Wednesday, December 30, 2009

"MJADALA ULIOVUNJA REKODI KATIKA BLOG YA MAISHA MWAKA 2009"

Ndugu wasomaji wa blog hii ya MAISHA, katika kupitia mada mbalimbali nilizowahi kuweka humu ili kupata ile ambayo ilivuta hisia za wasomaji wengi na kuleta changamoto, nimevutiwa na mada hii ambayo ilileta vuta ni kuvute miongoni mwa wadau wa blog hii.
Kwa hiyo basi nimeichagua mada hii kuwa ndio mada iliyovunja rekodi kwa mwaka 2009.
Natoa shukrani kwa wadau wote mlioshiriki katika kuichangia mada hii.
Naomba muungane nami katika kujikumbusha kile kilichotokea katika mjadala huu.

MISHAHARA HAITOSHI+TUACHE UZEMBE KAZINI
Makala hii nimeipenda ndiyo maana nikaamua kumwomba http://hapakwetu.blogspot.com/ Kwani najua nakamilisha lengo lake la kuifanya isomwe na wengi.

Katika nchi yetu ya Tanzania, watu wanalalamika muda wote kuwa mishahara haitoshi. Gharama ya maisha ni kubwa kuliko mishahara. Hata kwa kuzingatia mahitaji muhimu tu, watu wengi wana haki ya kusema kuwa mishahara haitoshi.

Malalamiko ya mishahara kuwa haitoshi yanasikika duniani kote. Hapa Marekani, shida kubwa inayowakabili watu ni kulipa bili na madeni mbali mbali. Marekani ni nchi ya madeni. Kutodaiwa popote ni sifa nzuri katika utamaduni wa Tanzania. Lakini Marekani, sifa inakuja kutokana na umakini wa kulipa madeni. Mishahara ya Wamarekani wengi inaishia kwenye kulipa madeni. Kwa hivi, nao wanalalamika kuwa mishahara haitoshi.

Wako Watanzania ambao wana mishahara ambayo ingeweza kutosheleza mahitaji muhimu. Tatizo ni kuwa dhana ya mahitaji muhimu ina utata.

Tunaweza kusema mahitaji hayo ni chakula, malazi, mavazi, matibabu, elimu, na usafiri. Lakini, katika utamaduni wetu, orodha ya mahitaji muhimu ni kubwa zaidi ya hiyo. Kumlipia ada mtoto wa shangazi ni wajibu. Kuchangia gharama ya msiba kwa jirani ni wajibu. Kama una gari, kumpeleka mtoto wa jirani hospitalini ni wajibu.

Kwa msingi huo, hakuna Mtanzania ambaye anaweza kusema mshahara wake unatosha. Suala haliishii hapo. Je, ukitembelewa na marafiki, utakaa nao tu nyumbani na kuongea nao, au unatakiwa kuwapeleka mahali wakapate kinywaji? Je, unaweza kuacha kuchangia gharama za arusi ya rafiki yako?Tukizingatia hayo yote, mishahara haitoshi.

Watanzania wengi wana tabia ya kutumia fedha kwa mambo mengi mengine, ambayo umuhimu wake ni wa wasi wasi, kama vile bia. Kwa Watanzania wengi, bajeti ya bia ni kubwa sana. Kwa mtu anayekunywa sana bia, mshahara hauwezi kutosha. Lakini je, bia ni kitu muhimu namna hiyo?

Kwa upande wa pili, Watanzania tunapaswa kutafakari dhana ya mshahara. Mshahara unapaswa kuwa malipo muafaka ya kazi ambayo mtu anafanya. Kazi ndio msingi. Lakini, kuna tatizo kubwa Tanzania.

Watu wengi hawafanyi kazi kwa bidii. Muda mwingi wanatumia kwenye gumzo. Lakini wanategemea kulipwa mshahara, na wanalalamika kuwa mishahara haitoshi. Je, wanastahili hizo hela wanazopewa kama mshahara? Je, wakiongezwa mishahara, wataongeza juhudi kazini au wataendelea kukaa vijiweni na kupiga soga?

Huku Marekani, watu wanachapa kazi sana. Mshahara unatokana na kazi. Mtu asipofika kazini, halipwi. Akichelewa, malipo pia yanapunguzwa. Kwetu Tanzania mambo si hivyo. Mtu akishaajiriwa, anategemea kupata mshahara wake kila mwezi, hata kama anatumia masaa mengi kijiweni. Je, ni bora kuanzisha utaratibu wa kuwalipa wafanyakazi kwa yale masaa wanayokuwa kazini tu, na kupunguza mshahara kwa masaa wanayokuwa kijiweni?

Nami nataka kuongezea ni kwamba hapa Sweden ni karibu sawa na huko Marekani. Yaani hapa hata kama upo likizo hulipwi, inategemea ni likizo gani. Halafu kama unaumwa na halafu huendi kazini zile ziku mbili za kwanza hulipwi kitu kwa hiyo hapo ukiumwa basi ujue mshahara wako unapungua/unakatwa. Kwa hiyo kwa mtindo huo utakuta hata kama mtu unaumwa unajikaza na kwenda kazini. Kwani mshahara wanaokata ni mkubwa sana na ukizingatia maisha nayo yapo juu.
Na: Yasinta Ngonyani kl. 6:26 PM



NA HAYA YALIKUWA NI MAONI YA WADAU...........

kamala Lutatinisibwa Lutabasibwa said...
nyie msituletee za kuletwa hapa kwetu tanzania.
yaani nyie kukaa sweden na marekani na kuona roho zao za kupenda na kuitukuza pesa basi mataka na kwenu tuige mambo ya wazungu? mtaiga mpaka lini nye wabongo msio fikiri?
mnadhani viwango vya mishahara vya huko utumwani mliko ni sawa na vya hapa tanzania?
boro kutawaliwa kimwili kuliko kutawaliwa kiakili na kiroho.
sasa kuna watu wanaolipwa shilingi lakini moja mpaka mbili kwa mwezi, huyu akiugua utakati shilingi ngapi kwa siku na abaki na kiasi gani na ataishi je?
kwa nini mnataka kuleta unyama wa huko utumwani hapa kwetu? mnataka kuleta mikono ya utumwa hapa ehe?
yaani mmewekewa mipaka ya kufikir kiasi kwamba hamna mwenye mawazo nje ya huo utumwa mnaouishi ehe?
kuweni makini mnapopendekeza upuuzi mwingine bwana. bongo binadamu wote ni sawa na ni ndugu na ndio maana unaweza kuwa huna ela lakini usife njee. kwa maneno mengine mshahra wa mtu mmoja unasaidia watu lukuki./
hapa ni ubinadamu kwanza mambo ya pesa na miliki za dunia hii ni baadaye. kaeni utumwani na mfurahie maisha ya utumwani na msituletee mizizi ya utumwa kwetu
na kama mnaona maisha ya uko ni sawa poa tu kivyenu.
March 18, 2009 8:25 AM
Yasinta Ngonyani said...
Kamala ndugu yangu, Kuhusu maoni yako kwanza nasema asante. Halafu napenda kukuambia ya kwamba hakuna mtu anaishi utumwani, Hapa kinachozungumziwa ni jinsi watu wengine wanavyofanya kazi na matumizi yake na jinsi watu wengine wanavyolalamika ya kuwa mshahara hautoshi wakati hawafanyi kazi. Jambo jingine ni kwamba mimi binafsi nimeona na nimesikia watu wakisema afadhali waishio ughaibuni mna maisha mazuri. Lakini hawajui ni taabu gani zipo huku kwa sababu wao mara nyingi wamakuwa au niseme "sisi waafrika" tumezoeshwa sana kupewa misaada kutoka huko Ughaibuni. Je? tunajua hiyo misaada inatoka wapi? watu kwa huruma zao wanaacha familia zao na kwenda kufanya vibarua na pia zile pesa wanapeleka Afrika. na pia watoto wadogo wanatafuta pesa kwa mtindo wa kuosha magari na zile pesa wanapeleka kwa watoto wenzao Afrika. Je? hapo sasa nani ni mtumwa?
Ndiyo nakubaliana nawe ktk sisi waafrika hata kama mmoja katika jamii hana hela basi hawezi kulala njaa na hata kama una rafiki au jamaa. Sawa, ila kuna wengi katika akili zao wanafikiri watu huku wana mshahara mzuri na maisha mazuri na wana kila kitu na wao hawana shida na mshahara wao huwa unatosheleza mahitaji yote HAPANA.
March 18, 2009 11:39 AM
kamala Lutatinisibwa Lutabasibwa said...
ysinta ndio maaana nakwambia kuwa huko ni utumwani. ni azima utumike vya kutosha sana.
wala usidanganyike na misaada itokayo ulaya. hakuna kitu kinachoitwa misaada ila kuna danganya toto. tangu uhuru afrika iliishi kwa misaada lakini hakuna maendeleo, unadhani misaada hiyo ina tija na hatuwezi kuishi bila yenyewe? mbona china sasa inakuja juu na kuwa super power, ulishawahi kuona inasaidiwa na nchi yoyote? si walijifungia na kuishi kivyao sasa hao wanaendelea wakati sisi tukipokea misaada kutoka utumwani na kuzidi kutuma watumwa wetu wakatumikishwe?
mbona kabla ya kuja kwa wakristo na waislilamu (wakoloni) afrika iliishi kwa amani, umoja na upendo bila ujinga wa kimsaada kutoka ulaya wala kupeleka watunwa huko?
sasa tumepeleka watumwa, wanazalisha na kuleta misaada mbona haupigi hatua yoyote?
muwe na macho mapana sio ya ndio mzee tu eti tunasaidiwa. waafrika hatuamini sana katika utajiri wa duniani japo tunao mwingi, tunajua kabisa kwamba dunia si chochote si lolote.

UTUMWA WA KIAKILI NA KIROHO NI MBAYA KULIKO HATA WAMIHEMKO.
March 18, 2009 12:13 PM
fred katawa said...
Yasinta,wazungu hawatupi misaada bali wanarudisha asilimia 0.00001 ya kile Wanachoiba Africa."THERE IS NO FREE LUNCH".Kuhusu kazi sisi tunafanya kazi zaidi ya hao wamarekani,hebu fikiria kubeba zege,kusukuma mkokoteni wenye magunia kibao ya viazi pamoja na kuendesha guta lililosheheni mzigo tani mbili.Huko wanaweza hayo?
Katika dunia hii ubinadamu umebaki Afrika ndo maana mshahara wa mtu mmoja unasaidia watu kibao.Haya mambo hayapatikani ulaya kwa kuwa hakuna binadamu huko bali kuna viumbe wanaofanana na binadamu.Usijaribu kutushawishi sisi tubadili maisha yetu yawe kama ya hao wanyama.
March 18, 2009 2:30 PM
Mbele said...
Ndugu Kamala, ninafuatilia maoni yako, kwani mimi hupenda kujumuika na Watanzania na wengine katika kufundishana na kuelimishana. Watanzania wanaonifahamu wanajua hayo, kama wanavyojieleza hao hapa.
March 18, 2009 4:29 PM
Bwaya said...
Ukimsoma Kamala haraka haraka unaweza pandwa jazba. Ila ukipunguza kasi ya kusoma, ukaongeza tafakari, unamwelewa. Mimi nimemwelewa. Anachotuzidi wengi, ni uwezo wa kusema wazi wazi anachoamini.
Hata hivyo ni kweli pia kuwa waswahili wengi hatufanyi kazi ipasavyo. Tunatumia muda mwingi kupiga domo maofisini. Nadhani tukibadilika, tukajiamini itatusaidia kwenda mbele.
March 18, 2009 4:53 PM
Mbele said...
Samahani, katika ujumbe wangu hapa juu, nilisahau kusema kuwa mimi ndiye niliyeandika makala ambayo Dada Yasinta ameiweka hapa kwake, kama aliyoelezea.
Kitu ambacho ningemshauri ndugu Kamala ni kufanya utafiti zaidi, ili aweze kuelewa fikra na misimamo ya watu asiowafahamu, kabla ya kuwadhania hili au lile. Kwa msingi huu, iwapo yeye ni mtu anayetafuta elimu, kama mimi, afanye hii juhudi, na anaweza kuanzia kwa kusoma blogu hii na hii.
March 18, 2009 5:08 PM
Anonymous said...
utajua tu nani ana hasira za kunyimwa visa, sijui tatizo ni lugha pale ubalozini! kufikiria kila aliye nje ya nchi anaishi utumwani ni utumwa na mwisho wa kufikiri pia! pole sana Yasinta, naona umevamiwa kijiweni kwako! ila ndio maisha hayo, kuna watu wanachukia sana habari za nje ya nchi kwa vile walishawahi kuwa na shauku ya kudaka pipa, wakashindwa kupata visa then wakaanzisha kampeni ya sizitaki mbichi hizi, kuna watu wapo nje wanaishi kama wafalme, na wengi tu hao wanaoitwa watumwa wanafanya kazi na kusaidia huko nyumbani. tunapotoa maoni ni vuzuri kuwa hekima fulani, hata kama tunachotaka kusema kina ukweli au ni lazima tuangalie tunawasilisha vipi ujumbe, zaidi ya hapo inakuwa ni upuuzi mtupu!!
March 18, 2009 11:29 PM
Anonymous said...
Uliyetoa maoni kuwa watu wakinyimwa visa ndo na kutokujua kiingereza ndo wanakuwa na hasira haupo sahihi hata kidogo.Hapa bongo kuna watu wanaishi vizuri zaidi ya wabongo waliohamia huko.
Na vilevile kuna watu wanayajua vizuri maisha ya huko na huku kwetu.Kuishi mbali na nyumbani haimaanishi kuwa una maisha mazuri kuliko uliowaacha nyumbani.
March 19, 2009 10:37 AM
Anonymous said...
Ndugu Kamala, unatia aibu! Nafikiri hata wanaokunyamazia wamekustahi. U're such an idiot! Hivi unawezaje kuwalopokea watu usiowajua? Inasikitisha sana tena sana. Kwa nini usifikirie namna nzuri ya kuwasilisha maoni yako? Uwazi gani wa kijinga kiasi hiki?
Una bahati unajadiliana na watu wastaarabu wanaojua kuchagua maneno ya kumwambia mtu.
March 19, 2009 11:22 AM
Anonymous said...
Mdau uliyesema kwamba sipo sahihi niliposema kwamba hasira na kutokujua kiingereza, naona wewe ndio umenisemea habari za kutojua kiingereza, kwani sikusema tatizo kutojua kiingereza. Nimesema tatizo lugha. Hili lina mambo mengi mojawapo ni namna unavyojieleza. pia kumbuka kwamba kiingereza sio lugha pekee kwani kuna nchi nyingi ambazo hazitumii kiingereza. na pia sikusema kwamba bongo hakuna watu wanaoishi maisha mazuri hata kidogo, naomba kanisome tena vizuri. Mimi pia nipo bongo na nayajua vizuri tu maisha ya nje ya nchi kwa vile nimeishi sana tu huko, hivyo najua ninachokiongea. Ninapokuambia hasira za kukosa visa nina mifano mingi sana, nin jamaa ambao wanaponda sana habari za kwenda kujitafutia nje ya nchi kwa sababu wao walikosa visa, hao wapo wengi ninaowafahamu japokuwa siwezi kuwataja hapa. natumaini umenielewa!
March 19, 2009 11:30 PM
Mbele said...
Ndugu Kamala

Leo nina fursa ya kuongelea masuali yako, kwani nilikuwa nimezidiwa na shughuli.
Mimi ni Mtanzania, kama wewe. Tanzania ni yangu, kama ilivyo yako, na sote tunawajibika kuichangia kwa hali yoyote tunayoweza.
Popote tulipo, tunawajibika kutafuta fursa ya kuichangia Tanzania. Ukifuatilia mawazo ya Mwalimu Nyerere utakuta alitoa mfano wa kijana anayepelekwa mbali akatafute chochote kwa ajili ya kijiji chake. Ni fundisho alilotoa, wakati anaongelea suala la kuwasomesha vijana na wajibu wa hao vijana wa kuchangia nyumbani. Cha muhimu ni ule moyo wako. Kama unaipenda nchi yako, utaitumikia popote ulipo.
Kwa mzalendo, kukaa nje si hoja. Nje kuna fursa tele za kuchangia, kwani fursa zilizopo nje hazipo nyumbani. Ninawafahamu Watanzania wengi huku Marekani ambao wanafanya makubwa kwa nchi yao kwa kutumia fursa zilizopo huku Marekani.
Kwa maana hiyo, kama wote ni wazalendo, hakuna sababu ya kuwatenga waliopo nje na walipo nchini. Haya mawazo uliyotoa hayatatufikisha mbali. Nchi za wenzetu, hata hapa hapa Afrika zinatambua hayo. Kenya, kwa mfano, ina kitengo katika wizara ya mambo ya nje, kinachoshughulika na watu wao waishio nje. Nchi ya Mali inayo wizara kamili ya kushughulika na wananchi wao wanaoishi nje. Nchi hizi zinatambua faida ya kuunganisha nguvu za hao walioko nje na wale walioko ndani. Tanzania tunajiumiza wenyewe tukiendekeza fikra kama ulizotoa.
Sisi hatupigi kampeni kuwa tuige mambo ya wazungu. Tumelenga kwenye suala la mishahara na kazi. Ndio mada pekee ambayo tumeongelea. Si haki kudai kuwa tunapiga kampeni ya kuiga mambo ya wazungu. Wazungu mambo yao ni mengi, mengine mazuri na mengine mabaya.
Kuhusu kufanya kazi kwa bidii, hatuna hata sababu ya kuwataja wazungu. Tulipopata Uhuru, Mwalimu Nyerere alituhimiza kwa usemi wa "Uhuru na Kazi." Na watu nchini kote waliitikia, wakawa wanafanya kazi sana. Sio suala la kuiga wazungu. Taifa letu lilianza na maadili ya kufanya kazi kwa bidii. Baadaye tumeingiza uzembe, na sasa watu wengi wanakaa vijiweni na kungoja mishahara hapo hapo kijiweni. Hili ndilo tatizo, wala si suala la kuiga wazungu.
Mtu yeyote anayeipenda Tanzania anawajibika kuunga mkono dhana ya kufanya kazi kwa bidii. Kutetea vijiwe ambavyo vinafanyika wakati wa kazi ni kuhujumu Taifa. Vijiwe vije tukishamaliza kazi, wakati tumechoka na tunahitaji kupumzika. Hapo ni sawa kwenda vijiweni kusogoa.
Kama tunakubaliana kuwa msingi huo wa Uhuru na Kazi ambao tulianza nao, ulikuwa sahihi, sioni kwa nini leo mtu akisema tufanye kazi kwa bidii iwe ni dalili ya kutawaliwa kiakili. Je, huyu Mwalimu Nyerere aliposema Uhuru na Kazi, alikuwa ametawaliwa kiakili? Wananchi nchini kote waliosikia wito wa Nyerere, walifanya vibaya?
Dunia ya leo, ya utandawazi, ina ushindani wa kutisha. Tusipofanya kazi hatutafika popote. Na kazi hizo si za kuzalisha tu katika uchumi, bali pia kujiongezea maarifa na elimu. Tusipopunguza vijiwe tutaangamia.
Ni kweli mishahara ya wengi nchini ni midogo. Lakini, dawa ya tatizo hili si kukaa vijiweni. Kufanya kazi ni njia ya kuinua uchumi na hii ndio njia ya kuinua kipato. Badala ya kukaa kijiweni, ni bora watu wawe wanajiongezea ujuzi na elimu, ili kujiweka katika nafasi ya kupata fursa bora kazini au kuweza kujiajiri. Ujasiriamali ni wazo ambalo wenzetu duniani wanatumia. Badala ya kukaa na kulalamikia mishahara midogo, ni bora kutafuta maarifa na ujuzi na kutafuta fursa za ujasiriamali. Vijiwe si dawa.
Mwishoni mwa ujumbe wako, umekiri kuwa wewe unajipatia kipato chako bila kuajiriwa na mtu, bali kutokana na juhudi yako ya kufanya kazi. Hujatuambia kuwa unashinda kijiweni. Sasa kwa nini unatulaumu sisi ambao tunasema hilo hilo unalosema, kuhusu umuhimu wa kufanya kazi? Kwa nini unatuambia sisi tuna akili za kitumwa, au tumewekewa mipaka ya kufikiri? Na wewe ambaye pia unazingatia kazi, tukuite una mawazo ya kitumwa au umepangiwa mipaka ya kufikiri?
Maadili ya kwetu ya kusaidiana ni mazuri, kama unavyosema. Hapa tunakubaliana. Ni jadi ya kuihifadhi. Mimi ni mwandishi, na nimeshaandika kuhusu tofauti za utamaduni wa Mwafrika na ule wa Mwamerika, na katika maandishi yangu huwa nataja mazuri na mabaye ya pande zote. Yako ambayo Waafrika tunaweza kujifunza kutoka kwa Waamerika, na yako ambayo wao wanaweza kujifunza kutoka kwetu.
Mimi ninawafahamu Wamarekani. NI watu kama sisi; wako ambao ni wema, na wako ambao ni wabaya. Hakuna tofauti na wanadamu wengine.
Mfumo wa uchumi wa nchi yao ni wa kibepari, na huu tunaweza kuuita unyama, kama alivyouita Mwalimu Nyerere, lakini si sahihi kuwaita Wamarekani wote kwa jina hilo. Wengi wao wanaupinga mfumo huo, kwani unawaumiza.
Binafsi, nachukulia maisha kuwa ni fursa ya kufanya mambo ya manufaa kwangu na wanadamu, sio fursa ya kustarehe. Suala unaloliongelea, la kufurahia maisha, halinihusu. Muda wangu mwingi natumia katika kujielimisha, ili niwe mwalimu bora zaidi na zaidi. Nikichoka napumzika kidogo, halafu naendelea na kazi. Dhana ya kufurahia maisha haina umuhimu kwangu.
March 19, 2009 11:42 PM

Koero Mkundi said...
kamala, kamala, kamala,
duh!!!!
hapa naona umekutana na wanubi,
je una cha kuongeza?
ndugu yangu, kamala mada nyingine ni za moto kuzivamia, mimi nilijua tokea mwanzo kuwa maoni yako yatawaamsha waliolala, na ndio sababu nikakaa kando kwanza ili nione segere......
binafsi nilikuelewa na naamini hata dada yasinta alikuelewa kwa sababu tumezoea staili yako ya kuchangia mada, lakini ndugu yangu sio watu wote wanaokufahamu ki hivyo, kwa hiyo walikuelewa ndivyo sivyo.
kaka usicheze na walioko ughaibuni, kwani hujui kilichowapeleka huko, wewe kula ugali wako na maharage kisha mshukuru mungu kwa kukujalia pumzi ya bure usiyoilipia kodi halafu lala.
duh! poe sana......
March 20, 2009 4:18 AM
kamala Lutatinisibwa Lutabasibwa said...
anony anayesingizia visa hajui mimi nimewahi kutembelea nchi ngapi mpaka sasa. anaona ni ukosefu wa visa tu na hajui nina uchaguzi gani katika maisha na labda sijui nini maana ya kuishi kama mfalme, wapi na vipi.
mbele, ni kweli uliyoyasema kwa kiasi kikubwa lakini mimi ninachokipinga ni tabia ya kuiga hata upuuzi na roho mbaya za wazungu.
kwa mfano kwanini tuanze na uwanyanyasa wafanyakazi kwa kuwanyima viisenti wanavyopata ambavyo hata hivyo haviwatoshelezi?
ni lazima tuanze na hiyo? kwani nyie mnaojiita wasomi na wataalamu wa dunia hii, hamna mawazo mapya na njia mpya za kujikomboa mpaka mfuurahie mfanyakazi wa bongo kunyimwa mshahara wake?
na je, pamoja na usomi wenu huo, unaonia ni sawa kwa bindamu mwenzako kunyimwa chakula (mshahala) wakati anaumwa? kama unaona nisawa, basi ukae tu ughaibuni.
na kama hayo ndio mawazo ya watu wa ughaibuni, basi mfilie huko huko hatuhitaji kuwa na wizara wala kitengo cha wakazi wa nje.
ninachosema hapa ni kwamba nchi kama yetu ambayo haina dira wala mwelekeo, watu watapata motisha gani wa kufanya kazi kwa bidii? watu wasiojitambua? wenye mawazo kama ya kwenu ya kukumbatia uzungu akija mzungu basi kuanzia kwa raisi mpaka mawazili wanachekelea?
kwani nyie hamuwezi kuja na njia mpya au hata kuwashauri wazungu kuachana na huo unyama wao na uuaji wakawa kama kwentu juu ya wafanyakazi wao wagonjwa, na kuwafikiria vyema kama watu wenzao?
upi utu kati ya wafanyiwavyo watanzania wagonjwa na wazungu au watumwa mlioko utumwani?
si kila kitu tutakiacha lakini ubinadamu wetu tutaondoka nao?
NB nayaongea haya lakini ninao ndugu wa kutosha huko utumwani, US na kanada na mipango yote ya mimi kwenda huko niliikataa mapema tu.
mdogo wangu koero, unaogopa nini? hujui tatizo la kusoma sana ni lipi?
ugali na hmaharage ndio chakula changu. sili vyakula vya viwandani wala vya wanyama. nikija kwenu we niandalia ugali maharage tena wa donna, mtenbele, mchiicha, njegele, mbaazi, karanga. lakini ukipika vyakula ya viwandani sitokula, am sory
March 20, 2009 1:59 PM
Mzee wa Changamoto said...
Alright!!
Amani, Heshima na Upendo kwenu nyote. Nami kama wengine ntawiwa kuikimbia mada na kutoa maoni kuhusu maoni maana ni sehemu kubwa na yenye nguvu kwenye ma-jamvi yetu haya.
Usomaji na utoaji wa maoni unatukutanisha na watu wenye uwezo, imani na mitazamo tofauti. Kwa hiyo kwangu naona kuna mawili kwa mtoaji na msomaji wa maoni hayo. Kwanza ni lazima kuzingatia kuwa hasira hupunguza busara. Namaanisha kuwa ukitoa ama kusoma maoni ukiwa na hasira kuna mengi utakayoshindwa kuwa nayo bayana. Na pili kwa msomaji kuna wakati yapaswa kuangalia zaidi "point of view" kuliko tone ya mtoa maoni. Na hili litasaidia maana kuna wengi wetu ambao huwa tunaandika kama tunavyoongea. Kwa hiyo kama hutazingatia hilo waweza kupata shida kiasi.
Na sasa nirejee ktk maisha ya kutatua tatizo kwa namna tulionavyo. Nilifundishwa kuwa katika kila linaloonekana kama jambo baya kuna uzuri ndani yake.
Nadhani wapo waliokerwa na maoni ya Kamala lakini nadhani kwa ujumla tunapaswa kujiuliza maswali ambayo yanapelekea kuwepo kwa mgongano wa mawazo hapa. Kwa mfano maoni ya Ndg Kamala yananipa CHANGAMOTO kujiuliza MAANA YA UTUMWA KATIKA ULIMWENGU WA SASA, YUPI MTUMWA NA VIPI UNATENDEKA.
Kwa hali ilivyo ntakubaliana kutofautiana na Kamala kuwa Utumwani ni huku. Na hata kama ni huku naamini kuwa utumwa ulioko nyumbani ni m'baya zaidi. Na pia sidhani kama kuna makosa ya kuiga mfumo unaoweza kuwa bora kutoka mahala ambapo unaamini si bora. Hata kama si masuala ya mshahara, lakini kuna mengi mema ambayo yanatendeka kuwawajibisha wanaofanya yasiyofanyika. Ukiangalia katika haki za wananchi, huduma za wateja (customer services), siasa na mengine mengi utagundua kuwa hatua waliyofikia huku ni kubwa ukilinganisha na nyumbani na sidhani kama tunaweza kupinga kujifunza kwa kuwa tu "tutaiga toka utumwani."
Utumwa unaofanywa na viongozi wetu kwa wananchi wetu nadhani ni wa kinyama kuliko uliofanywa na watu ambao lengo lao lilikuwa kuja kutenda hilo. Sasa hivi watu wanahenya kufanya kazi, kuonekana wanajenga nchi na kisha matokeo yake pesa inaingia kwenye akaunti za watu ambao wanatenda makosa hayo huku wakipindisha katiba tena kwa makusudi na kisha wanatumia kinga za kikatiba kutokwenda kujibu mashitaka. Huwezi fanya hayo huko unakokuita "utumwani".
Huku "uhuruni" ambako watu wanajilimbikizia mali kwa mshahara usiojulikana tena akiwa kwenye nafasi ya kuitumikia jamii na hakuna mwenye uwezo wa kumuuliza, huwezi kufanya hivyo ukiwa huku "utumwani."
UKWELI NI KWAMBA TAFSIRI YA UTUMWA IMEBADILIKA NA SASA TUNAKUWA WATUMWA WA KAKA NA DADA ZETU HUKU WANAOPANGA HAYO WAKISTAREHE NA KUSHEREHEKEA HAYO NJE YA NCHI.
Utumwa wa zamani ulikuwa nyumbani ukitendwa na wakoloni lakini UTUMWA ULIOSEMA KUWA NI M'BAYA ZAIDI ni huu unaotendwa na viongozi wetu wanaosema kuwa WANAWAPENDA NA WAKO HAPO KUTETEA MASLAHI YA NCHI YETU ilhali hakuna wanalofanya zaidi ya kuiba na kutumikisha jamii.
Naomba kuwakilisha kipande hiki. Ni mtazamo wangu kulingana na namna nionavyo tatuizo, na naendelea kutunza haki ya kukosea na kukosolewa.
Blessings
March 20, 2009 2:18 PM
kamala Lutatinisibwa Lutabasibwa said...
mzee wa changamoto mimi binafsi sijawahi kuongozwa na hasira katika kujibu hoja zozote,. hisara ni sehemu ya hisia au mihemko muhimu katika maisha ya binadamu na bila hiyo twaweza tusiishi, hata hivyo ushujaa wetu unaonekana pale tunaposhinda hisia na mihemko yetu na hivyo mimi najitahidi kuwa bingwa katika hilo.
utumwa wa kwenu huko ughaibuni ni mbaya sana kuliko wa kwetu nyumbani hata katika miwani tofauti. watu wanaishi katika mbavu za mbwa, lakini wana amanai na wanaisha sasa (maisha waliyonayo) kuliko huko.
wale wanaoficha fedha huko ughaibuni (labda nyie mmezifuta) nao ni watumwa wabaya kwani wanamabwana wawili, wale wa kwenu pamoja na ujinga na roho mbaya.uhuru wa kusema nk ulioko huko na vitu vingine, inabidi uviangnalie kwa miwani mipana, sio uhuru wa kweli kama ukiangalia, utaona ila ukitazama, utaendelea kutizama bila kuona na utasifia tu majamaa yalivyo kuosha akili (brainwash).hata wale wanaojifanya mabwana huku, kuna vitu wanavikosa au vinawaumiza huko kwenu.
napinga kuiga eti kwa sababu ya usomi wenu wowote ule
March 20, 2009 2:52 PM
SIMON KITURURU said...
Kuna uwezekano watu wanaogopa kuitwa watumwa kwa sababu ya kutokuwa na uhakika wa WAO Uhuru.
Mimi tokea nizaliwe mpakaleopamoja na nchi zote nilizo wahi kuishi ambazo ni kadhaa , bado najihisi sijawa huru.
Na naamini kuna watu wanaongelea ya nchi wakati wako huru chooni tu na hata sebuleni au chumbani kwao hawako huru.:-(
Mimi bado mtumwa na nahangaikia uhuru!:-(
March 20, 2009 10:46 PM
Kissima said...
Kaka Simon samahani, wewe unasema ni mtumwa kwa maana hiyo hauko huru, utumwa unaouongelea ni upi? Kuna utumwa wa akili/mawazo, ambao unasababisha utumwa mwingine wa kukandamizwa,wachache kula jasho lako n.k.
Kwa mfano , miaka minne ya mateso huwa tunaisahau kabisa, kisa mwaka wa tano vibarabara vinarekebishwa kidogo, vizahanati vinajengwa, maneno matamu matamu yenye upanga mkali ndani yake,soda na bia mbili tatu, kisha miaka minne tena utumwani. Yote haya ni matokeo ya utumwa wa akili.
Naomba ufafanuzi kuhusu utumwa.
March 22, 2009 10:46 AM
Bwaya said...
Kamala,
Japo naweza kuwa sikubaliani na unachokisema, lakini naamini unayo haki ya kuutetea uhuru wako wa kusema.
Aidha, naamini kwamba katika kusema, una haki ya kusema kwa namna yoyote ile unayoona inafaa isipokuwa ile inayoweza kumletea msomaji hisia zisizo za lazima katika kukuelewa.
March 22, 2009 4:32 PM
Egidio Ndabagoye said...
Nibamize kwenye mada kwenyewe.Suala la mishara halian ubishi hamna sehemu duniani watu wanaridhika na mishahara.
Dhana la mshahara kuwa mdogo inatokana na majukumu uliyonayo,mfano majukumu yanapozidi mshahara unakuwa mdogo.
Wachumi wana kanuni zao za maisha kwamba kila kipato kinapoongezeka na matumizi yanaongezeka.Suala la kulia mshahara mdogo linabaki pale pale.
Suala la kazi halina ubishi sisi watanzania ni wavivu wa kutupwa kutwa kupiga domo vijiweni.Nenda maofisini leo hii utalia,utajiuliza huyu mtu kawekwa pale auze sura au afanye kazi?
Kuhusu utumwa nakubaliana na Simon.
March 22, 2009 6:42 PM
EVARIST said...
Prof Mbele umeleta mada ya moto...inanikumbusha makala moja katika gazeti la TIME (sikumbuki ni la mwaka gani ila ni 2000s ambapo gazeti hilo lilimtaja kuwa Man of the Year).Aliulizwa kuhusu upinzani uliosambaa ndani na nje ya Marekani kuhusu baadhi ya mitizamo yake hususan War on Terror.Jibu lake ndio nalotaka kuli-refer hapa:ukiona watu wana-react (positively or negatively) ina maana hoja ina mguso kwao,maana ingekuwa kinyume wasingeizunngumzia.
Kuhusu hoja iliyopo,binafsi sina comment bali naomba kugusia kasumba iliyojengeka muda mrefu huko nyumbani juu ya dhana nzima ya maisha ya Ughaibuni.Naomba kukiri kwamba dhana hiyo ndio ilinipa changamoto kubwa ya kuibatiza blog yangu jina hilo.
Kuna dhana (miongoni mwa wenzetu)kwamba Watanzania walioko ughaibuni wanapotoa uchanganuzi wao kuhusu masuala flani yanayoihusu nchi yetu basi wanafanya hivyo kama "kuwasanifu" wenzao walioko nyumbani Tanzania.Mantiki ya kinachoandikwa na Mtanzania aliyeko ughaibuni inafunikwa na na ukazi wake huko nje.Naomba kusisitiza kuwa si kila Mtanzania ana kasumba hiyo,na hapa nazungumzia zaidi uzoefu (experience) wangu binafsi na wa marafiki wachache waliokumbana na hali hiyo.
Naomba kusisitiza kwamba asilimia kubwa ya Watanzania walio nje ni watu wanaoipenda nchi yao,wanasikitishwa na baadhi ya yanayotokea huko nyumbani na pia WANAGUSWA (kwa sababu sidhani kama kuna yeyote kati yao ambaye hana family connection huko nyumbani).Again,hapa nawazungumzia Watanzania naowafahamu tu(ikimaanisha kuwa inawezekana kuwapo exceptions).
Kuhusu kasumba hiyo,nadiriki kusema angalau huku kwenye blogs kuna afadhali.Kuna wakati nilikuwa naandika makala katika baaadhi ya magazeti ya huko nyumbani,na ilikuwa nadra kwa wiki kupita pasipo msomaji flani kutoa tuhuma kwamba "aaah unataka kutwambia nini wewe?unadhani Ulaya ndio kila kitu..."na kauli kama hizo ambazo binafsi naziona ni za kibaguzi just like Mzaramo atapomwona Mndamba hana nafasi ya kuzungumzia Dar es Salaam,au Mporogo "kumkwida" Mmachame kuhusu masuala ya Mahenge.
Sote ni Watanzania,tofauti pekee ni mahala tulipo ambapo kimsingi hata kwa wale waliobadili uraia bado damuni mwao ni Watanzania hususan kutokana na connections za kifamilia,koo na kabila,vitu vinavyounda taifa letu pendwa.
Kuhusu "utumwa wa huku ughaibuni" naomba nichangie kwa mfano hai.Wakati flani rafiki yangu mmoja Mmarekani Mweusi aliwahi kunidadisi kuhusu ubaguzi hapa Scotland.Niliamua kuwa mkweli kwake na kumwambia upo na unanisumbua.Alichonijibu kilinifanya nifikirie mara mbili.Alisema "japo ubaguzi ni ubaguzi popote pale,lakini angalau wewe ni Mtanzania uliyeko kwenye nchi ya watu,wakikubagua wanaweza kuwa na excuse-hata kama ni muflisi.Vipi je kuhusu mie mzaliwa wa hapa Marekani na mwenye asili ya hapa lakini kuna nyakati nabaguliwa kwa vile tu mie ni mweusi?"
Majibu ya rafiki yangu huyo yanaweza kuwa muhimu katika ulinganifu wa "utumwa wa ugahibuni" na "utumwa wa nyumbani."Japo utumwa ni utumwa,na haupaswi ku-exist popote pale,lakini utumwa wa nyumbani unachukiza zaidi kuliko ule wa nje.Na hapa sitetei utumwa.Let's be realistic.Kuna mambo tunayokumbana nayo katika kutafuta maisha huku kwenye nchi za watu ambayo yanakera kupindukia,lakini tunajipa moyo kwa kusema aah hapa ugenini (kwa wale ambao hata wakiishi nje milele,Tanzania bado ni nyumbani) nikirudi nyumbani hakuna wa kunitenda hivi.Na unakanyaga pale Mwl Nyerer Intl Airport unatendwa maradufu ya kule ugenini!
Tujaribu kuiweka hivi pia.Mkoloni alitunyanyasa kwa vile alikuwa mgeni,hakuwa na uchungu na nchi yetu.Of course,ilikuwa inatuuma na ukoloni haukuwa sahihi.Lakini hebu tuangalie hawa Watanzania wenzetu wanaotutenda vibaya zaidi ya wakoloni.Wakoloni wangeweza kabisa kujitetea kuwa "ah sie sio Watazania ati!".Je vipi kuhusu mafisadi wanaoitafuna nchi yetu kwa jasho la walipa kodi masikini?
Ni dhahiri unyama unaofanyiwa na nduguyo unauma zaidi kuliko wa mtu baki,na hili halihitaji utafiti.
Mwisho,nimalizie kwa mfano mwingine mdogo.Majuzi nilikuwa nazungumza na mtu flani ambaye awali sikufahamu kuwa anaijua Tanzania vema.Yeye amezaliwa Mashariki ya Mbali na kuzunguka sehemu mbalimbali duniani,kwa sasa ni mhadhiri hapa chuoni.Kwa kifupi,nilizungumzia "WATANZANIA..." na yeye akaniuliza "hivi unaposema Watanzania kwa umoja unamaanisha watu gani hasa?Maana nchi yenu ina makabila zaidi ya 120 na ni dhahiri kuna tofauti za msingi miongoni mwao...maana nchi yenu ni moja ya nchi zilizo highly diversified kuliko nyingi barani Afrika....ni vizuri unapozungumzia Tanzania unyambulishe kwa makini ni watu gani hasa unaowazungumzia badala ya kuwajumlisha kana kwamba unazungumzia Rwanda ya Wahutu na Watusi ni makabila mengine machache nchini humo..."
Je tunapohitimisha kuwa "Watanzania ni wavivu...hawapendi kazi...wanataka mshahara pasipo kazi...walalamishi..." tunazungumzia wale mamwinyi wa Kiembesamaki,masamjo wa Kariakoo,maalwatan wa Makorora Tanga,nk au tunajumuisha pia akina Mwangaluka wanaopiga jembe kwa nguvu zote kule Mwanza na Shinyanga,Morani wa Kimasai wanaokabiliana na wanyama wakali maporini wakati wanatafuta lishe ya mifugo yao,Wandamba wenzangu pale Ifakara wanaopiga jembe robo tatu ya mwaka kuhangaikia na kilimo cha mpunga,nk?
Uvivu,uzembe,ulalamishi,nk ni tabia ya mtu mmoja mmoja na sidhani kama kuna kabila la wavivu let alone Watanzania wote kuwa wavivu.
Binafsi naamini kuna Watanzania wanaopenda sana kazi (angalia wenda/warudio kazini kwa miguu pale bonde la Jangwani,angalia wamachinga wanaokesha juani kuuza bidhaa za mabwanyenye wanaopigwa na viyoyozi,nk) lakini wanakwazwa na mfumo dhalimu uneoelekea kuzingatia kwamba "mwenye nacho ataongezewa na yule asie nacho atanyang'anywa hata kile kidogo alichonacho."Napo hapo nadiriki kabisa kusema kuwa kuna utumwa wa mchana mweupe katika maeneo mengi tu ya huko nyumbani.Angalia asilimia kubwa ya dada zetu baamedi wanaolipwa shs 30,000 kwa mwezi (ataishi vipi huyu kama "asipowachangamkia wateja"),wengi wa mahauziboi na mahauzigeli (wanaonyimwa sio tu haki yao ya kipato halali bali pengine hata uhuru wa kuingia sebuleni kwa tajiri au kuwasha redio au runinga),nenda "uhundini" uone jinsi wahindi wengi wanavyowadhalilisha wengi wa wafanyakazi wao (ambao kimsingi ndio wenyeji wao-wazawa)...huu ni utumwa m-baya zaidi kuliko huo mie na Braza Kitururu tulioufuata kwa hiari yetu kwenye nchi za watu.
Ni rahisi kuhitimisha kuwa Watanzania wanapenda sana kukaa vijiweni na kusahau kuwa mashirika waliyokuwa wakiyategemea kwa ajira yameuzwa kwa "wawekezaji",mazao yao kwenye vyama vya ushirika yanaendelea kukopwa kila mwaka huku yakiwaneemesha mafisadi wa co-ops,wamachinga wanaojiajiri wanamegeuzwa na askari wa jiji kuwa kama wako kwenye mgogoro wa Wapalestina na Wayahudi,respectively,mabilioni ya JK "kuleta maisha bora" yameishia mifukoni mwa wajanja (isomeke mafisadi,nk,nk....na wakikaa vijiweni kupoteza maumivu ya kufanywa watumwa ndani ya nchi yao wanaitwa wavivu.Tuwatendee haki,tafadhali

Samahani kama kuna niliemkwaza katika maoni yangu.
March 24, 2009 1:34 AM
Mbele said...
Ndugu Evarist, shukrani kwa mchango wako, ambao naona umetoa mwanga kwenye vipengele vipya katika suala linalojadiliwa. Kwa upande wangu, naafiki kauli yako kuwa tunapaswa kufafanua ni akina nani tunaowaongelea tunaposema Watanzania wanapenda vijiwe kuliko kazi. Hoja yako hii naiona muhimu.
March 24, 2009 4:52 AM
kamala Lutatinisibwa Lutabasibwa said...
asante sana ndugu evarist kwa hoja yenye mifano hai na inayoelimisha. ndio maana nakaongelea hawa jamaa na kuseam wako utumwani. ni utumwa wa kiakili kwa kuwa wao wamezoea kila siku kuambiwa kuwa ni wazembe na kutumikishwa kama farasi, basi wakija nyumbani nao wanataka wawe kama mabosi wao wa halifanyi kazi hili liafrika!
natokea vijijini na hali za wazee wetu kuchwazika nazijua vizuri. yaani asilimia 80 ya watanzania kila siku wako mashambani, akina Mbele (eti ni professa, uprof. gani huo usiowezesha kuona hali halisi) wanakuja na kusema kila jitu ni livivu hapa na yanasingizia mishahala haitoshi!!!
yaani vitu vingine vinashangaza ehe? jamaa wamejaa negatives tupu wakija kwa watanzania wenzao. narudia utumwa wa akili kama watumikishwao akina mbele na yasinta, ni mbaya sana kwakweli!
evarist umenihakikishia kwamba kumbe kuna wasomi wanaofikiria na vizuri ba labda wanaweza kuleta mabadiliko. nilidhani kwamba natofautina na wengi kwa sababu ya kujikita katika maarifa ya utambuzi kumbe sivyo.
kwa kweli nilikuwa na mtizamo hasi kuhusu kusoma zaidi kwani kila niliposhauliwa kurui shule, niliona kama nikujipoteza na kupotoka kwani wasomi wengi wanafikiria ndani ya vijisanduku vya walimu wao tu na kukuza ego, kumbe sio.
bwaya, ulitaka niseme kile nilichotaka kukisema kwa njia inayonipendez mimi msemaji au wewe?
March 24, 2009 10:16 AM
Mbele said...
Ndugu Kamala, kwa vile unaongea kwa kujiamini sana, kwamba watu kama mimi tuna mawazo ya kitumwa na tumewekewa mipaka ya kufikiri, naomba kukueleza kuwa nimeandika vitabu, ambavyo baadhi vinapatikana hapa hapa Dar es Salaam. Kama ingewezekana ukavisoma, ungepata ushahidi zaidi wa utumwa wa mawazo yangu. Lakini kwa sasa, kwa vile tuko kwenye maandishi ya blogu, naomba tu unisaidie kwa kuichambua makala yangu hii hapa.
March 24, 2009 4:17 PM
Bwaya said...
Naam, mchango wa Evarist umeleta changamoto nzuri.
Evarist pamoja na uwezo mkubwa wa kujenga hoja, amefanikiwa kuchagua kwa makini kila neno alilolitumia. Si tu kufikisha ujumbe ulioukusudia, bali pia kumpata msomaji wake. Hili liwe somo la bure kwetu sote.
Kama alivyosema, watanzania walio ughaibuni wana fursa nzuri ya kuchangia mawazo yao katika masuala yanayoihusu nchi yetu. Na wanapofanya hivyo, hatutatenda haki kuwaona kama watu 'wanaotusanifu'.
Tusiruhusu mawazo mazuri kufunikwa na suala la ukazi, na kuwaona kama watu 'wanaotuchora' tu kwa kile wanachosema.
Mimi siamini kwamba mtu anaweza kuwa mvivu wa kufikiri kwa sababu tu hajasema ninachokijua. Nikifanya hivyo nitakuwa ninajijengea uzio wa kutokujifunza zaidi.
Utumwa hauna mahali. Wa ughaibuni anaweza kuwa huru kuliko sisi tulio nyumbani tunaoweza kuwa tunaogelea kwenye utumwa mbaya sana kuliko huo tunaouhisi huko nje.
Bado naamini kuwa wa-tanzania wengi (sio wote), hatufanyi kazi kwa bidii. Well, inawezekana pakawepo sababu nyingi kama alizoziainisha Evarist, lakini ukweli unaonekana. Sasa tufanyeje tuondokane na hali hii, huo ni mjadala unaojitegemea. Na mchango wa Evarist unatusaidia kupanua mjadala.
March 24, 2009 5:16 PM

Tuesday, December 29, 2009

PICHA YA LEO:-NAOMBA TUTAFAKARI PAMOJA!!

Hapa itakuwa ni picha ya mwisho kwa mwaka huu kuwa katika blog MAISHA. Je unaona nini hapa?

Sunday, December 27, 2009

KATARINA KWA NINI ULIKUFA?

Wapendwa wasomaji wa blog hii na wanablog wenzangu nimekuwa nikipokea email nyingi toka kwa wasomaji wa blog hii wa huko nyumbani Tanzania, wengi wakielezea uzoefu wao na wakitaka niziweke hapa ili tujadili kwa pamoja, na mimi sina kinyongo kwa kuwa blog hii inazungumzia Maisha, basi nitakuwa nikiziweka hapa ili wasomaji wengine wapate kujifunza

Leo nimewaletea kisa cha kusikitisha cha binti aitwae Katarina, naomba muuangane na msimulizi wa kisa hiki.

**********************************************************************

Alikuwa ni mtumishi wa nyumbani na alikuwa na umri wa miaka 14 wakati huo, nakumbuka ilikuwa ni mwaka 1993, ndio aliletwa kufanya kazi kwa shemeji yangu.
Nakumbuka nilikuwa naenda kwa shemeji yangu kila baada ya wiki kumjulia hali yeye na wanae.

Huyu Binti ambae alikuwa akijulikana kwa jina la Katarina mwenyeji wa kule Iringa alitokea kunipenda kweli na hakuficha hisia zake, kalikuwa ni kabinti kazuri na kadogo sana na kalikuwa na heshima kweli.

Siku moja shemeji yangu aliniambia kwa utani lakini, kuwa Katarina ananipenda na Kama nikitaka kuoa basi nisitafute mwanamke mwingine bali Katarina angenifaa zaidi.

Sikutilia maanani kauli ya shemeji yangu, na niliichukulia kama utani tu. Nilikuwa kila nikienda kwa huyo shemeji yangu Katarina atahakikisha ananipikia na kuniandalia maji ya moto ya kuoga tena kwa heshima kweli na nikishaoga kama nitalala pale alipenda sana kupiga soga na mimi na alikuwa akivutiwa sana na simulizi zangu za uongo na kweli.

Ilitokea nilipata kazi moja ya muda mfupi ambapo nililazimika kwenda Msolwa Morogoro ambapo nilikaa kwa miezi sita niliporudi nilikaa kama mwezi mmoja kabla sijaenda kwa shemeji yangu ambaye alikuwa akiishi Mbezi kwenye nyumba yake mwenyewe kumjulia hali.

Siku moja nilijikuta nikipata hamu sana ya kwenda kumuona shemeji yangu na nakumbuka ilikuwa ni mwaka 1994 mwishoni. Nilipotoka kibaruani jioni nilikwenda kwa shemeji yangu, lakini nilipofika nilikuta kuna mtumishi mwingine pale nyumbani, nilikaribishwa na kwa bahati mbaya shemeji yangu hakuwepo nyumbani alitoka kidogo kwenda kwa shoga yake aishiye mtaa wa pili.

Kumbuka kwamba kipindi hicho kulikuwa hakuna simu za mkononi, ilibidi nikae pale sebuleni peke yangu kwani hata watoto wa shemeji walikwenda kwa marafiki zao kusoma tuisheni.

Nilikaa pale sebuleni peke yangu kama saa moja na nusu na ndipo shemeji akarudi na aliponiona alifurahi sana. Tulizungumza mambo mengi sana lakini sikumsikia akimzungumzia Katarina, mwishowe ikabidi nimuulize. “Shemeji, tangu nimefika hapa sijamuona Katarina, mchumba wangu, je yuko wapi?” niliuliza kwa utani.

Niliona uso wa shemeji yangu ukisawajika kwa huzuni na alinyamaza kimya kwa sekunde kadhaa, kabla hajasema kitu alimuomba yule binti aliyenipokea ambaye niliambiwa ni mtumishi wa pale nyumbani amletee maji ya kunywa.

Muda wote tukisubiri maji yaletwe tulikaa kimya na alionekana kuwaza sana, hali ile ilinitisha sana. Mara maji ya kunywa yakaletwa, alikunywa funda kadhaa za maji kisha akaweka ile glasi chini na kushusha pumzi ndefu, kisha akasema.

“Shemeji ni jambo la kusikitisha kukujulisha kuwa Katarina alifariki wiki iliyopita na taarifa hizo tumezipata juzi” Alisema shemeji yangu kwa upole, niliposikia taarifa ile kuna kitu kilinichoma moyoni kama msumari wa moto na nilijihisi kama natetemeka na kijasho chembamba kilinitoka.

“Amefia wapi, aliugua nini, na amezikwa wapi?” yalinitoka maswali mengi mfululizo.
Shemeji yangu alinisimulia kuwa, aliamua kumtafutia shamba boy wake wa zamani kibarua katika kiwanda fulani cha wahindi kwa kuwa alitarajia kuoa na kabla ya kuanza kazi alimtuma kwao Singida akamletee shamba boy mwingine ili amfundishe kazi awe ni mrithi wake kabla hajaanza kazi yake mpya.

Alikwenda Singida na akaja na huyo kijana na baada ya kumfundisha alikwenda kuanza kazi na kumuacha yule kijana mpya pale nyumbani.

Kumbe kuna siku yule kijana shamba boy mpya alimbaka Katarina, lakini alimtisha kuwa akisema atamuua na kukimbilia kwao Singida asionekane tena.

Katarina aliogopa kusema na akabaki kimya akiugulia maumivu baada ya kitendo kile. Haikupita muda , yule binti alianza kuumwa umwa na kutapika kusikoisha, ikawa kila anachokula anatapika. Utendaji wa kazi ukapungua na akawa anatumia muda mwingi sana kulala. Shemeji yangu akajenga wasiwasi ikabidi amdadisi kama ana mimba.

Awali Katarina alikataa katakata kuwa ni mjamzito, lakini shemeji alimtishia kuwa atampleke Hospitali kesho yake akapime ili kujiridhisha Katarina alikiri kuwa ni mjamzito. Sasa Shughuli ikawa kwenye kumtaja mhusika, Katarina alikataa kabisa kumtaja mhusika shemeji ilibidi atumie mbinu ya kumtisha kuwa atampeleka Polisi na ndio akamtaja yule kijana lakini alisema kuwa alitishwa sana kuwa akimtaja atamuua ilibidi shemeji amfuate yule kijana chumbani kwake ili kumdadisi lakini kumbe yule kijana alikuwa akifuatilia ule mzozo kupitia dirishani na aliposikia jina lake likitajwa kuhusika na ile mimba alitoweka haraka sana asijulikane alipokwenda.

Ilibidi shemeji abaki na ule mzigo, kwanza alikuwa ni mjane pili hakuwa na mfanya kazi wa Ng’ombe maana yule kijana katoweka na pia mtumishi wake wa ndani yaani Katarina ndio huyo ni mjamzito, na yeye ni mtumishi serikalini, ilikuwa ni kaazi kweli kweli.

Ilibidi afanye mawasiliano na marafiki zake na kwa kushirikiana na yule boy shamba wake wa zamani alifanikiwa kupata mfanyakazi wa ng’ombe mwingine, na baada ya wiki akapata House girl mwingine.

Baadae alimshauri Katarina arudi kwao Iringa na alimuahidi kumpa pesa ya kutosha ili imsaidie kujifungua na akijifungua alimtaka arudi kwake ili aendelee na kazi.
Ni kweli Katarina alikubali japo shingo upande na alikuwa na wasiwasi jinsi atakavyopokelewa nyumbani kwao na wazazi wake.

Baada ya wiki moja Katarina alipakiwa ndani ya basi na kurudishwa Iringa na yule Shamba Boy wa zamani. Shemeji aliandika barua ndefu kueleza mkasa uliompata Katarina ili wazazi wake wasije kumuadhibu.

Aliporudi kutoka Iringa yule shamba boy aliyempeleka Katarina alisimulia kuwa walipokelewa lakini kwa wasiwasi kutokana na hali aliyokuwa nayo Katarina. Na kama si ile barua alioandika shemeji, basi yule shamba boy angelipishwa mahari na kuozeshwa yule binti, lakini ile barua iliposomwa ndio wakaamini japokuwa wapo walioitilia mashaka kuwa huenda imetengenezwa makusudi ili kumnasua yule kijana. Hata hivyo yule binti alikanusha kuwa yule kijana aliyefuatana naye hahusiki.

Baada ya kupita mwezi mmoja shemeji yangu alipokea taarifa kuwa Katarina alifariki wiki moja iliyopita baada ya jaribio la kutoa mimba kushindikana.
Taarifa zaidi zilisema kuwa alipata manyanyaso pale nyumbani kwao kwa wazazi wake kutokana na kwamba walikuwa wanamtegemea na baada ya kurudi pale nyumbani wakawa wana hali ngumu na hivyo kumtupia Katarina lawama kuwa amekuwa mzembe kaharibu kazi kwa umalaya.

Katarina alikusudia kuitoa mimba ile ambayo ilishatimiza miezi sita na ndipo ikashindikana na akapoteza maisha yeye na kiumbe kilichokuwa ndani.

Nilishikwa na butwaa wakati wote shemeji yangu alipokuwa akinisimulia mkasa huo wa Katarina.

Ni miaka 15 sasa tangu binti huyu afariki Dunia, lakini leo katika hali ya kushangaza nimetokea kumkumbuka, sijui ni kwanini.

Dada Yasinta nakuomba uuweke mkasa wa binti huyu katika blog yako kama Dedicationa kwa binti huyu ambaye alifariki mwezi huu wa Disemba japo tarehe siikumbuki.

Ni mimi msomaji wa blog yako Miki Malissa

LEO NI JUMAPILI YA MWISHO YA MWAKA HUU NA NI JUMAPILI YA FAMILIA TAKATIFU!!! NAWATAKIENI WOTE JUMAPILI NJEMA!!


Mwanangu, sikiliza mwongozo wa baba yako,

Wala usiyapuuze mafundisho ya mama yako.

Maisha ya kila binadamu huanza na hatua ya utoto. Mafanikio ya kila mtoto hutegemea malezi na makuzi ya wazazi au walezi.

Saturday, December 26, 2009

Alifanananishwa na mungu

Hii nimeipata katika Jamii forum nimeona niiweka hapa ili nanyi wasomaji mcheke kama nilivyocheka mimi, karibuni.

Kulikuwa na jamaa watatu kila mmoja alitoa sifa yake ya kufanana na mtu maarufu duniani.
Wa 1, mimi wananifananisha na Idd Amini
Kwa sababu gani?
Kutokana na umbile langu refu na rangi yangu nyeusi watu wananifananisha na Marehemu Idd Amini dada.
Wa pili: Mimi na Osama bin Laden
Kwa sababu gani?
Kutokana na weupe wangu na ndevu nyingi hata jina langu limekufa siku hizi naitwa Osama
Wa tatu ambaye alikuwa na umbile dogo kuliko wote.
Mimi nafanishwa na Mungu
Watu wote walishtuka na kumuona yule jamaa kama anamkufuru Mungu lakini aliwathibitishia kweli kuna mtu alimfananisha na Mungu.
Najua hamuwezi kuamini kama mjuavyo mimi mwenzenu mpenda ulabu na vifungu haviniishi, kila nilipopelekwa polisi nilihukumiwa na hakimu mmoja siku moja baada ya kupanda kizimbani hakunihukumu bali alinieleza kuwa ameniachia huru na nisirudie kufanya tena makosa.
Lakini kwa bahati mbaya nilikamatwa na kupandishwa kizimbani, na hakimu alikuwa yule yule wakati napanda alikuwa ameinama akiandika ripoti baada ya kuandika aliponyanyua macho akaniona na kushtuka huku akisema.
Mungu wangu umerudi tena
Bado tu hamjaamini kuwa niliitwa Mungu, jamaa alibakia wakitazama kutokana na mwenzao kushindwa kumuelewa hakimu alikuwa na maana gani na si kumfananisha na Mungu

Friday, December 25, 2009

MSAADA.....Namtafuta RENATHA BENEDICTO

Heshima kwako Ndugu.
Naomba uniwakilishie ombi hili barazani kwako. Namtafuta Dada Mdogo RENATHA BENEDICTO ambaye tumepoteana kwa takriban miaka 7 sasa.
Renatha alikuwa mwanafunzi wa shule ya Sekondari Kibasila jijini Dar kati ya mwaka 1998 - 2001 na baada ya hapo alienda Songea TTC kujiunga na masomo ya ualimu.
Pia alikuwa kati ya wahanga wa ajali mbaya ya Tawfiq iliyotokea tarehe kama ya leo mwaka 1999 ambapo alikuwa msaada mkubwa saana kuokoa maisha yangu. (Maelezo kamili yako
http://changamotoyetu.blogspot.com/2009/04/namtafuta-renatha-benedicto.html )

Niliwasiliana naye kwa miaka miwili iliyofuata mpaka alipoenda chuoni Songea nami nikaondoka nchini mwaka uliofuata na kwa miaka mingi sasa nimekuwa nikijitahidi saana kumtafuta bila mafanikio.
Naomba kama anaweza kusoma ama kuna anayesoma na kumfahamu anisaidie kuwasiliana naye.
Email yangu ni changamoto@gmail.com

Thursday, December 24, 2009

SALAMU ZA NOELI KUTOKA SWEDEN KWA WOTE ULIMWENGUNI!!!!

Kwa kawaida au niseme Noeli kwa sehemu nyingi ni kesho au kwa mimi lakini hapa Sweden Noeli ni leo 24/12. Kwa hiyo sisi au mimi na familia yangu tunapenda kuwatakieni wote
CHRISTMAS NJEMA/GOD JUL.

Wednesday, December 23, 2009

BINTI YULE AKANILETEA KIDAMISI: MLETA HABARI ANAOMBA KUFUNGA MJADALA

"Wasomaji wapendwa, hii ni email kutoka kwa mleta habari baba Gabby, na mimi naiweka kama ilivyo"

Dada Yasinta, ahsante sana kwa wema wako wa kuiweka ile email yangu hapo kwenye blog yako na hivyo wasomaji kupata fursa ya kuchangia na kutoa maoni yao na mitazamo yao.

Kwa kweli sikutarajia kuwa habari yangu hiyo ingeleta malumbano kiasi hicho, lakini nashukuru kuwa pamoja na malumbano hayo lakini kuna jambo nimejifunza.

Nasikitika kusema kwamba, sitaweza kumshirikisha mke wangu katika huu mjadala kwa sababu ni kutaka kuibua jambo ambalo tumeshalimaliza kwa sasa, ila nashukuru kwa kuwa wote yaani mimi na mke wangu tumejifunza kutokana na tukio hilo.

Amani imerejea katika nyumba yetu na ninashukuru kwa kuwa mke wangu amenielewa na sasa uhusiano wetu umeanza kuimarika kama mwanzo.

Dada Yasinta, naamini kuwa hata wewe unafahamu kuwa katika maisha ya ndoa changamoto haziepukiki na mara nyingi huhitaji pande mbili kufanya kazi kwa pamoja katika kuzikabili changamoto hizo na hivyo maisha ya ndoa humarika zaidi na zaidi, kwani kama mkishindwa kuzikabili changamoto hizo kwa njia ya busara basi kati ya pande hizo mbili, upande mmoja ni lazima utakuwa ni dhaifu.

Nakushukuru sana wewe na wasomaji wa blog yako kwa ushirikiano mlio unyesha, na sasa naomba nifunge mjadala huu.

Idumu Bloga ya Maisha.

Ahsanteni sana.
Ni mimi Baba Gabby

Monday, December 21, 2009

JAMANI MWENZENU JUZI NIMEONA MIUJIZA

Rafiki yangu mpya!
Kublog ni kuzuri sana maana kama wewe ni mtu wa kublog, basi kila unalokutana nalo katika mizunguko yako ya kawaida linakuvutia kuwashirikisha wasomaji na wanablog wenzako. Mimi huwa napenda sana kufikirisha upande wa pili katika kutafakari ili kujua kama niwazavyo mimi ni sawa na wezangu.

Nina kamkasa kadogo hapa ambako sio ka kawaida kalinitokea jana kakanivutia sana au niseme kaliifanya siku yangu ya jana kuwa ya kipekee…Jamani sio kwamba nimeokota almasia au dhahabu, la hasha. ngoja nisipoteze muda niwasimulie kisa kilichoifanya siku yangu ya jana kuwa ya pekee.

Juzi wakati nasubiri basi kwenye kituo cha basi kwa safari ya kwenda kusuka, mara akaja bibi mmoja,. Nikamsalimia akajibu kwa bashasha, nikashangaa sana kwani sio kawaida hapa, kumsalimia mtu usiyefahamiana naye akakuitikia tena kwa bashasha. Bibi yule hakuishia hapo, nikawa nimepata rafiki tukawa tunaongea mengi sana kuhusu maisha na kama kawaida hali ya hewa, maana huku hali ya hewa ni ya baridi mtindo mmoja, kila mahali ni theluji tu.

Yule bibi alionekana kunifurahia sana mpaka nikashangaa, maana tulikuwa tunaongea kama marafiki tuliofahamiana siku nyingi...ajabu eee!!!!

Najua wengi mtashangaa kwa nini nazungumzia jambo hili. Nimelizungumzia jambo hili kwa sababu hapa Sweden watu hawana ukaribu kama ilivyo huko nyumbani yaani Tanzania. Hapa watu wakiwa kwenye vituo vya mabasi wakingoja basi hawazungumzi na wala hawasalimiani. Sio kama nyumbani watu mnaweza kukutana kwenye kituo cha basi au kwenye basi na mkaanza kuzungumza kwa bashasha na kuzoeana na wakati mwingine mkajenga urafiki na hata kupeana namba za simu.

Huku hali haiko hivyo, eti umsemeshe mtu mmekutana tu kituo cha basi au kwenye mighahawa, mahospitalini au hata kwenye mikusanyiko isiyo rasmi….thubutuuu, mtu atakuangalia na asikujibu kitu.

Halafu hapa hata kukaa kwenye siti ndani ya basi watu wanakaaa kama mmoja mmoja hawakai pamoja na ukiingia wewe uliyezoea kuongea kama Kapulya mdadisi basi inakuwa shida kweli. Kukaa kama bubu safari nzima bila kuongea kazi kwelikweli.

Kuna mambo ambayo huenda angalau ukapata msaada kwa watu hawa, kwa mfano kama umepotea unaweza kusaidiwa tena utajibiwa kwa swali ulilouliza tu na hakuna blah blah zaidi au kama umepata matataizo ya kiafya na unahitaji masaada wa haraka kupelekwa hospitali, anaweza kujitokeza mtu akapiga simu kuita gari la wagonjwa au kama wakipata namba za simu za ndugu zako watawapigia kuwajulisha basi hakuna msaada zaidi ya huo.

Je mmeona ni kwa nini nilivutiwa sana na yule bibi? Ni kwa sababu nilijihisi niko nyumbani, na nilihisi kupendwa na mtu baki nje ya familia yangu.

Basi mwenzenu nilifurahi kweli nilijisikia nipo nyumbani ambako ni kawaida kuongea na kumsalimia kila mtu. Na hii Christmas wenzangu wee nilihisi niko Ruhuwiko kabisaaa…ama kweli bibi yule sijui ni muujiza au ni bahati.

Basi mwenzenu jana nilipata rafiki au niseme nimeona miujiza.

Sunday, December 20, 2009

Jumapili njema: Tusikilize wimbo huu uitwao BIDII na Marlwa


Bado jumapili moja tu kumaliaza mwaka huu . Na leo ni jumapili ya mwisho ya majilio nadhani nimechelewa kuwatakieni lakini ndo hivyo majukumu ni mengi.

Jumapili njema kwa wote

Saturday, December 19, 2009

NARUDI NYUMBANI NA REMMY ONGALA:- Nakwenda kula likolo la nanyungu



Jamani mwenzeni baada ya kazi leo nimefika nyumbani na nikajikuta tu mara moja namsikiliza Dr. Remmy Ongala na mara ukaja wimbo huu NARUDI NYUMBANI.Nusura nilia alipoimba nakwenda kula likolo la nanyungu duh! roho iliniuma kweli. Halafu anasema narudi Songea.... NIMEKUMBUKA KWELI NYUMBANI ndio nikaona niuweka hapa huu wimbo na wengine labda watatamani kama mimi. JUMAMOSI NJEMA NDUGU ZANGUNI !!!!

Friday, December 18, 2009

BINTI YULE AKANILETEA KIDAMISI

Nimetumiwa barua hii ya kusikitisha na nimeona ni vema niwashirikishe na wenzangu. Haya karibuni kuisoma,


Kwa dada yangu Yasinta Ngonyani, mimi ni msomaji wa blog yako wa siku nyingi na nimekuwa nikijifunza mambo mengi sana katika blog yako hii ya maisha hususan juu ya maswala ya ndoa na mahusiano. Nimekuwa nikijifunza mambo mengi sana juu ya maisha na mambo ya kifamilia na malezi kwa watoto. Nakupongeza sana kwa hilo.

Dada dhumuni la kukuandikia email hii ni kutaka kufikisha dukuduku langu juu ya mkasa ulionipata hivi karibuni. Naomba nikupe ruksa ukipenda uweke email hii hapo kibarazani kwako ili watu wengine watoe maoni yao au wapate kujifunza katika uzoefu wangu huu.

Mimi ni mvulana ambaye nitatimiza miaka 30 hapo mwakani 2010, Januari. Nilioa mwaka jana na mke wangu ndio amejifungua hivi karibuni mtoto wa kiume, kwa hiyo sasa hivi naitwa baba Gabriel au ukipenda baba Gabby.

Dada Mkasa wenyewe uko hivi, mimi naishi maeneo ya Kijitonyama hapa jijini Dar na ninafanaya kazi katika kampuni moja binafsi inayojishughulisha na uuzaji wa vifaa vya teknolojia nikiwa kama meneja masoko na mke wangu ni mtumishi wa mojawapo ya benki zinazomilikiwa na wawekezaji hapa nchini.

Kabla mke wangu hajachukua likizo ya kujifungua, nilikuwa na mazoea ya kumpeleka kazini kwake, na ndipo niende kazini kwangu na jioni nilikuwa na kawaida ya kumfuata na kurudi naye nyumbani.

Alipochukua likizo nilikuwa naenda kazini peke yangu, lakini siku moja nilikuwa nimechelewa kwenda kazini kwa kuwa nilikuwa namhudumia mke wangu kwa sababu alikuwa anajisikia vibaya siku hiyo. Nilipofika maeneo ya kituo cha Sayansi kwa wale wanaoishi Dar wanapafahamu mahali hapo, niliwaona wanafunzi wawili wakisukumwa na kondakta wa daladala ili wasipande, kulikuwa na foleni na nililiona lile tukio vizuri sana.

Adha ya usafiri kwa wanafunzi hapa jijini Dar ni tatizo sugu, na afadhali watoto wa kiume wanaweza kugombea hadi wakapanda, tofauti na watoto wa kike hawajazoea mikiki mikiki, ya makondakta wa daladala. Nilishikwa na huruma na ilikuwa ni dhahiri kuwa wale mabinti walikuwa wamechelewa shule. Nilipaki gari langu pembeni na kuwaita wale mabinti. Awali hawakuniona, badala yake akaja binti mmoja mtanashati hivi, nilimuomba aniitie wale wanafunzi ili niwasaidie kwa kuwa wamechelewa shule, ni kweli aliwaita lakini alitumia nafasi ile kuniomba lifti na yeye nimsogeze mjini maana amechelewa kazini, nilisita, lakini nilimkubalia.

Wale mabinti ambao waliniambia wanasoma Shule ya sekondari Kisutu, niliwaambia kuwa nitawasogeza mpaka maeneo ya akiba walifurahi kwa ule msaada wangu. Njiani yule binti aliyeomba lifti aliaanzisha mazungumzo, na ilionekana alitaka kunifahamu zaidi lakini nilikuwa namjibu kwa mkato tu kwa kuwa siku udadisi wake.

Aliniambia kuwa anafanya kazi kampuni moja ya mawasiliano (Jina kapuni) na alitaka kujua kama huwa napita njia ile kila siku nilimjibu kuwa ile ndio njia yangu, alitumia nafasi hiyo kuniomba niwe namsaidia kwa kumpa lifti kwa kuwa usafiri ni mgumu kweli na hawezi kugombea daladala, nilimwambia kuw akama nikimkuta njiani nitampa lifti. Tulipofika mjini nilimshusha pamoja na wale wanafunzi nami nikaenda kazini kwangu.

Siku zikapita na nikasahau kabisa habari ile, lakini siku mmoja nikiwa njiani kuelekea kazini nilikuta foleni maeneo ya kituo cha Sayansi mara nilisikia mtu akigonga kioo cha dirisha nilipotazaa nilimuona yule binti wa lifti, nilifungua kioo na kumuuliza kama anashida gani, aliniomba lifti tena, nilimfungulia mlango akaingia ndani ya gari.

Aliniambia kuwa nimekuwa nikimpita kila siku pale kituoni na hata akinisimamisha nakuwa simuoni, nilimjibu tu kuwa sikuwahi kumuona, aliniomba namba ya simu, nikamwambia sina simu, lakini alionesha msisitizo na alidai kuwa haiwezekani nimiliki gari zuri vile halafu niwe sina simu, nilimpa namba yangu ya simu.

Nilimshusha pale Posta mpya kisha nikaelekea kazini. Mke wangu alipojifungua niliomba ruksa ya kumhudumia na nikapewa siku tatu. Siku ya pili yule binti alinipigia simu majira ya usiku akitaka kujua kama nipo maana hakuniona siku hiyo. Nilimjibu kwa kifupi kuwa sitakwenda na nilimuonya kuwa asije akanipigia tena simu usiku.

Siku mbili baadae nikiwa naelekea kazini alinipigia simu akitaka kujua kama naenda kazini, nilimjibu kuwa niko njiani, na kweli nilimkuta njiani na nikampa lifti, safari hii
Alianza kunikalia mikao ya ajabu ajabu huku akipandisha mini skirt yake kiasi cha kuacha mapaja yake wazi, nilijitahidi sana kutomwangalia lakini alikuwa akinisemesha kiasi kwamba kuna wakati nililazimika kumwangalia.

Alikuwa akinidadisi sana juu ya mke wangu na akitaka kujua mengi kuhusu sisi, sikumpa ushirikiano sana nililazimika kumdanganya mambo mengi kwani huyu binti alikuwa ni mgeni kwangu na nilikuwa nampa msaada tu lakini sasa nilianza kujuta kumfahamu.

Nililazimika kubadili njia kuanzia siku ile nikawa napita barabara ya shekilango ili nitokee magomeni na kisha mjini kwa kutumia Morogoro Road, kwa hiyo nikawa nimeepusha shari. Kumbe kulikuwa kuna bomu linakuja.

Wiki moja baadae tangu nimkwepe yule binti, nikiwa nyumbani mke wangu alikuwa akitumia simu yangu, kutuma meseji kwa rafiki zake kwani yakwake iliisha credit.

Kumbe yule binti alituma meseji akiniuliza mbona sionekani siku hizi, mke wangu alijifanya ni mimi na kanza kuchat naye, yule binti alituma meseji nyingi za kimapenzi huku akimponda mke wangu na kuniahidi kunipa penzi ambalo kamwe sijawahi kulipata.

Muda wote mke wangu alipokuwa akichati na huyo hayawani mimi nilikuwa nimeweka uzingativu kwenye luninga, na ili kuwa na ushahidi zile meseji zote zilizotoka kwa huyo binti alizi forward kwenye simu yake, kisha akanipa simu yangu na kuniambia nisome meseji za mpenzi wangu kisha akaingia chumbani kulala, awali sikumwelewa lakini niliposoma zile meseji, nilipatwa na mshituko, na nikajua kuwa leo patachimbika, nilikwenda kumwamsha mke wangu ili nimweleze ukweli lakini hakukubali alikataa na alikuwa akilia sana. Nilijitahidi sana kujieleza lakini haikusaidia kitu, nilijaribu kumpigia simu yule binti lakini simu yake ilizimwa.


Nilijikuta nikiwa na wakati mgumu sana na hatukulala usiku ule kutokana na malumbano kati yangu na mke wangu. Asubuhi niliamka na kumuaga mke wangu kuwa naenda kazini lakini hakunijibu. Niliondoka nikiwa nimechnganyikiwa.

Nilipofika kazini nilimpigia simu yule binti na alipoipokea simu yangu alinishambulia kwa matusi eti nimkanye mke wangu asithubutu kumpigia simu na kumweleza upumbavu na tena amkome na kam akiendelea atamfanyizia alijue jiji, alipomaliza kusema hivyo alinikatia simu. Nilishikwa na butwaa.

Niliporudi nyumbani nilimkuta mke wangu kafura kwa hasira, kumbe mke wangu alimpigia simu yule binti ili kutaka kujua ukweli kama ana mahusiano na mimi, yule binti alimshambilia mke wangu kwa maneno makali na kunisingizia kuwa eti mimi ndiye niliyemtaka na huwa nampa lifti kila siku kumpeleka kazini na kumrudisha na nilimuahidi kuwa nitamuao.

Nilimpigia simu yule binti ili athibitishe maneno yake lakini simu yake haikupatikana. Nilijitahidi sana kumwelewesha mke wangu na kumweleza ukweli wote bila kumficha. Kidogo amenielewa, lakini amepunguza sana mapenzi na mimi, kwani amekuwa tofauti sana na mwanzo.

Baada ya kuvutana sana na mke wangu alinitaka twende tukapime ili niisije nikawa nimeambukizwa Ukimwi na huyo mwanamke na baada ya kuonekana hana, mke wangua akaniambia kuwa hatashiriki na mimi tendo la ndoa mpaka nikae miezi mitatu kwa ajili ya kupimwa kwa mara ya pili ili kudhibitisha kama sijaambukizwa Ukimwi.( Kwa mujibu wa wataalamu kwa kawaida ukimwi hauwezi kuonekana kama maambukizi ni ya hivi karibuni, wataalamu wanadai mpaka ipite miezi mitatu baada ya maambukizi ndio vipimo vinaweza kuthibitisha kama umeathirika,) sijui hili lina ukweli kiasi gani.

Tulikuwa tumejiandaa kwa ujio wa mtoto wetu wa kwanza lakini sijui hayawani yule alitokea wapi na sasa kanitibulia kila kitu, na kuiacha ndoa yangu ikiwa katika hati hati.

Kwa sasa natumia muda mwingi kuwepo nyumbani kila nitokapo kazini na niwapo off, ili niwe karibu na mke wangu na mtoto wetu mpendwa.Gabriel. Nimeweka gari yangu vioo vya Tinted ili kuepuka kidamisi kingine.

Thursday, December 17, 2009

DUH! NIMERUDI KUTOKA KUSUKA LEO 17/12-09

Mwanadada /mwanamama karudi toka kusukwa!!!
Kazi kweli kweli nilianza kusukwa hizo nywele saa sita mchana na ilipofikia saa kumi na moja jioni ndo kazi iliisha. Bahati mbaya msusi amekataa kuwa kwenye picha la sivyo mngeona jinsi nilivyopata mateso. Lakini ndo hivyo kuna msomo unasema:- Ukitaka kupendeza lazima uvumulie mateso:-) (Vill vara fin får du lida pin) Na kizuri zaidi picha hii ya leo kapiga binti yangu.

Wednesday, December 16, 2009

NGOJA TUANGALIE PICHA ZA LEO!!!!!


Hapa ni Septemba 2009 mwanadada ana manywele ya ajabu kichwani kwake. Na inaonekana kama anafanya kazi ya kublog.

Na hapa ni 16.Desemba 2009 yaani leo Jumatano mwanadada anaonekana ni mwafrika/mTanzania mwanaafro KABISA:-)
Swali je? picha ipi ni bora kuliko nyingine? au tuseme mwanadada awe na nywele za aina gani?

Tuesday, December 15, 2009

Kamala Lutatinisibwa:- nawowa jamani nafunga ndoaz

Kamala Lutatinisibwa,
kuna mijadala miingi kuhusu ndoa, kufunga ndoa na harusi katika jamii yetu. kwakuwa naishi katika jamii, nimejikuta nami nikipaswa kufunga ndoa ya kanisani kwani kumbuka kanisa sio baya na nizuri.

basi weekend hii jpili saa 7 mchana, mimi na my beloved waifu tutavaa nguo mpya na kwenda mbele ya hadhira na pasta ili tuvalishwe pete na kukla viapa kidogo nakiasi katika kanisa la KKKT pale posta.

wanablogu woote mnakaribishwa. kutakuwepo na kijisheree kidogo tu na hakuna mchango wala nini kwa wanaojisikia njooni tu.

tumelazimika kufanya hivyo baada ya wife kupata kazi anayoipenda katika KKKt na hivyo hawezi kuajiriwa nakuzaa bila kufunga ndoa kwani itakuwa muujiza huo.

NB; Chacha Wambura ndiye atakuwa bodyguard wangu siku hiyo

Monday, December 14, 2009

Haya ni baadhi ya matatizo ya kuchaguliwa mchumba

Kuna mwanadada mmoja ambaye ni miongoni mwa watu wasomi sana. Amemaliza chuo hapa mlimani. Wakati alipokuwa chuoni alibahatika kupata mchumba ambaye walikubaliana kuoana. Na walikuwa katika maelewano mazuri katika uchumba wao,

Baada ya uchumba wao huo kuendelea, aliamua kumpeleka kwa wazazi wake na kuwafahamisha kuwa mimi nimepata mtu ambaye naona atanifaa katika maisha yangu. Baada ya kuwafahamisha ishu hiyo, mama wa dada huyo alikubaliana na wazo lake la kutaka kuolewa na huyo mchumba wake lakina upande wa baba yake kulikuwa na shaka. Huyo binti alikuwa karibu sana na baba yake na aligundua kuwa baba yake hataki kukubaliana na wazo lake. Baada ya mazungumzo ya hapa na pale na baadaye mvulana yule kuondoka, binti alimfuata baba na kuzungumza naye na akasema kwa jinsi nilivyomuona huyo mvulana hakufai. Binti akamwambia si vizuri kumhukumu mtu kwa kumwangalia tu. Mimi nimekuwa naye kwa muda mrefu namfahamu vizuri sina shaka naye. Baba yake bado hakukubaliana na hilo lakini upande wa mama yake hakukuwa na shida.

Uchumba uliendelea na yule mvulana akasema inaonesha baba yako hataki kabisa, lakini nitaumia sana endapo kama bado ataendelea na msimamo wake huo. Ni mtu ambaye nimekuzoea, tumeheshimiana sana. Yule binti akamwambia kila kitu kinawezekana na itawezekana tu.

Siku moja yule binti akiwa katika mizunguko yake ya hapa na pale akiwa mjini, alikutana na kaka mmoja akiwa katika mavazi ya kijeshi, na alikuwa na mwonekano mzuri sana, lakini cha kushangaza yule kaka baada ya kumwona binti huyu aliduwaa. Baada ya kuduwa kwa kipindi aliamua kumfuata binti na kumsalimia na kumwuuliza kila kitu, na baadaye walianza kuwasiliana mawasiliano ya kawaida kabisa lakini mwanajeshi huyo alikuwa na mawazo tofauti, na ndipo siku moja akamweleza kuwa angetamani siku moja awe mke wake. Yule binti akamwambia hapana, mimi tayari nina mtu wangu na tunaheshimiana sana, akamwambia sawa. Kwa ni watu marafiki alimrudisha mpaka kwao, kumbe lengo lake yule kijana ni kutaka kujua binti anaishi wapi.
Na ndipo siku hiyo yule kijana aliamua kwenda peke yake nyumbani kwa wazazi wa binti huyo na kukutana na baba yake (Baba wa binti). Na ndipo alipozungumza ukweli wa kile alichokiona na lengo lake ni lipi. Na mzee aliweza kumdadisi kijana na kumweleza kila kitu. Kwa wakati huo yule binti pamoja na mama yake walikuwa hawapo na binti aliporudi akamweleza akaelezwa na baba yake kuwa kuna kijana mmoja alikuja yuko hivi na hivi akanieleza kila kitu, nadhani huyo ndiye atakayekufaa. Binti akamwambia hapana, wewe ndiye umemuona na mimi itabidi nimuone. Baadaye yule mjeshi akaja wakazungumza.

Baadaya ya mazunguzo marefu ya hapa na pale yule kijana mjeshi aliamua kuondoka, na kwa kuwa binti hakutaka kukorofishana na baba yake aliamua kukubaliana na mawazo yake na baadaye wakamwita tena kijana huyo mjeshi. Baadaye taratibu zote za kuoana na mjeshi huyo zikafanyika, kisha binti huyo alienda kwa mchumba wake wa kwanza na kumweleza yote yaliyotokea na kumrudishia pete ya uchumba waliyovishana hapo awali. Kijana huyo alisikitika sana kwa uamuzi aliouchukua lakini hakuwa na jinsi aliamua kufuata shinikizo la baba yake. Hatimaye baadaye yule binti aliolewa na mwanajeshi na ndoa ilifungwa kanisani.

Baada ya tu ndoa kinachotokea sasa hivi ni kwamba kosa kidogo tu anaambulia kipigo ambacho hajawahi kukipata, kiasi kwamba inampelekea kumkumbuka yule wa kwanza ambaye walikuwa wakiongea naye kwa utaratibu kabisa.

Ndipo baadaye binti (ambaye sasa ni mke wa mwanajeshi) akamtafuta yule mchumba wake wa kwanza na kumweleza kila kinachotokea. Lakini kijana huyo alijaribu kumweleza namna ya kufanya ili waendelee kuishi vizuiri na mme wake na kuzidi kumwombea ili waishi vizuri.

Kwa wakati huu kijana huyo bado hajaoa na anamweleza binti huyo kuwa itachukuwa muda mrefu kwa sababu kwanza itabidi nikusahau wewe pili nikae chini nitulie tatu nijianze upya hivyo itachukuwa muda sana.

Kikubwa zaidi ni kuwa binti huyo amekubali kuolewa na mwanajeshi kwa shinikizo la baba yake, lakini kinachoendelea ni kwamba kosa dogo tu anaambuliwa kipigo kisicho cha kawaida na kinachomuuma zaidi huyo dada ni kuwa siku walipotoka OUT walienda sehemu ile ile ambayo walikuwa wakienda na mvulana yule wa kwanza na hivyo kuumia zaidi.

Sasa dada huyu anaomba mawazo, ushauri na maoni afanyaje?
Makala hii inataoka Jamii Forum. Nimeona si mbaya kama tutaweza kujadili kwa pamoja hapa kibarazani.

zijue dondoo muhimu za kutunza kucha zako

Wanawake na hata Wanaume wanashauriwa kuzingatia usafi wa kucha zao, kwani kucha inapokuwa safi inamfanya muhusika kuwa na mvuto na mwenye kupendeza.

Wanawake wengi na hata Wanaume pia wanaume hupenda kutunza kucha zao, kwani hujikuta wakikutana na vikwazo vya kushindwa kukabiliana na matatizo ya kukatika kwa kucha zao, kutokana na kusahau masuala kadhaa muhimu wanayopaswa kuzingatia ili kuzipa kucha uimara na afya njema pia.

Kwanza kabisa ni marufuku mtu kula kucha zake kwani nasema hivyo kwa sababu wapo baadhi ya watu ambao hupenda kula kucha zao, hivyo husababisha kuzikata bila mpangilio maalumu na wakati mwingine husababisha vidonda kwani hula mpaka nyama zinazogusana na kucha.

Tumia glovsi au hata mfuko wa plastiki unaposhika vitu vyenye kemikali, kwani vinaweza kuharibu kucha zako kama dawa za nywele.

Dawa hizi za nywele ni kali sana hivyo huleta madhara makubwa endapo itashikwa bila kizuizi chochote na kusababisha rangi hiyo kushindwa kukaa vizuri.

Safisha kucha zako mara kwa mara kwa kutumia vifaa maalum wanashauri kusafisha kucha zako kwa kutumia maji ya uvuguvugu.

Usitumia kucha zako kukwangulia vitu vigumu, kuparua au kuzolea uchafu. Kwani watu wengi hupenda kukwangua vocha za simu kwa kutumia kucha zao, hii husababisha kucha zako kukatika vibaya na kuwa na uchafu mweusi usiopendeza.

Usitoe hovyo vinyama vinavyojitokeza pembeni mwa kucha kwani vipo vifaa maalum vya kutolea vinyama hivyo, unashauriwa kutumia vifaa hivyo ili kuziwezesha kucha zako kupumua pamoja na kukuwa vizuri.

Paka rangi kucha zako mara kwa mara kwani wakati mwingine unashauriwa kumechisha rangi ya kucha zako na baadhi ya rangi ya nguo utakazovaa.

Tumia dawa maalumu ya kutoa rangi maarufu kama remover, baada ya kutoa rangi hiyo kwa kiwembeau kitu chenye makali.

Sunday, December 13, 2009

Hongera kaka John Mwaipopo kwa kuongeza mwaka"!!!


Katika pitapita zangu nimekuta kaka mwaipopo anatimiza miaka leo. Lakini sijui
ni miaka mingapi umetimiza?. Hongora kaka JOHN KWA SIKU HII MAALUMU.

Ni Jumapili ya tatu ya majilio:- Ngoja tusali Sala ya Wazazi wakiwaombea Watoto wao

Tunawaangalia , Ee Bwana
Hawa uliotujalia.
Katika hawa tunajiona sisi wenyewe.
Je, kweli tulikuwa hivi sisi
Tulipokuwa watoto?

Tulipigana hivi?
Tulipaga kelele hivi?
Tulileta furaha namna hii
Na mateso namna hii kwa wazazi wtu?
Tunashangaa na kujiuliza....

Tunajaribu kukumbuka-----
Kukumbuka jinsi ilivyokuwa
Tulipokuwa watoto wadogo bado
Tukiwatazama watu wakubwa.

Wakati mwingine wanatutia wasiwasi, Bwana.
Au kwa namna nzuri zaidi, tunajitia wasiwasi sisi wenyewe
Kwani si rahisi kuwa sawa daima.

Lakini kuna furaha pia,
Furaha kubwa wanayotuletea;
Nao hutufanya tuone fahari,
kwani ni watoto wema.

Tunakushukuru kwa ajili yao Bwana,
Wao ndiyo zawadi yako bora kwetu,
baada yetu sisi wenyewe.

Utusaidie
tuunganisha mikono yetu na mkono yako
Ili, Ee Baba,
Wawe kweli
Watoto wetu.
Amina.
JUMPILI NJEMA KWA WOTE

Friday, December 11, 2009

Mwanamke maarufu kuliko wote duniani....

Kila mtu akiulizwa ni mwanamke gani maarufu au aliye ngangari zaidi, kama anatafakari vizuri, atasema kuwa ni mama yake, hasa kama alimlea kwa uadilifu. Pengine mwingine atasema ni mkewe, kutegemea na namna wanavyoishi kwenye uhusiano wao wa kindoa.
Lakini, linapokuja suala la mwanamke ambaye hakuhusu, ambaye unaamini au kudhani kwamba, ndiye ngangari zaidi hapa duniani, hasa katika siasa na uchumi, inaweza kuwa mtihani mgumu kwako kutoa jibu sahihi.
Ni kweli, unaweza kutoa jibu, lakini siyo lazima jibu lako liwe sahihi.
Kama ni sahihi, itakuwa ni kwa sababu tu, unamjua huyo uliyemtaja, na wengine huwajui.
Hivi ndivyo ambavyo imetokea kwenye kura iliyofanyika ya kuwataja wanawake wanaodhaniwa kuwa maarufu hapa chini ya jua kwenye nyanja ya siasa na uchumi.
Karibu kila Mtanzania angetarajia kuwa wakitajwa wanawake 100 duninai ambao ni maarufu kwa sasa, huenda Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Dk. Asha Rose Migiro angetajwa. Matarajio hayo yangetokana na sababu mbalimbali.
Kwanza, unaibu wa Katibu Mkuu wa UN, siyo nafasi ndogo hapa duniani. Pili, kwa mwanamke kutoka Afrika tena kwa nchi ambayo ni miongoni mwa zile maskini kabisa, kushika nafasi hiyo, ni jambo la kinasibu zaidi kwa mitazamo ya mgawanyo wa dunia. Tatu, ingetarajiwa naibu atoke angalau bara Amerika, kwani Katibu Mkuu anatoka Asia, bara maskini karibu sawa na Afrika kwa uwiano.
Kwa bahati mbaya, jarida maarufu duniani kwa kufanya tathmini za viwango mbalimbali kuanzia utajiri, uzuri na umaarufu wa binadamu, la Forbes linaonesha katika taarifa zake za wiki mbili zilizopita kwamba, Migiro hayumo kwenye orodha ya wanawake 100 maarufu duniani katika nyanja za uchumi na siasa.
Kutoka Afrika ni wanawake wawili tu walio kwenye orodha hiyo. Kwanza ni , Waziri Mkuu wa Msumbiji, ambaye anashikilia nafasi ya 89 diuniani kwa umaarufu. Halafu anafuatiwa na Rais wa Liberia, , ambaye anashikilia nafasi ya 100.
Hii ina maana kwamba, Waziri Mkuu wa Msumbiji ni maarufu zaidi duniani, ukilinganisha na Rais wa Liberia, , nchi iliyoweka historia duniani kwa vurugu kubwa za kisiasa, zilizopelekea marais wawili kuuawa kinyama na mmoja kupamba vyombo vha habari dunia kuhusiana na mashtaka ya mauaji ya kimbari.
Rais Ellen Johnson ndiye Rais wa kwanza mwanamke barani Afrika, lakini anakuwa Rais baada ya uchaguizi huru na wa haki uliofuatia umwagikaji wa damu nyingi ya kutosha. Bado huyu anashikilia nafasi ya 100, wakati Waziri Mkuu wa Msumbiji anashikilia nafasi ya 89!
Hapa ndipo ambapo matokeo haya ya jarida la Fobes yanatia mashaka. Ni kweli kwamba, uchaguzi huo umefuatia kura kutoka kwa watu duniani kote.
Bahati mbaya ni kwamba, kura hizo kwa sehemu kubwa zimehusisha matumizi ya vyombo vya kisasa ambavyo havipo kwa wingi Afrika, hasa mtandano wa intaneti.
Katika orodha hiyo kuna majina ya wanawake ambayo huenda kwa umaarufu, akili ya kawaida inaweza kukuonesha kwamba, hawawezi kumzidi Asha Rose Migiro. Hebu kwa mfano, tuchukulie mwanamke kama , ambaye ni mtendaji kuuu wa Benki ya Leumi ya Israeli. Je, huyu mama uliwahi kumsikia au hata kumsoma kwenye chombo chochote cha nje? Huyu anashikilia nafasi ya 83 kwa umaarufu.
Huenda inabidi Afrika nayo sasa iwe na utaratibu wa kutafuta maoni ya dunia nzima ambapo waafrika nao watashiriki sawa kusema kuhusu nini wanaona, sawa na watu wengine duniani. Inaonekana wazi kwamba, hata viwango vya umaskini vinavyopangwa kutoka Ulaya na Marekani ni kwa vigezo ambavyo havifutu na kukidhi ukweli mkubwa zaidi unaowahusu Waafrika.
Kwenye orodha hiyo, inaonekana kuwa, Rais wa Ujerumani, , ndiye mwanamke maarufu zaidi duniani. Wu yi, ambaye ni makamu mwa Rais wa China anashikilia nafasi ya pili.
Nafasi ya tatu inashikiliwa na ambaye ni mtendaji mkuu wa kampuni ya Temasek Holdings, ya Singapore.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, anashikilia nafasi ya nne.
Wengine ni , mwenyekiti wa kampuni ya PepsiCo ya Marekani. Namba sita ni , Rais wa India. Namba saba imeenda kwa, mtendaji Mkuu wa kampuni ya Anglo American ya Uingereza.
Nafasi ya nane anaishikilia ambaye ni mwenyekiti, kampuni ya Archer Daniels Midland ya marekani.
Namba tisa ni , mwenyekiti kampuni ya Kraft Foods ya Marekani, na namba kumi ni , Mtendaji Mkuu wa Alcatel-Lucent ya Marekani.
anashikilia nafasi ya 21, wakati Malkia Elizabeth anashikilia nafasi ya 23.
Mke wa Rais wa zamani wa Marekani, , anashikilia nafasi ya 25.
Kama orodha hii ya Forbes inaonesha ukweli na uhalisia wa umaarufu unaotokana na michango ya wanawake katika jamii zao au jamii ya dunia, ina maana kwamba, kwa Afrika, wanawake hawajafanya lolote kwa jamii zao na jamii ya dunia.
Lakini, huo utakuwa pia ni uongo mkubwa, kwa sababu kuna idadi kubwa ya wanawke hapa Afrika ambao wamejitahidi kwa viwango vya kimataifa kubadili hali za watu wengine katika jamii.
Kama ni umaarufu kwa maana ya kujitangaza na kutangazwa sana na vyombo vya habari, ni wazi suala zima linakosa mantiki na linajaribu tu kuwavunja moyo wanawake wa Afrika. Orodha hiyo ni wanawake maarufu duniani katika nyanja za siasa na uchumi, ambapo ni uongo kudai kwamba, kati ya wanawake 100 duniani, Afrika inaambulia nafasi mbili, tena za mwisho.
Hii ina maana dunia inawatambua wanawake wawili tu Afrika katika nyanja hizo? Ndiyo maana naamini kwamba, Migiro angepaswa kuwemo kwenye orodha hiyo, kama kweli inakagua mambo kwa uhalali.
Lakini, mtu akikagua orodha hii tena na tena anaweza kupata picha kubwa zaidi na kuikubali, ingawa baadaye anaweza kuipinga. Ni matokeo ya kura yenye utata. Kwa mfano, Hilary Clinton anafahamika, kama ilivyo kwa Oprah Winfrey, lakini nao wametupwa hadi nafasi za 20, kama ilivyo kwa Malkia Elizabeth.
Lakini, hapohapo kuna majina kati ya namba 11 hadi 20, ambayo ni ya wanawake ambao hata watazamaji, wasomaji na wasikilizaji wazuri wa vyombo vya habari vya nje hawajawahi kuwasikia.
Kama ilivyo kwenye nyanja nyingine, hasa uchumi, vyombo vya habari vya Magharibi, bado vinaitendea Afrika kama vile ni bara wanamoishi wanyama, badala ya binadamu.
Vyombo vyetu vya habari, kwa bahati mbaya, navyo ni kama sauti za vyombo vya habari vya Magharibi.
Vikifanya tafiti zao, vinafanya kwa njia finyu na iliyofubaa, isiyoweza kuwahamasisha Waafrika.

Hii iliandikwa kwenye gazeti la jitambue iliandikwa na Hayati Munga Tehenan.

Thursday, December 10, 2009

HONGERA KWA SIKU YA KUZALIWA ABRAHAM!!!!!!

Mtoto Abraham miaka 2 leo.


Leo tarehe 10 Desemba 2009 mtoto huyu anatimiza miaka miwili kamili tangu kuzaliwa kwake. Ni furaha iliyoje kwake kushrehekea siku yake hii ya kuzaliwa huku akiendelea kukua kwa umri na kimo pamoja na afya njema.

Safari ya kutimiza mwaka huu wa pili haikuwa rahisi sana kwa mtoto huyu. Mnamo tarehe 20 Juni 2009, binadamu fulani ambao kutokana na tamaa zao za kutafuta fedha kwa njia ambayo ni ya kudhuru, walitaka kukatisha uhai wa mtoto huyu kwa kumtumia kama ngao ya kutaka kupata kile walichotaka.

Akiwa amening’inizwa kichwa chini miguu juu huku panga lenye makali ya kutisha likiwa shingoni, tayari kwa kukata kichwa iwapo wazazi wake wasingetekeleza kile walichotaka wadhalimu hao, mtoto huyu aliendelea kuwa mtulivu.

Wazazi wa mtoto huyu waliona fedha na vitu vingine haviwezi kuwa na thamani zaidi ya ya uhai wa mtoto wao, walikubali kupoteza vyote na sio mtoto wao mpendwa.

Pamoja na msukosuko huo, mtoto huyu ameendelea kukua huku akiwa na afya njema, na furaha tele. Hiyo inadhihirisha kwamba tukio lile ni ishara ya ujasiri alionao.

Mungu amjaalie mtoto huyu akue kwa umri na kimo ili aje aitumikie jamii na kuifanya dunia hii kuwa ni mahali salama pa kuishi.

Happy Birthday Mtoto Abraham Shabani Kaluse.

Picha kwa hisani ya Utambuzi na kujitambua Blog.

Wednesday, December 9, 2009

TANZANIA BARA LEO INATIMIZA MIAKA 48 YA UHURU



Ni siku ya UHURU NA JAMHURI kwa taifa lote la watanzania kokote walipo.

Monday, December 7, 2009

KWA NINI WANAUME WANASHINDWA KULING'AMUA HILI?

Kuna wakati niliwahi kueleza juu ya wanaume kudhani kuwa kuwanunulia wake au wapenzi wao kila kitu kwa maana ya nyumba nzuri, magari ya kifahari na mavazi ya thamani, inatosha kupeleka ujumbe kwa mke au mpenzi wake kuwa anapendwa. Nilieleza kwa kirefu sana juu ya dhana hiyo jinsi isivyo sahihi na niliweka bayana kuwa, wanawake ni viumbe wanaohitaji kusikilizwa kuliko kitu kingine, bila shaka mlio wengi mnakumbuka makala hiyo.

Kwa asili wanaume wanapenda sana kuwasikia wake au wapenzi wao wakikiri kuwa wanawapenda na kufurahia tabia zao nzuri wema walio nao, vipaji walivyo navyo na sifa nyingine lukuki. Wanaume wanapopewa sifa za aina hii na wake au wapenzi wao hufurahia na kupata nguvu na kuona kwamba wana thamani kubwa mbele ya wake au wapenzi wao, kinyume na hivyo wanaume hukerwa na kutowajali wake zao.

Pamoja na kuoneshwa upendo lakini hata hivyo hiyo haitoshi kuwafanya wanaume wawapende na kuwajali wake au wapenzi wao. Kuna wakati mwanaume anakuwa na kazi nyingi sana na anatumia muda mwingi kwenye kujisomea au kuangalia Luninga, hata pale mke au mpenzi wake anaponyesha kwamba anahitaji kuwa naye kwa muda fulani. Kuna wakati pia mwanaume anajali zaidi kazi zake kuliko mambo mengine ambayo mkewe anayataka na kuyaona ya maana.

Naamini wengi mtakuwa ni mashahidi wa kauli hizi, “Yaani niache kazi zangu nikae kukusikiliza wewe na upuuzi wako, subiri nikipata muda tutaongea mambo hayo” kauli hizi ni sumu kali sana katika uhusiano, na huchangia kwa kiasi kikubwa ndoa na mahusiano ya wapenzi wengi kuporomoka.

Ni kweli kuwa kuna wakati mwanaume anaweza kuwa bize na shughuli zake,lakini pale mke au mpenzi wake anapohitaji ukaribu na yeye ni wajibu wake kuonesha kujali.
Kama mwanamke anahitaji kufanya jambo fulani ambalo inabidi mwanaume amsaidie, lakini inapotokea mwanaume kuonyesha kwamba hajali sana juu ya jambo hilo bila kujali kama yuko bize au hayuko bize, mwanamke huhisi kutothaminiwa na hiyo humuumiza sana kihisia. Lakini kama mwanaume ataonesha kujali hisia za mkewe na kumsikiliza kwa makini hata kama hatatoa ushirikiano hiyo tu inatosha kumridhisha mke au mpenzi kuhisi kuwa anapendwa na anasikilizwa.

Lakini utakuta wanaume wengi hawajali utashi wa kihisia wa wake zao na huamini kwamba wanawake wanachohitaji ni kupewa fedha au mali na kuhakikishiwa maisha ya kifahari basi.
Ukweli ni kwamba wanawake wanahitaji sana kusikilizwa hisia zao na kupewa nafasi pekee na mume au mpenzi wake pale anapohitaji nafasi hiyo ya kusikilizwa. Kumuonesha mwanamke kwamba hana thamani na hana nafasi ya kusikilizwa na badala yake kazi na kusoma, au kuangalia luninga kukaonekana ndio kuna thamani kuliko yeye ni kosa kubwa.

Ni jambo la msingi sana kwa wanaume kulifahamu hili kwa ustawi wa ndoa au mahusiano yao na wake au wapenzi wao, kwani wanawake wanahitaji nafasi kutoka kwa wanaume au wapenzi wao zaidi ya kitu kingine, maana hayo mengine yatakuja kujazia tu.

Sunday, December 6, 2009

KUELEKEA MIAKA 48 YA UHURU: TANZANIA YETU NA ELIMU ZA CHINI YA MITI

Nimevutiwa sana habari iliyowekwa na Profesa Mbele kwenye kibaraza chake akizungumzia juu ya mustakabali wa elimu huko nyumbani Tanzania, bofya hapa umsome .

Hakika habari hiyo imenikumbusha mbali sana yaani simulizi nilizopata toka kwa baba na mama yangu. Maana wao pia wamepata elimu ya aina hii, nakumbuka wakati fulani nilipokuwa mdogo nikisoma shule ya msingi wakati huo mama yangu alinisimulia kuwa wakati alipokuwa akisoma shule ya msingi alikuwa anatembea masaa yasiyopungua matano kutoka nyumbani kwao mpaka shuleni.

Baba naye alinisimulia kuwa yeye alipata elimu yake chini ya mti wa mkorosho na huku akiwa amevaa LUBEGA YA KANIKI (kufunga nguo nyeusi shingoni) lakini hata hivyo alimudu kupata elimu bora mpaka akawa mwalimu.

Kumbuka kwamba walikuwa wanazungumzia mambo ya miaka ya 60 wakati huo tukiwa ndio nchi yetu imejipatia uhuru na kuanza kujitawala. Wakati huo wananchi waalikuwa na mwamko wa Elimu huku wakichagizwa na serikali yao walimudu kusoma hata chini ya miti kwani kulikuwa na kampeni maalum iliyoanzishwa na serikali ya awamu ya kwanza ya kuhakikisha kuwa kila mtu anapata elimu ikiwa ni pamoja na elimu ya watu wazima. Wakati huo Serikali ilikuwa imetangaza vita ya kuwashinda maadui watatu ambao ni Ujinga , Maradhi na Umasikini, na tuliambiwa kuwa hauwezi kuwashinda maadui wawili yaani maradhi na umasikini iwapo hatutafuta ujinga, na ili tufute ujinga ilikuwa ni lazima watu wapate elimu, kwa hiyo swala halikuwa ni madarasa mazuri yaliyonakishiwa bali ilikuwa ni elimu kwanza, hata ikibidi chini ya miti ilimradi watu wapate elimu, halafu baada ya hapo hao maadui wengine yaani umasikini na maradhi itakuwa ni rahisi kuyashinda.

Wiki ijayo tunashereheka miaka 48 tangu tujitawale. Hii ina maana kwamba kama ni mtoto alizaliwa wakati huo tunapata uhuru, basi atakuwa ni mtu mzima ambaye amekwishajitambua na kumudu kujitafutia kipato na kujitegemea. Hapa nazungumzia mtu mzima ambaye amezaliwa akiwa na hana dosari ya kimaumbile yaani sio mlemavu, maana kama angekuwa ni mlemavu tungesema kuwa atakuwa anahitaji uangalizi ili amudu kusimama mwenyewe. Nchi yetu inayo utajiri wa asili kwa maana ya kuwa na ardhi yenye rutuba, madini,uoto wa asili, Misitu, na mbuga za wanyama. Hebu tujiulize hapa, hivi kama utajiri huo tulio nao ungetumika kwa busara hivi kweli tungekuwa na watoto wanaosomea chini ya miti leo hii hata baada ta miaka 48 ya uhuru?

Hii ni sawa na kijana aliyezaliwa miaka 48 iliyopita akiwa na siha nzuri, halafu akakuta baba yake amemuachia utajiri wa kila aina lakini akabaki kulia umasikini na kuishia kuombaomba.Ni aibu iliyoje nchi yetu hata baada ya miaka 48 ya uhuru bado tunaombaomba na kulia eti sisi ni masikini wakati Wenzetu wanakimbilia katika nchi yetu na kujichotea utajiri na kuhamishia kwao utadhani shamba la bibi.

Raisi wetu haishi safari za nje na hata alipoulizwa wakati fulani sababu ya yeye kusafiri mara kwa mara nje ya nchi, alidai kuwa kama ni kuomba misaada katika nchi hizo anazotembelea hawezi kumtuma waziri wake au mtu mwingine kwa sababu hawawezi kupewa kile watakachoomba, isipokuwa yeye.

Yaani mpaka leo hii Raisi wetu anajisifu kwa kuomba tena wazi wazi, wakati hilo ni jambo lenye kutia aibu. Wazungu ni watu wa ajabu sana, wakati unapowaomba misaada wataongea na wewe kwa bashasha na kwa akili ndogo utadhani wanakujali sana lakini amini kwamba ukiondoka huku nyuma wanakung’ong’a na kukudharau sana. Na usidhani huo utakaopewa ni msaada wa bure, ni lazima tu utaulipa kwa namna yoyote.

Na ndio maana hata mheshimiwa Rais akasema kwamba akienda yeye ni rahisi kupewa kwa sababu yeye ndiye mwenye jibu la mwisho. Kwa mfano kama waziri wa Nishati na madini akienda kuomba misaada na akapewa sharti la kuipatia tenda kampuni maarufu ya nchi hiyo ili ije ichimbe madini au Gesi hapa nchini kwa mrahaba mdogo, itakuwa ni vigumu kwa waziri huyo kutoa jibu la moja kwa moja bila kushauriana na mheshimiwa rais, hivyo kutakuwana mlolongo wa safari za kwenda na kurudi mpaka kufikia makubaliano wakati akienda Raisi mwenyewe anakuwa na jibu moja tu, ndio au hapana.

Nchi yetu bado inayo kiwango kidogo cha ongezeko la watu, hii ina maana kwamba bado tunayo ardhi ya kutosha na kwa kuwa bado kuna mapori wananchi wamekuwa wakitawanyika huku na huko kujitafutua makazi na kutafuta ardhi yenye rutuba kwa ajili ya kilimo, lakini cha kushangaza serikali yetu bado imelala usingizi wa samaki aina ya pono bila kuharakisha usambazaji wa miundo mbinu katika maeneo mapya yanayokaliwa na watu. Ni aibu mpaka sasa serikali kusubiri ripoti za vyombo vya habari ili kupata taarifa kuwa ni mahali gani wananchi wanahitaji shule, barabara, zahanati na maji safi.

Na ndio maana wananchi wanaamua kujianzishia shule zao chini ya miti na kutafuta mwalimu ili watoto wao wapate elimu. Kuliko watoto kutembea masaa matatu kwenda shule na masaa matatu kurudi nyumbani . Zamani hatari kubwa iliyohofiwa na wazazi juu ya watoto wao wanapokwenda shule za mbali ilikuwa ni wanyama wakali na nyoka, lakini siku hizi mambo ni tofauti, kuna kubakwa kwa watoto wa kike au hata kuuawa na kukatwa viungo au kuchunwa ngozi.

Athari za watoto kusoma mbali ni nyingi sana lakini kubwa kabisa ni uchovu na njaa. Ni jambo lisilo na ubishi kuwa ni vigumu hata wanafunzi kumuelewa mwalimu kutokana na kusinzia. Maana hapo watakuwa wamechoka. Kwani mwendo mwingi waliutumia kutembea na wakifika shuleni ni kusinzia tu.

Kwa ujumla naweza kusema , mwalimu ni muhimu kuliko vyote.Lakini mazingira ni muhimu pia. Bila kusahau wanafunzi wenye afya na wenye shibe ili kumudu kusoma na kuelewa kile wanachofundishwa na waalimu wao.

JUMAPILI YA LEO NAPENDA KUSALI SALA HII KWA WAGONJWA

Na tuwaombee wagonjwa
EWE Baba Mwenyezi, Mpaji wa maisha na afya, twakuomba uwaangalie kwa rehema wagonjwa wote, hasa wao wanaotakiwa maombi yetu, ili kwa baraka yako juu yao, na juu ya wao wawatumikiao, ikiwa mapenzi yako warudishiwe afya yao ya -mwili na ya roho, nao wakutolee shukrani katika kanisa lako takatifu; kwa Yesu Kristo, Bwana wetu. Amina.

Friday, December 4, 2009

Hongera wajina wangu kwa siku ya kuzaliwa:- Yasinta

Leo napenda kuwapongeza shangazi zangu kwa siku zao za kuzaliwa. Lakini hasa kwa siku hii ya leo napenda kumpongeza wajina wangu Yasinta kwa kutimiza miaka 6. HONGERA sana kwa siku yako wajina na uwe na wakati mzuri na Mungu akulinde ukue na uwe msichana mwema na pia uwe na afya njema.

Thursday, December 3, 2009

Sheria/Utaratibu/Maoni tofauti

Kuna mambo mengine huku ughaibuni ukiyafananisha na huko nyumbani unabaki na maswali chungu mzima, kuna wakati niliwahi kuzungumzia juu ya taratibu za mazishi hapa Sweden.

Lakini hebu leo tuangalie upande wa mambo ya starehe hususan pombe na sigara.
Tuanze na ununuzi wa pombe, ununuzi wa pombe hapa ni tofauti sana na nyumbani TZ. Hapa huruhusiwi kununua pombe kama hujatimiza miaka 20 na ni lazima uonyeshe kitambulisho.

Haya yalinipata mie siku moja nilikuwa kwenye duka la pombe nilikuwa nataka ninunue pombe. Kilichotokea ni kwamba nilikataliwa na hata nilipowaonyesha kitambulisho changu walibisha . Nilitoka bila pombe, toka siku hiyo sipendi kabisa kwenda kwenye duka lile la pombe. Yaani hawakuniamini kabisa miaka yangu.
Sio kama TZ unamtuma mtoto wa miaka 5 kununua pombe bila wasiwasi kabisa

Sheria hii vivyo hivyo kwenye kununua sigara ni lazima uwe na miaka 20 au zaidi. Lakini cha ajabu utakuta watoto wa shule za msingi wanavuta sigara. Na utajiuliza wamepata wapi ? Ndiyo! Magendo yapo Ulimwenguni kote wanawatuma kaka zao,dada zao, au hata wazazi wao wawasaidie kuwatafutia vitu kama hivyo

Kwa hiyo hapa ukiwa na umbo dogo ni vigumu kupata huduma ya pombe au sigara hata kama una miaka 40. Sweden ni nchi yenye sheria kali kidogo sio nawatisha hapana. Hapa kila mtu ana namba ya utambulisho (person number) na ni lazima uijue kwani karibu kila sehemu unatakiwa kuitaja hiyo namba.

Hata hivyo pamoja na masharti hayo pamoja na sheria zao kali msije mkadhani kuwa kuna nidhamu ya hali ya juu kwa watoto, hiyo ni kujidanganya, kwani kuna ukosefu wa nidhamu miongoni mwa watoto na vitu kama pombe, sigara na madawa ya kulevywa yanatumiwa sana na watoto na hivyo nidhamu kushuka kwa kiasi fulani.

Wapo watoto wenye nidhamu, lakini kuna wale ambao kutokana na aidha malezi au wazazi kutalikiana na hivyo kujikuta wakiwa hawapati malezi yanayostahili, wengi wametumbukia kwenye matumizi ya pombe na sigara na hata madawa ya kulevya wakitafuta faraja.

Sina uhakika na huko nyumbani juu ya sheria hii kama inatekelezwa na kama inatekelezwa , je ni kwa kiasi gani? Lipo tatizo moja ambalo niliona hapo nyumbani Tanzania, kuna mlolongo wa visheria vidogovidogo ambavyo vinatungwa kwa staili ya kuzima moto hasa pale linapotokea tatizo, lakini baada ya muda mfupi tu, husahaulika na watu wanaendelea kuvunja hiyo sheria kama kawaida. ”Sidhani nitakosea kusema kuwa inawezekana sheria ipo, lakini je ni kweli na inafanya kazi?”