Wednesday, June 30, 2010

Kinamama Kilindi wakiri kuwakeketa watoto wa kike

WANAWAKE wa jamii ya wamasai wilayani Kilindi mkoani Tanga wameeleza waziwazi kuwa wimbi la ukeketaji wasichana bado linaendelea katika jamii hiyo ya wafugaji, licha ya kampeni mbalimbali zinazofanywa na mashirika mbalimbali kukomesha shughuli hiyo.
Kina mama hao, walisema pamoja na kuendelea na vitendo hivyo vya ukeketaji kwa usiri mkubwa, pia wameeleza wamekuwa wakiwauguza mabinti zao nyumbani wanapopata madhara sehemu za siri kutokana na majeraha baada ya kukeketwa na wakati mwingine kupoteza maisha.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti wakati wa mkutano wa hadhara ulioshirikisha marika na jinsia zote katika eneo la Shule ya Msingi Mbogoi Kata ya Mkindi wilayani hapa juzi,kina mama hao, walisema wanaendelea na ukeketaji kwa madai kuwa hawajapata elimu ya kujua madhara yake.
Mimi tangu nianze kuwazalisha wazazi tangu miaka mingi iliyopita sijawahi kuona mwanamke ambaye hajakeketwa. Sisi tulifikiri kuwa duniani hakuna mwanamke ambaye hakeketwi na tuliona ni muhimu kwa kuwa ni kudumisha mila zetu. Lakini pia tukielimishwa zaidi tutaacha ukeketaji,†alisema Yosephat Taringo.
Naye Wiliam Tangoro (65) katika mkutano huo, alisema wanashukuru Shirika la AMREF kuchukua jukumu la kuwaelimisha wafugaji ili kuepuka mila hizo, ambazo sasa zimepitwa na wakati.
“Sisi tunalishukuru shirika hili la AMREF kwa kutujali na kutuelimisha ili tuachane na mila hii ambayo sasa elimu hiyo, imeanza kuenea sehemu mbalimbali za makazi yetu wafugaji,†alisema Tangono.
Mafunzo hayo, yanayofanyika usiku kwa njia ya mijadala na sinema na kushirikisha watu wa rika zote na jinsia zote ikiongozwa na Afisa Utamaduni wa wilaya hiyo, Adelina Ndumbaro na yamekuwa yakivutia watu wengi huku wachangiaji wakielezea undani wa maisha yao kwa uwazi zaidi.

Habari hii imeandikwa na Hussein Semdoe,Kilindi iliandikwa 25/3/2010 nimeona si vibaya kama wengi tukiisoma kupitia kibaraza hiki cha Maisha na Mafanikio.

7 comments:

o'Wambura Ng'wanambiti! said...

kazi ipo. pamoja na ile sheria ya SOSPA lakini mmmh!

EDNA said...

Mweeeh hawa watu wataelimika lini?

Anonymous said...

Jamani lini hawa watu watajua kama hivi wanavyofanya sivyo

Anonymous said...

Lakini mboa wanume nao wanakeketwa lakini watu hawapigi kelele....LOL

kamala Lutatinisibwa Lutabasibwa said...

swali la anony wa pili limenichekesha.

karibia wanaume wote tuliochangia hapa tumekeketwa ila hatulalamiki sisi, baba zetu au hata mama zetu kama sio wake zetu!!

Penina Simon said...

Duh!! hawa wako kama sisi wakurya, kukeketwa sidhani kama kutaisha hata serikari ipige marufuku vp haiwezi kuondoa hii mila, kwn hata baadhi ya wanawake wa makabila mengine hujikuta wamekeketwa bila kujua hasa wakati wa kujifungua. Labda neema ya Mungu itushukie.

Anonymous said...

Amref inafanya kazi kubwa sana hapa kilindi,tuungane nao katika level ya binafsi,familia na jamii pia ili kuleta mabadiliko.Kweli ukeketaji ni kinyume na haki za binadamu.