Wednesday, March 31, 2010

Tusisahau nyimbo za utotoni na za zamani +nimekumbuka zamani leo!!

Sungura mjanja wee



Mwenzenu leo nimeamka na kujikuta naimba wimbo huu yaani nimekumbuka kweli nilipokuwa darasa la kwanza na pili haya unganeni nami na tuimbe:-

1. Sungura sungura mjanja wee x 2
Ingawa mdogo hushinda wakubwa x 2

2. Akili akili zatoka wapi x2
Ingawa mdogo hushinda wakubwa x 2


3. Akili watoto sisi tunazo x 2
Hata za kumshinda mjanja sungura x 2

4. Akili watoto sisi tunazo x 2
Shuleni twafunzwa mambo mbalimbali x 2




Tuesday, March 30, 2010

Robo mwaka inakatika...Tumesonga mbele ama nyuma???

Amani, Heshima na Upendo kwenu.



Kwanza namshukuru MUNGU kwa baraka ya uhai ambayo mimi nawe tunayo.
Pili nikupe pole kwa harakati za maisha ambazo sote twazipitia kufanikisha yale mema tupendayo.
Nafurahi kuwasiliana na kila mmoja wetu kuweza kuwaza changamoto zilizo mbele yetu kama JAMII YA WANA-BLOG wenye lengo la kuigusa jamii na kisha tujiulize kama tunasonga mbele ama nyuma katika harakati zetu. Nashukuru kwa blogs na tovuti mpya ambazo zinachipuka na kuendeleza nia njema ya kuigusa jamii. Kaka Luta Kamala aliwahi kuandika akijuliza KWANINI TUNA-BLOG? (http://kamalaluta.blogspot.com/2009/07/swali-kwa-wenye-blogu.html) na hata Kaka Chambi Chachage aliuliza kama uwepo wa blog zetu unakuza ama kufifisha tasnia nzima ya uandishi (http://udadisi.blogspot.com/2009/08/blogu-zinachochea-au-zinafifisha.html). Jibu halisi tunalo mioyoni mwetu kulingana na dhamira tulizonazo.
Lakini kwa ujumla, haijalishi ni sababu gani ilikufanya u-blog, mwisho wa safari sote tunajikuta na zao moja ambalo ni JAMII. Awekaye picha anataka kuionesha jamii alichokiona, ahabarishaye anataka kuihabarisha jamii. Yule aandikaye Utambuzi anataka jamii ijitambue. Anayeweka kumbukumbu ni sababu anataka jamii ije isome baadaye. Atangazaye biashara anataka jamii ijue ilipo huduma. Afunzaye mapishi, mitandao, mavwazi, mitindo nk, woote wanalenga katika kuielimisha jamii.
Kwa maana nyingine sote twaiandikia JAMII.
Lakini je, mwaka huu ambao unamaliza robo yake ya kwanza wiki hii unaonekana kuwa hatua gani kwetu? Tumeshuhudia KUTHAMINIKA KWA KAZI ZA BLOGGERS kwa aina mbalimbali.
Tuliona wenzetu wakitunukiwa vyeti vya kuthamini kazi zao, tumesikia wengine (kupitia utambulisho wa blog zao) wamepata nafasi ya kushiriki vipindi vya idhaa za kimataifa kufanya uchambuzi wa habari. Hivi juzi tumemuona Kaka Michuzi akishiriki Diaspora huko London kwa nafasi yake kama blogger. Hizi ni chachu kwetu kuwa kuna kuonekana mchango wa kile tufanyacho na pia kuna kukua kwa ueleweka wa kazi zetu.
Ninalowaza ni VIPI TUNAWEZA KUWEKA NGUVU NA JITIHADA ZETU PAMOJA KUWEZA KUITUMIKIA VEMA JAMII?
Mafanikio ya blogger mmoja mmoja yanaweza kudhihirisha kuwa TUNAWEZA na tunalostahili kufanya ni kushirikiana na kuwa makini katika kila jema tutendalo.

Tunapoianza robo ya pii ya mwaka 2010, tuangalie nyuma na kujiuliza, robo ya mwaka inakatika....Tumesonga mbele ama nyuma??
Na hii iwe CHANGAMOTO YETU sote

Baraka kwenu nyote

http://www.changamotoyetu.blogspot.com

Monday, March 29, 2010

Nani wa kwanza kujulishwa mtoto anapozaliwa??

Nimewahi kusuluhisha ugomvi uliotishia ndoa ya mtu mmoja.

Mkewe alipojifungua mtoto wao wa kwanza aliwaambia kwanza rafiki zake (mashosti au mashoga zake) wote na mmoja wao ndiye aliyemwambia kwa msg mume kuwa kapata mtoto na jinsia ya mtoto. Mume akiwa haamini kama mkewe anaweza kujifungua bila kumjulisha alianza kwa kubisha na baadaye alipokwenda kumtazama alipokuwa amepumzishwa alimkuta kweli mkewe kajifungua na alipokagua simu yake alijiridhisha kuwa amejifungua zaidi ya masaa mawili yaliyopita na muda wote huo tayari alikuwa kishawajulisha mashosti wake wote bila kumkumbuka mumewe, mume alidai mkewe kamdhalilisha sana na hampendi tena.

Kwa mujibu wa maelezo yao hawakuwa na ugomvi wowote na wakati wote mama alipokuwa kwenye chumba cha kujifungulia mume alikuwa nje katika maeneo ya hospitali anahangaika huko na huko kuweka mambo sawa mama amaliza shughuli salama.

mnaonaje waungwana, nani anapaswa kuwa wa kwanza kujulishwa?

Mada hii nimeichukua kutoka JAMII FUROM, nami nimevutiwa nayo nikaona sio vibaya kuiweka hapa na tujadili kwa pamoja

Karibu kwenye ulimwengu wa Ku-blog kaka Renatus Kiluvia!!!




Mimi ni mwandishi wa habari na mtangazaji wa kituo cha redio cha 87.8 Ebony fm cha Iringa lakini mimi niko Dar-Mini Studio, naitwa Renatus Kiluvia,ni mmoja wa wafuatiliaji wazuri wa blog yako,naomba msaada wako wa kunitangazia blog yangu mpya http://www.muzikinamaisha.blogspot.com/ ,blog yangu inahusu muziki na maisha katika nyanja tofauti-tofauti,pia itahusika kuzungumzia burudani zingine kama filamu n.k.
Akhsante!!!!!!!!!!!

Sunday, March 28, 2010

NIMEFUNGUA BLOG MPYA!!!


Hatimaye leo nimeamua kufungua blog mpya yenye uasili wangu sio mwingine tena ni uasili wa kingoni KARIBUNI SANA WOTE. http://ungoni.blogspot.com/

Sala kabla kula chakula + Jumapili njema kwa wote!!

Kwa jina la baba na mwana na roho mtakatifu, Utubarikie Mungu wetu sisi na chakula chetu tupate nguvu ya kukutumikia vema Amina. NAWATAKIENI WOTE AMANI KATIKA JUMAPILI HII YA MATAWI NA YA 13 PIA YA MWISHO YA MWEZI HUU MACHI NA WOTE MNAPENDWA!!


Friday, March 26, 2010

Mgomo utamuathiri kila Mtanzania

Tanzania iko katika wasiwasi wa mgomo mkubwa ambao haujawahi kutokea nchini. Wafanyakzi wamekuwa na madai takriban matatu ya msingi ambayo wanataka Serikali iyashughulikie. Dai la kwanza ni Ongezeko la kima cha chini cha mshahara ambapo wameiomba serikali kupandisha kima hicho kutoka sh. 80,000 hadi 315,000 lakini Serikali iliongeza asilimia kidogo sana na ku[pandisha hadi sh. 84,000 tu. Dai lingine wanaomba kodi na makato mbali mbali yapunguzwe na ombi lingine serikali ipanue wigo wa kodi ili kumpunguzia mzigo mfanyakazi.

Kwasababu haya hayajatekelezwa kama walivyoomba sasa wafanyakazi wamedhamiria kugoma nchi nzima kuishinikiza serikali kutekeleza mahitaji yao. Jambo hili ni la hatari kwa mustakabali wa ustawi, maendeleo na usalama wa taifa letu. Hatua hii italeta adha kubwa kwa watanzania wote kuanzia wagomaji wenyewe mapaka ndugu zao. Na kibaya zaidi wananchi wengi wasio na hatia wataumia na wengine watakufa kutokana na madhara ya mgomo huo. Mama lishe wanaoishi kwa kuwauzia chakula wafanyakazi hawatafanya biashara, wanaopata riziki kwa kuosha magari hawatapata ridhiki kwa siku hizo. Wagonjwa watakufa kwa kukosa huduma. na kadhia mbali mbali zitaibuka.

Jambo lingine la hatari ni kuporomoka kwa uchumi wa Tanzania kwani siku za mgomo taifa litapoteza fedha nyingi sana. Madhara hayo yataendelea kwa muda mrefu hata bada ya mgomo huo kwisha Nilifanya mkutano na waandishi wa habari tarehe 22 machi mwaka huu, kuwasihi wafanyakazi wasigome, kuisihi Serikali iyashughulikie malalamiko hayo. Lakini hakukuwa na respond nzuri kutoka vyombo vya habari jambo ambalo limenifanya nihisi kuwa vyombo vya habari vinashabikia mgomo huo. Ni redio chache, na magazeti machache tu yaliripoti.

Kimsingi mgomo utayumbisha nchi na sekta zote. Maana mgomo wa nchi nzima, hata hivyo vyombo vya habari havitauza magazeti maana wafanyakazi ndio wanaonunua zaidi magazeti. Huwezi kukuta mama lishe, mmachinga, mfyatua tofali ananunua magazeti. Kipindi hicho kila mtu atakuwa anatunza hela yake isiishe mapema.

Makampuni mengi yataingia hasara na mwisho wa yote mgomo ukiisha kila sekta itaendelea na msukosuko wake na hatimaye upunguzaji mkubwa wa wafanyakzi utafuatia ili kuweka mambo sawa.

Kugoma ni sawa na kujilipua maana wafanyakazi watawatesa mpaka ndugu zao na watajiathiri wenyewe. Mgomo ni sawa na unamdai mtu halafu unamnyima mapato.

Malamiko haya ni ya msingi sana na serikali lazima isizibe masikio Ni wakati muafaka kwa wafanyakazi kufuta mgomo, kurudi mezani na Serikali ili kila upande ujue madhara na kuchukua hatua muafaka. Watanzania wanasifa kuu ya huruma, upendo na uvumilivu ni vema wajiangalie katika kioo hicho.



Na Jacob Malihoja

Thursday, March 25, 2010

MILA NA DESTURI ZA WANGONI:- Upande wa ndoa na kuchumbia

Kwanza uchumba halafu harusi/ndoa.

Katika mila za wangoni, hapo zamani kijana na msichana wakikua kufikia umri wa kuoa walioa. Kwa mila za wangoni, mtoto wa kiume hata kama akikua na kuoa halafu hajaenda vitani ilikuwa haionyeshi maana. Wakati wa kupigana vita kijana ilibidi aonyeshe nguvu zake zilivyo. Kijana ambaye bado hajaenda vitani aliitwa (walimwita) ”lijaha” ikiwa na maana ya kijana/mvulana mdogo. Kijana ambaye ametoka vitani walimwita/aliitwa ”lidoda” ikiwa na maana mkubwa . Mke wa kuoa walimtafuta ambaye ni mwenye ukamilifu, anayejua kufanya kazi za nyumbani. Anatafutwa mwanamke anayeweza kuokota kuni, kuchota maji, kutwanga, kupika chakula, kupika pombe na awe mwanamke anayecheka vizuri na watu wote katika mji.

Ndoa haifungwi katika ukoo. Kwa wangoni hawaoi mke au kuolewa na mume mwenye (kibongo) ubini mmoja. Kama watu wakioana katika ukoo, basi wazee wataulizia kwanza kama ukoo huo ni wa karibu au wa mbali. Kama hawa watu walioana katika ukoo wa karibu, basi watawaapizia. Watu wnaogopa kuoana ndani ya ukoo kwasababu wakifanya hivyo watoto watakaozaliwa watakufa. Na pengine watoto hao watapata kifafa au pengine mababu (mahoka) watakasirika.

Mtenga:-

Kwa kingoni cha zamani mtenga ni mtu anayenunua au kuuza kitu. Mtenga anamuuza mototo wa kike. Yeye ndiye atoaye ”Chiyagabuli” yaani mali ya mwanzo na ”Mawolowolo” ikiwa na maana mali yote kwa wenye mtoto wa kike.

Kulonda mdala=Kutafuta mke:-
Wenye mtoto wa kiume wanapotaka kumwoza kijana wao , wazazi wengine walimtafutia mke. Wazazi wengine walimwacha kijana wao atafute mwenyewe mke. amtakaye. Kama walimwona msichana mrembo watamtafuta ndugu yao ambaye watamtaka na kumwelezea habari za ndoa. Na huyu ndiye atakayekuwa MTENGA wao. Mtenga huyu ataanza kuulizia kwa siri mambo ya wazazi wa msichana yule na wanaukoo wake wote na halafu ataenda kuwaeleza wazazi wa kijana. Kama wazazi wataona ya kuwa ni msichana wa hodari, watenga wale wataenda kwa wazazi wa msichana na kuuliza kama wanaruhusiwa kumwoa? Kama wenye binti watakataa, watenga wataombeleza.

Kujitokeza:- Ni lazima wawe na kiulizio , watenga ndio wataenda kuulizia kumwoa mke. Wanapoenda kule , wanachukua kitu fulani ”lukotelu au luhongelu” ni kiulizio , kitu hicho chaweza kuwa nguo, ushanga au hela nk.

Chiyagabuli= Mahari ya mwanzo

Kama wakwe wa pande zote mbili wanakubaliana watoto wao waoane, watenga watapeleka mahari kidogo kwa mama na baba wa binti ambayo ni mahari ya mwanzo. Baada ya muda yatapelekwa tena mahari ya mwanzo yaani kwa mara ya pili itakuwa jembe moja LUSUKA. Kama aina fulani ya jembe "ngwamba" ni jembe lenye tundu pale pmini unapotumbukizwa. Hii itamaanisha binti yao tayari amekwisha poteza ubikira

Kuchicha= kumtembela mchumba
Kuchicha ni kitendo cha msichana aliyechumbiwa kwenda rasmi kumtembelea mchumbake, kimila huyo msichana aliyechumbiwa anaenda na rafiki yake wa kike. Hivyo basi siku hiyo inakuwa ni kama anaenda kuona mazingira atakayokuja kuishi. Kimsingi katika siku ya kuchicha hairuhusiwi kulala pamoja na kufanya mapenzi ndio maana msichana alipaswa kusindikizwa na msichana mwenzake. Lakini basi mara nyingi imekuwa ngumu kujizuia wengi wamekuwa wakiishia kufanya mapenzi, mbaya zaidi unakuta mvulana anaalika na mvulana mwenzake halafu wanagawana hao wasichana waliofika hapo. Lakini pia hilo neno limekuwa likitumika isivyo rasmi kama vile kitendo cha msichana kutongozwa na mvulana wapo walioita kitendo hicho kuchicha na imezoeleka na wengi.

Au pia inakuwa kinyume:- Kijana wa kiume pamoja na vijana wenzake wanaenda rasmi kumtembea mchumba/msichana. Huko anafanya kazi nyingine nyingi. Kwa kufanya hivyo, wakwe watamwona ni kijana /mume wa uhakika, kuwa anaweza kufanya kazi za kianaume, kama anajua/weza kulima kukata matema(kukata miti shambani kwa ajili ya kuandaa shamba), kama ana kaa/ishi vizuri na watu au kama hana haraka ya kula. Muda wote huo wa aliokuwepo, kijana huyu hajionyeshi kwa wakwe zake. Anapotaka kutoka nje ya nyumba alalayo ni lazima ajifunike nguo usoni gubigubi. Kijana atafanya hivyo atakapotaka kumwona mtarajiwa mkewe, hakuna kujionyesha kwa wakwewe mpaka atakapozaa mtoto. Na mwanamke atafanya hivyo kwa wazazi wa mumewe.

Nimefanya utafiti katika kuon au kulipa mahari inaweza kuwa kama ifuatavyo
Mbuzi 1 dume
Mbuzi 5 dume 1 , majike 4
Sufuria kubwa 1
Mablanket 2
Nguo- kanga doti 2
Nguo vitenge doti 2
Nguo shuka 2
majembe 2
Simulizi/maelezo ni kutoka kwa babangu mzee Ngonyani

Ngoja tusikilize pia ngoma hii ya kitoto/lizombe ambayo ni ngoma ya wangoni karibuni!!

Tuesday, March 23, 2010

WANYAMA TU WANAJIFUNZA YAWAJE SISI TUSHINDWE???

Wanyama jamii hii ni wepesi kufundishwa!!
Wanasaikolojia watafiti walijaribu wakati Fulani kufanya utafiti ili kuona kama kweli wanyama wana uwezo wa kujifunza. Katika maeneo mbalimbali na kwa wanyama tofauti, waligundua kwamba kwa kiasi Fulani wanyama nao wanaweza kujifunza, wanaweza kubadilika kutoka maisha duni na kwenda maisha bora zaidi kwa kuiga.

Waligundua kwa mfano kwamba mnyama kama nyani anaweza kujifunza. Waligundua hilo baada ya kumuonyesha nyani tofauti ya vitu na baadae nyani huyo akaweza kubainisha au kupambanua kutoka katika vitu vitatu alivyowekewa, kitu kimoja ambacho ni tofauti na vile vingine viwili. Kwa mnyama kama nyani kujua na kubainisha tofauti ya vitu, siyo jambo dogo kama mtu anavyoweza kufikiria.

Njiwa naye aliwahi kufundishwa na kumudu kubainisha au kuchagua picha ya binadamu kutoka katika kundi la picha za vitu tofauti alilokuwa amewekewa. Njiwa anapofikia kumudu kujua kwamba hii ni picha ya binadamu na hizi nyingine ni za vitu vingine, sio jambo dogo. Hasa pale anapomudu baada ya kupewa mafunzo Fulani, kwani ina maana kuwa anaweza kujifunza na kuelewa.

Siyo hao tu, bali hata sokwe mmoja aliyekuwa akifahamika kwa jina la Lana aliwahi kufundishwa kompyuta na kumudu kuondoa kutoka kwenye kompyuta, maumbo Fulani kufuatana na namba baada ya kuwa ameonyeshwa tarakimu 1,2,3.

Mbweha-bahari naye kwa kujifunza mwenyewe ameweza kugundua kwamba kwa kutumia jiwe lingeweza kumtoa kutoka kwenye gamba lake konokono-bahari na kuji patia mlo. Hapo kabla, mnyama huyo hakuwa na uwezo huo hadi pale ilipotokea nasibu ambapo aligundua kwamba jiwe lina uwezo wa kuvunja gamba la konokono-bahari.

Ingawa baadhi ya wanasaikolojia wanabisha kwamba huko siyo kujifunza, kwa fasili yetu ya kujifunza tunaamini kwamba huko ni kujifunza. Kwa hali hiyo, tunaona kabisa kwamba hata wanyama wana uwezo wa kujifunza, pale inapotokea nafasi ya kufundishwa.

Lakini ni jambo la kusikitisha sana kuona kwamba, binadamu ambaye ana akili na nafasi ya kujifunza, anakuwa mgumu wa kujifunza, na hata akijifunza anaweza kutokea kuwa mgumu wa kubadilika. Kama njiwa anaweza kufundishwa na akamudu kuitambua picha ya binadamu kutoka katika picha nyingi nyingine, sokwe akaweza kucheza na kompyuta na mbweha-bahari akaweza kugundua udhaifu wake, ni kwa nini binadamu ambaye ni bora kuliko viumbe wote awe au ajiweke katika kiwango cha chini kuliko hao wanyama?

Tunajua kuna mazoea na tunajua mazoea ni magumu kufutika, lakini hatuwezi kufuta mazoea yetu mabaya kama kwanza hatutakubali kwamba sisi ni viumbe bora kuliko wanyama kwa sababu tuna uwezo wa kujifunza na kubadilika kwa manufaa yetu. Kama wanyama wanaweza kufundishwa na wakaelewa, ni kwa nini nasi tusiwe tayari kujifunza kila siku? Kuna njia mbalimbali za kujifunza kuhusu maisha, tunaweza kuzitumia na kuzifuata ambapo tunaweza kubadilika kabisa.

Kila siku tunapambana na mambo ambayo kama tutakuwa weerevu yanaweza kutusaidia sana katika kubadili maisha yetu. Kila jambo linalomtokea mtu ni elimu ya kutosha kabisa. Kama umepoteza fedha, kama umedhulumiwa, kama umepata hasara, kama umeachana na mpenzi wako au kama umefanikiwa, kama umefaulu na mengine ya aina hiyo, ni matukio lakini ni elimu pia. Tujifunze kuwa na tabia ya kujifunza kupitia katika matukio yote tunayopambana nayo.

Tujiulize kila tukio Fulani linapotupata kwamba tumejifunza kitu gani, badala ya kulalamika, kulaani au kufurahia tu. Kila tukio katika maisha yetu lina elimu ambayo tukiipata inasaidia kulielewa vizuri zaidi tukio litakalofuata. Tunaposhindwa kujifunza na kubaki watu wa kulaani nakurukaruka kwa furaha tu kila tukio Fulani linapotufika, tunakuwa tumejishusha sana na pia kupoteza mengi ya manufa. Kumbuka kila tukio maishani ni elimu ya kutosha kwa ajili ya mtihani wa maisha wa kesho yake.

Habari hii chanzo ni Jitambue....

Monday, March 22, 2010

Aliyedaiwa kufa na kuzikwa aibuka hai!!!

MKAZI wa mjini Mafinga ambaye alidaiwa kufa na kuzikwa mwezi Oktoba mwaka jana, amerejea kwao akiwa hai na kusema"sikumbuki kama niliwahi kufa".
Kijana huyo, Nickson Kabonge, 23, aliwasili nyumbani kwao juzi mchana akitokea msitu wa Kihanga ulio Mafinga ambako amedai alikuwa akifanya shughuli za kupakia mbao na magogo kwenye magari.
Wakati familia yake, na hasa baba ikiamini kuwa alishafariki na ilishiriki kumzika, kijana huyo aliiambia Mwananchi kuwa aliamua kurejea kwao baada ya kuota kila mara kuwa baba yake amefariki.
Kurejea kwa kijana huyo kulizua yaharuki kwa wakazi wa mjini hapa ambao walifurika nyumbani kwao kumshangaa, wakionekana kutoamini kuwa aliyerejea ni kijana waliyemzika na badala yake kumchukulia kuwa ni msukule.
Pamoja na kurejea kwao, baba wa kijana huyo, Boniface Kabonge alisema kuwa mwanaye Nickson alifariki dunia Oktoba 6 mwaka jana na kuzikwa kwenye makaburi ya Mufindi.
"Nilishtuka mwanangu alipobisha hodi na kuingia ndani wakati najua alishakufa na tulimzika, sijui imekuwaje hadi aliyekufa arejee nyumbani,"alisema
Alisema kabla ya kifo chake kijana huyo alikuwa akifanya kazi ya kupasua mbao kwenye msitu huo wa Kihanga, lakini alifariki baada ya kuangukiwa na gogo ambalo lilimjeruhi vibaya kichwani.
Alisema mwili wa kijana huyo ulipelekwa Hospitali ya Wilaya ya Mufindi na kuhifadhiwa katika chumba cha maiti hadi siku ya pili ulipopelekwa nyumbani kwao kwa ajili ya kuagwa.
"Mimi ndiye niliyemuosha mwanangu kutokana na mila zetu, tulimpeleka nyumbani watu waliaga kama kawaida na baadaye tulimzika kwa sababu kila mmoja alijiridhisha na kifo chake," alisema
Akizungumza na Mwananchi kijana huyo alisema hafahamu habari za kifo chake.
"Nashangaa wanaponikimbia ila sikumbuki kama niliwahi kufa, nachojua nilikuwa nikiishi na wenzangu kumi katika msitu wa Kihanga ambako tulikuwa tukila pumba na maji,"alisema
Alisema kuwa kilichomrejesha nyumbani kwao ni ndoto alizokuwa akiota kuwa baba yake amefariki hali iliyomlazimu arudi kuhani msiba.
"Kila nikikaa mwili wa baba yangu ulikuwa ukipita mbele yangu kwenye jeneza huku ukiwa umefunikwa kitambaa chekundu, ndio maana nikaamua kuja kumzika.
Nashangaa nilipofika hapa nikaambiwa kuwa mimi ndio nilikuwa nimekufa,†"alisema.
Kijana huyo alishangaa zaidi baada ya kuonyeshwa kaburi ambalo mwili wake umezikwa na akataka lifukuliwe kukujua ulizikwa mwili gani.
Jeshi la polisi limethibitisha kupokea taarifa za kurejea kwa kijana huyo ambaye mwili wake ulihifadhiwa katika Hospitali ya Mufindi kabla ya kuzikwa.
Mganga msaidi wa hospitali hiyo, Meshack Mlyapatali alisema wapo tayari kufanya uchunguzi wa kisayansi wa tukio hilo, lakini wanasubiri agizo kutoka serikalini au Jeshi la Polisi.
Baba yake alisema kija huyo amebadilika kwa kuwa siku hizi anazubaa na kujikunyata na kuwa wakati mwingine amekuwa akiweweseka kuwa anaona jeneza likipita mbele.

Nimeona si vibaya nikiweka habari hii hapa kibarazani kwangu kwani wote tuna nia moja ya kuhabarisha jamii.
Imeandikwa na Tumaini Msowoya, Mufindi


Sunday, March 21, 2010

Nawatakieni Jumapili njema wote na neno Upendo!!!

Ufanyacho upendo:-

Upendo kidogo ni kama jua, ambalo ni rafiki yetu wa daima. Hufukuza baridi, kuimarisha mazao yetu na kuyaivisha. Hivyo ndivyo ufanyavyo upendo; kama jua. Katika kupendana, yule mwenye kupendwa hibadilika. Anabadilishwa kutoka hali ya mashaka, wasiwasi, hofu, upweke na kutoamini; anakuwa mtu mwingine kabisa. Mwanzoni alikuwa mwenye hofu na mashaka, sasa ni mwenye kujiamini na kuthubutu kutenda. Badala ya uchungu na upweke, imekuwa furaha na heri. Ni kama nyoka abadilishaye ngozi yake ya zamani kwa wakati fulani, na kubaki na ngozi mpya. Kwa upendo aliopata mtu huyu amefanywa kuwa mpa.

Mara nyingi twasikia watu wakisema , "Huyu mvulana anampendaje msichana huyu?" au " nini cha kuvutia alicho nacho Bwana huyu?" Haina maana kuuliza kwa nini twampenda mtu mwingine. Kama ni mapendo kweli, hatumpendi mtu kwa kuwa ana vitu fulani vya kuvutia wala hatumpendi ingawa ana kasoro, bala tunampenda mtu aliye ndani ya yote haya.

Na kwa kweli tunaweza kupata maana kamili ya upendo kutoka kwa Mungu peke uyake ambaye Neno lake latuambia

upendo: huvumiliam hufadhili,
Upendo: hauhusudu,
Upendo: hautabakari, haujivuni,
Upendo: haukosi kuwa na adabu, hautafuti mambo yake,
Upendo: hauoni uchungu, hauhesabu mabaya
Upendo: haufurahii udhalimu, bali hufurahi pamoja na kweli
Upendo: huvumilia yote, huamini yote, hutumaini yote, na hustahimili yote
(1 Wakorintho 13: 4-7)
NAPENDA KUWATAKIENI WOTE JUMAPILI/DOMINIKA HII YA 12 YA MWAKA HUU. MWENYEZI MUNGU AWA NANYI WOTE. AMINA



Friday, March 19, 2010

Ijumaa ya leo ngoja tuwasikilize hawa watoto, ni somo shuleni!!


Hapa ni dada Camilla akitupigia Trombone/trombon ni moja ya soma shuleni



Na hapa ni Erik naye akitupigia Violine/fiol =kiswahili fidla ni somo pia shuleni

Wednesday, March 17, 2010

Utamaduni katika baadhi ya nchi Duniani!!!!

Kwetu bila mshenga mke hupati





Asia:

Vijana hukaa na wazazi hadi anapofikia wakati wa kuoa na akisha oa au kuolewa huchagua mzazi mmoja na kuishi kwake kwa muda fulani ndipo huanza maisha.


Australia:

Mabinti huwaomba vijana wa kiume kwenda nao “outing” kwa ajili kuombwa uchumba na analipa gharama zote kama vile chakula na vinywaji.


Columbia:

Kama msichana unatoka naye kwenda kuongea kwa mara ya kwanza kawaida huambatana na rafiki yake mmoja wa kike unawajibika kuwalipia gharama zote.

Finland:

Vijana wa kiume na kike huenda kwa kundi moja kama 30 hivi lengo likiwa ni kutafuta wachumba (matching).

Latin America:
Kaka au dada yeyote atakaye muomba mwenzake kutoka naye kwa ajili ya mazungumzo ya faragha (uchumba) anawajibika kulipa gharama zote za vinywaji na chakula.

Japan:
Siku Valentine wanwake huwapa zawadi wanaume na baada ya mwezi kuna white day ambayo wanaume nao hutoa zawadi kwa wapenzi wao wa kike.

India Kaskazini:
Hakuna uchumba hadi wazazi wamkubali msichana ambaye unataka kumuoa kama wewe ni kijana wa kiume, wazazi wakikataa umeumia na kama wakikubali unaruhusiwa full speed kuoa.

Je, sehemu unayoishi wewe tamaduni za kuoana zipoje?
Au hakuna kanuni na taratibu rasmi?
Je, njia mnazotumia zinasaidia vipi kuhakikisha wachumba wanafahamiana na kujuana ili kuwa na maisha ya ndoa yenye mshikamano na si migongano

Habari hii nimeipata kutoka kwa kaka Mbilinyi :-http://mbilinyi.blogspot.com/

Tuesday, March 16, 2010

WALIANZA WANAWAKE NA SASA NI WANAUME!

Je? na huyu naye ni mchina au?

Kuna simulizi nyingi sana ninazipata kutoka huko nyumbani Tanzania ambazo huwa zinanishangaza sana. Awali ilikuwa ni wanawake ndio waliokuwa waathirika lakini sasa hivi na wanaume nao inasemekana wameingia katika mkumbo huo mpaka najiuliza, sababau ni nini hasa. Je ni uelewa mdogo au ndio athari za utandawazi zinawaathiri ndugu zangu?

Kuna wanawake wengi wamekuwa ni wahanga wa madawa ya Kichina ya kuongeza makalio, kiasi kwamba wengine wamepoteza maisha. Ni jambo la kushangaza kidogo kuona kwamba serikali yetu imeshindwa kusimamia na kudhibiti uingizwaji wa haya madawa ya kichina yenye athari lukuki kwa binadamu mpaka pale zinapotokea athari za wazi.

Haya, sasa mambo yamegeuka, wanaume nao wameingia kwenye mkumbo huo. Hivi karibuni kuna habari zimesambaa huko nyumbani kuwa kuna mwanaume mmoja amejikuta akiwa na maumbile ya sehemu zake za siri makubwa kupita kiasi, inasemekana hata mkewe amemkimbia. Kisa, alitumia dawa za kichina za kukuza maumbili ya wanaume.

Habari zaidi zinadai kuwa mkewe alikuwa anatoka nje ya ndoa sana na baada ya mume huyo kumuuliza mkewe sababu ta kutoka nje ya ndoa ndio akajibiwa kuwa ana maumbile madogo na ndio maana akaona akatafute dawa za kichina ili akuze maumbile yake kumridhisha mkewe. Lakini kinyume na matarajio yake, maumbile yake yakawa makubwa kupindukia, hata mkewe akamkimbia.

Kuna wakati niliwahi kuandika juu ya wanaume kununua dawa za kuongeza nguvu za kiume maarufu kama mkuyati, kama ukitaka kujikumbusha bofya hapa. Nakumbuka nilipata upinzani mkubwa kutoka kwa wanaume, lakini naamini kwa hili watakubaliana na mimi.

Kwangu mimi wale wanawake wenzangu wanaokimbilia dawa za kichina ili kuongeza makalio yao na wale wanaume wanaotumia dawa za kuongeza nguvu za kiume maarufu kama mkuyati na dawa za kichina ili kuongeza maumbile yao nawaona kama watu wasiojiamini.

Mara nyingi tunapozungumziwa matatizo katika ufanyaji wa tendo la ndoa huwa tunafikiria matatizo ya ufanyaji kazi wa viungo vyetu tunavyotumia katika kutekeleza tendo hilo. Kwa kawaida tendo la ndoa halina kanuni moja, yaani sio jambo ambalo kila mtu anaweza kulifanya kwa kufuata kanuni moja na akaridhika, inategemea kwa kiasi kikubwa kuwa mhusika analichukuliaje tendo hilo ukilinganisha na kile alichojifunza juu ya tendo hilo tangu utotoni.

Kuna wengine wanalifurahia kutegemeana na mkao wakati wa tendo hilo, wengine watasema wanalifurahia zaidi pale walifanyapo na mtu wampendaye kwa dhati, ili mradi kila mtu atakwambia sababu ya kulifurahia tendo hilo, lakini je, vipi kuhusiana na ukubwa wa maumbile ya wanaume, yanayo nafasi kubwa kiasi gani katika kuwafurahisha wenzi wao katika tendo?
Katika hilo kuna kiwango kikubwa sana cha dhana kuhusiana na ukubwa wa maumbile ya wanaume na tendo la ndoa. Dhana hii imekuzwa kwa kiasi kikubwa sana na wanaume wasiojiamini kiasi kwamba imepewa nafasi na jamii na kuonekana kama jambo la msingi sana wakati hakuna uhusiano wowote kati ya ukubwa wa maumbile na ufanisi katika tendo la ndoa. Hata baadhi ya wanawake nao wameingia katika mtego huo na kuona kama hilo ni jambo la msingi wakati swala hilo halina kanuni.

Vipi kuhusiana na swala la hamu ya tendo la ndoa nalo? Kuna dhana imejengeka kuwa wanaume ndio wenye uchu mkubwa wa kufanya tendo la ndoa ukilinganisha na wanawake, dhana ambayo ina ukweli kwa kiasi fulani ingawa sio mara zote.

Je na wale wanawake wenye uchu wa tendo la ndoa kuliko wenzi wao inakuwaje? Hapa ni vigumu swala hili kuwekwa wazi sana na wahusika kutokana na kile tulichojifunza. Jamii imetufundisha kuwa wanawake ni wa kungoja tu waombwe tendo na sio vinginevyo. Pale mwanamke napokuwa hajaridhika na tendo la ndoa na mwanaume kuonekana kukosa hamu ya kuendelea, ujumbe unakwenda kichwani kwa mwanamke ni kujiona kama vile mumewe hampendi au amepata mwanamke mwingine nje ya ndoa au wakati mwingine hujihisi kupoteza ule uzuri wake uliomfanya mumewe ampende.

Je na ukubwa wa makalio ya wanawake nao unayo nafasi kubwa kiasi gani katika kuwavutia wanaume linapokuja swala la kufanya tendo la ndoa? Hii nayo ni dhana ambayo imepewa nafasi kubwa na wanaume na kuonekana kama vile ni jambo la msingi sana, wakati yale ni maumbile ya kawaida tu ambayo hayana uhusiano wowote na ufanisi katika tendo la ndoa. Lakini kutokana na ushabiki tu wa wanaume, hasa baada ya hii mitindo ya mavazi iliyoingia ambayo huacha maumbile ya wanawake wavaao mavazi hayo nusu uchi, na ndio maana swala hilo limepewa nafasi.

Bado tunayo safari ndefu sana katika kufikia muafaka juu ya swala hili, je ukubwa wa maumbile ya wanaume na ukubwa wa makalio ya wanawake unayo nafasi kiasi gani katika kulifurahia tendo la ndoa?

Tutafakari kwa pamoja……………………..

Monday, March 15, 2010

Pendo langu kwako wewe

Uketi chini mpenzi, ya moyoni nikwambie,
Daima nitakuenzi, uhai uniishie,
Hutoipata simanzi, nataka ufurahie,
Pendo langu kwako wewe, halipimwi kwa mizani.

Halipimwi kwa mizani, uzitowe wazidia,
Pendo linayo thamani, hakuna cha kufikia,
Hata kwa mizani gani, huwezi kulipimia,
Pendo langu kwako wewe, hutolikuta dukani.

Hutolikuta dukani, ati labda lauzwa,
Pendo li ndani moyoni, kwalo pendo nimemezwa,
Kwani halina kifani, kwa kitu likaigizwa,
Pendo langu kwako wewe, kwa mwingine hulikuti.

Kwa mwingine hulikuti, pendo akakupatia,
Nina pendo lenye dhati, ya moyo uloridhia,
Pendo liso na wakati, daima kufurahia,
Pendo langu kwako wewe, ling'aalo kama nyota.

Ling'aalo kama nyota, maishani kuwa nuru,
Pendo raha kulipata, kufaidi kwa uhuru,
Pendo chozi kunifuta, kwa nini nisishukuru,
Pendo langu kwako wewe, liishi zote dawamu.

Liishi zote dawamu, linipe raha ya moyo,
Pendo hili na lidumu, kwa furaha linipayo,
Pendo hili mbona tamu, kwa tamu niipatayo,
Pendo langu kwako wewe, kamwe halina mipaka.

Kamwe halina mipaka, pendo mali yako yote,
Kukupenda sitochoka, pendo ulimi na mate,
Juwa kwangu umefika, wala us'ende kokote,
Pendo langu kwako wewe, waache waone wivu.

Waache waone wivu, kwa pendo ninalokupa,
Sisi tule zetu mbivu, pendo lizidi nenepa,
Kwako niwe msikivu, sitowaza kukutupa,
Pendo langu kwako wewe, wacha lizidi shamiri.

Wacha lizidi shamiri, wacha pendo na ling'ae,
Kukupata ni fahari, wengine uwakatae,
Pendo kwako li mahiri, unifae nikufae,
Pendo langu kwako wewe, mbona linanipa raha.

Mbona linanipa raha, ni bahati sana mie,
Pendo lajaa furaha, wacha nilifurahie,
Kwa pendo nipate siha, nishibe na nichanue,
Pendo langu kwako wewe, ni mwisho wa mambo yote.


Nimelipenda shairi hili na nimeona sio vibaya kama nikiliweka hapa kuwakilisha ujumbe huu. Nimelipata toka kwa http://fadhilimshairi.blogspot.com/. Haya tufurahi pamoja.

Friday, March 12, 2010

Majira katika mwaka:- kaskazi/baridi, kiangazi, masika na kipupwe hapa Sweden!!

Nipo juu ya mlima Kilimanjaro!!Majira ya baridi kali , ni mwezi huu wa tatu na hapa ilikuwa jumamosi iliyopita

Hapa baridi inaanza ni mwezi wa nane mwaka 2009 (autumntime) Höst. Ni majira ya kupukutika kwa majani.
Hapa ni 2009 mwezi wa nne-tano (Springtime) Majira ya kuchipua.


Na hapa ni mwaka 2008 (Summertime) Majira ya joto hapa tupo mji wa Karlstad nje ya tangi kubwa la maji.

NAPENDA KUWATAKIENI WOTE MWISHO MZURI WA JUMA HILI , MUWE NA WAKATI MZURI NA AFYA NJEMA !!!!!


Thursday, March 11, 2010

BROWN ASHIKA TAMA

Tujifunze lugha yetu

Brown ashika tama
“Mmetawala nchi hii kwa muda usiopungua miaka arobaini , na maisha ya watu yamekuwa ya wasiwasi mpaka sasa. Twawaambieni kwamba fungeni virago mrudi kwenu Ulaya, mtuachie nchi yetu tuiongoze wenyewe. Tunawahakikishieni kuwa kwa muda wa miaka kumi ya uhuru wetu, nchi itakuwa imebadilika. Wakati huo, njooni mwone, nchi itakuwa imefika kiwango gani cha maendeleo.” Maneno hayo yalisemwa na Mheshimiwa Baba wa Taifa Mwalimu Julius K Nyerere wakati TANU ilipokuwa inadai uhuru.

Usemi wa Rais wetu haukuadhirika. Siasa safi na uongozi bora ndiyo ulionufaisha usemi huo. Siasa tunayoifuata ni ile yakutofungamana na upande wowote wa nchi nyingine za ulimwengu. Ni siasa ya ujamaa na kujitegemea ambayo si ngeni katka nchi hii. Sisi tunafuata mfano wa jadi zetu. Ufanisi uliopatikana katika maendeleo yetu umeshtua ulimwengu mzima. Watu wa mataifa mbalimbali huja Tanzania kujionea wenyewe jinsi wananchi tunavyojenga taifa letu.

Siku moja Brown, Mwingereza ambaye aliwahi kuwa Bwana Shauri katika sehemu mbalimbali za Tanzania wakati wa ukoloni, alitalii Tanzania. Yeye alikuwa mwandishi wa gazeti moja huko Uingereza: na aliona kuwa angeweza kukusanya habari nyingi za Tanzania na maendelea yake. alikuja kuona ukweli wa maneno ya Rais Nyerere ambayo zamani aliwaambia wakoloni. Brown alifika Tanzania baada ya mika tisa tu tangu nchi kupata uhuru.

Baada ya kuwasili Dar es Salaam kwa ndege, akaamua kukaa jijini kwa muda wa siku mbili. Halafu alisafiri Tanzania bara kutembelea mbuga za wanyama na sehemu nyingine za kuvutia. Alitembembelea vijii vingi vya ujamaa katika mikao ya Mtwara, Ruvuma, Mbeye, Tabora, Mara, Pwani na mingineyo. Kila alipotembelea, alizungumza na wananchi habari za maisha yao katika vijiji hivyo vya ujamaa. Mazungumzo yaliyomfanya Bwana Brown ashike tama hasa ni yale yaliyosemwa na Mzee Kaswiga wa kijiji cha Mbalizi Mkoa wa Mbeya. Walizungumza chini ya mti mkubwa uliosimama kando ya barabara ya mtaa mmoja wa kijiji hicho.

Bwana Brown alianza mazungumzo kwa kuuliza, “Je, Mzee Kaswiga, unaweza kuniambia shabaha za kuanzisha vijiji vya ujamaa katika nchi hii, au unafahamu sababu ya kuanzisha kijiji hiki tu basi? Mzee Kaswiga akajibu, “ndiyo naweza. Shabaha katika vijiji vyote vya ujamaa ni Umoja. Tumekuwa wanyonge wa maisha kwa muda mrefu sana kwa sababu ya kuishi kwa ubinafsi. Sasa tumeamua kuishi kijamaa ili tufanye kazi pamoja, na mapato ya kazi yawe kwa faida ya wote vijijini. Matokeo yake ni haya unayoyaona katika kijiji hiki.” Bwana Brown akauliza tena, “Unamaanisha nini unaposema kuishi pamoja kijamaa? Kwani hamkuwa mnaishi hivyo kabla ya sasa?” Mzee akajibu, “Babu zetu wa kale walikuwa wanaishi namna hii, wakoloni walipotawala wakaingiza ubinfsi ili mabepari wastawi. Maendeleo ya watu yalikwama, kwani waligeuzwa kuwa na mioyo ya ubinafsi. Lakini sasa hali hiyo hatuna. Wana-Kijiji hujiona kuwa ni kitu kimoja. Kazi zetu tunazozifanya zina lengo la kuinua maisha yetu. Mwana-kijiji huwa amejiweka katika bima ya maisha kwa vile huwa chini ya uangalizi wa kijiji. Huo ndio msingi wa kuishi pamoja, kwa ajili hiyo watu hupendana, huheshimiana kindugu na kusaidiana katika matatizo mbalimbali. Bepari au kabaila hana lake tena.”

Bwana Brown aliandika maneno katika daftari yake. alimtazama mzee Kaswiga kwa tabasamu ya husuda, kisha akamwuliza, “Kwa hiyo una maana kwamba hizo tu ndizo faida mnazopata?” Mzee akajibu, “La, hasha, hizo ni baadhi tu. Shule na hospitali zimejengwa. Maji yamepelekwa vijijini kwa mabomba, pia kuna faidanyingine nyingi. Siku hizi maisha yameanza kutakata ukilinganisha a enzi za wakoloni.” Bwana Brown alionyesha kufadhaika kwa vile maneno ya Mzee Kaswiga yalimsuta. Akajitetea kwa kusema. “Lakini wakoloni walikusudia kutenda hayohayo, kwani walianza kujenga shule na hospital..........” Mzee Kaswiga akamdakiza, “La, la, la, sisemi hamkufanya lolote. Ingawa mlipanga kutenda mengi, kutimiza kulikuwa kwa pole pole; na kwa upande mwingine nataka ufahamu kuwa kukusudia si kutenda, kwani mawazo peke yake hufiki mbingu ya saba! Ni kama ruya ya kupaa hewani usiku.”

Mazungumzo yalizidi kukolea. Bwana Brown akatambua kwamba yule mzee alikomaa na siasa ya ujamaa na mabadiliko ya maendeleo nchini. Hata hivyo alimuliza swali jingine. “Mambo gani yanasababisha kuanzisha vijiji vya ujamaa?” Mzee alichelewa kidogo kujibu swali hilo kwani alikuwa ananusa ugolo. Baada ya kufuta pua na machozi alijibu, “Vijiji vingine vimeanzishwa kwa sababu ya mafuriko ya maji. Watu wanaoishi kando kando ya mito huingiliwa na mafuriko, kwa hiyo huamua kuhama na kuanzisha makao mapya sehemu zilizoinuka. Vijiji vya ujamaa katika wilaya ya Rufiji Mkoa wa Pwani vilianzishwa namna hiyo. Sababu nyingine ni ya kudumisha usalama wa maisha ya watu kwa urahisi. Wakikaa pamoja, huwa ni rahisi kujilinda kutokana na maadui. Vijiji vingi vya Mkoa wa Mtwara vilianzishwa kwa sababu hiyo. Vijiji huanzishwa kwa njia mbalimbali. Njia ya kwanza ni kwa hiari ya watu wenyewe badala ya kuelewa na kuridhika na siasa ya ujamaa. Pili nikwamba watu wanaweza kugeuza kijiji chao cha zamani na kukifanya cha ujamaa.” Wakati Mzee Kaswiga alipokuwa anasimulia hayo, Bwana Brown alikuwa ameegemesha shavu lake juu ya kiganja cha mkono wa kulia huku akimsikiliza kwa makini. Alistaajabu kumwona mzee huyo akisimulia habari za vijiji mbalimbali vya Tanzania kwa uhakika kabisa.

Wakati ulikuwa mwingi sana, lakini Bwana Brown hakuonyesha dalili ya kuchoka. Alitaka kufahamu uongozi wa kijiji kwa jumla. Mzee Kaswiga akamweleza Bwana Brown hivi, “Uongozi wetu unatawaliwa na Katiba ya kijiji ambayo imetengenezwa na wana-kijiji wenyewe. Katiba inaonyesha viongozi na kamati za kijiji. Kadhalika inaonyesha masharti yanayotawala maisha ya wana-kijiji, utaratibu wa kufanya kazi na kadhalika. Mipango ya uchumi imepangwa ili itimizwe kwa muda ule wa miaka ya maendeleo iliyopangwa na serikali. Ili mipango hiyo itimizwe ipasavyo, wana-kijiji hugawanywa katika vikosi. Kila kikosi hupewa kazi maalum ya kufanya kila siku iliyo tofauti na kazi ya kikosi kingine. Kwa mfano katika vijiji vya Rufiji kila mabalozi kumi hufanya kikosi kimoja ambacho kinakuwa chini ya kiongozi anayeitwa Mhenga. Kazi ya Mhenga ni kuangalia na kuhakikisha kuwa kazi ya siku inafanywa, na baada ya kazi hupeleka ripoti kwa Mwenyekiti wa Kijiji ambaye huingiza mahudhurio yote katika daftari. Kwa njia hii inakuwa rahisi kuwafahamu watu wasiohudhuria kazi. Wapiga uvivu huchukuliwa hatua kwa mujibu wa katiba. Kazi muhimu hasa zinazoweza kuendeshwa katika vijiji vya ujamaa ni kama kilimo, ujenzi, uvuvi, ufinyanzi ususi, na kadhalika. Ni shabaha ya wana-kijiji kuendesha viwanda vidogo vidogo ili kupata mahitaji yao ya kila siku. Natumaini umeona kazi kama hizo katika vijiji vingine ulivyotembelea.”

Bwana Brown alitosheke sana na maelezo hayo. Alijionea mwenyewe jinsi Watanzania walivyokuwa wanapiga vita umaskini, maradhi na ujinga. Maneno ya Rais hayakuwa bure na kwamba Tanzania yastahili pongezi machoni pa ulimwengu. Baadaye Bwana Braun aliwaaga wazee wa Mbalizi kwa furaha na alimsifu sana Mzee Kaswiga alivyozungumza naye kwa busara sana. Aliwatakia kila la heri katika kukiendeleza kijiji chao na nchi yao kwa ujumla.

Wednesday, March 10, 2010

Wakati leo ni siku ya mayatima, hebu sikilizeni story ya rafiki yangu huyu!!!

Hakuna asiyehitaji upendo
sikieni story ya rafiki yangu huyu.. Kila tarehe 10 march huadhimisha siku ya watoto wa mitaani kwani miaka kadhaa iliyopita tarehe na mwezi kama huo aliingia rasmi mitaani kama mtoto aishiye kwenye mazingira magumu hadi miujiza ilipotokea akakombolewa baada ya kusota huko mitaani zaidi ya miaka miwili. Baadhi ya shida alizopata akiwa huko mitaa ni pamoja na

1. Kunusurika kuuwawa na watu wenye hasira akidhaniwa mwizi, baada ya kukurupushwa usiku kwenye vilabu vya pombe za kienyeji alikokuwa amelala, aliokolewa na msamaria mwema aliyekuwa akimfahamu
2. Kulala kwenye vilabu vya pombe za kienyeji, stand za mabasi na madarajani hata wakati wa masika
3. Kulimishwa mashambani, madukani na migodini kwa ujira wa ugali, nk.

Anasema katika maisha yake amewahi kujaribu kujinyonga mara mbili ……anaongeza kuwa hajawahi kuona mtu akimpenda kwa dhati maishani mwake………….. hata wanawake alianza kuwapata baada ya kupata kazi na hivyo kuwa na pesa za kuwahonga.

Ilitokea miujza, akatokea mtu akamuingiza shule na kumtunza kwa miezi sita tu kabla hajasema mzigo wa kulea umemuelemea na kumfukuza nyumbani……..lakini kamwe hamsahau mtu huyo, kwani kwake ana hadhi ya malaika wa Mungu …………….. kuna maelezo marefu hapo yanafuatia lakini sasa tuko naye chuo kimoja huku nje ya nchi, yeye akichukua PhD,………….

Amenisimulia haya baada ya kumkuta amepamba chumba chake kwa maua na akisikiliza nyimbo za gospel kwa wiki nzima mfululizo (kumbuka tarehe 10 march ni jumatano ijayo), ndivyo anavyoadhimisha siku hii kwa mwaka huu,………… kweli story yake inasikitisha sana……… machozi yamenitoka leo…………

je, tumfariji namna gani huyu ndugu?...............

HII NIMEIDESA JAMII FORUM nami nimeona sio vibaya nikiweka hapa Maisha na Mafanikio tuweze kujadili/kujifunza kwa pamoja!!!!.

Monday, March 8, 2010

Heri wanawake wote duniani/Internationella kvinnodagen



Napenda kwapa pongezi wanawake wote Duniani, kwanza kabisa mama yangu, binti yangu, na marafiki zangu wa kike wote na bila kujisahau mimi mwenyewe. Na pia napenda kuwapa pongezi wanaume pia.WANAWAKE HOYEEEEEEEEE!!!

Call for nominations- 2010 Rights & Democracy John Humphrey Award

Rights & Democracy (International Centre for Human Rights and Democratic Development) presents the John Humphrey Award each year to an organization or individual from any region of the world for outstanding achievement in the promotion of human rights and democratic development. The Award consists of a grant of $30,000 and a speaking tour of Canadian cities to help increase awareness of the recipient’s human rights work. It is named in honour of the late John Peters Humphrey, the Canadian human rights law professor who prepared the first draft of the Universal Declaration of Human Rights.

Eligibility

The nominee (an individual or an organization) must be committed to peace and non-violence.
The nominee must be independent of any political party or governmental affiliation.
Preference is given to those working at the frontline for the benefit of developing countries, under conditions hostile to the recognition and application of basic human and democratic rights.
Preference will be given to those involved in the priority issues of Rights & Democracy: democratic development, women’s rights, rights of indigenous peoples, social and economic rights.
The Award is given only to an individual or to an organization that is still active.
Former staff or board members of Rights & Democracy are not eligible.
Self-nominations by individuals or organizations are not eligible.

An International Jury

The winner will be selected by an international jury composed of five members of Rights & Democracy’s Board of Directors : Aurel Braun, Guido Riveros Franck, Soyata Maïga, Marco Navarro-Génie and David Matas.

How to Submit a Nomination
Rights & Democracy invites you to submit a nomination by April 30, 2010.
This can be done by mail, fax or e-mail together with all the following documents in one package:

A letter from the nominator (with his or her address, phone number and e-mail) describing the nominee, his or her work and why he or she merits this Award;
A curriculum vitae or a profile of the nominee;
Supporting documentation such as articles written by or about the nominee, (e.g., press clippings, websites links);
At least three references (with addresses, phone numbers and e-mail addresses), who have in-depth knowledge of the candidate’s work, and who may be contacted by members of the jury for more detailed information.

Mailing address: Rights & Democracy 2010 John Humphrey Award
1001 de Maisonneuve Blvd. East, Suite 1100
Montréal, Québec Canada H2L 4P9
Fax: (514) 283-3792
E-mail: pdaigle@dd-rd.ca
Deadline: April 30, 2010.

* Only the nominator will receive an acknowledgement of receipt and a letter informing him or her of the selection of the laureate.


SOURCE: http://www.dd-rd.ca/site/humphrey_award/index.php

MDAU,

MAKULILO, Jr.
San Diego, CA

Sunday, March 7, 2010

NAPENDA KUWATAKIENI WOTE JUMAPILI HII YA KUMI YA MWAKA HUU NA YA KWANZA YA MWEZI HUU!!!

Ukitaka kula lazima ufanye kazi
Maandalizi ya kupata ugali

Na hapa maandalizi ya mboga
Huyu dada sijui ni nani? kama namfahamu vile:-)







JUMAPILI NJEMA KWA WOTE

Saturday, March 6, 2010

Habari mchecheto!!

Kwa mujibu wa matokeo ya uchunguzi wa kitabibu, baadhi ya kuku wa kufugwa wanaoingia sokoni wamekuzwa kwa kutumia ‘utundu’ wenye hatari wa baadhi ya wafugaji wasio waaminifu kwa kulisha mifugo hiyo dawa za ARV ambazo huwafanya kuku hao kuonekana wakubwa na wanene kwa muda mfupi.

Uchunguzi huo unakwenda mbele zaidi na kubainisha kwamba, tabia za dawa hizo ambazo ni kujenga mwili na kuimarisha kinga ya magonjwa kwa mwathirika wa Virusi vya Ukimwi, ndiyo inayompata mlaji wa kuku hao.

Inadaiwa kuwa, kuku hao wanapokula chakula kilichochanganywa na dawa hizo, huweza kutumia siku kumi na mbili hadi kumi na nne kutoka kuwa vifaranga hadi utayari wa kuingizwa kwenye soko la walaji.

Ili kukamilisha uchunguzi huo, Amani lilituma machero wake maeneo ya Kibamba, nje kidogo ya Jiji la Dar ambapo ndipo kwenye viwanda vya kuzalisha kuku wa ‘sampuli’ hiyo.

Kwa mujibu wa kijana mmoja ‘profesheno’ wa kutunza kuku katika moja ya nyumba maarufu kwa uzalishaji maeneo hayo, ambaye hakutaka jina lake lichorwe kwenye ‘pepa’ hii, alikiri kuwepo kwa ishu hiyo, lakini alibainisha kuwa hajui bosi wake anapochukulia vidonge hivyo vya ARV’S.

MADHARA:
Kwa mujibu wa Daktari mmoja wa Hospitali ya Taifa Muhimbi ambaye aliomba hifadhi ya jina lake, mtu anayependa kula kuku waliokuzwa kwa kutumia ARV na yeye huanza kunenepa kupita kawaida, lakini uzito unaweza kuwa tofauti na unene ‘boya’.

Mtabibu huyo aliongeza kuwa, watoto wengi wanaozaliwa siku hizo ambao wazazi wao wamekuwa watumiaji wazuri wa kuku, hukua haraka kiasi kwamba, mtoto wa miaka 18 huonekana kama ana miaka 27.

Aidha, alidai kuwa, wengi ambao kuku hao wamekuwa chakula chao kikuu, hufika mahali wanakuwa ‘legelege’ katika utendaji wa kazi wa kila siku tofauti na zamani huku sehemu kubwa ya chakula hicho ikiangamiza ‘pati’ ya subira na uvumilivu na mlaji kuwa na hasira.

Dalili nyingine ni mtu kuhisi muda wake wa kuchoka unakuwa mfupi akilinganisha na zamani na wakati mwingine hali ya kuhisi kusinzia humtawala hata kama anafanya kazi.

Habari hii nimeidesa mtandaoni na nimeona si vibaya kama nikiiweka hapa ili wenzangu nanyi msome..........

Friday, March 5, 2010

Heri ya Siku ya Kuzaliwa Mume,Baba na Shemeji pia Rafiki yetu

Ni siku yako leo mwl. Klayson
Tunaanza na kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa sala hii :- SALA YA MKE KUMWOMBEA MUMEWE

Ee Bwana , ni ajabu,
Jinsi fikra zangu zinavyomrudia kila mara
Huyu, mume wangu,
Mwenzi anayeshiriki maisha yangu kwa namna ya pekee.
Ninapofagia nyumba na mazingira yake,
Nataka kutengeneza nyumba nzuri kwa ajili yake.
Ninapopika chakula vizuri,Napenda kumfurahisha.
Ninaponunua nguo mpya na kujaribu kuonekana mrembo,
Ni kwa ajili yake tena, Ee Bwana.

Na ninaweza kukuambia kwamba
Ninamwonea fahari,
Anafanya kazi kwa bidii ili kupata riziki yetu;
Ni mtu mwenye haki, mwadilifu,
Naye hujitahidi kutufurahisha.
Kwangu, yeye ni mpole na mwangalifu.
Hunijali na kuonyesha kweli kwamba anajali.
Hunifanya mimi nijiamini mwenyewe,
Anajua jinsi ya kuondoa hofu zangu,
Hunipatia usalama na upendo ambao nahitaji sana.

Ee Bwana, ninakuomba,
Umbariki na umlinde.
Katika safari zake, umfikishe salama.
Kazini mwake, umpe fanaka
Na hapa, nyumbani petu naomba apate amani na heri.

Bwana, unisaidie mimi pia
Niweze kuwa yule mke anayehitaji.
Unifanye niwe mtu anayeweza kumwamini daima,
Mwanamke ambaye anaweza kumfurahia,
Niweze kumsaidia asahau matatizo yake,
Niweze kuondolea mbali hofu zake na kupunguza uchungu wake.

Bwana, Wewe ndiwe uliyenipa mume huyu,
Na katika yeye,Umenipatia sehemu ya nafsi yako mwenyewe.
Ninakusifu kwa ajili yake, Ee Bwana.

Na leo twakumbuka siku muhimu saana maishani mwako. Siku iiliyoanzisha yote mazuri/mema tujivuniayo maishani kwa uwepo wako. Ni SIKU HII ULIYOZALIWA

Zaidi mtembelee Mwalimu Klayson http://matetereka.blogspot.com/

Tunapenda kusindikiza siku hii na mwanamziki ambaye anampenda sana kwa wimbo huu wa DR. REMMY ONGALA Uitwao NARUDI NYUMBANI ni.



Wednesday, March 3, 2010

AHSANTE MUNGU KWA KUITENDEA FAMILIA YA MZEE NGONYANI MIUJIZA

Nakumbuka mwaka 1996, kuna tukio la kushangaza kidogo lililotokea katika tasnia ya Michezo kule nchini Italia na kuushangaza ulimwengu.
Tukio hilo lilimtokea mchezaji wa Kimataifa aitwae Nnwanko Kanu. Huyu alikuwa ni mchezaji wa Timu ya taifa ya Nigeria, ambaye alikuwa akichezea timu ya Ajax ya Uholanzi.

Ni baada ya Kuiwezesha nchi yake kutwaa kombe la Olympic, hapo mnamo mwaka 1996, ndipo alipopanda kilele cha mafanikio na kununuliwa na timu maarufu ya kule Italia inayoshiriki ligi ngumu ya almaarufu kama Serial A.

Mchezaji huyu alinunuliwa na timu ya Inter Milan na ni wakati alipokuwa akifanyiwa vipimo vya afya,(Medical Check Up) ndipo matokeo ya vipimo hivyo vilipoushangaza ulimwengu. Nnwanko Kanu aligundulika kuwa na matatizo ya moyo na alitakiwa kufanyiwa upasuaji haraka sana ili kunusuru afya yake.

Ikumbukwe kuwa mchezaji huyo tayari alikuwa akishiriki ligi za kimataifa, akichezea timu ya Ajax ya Uholanzi pamoja na kuchezea timu yake ya Taifa ya Nigeria na kuiwezesha kutwa kombe la Olympic, lakini katika kipindi chote hicho haikuwahi kugundulika kuwa na tatizo hilo. Hata hivyo kulikuwa na kupingana kwingi kitaalamu kati ya madaktari wagunduzi wa tatizo hilo na wale wa Uholanzi, lakini hatimaye alifanyiwa upasuaji na kurejea katika anga za michezo na kupata mafanikio makubwa.

Nimelikumbuka tukio hili kutokana na kile kilichomtokea mdogo wangu Asifiwe, huyu ni mdogo wetu wa mwisho kuzaliwa. Tukiwa tumezaliwa wanaume watano na wanawake wawili, yaani kati ya watoto saba wa Mzee Ngonyani na mama Ngonyani tuko watoto wakike wawili tu, yaani mimi na huyu mdogo wangu Asifiwe.

Akiwa darasa la sita ndipo alipoanza kuugua, ghafla, na tatizo kubwa lililokuwa likimsumbua ilikuwa ni tatizo la kukosa nguvu ghafla na kubanwa na kifua, lilikuwa ni tatizo ambalo kule Songea katika Hospitali ya Peramiho hawakuweza kugundua kuwa ni tatizo gani lakini kwa juhudi za madaktari aliweza kupewa tiba ambayo hata hivyo ilimletea nafuu badala ya kumponyesha.


Ni mwaka jana mwezi wa pili nilipokuwa nyumbani Tanzania ndipo nilipokata shauri tumpeleke katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa ajili ya vipimo zaidi. Ni hapo ndipo tulipo shangawa na matokeo ya vipimo kuwa mdogo wetu Asifiwe anayo matatizo ya Moyo na anatakiwa kufanyiwa Upasuaji nchini India.

Naamini hata wewe unayesoma hapa unaweza kuhisi ni kwa kiasi gani nilikuwa naumia kwa kile kilichomtokea mdogo wetu.

Hata hivyo baada ya kushauriana na madakatari alipangiwa kuwa awe anakuja pale Muhimbili kwa ajili ya matibabu yaani kliniki huku mchakato wa kufanyiwa upasuaji nchini India ukiendelea.

Kwa hiyo akawa anakuja Muhimbili na kurudi Songea (Ruhuwiko). Lakini mara hii ya mwisho yaani mwezi wa kwanza mwaka huu alipofika Kliniki aliandikiwa kufanyiwa upasuaji hapa hapa nchini na hivyo kulazwa pale Muhimbilli akisubiri kufanyiwa upasuaji.

Ni katika kipindi hicho sala na maombi vilifanyika kumuomba mungu afanikishe upasuaji huo ili mdogo wetu apone na kurejea shule kuendelea na masomo.
Mnamo tarehe 16/02/2010 mdogo wetu Asifiwe alifanyiwa upasuaji wa moyo na kwa uwezo wa Mwenye Enzi Mungu upasuaji ulikwenda vizuri na ijumaa tarehe 27/02/2010 ametolewa nyuzi zake na tarehe 01/03/2010 jumatatu ameruhusiwa.

Leo napenda kumshukuru Mwenye Enzi Mungu, Madaktari, Manesi na watu wote kwa Juhudi zao katika kumuhudumia mdogo wetu Asifiwe, sisi tunasema kwamba kwa uwezo wake ameweza kuisimamia kazi hiyo ya madaktari na kufanikisha upasuaji huo.Pia shukrani nyingi sana kwa daktari Mrs. Mushi wa kule Peramiho yeye ndiye aliyetupa ushauri wa kumpeleka Asifiwe, Kwanza katika kliniki moja hapa Dar ya Dr. Johnson M. Lwakatare. na ndipo tukapata rufaa ya kwenda Muhimbili .

Sisi tunaamini ni mungu pekee kwa kupitia mikono ya madaktari wale pamoja na manesi ameweza kufanikisha upasuaji huo. Nakumbuka siku tatu kabla ya kufanyiwa upasuaji huo nilizungumza na mdogo wangu, na kwa huzuni alinijulisha kuwa watoto wawili wa kike ambao walitangulia kufanyiwa upasuaji kabla yake wamepoteza maisha, ni watoto ambao walikuwa wana umri wa chini ya miaka 10, na walihitaji bado kuishi lakini Mwenye Enzi Mungu aliwapenda zaidi, na hivyo kuwatwaa. Ila namsifu Asifiwe, yeye hakuwa mwoga isipokuwa hakupenda kama ingetokea bahati mbaya kutuacha sisi nduguze.

Tulifanya maombi kwenye simu na nilimpa moyo mdogo wetu kuwa yote tumuachie Mungu kwani tunaamini atatenda miujiza. Lakini hata hivyo upasuaji uliahirisha tena kutokana na ziara ya ghafla ya mheshimiwa Raisi Jakaya Kikwete alipotembela hapo hospitali ya Muhimbili kuzungumza na madaktari.

Leo hii kwa niaba ya familia ya mzee Ngonyani napenda kuchukua nafasi hii kusema Ahsante Mungu kwa kuitendea familia ya Mzee Ngonyani Muujiza, Pia ningependa kuwashukuru wote mliokuwa nasi katika sala, katika kutupa moyo wakati tulipokuwa na mawazo. Na shukrani nyingi zimfikie kaka yetu Ngonyani na mkewe wa pale Kinondoni Kinondoni Mkwajuni kwa kuwa karibu nasi wakimhudumia mdogo wetu katika kipindi chote alipokuwa akija kliniki na hata wakati wa kufanyiwa upasuaji. Ninawashukuru kwa kuwa walitumia muda wao mwingi kwenda na kurudi Muhimbili ili kuhakikisha mdogo wetu Asifiwe hajisikii mpweke.
Na pia napenda kumpongeza yeye mwenyewe Asifiwe kwa kutoonyesha uoga.

Ningependa kuzisindikiza shukrani hizi kwa wimbo wa Upendo Nkone uitwao Hapa nilipo.







Tuesday, March 2, 2010

Je? ulijua kuwa mwanamke wa kwanza ambaye amekuwa mke wa marais kwa nchi mbili ni Grace Machel?!!!

Grace Machel mwanamke wa kwanza,
kuolewa na marais wa nchi mbili.

Grace Machel alikuwa amefunga ndoa na Samora Machel (1933 -1986) , ambaye alikuwa rais wa Mozambique kati ya mwaka 1975-1986. Alifariki kwa ajali ya ndege tarehe 19 Octoba 1986.

Tarehe 18 Julai 1998 Grrace alifunga ndoa tena na Nelson Mandela ambaya wakati ule alikuwa rais wa Afrika ya kusini. Kwa mtindo huu, Grace amekuwa mwanamke wa kwanza ambaye ameolewa na marais wa nchi mbili.

Monday, March 1, 2010

NDOA YA MALAIKA HAIJAWAHI KUWEPO DUNIANI



Wakati mwingine misukosuko ya ndoa huwaliza wanawake,
lakini hizo zote ni changamoto !


Kuna kudanganyana kwingi kuhusu ndoa pale mtu anaposhindwa kuwa mwangalifu sana kwa kauli za wengine walio kwenye ndoa. Hii hutokana na ukweli kwamba kuna kujumuisha kwingi sana. Kuna wakati huwa tunasikia au kuambiwa kwamba ndoa ni sawa na jehenamu. Baadhi ya watu walio kwenye ndoa kuna wakati huzungumza kwa njia ambayo hutufanya tuamini kwamba kuoa au kuolewa ni jinai. Ndoa ni ujinga mtupu haina maana, mtu anaweza kusema. Wasemaji hawa wanaweza kuwa ni watu tunaowaamini sana kama wazazi wetu na wengine wa aina hiyo.
Baadhi ya watu badala ya kuponda na kubeza kuizungumzia kama kitu kizuri sana kisicho na doa wala chembe ya usumbufu. Inawezekena kabisa nasi tukawaamini wazungumzaji hao, hivyo kuamini kwamba, ndoa hazina usumbufu.
Inawezekana dhana hii ikaingizwa vichwani mwetu wakati tukiwa wadogo au hata tukiwa watu wazima. Hebu fikiria juu ya mtu ambaye anajisifu kwamba ndoa yake haina hata chembe ya mkwaruzo. Ambaye anaieleza ndoa yake kwa njia yenye kushawishi kuwa, kumbe ndoa zenye matatizo siyo ndoa bali kisirani kitupu. Kama nawe uko kwenye ndoa na ndoa hiyo ina matatizo hata madogo unaweza kudhani kwamba ulikosa kuoana na huyo mwenzako. Dhana hiyoinaweza kuchipuka kutokana na kauli kama hiyo inayoelezea ndoa kama kitu kisicho na mikwaruzo hata kidogo.
Kama usipokuwa mwangalifu unaweza kuacha kuchukua hatua za kujaribu kuondoa tofauti zilizo kwenye ndoa yenu. Utaacha kufanya hivyo kwa sababu mtu fulani atakuwa tayari ameingiza kichwani mwako uongo kwamba ndoa ni “asali” na “maziwa” matupu. Ni uongo kwa sababu hakuna ndoa isiyo na mikwaruzo.
Tunatakiwa kujua kwamba lengo la ndoa siyo kuepuka kukorofishana , hapana . Ukweli ni kwamba kukorofishana kunapotumiwa vema huweza kujenga uhusiano mzuri na imara sana. Kwa sababu kukorofishana hakuwezi kuepukika kwenye ndoa kunatakiwa kutumika kama shule na dawa ya kuimarisha ndoa.
Bila kukwaruzana kwenye ndoa zetu inaweza ikawa vigumu sana kwetu kubandua tabaka la uongo lililotufunika ambalo humfanya kila mmoja kati yetu kushindwa kuona na kumfahamu mwenzake katika tabia yake halisi.
Bila kukwaruzana, kila mmoja wetu atajidanganya kwamba anamfahamu mwenzake kama alivyo wakati siyo kweli. Tunapokwaruzana tunapata nafasi ya kufahamiana vizuri katika hali halisi.
Mwanamke mmoja maarufu aliwahi kuulizwa kama huwa anakwaruzana na mumewe. Alikiri kwamba huwa wanakwaruzana kwa kusema , “ndiyo tunakwaruzana, vinginevyo tungekuwa hatuna tofauti, na hapo bila shaka ndoa na maisha vingekuwa vimepooza sana”. Huo ndiyo ukweli wenyewe, kwamba bila kukwaruzana hatuwezi kufahamiana vema na kujua kwa undani tofauti kati yetu na wenzetu.
Inabidi tujue kwamba hakuna binadamu aliyekamili, yaani asiyekosea, kama ilivyo dunia yenyewe. Kwa hali hiyo hakuna ndoa ambayo haina makosa, kwa sababu ndoa ni binadamu hao ambao siyo kamili. Kwa hiyo, mtu anapotarajia kuwa au kuishi kwenye ndoa isiyo na kukwaruzana, ni sawa na mtu huyo kutarajia kukutana na binadamu ambaye ni kamili, yaani asiyekosea.
Kutarajia kuwa na ndoa ambayo haina kukwaruzana kunaelezwa kuwa ni chanzo kizuri sana kwa ndoa nyingi kulegelege au kuanguka kabisa. Mtu anapoingia kwenye ndoa akitarajia kwamba huko hatapambana na maudhi au kero za aina fulani, ni lazima ajue kwamba, hatadumu kwenye ndoa yake kwa sababu ndoa hiyo anayoitarajia haipo.
Mtu ambaye hakubali au angalau hataki kuelewa kwamba, ndoa ni lazima iwe na mikwaruzo anaweza kukabiliwa na tatizo lingine baya zaidi kwenye ndoa yake. Kwa kutokujua au kuepuka kukwaruzana, hawezi kuwa tayari kukubali kujadili migogoro ya kindoa ili kupata ufumbuzi. Hawezi kulikubali hilo kwa sababu haamini kwamba ndoa yenye kukwaruzana ni ndoa.
Wakati mwingine rafiki, ndugu au jamaa zetu hutusimulia jinsi ndoa zao zisivyo na kukwaruzana kama kwamba ni za malaika watupu. Bila kujua, huwa tunajikuta tumewaamini. Tunapowaamini huwa tunachukulia kukwaruzana kuliko kwenye ndoa zetu kama jambo au kitu ambacho hakikutakiwa kuwepo. Hapo hujikuta tukitamani kuondoka kwenye ndoa hizo kwa matarajio kwamba tunaweza kukutana na “malaika” ambao tutajenga nao ndoa zisizo na doa.
Hata pale ambapo tunasema wanandoa wanapendana sana, bado ndoa yao ni lazima itakuwa na kukwaruzana. Lakini wanachofanya hawa na ambacho huenda wengine hawafanyi ni kujadili tofauti hizo sawia na kuamua kuzisahau na hapo wote kukubali kujifunza kutokana na tofauti hizo.
Wale walio tayari kujadili tofauti zao sawia ndiyo ambao ndoa zao huwa na afya sana hadi wengine kushangaa kama siyo pamoja na kuona wivu. Wale wanaodhani ndoa ni mahali pa kila jambo kwenda kama mtu atakavyo, ndoa zao hupogoka vibaya na kufa kwa kishindo........
Makala hii nimeitoa katika Gazeti la Jitambue la hayati Munga Tehenan.