SIYO LIMBWATA AU MAPENZI MOTOMOTO BALI NI MATOKEO YA HOMONI!

Wakati mwingine huwapigia simu wapenzi wao wa nje waziwazi

Tunajiuliza siku zote ni kwa nini penzi linapoingia mahali huweza kuharibu kila kitu? Tumekuwa na misemo yetu ya siku nyingi kama siyo ya asili, kama vile ule wa ‘penzi ni ulevi’ au ‘penzi ni upofu’ na mingine yenye kuonyesha kwamba penzi lisipoangaliwa kwa makini linaweza kuleta athari mbaya na kubwa kwa binadamu.

Ni nani ameshawahi kujiuliza ni kwa nini hali hiyo hutokea? Kuna yeyote ambaye hata mara moja ameshawahi kujiuliza ni kwa nini penzi halina shujaa au mnyonge pale linapoingia wote huwa kama waliopagawa? Bila shaka sio wengi, kama wapo ambao wameshawahi kujiuliza swali hili. Kila mmoja anadhani ndivyo ilivyo na hakuna awezaye kujua ni kwa nini.

Ukweli ni kwamba penzi halina tofauti na ulevi sugu kama ule wa pombe au madawa ya kulevya. Penzi linaelezwa kwamba ni sawa na ubobeaji wa mcheza kamari. Ile starehe na pumbazo la akili ambalo mtumiaji wa madawa ya kulevya au mlevi sugu analihisi, ndilo hilo hilo ambalo mtu aliye katika mapenzi anahisi.

Penzi(Kwa maana ya mtu kumpenda mwingine wa jinsia tofauti kwa penzi la kawaida au hadi kwa kufanya mapenzi) na usugu wa madawa au pombe, vyote huwa vinauchochea mwili wa anayehusika kutoa homoni inayofahamika kama dopamine. Homoni hii ambayo ni kemikali katika ubongo huwa inaujaza mwili raha na ni kemikali hii hii ndiyo ambayo inahusika katika kuupa mwili tabia ya usugu katika mambo fulani kama ulevi.

Ni kitu gani kikubwa katika hili?

Ni kwamba kama ni hivyo, ina maana kuwa mtu kuwa kwenye kiwango kikubwa au cha juu cha kupenda, yaani kama tulivyozea kusema ‘kuwa hoi kwa penzi’, ni sawa na wakati ule mlevi sugu wa madawa akiwa ameshavuta au kunywa.

Mbaya zaidi ni pale penzi linapofikia hatua ya kuwa penzi la kukutana kimwili. Ni mbaya kwa sababu katika hatua hii homoni ya depomine inayotolewa inaweza kuizinga akili milele.

Kinachotokea ni kwamba kama homoni hiyo itajizinga kwenye akili, mhusika anakuwa sawa kabisa na mlevi sugu wa pombe au madawa ya kulevya, inakuwa ni vigumu sana kumtoa mtu kama huyo kwenye penzi na huyo fulani wake.

Bila shaka umeshawahi kuona au kusikia juu ya watu ambao wanaishi kwenye uhusiano mgumu sana na wapenzi wao, lakini bado wakawa wagumu wa kuondoka kwenye uhusiano huo. Kwa mawazo yetu wengi huwa tunadhani kung’ang’ania huku kunatokana na hali kama utegemezi, hasa kwa wanawake.

Baadhi yetu huwa tunaamini kwamba hali hiyo inaweza kuwa inasababishwa na dawa za asili au uchawi maarufu kama Limbwata, hasa pale mwanaume anapokuwa ameshikwa kwenye mapenzi na mpenzi wake au mkewe. Hii sio kweli.

Kuna wakati unakuta kwamba mwanamke ana uwezo wa kuendesha maisha yake na pengine yeye ndiye anayemsaidia mwanaume katika maisha, lakini pamoja na kuteswa au kuburuzwa na mwanaume huyo, bado atang’ang’ania kuishi naye. Kuna wakati tunaona kabisa kwamba, mwanaume anajua kwamba mwanamke anamfurusha kwenye uhusiano wao na anakiri, lakini bado anang’ang’ania kwenye uhusano huo na mwanamke huyo.

Inaanzaje?

Watu wawili hupendana. Kama nilivyosema, kupendana huku husababisha homoni hii kuzalishwa ubongoni. Kuzalishwa kwa kemikali hii ndiko ambako humfanya mtu aliyependa kuwa katika raha fulani isiyoelezeka. Kama ilivyo kwa mlevi wa pombe au madawa ya kulevya, kuna wakati kiwango cha nishai hushuka ambapo inabidi avute au kunywa tena. Kwa mtu aliyependa naye, kuna wakati hali ya raha hii hushuka, kutegemea mazingira.

Lakini kama wapendanao wamekutana kimwili na kukutana huko kukawapa raha kubwa sana, uwezekano wa kemikali hii kuizinga akili moja kwa moja ni mkubwa sana. Akili inapozingwa na homoni hii, mpendaji kamwe hataacha tena kumpenda huyo mtu wake.

Inakuwa kama mlevi sugu anavyotegemea pombe au madawa kupata raha ya maisha, huyu mpendaji naye atakuwa hajisikii raha bila kuwa na huyo mpenziwe, bila kujali visa na vibweka anavyomfanyia. Hata kama hashiriki naye tendo la ndoa, bado atakuwa anajisikia raha tu kuwa naye.

Msomi mmoja wa chuo kikuu cha Guelph huko Canada, George Bubenik anakiri kuwepo kwa hali hii na anasema ndio maana unaweza kukuta mtu akiishi kwenye ndoa ya mashaka na vurugu huku huku wengine wakishangaa na kutoelewa sababu. “Mtu ambaye anafurahia sana tendo la ndoa mwanzoni mwa uhusiano na mwenzake anaweza kung’ang’ania kwenye ndoa hata kama imejaa vurugu”

Anasema watu hawa wangetarajiwa kuondoka au kuzikimbia ndoa za aina hii lakini huwa hawafanyi hivyo kwa sababu wamepata usugu wa kiakili kwa zile hisia wanazozipata wakati waliposhiriki tendo la ndoa na wapenzi wao. Kama mlevi sugu wa pombe asivyoweza kuacha pombe hata kama inakaribia kumuuwa, ndivyo inavyokuwa kwa watu wa aina hii.

Haina maana kwamba hao wapenzi wao ni watu wenye kujua sana mapenzi, hapana. Ni kwamba siku ya kwanza walipokutana , ubongo ulizalisha homoni kwa wingi na ikawa imeizinga akili. Kinachojirudia hapa ni zile hisia za awali. Sawa kabisa na mlevi sugu, ambaye anaweza kuwa anakunywa pombe kali na isiyo na utamu, kwa sababu anachohitaji siyo ladha ya pombe, bali zile hisia wakati au baada ya kunywa. Hapa mwanamke au mwanaume aliye katika hilo penzi anaendeshwa na hisia anazozipata wakati wa tendo la ndoa, ambazo zimeganda akilini kupitia homoni hii ya dopamine.

Huwa hakuna kulogwa wala limbwata au mapenzi motomoto, hapana., hapa kuna tatizo la utegemezi. Mhusika ni mtu ambaye inabidi asaidiwe kama anavyosaidiwa mlevi sugu. Wengi wetu huwalaumu watu hawa au wapenzi wao, jambo ambalo bila shaka siyo haki.

Tumeshawahi kusikia bila shaka watu wakisema, ‘wewe hujui ni kwa nini anang’ang’ania uhusiano ule, anajua mwenyewe anachokipata’. Wengi wanaposema hivyo wana maana ya kile mtu huyo king’ang’anizi anachokipata hadi kutokuwa tayari kuvunja uhusiano na mpenzi anayemtesa au kumdhalilisha. Mara nyingi wana maana ya mapenzi motomoto ya kitandani. Huu siyo ukweli hata kidogo, kwani unaweza kukuta hata mapenzi ya kitandani mtu huyo hapati. Anachokipata hapa ni ridhiko linalotokana na dopamine iliyozinga ubongoni mwake.

Inakuwaje ikibidi uhusiano huo ufe:

Kuna wakati kwa sababu ya mazingira fulani fulani inabidi uhusiano huu ufe, hata kama mmoja ni king’ang’anizi vipi. Hilo linapotokea yule king’ang’anizi hukabiliwa na athari za matokeo kama vile wasiwasi, aina ya hamu ya mapenzi au kupendwa isiyoweza kuridhishwa, huzuni na hasira. Hali hizi pia huwa zinapatikana kwa mlevi au mvutaji sugu ambaye anajaribu kuacha kuvuta au kunywa.

Kuthibitisha hii Bubenik aliwafanyia utafiti panya wadogo wa porini na kugundua kwamba wanyama hawa wakizuiwa wasitoe homoni iktwayo oxytocin ( sawa na homoni ya dopamine kwa binadamu) wakati wakipandana huwa hawadumu pamoja. Lakini pale wanapoachiwa watoe hiyo homoni huwa hawaachani hadi kufa.

Tunaweza kusema mtu kushikwa au kunaswa kwenye mapenzi ni suala ambalo hakuna mtu anayeweza kudai kwamba anaweza kulizuia. Kulizuia kunawezekana kama mtu ataamua kuachana na tabia ya uzinzi tu, kwani hatafikia mahali ambapo akili yake itazingwa na homoni hii.
Makala hii nimeipata kutoka kwa kaka Shaban Kaluse na nimeona si vibaya kama nikiweka hapa Maisha na Mafanikio kwani wote tuna lengo moja. Kwa kumsoma kaka huyu zaidi bonyeza hapa kaluse.blogspot.com

Sunday, June 27, 2010

Baada ya kuadimika kwa siku chache nimerudi tena!! na nipo nanyi tena!!!! Jumapili njema wote!!

Karibuni Chai

Karibuni Kahawa pia...

Napenda kuwaomba radhi wasomaji wa kibaraza hiki kwa siku hizi tatu kwa kutopata kitu cha kusoma. Kwa hiyo nimeona niwaombe radhi kwa kikombe xha Chai pia Kahawa. Ni pilika pilika za hapa ba pale. Haya Nawatakieni wote Jumapili njema na Chai åia kahawa njema. PAMOJA DAIMA.!!!! na nawatakieni wote jumapili njema






Thursday, June 24, 2010

Salaam kutoka Seminary ya Likonde!!

Jengo la Seminary kuu ya Likonde


Nimtume nani unatume mimi nitume bwana.
Leo nimetembelea Likonde Seminary na nimeona iwe picha ya wiki hii. Najua wengi mtakuwa na kumbukumbu nyingi kuhusu Likonde. Tukutane tena wakati mwingine.


Wednesday, June 23, 2010

Barua ya wazi kwa baba mkubwa huko kijijini..

Mpendwa Baba mkubwa,
Salamu ama baada ya salamu mimi huku ni mzima na ninaendelea vizuri. Hofu ni kwenu huko mlio mbali na upeo wa macho yangu.
Madhumuni hasa ya barua hii ni kukushtakia kuhusu tabia ya kaka na dada zangu huko nyumbani. Si hao tu kwani akina shangazi na akina shemeji pia ningependa kuwashtaki kwako.
Baba kama unavyofahamu mwanao siku hizi naishi ughaibuni. Niliwasili hapa miaka kadhaa iliyopita ili niweze kupata kaelimu kidogo na kuboresha maisha yangu na ya ndugu zangu. Namshukuru Mungu kwakweli tangu niwasili hapa nimekuwa bukheri wa afya. Tangu kufika kwangu hapa baba nimejitahidi sana kufanya kazi kwa bidii na kutuma njuluku kidogo huko nyumbani kwa ndugu zangu.Orodha ya niliowatumia pesa hata wewe baba unaifahamu kwani ni ndefu sana. Kusaidiana katika jamii ndio utamaduni wetu kwani nami nakumbuka vizuri akina kaka,dada na shangazi jinsi walivyonisaidia wakati nikiwa sina kazi na bado mwanafunzi. Malalamiko yangu baba si kuhusu kuwasaidia bali jinsi ambavyo wamekuwa hawathamini mchango niutoao katika familia. Je inawezekanaje pesa zote nilizotuma ni mmoja tu ndie kafanya kitu cha maana?? Hata wewe baba unamfahamu ni nani ninamuongelea. Wengine wote pamoja na kuwapa pesa za mitaji waliyoomba hawakuweza kufanya kitu cha maana. Chonde baba nakuomba unishauri nifanye nini kwani nimechanganyikiwa. Nikiangalia katika familia, umaskini ndio unazidi kujikita. Hata pamoja na kuwa tumeweza kupata kauwezo ka kupata tumitaji lakini bado hali inazidi kuwa mbaya. Angalia lile duka pale Tandale, mpwa wangu kalifilisi. Hata lile duka la vipodozi kule Namanga limefilisikaje? Yule aliyeomba mashine ya kusaga kule kijijini ana maelezo gani kuhusu kupotea kwa hizo mashine? Lile pick up kule Kibaha iweje liwe juu ya mawe na lilikuwa linazalisha pesa nzuri tu? Kaka Ubwa yeye ndie alinichosha kabisa. Ati kaenda posta kuchukua pesa za mtaji alizoniomba, akapotea nyumbani wiki mbili. Karudi baada ya pesa kwisha. Jee huu ni uungwana? Je nitaendelea kutuma ada za watoto wa ndugu zangu mpaka lini? Je ulisikia shemeji Makame haongei na mimi ati kwa kuwa nilimuomba anivumilie nimalize mitihani ili nimtafutie pesa aliyotaka? Eti ananiita mimi mpiga boksi!! je haki hiyo baba? Dada Hija huniita mimi ATM ati kila mara awapo na shida basi mimi humtatulia shida zake. Jee Huu ni Uungwana?? Sijasahau siku ile dada Hawa aliponieleza kaibiwa shilingi laki saba alizotoka kuchukua Western Union, ati aliziweka kwenye backpaki na kuiweka backpaki mgongoni. Watoto wanatakiwa shule wiki ijayo, nitatoa wapi pesa zingine? Namthamini sana dada yangu ndio maana watoto wake niliwatafutia shule nzuri?? Jee Baba huu ni uungwana??
Yaliyo moyoni ni mengi lakini kwa leo ni hayo tu. Chonde baba nishauri. Wasalimie wote hapo nyumbani.
Ndimi mimi mwanao
Kimenyanga Kaladamu wa Esimingori

Nimeipenda baraua hii nimekuwa nikipita kwenye kibaraza hiki na kusoma hata sijui ni mara ngapi na leo nimeona si vibaya nikiiweka hapa kibarazani ili wengi tufaidike. zaidi soma hapa . Ahsante sana kaka Mfalme Mrope.

Tuesday, June 22, 2010

Je? barabara hii itakufikisha wapi??

Barabara hii imenikumbusha mengi sana wakati wa utoto /zamani mtu umechoka una mzigo kichwani na barabara unaiona ndefuuuuuu. Haya karibu ni wapi hapa?

Monday, June 21, 2010

WANGONI NA VISA ASILI VYAO!

Sijui nimfundishe mwanangu juu ya mila hizi?

Kuna visa asili vingi sana ambavyo nimevishuhudia katika makuzi yangu. Lakini miongoni mwa visa asili hivyo, kuna kisa asili kimoja ambacho mpaka leo bado ninakikumbuka.

Bila shaka hata wewe unayesoma hapa huenda vipo visa asili ambavyo unavikumbuka na umekuwa ukiviamini au umeachana navyo kutokana na utamaduni wetu kumezwa kwa kiasi kikubwa na utamaduni wa kigeni.

Leo nimekumbuka kisa asili kimoja ambacho ningependa kuwashirikisha wasomaji wa kibaraza hiki.

Nakumbuka nilipokuwa mdogo mama alipokuwa jikoni akipika, alikuwa na kawaida ya kuita mmoja kati ya sisi watoto wake ili kwenda kumuwekea chumvi kwenye chakula na kama tulikuwa mbali au shuleni basi atamwomba mtoto wa jirani na kama hayupo mtoto wa jirani basi atapika bila kuweka chumvi.

Hali iliendelea kuwa hivyo mpaka siku nilipovunja ungo, ndipo nami nikaingia kwenye mkumbo huo. Niliambiwa kuwa nisitie chumvi tena kwenye chakula au mboga. Lakini cha kushangaza kaka zangu pamoja na wao kubalehe lakini hawakuwekewa vikwazo kama mimi.
Kama kawaida na UKAPULYA wangu nikataka kujua KWANINI?
Jibu lake lilikuwa hili:- Niliambiwa kuwa nikitia chumvi hasa wakati ule nipo hedhini na baba yangu akila chakula kile basi atavimba miguu Nadhani kama nakumbuka vizuri niliambiwa kuwa hata kaka zangu pia mume wangu wanaweza kuathirika.
Cha kushangaza ni kwamba mila hiyo niliiacha siku nyingi huko nyumbani na nimekuwa nikimpikia mume wangu kama kawaida bila kutafuta mtu wa kuniwekea chumvi na wala haijatokea akavimba miguu. Hata hivyo sina uhakika sana kama imani hii bado ipo au la. Kwani tangu niondoke nyumbani kuna mambo mengi sana yamebadilika.
Swali langu kwa wasomaji wa kibaraza hiki. Je? hii imani ni ya wangoni tu au ipo kwenye makabila mengine?

Sunday, June 20, 2010

Nawatakieni jumapili njema kwa wimbo huu!!



JUMAPILI NJEMA KWA WOTEEEEEE. NA TUKUMBUKE YA KWAMBA KRISTU NDIO TUMAINI LETU!!

Thursday, June 17, 2010

Picha ya wiki hii!! Je? Unajua mwanamtindo huyu ni nani?

Nimeipenda hii picha na nimeona iwe picha ya wiki hii. Rangi za mavazi ni rangi ambazo zinawakilisha nchi yetu Tanzania. Na pia nimependa mwanamtindo huyu kwa mtindo wake wa nywele..

Na sasa ngoja tusikiliza kibao hiki ambacho kinawakilisha ujumbe murwaaaaaaaaaaaaaaaaaNi "Reggae sasambua sytle" iliyoimbwa na Dada Saida Karoli kuhusu sweet Tanzania

Wednesday, June 16, 2010

HIVI HIZI LEBASI ZA ULIMBWENDE ZATUFAA KITU GANI?

Mwisho wake hutuletea maumivu


Bado nina ndoto za Alinacha, leo nikiwa nimejipumzisha hapa kwangu, nikawa najiuliza. Hivi ni nani aliyevipa vito na madini thamani? Je mtu kumiliki vito na madini yenye thamani ni ili iweje?
Kuna siku nilipita duka moja linalouza vito na kukuta kuna ulinzi mkali ajabu, na si hayo tu bali pia visa vya wanawake kukatwa masikio na kujeruhiwa shingo na vidole vya mikono wakiporwa Pete, Hereni, Cheni za Dhahabu na vito vya thamani haviishi kila kukicha.

Kuna wakati nilipokuwa nyumbani Tanzania niliwahi kukoswa koswa kukatwa sikio na vibaka wakitaka kunipora hereni zangu za dhahabu, na kama sio wifi yangu kuwahi kupiga kelele, leo hii Yasinta ningekuwa na sikio nusu.

Labda niwaulize wanawake wenzangu, hivi hizi Lebasi za Ulimbwende zatufaa kitu gani il-hali zatuhatarishia maisha?

Tuesday, June 15, 2010

LAU KAMA WANAUME WANGEKUWA WANANYONYESHA!!

Tujikumbushe hili. Hivi ingekuwa wanaume ndio wananyonyesha watoto na mihasira yao sijui ingekuwaje?. Lakini Mungu kwa kuona mbali akaona hapana. Kama mwanaume ataona mtoto ni wake kwa ubini wa jina lake na kwa ubabe lakini watoto watanyonyweshwa na mama zao. Ukiwa kama baba umejaribu kumpa mkeo upendo wa ziada kuwa anayofanya kwako, kwa watoto na familia kwa ujumla?
Kumbuka mwanamke hata akipita vitani wanajeshi hushauriana kama wamuue au la. Mwambie mkeo Ahsante kwa yote!

Monday, June 14, 2010

Rose: Ninaishi Stendi ya Ubungo huu ni mwaka wa tano sasa

STENDI ya Mabasi yaendayo Mikoani ya Ubungo, Dar es Salaam, kama lilivyo jina lake ndimo watu wanaosafiri kwa barabara kwenda mikoani na hata nje ya nchi wanapopandia na kuteremkia.

Shughuli zinazofanywa hapo si hizo tu, kuna biashara mbalimbali na hata huduma kama vile posta, simu, polisi na nyinginezo. Lakini kwa baadhi ya watu hayo ni makazi, ndipo wanapopategemea kwa kila kitu kuanzia malazi mpaka chakula.

Mmoja wao ni Rose Peter ambaye anasema huu ni mwaka wake wa tano akiishi katika stendi hiyo alifika hapo mnamo mwaka 2006 akitokea Same mkoani Kilimanjaro ambako alifunga safari hiyo kwa kile alichoeleza kuwa ni kufukuzwa na mjomba wake baada ya kupata ujauzito ambao wakati huo ulikuwa wa miezi mitatu.

Rose alililewa na mjomba wake baada ya mama yake kufariki wakati alipomzaa. Anasema hajawahi kumuona baba yake mzazi.

Rose anasema kwamba aliponzwa na kijana mmoja anayemtaja kwa jina moja la Jerome ambaye alimpachika mimba lakini baada ya kufukuzwa na mjomba wake, naye alimkana hivyo kulazimika kukimbilia Dar es Salaam... "Nilipomweleza kuwa ni mjamzito alinigeuka na kuniambia hanijui, nimtafute mwanamume aliyenipa mimba hiyo. Alinitisha na kuniamba nikiendelea kumfuata atanipiga.”

Kuona hivyo, alikwenda kwa shiga yake ambaye hata hivyo, hakutaka kumtaja jina ambaye alimshauri kwamba njia bora ni kwenda Dar es Salaam akatafute maisha ili aje kumudu kumhudumia mtoto wake atakapojifungua.

Aliondoka Same akiwa hana mbele wala nyuma, hakuwa na ndugu wala jamaa wa kumfuata Dar es Salaam na haikushangaza kwamba maisha yake Dar es Salaam mpaka leo yameanzia na kuishia hapo hapo stendi ya mabasi.

“Nilitegemea kwamba nikifika huku Dar es Salaam maisha yangu yangeninyookea. Ningepata kazi kirahisi nilijua kwamba kwa kuwa ni jiji kubwa si rahisi kukosa kazi matokeo yake maisha yangu yakawa magumu,” anasema Rose.

Binti mjamzito, anahitaji kula achilia mambo mengine kama malazi ambayo hadi sasa anayepata humo humo katika eneo ambalo limetengwa kwa ajili ya abiria wanaosubiri usafiri. Hali hiyo na ukizingatia kwamba kuna msemo wa hakuna cha bure, amekuwa wakati mwingine akilazimika kutumia mwili wake kupata riziki.

Baada ya maisha kuzidi kuwa magumu hasa baada ya mimba kufikisha miezi minane, aliamua kutoka 'nyumbani kwake' hadi katika Kituo cha Polisi Buguruni kuomba msaada wa kupatiwa mahali pa kuhifadhi walau kulala tu. Aliamini kwamba kwa hali aliyokuwa nayo wangemuonea huruma.

“Namshukuru Mungu walinikubalia nikawa nalala hapo. Kulikuwa na usalama zaidi tofauti Stendi ya Ubungo watu hawakujali hata ukiumwa wanakupita hapo utajijua mwenyewe. Nilikimbilia kule ili kama nikianza kuumwa wanikimbize hospitali,” anasema Rose.

Akiwa kituoni hapo, askari polisi mmoja wa kike anayemkumbuka kwa jina moja la Joyce alimuonea huruma na kumchukua kwenda kuishi naye kwake kwake Ilala.

Alipopata uchungum askari huyo alimpeleka Hospitali ya Taifa Muhimbili na alijifungua salama mtoto wa kike ambaye alimpa jina la Inura Jerome.

"Afande Joyce alinihudumia vizuri hata baada ya kutoka hospitali. Nilipata huduma zote anazotakiwa kupawa mzazi bila kujali kuwa si ndugu yake. Mwili wangu ulirudi katika hali ya kawaida nilinenepa kama vile sikutoka kujifungua. Kwa kweli ninamshukuru sana ninamthamini kama mama yangu mzazi, hata ndugu zangu wasingenifanyia hivi.”

Baada ya kumaliza miezi miwili anasema mama huyo alimwombea kuishi kwa rafiki yake mwingine wakati huo akijikusanya kumtafutia nauli ya kurudi kwao Same.

Lakini anasema dada huyo alishindwa kukaa naye kwa kuwa mumewe hakuwa tayari kubeba mzigo huo... “Niliambiwa niondoke kwani angeweza kuachwa na mume wake. Niliondoka kuogopa kuachanisha ndoa ya watu.”

Hakuwa na pengine pa kwenda isipokuwa kurudi Stendi ya Ubungo. Lakini safari hii alipokewa kwa mikono ya huruma kwani anasema baadhi ya wasamaria wema walijitokeza na kumpa nauli ya kurudi kwao hasa baada ya kumwona akihangaika na mtoto.

Kwa kuwa maisha yale yalikuwa yameshamchosha, aliitikia wito huo na kupanda basi kurejea kwao. Hata hivyo, adhabu ya mjomba wake ya kumfukuza ilikuwa palepale alimwambia aende kwa mwanamume aliyemzalisha.

“Nilirudi tena Dar es Salaam na kuendelea kuishi Ubungo Stendi. Pale ninalala sehemu wasafiri wanapokaa wakiwa kusubiri mabasi. Hakuna hata ndugu ninayemfahamu,” anasema.

Baada ya kurejea alipata bwana aliyekuwa akifanya kazi katika moja ya gereji ndani ya stendi hiyo... “Alinidanganya kuwa atanioa. Alikuwa anautumia mwili wangu kwa ajili ya starehe zake na alinipa fedha kidogo sana.

"Nikimwuliza mbona fedha unazionipa hazinitoshi hata mwanangu akiumwa nashindwa kumpeleka hospitali ananiambia haya mambo hayataki haraka.”

Ni dhahiri kwamba alikuwa akimhadaa kwani Rose anasema kila walipokuwa wakitaka kukutana faragha wala hawakutoka nje ya stendi hiyo bali kuvizia usiku hasa umeme ukiwa umekatika.

Ukweli wa mapenzi yao ulidhihirika mnamo mwaka 2009... "Nilimwambia kuwa amenipa mimba. Aliikubali lakini matokeo yake aliacha kazi na hayaonekana tena maeneo ya stendi."

Baada ya mimba hiyo ya pili kukua anasema alimfuata mama mmoja 'Mama Saidi' aliyekuwa anaishi Mbagala Kongowe na kumweleza shida zinazomkabili. Alimwomba aka kwake kwa muda na kwamba akishajifungua ataondoka.

Alimkubalia na kuishi hapo hadi alipojifungua mtoto wa kiume aliyempa jina la Gerard na siku nne tu baada ya kujifungua alirejea 'nyumbani' Stendi ya Ubungo.

“Nilikuwa na wakati mgumu fedha sina, ndiyo kwanza mwanangu ana siku nne tu. Ninatakiwa nile chakula cha nguvu ilibidi wakati mwingine kulala na wanaume hivyo hivyo ili nipate pesa ya kula.”

Baada ya kuona kwamba anahaingaika na watoto wawili, mama mmoja anayefanya biashara ya kuuza mikate katika stendi hiyo alijitokeza na kumchukua mwanae na kwenda kuishi naye kwake Buguruni hivyo kumpunguzia mzigo.

Rose hataki kupata watoto tena kwani anajua ugumu wa kuwalea ... “Kwa sasa nimejiunga na uzazi wa mpango ili nisishike mimba mwanangu bado mdogo ana miezi minane.”

Lakini siyo Rose aliyepageuza Stendi ya Ubungo kuwa ni makazi yake ya kudumu: “Pale tupo wengi siko peke yangu. Wanawake tupo zaidi ya 10 na tunaye mzee mwenye umri zaidi ya miaka 60 nimemkuta anaishi pale.”

Rose amechoshwa na maisha hayo. Lakini hana mtaji wala pa kwenda ingawa ndoto yake ni kupata angalau uwezo wa kupanga chumba chake na kufanya biashara halali itakayomwezesha kuwalea watoto wake.

“Nikisaidiwa fedha nitafanya biashara au nikitafutiwa kazi nitafanya, maisha haya ya sasa ni hatari kwani ninaweza kuambulia kupata Ukimwi na wanangu bado wadogo wanahitaji malezi yangu hasa ukiangalia hawana baba. Nikiupata Ukimwi wanangu watalelewa na nani? Hawana ndugu wanayemtambua kama kwetu Same hawatakiwi kuonekana.”


Na Pamela Chilongola wa Gazeti la Mwananch. Habari hii imenigusa sana na nimeona si vibaya nikiweka hapa kibarazani.

Sunday, June 13, 2010

Iweje tujitie kitanzi wenyewe?

Watu tuliojitambua tunaishi leo sio jana ambayo imeshapita na sio kesho ambayo sio yetu. Ishi leo sasa hivi ndio yako. Je? Ulishawahi kujiuliza mapungufu ya Dini juu ya mapenzi? Wakrito, NDOA YA MILELE. Padre au Askofu anajua wanaume na wake wakorofi. Waislam nao eti kuoa wake 4 ruksa. Wanajua wivu au ubabe ambao umetawala katika ndoa? Kuwa huru usitishwe na sheria hewa za dini. Usifujwe kwenye ndoa na mumeo au mkeo kwa kisingizio cha dini, ishi huru. Dini ni maandiko tu. Hata wewe kuandika unaweza. NAWATAKIENI DOMINIKA NJEMA WOTE

Saturday, June 12, 2010

ACHA MASARAU!!!


Mimi sipendi masarau

Mmasai alikwenda maeneo ya Jolly Club jijini Dar, na kuopoa changu (Wasichana wanaojiuza) na kuondoka naye hadi Kinondoni kwenye Guest House aliyofikia.

Lakini kabla ya kuingia chumbani kujivinjari na binti yule aliamua kupata bia mbili tatu kabla ya kujivinjari na kimwana.


Waliagiza Bia na nyama choma na wakati wanaendelea kunywa na kula nyama choma yule binti akambusu (Kiss) Mmasai kwenye shavu la kulia.


Mmasai: We ndito acha hiyo…….

Binti: Akambusu tena shavu la kushoto

Mmasai: (Akifoka kwa hasira) Aaagh….. nimesema acha hiyo wewe haisikii…

Binti: (Akiongea kwa kulegeza sauti kimahaba) Kwani vipi sweetie….

Mmasai: (Akafoka kwa hasira) Nimesema acha hiyo masarau lakini wewe bado nafanya hiyo masarau yako….eh!

Binti: Basi Honey, naomba yaishe kama hutaki….

Mmasai: (Akinyanyuka kwa hasira) naona wewe umesidi masarau yako.

Mmasai akatoka nje kumuita mlinzi wa ile Guest na kuja naye pale kwenye meza waliyokuwa wamekaa na yule binti.

Mmasai: Askari, mimi nimekuja na huyu binti hapa, lakini yeye ameanza masarau. Mara ya kwansa alinisonya kipande ya huku (akionyesha shavu la kulia) nikamwambia acha masarau, lakini yeye akaendele na masarau yake kwa kunisonya kipande ingine ya huku ( akionyesha shavu la kushoto) nikamwambia bado tu naendelea na masarau yako, lakini yeye akainiita Fisi (Yaani alipoitwa Sweetie) nikamwambia mimi sitaki hiyo maneno lakini tena ikaniita Nyani (Yaani alipoitwa Honey) sasa askari hiyo sio masarau?

Mimi nasema hivi, nataka utoe hii ndito nje, sitaki kuona mtu mwenye masarau.


Watu waliokuwa karibu walivunjika mbavu kwa kicheko………..

Habari hii nimetumiwa na rafiki toka nyumbani Tanzania na nikaona niiweke hapa ili isomwe
nanyi wenzangu pia. JUMAMOSI NJEMA JAMANI!!!

Friday, June 11, 2010

Picha ya wiki hii:- Je? unamfahamu huyu aliye kwenye picha hii??

Je? hii picha ilipigwa mwaka gani ?
Na napenda kuwatakieni wote Ijumaa njema na tutaonana wakati mwingine!!

Thursday, June 10, 2010

Jinsi lugha inavyotatanisha ukiwa mgeni!!!

Ngoja leo niwasimulia kajambo:- Siku moja nikiwa nimekaa nimetulia nikijisomea kitabu changu, mara akatoka kijana mdogo akinitazamana kwa huruma. Akaniambia NAAZIMA choo, nikabaki mdomo wazi , na nikamuuliza unaazima choo utanirudishia lini? Naye akabaki mdomo wazi huku akijifinyafinya kuonyesha amezidiwa sana na haja kubwa.

Nikaendelea kumwuuliza kwa nini asiingie ndani na kutumia choo na kuondokka ni lazima AKIAZIME? Akaniambia ndo alikuwa na maana hiyo kuwa ana-OMBA atumie. Nikaona hiii ni kaazi kweli kweli katika kuelewana. Sasa hapa ninachoomba kwa wewe msomaji uniambia kama nimekosea maana kwa ueleo wangu neno haya maana mimi nimeelewa hivi:- KU-AZIMA maana yake utarudisha tena na neno KU-OMBA maana huhitaji kurudisha. Swali:- Je kuna maana nyingine?

Tuesday, June 8, 2010

UPENDO GANI HUU WA MAJI KUPWA MAJI KUJAA!!

Kwa kawaida sisi wanaadamu huwa hatuna hisia za aina moja wakati wote... kuna wakati tunakuwa na hisia za upendo kwa wake au waume zetu na wakati mwingine hujikuta tukiwa na hisia za chuki bila sababu. Kama vile bahari klupwa na kujaa , basi ndivyo zilivyo hisia zetu-

Je? twawezaje kupunguza hisia hizi za chuki kwa wenza wetu? Nasema kupunguza kwa sababu ni vigumu kuziondoa kabisa. Sisi tumeumbwa na hasira, hata Yesu pia alikuwa na hasira, na ndio maana alimwaga bidhaa za wale wajasiriamali kule hekaluni. Kwa sababu waligeuza hekalu lla kuabudia kuwa pango la wachuuzi. Je? tutawezaje kujiepusha na hasira?

Sunday, June 6, 2010

JUMAPILI NJEMA KWA WOTE NA UJUMBE NI HUU UPITIOA KWA WIMBO HUU WA ZAKAYO!!!



Wimbo huu nadhani unaimbwa kwa kimasai nimeusikiliza mara nyingi na nikaona ni vema kulinukuu hili neno:-
Mtakatifu Luka 19: 1-10
”Naye alipoingia Yeriko alipita katikati yake. Na tazama, palikuwa na mtu, jina lake Zakayo, mkubwa mmoja katika watoza ushuru, naye ni tajiri. Huyu alikuwa akitafuta kumwona Yesu ni mtu wa namna gani, asiweze kwa sababu ya umati wa watu, maana ni mfupi wa kimo. Akatangulia mbio, akapanda juu ya mbuyu apate kumwona , kwa kuwa atakuja kuipitia njia ile. Na Yesu, alipofika mahali pale, alitazama juu akamwambia, Zakayo, shuka upesi, kwa kuwa leo imenipasa kushinda nyumbani mwako. Akafanya hharaka, akashuka, akamkaribisha kwa furaha. Hata watu walipoona, walinungúnika wote, wakisema, Ameingia kukaa kwa mtu mwenye dhambi. Zakayo akasimama, akamwambia Bwana, Tazama, Bwana nusu ya mali yangu nawapa maskini, na ikiwa nimenyang´nya mtu kitu kwa hila namrudishia mara nne. Yesu akamwambia, Leo wokovu umefika nyumbani humu, kwa sababu huyu naye ni mwana wa Ibrahimu. Kwa kuwa mwana wa Adamu alikuja kutafuta na kuokoa kile kilichopotea.”
TUMSIFU YESU KRISTO MILELE AMINA. JUMAPILI NJEMA WANDUGU!!!

Saturday, June 5, 2010

Sweden yaibana zaidi Tanzania

BALOZI wa Sweden aliyememaliza muda wake, Staffan Herrstrom

BALOZI wa Sweden aliyememaliza muda wake, Staffan Herrstrom jana alitoa hotuba kali ya kuitaka serikali kutekeleza ahadi inazozitoa, ikiwemo kuwafikisha mahakamani watuhumiwa wote wa kesi kubwa za rushwa na kuondokana na utamaduni wa kulipana posho.

"(Serikali) isiache hata jiwe moja juu ya jiwe jingine," ameeleza balozi huyo katika hotuba yake iliyokuwa na ujumbe mzito kwa serikali wakati wa hafla ya maadhimisho ya siku ya Sweden ambayo ilitumiwa kumuaga.

Katika hotuba hiyo kali inayosisitiza msimamo wa Sweden katika vita dhidi ya rushwa, Balozi na Herrstrom alitaja mambo mawili makubwa muhimu katika kuondoa umaskini ambayo yanatakiwa kushughulikiwa kuwa ni utekelezaji wa maamuzi yaliyokwishafikiwa na sera pamoja na haki za watoto.

Hotuba yake imekuja zaidi ya wiki moja baada ya Sweden na nchi nyingine wahisani kutangaza kuzuia theluthi moja ya mchango wao kwenye bajeti kuu ya serikali ya Tanzania, kufuatia kutoridhishwa na kasi ya utekelezaji wa masuala kadhaa, ikiwa ni pamoja na kubadilisha mfumo wa usimamizi wa fedha za umma na utekelezaji wa mazimio yaliyofikiwa wakati wa kusaini makubaliano ya kutoa fedha hizo.

Nchi hizo zilitangaza kuwa zimezuia Sh297 bilioni kwenye bajeti kuu ya serikali ya mwaka 2010/11 na kwamba, zinaendelea na mazungumzo na serikali, huku zikisema kuwa iwapo serikali haitatekeleza ahadi zake fedha hizo ambazo ni za walipa kodi wa nchi hizo zitahamishiwa kwa taasisi zisizo za kiserikali ili ziendelee kusaidia katika kupunguza umaskini.

Jana Balozi Herrtsron, ambaye nchi yake inachangia dola 45 milioni za Marekani kwenye bajeti hiyo, alikuwa mkali zaidi.

"Tekelezeni nia iliyoelezwa ya kushughulikia kesi zote kubwa za rushwa mkihakikisha kuwa watuhumiwa wote wa rushwa wanafikishwa mahakamani na kesi zote zinatolewa maamuzi muafaka. Iwe ni moja au zote, bila ya kuacha jiwe moja juu ya jingine," alisema balozi huyo katika hafla hiyo.

Kauli hiyo imetolewa wakati vita dhidi ya rushwa ikionekana kupoa, huku watuhumiwa wa rushwa kubwa wakianza kujitokeza hadharani baada ya kupotea kwa kipindi kirefu kutokana na kuelekezewa tuhuma kali kwa takriban miaka miwili.

Baada ya wahisani kuzuia fedha kwa mara ya kwanza takriban miaka mitatu iliyopita, serikali iliamka na kuwafikisha mahakamani watu wanaotuhumiwa kuiba fedha kwenye Akaunti ya Malipo ya Madeni ya Nje (EPA), kushughulikia ubadhirifu wa fedha za walipa kodi kwenye Benki Kuu ya Tanzania (BoT), kwa kuwafikisha mahakamani watuhumiwa na kushughulikia tuhuma za rushwa kwenye wizara iliyosababisha mawaziri wawili wa zamani kufikishwa mahakamani.

Lakini hatua hizo za serikali zimeonekana kutowagusa watuhumiwa wakubwa hasa kwenye suala la EPA, ambalo baadhi ya watuhumiwa walipata msamaha wa Rais baada ya kutakiwa kurejesha fedha hizo kabla ya Novemba mwaka 2008, huku tuhuma nzito kama za Meremeta Gold zikiwa hazijashughulikiwa kisheria.

Hata hivyo, vita hiyo inaonekana kupungua nguvu na wahisani wameonyesha kuwa na wasiwasi na mwenendo huo, ikiwemo Sweden.

Balozi Herrstrom, ambaye mapema wiki hii alizungumzia ugoigoi huo wa serikali katika kutekeleza ahadi zake, alizungumzia pia uhuru wa habari katika hotuba hiyo.

"Tekelezeni ahadi zote mlizotoa za kupata njia ya kisasa itakayohakikisha haki ya kupata habari inakuwepo; kuwepo kwa uhuru wa vyombo vya habari na hivyo kuwa na uwazi na uwajibikaji, kutekeleza mabadiliko sita muhimu yanayotakiwa kwa haraka sana, kama mabadiliko katika serikali za mitaa na usimamizi wa fedha za umma" alisisitiza balozi huyo.

"Tekelezeni azma mliyoeleza ya kuachana na utamaduni wa kulipana posho ambao ni hatari sana katika suala la ufanisi na utawala."

Balozi huyo pia ameitaka serikali kuwasilisha muswada wa Sheria ya Watoto na kusema: "Tafadhali tekelezeni ahadi mliyoweka ya kuruhusu wanafunzi wanaopata mimba ambao wanakuwa wazazi mapema, kuendelea na shule badala ya kutimuliwa hivyo kunyimwa haki yao ya kupata elimu".

Alisema jambo la pili muhimu ni haki za watoto, akitaka walindwe, wasikilizwe na kupewa uwezo na kutaka adhabu kali dhidi ya watoto ziondolewe.

"Tuweke ahadi ya pamoja kwa niaba ya watoto wa nchi hii. Watoto wote wa Tanzania Bara na Zanzibar wasipigwe na tuhakikishe kuwa Zanzibar inakuwa na sheria nzuri ya haki za watoto kabla ya uchaguzi mkuu," alisema.

Hotuba yake ya jana haitofautiani sana na hotuba aliyoitoa mwezi mmoja uliopita katika mkutano wa kitaifa wa kupambana na rushwa ulioandaliwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa(Takukuru), jijini Dar es Salaam.

Katika mkutano huo, Balozi Herrstrom alisema hakuna nafasi ya kupunguza kasi katika vita dhidi ya rushwa na kuitaka serikali kumsikiliza Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu (CAG) na kwamba ifanyie kazi mambo yote yanayoibuliwa na ofisi hiyo katika mwaka uliopita na kutekeleza mapendekezo yake.

Mwandishi Wetu-Gazeti la Mwananchi


Friday, June 4, 2010

UMASIKINI SAWA, LAKINI KWA NINI TUWACHUKIE WALIOFANIKIWA?


Hatuna haja ya kuchukia hali zetu
Ni kitu gani kinachotofautisha binadamu yaani kutoka binadamu mmoja hadi mwingine? Ni wazi ni vitu vingi sana kiasi kwamba haiwezekani kwa kuvitaja vyote na kuvimaliza katika nafasi hii ndogo. Lakini bila shaka inatosha kusema kwamba kama binadamu hatuwezi kulingana.
Kuna miongoni mwetu ambao tuna mafanikio makubwa kimaisha na wengine tukiwa katika kukubali ugumu mkubwa kimaisha. Katika hali hizo mbili kila mmoja wetu ana namna anayoichukulia hali yake. Kati yetu hufurahia na na kuringia mafanikio yetu huku tukitaka zaidi na zaidi wakati wengine tukichukia na kujichukia kutokana na ulitima tuliokuwa nao.

Hebu tujiulize sisi ambao tunaishi katika ulitima au ufukara huwa tunajitazama vipi, huwa tunaichukulia vipi hali yetu na kuiamulia vipi? Tukijiuliza kwa makini tutagundua kwamba kwa sehemu kubwa huwa tunaichukia hali yetu ya ulitima au ufukara. Kuichukia hali hii siyo kuichukia kwa kwa kufanya juhudi kuiondoa, bali ni kuichukia kwa kutafuta ‘mchawi’ ambaye tunadhani ndiye anayetusababishia hali hii.

Kwa kawaida kwa kuzingatia kanuni za mfumo wa mawazo ya binadamu ni kwamba tunapochukia hali zetu ina maana pia kuwa tunajichukia wenyewe ingawa huwa hatujui kwamba tunajichukia. Kwa kuwa tunajichukia wenyewe siyo rahisi kubaini kwamba mitazamo yetu kuhusu hali zetu ni kioo cha sisi na udhaifu wetu. Tunapotafuta mchawi wa hali zetu huwa tunafanya hivyo kwa sababu ya udhaifu wetu ambao kamwe hatuko tayari kuukubali.

Inapotokea tukaanza kuchukia ufukara tulio nao kwa njia ya kulalamika na kulaani ama kukata tamaa tukafikia mahali pa kujidharau na kujibeza na huku tukiamini kwamba hatuna thamani ndipo ambapo hufikia mahali pa kuanza kuwachukia wale wote ambao wana mafanikio maishani. Tunawachukia hao kwa kudhani kwamba wao wana thamani kubwa kuliko sisi kwa hiyo wanatubeza. Tunawachukia hawa kwa njia ya kujaribu kupunguza ugigili tulionao kwa hali zetu.

Tunajisikia ahueni kuwachukia na kuwasema vibaya huku tukijaribu kurusha ‘dua za kuku’ ambazo ni wazo haziwezi kuwapata kwa sababu hawako kama sisi tunavyowatazama. Kile tunachokiona kwao ndiyo udhaifu wetu tukiona kujichukia kwetu kupitia kwao kwa sababu kama binadamu tunajipenda sana na hivyo kuwa vigumu kwetu kujichukia.

Ni kweli kwamba wengi wetu tusio na uwezo kamili ambao ni mafukara, wengi wetu tusio na elimu, tusiojua au kutumia vipaji vyetu huwa tunawachukia wale wenye uwezo waliosoma na wenye vipaji au wanaojua kuvitumia. Chuki hizi huwa tunazitoa kwa kutamani kwetu kuona wakianguka kujaribu kuwaharibia majina kufurahi wanapoingia kwenye matatizo na kuwapiga vita ya moja kwa moja..

Siyo kweli kwamba ufukara wetu ndiyo unatufanya kuwa na tabia hiyo, bali namna tunavyoutazama na kuutafsiri ufukara huo. Kama tunaamini kwamba ufukara wetu siyo jambo la ajabu na wala hautuondolei thamani yetu na kuwaona waliofanikiwa kama watu sawa na sisi hatuwezi kuwajengea chuki na kuwapiga vita. Kama tukiuchukulia ufukara wetu kama jambo la kawaida na la muda mfupi ambalo litarekebishwa na kuondoka siku fulani hatuwezi kuwachukia waliofanikiwa.

Badala yake tutawatazama kama kioo cha kuonea udhaifu wetu na kuwakubali. Tutawatazama na kujiuliza ni kwa vipi wao waweze, tutajaribu kuiga au kuuliza mbinu zao za mafanikio tutawachukulia kama mfano hai wa uwezo wa binadamu kupata akitakacho maishani na tutawapenda kwa sababu hatuna sababu ya kuwachukia. Kwa kufanya hivyo nasi tutajikuta tukipambana na maisha ili kutoka katika hali tulionayo. Tutafanya hivyo kwa sababu tutakuwa tumekubali kujifunza kutoka kwao.

Lakini kama hatutakuwa tumewatazama kwa njia hiyo na badala yake kuwatazama kinyume tutajikuta tukiwajengea chuki tukiwaona wanaringa tukiwaona ni wajuaji na kuwaona wakiwa na kila kasoro. Chuki ni kama tulivyobainisha ni kujichukia kwetu kwa kushindwa kwetu kujua namna ya kusogea hivyo kwa kujichukia kupitia kwao tunapata ridhiko na kuendelea kubaki katika hali zetu. Tunabaki katika hali zetu kwa sababu hutujifunzi kutoka kwao udhaifu wetu na kuukubali bali tunajifunza uongo kwamba watu hao ndiyo dhaifu au wenye matatizo na kasoro.

Jaribu kufanya uchunguzi au utafiti utagundua kwamba watu wote fukara wenye chuki dhidi ya wale waliofanikiwa kamwe maisha yao hayawezi kubadilika hadi wanakwenda kaburini. Hayawezi kubadilika kwa sababu badala ya kujifunza na kuujua udhaifu wao kupitia kwa wengine waliofanikiwa wao hujifunza kuukimbia udhaifu wao kupitia kwa hao waliofanikiwa.

Ni vizuri tukawaambia wale ambao wana hali mbaya kimapato kwamba hiyo siyo hali yao. Hakuna binadamu ambaye ameandikiwa kuwa kama alivyo leo bali kila mmoja kwa sehemu yake kubwa huamua mwenyewe awe vipi. Tunapotaka kujitoa katika ulitima tuliyomo inatubidi tuwe na ruwaza nzuri ya kufikiri kama tunaamini kwamba ufukara wetu ni kwa sababu tumeandikiwa hivyo, ni kwa sababu tumelogwa ni kwa sababu hutukusoma ni kwa sababu hii au ile hivyo hatuwezi kutoka humo kamwe hatutatoka na kuendelea kuwachukia wanao vuka vizingiti vya ufukara.

Lakini tukiamua kwamba wanaopata wamepata kutokana na kuamua kwao kupata na hivyo hata sisi tunaweza kupata kwa kukagua njia na mbinu walizotumia ni wazi hatuwezi kujichukia na hivyo kuwachukia hao bali tutajifurahia na kujifunza mengi kutoka kwao na ni dhahiri tutakuja kuvua koti la ufukara..
Makala hii nimeipata kutoka kwa kaka Shaban Kaluse na nimeona si vibaya kama nikiweka hapa Maisha na Mafanikio kwani wote tuna lengo moja. Kwa kumsoma kaka huyu zaidi ingia hapa.

Thursday, June 3, 2010

HONGERA KWA SIKU YA KUZALIWA KWAKO ERIK!!

Imetimia miaka 10 leo tangu kijana wetu Erik azaliwe. Ni kijana ambaye anapenda sana kusoma, kuandika, kucheza mpira wa miguu (football), kuendesha baiskel na marafiki mountain bike pia anapenda kupiga aina ya mziki wa fidla au (Violin. ) Twakuomba Mwenywezi Mungu uwe /uzidi kumbariki kijana wetu Erik azidi kuwa kama na hekima . Na pia twakoomba uzidi kutupa sisi wazazi/walezi nguvu ya kumlea ili azidi kuwa kijana mwema na mwenye busara. ERIK HONGERA SANA KWA SIKU YA KUZALIWA.

Wednesday, June 2, 2010

SWALI LA LEO:- HIVI NI KWELI HAPA DUNIANI MUNGU AMETUUMBA WAWILI WAWILI??

Mama Mubelwa /Mzee wa Changamoto au hapa
changamotoyetu.blogspot.comDada Agness Andersson kiduchu.blogspot.com
Mwenzenu nimechoka kufananisha peke yangu na leo nimeona niwashirikishe wenzangu au sijui ndo uzee unaniingia? Je? Hawa watu kweli hawajafanana?

Tuesday, June 1, 2010

‘Housigeli’ anataka kuniharibia ndoa

habari yako. Nategemea mzima wa afya na hutasita kunisaidia kunipa ushauri unaonifaa. Mimi ni mwanamke mwenye watoto wawili. Tangu nimeolewa miaka sita iliyopita, nimekuwa na msichana wangu wa kazi mmoja ambaye nimempenda sana hasa kwa kuwalea vizuri watoto wangu na kuwa mwepesi wa kazi. Kutokana na kuishi vizuri na ‘housigeli’ huyu, amekuwa kama mtoto wa nyumbani na hata ndugu zangu na wa mume wangu wanampenda sana na wamemzoea kupita kiasi.

Tatizo hili la kuwazoea ndugu wa mume wangu sasa naona linataka kuharibu ndoa yangu kwani huyu msichana ameanza tabia mbaya na amemweleza mkwe wangu kuwa mimi situlii nyumbani na sina muda wa kumshughulikia mume wangu kwani kazi zote anafanya yeye, mimi kazi yangu kusafiri na kushinda kazini. Huyu mama mkwe wangu kusikia hayo, amekuja juu na sasa anamshinikiza mume wangu aniache eti nashindwa kuhudumia nyumba na badala yake amuoe ‘housigeli’. Mume wangu ameshtuka na amenieleza kila kitu hali iliyonikasirisha sana.

Sasa naomba ushauri wako kwani mama mkwe bado yupo kwangu, je, nifanyeje kabla hajaondoka kurudi kwake? Mama Kelvin Tabata, Dar es Salaam. Mama Kelvin pole sana kwani inaonekana huyo mama mkwe wako hajaelimika vya kutosha. Uzuri wa mwanamke haupimwi kwa kazi za nyumbani pekee, bali kuna mambo mengi na mkwe wako anapaswa kutambua kuwa wewe unafanya kazi hivyo huwezi kukaa nyumbani muda wote na ndiyo sababu ukatafuta msaidizi.

Lakini pia ni vyema ukiwa nyumbani ufanye kazi zilizopo ikiwamo kumpikia mumeo na kumhudumia ipasavyo. Usiwe na hasira za haraka kwa msichana wako wa kazi kwani inawezekana aliulizwa kimtego naye akajibu vizuri tu lakini mkweo akawasilisha kwa mumeo vibaya. Nadhani mumeo pia anapaswa amweleze mama yake kwa upole kuwa wewe unafanya kazi na huwezi kufanya kazi zote za nyumbani. Pia amweleze kuwa huyo msichana wa kazi kamwe hawezi kuwa mke wa mtoto wake.

Naamini mtoto wake akimwelimisha na akawa na msimamo, mama mkwe wako ataelewa au hata kama hataelewa, atashindwa kuendelea kusisitiza anachotaka. Ni vyema pia ukakaa na msichana wako na kumhoji ilikuwaje hata wakazungumza hayo na mkweo na ukiona kama alichokonolewa basi mtahadharishe akae mbali na mama mkwe na asiwe mwepesi kueleza mambo ya ndani ya nyumba kwa mkweo.

Hata hivyo fanya uchunguzi wako kwa siri na ukiona msichana wako anapalilia ili aolewe yeye, basi ni vyema ukatafuta msichana mwingine wa kazi na huyo kumwondoa ili asije kuharibu ndoa yako. Haina haja kugombana na mtu yoyote kwani naamini huyo mkweo ataondoka na nyinyi mtaendelea na maisha yenu. Pia jifunze kuvumilia kwani wakwe wengine uelewa wao ni mdogo.

Habari hii nimeipata Jamii Forum nimeona si vibaya kama tukijadili kwa pamoja!!