Monday, March 15, 2010

Pendo langu kwako wewe

Uketi chini mpenzi, ya moyoni nikwambie,
Daima nitakuenzi, uhai uniishie,
Hutoipata simanzi, nataka ufurahie,
Pendo langu kwako wewe, halipimwi kwa mizani.

Halipimwi kwa mizani, uzitowe wazidia,
Pendo linayo thamani, hakuna cha kufikia,
Hata kwa mizani gani, huwezi kulipimia,
Pendo langu kwako wewe, hutolikuta dukani.

Hutolikuta dukani, ati labda lauzwa,
Pendo li ndani moyoni, kwalo pendo nimemezwa,
Kwani halina kifani, kwa kitu likaigizwa,
Pendo langu kwako wewe, kwa mwingine hulikuti.

Kwa mwingine hulikuti, pendo akakupatia,
Nina pendo lenye dhati, ya moyo uloridhia,
Pendo liso na wakati, daima kufurahia,
Pendo langu kwako wewe, ling'aalo kama nyota.

Ling'aalo kama nyota, maishani kuwa nuru,
Pendo raha kulipata, kufaidi kwa uhuru,
Pendo chozi kunifuta, kwa nini nisishukuru,
Pendo langu kwako wewe, liishi zote dawamu.

Liishi zote dawamu, linipe raha ya moyo,
Pendo hili na lidumu, kwa furaha linipayo,
Pendo hili mbona tamu, kwa tamu niipatayo,
Pendo langu kwako wewe, kamwe halina mipaka.

Kamwe halina mipaka, pendo mali yako yote,
Kukupenda sitochoka, pendo ulimi na mate,
Juwa kwangu umefika, wala us'ende kokote,
Pendo langu kwako wewe, waache waone wivu.

Waache waone wivu, kwa pendo ninalokupa,
Sisi tule zetu mbivu, pendo lizidi nenepa,
Kwako niwe msikivu, sitowaza kukutupa,
Pendo langu kwako wewe, wacha lizidi shamiri.

Wacha lizidi shamiri, wacha pendo na ling'ae,
Kukupata ni fahari, wengine uwakatae,
Pendo kwako li mahiri, unifae nikufae,
Pendo langu kwako wewe, mbona linanipa raha.

Mbona linanipa raha, ni bahati sana mie,
Pendo lajaa furaha, wacha nilifurahie,
Kwa pendo nipate siha, nishibe na nichanue,
Pendo langu kwako wewe, ni mwisho wa mambo yote.


Nimelipenda shairi hili na nimeona sio vibaya kama nikiliweka hapa kuwakilisha ujumbe huu. Nimelipata toka kwa http://fadhilimshairi.blogspot.com/. Haya tufurahi pamoja.

12 comments:

Fadhy Mtanga said...

Ahsante sana mweeh!

Simon Kitururu said...

Bonge la tungo hili Askofu Fadhy!

o'Wambura Ng'wanambiti! said...

Ningenona sana kama ningepata wa kuniimbia namna hiyo....lol

Kazi nzuri

EDNA said...

Kazi nzuri sana, nitamuimbia msweet wangu.

Upepo Mwanana said...

Hilo ni tungo MWANANA he he heee

Anonymous said...

Ng'wanambiti pole wee.. Unasubiri nini hadi leo?

PASSION4FASHION.TZ said...

Kweli hiki ni kipaji,kila mmoja amejaliwa chake,asante kaka Fadhy kwa kutungo nzuri.

Baraka Chibiriti said...

NA MIMI PIA KWAKO, ha ha ha haaaa....!!!! asante sana kwa maneno mazuri.

Mija Shija Sayi said...

Hivi mafeministi wanaweza kuwaimbia waume zao hivi? Najiuliza tu kama Mt.Kitururu

watila said...

mimi nimepigwa na mshangao sijuwi kama nitaweza kuchangia kitu leo da yasinta duhhhhh

o'Wambura Ng'wanambiti! said...

Anony: namsubiri huyo huyo....lol

Yasinta Ngonyani said...

Ni kweli hili shairi ni bonge la tungo Mtani Fadhy una kipaji sio mchezo. Ahsante kwa kuniruhusu niweka hapa kibarazani kwangu. Na asanteni wote kwa kuchangia kimaoni ni furaha kuona tupo wengi tunaopenda tungo zako mtani.