Tuesday, August 31, 2010

Huko mashuleni walimu wana kazi kubwa sana!!


Kaazi kwelikweli sijui ipitishwe sheria ya kwamba masomo yote yafundishwa kwa lugha zetu za asili kama vile kingoni, kisukuma, kibena kimatengo?? nk, nk. Katuni hii nimeipata gonga hapa kwa kusoma zaidi katuni nyingine. Nimeona tuufunge/tuumalize mwezi huu kwa hili. Walimu kwa kweli kazi mnayo.

Monday, August 30, 2010

Umejiuliza kwa nini mwanafunzi wa kike anakutaka?

Wanafunzi wasichana wakiwa katika picha ya pamoja

Wapo wanaofanya ngono kwa lengo la kusambaza magonjwa waliyo nayo. Nakumbuka niliwahi kusoma habari moja kuhusu mwanafunzi mmoja wa chuo kikuu fulani aliyetenmbea na wanaume zaidi ya 100 kwa lengo tu la kuwaambukiza ugonjwa wa Ukimwi
Umejiuliza kwa nini wanafunzi wa kike au wanawake wanafanya ngono? Inawezekana kusiwepo na jibu la moja kwa moja na kwa wewe msomaji wa makala hii labda unaweza kutaja sababu kadhaa kama vile kutafuta watoto, kujiridhisha nafsi zao na hata ishara kuwa wanawapenda wanaofanya nao tendo hilo. Mwandishi Wetu Christine Chacha anafafanua zaidi.
UNAWEZA kuendelea kutaja sababu kadhaa unazozijua lakini ukweli ni huu, wanawake wana sababu nyingi sana zinazowasukuma kufanya ngono tena nyingine unaweza usizijue.
Kwa mujibu wa kitabu kilichochapishwa hivi karibuni kiitwacho " Why Women Have Sex kuna sababu 237 zinazowafanya wanawake kuvutiwa na tendo hili.
Hivi ndivyo wanavyosema wanasaikolojia wawili Cindy Meston na Davis Buss walioandika kitabu hiki kilichopata umaarufu mkubwa wa kupendwa na watu wengi duniani.
Unaweza ukashangaa lakini huu ndio ukweli, sababu nyingi zinazotajwa na wanawake zaidi ya 1000 waliohojiwa hazihusiani kabisa na kitu kinachoitwa mapenzi na kwa zile zinazohusiana basi si kwa uhusiano wa ukaribu.
Kwangu, habari hii niliipokea kwa mstuko kwa kuwa najua hakuna hata mmoja asiyezungumzia kwa nini tumekuwa tukifanya ngono.
Nilichokuja kukimaizi mwishoni ni kwamba sababu zinazowasukuma wanawake kujihusisha na tendo hili zinatofautiana kwa sababu za kiumri na nyakati.
Nitoe mfano kwa wanafunzi wa shule za sekondari hasa ile ya juu, wengi wetu tuliweza kufanya tendo hili kimajaribio, tulitaka tudadisi ladha ya jambo hili hatimaye tukapoteza usichana wetu.
Kwa ngazi ya chuo kikuu, ngono haikuwa tena mchezo wa majaribio bali kitu tofauti, kipi hicho? Wengi tulifaya kama mojawapo ya njia za kujipa raha na kila mmoja alikuwa akifanya.
Muulize mwanachuo yeyote wa kike hatosita kukwambia kuwa njia rahisi zaidi ya kumpata mwanamume basi zungumza naye kuhusu ngono. Huwezi kufeli kama utamkabili kwa kutumia mtego huu. Wapo hata waliokuwa wakilazimika kufanya ngono ili wawe karibu na wanaume ili hatimaye waje kupata alama nzuri katika masomo.
Leo ninapohudhuria katika sherehe za kuwafunda wanawake wanaoolewa maarufu kama kitchen party, ngono huku imechukua sura nyingine. Wanaotarajia kuolewa wanaambiwa ngono ni sawa na kazi ama jukumu lao muhimu pale wanapokuwa kwa waume zao. Na lazima jukumu hili walikamilishe ipasavyo wanapokuwa katika maisha ya ndoa.
Tena jukumu hili ni maalum kwa ajili ya kumfurahisha mume na ilivyo wanatakiwa walifanye kiustadi mkubwa ili wawavutie waume zao ili wasipate mawazo ya kwenda nje kutafuta wanawake wazuri zaidi katika tendo hili. Hapa ngono hailengi kumpa raha mwanamke bali mwanaume.
Kwa mujibu wa kitabu nilichokitaja hapo awali, asilimia 84 ya wanawake walisema wanafanya ngono kuwaridhisha wanaume zao na si kama wanafurahia kwa kiwango kikubwa kufanya hivyo.
Mpaka hapa nikawa hoi, ndipo niliopoamua kutafiti hapa mkoani Dar es Salaama nikitaka kujua kwa nini wanawake wanajihusisha na tendo la ngono.
Visasi
Kumbe kulipiza kisasi kunaweza kuwa sababu ya wanawake kujiingiza katika tendo la ngono hasa pale wanaposalitiwa na wapenzi wao. Wengine hutaka tu kuwarusha roho wanaume zao kwa kuwapa hisia kali za wivu.
Martha Peter (29) anayefanya kazi za usanifu kurasa ni mfano mzuri wa wanawake walioamua kufanya ngono kulipiza kisasi baada ya kusalitiwa na wapenzi wao waliowachunuku kwa kiwango kikubwa.
"Nilitaka alipe kwa mabaya aliyonitendea, nilitaka nimkabili katika njia ambayo ingemuumiza sana,’" anasema
Nini alichokifanya kumuumiza mpenzi wake wa zamani? Anasema, "Nilijua ukaribu aliokuwa nao na kaka yake wa kufikia hivyo nikatembea naye, kilichotokea ni vurumai kubwa katika familia yao, baadaye nikaachana na wote."
Kusambaza magonjwa
Wapo wanaofanya ngono kwa lengo la kusambaza magonjwa waliyo nayo. Nakumbuka niliwahi kusoma habari moja kuhusu mwanafunzi mmoja wa chuo kikuu fulani aliyetenmbea na wanaume zaidi ya 100 kwa lengo tu la kuwaambukiza ugonjwa wa Ukimwi.
Alipoulizwa alisema alifanya hivyo kulipiza kisasi baada ya yeye kuambukizwa na mpenzi wake wa kiume waliokuwa wakisoma pamoja chuoni.
Ngono kama njia ya kujifurahisha
Leo wanawake wanakataa ule usemi eti kwa sababu za kijinsia wao hufanya ngono kwa kuwa tu wanawapenda wapenzi wao na kwamba wanaume wao ndio pekee wanaolichukulia tendo hilo kama njia ya kujipa raha.
Ilivyo hata wanawake nao wanapenda kufanya ngono kwa kuwa wanaburudika kufanya hivyo. Tena kwa wanawake vijana hii ni njia nzuri ya kuburudika na kujiliwaza kimwili. Kama ilivyo kwa wanaume, hii nayo ni raha na wala hawajuti kufanya hivyo.
" Nafanya ngono kwa sababu nataka kufanya hivyo, ngono inaburudisha na kusisimua," anasema Bella Roman, Meneja wa Fedha wa kampuni moja nchini.Anaongeza kwa kusema:
"Tupo katika jamii huru, sina sababu nyingine ya kufanya ngono.
Kwa nini nami nisifanye nikafurahi kama wanaume."
Roman (34) anashangaa kwa nini jamii inakubali wanaume kupenda ngono lakini ikitokea kwa wanawake wanashukiwa kwa sababu kadhaa kama vile kuitwa makahaba. Anauita huu kuwa ni mtazamo wa unaopaliliwa na hisia za mfumo dume.
“Inawafanya wanawake kujihisi vibaya pale wanapotaka kutimiza matakwa yao ya kufanya ngono. Naweza kufanya ngono kama kujiridhisha moyoni na wakati huo huo nisiwe kahaba, jamii lazima ilikubali hili,†anatetea mtazamo wake.
Roman anakiri kuwa ana marafiki kadhaa wa kiume na wote anafanya nao ngono pale anapojisikia. Na wanaume hawa wote wanajua kuwa hawana mkataba naye kwa kuwa anawatumia kutimiza haja zake kingono.
Kumchunga mwanaume
Baadhi ya wanawake akiwemo Aysha anayesoma chuo kikuu wanaamini kuwa ukitaka mwanamume awe wako pekee basi usimyime raha.
"Nimekuwa nikifanya ngono na rafiki yangu wa kiume ili kumweka karibu nami katika uhusiano na asijaribu kunitoroka. Niliamua kufanya hivi baada ya kuomba ushauri kutoka kwa marafiki walioniambia huwezi kumchunga au kummiliki mwanamume kwa kumpenda tu, waliniambia nitumie ngono kumweka katika himaya yangu," anafafanua.
Aysha hana jinsi amekuwa akifanya ngono ili kumridhisha mpenzi wake ambaye hakika ndiye aliyekuwa kinga’ng’anizi wa kutaka kufanya kitendo hicho. Na kwa kuwa hataki kumpoteza Aysha hana jinsi ila kujisalimisha.
Anawakilisha wanawake wengi ambao wamekuwa wakifanya mgono kwa kuwa kwa namna fulani wanalazimishwa na wapenzi wao japo wao wenyewe hawapo tayari.
Wengine huruma huwaponza, kwa nini wasiwape unyumba wanaume wanaowazengea kwa muda mrefu wakiomba kupewa bahati ya kukutana nao kimwili? Kwa wengine hawa wana lao jambo, wanataka ngono na wanaume ili kujua tu ukubwa wa maumbile walioyajaaliwa.
Fanya ngono umsahau wa zamani
Kwa hili Aysha ana haya ya kusema: " Baadhi ya marafiki zangu nami nikiwemo baadhi ya nyakati tunafanya ngono kama njia ya kuwasahau wanaume wa zamani. Sote tunaamini njia bora ya kumsahau mwanamume ni kuanza uhusiano na mwanaume mwingine."
Huna haja ya kuomba ngono inatosha
Baadhi ya watu wanafikiri wanawake wanaofanya ngono kwa lengo la kutaka kupewa chochote ni makahaba, si kweli. Ukweli ni kuwa hata walio katika ndoa na aina nyingine za mahusiano ya kimapenzi wanatumia ngono kama silaha ya kuwalazimisha wapenzi wao wawape yale wanayoyataka.
"Ninapotaka kitu fulani kwa rafiki yangu basi nahakikisha usiku nampa raha zote kisha asubuhi inayofuata namwomba kitu hicho, najua hawezi kusema hapana,’" anasema Anna Tagaru
Hata kwenye maeneo ya kazi wanawake wamekuwa wakitumia njia hii kupata nafasi za juu au kupendelewa na wakubwa.
Kinachofanyika mwanamke anaanza uhusiano na wakubwa katika utawala na hatimaye kama ni mshahara aliotaka au cheo vinaongezeka.
Kwa Tagaru hili kwake si tatizo kama anavyobainisha:"Nawajua marafiki kadhaa wanaotumia ngono kujipatia fedha, si makahaba lakini ni wanawake wanaohakikisha wanapata wanavyovitaka kwa gharama yoyote."
Anasema ana marafiki kadhaa waliotoa miili yao kwa wanaume na kufanikiwa kulipiwa pango katika nyumba wanazoishi, kulipiwa bili za bidhaa na kupewa zawadi za gharama kubwa.
“ Wanaume wanalichulia tendo hili kwa uzito mkubwa na wapo tayari kufanya chochote ili walipate. Kwa kufanya hivi wanawapa wanawake nguvu ya kuitumia ngono kama njia ya kutaka wanayoyataka," anaongeza Tagaru, mama wa mtoto mmoja.
Aidha anasema wakati mwingine anatumia ngono kama njia ya kumpa pongezi au kumwadhibu rafiki yake. Atamfariji kimwili pale anapofanya jambo zuri na pale anapoboronga asahau kama kuna kinachoitwa ngono.
Kuongeza uzao
Hii ni sababu maarufu ya wanawake kufanya ngono na hata dini zimekuwa zikisisitiza hili kuwa mojawapo ya malengo makuu ya kufanya jimai kwa wanandoa.
Hivi ndivyo ilivyo japo leo hii sababu zimekuwa nyingi huku baadhi ya wanawake wa kisasa na wasomi wakitaka tu watoto lakini si kwa kupitia ndoa.
Sikiliza anachosema tena Tagaru"Nilipogundua muda unayoyoma, nilichofanya ni kumtafuta mwanaume anayeweza kunizalisha mtoto mwenye sifa ninazotaka."
Kwa nini tusiwe kama wengine?
Kwa miaka mingi wanaume wamekuwa wakiichukulia ngono kutimiza shauku zao na hata kushindana wenyewe kwa wenyewe kujua nani ana nguvu zaidi. Wapo wanawake nao wanasema kwa nini asiwe kama wanaume?
"Nilipokuwa shuleni, marafiki zangu walikuwa wakizungumzia jinsi walivyotembea na wanaume na kuona uzoefu wa tendo hili, nami nikajaribu," anasema Safia Abdul anayefanya kazi kitengo cha huduma kwa wateja katika kampuni moja ya simu.
Anasema alichotaka ni kuona kwa namna gani angeweza kufika kileleni jambo alilokuwa akilisoma tu vitabuni na hata kuhadithiwa na wenzake.
Alipata alichokitaka kama anavyobainisha: "Nilijaribu kufanya ngono na wanaume kadhaa ili nijaribu kufikia kileleni, nilifanya hivyo hadi nikafanikiwa."
Ushindani wa ngono
Hii inaweza ikawa sababu ngeni lakini ipo na baadhi ya wanawake wanaitumia. Hapa nakusudia kundi la wanawake wanaotoka kwenda kumtafuta mwanaume mmoja mzuri na kisha kila mmoja kufanya awezalo kuhakikisha anafanya naye mapenzi.
Safia anasimulia kuwa hili liliwahi kutokea kazini kwake pale wanawake kadhaa walipokuwa wakimtaka mwanaume mmoja aliyeonekana kuwa mzuri wa umbo na aliyejaaliwa fedha mfukoni. Kila mwanamke akiwemo yeye alimtaka.
“Alikuwa ni ndoto ya kila mwanamke, wote tulitaka kujua atamtongoza nani. Nilipoona kila mtu anamtaka niliamua niwe wa kwanza kumpata kwa gharama yoyote, nilijiuliza hivi kuna njia nyingine ya kumpata zaidi ya ngono?’’
*Makala hii ya Christine Chacha kwa mara ya kwanza ilichapishwa katika gazeti la The Citizen toleo la Novemba 14 ikiwa na kichwa cha habari Why Women Have Sex na imetafsiriwa na Abeid Poyo kwa ajili ya wasomaji wa Kiswahili.
'
HABARI HII NIMEIPATA KATIKA GAZETI LA MWANANCHI.

Sunday, August 29, 2010

Jumapili ya leo, Mke: Furaha ya mume wake!!!

Mwanamke ni furaha ya nyumba!!

Kitabu cha Mithali kinaeleza jinsi mwanamke mkamilifu alivyo, mwanamke aliye furaha na fahari ya mume wake. Mwanamke huyu anafanya kazi zake kwa bidii, ana hekima ni mwaminifu na hutunza kwa uangalifu watu na vitu vya nyumbani. (Mit. 31:10-31)


Kitabu kingine, Hakima ya Yoshua bin Sira, kinamsifu mume mwenye mke wa namna hiyo:-

Apataye mke hujipatia mali iliyo bora, msaidia wa kufaa, na nguzo ya kumtemeza. (Y. b. s. 36: 24).


Yu heri mume aliye na mke mwema kweli,

Mwanamke mwema ni furaha ya mume wake,

Ataishi miaka ya maisha yake katika amani.

Mwanamke mwema ni tunu bora,

Mcha Mungu atatunukiwa huyo watajaa furaraha moyoni hata kama ni maskini au tajiri,

Watakuwa na nyuso zilizochangamka wakati wowote. (Bin Sira 26: 1-4)


Hivi ndivyo mwanamke anavyokusudiwa kuwa kwa mwanaume. Katika maneno yake Mungu kwa nabii Ezekieli, mwanamke huwa; "Furaha ya macho". (Ez. 24-16).

Lakini kwa nabii Hosea, mke huyu aliyekusidiwa kuwa furaha yake, amekuwa chanzo cha mateso ya uchungu wake. (Hos. 2: 4-9) mke huyu hana uaminifu naye huenda kwa wanaume wengine. Amina!!

NAWATAKIENI WOTEEE JUMAPILI HII YA MWISHO YA MWEZI HUU WA NANE IWE NJEMA NA PIA BARAKA ZA MUNGU ZITAWALE NYUMBANI MWAKO/MWENU NA POPOTE PALE U/MTAKAPOKUWA.!!!!



Saturday, August 28, 2010

Kumbukumbu:- Swali la leo nadhani wengi wetu tumecheza michezo hii tulipokuwa watoto au?

Wengi tumecheza michezo hii!!
Ndiyo, Ndiyo!! ndugu zanguni ngoja leo tukumbuke ya kale .. kuna michezo mbalimbali ya utoto ambayo ilikuwa ni burudani, vituko na wakati fulani ilizaa urafiki wa kudumu sana. Michezo ambayo watoto wetu leo hii wanaweza kuona kuwa haina maana tena na wamebakia kucheza na computer, TV nakadhalika.

Kombolela au rede
Kioo kioo
Ukuti ukuti
Kuruka kamba
Hiki na Hoko
Namtafuta rafiki
Tiari bado (mchezo huu ungepigwa marufuku!!!)
Kitambaa changu cheupe
Tukuone maringo yako!
Watoto wangu eh

Upi uliupenda na kwanini?
Kama kuna mchezo nimeusahau unaweza kuutaja.
Jumamosi njema wote!!

Friday, August 27, 2010

Hii imetokea ndani ya daladala jijini Dar jana!!

Wengine walikuwa wamesinzia
Niko kwenye daladala, watu wametulia kila mtu akitafakari mambo yake. Mara kaibuka abiria mmoja akavunja ukimya akauliza." WaTanzania wenzangu naomba kuuliza swali". Abiria wote tukageuka kumwangalia. akajitolea dada mmoja akamjibu, "uliza tu baba" unajua aliuliza swali gani? ha ha haaaaa!!

Akauliza:- Jamani mie binti yangu anaolewa tarehe 31 siku ya uchaguzi, sasa aolewe au asiolewe?Maana polisi wasije wakatukamata kwa kufanya sherehe siku ya uchaguzi.

Pakazuka malumbano miongoni wa abiria, wengine wakisema aolewe na wengine wakisema asiolewe kwani watakamatwa kwa kufanya sherehe siku ya uchaguzi. Mpaka nateremka kwenye daladala bado malumbano yalikuwa yanaendelea. Kaazi kwelikweli!!!
Habari hii nimetumiwa na msomaji wa Maisha na Mafanikio aishiye jijini Dar es Salaam.
NAWATAKIENI WOTE IJUMAA NJEMA NA PIA MWISHO WA JUMA MWEMA BINAFSI NITAKUWA NAFANYA KAZI. KILA LA KHERI!!!!!!!!!!

Thursday, August 26, 2010

India inateswa na malaria tena!!

Anopheles gambiae
mosquito,






P Falsiparum
India inateswa na malaria, hasa Mumbai watu 9000 wamepatwa na malaria.
Hata ile sehemu ambayo watalii wanaipenda Kerala, ambayo inasemekana ilikuwa hakuna malaria kwa miaka kadhaa uiliyopita nako sasa watu wanapata mmateso tena.

Mwaka jana waliambukizwa watu 154 na mwaka huu mpaka sasa wameambukizwa watu 82.
Kuna aina nne (4) za malaria na mojawapo ni P Falciparum ambayo ni hatari sana kuliko nyingine zote. Aina hii inasemekana imeingia India.

Chanzo Aftonbladet la 4/8/2010

Wednesday, August 25, 2010

HATIMAYE MIAKA MIWILI IMETIMIA TANGU BLOG YA CHANGAMOTO YETU IANZISHWE. HONGERA!!!


miaka yaenda kasi mno yaani leo ni miaka miwili blog hii ya CHANGAMOTO YETU tangu ianze kublogu. Blog ya MAISHA NA MAFANIKIO yakutakia yote utakayotenda yawe na mafanikio mema. Hongera sana na uwepo wako unathaminiwa sana. zaidi ingia hapa utapata mengi zaidi.

MAJINA YA KIJAMII

Wanablog wenzangu nimetumiwa ujumbe huu kwa njia ya barua pepe nami nimeona palipo na wengi hapakosi... au Umoja ni nguvu kwa hiyo naomba tusaidiane kulijibu swali hili kwani nina uhakika wengi tutakuwa tumejifunza kitu hapa. Haya hapa chini ndio ujumbe wenyewe:-
----------------------------------------------------------------------------------

Hujambo?

Mimi ni Mkenya na ninapenda kusoma makala yako kwenye blogi yako. Ningependa unitafutie jina mwafaka la wazazi wa mume na mke wanavyopaswa kuitana. Nimepekuwa kwenye kamusi lakini juhudi yangu haijazaa matunda.

Nitashukuru.

Tuesday, August 24, 2010

Ilikuwa Jumapili ambayo sitaisahau!!

Kanisa la Makwai Lundo hapa ni 2007!!



Nataka leo kuwasimulieni kisa kilichonipata wakati nilipokuwa miaka 8-9 hivi:- Haya ungana nami katika simulizi ya kisa hili.

Ilikuwa siku ya jumapili asubuhi wote tukiwa katika maandalizi ya kwenda kanisani. Kanisa letu la Makwai Lundo (Nyasa). Nadhani baadhi yenu mnajua kuwa baba yangu alikuwa mwl. Ndiyo!! basi kama sikosei kulikuwa ni wakati wa kufanya mitihani. Na baba alikuwa na tabia ya kuchukua kazi zake za shule na kufanyia nyumbani.

Asubuhi hii ilikuwa si nzuri kwangu. Baba alikuwa bafuni akioga, kujiandaa kwenda kanisani. Basi akaja kaka yangu na kuniambia "Yasinta njoo tuangalie hii mitihani tuone nani kafaulu, mmmhh! mimi nikasita nikamwambia mimi naogopa, akasema njoo baba anaoga hatatukuta". Nikanaswa nikaenda kwenye ile meza iliyolundikwa makaratasi ya mitihani na ndio nikawa mpekuzi wa ile mitihani na kaka akawa anaangalia kama baba anakuja? Lakini naye akataka kuona na sasa kukawa hakuna mwangalizi baba huyu akatokea.

Eeeehh! bwana weeee, mzeee alikasirika huyo sikuwahi kumwona. Akamtuma kaka yangu akakate fimbo/kiboko. Nawaambieni hapo nilikuwa natetemeka, jasho lilinitoka na nusu nijisaidia hapohapo. Fimbo/kiboka kikaja, baba akatoa amri Yasintaaaa lala chini na bana kanzu yako akiwa na maana nibane gauni langu. We acha tu, maana kiboko kiliingia hicho tena bado nakisikia, kwa jinsi kilivyodunda.
Je wewe unayesoma unadhani jumapili hii iliisha vipi? Na je? ungekuwa wewe ungefanya nini?

Ni mimi kama kawaida KAPULYA wenu au kama wengine waniitavyo MTEMBEZI. Tukutane tena wakati mwingine!!!!

Monday, August 23, 2010

Unapojikuta unashindwa kujieleza nini maana ya baadhi ya maneno kwa kiswahili!!

Wakati nipo likizo nimepata swali kutoka kwa msichana mmoja ambaye alikuwa juzi juzi tu Tanzania, Zanzibar na Mombasa. Aliniuliza kwanini waswahili tunasema/itana BWANA NA NDUGU?
Mmmmhh! nikasema hapa ipo kazi, nikarudi nyumbani nikafanya upekuzi kwanye KAMUSI sanifu ya kiswahili. Na hapo nilipata kama zifuatazo:- Bwana- Ni jina la heshima la mwanamume bwana ni mume, bwana ni mwanamume umfanyiaye kazi, mtu mwenye cheo, tajiri, mwajiri. Bwana ni Mwenyezi Mungu, Allah. Pia bwana hutumika kumfanya mtu asikilize, hutumika kumgutusha mtu.

NDUGU:- Ni watoto waliozaliwa tumbo moja, yaani baba na mama mmoja au mama mmoja au baba mmoja. NDUGU- n watoto wa jamaa au ukoo mmoja, NDUGU ni rafiki mkubwa, NDUGU ni mtu mwenye kushirikiana naye katika shughulu za dini au siasa.
Haya yalikuwa maelezo yangu kwa msichana huyu. Lakini hata hivyo hakunielewa kwani alisedma alisikia watu wakiitana haya majina hata kama hawakuwa wanafahamiana. Je? ungekuwa wewe ungemjibu nini? naomba msaada wenu!!!!!

Saturday, August 21, 2010

Twendeni Afrika kwetu: Mama Afrika!!!




JUMAMOSI NJEMA KWA WOTE NA PIA MWISHO WA JUMA MWEMA!!!

Thursday, August 19, 2010

HUYU NDIYE YASINTA NGONYANI!!!

Yasinta Ngonyani, Picha kwa hisani ya Maisha Blog

Ni binti halisi wa kitanzania, ingawa anaishi ughaibuni lakini hujivunia asili yake na utaifa wake, ni binti pekee aliyejitolea muda wake kuwaelemisha watu wa rika zote bila kujali rangi, kabila, itikadi, taifa wala jinsia.

Binti huyu si mjivuni na hupenda kubadilishana mawazo na watu mbali mbali, na pia hupenda kufuatilia habari za nyumbani kwao alikotoka na haoni tahayari kuongea lugha ya kwao. Daima hujitambulisha kwa jina la asili ya kwao na huona fahari kutumia jina hilo.

Binti huyu hakuona ajizi kuwajuza wanae asili ya kwao japo wamezaliwa ughaibuni, amekuwa msitari wa mbele katika malezi ya wanae ili kuhakikisha wanae hao hawajitengi na asili ya aliotoka yeye.

Si mchoyo wa ushauri na kupitia makala zake aziwekazo kibarazani kwake amekuwa ni msaada kwa wengi, amekuwa mstari wa mbele katika kuilemisha jamii bila kujali rika. Amejitolea kufundisha kile akijuacho juu ya malezi na matatizo mbali mbali yanayowakabili wanandoa na malezi ya watoto.

Kibaraza chake kimekuwa ni kitovu chenye kukutanisha wadau mbali mbali wenye fikra pevu, na kuibua mijadala yenye kuelimisha, kufundisha, kuburudisha na kuhuzunisha pia.

Binafsi napenda kumuita dada na kwangu mimi ni zaidi ya dada, kwani amekuwa ni mwalimu mzuri kwangu nikijifunza mambo mengi kupitia kibaraza chake nimekuwa nikijifunza mengi, na sisiti kukiri kwamba chimbuko la kibaraza cha VUKANI ni kutokana na kile nilichojifuza kwake.

Ni mkweli na muwazi, na hasiti kusema wazi hisia zake, lakini huwa makini sana ili kuepuka kumuumiza mtu mwingine kihisia, na kama kwa kusema huko kutamkera mtu mwingine, ni mwepesi kuweka sawa maelezo yake ili kuondoa msigishano wa mawazo.

Nakumbuka wakati fulani nlipopata msongo wa mawazo kutokana na tofauti zangu na wazazi wangu, alikuwa ni mtu wa kwanza kunitumia email binafsi akijaribu kuniliwaza na kunitaka nisichukue hatua yoyote kujidhuru, naomba nikiri kwamba email ile ilinisaidia sana kurudi katika hali yangu ya kawaida na nilijisikia fahari kuona kwamba kuna mtu ananipenda na kunijali japo sijawahi kuonana naye uso kwa uso.

Huu kwangu ulikuwa kama muujiza, inakuwaje, mtu kusoma mawazo yangu kupitia blog tu halafu awe karibu nami kiasi hiki, ni kitu gani kimemvuta? Kusema kweli tangu siku hiyo niliamni kuwa maandishi yana nguvu sana na kupitia maandishi yawezekana mtu mwingine kukufahamu vizuri sana.

Nimekuwa karibu sana na binti huyu, na amekuwa ni mwema sana kwangu na mshauri wangu pia, na kupitia vibaraza vyetu, tumekuwa tukibadilishana mawazo na kupeana ushauri mbali mbali ili kuboresha ustawi wetu na wa familia zetu.

Huyu ndiye Yasinta Ngonyani, kwa kumsoma zaidi bofya hapa.

Makala hii iliandikwa na mdogo wangu wa hiari Koero Mkundi mwaka 2009/08/14 bado nimevutiwa sana na hii makala na nimeona niiweke hapa kwangu pia kama kumbukumbu na pia kujikumbusha yaliyopita kwani si vibaya. Pia nachukua nafasi hii kwa kumshukuru sana mdogo wangu huyu wa hiari Koero Mkundi kwa kazi nzuri anazozifanya kwa kumsoma zaidi kazi zake ingia hapa. Pia nauthamini sana uwepo wake Mwenyezi Mungu na akulinde na akuongoze na yote utendayo yawe mema. Kwanni yeye ndiye mwezeshaji wa yote na yeye ndiye ajua anavyotuwazia maana mawazo atuwaziayo ni mema. Ni hayo tu kwa leo.

Wednesday, August 18, 2010

Hatua za kuomba nafasi za masomo Ughaibuni

Naamini unaendelea vizuri kabisa na maisha.

Naomba uweke kwenye BLOG/Tovuti yako interview yangu niliyofanya na Gazeti la Mwananchi la August 10th, 2010 kuhusu NONDOZI Ughaibuni.
-------------------------------------------------------------------------------------------------



Makulilo
ALIHANGAIKA kutafuta nafasi za masomo ya elimu ya juu, hatimaye akaja kuipata nafasi hiyo
nchini Marekani. Baada ya kufanikiwa, Ernest Makulilo, Mtanzania anayeishi na kusoma
nchini… ameamua kuwasaidia wengine jinsi ya kuomba nafasi za masomo ya juu katika nchi za
Ulaya na Marekani ikiwa ni mchango wake kama anavyoeleza katika mahojiano haya na
mwandishi wetu.

Swali: Sababu zipi zilikusukuma kuwasaidia wanaotafuta nafasi za masomo nje ya nchi?

Jibu: Kwanza naomba niseme kuwa nilianza kuitoa huduma hii rasmi Julai mwaka 2007, na huu
ni mwaka wangu wa tatu. Sababu kubwa ya kuingia katika huduma hii ni kwa kuwa nilihangaika
sana kutafuta nafasi za masomo hadi kufanikiwa kuja hapa Marekani. Hivyo nikawa na taarifa
nyingi za mtu unawezaje kupata nafasi hizi kwa Marekani na Ulaya.

Sikuona kama ni jambo la busara kwa kuwa mimi nimehangaika basi na wengine nao
wahangaike, hivyo niliamua kurahisisha njia ya watu wanaopenda kutaka kusoma zaidi kwa
kupata udhamini ughaibuni.

Kitu kingine kilichonisukuma kujikita katika suala hili ni kuwa na blog (gazeti tando) mahsusi
kwa ajili ya kuweka taarifa za misaada ya masomo kwa watu wa nchi maskini.

Niligundua kuwa blog nyingi zilizopo Tanzania zina vitu mchanganyiko, nikaonelea ni vema basi
nianzishe kitu ambacho mtu akisema anataka nafasi za masomo basi ajue wapi pa kwenda na
kupata msaada.

Swali: Ukoje mwamko wa Watanzania katika kupata taarifa za vyuo ambazo wewe umekuwa
ukizitangaza?
Jibu: Mwamko wa Watanzania ni mdogo sana tofauti na mataifa ya Afrika Magharibi, Amerika
ya Kusini na Asia. Watanzania wengi bado wana ile dhana na kasumba kuwa ili mtu aende Ulaya
au Marekani kusoma ni lazima atoke katika familia tajiri au ya kisiasa. Hivyo wengi hukata tamaa
mapema. Kitu kingine kinachosababisha mwitikio mdogo kutoka kwa Watanzania ni wengi wao
kukosa ari ya ushindani kama ilivyo kwa Wakenya na watu wa nchi za Afrika Magharibi.

Ukiachilia hayo, wengi hudhani upatikanaji wa nafasi hizi ni kitu rahisi mno. Ninapompa mtu
taratibu za vitu gani ajiandae navyo ili aweze kuwa mshindani mkubwa na kufanikiwa kupata
nafasi, wengi hukata tamaa. Baadhi ya Watanzania tunapenda vitu mteremko sana wakati
uhalisia si huo tena. Dunia hii ni ya ushindani, inabidi Watanzania tubadilike, tuendane na
ushindani uliopo katika dunia ya kibepari. Tuachane na fikra za kijamaa)

Swali: Je wewe ni wakala wa vyuo au unaiendesha vipi huduma hii?
Jibu: Mimi si wakala wa chuo au taasisi yoyote ile. Na hakuna mtu, chuo au taasisi yoyote ile
inayonilipa kwa huduma hii. Naiendesha huduma hii kwa imani kwamba kuna watu wana ndoto
kubwa za maisha yao, lakini ndoto hizo mara nyingi hufa kutokana na ufinyu au ugumu wa
upatikanaji wa elimu ya juu Tanzania na katika nchi nyingi zinazoendelea. Hivyo ninachokifanya
ni kuhakikisha watu hawa wanatimiza ndoto zao za kielimu na maisha yao kijumla.

Aidha nimekuwa nikizipitia tovuti mbalimbali za vyuo na taasisi ambazo zinatoa udhamini wa
elimu kwa watu wanaotoka nchi zinazoendelea. Nikishapata taarifa hizi, nazichuja kwa umakini
na kuzihakiki kisha nazitangaza kwenye tovuti zangu ambazo ni www.makulilo.blogspot.com
na www.scholarshipnetwork.ning.com. Kwa wale wenye maswali zaidi kuhusu taarifa fulani
niliyoitangaza huniandikia barua pepe nami huwajibu kwa kutoa ufafanuzi husika.

Swali: Nani hasa walengwa wa huduma zako na kwa nini?
Jibu: Walengwa wakuu ni watu wenye nia na sifa ya kufanya shahada za Uzamili na Uzamivu,
kwa Kiingereza Masters Degree na PhD. Kuna nafasi nyingi za makundi haya mawili kuliko
wale wanaotaka kusoma shahada ya kwanza.
Kwa digrii ya kwanza, inakuwa ngumu kupata udhamini kwa kuwa sababu nchi zote ambazo
lugha mama si Kiingereza, hutumia lugha zao kama Kijerumani, Kifaransa na nyinginezo
kufundishia katika daraja hili.
Hali hii huwa kikwazo kwa waombaji wengi kwa kuwa wanalazimika kujifunza lugha hizi na
baada ya kufaulu mitihani ya lugha ndio upate nafasi. Nchi zinazotumia lugha zao za ndani ni
kama Sweden, Denmark na Ujerumani. Lakini kwa shahada ya pili na tatu, nchi hizi zimekuwa
zikitumia pia Kiingereza

Swali: Kwa hiyo unawaeleza nini Watanzania kuhusu hali hii?
Jibu: Ninachowaambia wasome shahada ya kwanza Tanzaniaa au katika nchi nyingine za Afrika
kisha shahada ya pili na tatu waende Ulaya, Marekani au nchi za mabara mengine.

Swali: Kuna watu wengi wanaotumia njia hii ya mitandao kutafuta na kuomba nafasi za masomo
bila mafanikio, nini sababu?
Jibu: Kuna sababu nyingi zinazomfanya mtu akiomba asipate. Hili nitalifafanua kwa
kirefu.Kwanza watu wafahamu kuwa kupata nafasi za masomo ughaibuni si jambo la bahati bali
vigezo na kufuata taratibu husika. Kwa kukosa vigezo au kwa kushindwa kufuata masharti, wengi
wamekuwa wakikimbilia kusema kuwa hawana bahati au kuna upendeleo.
Kwa mfano ili mtu aweze kupata udahili na kisha udhamini, vitu vifuatavyo ni muhimu:Mosi,
matokeo bora ya vyuo, vyuo vingi vinataka wastani wa daraja la pili la juu yaani Upper Sercond
kwa Kiingereza.Pili, mwombaji aandike malengo yake kwa umakini na ufasaha kupitia kitu
kiitwacho
Statement of Purpose/Interest. Ukiandika kwa kulipua hata kama una matokeo mazuri, sahau
kupata udhamini.

Tatu, kuna kitu kinaitwa Writing Sample, hii ni kazi ambayo umeshawahi kuandika kama insha
au utafiti wowote ule wakati unasoma. Lengo lake wanataka kujua uwezo wako wa kuandika
mambo ya msingi. Nne,ni barua ya kukupendekeza kutoka kwa walimu wako au mahala
unapofanyia kazi.Hawa nao wanapswa waiandike vizuri, waonyeshe uwezo wako wa taaluma na
kazi.

Pia kuna zoezi la kupima uwezo wa lugha kwa muombaji. Uingereza wana mitihani ya TOEFL na
IELTS, wakati Marekani wana mitihani kama GRE na GMAT. Waombaji wahakikishe vyeti vyao
vimethibitishwa uhalali na wakili au mahakama kama si nakala halisi.
Baada ya hatua hii na ukishakuwa na vigezo, omba vyuo ila kumbuka vyuo unavyoomba viwe
vimeshatangaza udhamini wa masomo kwa wanafunzi kutoka nje ya nchi husika.
Lakini pia mwombaji asitosheke kuomba chuo kimoja. Anatakiwa kuomba vyuo zaidi ya ishirini
ili kuwa na uhakika wa kupata udhamini mkubwa na ulio mzuri.

Swali: Unanufaika vipi kama mtu binafsi kwa kuendesha huduma hii?
Jibu: Mafanikio makubwa ninayopata ni kuwa na furaha ya kweli kutoka moyoni. Ninafurahi sana
watu wanapozipitia tovuti zangu, kuzifanyia kazi na kisha kufanikiwa. Furaha hii ni zaidi ya pesa
kwangu, maana mimi kujua mbinu hizi si kwa ujanja au werevu nilionao kwa wengine. Kwa
kuwa Mwenyezi Mungu kanipa maarifa haya, sina budi kuyafikisha kwa wengine wanaotafuta
elimu au maisha.Moyo huu ndio ulionisukuma pia kuanzisha mfuko wa kijamii utakaoitwa
Makulilo Foundation kwa lengo la kuongeza wigo wa taarifa na mbinu zaidi za upatikanaji wa
nafasi za masomo.

SOURCE: http://www.mwananchi.co.tz/magazines/33-maarifa/3780-hatua-za-kuomba-nafasi-za- masomo-ughaibuni.html

Tuesday, August 17, 2010

Kwanini kuwatumia ma- house girl kama watumwa??


Kuna jambo nimekuwa nikiliwaza na pia nimekuwa nikitumiwa barua pepe na wasomaji wa blog hii ya Maisha na Mafanikio. Wakitaka niandike kuhusu kwa nini tunawatumia sana ma-housegirl/boy(wasaidizi wa nyumbani)kama sio binadamu.

Kwanza kabisa niseme binafsi sijawahi kuishi na/kuwa na msaidizi wa nyumba. Nakumbuka kuna rafiki yangu mmoja aliniuliza:- "kama nina msaidizi wa nyumba, nikamwambia HAPANA, akaniuliza inakuwaje? unawezaje kumudu kazi zote za nyumbani na wakati wote wawili mnafanya kazi?" Nikamjibu tunazifanya wenyewe. Tunasaidiana

Kuhusu wasaidizi wa nyumbni sitakikusema kuwa watu wasiwe na wasaidizi la hasha! Ila tu kuna wakati utakuta wengine wanawatumia wasaidizi hao kama mashine na sio binadamu. Yaani atafanya vijikazi hata ambavyo mke /mume au mtoto angeweza kufanya mwenyewe kwa mfano kufua nguo za ndani(chupi) kuchota/kuchukua maji ya kunywa. Nimewahi. Na halafu la kusikitisha zaidi utakuta msaidizi huyohuyo anatamaniwa na mwisho kupachikwa mimba. nimewahi kusikiliza wimbo mmoja wa Dr Remmy Ongala Hamisa ukisema hivi "Akina mama nao jamani eti mfanyakazi wake anaanguka naye" au pia ni kinyume "akina baba nnao jamani eti mfanyakazi wake anaanguka naye". Na hii inatokea mara nyingi na bado tatizo hili linatokea kila siku katika jamii/ndoa zetu.

Naweza nikasema maisha ya ndoa au maisha kwa ujumla kikubwa zaidi ni KUSAIDIANA:- Nikiwa na maana ni vizuri sana kusaidiana kwani ukimwacha mwanamke afanye kila kitu ndani ya nyumba atakuwa anachoka na mwisho wake atashindwa kuitumikia ndoa yake. Na matokeo yake mume ataanza kutafuta nyumba ndogo. Lakini kama kungekuwa na umoja haingetokea hivi.

Tuwe waaminifu na ndoa zetu zitadumu na tuwatumie wasaidizi wetu kama binadamu, tuaache utumwa.

Monday, August 16, 2010

HODI HODI NDUGU ZANGU SASA LIKIZO IMEKWISHA NA NIPO NANYI TENA KAMA KAWAIDA!!!


Nimekuwa likizo wiki tatu sasa na bahati mbaya au nzuri wakati huu wote kumekuwa na mvua tu kwa maana hiyo likizo yangu haikuwa nzuri na hakuwa kama nilivyopanga- Haya sasa nimerudi tena katika ulimwengu huu wa kublog na nipo nanyi ndugu zangu tena. Ni furaha sana kuwa nanyi na nilikuwa nimewa-miss sana sijui kama nanyi mlini-miss mie?

Sunday, August 15, 2010

SWALI LA JUMAPILI YA LEO:- Msamaa ni nini?

Nisamehe



Je utaratibu sahihi wa kumsamehe /kusamehewa kwa mtu aliyekosa ni upi?

1. Mtu aombae msamaha kwanza/atubu ndipo asamehewe?

2. Asamehewe hata pasipo kuomnba msamaha au?

3. Vyote viwili ni sawa?



Jumapili njema wote na tuonane wakati mwingine!!!

Thursday, August 12, 2010

Swali la leo:- Hivi hapa ni wapi vile????


Sijui patakuwa wapi??? Mshindi kuna zawadi nono imeandaliwa haya karibuni. Au niseme mshindi wa kwanza atakula chakula cha jioni na mimi popote atakapo, mshindi wa pili atakaribishwa Ruhuwiko na mshindi wa tatu ni siri.

Tuesday, August 10, 2010

HERI KWA SIKU YA KUZALIWA KAKA MUBELWA T. BANDIO

Ni jambo la kumshukuru Mola kwa kututunza tangu siku ile tuzaliwapo mpaka kila mwaka kuongeza mwaka mmoja zaidi. Na leo ni siku kubwa sana kwako. Maana umetimiza makumi matatu sasa ni safari ndefu sana. HONGERA SANA. NA MOLA AKUBARIKI PIA AIBARIKI FAMILIA YAKO.

Tuesday, August 3, 2010

Mawazo/Maswali kuhusu Maisha!!!



Nawaza mwenzenu

Muda mrefy au nisema tangu niwe hapa duniani nimekuwa nikijiuliza maswali haya na bila kupata majibu na leo nimeona si vibaya nikiwashirikisha kwani kama tusemavyo umoja ni nguvu ......!Ni hivi:-



1. Kwanini maisha ni mapambano?

2. Kwanini wengi wanafikiri kuwa wanawake ni tegemezi (sio wote)

3. Hivi tabia inatokana na nini?

4. Na jamani maisha ni nini na kwanini watu tunahangaika ili kuishi?

5. Na mwisho , hiv kwanini mtu unaweza ukawa na pesa na ukaona hazina maana, na kuna wakati mtu unaweza ukafanya jambo la furaha wakati unalichukia je? hapa utasema mtu huyu/mimi nina matatizo?

Sunday, August 1, 2010

Malezi ya Watoto Katika Mpango wa Mungu!!!!

Malezi bora kwa watoto


Watoto ni kitu cha thamani sana ambacho Mungu anawazawadia watoto wake kadiri apendavyo yeye. Inashangaza sana kuona watu wanavyosahau kuwa watoto wametoka kwa Mungu na wanapaswa walelewe kwa upendo na misingi ya neno la Mungu na badala yake wanawaona kama ni mzigo. Jinsi unavyomlea mtoto tangia akiwa bado mdogo kabisa ndivyo unavyoyajenga maisha yake ya baadaye.
Kwanza kabisa yakupasa uifahamu thamani ya mtoto ambaye Mungu amekupatia. Umhesabu kama zawadi toka kwa Mungu na sio mzigo hata kama haukupangilia kuwa naye kwa wakati huo maana Mungu alishamfahamu kabla hata hajazaliwa. Katika vitabu vya Yeremia na Zaburi tunaona kuwa Mungu anayafahamu maisha ya kila mtoto kabla hata mimba yake yaijatungwa.
Yeremia 1:5a Kabla sijakuumba katika tumbo nalikujua, na kabla hujatoka tumboni, nalikutakasa;
Zaburi 139:16 Macho yako yaliniona kabla sijakamilika; chuoni mwako ziliandikwa zote pia, siku zilizoamriwa kabla hazijawa bado.
Tambua kuwa Mungu amekuheshimu na kukupendelea kwa kukupa watoto/ mtoto ili umlee na kumtunza, kwa hiyo yakupasa umpende na kumlea kwa hekima ya ki Mungu na hata siku moja usimuone kama mzigo au kumsema vibaya kwa watu wengine. Hata kama mtoto wako atakuwa na mapungufu kitabia wewe kama mzazi unayemjua Mungu na unaitambua thamani ya mtoto uliyenaye, usimseme vibaya kwa watu bali umuombee, kumuelekeza kwa upendo na kumuonya kwa busara. Fahamu kuwa mtoto wako anathamani kubwa mbele za Mungu naye ndiye anayemjua vyema. Wewe kama mzazi unawajibika mbele za Mungu kwa jinsi unavyomlea mtoto wako ha hivyo yakupasa kujitoa kwa uaminifu katika kumlea kwa upendo na uvumilivu wote.
Tafuta kulifahamu neno la Mungu na kuitafuta hekima ya kiMungu katika malezi ya mtoto wako kuliko hekima ya mwanadamu. Jifunze Mungu anasema nini kuhusu malezi ya watoto na uyafuate hayo kwa uaminifu hata kama kibinadamu yanaonekana yamepitwa na wakati. Tumia muda kwenye maombi kumwombea mtoto wako na maisha yake ya kimwili na kiroho ili aweze kuongozwa na Mungu siku zote za maisha yake. Mfundishe mtoto wako tangia akiwa na umri mdogo habari za Mungu na kweli yote ya neno la Mungu. Katika maisha ya siku hizi ni kawaida kuona baba na mama wote wanafanya kazi nje na nyumbani hali inayopelekea watoto kubaki na mlezi muda mwingi wa mchana. Hali hii usipoiwekea mikakati katika malezi ya mtoto wako kiroho inaweza kuleta madhara makubwa hapo baadaye. Hakikisha muda unaoupata kuwa na mtoto wako unautumia kumweka karibu nawe na kumfundisha habari za Mungu.
Kuna njia nyingi ambazo mzazi unaweza kuzitumia katika kumfundisha mtoto wako habari za Mungu kwa ufanisi kuanzia katika umri mdogo kabisa. Anza kwa kuomba na mtoto wako wakati wote iwe ni asubuhi, wakati wa kula, usiku na wakati mwingine wowote ambao unafanya maombi. Mfundishe kuwa ni muhimu kuomba kabla ya kula na kulala na pia asubuhi baada ya kuamka. Kwa kufanya hivi mara kwa mara basi taratibu ataaza kuona kuwa maombi ni kitu cha muhimu na kadiri anavyokuwa mkubwa ataendelea na tabia ya maombi. Biblia katika kitabu cha mithali inasema mlee mtoto katika njia impasayo naye hataiacha hata atakapokuwa mzee. (Mithali 22:6).
Msimulie hadithi za biblia kwa njia ya kufurahisha huku ukiwa unamsomea biblia. Mwanzoni itakuwa ngumu kukuelewa lakini kadiri unavyoendelea na kurudia rudia mara kwa mara itakaa ndani yae na itamjengea hamu ya kusoma biblia ili ajue kwa undani zaidi habari ambazo unamsimulia pale atakapokuwa anajua kusoma. Ukiweza mtafutie biblia ya watoto yenye hadithi fupifupi za biblia kwa picha. Waweza pia kutafuta video za hadithi za biblia kwa watoto na mkawa mnaangalia pamoja naye huku ukimsimulia , pamoja na kupata nafasi ya kumfundisha neno la Mungu pia utapata muda mzuri wa kufurahi na mtoto wako na kuwa karibu naye.
Mfundishe kuonyesha shukrani pale mtu anapompatia kitu au kumtendea jambo jema. Hata kama hajui kuongea mwambie sema asante hii itamfundisha kuwa ukitendewa jambo ni lazima kuonyesha shukrani. Mfundishe kumshukuru Mungu kwa kuamka salama, kupata wazazi wanaomlea vyema, kununuliwa michezo mbali mbali, n.k Moyo wa shukrani utamsaidia kumjua Mungu zaidi na atakuwa anatafuta mema ya kumshukuru Mungu kila siku. Ishi maisha ya upendo, furaha, amani na ukarimu wakati wote ili mtoto aone uhalisia wa Mungu katika maisha yako.
Nenda na mtoto wako kanisani kila jumapili na uwe unamwambia kwanini unaenda kanisani. Usisahau kumpa sadaka naye awe anatoa na umweleze kwa nini tunatoa sadaka kuwa ni njia ya kumshukuru Mungu kwa vingi alivyotupatia. Kumbuka kila mara kumkumbusha upendo wa Mungu, wema na ukuu wa Mungu.
Malezi ya mtoto ni huduma inayojitosheleza, ni jukumu ambalo umuhimu wake ni mkubwa sana na pale unapokosea matokeo yake kuyabadilisha huwa ni kazi ngumu sana. Mwamini Mungu katika jambo hili na mtegemee na kumtazamia yeye pekee, kama alivyokupa mtoto atakuwezesha kumlea katika njia impasayo.
–Magreth Riwa–

Habari hii nimeipata hapa nikaona si vibaya kama nikieweka hapa katika blog ya Maisha na Mafanikio ili wengi tujifunze. PIA NACHUKUA NAFASI HII KUWATAKIENI JUMAPILI HII YA KWANZA YA MWEZI WA NANE IWE NJEMA SANA. MWENYEZI MUNGU AWE NANYI NA BARAKA ZAKE ZITAWALE NYUMBANI MWENU!!!!!!