Wednesday, August 31, 2011

Mtoto huyu ametelekezwa na wazazi wake baada ya kuzaliwa na ulemavu njia ya haja kubwa!!!!

Haya ndugu zanguni ile siku ya kipengele cha marudio ya makala/mada mbalimbali ndio leo yaani ile JUMATANO. Na leo katika pita pita zangu nimekutana na makala hii ebu soma mwenyewe...Mimi nimeipata hapa.
----------------------------------------------------------------------------------------------
Na Albano Midelo.
MTOTO Anna Mapunda mwenye umri wa miaka mitatu mkazi wa kijiji cha Mkako wilayani Mbinga mkoani Ruvuma anahitaji msaada wa matibabu katika hospitali ya Muhimbili jijini Dar es salaam baada ya kuzaliwa na ulemavu sehemu ya haja kubwa.
Mtoto huyo anasumbuliwa na tatizo la kutokwa na sehemu ya haja kubwa nje kila anapokwenda kujisaidia na kwamba sehemu hiyo hukaa nje kwa hadi saa tatu kisha huanza kurudi yenyewe taratibu ambapo mtoto huyo hupata maumivu makali.
Kutokana na mtoto Anna kuzaliwa na tatizo hilo,baba yake mzazi anadaiwa alikuwa anampiga mtoto huyo kila sehemu ya haja kubwa inapotoka nje wakati anajisaidia hatimaye aliamua kumpa talaka mke wake na kwenda kuoa mwanamke mwingine ambapo mama mzazi wa Anna naye aliamua kwenda kuolewa na mume mwingine katika mji wa Mbambabay mwambao mwa ziwa Nyasa.
Mtoto Anna akiwa na mama yake mzazi tatizo hilo liliendelea kumsumbua mtoto huyo ingawa alimpeleka katika zahanati ya kijiji pamoja na kwenda kwa waganga wa jadi kwa ajili ya kutafuta tiba za jadi ,hata hivyo tatizo liliendelea hali iliyosababisha mama huyo kumtelekeza mtoto wake baada ya kukata tamaa.
Mtoto Anna mapema mwaka huu alichukuliwa na shangazi yake ambaye anaishi mjini Songea na kwamba baba mzazi wa mtoto huyo alimwambia dada yake ambaye ni shangazi ya mtoto huyo kuwa amchukue ampeleke hata kwa wachuna ngozi yeye hamtaki kwa madai kuwa ameleta laana katika familia yake.
Shangazi ya mtoto huyo alimchukua mtoto huyo na kuanza kuhangaika ili kutatua tatizo hilo ndipo alimpeleka kwa rafiki yake katibu ya Tanzania Assemblies Of God TAG kanisa la Ruhuwiko Songea Veronika Milanzi pichani kulia akiwa na mtoto Anna ambaye alikuwa akimpeleka katika kanisa hilo kwa ajili ya kumfanyia maombi kila siku.



“Nilimpompeleka siku ya kwanza kanisani kwa ajili ya kufanyiwa maombi mtoto huyu alikataa kurudi tena kwa shangazi yake tangu wakati huo hadi sasa ni karibu mwezi wanne mtoto huyu anaishi na mimi ,shangazi yake amekubali niendelea kuishi naye hadi sasa lakini tatizo lake la kutoka haja kubwa bado linaendelea’’,alisema
Katibu huyo wa TAG licha ya kumfanyia mtoto maombi kila siku lakini pia alichangishana fedha na baadhi ya waumini ili kumpeleka mtoto katika hospitali ya misheni ya Peramiho ambako walimchunguza na kudai kuwa angekuwa na tatizo la kutoka utumbo wa haja kubwa bila kurudi ndani wangemfanyia upasuaji na kumaliza tatizo hilo na kwamba kwa kuwa utumbo wa haja kubwa wa mtoto huyo unatoka nje anapokwenda haja na kisha unajirudi ndani pole pole hawana uwezo wa kumfanyia upasuaji.
Akizungumzia kitaalamu kuhusu tatizo hilo Dk Henry Mayala anasema magonjwa katika njia ya haja kubwa kitalaamu yanaitwa bawasiri ambayo ni mojawapo ya tatizo ambalo mara nyingi linapotokea humfanya mtu kuwa na aibu kuelezea au kwenda hospitali ili kupata tiba sahihi.
Dk.Mayala anabainisha kuwa bawasiri au hemorrhoids husababishwa na kuvimba kwa mishipa ya damu aina ya vena katika eneo la mfereji wa haja kubwa na kwamba kuna aina mbili za bawasili ambazo ni bawasili ya nje na ndani“Bawasili ya nje hutokea katika eneo la mwisho kabisa la mfereji wa haja kubwa, na huweza kuambatana na maumivu, pamoja na kuwashwa kwa ngozi katika eneo hilo. Mara nyingine mishipa hiyo ya damu (vena) hupasuka na damu huganda na kusababisha aina kitaalamu inaitwa Thrombosed hemorrhoid na bawasili ya ndani hutokea ndani ya mfereji wa haja kubwa. Na huwa haimbatani na maumivu na wengi huwa hawatambui kuwa wanatatizo hili’’,alisisitiza.
Kulingana na mtaalamu huyo bawasili ya ndani imegawanyika katika madaraja manne ambayo ni daraja la kwanza la ni kutotoka katika mahali pake pa kawaida,daraja la pili bawasiri kutoka wakati wa haja kubwa na kurudi yenyewe baada ya tukio hilo,daraja la tatua bawasiri kutoka wakati wa haja kubwa na mtu kuweza kuirudisha mwenyewe baada ya tukio hilo na daraja la nnebawasiri kutoka wakati wa haja kubwa na vigumu mtu kuirudisha baada ya tukio hilo.
Amezitaja sababu zinazosababisha magonjwa ya haja kubwa kuwa ni pamoja na Tatizo sugu la kuharisha,Kupata kinyesi kigumu Ujauzito,Uzito kupita kiasi (obesity), Ngono ya njia ya haja kubwa (anal sex),Kwa ujumla mambo yanayo ongeza shiniko katika tumbo.• Umri mkubwa.
Milanzi ambaye anataka kumpeleka mtoto huyo katika hospitali ya Taifa ya Muhimbili jijini Dar es salaam au hospitali nyingine ambazo zinaweza kutoa matibabu anatoa rai kwa watu wenye mapenzi mema kumsaidia mtoto huyo gharama za matibabu,usafiri na kujikimu kwa kuwa yeye haina uwezo.
Iwapo umeguswa na ungependa kutoa ushauri au msaada wa wowote wa kufanikisha matibabu ya mtoto Anna Mapunda andika albano.midelo@gmail.com,simu+255 766463129

Tuesday, August 30, 2011

NILIPOKUTANA NA MWANABLOG MARKUS MPANGALA

Baada ya kukutana na kaka S hapa Ruaha safari ikaendelea kufika Dar es Salaamau, ikawa bahati tena nika/tukakutana na mwanablog mwingine pia ni mjomba na rafiki wa karibu sana. Si mwingine tena ni Mzee wa Lundu Nyasa.


Alijitahidi na akaja hapa Silver Sands kutusalimia hapa ni yeye Mzee Lundu Nyasa/Markus Mpangala, Yasinta na Kijana Erik.
Na hapa ni Markus na wajomba zake Erik na Dada Camilla.... Ilikuwa ni furaha kukutana na yeye. Kwani kama kawaida huwa furaha sana kuonana tulibadilisha maneno mawili matatu na muda ukawa ni mdogo ....

Monday, August 29, 2011

BREAKING NEWS:MNADHIMU MKUU WA JWTZ (SHIMBO) CHINI YA ULINZI WA POLISI WA INTERPOL

MNADHIMU MKUU WA JWTZ LUTEN JERALI ABDULRAHMAN SHIMBO

Shimbo na wizi wa Trilioni 3: Apata mshtuko na kuzirai!

Hali ilivyokuwa:
JK alienda AFRICA YA KUSINI majuzi na alikuwa anajaribu kuomba msaadakuisaidia TZ, wakamwambia hatutaweza kukusaidia maana una watu wanahela ambazo ni zaidi ya ambazo tungekusaidia. Ndipo wakamfahamisha juuya Mnadhimu wetu kuwa na account huko yenye zaidi ya TZS zaidi yatrilioni 3. Habari hii ilimshtua JK naye akataka ufanyike uchunguziambao uliibuka na usahihi wa taarifa toka SA kwani ilikutwa kwelijamaa ana hela hizo.
Inasemekana Interpol wamempatia Afande Shimbo ukweli wa Account zakenje ya nchi zenye pesa nyingi sana na amechukuliwa chini ya Ulinzi waInterpol kwenda Africa ya kusini kwa matibabu.
Amekuwa akiwakata posho wanajeshi wanaoenda kujitolea kusaidia mataifaya nje na wa ndani.
Hela nyingi zaidi ni pale alipokata fungu kubwa sana toka fedha zashukrani toka Comoro baada ya Tanzania kuisaidia nchi hiyo. Fedha hizozilitakiwa kugawiwa kwa wanajeshi kwa kuisaidia nchi hiyo lakini mkuuhuyu alizipiga panga na hawakujua kuwa alikuwa kafungua akaunti nje yanchi na kuzihamishia kule.
Ameshindwa kueleza kwa undani alizipataje pesa hizi kwenye akaunti naaliishiwa nguvu na kudondoka!
Si Shimbo pekee...
Kuna kijana mdogo sana anaitwa PTE Gwilla, huyu yupo Kurugenzi ya DPAana-deal na salaries za wanajeshi... Kinachoshtua ni askari mdogo sanalakini alikuwa ana maghorofa mawili makubwa, magari aina ya Coastermawili na benki alikutwa na zaidi ya 73mil TZS (kwa mshahara wakeasingeweza kuwa na vitu hivi)
Uchunguzi umeonyesha Gwilla alikuwa anacheza na mishahara ya wanajeshikwa muda mrefu (4yrs) kwa aidha mishahara hewa, kukata 500 kwa kilamwanajeshi (4yrs) na zaidi akawa anakula hela za likizo za wanajeshikwa zaidi ya miaka 3 (2009-2011).
Huyu naye kakamatwa na anashikiliwa Mgulani.
Kuna mwingine...
Ni Mkurugenzi wa malipo jeshini, Brigedia (CC) Zakayo, naye kalambamabilioni ya hela (kiasi sijakinasa vema bado lakini ni zaidi ya EPA)naye anashughulikiwa kwa karibu.
So far, niseme kazi nzuri Interpol, walau watu wataanza kuelewa kuwawatakuja kugundulika wakifanya uhuni wa namna hii.
HABARI HII KWA HISANI YA JAMII FORUM

NYIMBO ZA MCHAKAMCHAKA/KUMBUKUMBU

Leo nimekumbuka wakati nasoma shule hasa shule ya msingi saa kumi na moja alfajiri kuwahi shule, kisa nini? Kuwahi namba na kukimbia mchakamchaka huku mnatweta kama nini na mkiimba nyimbo:- Kwa mfano:-1. Panda mlima panda, panda, panda, panda usichoke........x2 wimbo wa 2. . Iddi amin akifa mimi siwezi kulia nitamtupa kagera awe chakula cha mamba.x2 wimbo wa 3. . Jua lille literemke mama, mwezi nao uteremke mama haiyahiyaaa hiyaa hiyaa mamaaaa.....x2wimbo wa 4. Alisema, alisema, alisemaaa Nyerere alisema vijana wangu wote mwalegea shart tuanze mchakamchakax2.....Kama kuna mtu anakumbuka nyimbo nyingine basi karibu kuongezea hapa.........Ila kuna kitu nimeumia sana. Ni kwamba safari hii nilipokuwa nyumbani, nimejaribu kuwahoji shangazi zangu kuhusu swala hili la kukimbia mchaka mchaka. Wakanijibu kuwa wao hawajui mchakamchaka, yaaniHAWAKIMBII KABISA...Sasa sijui ni Ruhuwiko tu au?..Nikaanza kujiuliza sasa wanafunzi hawa watakuwa kweli wakakamavu au? Sijui wenzangu mnalionaje hili swala? Tuendako kweli kuzuri?....Mmmmhh !!!

Friday, August 26, 2011

IJUMAA YA LEO:- NA METHALI HII!!!

Mtu huwezi kuchagua utakufaje. Isipokuwa unaweza kuamua ni vipi utaishi.


.......NAWATAKIENI WOTE MWISHO MWEMA WA KUANZA MWISHO WA JUMA.......

Thursday, August 25, 2011

Mwanablogger wa week hii - Emu Three kutoka Diary Yangu Blog

Karibuni katika mahojiano yetu ya kila week. Week hii nimepata bahati kufanya mahojiano na Emu Three ktoka blog ya Diary Yangu. Kama wewe ni mpenzi wa riwaya natumaini mara ukiifahamu hii blog kila siku utajikuta utarudi kusoma hadithi moto moto anazoziandika Emu Three.



Karibu hapa na tunafurahi kuweza kufanya mahojiano na wewe. Unaweza kutueleza kidogo kuhusu wewe na blog yako?

Mimi naitwa emu-three, na nimetumia emu-three kama ufupisho wa majina yangu matatu yaani jina la kwangu la baba na la ukoo yote yakianzia na herufi M. Na wakati naanzisha hii blog, nilikuwa nawaza niweje jina gani , na mara likanjia jina hilo la miram3. Mira ikiwa ni jina langu halisi kwa kifupi na m3, ikiwa M.M.M.
Je blog yako unatumia jina lako kamili au unablog kwa kutumia kivuli kingine na watu wanasoma na kuenjoy blog yako lakini hawajui wewe ni nani?
Blog yangu situmii jina langu kamili, natumia jina la kubuni tu `nick-name’, na watu wananitambua kama emu-three, kama nilivyosema awali kuwa ni kifupisho cha majina yangu matatu. Sina nia mbaya kutojiweka jina kamili na picha yangu, ila nililenga kuwa ninachokiandika ndicho kinieleze mimi. Nia ni kutoa kile nilichokuwa nacho, lakini ikiwa ni muhimu sana nitaweka picha yangu na kujielezea zaidi, hapo wapenzi wa blog hii watakapokuwa wengi na kupendekeza hivyo.!

Ni miaka mingapi sasa umekua ukiblog?
Nina miaka mitatu sasa tangu blog hii ianzee kuwa hewani, mwanzoni na nilituma nianze kublog, kwani nilituma maelezo ya mwanzo kabisa kama utambulisho tarehe 14-7-2009.

• Ni nini kilikufanya uanzishe blog?
Mimi ni mpenzi sana wa kuandika hadithi, kuweka kumbukumbu za matukio(diary) na napenda sana kusoma vitabu vya hadithi, hasa riwaya(novels) , tamithiliya nk. Nikawa naandika visa, au hadithi katika makatasi, na mwisho wa siku hayo makaratasi yanapotea au kuharibika, nikawa naandika kwenye computa za ofisini, nazo zinakumbana na virusi, au unaondoka kwenye hiyo kampuni na ina maana kila kitu kinamepotea. Nikaja kugundua kuwa kumbe kwenye blog unaweza ukaweka hizi kumbukumbu, za visa, hadithi nk na sio kuweka tu, bali unaweza kupata watu wakazisoma, na mkachangiana mawazo. Na kwa vile nia yangu ilikuwa sio kuandika tu, bali pia kutoa maoni yangu, kushauri,nk kuhusu hili na lile, nikaona blog ni sehemu nzuri kabisa. Kwa mfano mimi ninaamini kuwa kuwa kila tukio lazima lina na sababu, basi kwanini nisiweke hayo matukio na kuanisha nionavyo mimi ni sababu gani likatokea kwa kupekenyua chanzo chake, na hatimaye iwe kama kisa ambacho sio burudisho tu, bali kiwe na mafundisho ndani yake!

• Je, wewe kazi yako ni kublog tu au hii ni kama kazi ya muda tu au hobby?
Kwakeli kublog niliichukulia kama Hobby, na nina kazi nyingine inayonifanya niishi mjini, na kama utachunguza blog yangu haina hata matangazo ya kibiashara, sio kwamba sipendi, bali sijawapata watu wa kutangaza biashara zao. Kama kuna atakayependa kuweka tangazo lake namkaribisha sana. Kwa ujumla natumia muda wangu wa ziada, gharama zangu mwenyewe, na nashukuru kuwa naweza kutumia vitendea kazi vya muajiri wangu kuweza kufanikisha hili, ingawaje ni kwa shida, na vinginevyo nategemea sana internet cafe.

• Nini changamoto unazozipata kwa kuwa na blog?
Changamoto ni nyingi, kwanza kama nilivyosema awali muda mwingine nategemea sana vitendea kazi vya muajiri wangu, kama computa na internet ingawaje najitahis sana kutokutumia muda wake wa kazi, ninachofanya nikuwahi asubuhii sana na kuandika kile nilichokusudia kabla ya muda wa kazi, na zaidi sana natumia internet cafe. Kwahiyo swala la muda, gharama na vitendea kazi ni changamoto kubwa kwangu kwa sasa.

• Ni nani wasomaji wa blog yako?
Ni wote hasa wale wanaoutumia lugha ya kiswahili, ingawaje wengine wanaweza kutumia nyezo zilizopo kwenye blogs, kutafsiri kwa lugha zao. Matarajio kama ningeliweza, nilitaka iwe kwa lugha mbili ya Kiswahili na Kiingereza, ili wengine waweze kutafsiri kwa kirahisi kwenye lugha zao kwa kupitia kwenye lugha ya Kiingereza.

Ni nini imekuwa mkakati wako kwa ajili ya kujenga kujulikana kwa mwenyewe na blog yako zaidi?
Hilo pia limekuwa ni moja ya changamoto kwangu, kwani nimejulikana labda kwa kupitia kwenye blog nyingine ambazo wamenisaidia kuniweka kama blog rafiki, na wengine wamekuwa wakiambizana, na kuweza kuwavuta marafiki zao kuja kusoma visa kwenye blog hii, nawashukuru sana kwa hilo. Kama ujuavyo, watu wengi sasa hivi hawapendi kusoma, wanapenda zaidi kutizama, na kwahiyo mtu akiona umeandika taarifa ndefu, na haina hata kivutio kama picha anaghairi. Kwahiyo mkakati wangu ni kuiboresha hii blog, iwe ya kisasa zaidi, iwe sio tu kusoma, bali hata kutizama pia.

• Je unatumia mitandao mingine kama Twitter au Facebook kuitangza blog yako? Kama unazo unaweza kutuambia ili wasiofahamu waweze kufahamu na kukufuata?
Ndio natumia Facebook, hata Twitter, kwenye Twitter unaweza kunitafuta kama `emu-three’ lakini kwenye face book unaweza kunipata kama `diary yangu’
au http://miram3.blogspot.com/

• Je ni nini mkakati wako na blog yako kwa ujumla?
Mkakati wangu ni kuiboresha hii blog kuwa ya kisasa zaidi, na kuweza kuingiza e-book, kweny hii blog, nikipata wataalamu wa kunisaidia nitashukuru sana, na kwa vile leng ni kuwa mtunzi wa vitabu, basi blog hii itakuwa sehemu ya kujitangaza pia. Na ikiwezekana nisiifanye blog tu kama hobby, lakini iwe kazi yenye kuleta manufaa, sio kwangu tu hata kwa jamii kwa ujumla.

• Ni jinsi gani (mtu) anaweza kuelezea style/theme ya yako unavyo blog?
Mtindo wangu wa kublog unaweza kuelezewa kama blog ya visa vya kusisimua kutokana na matukio halisia. Ni kumbukumbu za kimaisha, kwani visa ninavyotunga ni vitu vilivyotokea na mimi naviboresha tu ili viweze kumsisimua msomaji.

• Je ni bloggers wapi ambao wewe unawaangalia na kufuata nyayo zao? Na kwanini?
Kwakweli kublog kwangu siwezi kusema nafuata nyayo za mtu fulani, sikumbuki kuwa nimeblg kwasababu ya mtu fulani, hapana, mimi nilipogundua tu kuwa kuna kitu kama hiki na unaweza kuweka vitu vyako bure, nikajimwaga, sio kwa ushawishi wa mtu, lakini wengi tu napenda blog zao, ikiwemo hii yako, na mimii huwa napenda sana kusoma walichoandika wenzangu, na nina imani kuwa kitu kipya ni kile hujakiona, kwahiyo kila blog ambayo sijaiona kwangu inanisismua kuisoma,na kuona mwenzangu ana nini katika mawazo yake!

• Je unafikiria kuwa unadaiwa na mtu akiacha comment/s kwenye blog yako?
Kuna jambo moja tuliweke akilini, mfano mtu akiweka comment kwenye blog yako, lazima atakuwa na shauku fulani, hasa iwe ya kuulizwa swali, ...au hata kama inakukwaza yeye atakuwa na matarajio fulani kuwa wewe mwenye blog unaweza kwa kutumia blog yako kumsaidia au kumsikia. Kwahiyo ni bora ukasema lolote, au usiitie kapuni, kwani ukifanya hivyo bila kuiweka hewani au bila kusema lolote, utakuona kama umemdharau, kwakweli ni deni...utakuwa hujamtendea haki mpenzi wa blog yako. Na pia kwa wale wanaosoma habari kwenye blog, ni busara pia ukasema lolote, kwani ni kama mtu kakupa kitu ukae kimiya,..ni busara kusema ahsante ...kwahiyo.unaweza hata ukaandika neno dogo tu la kushukurui au ukaandika `mmmh’ inatosha kabisa, ni maoni yangu tu.

• Je kuna thamani kujibu comment iliyoachwa kwenye blog yako wakati ukijua kuwa huyo aliyeiandika labda hatarudi kusoma jibu lake tena?
Ukiulizwa swali ni vyema kulijibu, kwasababu mara nyingi ukikaa kimya unatafsiriwa kuwa umezarau au sio, kwahiyo kinachotakiwa ni kulijibu lile swali, kwani muulizaji anaweza kuwa aliuliza hilo swali kwa maslahi yake, lakini swali hilo linaweza likawa limesomwa na watu wengi na hata kuwagusa watu wengine, kwahiyo kama yeye hakurudi kusoma majibu ya hilo swali watafaidika wengine, walioguswa nalo.
Nakushukuru sana kwa kunitupa fursa hii na sina cha kukupa zaidi ya kukuombea heri na fanaka katika utendaji wako, kwani wewe umekuwa mtu wa watu. Kujali wengine, ni kazi kubwa sana, inahitaji moyo, wewe hili umeliweza hilo, shukurani sana.
Asante sana Emu Three Kwa kufanya mahojiano haya na sisis na tunakutakia mafanikio mema katika blog yako........kuendelea kusoma habari/maelezo haya bonyeza hapa.

PICHA ZA WIKI HII:- MAMA NA MWANA!!!


CAMILLA NA MAMA YAKE YASINTA (mwaka jana 2010 mwezi wa saba)




NA HAPA NI MALIA NA MAMA YAKE MICHELLE

Ni ujumbe tu mfupi ambao unaweza kukufanya utafakari kitu fulani....PAMOJA DAIMA!!!



Wednesday, August 24, 2011

Unajifunza nini toka kwa umchukiaye?

Kama kawaida leo ni siku ya Jumatano na ndiyo ile siku ya kipengele chetu cha marudio ya mada/makala, picha pia matukio mbalimbali. Na leo katika kupekua pekua nimekutana na makala hii ambayo binafsi imenigusa sana na pia imenifunza kitu. Nadhani nanyi ndugu zanguni mtajifunza kitu...Makala hii inatoka kwa Mzee Wetu Wa Changamoto. Kribuni sana.




Photo Credits: Relationshipplaybook.com


Kuchukia si kitu kizuri. Lakini ukweli haupingiki kuwa watu wanawachukia wenzao. Na wengine wanawachukia watu kwa kuwa wanahisi watu hao wanawachukia wao. Sijui hapo nani anatibu nini!!! Nakumbuka kusoma nukuu ya mtu mmoja ikisema "huwezi kutatua tatizo kwa kutumia njia iliyopelekea tatizo hilo kutokea." Ina maana kwa kumchukia umdhaniaye anakuchukia nawe unakuwa na chuki kama yeye. Na kwa undani zaidi ni kama vile unataka kumdhihirishia kuwa nawe unaweza na pengine unasikitika kuwa hukuanza wewe kumuonesha hivyo. Tayari umeshakuwa kama yeye. Kisha nikasoma nukuu nyingine isemayo "If you hate a person, you hate something in him that is part of yourself. What isn't part of ourselves doesn't disturb us." Hermann Hesse Swiss author (1877 - 1962)
Lakini kuna binadamu aliye sahihi katika kila atendacho? HAPANA. Hata mapacha walioungana wana tofauti japo ya fikra (na twajua kuwa fikra hufuatwa na matendo) kwa hiyo lazima tukubali kuwa hatuwezi kuwa kama kila mtu na si kila mtu anaweza kuwa kama sisi. Na Je! Kuna binadamu asiye sahihi katika kila kitu? HAPANA. Hata umuonaye si sahihi ana wafuasi wamuonaye sahihi. Ukimuona adui wengine wanamuona shujaa kwao na wanamuiga.
Sasa kama kila mtu si kamili na si kila mtu ana mapungufu kama tuyaonayo sisi (na pengine tunaona hivyo kwa kuwa tuna mapungufu kwenye sehemu hizo) unadhani wao wanatuonaje katika misimamo yetu? NAO WANATUONA TUNA MAPUNGUFU.
Sasa kama ni mtu ambaye huna nafasi yoyote ama uwezo wa namna yoyote kum'badili tabia ama mwenendo utaendelea kuumia kwa chuki ndani mwako? Si suluhu ya tatizo na pengine usipokuwa makini utajikuta unakutana na mwingine kama wa awali na kama hukujifunza kitu toka kwa huyo wa mwanzo utaendelea kuwa mhanga wa watu hao. Ni kama waibiwavyo watu kwa kuwekewa "kanyaboya" na bado hawawi makini wanapofungiwa walichonunua.
Kubwa ni kwamba kila mtu ana kitu unachoweza kujifunza toka kwake. Uwe unampenda ama unamchukia. Ni namna tunavyojijengea utashi wa kujifunza kutoka kwa watu. Na kama kuna mtu m'baya kuliko wote uliowahi kukutana nao duniani, funzo la kwanza ni kuwa "kumbe wapo wabaya zaidi ya nilivyokuwa nafikiria!?"na kuanzia hapo unaweza kuamua kujifunza kujiepusha na / kukabiliana nao.
Ukikutana na mchoyo jifunze kwamba si kila mahali utakuwa na aliye tayari kukupa.
Ukikaa na mlafi jifunze kuwa usipokuwa makini utalala na kufa njaa.
Ukimuona muuaji jifunze kuwa maisha ya binadamu hayana thamani sawa machoni pa wengi.
Ukimuona fisadi jifunze kuwa tunaweza kutafsiri tofauti neno "mali ya umma."
Na mengine mengi.
Lengo kuu hapa ni kujua kuwa kila anguko lina nafasi ya kukupa funzo la ulipoanguka na ukiamua utajifunza kuwa makini usianguke tena, na hata ikitokea ukaangua basi isiwe kwa sababu iliyokuangusha awali.

Labda ni namna nionavyo tatizo, maana namna uonavyo tatizo ......................
Jumatatu njema.

-----------------------------------------------------------------------------------------

TUKUTANE TENA JUMATANO IJAYO... !!!!!

Tuesday, August 23, 2011

MDADA HUYU /YASINTA SIO MPENZI WA SAMAKI KWA UGALI WA MUHOGO TU BALI ....

....Ni mpenzi sana wa kuchuma/kutafuta na kula UYOGA pia . Leo nimeamka nikawa najisikia hamu kweli ya uyoga basi nikaamua niende mstuni na kutafuta matokeo yako ni hayo hapo juu. Nimechuma mwenyewe kwa mikono yangu . Jambo jingine ambalo ni zuri kwenda mstuni sio kutafuta uyoga tu. Ni kwamba ni dawa nzuri sana ya kupoteza mawazo. Kama mtu una mawazo sana . Maana ukiwa mstuni unakuwa peke yako na pia kimya utakachosikia sana sana ni milio ya ndege tu. NAPENDA SANA KUWA MSTUNI NIKIWA KATIKA HALI HII YA MAWAZO. PIA KULA UYOGA...KARIBUNI TUKULE JEMENI. Ila kwa sasa ntashindwa kuupika kwani inabidi niende kubeba maboxiiiiiiiiii.....kesho tutaangalia jinsi ya kupika...Jumanne njema kwa wote.:-)


Monday, August 22, 2011

MWANABLOG YASINTA NGONYANI/KAPULYA ALIVYOKUTANA NA KAKA SAMWELI MBOGO/KAKA S!!!




Picha ya pamoja ,Yasinta/kapulya, kaka S na binti yake Yasinta dada Camilla hapa ni Rwaha (mbuyuni)



Mama Maisha na Mafanikio a.k.a Kapulya akiwa na kaka S

Kweli wahenga walisema milima haikutani bali wanadamu hukutana... Nimetoka zangu Ruhuwiko/Songea mida ya mchana mchana hivi . Giza likaingia na kituo cha kwanza kikawa Njombe..Asubuhi yake safari ikaendelea , kufika Iringa tukapumzika na kupata soda moja na bila kusahau kuchimba dawa. Mara Mnyasa nikaona Samaki nikashindwa kuvumilia nikanunua samaki wawili...Safari ikaendelea mpaka kufika Rwaaha na hapo ikawa ni muda wa kupata chochote/chakula cha mchana. Basi mnyasa huyu na binti yake wakakaa na kuanza kuwatafuna wale samaki huku wakitelemshia maji..wakati wengine waliamua kula sambusa.

Sasa ngoja nikuambia nilichotaka kusema ni kwamba wakati nakula samaki hao...mara akaja kijana/kaka mmoja. Akasimama mbele yangu nami nikawa nakereke, na nikajiuliza huyu kijana/kaka anataka nini? au anataka samaki wangu nini? kwanini anasogea sana nilipokaa na nilivyo mwoga nikaanza kuogopa. Lakini kaka huyu akawa ananisemesha utazani anaifahamu au kama vile tumeonana miaka mingiiiii iliyopita. Kila nikimtazama sipati kabisa picha yake. EEeeh, nikaona hapa kaaazi kwelikweli nikawa najiuliza ananifanananisha au?...Baadaye akajieleza kuwa yeye ni msomaji, mchangiaji na mtembeleaji mzuri sana wa Maisha na Mafanikio... Hata hivyo nikawa sipati kabisa picha yake...unajua kwa nini? yeye hana picha ndio maana sikumjua maana sikuwahi kuiona picha yake. Hakika hapo ndio niliposema kweli unaweza kujuana na mtu bila kuijua sura yake, kweli MILIMA HAIKUTANI BALI WANADAMU HUKUTANA. Na pia kusafiri kwa usafiri wako ni kuzuri unaona mengi na unakutana na usiokutana nao. Ahsante!!

Saturday, August 20, 2011

WILAYA MPYA YA NYASA YAKABILIWA NA CHANGAMOTO ZA AFYA KWA WANAWAKE

Hili ni gari la wagonjwa lililotolewa na kamanda wa vijana wa CCM na mbunge wa Ludewa Deo Filikunjombe kituo cha Manda Ludewa.

Baada ya kupumzika jumamosi hii ya leo nikaona si vizuri nikipitia badhi ya vibaraza na kusafisha macho kidogo. Na kweli nimekutana na habari ambayo imenigusa sana hasa ukizingatia nimekwisha wahi kuishi katika mazingira haya. Lundo ndicho kijiji nilichozaliwa binadamu mimi kwa hiyo nimeona nami niweke hapa ili habari iweze kuenea na wengi walijue hili jinsi wanawake tunavyopata taabu. Habari hii nimeipata hapa.

-----------------------------------------------------------------------------------------------
SEKTA ya afya katika nchi yoyote duniani ina umuhimu mkubwa sana katika kuleta ustawi wa jamii na kwamba ili jamii iweze kujitegemea kielimu,kisiasa,kiuchumi ni lazima iwe na afya bora itakayowezesha nchi kupiga hatua kusudiwa
Uchunguzi uliofanywa na mwandishi wa mtandao wa TGNP na mtandao huu Stephano Mango kutoka Nyasa umebaini kwenye wilaya mpya ya Nyasa Mkoani Ruvuma katika shughuli za kiuandishi kufuatilia hali ya huduma ya afya ya uzazi kwa wakazi wa wilaya hiyo iliyopo mwambao mwa Ziwa Nyasa
Nilibahatika kufika huko kwa ufadhiri wa Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP)na kuweza kufanikiwa kutembelea kata sita za Lituhi,Mbaha,Kihagara,Mbambabay,Chiwanda na Kilosa katika wilaya hiyo
Katika shughuli zangu za uandishi nilibaini mambo kadhaa yanayowakumba akina mama wajawazito kabla na baada ya kujifungua wakati wa kwenda katika vituo vya afya na Zahanati kupata huduma ya afya ya uzazi na mtoto
Miongoni mwa mambo hayo ni umbali mrefu kutoka kwenye makazi hadi kufika katika vituo vya afya ili kuweza kupata huduma ya kliniki kwani akina mama wengi wajawazito wamekuwa wakitembea umbali mrefu pekee yao bila hata kusindikizwa na wenza wao
Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili kutoka katika vijiji vya
Chimate,Mtupale,Chinula,Ndengele na N’gombo umebaini kuwa akina mama wengi wajawazito wamekuwa wakikumbana na kero kubwa ya usafiri wa kutoka kwenye vijiji wanavyoishi hadi kwenye vituo vya afya kufuata huduma za kliniki ya mama na mtoto
Imebainika kuwa akina mama hao wajawazito wamekuwa wakichelewa kufika katika vituo vya afya na wakati mwingine kukosa kabisa huduma muhimu ya afya ya mama na mtoto kutokana na adha kubwa ya usafiri jambo linalopelekea kudhoofika kwa afya zao kabla na baada ya kujifungua
Baadhi yao kutoka katika Vijiji vya Mtupale,Mtipwili,Chiulu,Kwambe,Mbaha na Kingirikiti wakizungumza na gazeti hili walisema kuwa kutokana na umbali mrefu uliopo toka wanakoishi hadi kwenye vituo vya afya wamekuwa wakishindwa kuhudhulia kliniki kabla na baada ya kujifungua kwani wakina mama hao wamekuwa wakilazimika kujifungulia majumbani kwa sababu ya kukosa nauli na wakati mwingine usafiri wa kuwafikisha katika vituo hivyo
Walisema kuwa hali hiyo licha ya kuwa ni hatari kwa afya zao lakini wamekuwa wakilazimika kufanya hivyo kutokana na mazingira magumu waliyonayo katika maeneo wanayoishi na kwamba Zahanati nyingi zilizopo kwenye maeneo jilani wanayoishi zimekuwa zikikosa dawa,wataalamu pamoja na vifaa tiba
Uchunguzi huo umebaini kuwa Wilaya mpya ya Nyasa ina vituo vya Afya Vitatu ambavyo ni Lituhi kinachomilikiwa na Kanisa Katoliki Jimbo la Mbinga,Liparamba na Mbambabay pamoja na Hospitali ya Liuli ambayo inamilikiwa na kanisa la Anglikana Dayosisi ya Ruvuma pamoja na Zahanati nyingi ambazo huduma yake ni duni
Imebainika kuwa wakina mama wajawazito kutoka kijiji cha Mango hadi kituo cha afya cha Mbambabay wamekuwa wakitembea kwa miguu umbali wa kilometa 43 na wakati mwingine wamekuwa wakitumia usafiri wa Yeboyebo(pikipiki) kwa nauli ya shilingi elfu 9,500 ambako kwa gari ni shilingi elfu 3000
Aidha imebainika kuwa gharama za matibabu ni kikwazo kwa akinamama hao kwani wamekuwa wakichangia huduma za kliniki na matibabu kati ya shilingi 2000 na shilingi 6000 kila wanapohitaji kupata huduma kinyume na sera ya taifa ya matibabu bure kwa wajawazito na watoto chini ya miaka mitano
Wakizungumza kwa nyakati tofauti na gazeti hili katika kata ya Lundo akina mama hao walisema kuwa Serikali imekuwa ikisema akina mama wajawazito na watoto chini ya miaka mitano wanatakiwa kupata huduma ya afya bila kuchangia malipo lakini wao wamekuwa wakichangia fedha nyingi
Kutokana na kuchangia gharama hizo ambazo kwao zimekuwa kero kubwa wamekuwa wakilazimika kwenda kliniki wanapokaribia kujifungua tu ili kuweza kukwepa gharama zinazotozwa mara wanapofika katika Zahanati na vituo hivyo kutokana na ugumu wa maisha
Walisema kuwa katika kata hiyo kuna Zahanati ya Lundo ambayo mara nyingi imekuwa ikikosa dawa muhimu za wajawazito na wahudumu wake wamekuwa na lugha chafu kwa wagonjwa hali inayopelekea akina mama wengi kutohudhulia Kliniki kwa kuhofiwa kutukanwa na kupoteza muda wa kufanya kazi zao za kujitafutia ridhiki
Mary Haule mkazi wa kata hiyo ambaye anaujauzito wa miezi saba alisema kuwa kutokana na hali hiyo amekuwa akienda kupata matibabu katika Kituo cha Afya cha Mbambabay kwa kuhofia usalama wake wakati wa kujifungua
Haule alisema kuwa wajawazito wengi wamekuwa wakinyanyaswa sana pindi wanapofika katika Zahanati kwa ajili ya kupata huduma za matibabu jambo ambalo linaonyesha uzalilishaji wa hali ya juu kwa wanawake
Uchunguzi uliofanya na Gazeti hili umebaini kuwa Zahanati nyingi za Mwambao mwa Ziwa Nyasa zimekuwa zikikosa dawa muhimu kwa ajili ya wajawazito na watoto chini ya miaka mitano kutokana na mgawanyo usio wa uwiano unaotolewa na Bohari ya Madawa Nchini(MSD)
Aidha kutokana na ukosefu huo wa dawa uchunguzi umebaini kuwa wahudumu wa Zahanati hizo wamekuwa wakiwauzia dawa na vifaa tiba wajawazito kwa bei kubwa hali inayopelekea unyanyasaji mkubwa kwa akina mama hao ambao wanatoka umbali mrefu kwa ajili ya kupata matibabu stahiki
Gazeti hili lilishuhudia baadhi ya wajawazito 3 katika Kituo cha Afya cha Mbambabay wakitokea Kata ya Tumbi umbali wa kilometa 43 ambapo wamekuwa wakitembea kwa miguu na wakati mwingine kwa pikipiki kwa kutozwa nauli kubwa kwenda kuhudhulia Kliniki
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga ambaye pia ni Diwani wa Kata ya Chiwanda Oldo Mwisho aliliambia gazeti hili kuwa kufuatia adha wanazopata wakina mama wajawazito alisema kuwa Halmashauri yake inazitambua adha hizo na kwamba sera ya afya ya Serikali imetamka wazi kuwa kila kata ni lazima ijenge kituo cha afya ili kukabiliana na adha hizo na kila kijiji ijenge Zahanati
Mwisho alisema kuwa kutokana na hali wananchi wamekuwa wakihimizwa ujenzi wa vituo vya afya kwenye kata zao ambapo changamoto kubwa inayoikabili Serikali ni ubovu wa miundombinu, upungufu wa wataalamu wa afya,dawa na vifaa tiba
Akizungumza na gazeti hili Mbunge wa Jimbo la Mbinga Magharibi Kapteini John Komba alisema kuwa Wilaya ya Mbinga ina eneo kubwa la kiutawala hivyo ilikuwa imezidiwa uwezo wake wa kutoa huduma kwa jamii kwani ilikuwa ina hudumia wakazi wa majimbo mawili ya uchaguzi la Mbinga Magharibi na Mbinga Mashariki
Komba alisema kuwa Serikali kuu kwa kutambua ukubwa wa eneo hilo imeamua kuyagawa majimbo hayo katika Wilaya na kupata Wilaya ya Mbinga na Wilaya mpya ya Nyasa ambayo inaanza rasmi katika kipindi hiki cha bajeti ya mwaka wa 2011/2012 hivyo mara itakapoanza itapunguza adha hizo za wajawazito kwa kiasi kikubwa
Alisema kuwa mara nyingi amekuwa akipigania ustawi wa afya za akina mama wajawazito anapopata wasaa wa kuchangia bungeni akiwa mwanasiasa aliyepewa dhamana na wananchi katika kushirikiana nao kujiletea maendeleo kusudiwa katika jimbo hilo.

Friday, August 19, 2011

NAMTAFUTA MDOGO WANGU KWA MAMA MWINGINE "HIARI" KOERO MKUNDI:- JE? KUNA ANAYEJUA WAPO ALIPO?

Ni muda sasa umepita tangu 24/6, mdogo wangu huyu sijamsikia wala kuona katika vibaraza vingine akitoa mchango wake.Si mwingine tena ni Koero Mkundi. Ninakumiss sana UPO WAPI? Je? kuna anayejua alipo. Koero, natumaini na naamini kwamba uko salama; na ukibahatika kusoma ujumbe huu tujulishe uliko koeromkundi.blogspot.com.


IJUMAA NJEMA :- NCHI YETU TANZANIA!!!


Nawataeni wote mwisho wa juma mwema.....

Wednesday, August 17, 2011

JUMATANO YA MARUDIO/KUMBUKUMBU..LEO NI KUMBUKUMBU YA MAMA YETU ALANA NGONYANI MIAKA SABA SASA HATUNAYE KIMWILI!!!

NI MIAKA SABA LEO TANGU UTUACHE MAMA
Hapo ni mama Alana ni huyo aliyekaa na mimi
nikimsuka mwaka 1997 kijijini Mahumbato Mbinga!!!


Ndugu zanguni leo ni ile siku ya JUMATANO ambayo ni:- kipengele cha marudio ya mada/makala, picha na matukio mbalimbali. Na leo imeangukia kuwa ni jumatano ambayo mama yetu Alana Ngonyani alituacha. Kwa hiyo nimeona iwe siku ya marudio ya mada hii au niseme kumbukumbu.
------------------------------------------------------------------------------------
Nimeamka leo nikiwa na majonzi mengi kwani hii tarehe huwa inanikumbusha sana mama. Kwani ndio ilikuwa pia JUMATANO ya tarehe 17/8/2004, ambayo alituacha kwa hiyo leo ni miaka 7. Nina mengi ya kuongea nawe mama, kuna wakati huwa nadhani upo nasi na nachukua simu na nataka kuongea nawe, nataka kuisikia sauti yako, kicheko chako pia kukuomba ushauri/mawazo. Na mwisho nabaki nikitoa machozi. Mweeh!!!.

Halafu natamani kweli kukusimulia jinsi wajukuu wako wanavyoendelea pia makuzi yao. Wao pia wanakukumbuka sana. Unakumbuka mara ya mwisho mwaka 2001, uliwapa zawadi Camilla ukamnunulia gauni na Erik shati na kaputula, bado wanavitunza mpaka leo. Na wanaviabudu mno.
Najua unanisikia huko uliko, sisi wote tunakukumbuka sana mama Ustarehe kwa Amani. SISI TULIKUPENDA LAKINI MWENYEZI MUNGU ANAKUPENDA ZAIDI. AMINA.

Tuesday, August 16, 2011

VYAKULA VYA ASILI NA KINYWAJI CHA ASILI (TOGWA) AMBAVYO NIMEKULA NA KUNYWA WAKATI NIPO NYUMBANI SONGEA/RUHUWIKO!!!



Siku hii nilikuwa na furaha sana kwa kupata togwa kinywaji ambacho nakipenda sana, ila nasikitika sikuwa na kisonjo au kata (deve) ila hata hivyo ilipanda...:-)


Baadaye nikasema ni lazima nile karanga za kuchemsha kwa vile mimi si mpenzi wa mtesa wala mboga za kuweka karanga. Nipendacho ni karanga za kuchemsha au ziwe mbichi na halafu kukaanga hapa utanipatia...ni kweli nikazipata...nyumbani ni nyumbani......





Nilivyokuwa na bahati ulikuwa ni msimu wa viazi vitamu (mbatambata) au wengine wanasema makapa...basi nakwambia mikate, chapati, maandazi nk nikavitupilia mbali kabisa nikawa na vyangu nilivyovizoea tangu utoto...mihogo, ndizi na magimbi pia ingawa nilipitiwa kupiga picha kwa utamu:-) TUONANE TENA WAKATI MWINGINE ....!!!!!!


Monday, August 15, 2011

KUMBE INAWEZEKAN​A EH!!!!!

MWANAMKE mkazi wa kijiji chaIkandamoyo, wilayani hapa, Veronica Saleh ‘Mama Kaela’ (50), amefanya uamuziadimu wa kuolewa na wanaume wawili ambao anaishi nao kijijini hapo.
Kijiji hicho kipo umbali wa takribani kilometa 30 kutoka mjini hapa katikaJimbo la Katavi linalowakilishwa na Waziri Mkuu Mizengo Pinda.

Pamoja na ndoa hiyo iliyowezeshwa na mume mkubwa kukubali kuishi na mume mdogo,imeelezwa kuwa mwanamke huyo ndiye ‘aliyewaoa’ wanaume hao kwa zaidi ya miakasaba sasa, huku akiwa na amri kuu katika nyumba, kama ilivyo katika ndoa zakawaida.
Wanaume hao ni Paulo Sabuni ‘Baba Kaela’ (60) ambaye ndiye mumemkubwa na Arcado Mlele (45) ambaye ni mume mdogo.

Taarifa za kuwapo kwa ndoa hiyo ya aina yake, zililifikia gazeti hili nakufanyiwa uchunguzi kwa zaidi ya wiki tatu, na hatimaye katikati ya wiki hii,wahusika walikubali wao wenyewe kuzungumzia suala hilo. Kwa mujibu wa maelezoya mwanamke huyo ambaye alionekana kuwa msemaji wa familia hiyo, yeye na mumewemkubwa, walifika kijijini hapo miaka 24 iliyopita, wakitoka kijiji cha Usumbwampakani mwa Chunya, Mbeya na Tabora.
Wakiwa kijijini hapo mume wake aliendelea kufanya kazi ya ukulima wakati yeyemama (Veronica), pamoja na kilimo hujihusisha na upishi na uuzaji wa pombe yakienyeji ya iitwayo kayoga.

Mwanamke huyo ambaye amesema ana watoto wanne, Alfred (20), binti mwenye miaka16 (ambaye ameolewa) na wengine wawili wa kiume, mmoja akisoma darasa la sitana mdogo ana miaka saba, amesema hana shida na waume wake.

Ingawa wanandoa hao walizungumza kwa hadhari, majirani walikiri kuwa mwanamkehuyo anaishi na wanaume hao wawili kwa amani na kwamba mwanamke huyo ndiye mwenyesauti na si waume zake.

“Si siri tena sasa, tumeshawazoea, kwani wanaishi kwa amani ila yule mume mdogoanaishi kwenye nyumba aliyoachiwa na marehemu baba yake, lakini anashinda kwamume mkubwa, ambapo inajulikana kijijini hapa kuwa ni nyumba kubwa. “Basi paleni mambo yote, kula na kunywa, mama huyu amewapangia zamu wanaume hao kamaafanyavyo mume mwenye wake wengi. Ama kweli ukistaajabu ya Musa utaona yaFirauni,” alisema mkazi mmoja kwa masharti ya jina lake kutoandikwa gazetini.Ilielezwa, kwamba wanaume hao wana akili timamu na hawatumii kilevi cha pombekama ilivyo kwa mke wao.
Hata hivyo, mume mkubwa anapewa sifa za upole tofauti na mume mdogo anayetajwakuwa mkorofi kiasi cha mara kadhaa kumchapa makofi mkewe anapomuudhi.

Majirani wanadai kwamba Mama Kaela na mumewe Paulo, walipofika kijijini hapo,walipokewa na kuishi maisha ya kawaida, lakini baadaye mama huyo alianza kuwana uhusiano wa kimapenzi na Arcado, ambaye naye alilazimika kuachana na mkewewa ndoa anayefahamika kijijini hapo kwa jina la Mama Pere.

Ilielezwa na mashuhuda hao kwamba mume mkubwa alipobaini uhusiano huo, alikujajuu, lakini mwanamke huyo inadaiwa alimweleza mumewe huyo, atake asitake lazimawataishi wawili, vinginevyo ataachana naye, ndipo mume mkubwa alipokubalikuishi na mume mwenza.
Katika maisha ya kawaida katika familia hiyo, inaelezwa kwamba katika baadhi yasiku ikitokea kuwa mama huyo amechoka kupika, mume mdogo huchukua jukumu lakupika na kumwandalia chakula na maji ya kuoga mume mkubwa.

“Lakini mara nyingi kwa mfano, ikiwa ni zamu ya mama huyo kulala kwa mumewemkubwa, basi humfulia nguo zake kisha anakwenda kwa mumewe mdogo nako anamfulianguo.

“Ndivyo wanavyoishi, nasi sasa tumewazoea ila yule mama ni mkali na ana sautipale kwake kwa wanaume wale ila tunaona kama ana wivu sana kwa huyu mdogoambaye naye pia ana wivu kwa mkewe huyo, labda anahofia kuwa mama huyo anawezakuongeza mwanamume mwingine,” anasema mmoja wa majirani hao.

Hakuna mazuri yasiyokuwa na machungu, japo familia hiyo inaelezwa kuwa naamani, mtoto wao mdogo nusura avuruge uhusiano wa wanandoa hao, baada yakuibuka mzozo wakati wa maandalizi ya ubatizo wake.

Kwa sababu anazojua mama, ingawa inafahamika kuwa wote ni watoto wa mumemkubwa, mke huyo katika hati za ubatizo aliandikisha ubini wa mtoto huyo kuwani Mlele (akimaanisha kuwa mtoto wa mume mdogo), lakini mume mkubwa aliwekapingamizi kanisani akidai yeye ndiye baba halali wa mtoto huyo.

Kwa mujibu wa mwanamke huyo, yeye na Arcado ni waumini wa madhehebu ya Katolikiwakati Paulo ni Mpentekoste. Madai ya mzozo wa uhalali wa `ubaba’ wa mtotohuyo, yalithibitishwa na baadhi ya wakazi wa kijiji hicho, akiwamo mwalimu wadini wa Kigango cha Kanisa Katoliki Uruira, Mashaka Abel. Walisema miaka sitailiyopita, mtoto huyo akiwa na umri wa mwaka mmoja, alifanyiwa taratibu zaubatizo, lakini ilishindikana, kutokana na wanaume hao, kila mmoja kudai ndiyebaba mzazi wa mtoto.

“Lilikuwa jambo la kustaajabisha sana, kwani familia hiyo ilifanya maandaliziyote ya sherehe ya ubatizo wa mtoto huyo, lakini siku hiyo kanisani wakati huoilikuwa ni kigango cha Katumba ambacho sasa ni Uruira, sakata lilianzia palePadri alipomwuliza mama wa mtoto huyo ubini wa mtoto naye akasema ni Mlele.

“Hapo ndipo mume mkubwa alipopinga na kudai kuwa mtoto yule si wa Arcado baliwake na yeye ndiye baba halali. Padri hakuamini, aliuliza tena na tena namajibu yakawa ni yale yale, ndipo ubatizo ukashindikana,” alisema KatekistaAbel.

Kazi ya kutafuta undani wa ndoa hiyo haikuwa rahisi kutokana na mazingira yawoga na usiri uliokusudiwa kubaki, ambapo awali mama alisema kwamba mume wakeni Paulo pekee japo siku ambayo mwandishi wa habari hizi alifika kijijini hapona baadaye nyumbani kwa wanandoa hao na kumkuta mume mdogo (Arcado akimsaidiamkewe kukoroga pombe. Awali katika utambulisho, walidai kuwa ni mtu na mdogowake na kusita kuzungumzia maisha yao ya kifamilia.
Mke wao ambaye alionekana wazi kuwa ni msemaji mkuu alifoka na kuja juu, akidaikuwa hayuko tayari kuzungumzia uhusiano wake na wanaume hao wawili, ingawaalikiri kuwa wanaishi pamoja.
"Kwa hiyo umefunga safari yote hii kutoka huko ulikotoka ili uje kwangumie Veronica … nasema sitaki kabisa mtu kuja hapa na kutaka kunivurugiampangilio wa maisha yangu, kwanza nani alikueleza hayo, wambea wakubwa haoyanawahusu nini watu hao?” alihoji.

“Mie mume wangu ni huyu Paulo basi … sasa leo umeniachia vurugu ndani ya nyumbanitapigwa na huyo mume wangu Paulo, kwani mmenishikisha ugoni?” alifoka MamaKaela. Hata hivyo, mume mkubwa alidai kuwa hatamwadhibu mkewe huyo na kwambawataendelea kuishi pamoja na mdogo wake Arcado kwa amani. Hata hivyo, akinamama wengi kijijini hapo wanalaani kitendo cha mama huyo kuishi na wanaumewawili ambapo waliomba uongozi wa Kanisa uingilie kati, ili mama huyo aweze kufungandoa na mume mmoja.
Lakini kwa upande mwingine, baadhi walimpongeza mwanamke huyo wakidai kuwakitendo hicho ni cha kijasiri kwa mwanamke, kumudu kuishi na wanaume wawili nakuwa na mamlaka juu yao.

Ndugu wa Arcado wao wanalaani kitendo cha ndugu yao kuolewa na mama huyo,wakidai kuwa walishamshauri na kumuahidi kuwa endapo ataachana na mama huyowatamwozesha mwanamke mwingine, lakini yeye Arcado, amedai kuwa yuko tayarikufa, lakini si kuachana na mama huyo, kwani ndiye ubavu wake wa maisha.

“Sasa tumebaki tunamwangalia tu huyu ndugu yetu Arcado, tumemshauri, lakinimkaidi, hatusikilizi. Basi nasi hatuna la kufanya zaidi ya kumwangalia,“alisema mmoja wa ndugu wa karibu wa Arcado. Kwa upande wake, Mwenyekiti waKijiji hicho, Florence Katobasho, alikiri kuwa mwanamke huyo anaishi kinyumbana wanaume wawili na wanaishi kwa amani kwani hajawahi kufikishiwa malalamikoyoyote kuhusu wanandoa hao.

“Ni ukweli usiopingika, kwamba Mama Kaela anaishi na wanaume hao wawili …lakini kwa kuwa sijafikishiwa malalamiko yoyote kuhusu maisha ya wanandoa hao,mimi kama kiongozi hapa sina la kufanya na siwezi kuwafukuza, kwa kweliwanaishi kwa amani, mengine ni yao,” alisema Mwenyekiti wa Kijiji.
Source: Habarileo

Sunday, August 14, 2011

Savannah Lodge!!!

New cheap and very nice. Close to Julius Nyerere International Airpor in Dar es salaam.Only 20 000TZS for a night. (about 14$)You´ll find it in Kitunda not far away from Banana in the beginning of the Kisarawe road.













JUMAPILI YA LEO:- IMANI IMEKWISHA/ KWENYE KIFO HAMNA KUJUANA, UNAMKANA HATA MUUMBA WAKO!

Nimeamka nikaona ngoja nifunguo kopo langu na kusoma barua pepe na mara nakutana na ujumbe huu kwa vile sina tabia ya kuwanyima ninyi ndugu zangu chochote nimeona niweke hapa ili wote tupate kuelimika. ujumbe wenyewe ni hivi....Karibuni.

Jamaa mmoja alikwenda msikitini na panga mkononi na kuwauliza waumini: "Nani muislamu kati yenu?"
Watu kimyaa! Akauliza tena kimyaa!! Akamfuata mmoja akamchukua akaenda nae nyumbani kwake akampa mbuzi wake amchinjie.

Kabla ya kumchuna akarudi tena msiktini na kisu chenye damu na kuwauliza tena waumin: "Ni nani muislamu?" wote kimya kwa woga.
Kwa mshangao akawauliza kwa SAUTI kubwa: "Yaani nyie mpo ndani ya msikiti halafu hamumjui Muislamu?"

......Ghafla wote huku wakitetemeka wakasema IMAMU wetu ndie muislamu.


IMAMU kusikia anatajwa akalalamika: "Jamani....jamani! yaani kuwaswalisha siku mbili tu ndo nshakuwa Mwisilamu? Muogopeni Mungu!!"

Kumbe yule jamaa lengo lake lilikuwa kuchinjiwa na kuchuniwa mbuzi wake!

JUMAPILI NJEMA KWA WOTE!!!


Saturday, August 13, 2011

NILIPOKUWA SONGEA NILIKUTANA NA CHRISTIAN SIKAPUNDWA NA JUMA NYUMAYO!!


Tulipokuwa Songea tulipata bahati ya kutembelea Mtaa wa Matarawe ambapo kuna ofisi ya Tujifunze Kanda ya kusini kama uonavyo hapa juu kwenye kibao.
Hapa ni kijana wetu Erik akiwa amekwisha tia sahihi kwenye kitabu cha wageni aliye kuwa naye ni Kaka Juma Nyumayo.

Na hapa wa kwanza ni mwenyewe mama Maisha na Mafanikio aka "Kapulya"Yasinta Ngonyani na wa pili ni Juma Nyumayo ambaye unaweza kumsoma habari zake hapa na wa tatu ni Christian Sikapundwa naye unaweza kumsoma habari zake hapa na pia ukitaka kuangalia picha nyingine ambazo zinahusiana na siku hii basi bonyeza hapa.


Thursday, August 11, 2011

NILIPOKUWA NYUMBANI SONGEA/RUHUWIKO:- NILIPATA BAHATI SIKU HII MTAANI PALIKUWA NA HARUSI YA KIISLAM!!

Hapa bibi harusi ni huyo aliyejitanda kanga yaani wa pili. Hapo tayari amekwisha funga ndoa/harusi na sasa akisindikizwa kwa mume wake. Nilivyosikia ni kwamba, bibi harusi inabidi siku ya harusi anafungia hiyo ndoa/harusi nyumbani kwake na baadaye ndio aenda kwa mume wake. Ila hapa kwa mimi inanitatanisha kidogo. Kwa sababu utawezaje kufunga ndoa bila bwana kuwa pembeni? Niliuliza lakini sikupata jibu kamili. Naamini hapa kibarazani nitasaidiwa kupata jibu.



Safari inaendelea ....na hapo kulia ndio ilipo nyumba yetu...bahati mbaya sikualikwa kwenye sherehe yenyewe :-)



Wednesday, August 10, 2011

KUNA AMBAO HAWAJUI TOFAUTI YA FEDHA NA UPENDO

Wanahitaji malezi mazuri

Kama kawaida leo ni Jumatano na ni siku ya kile kipengele cha marudio ya mada zilizopita kutoka kila upande...Leo nimepitapita na nimekutana na mada hii kutoka kwa kaka yangu Shaban Kaluse . Sijui ni wangapi mmeisoma lakini Kapulya ameona si mbaya kama tukirudia tena kwani ndiyo kuelewa zaidi. Karibuni sana....Tutaonana Jumatano ijayo-----
-------------------------------------------------------------------------------------------------
Kuna wazazi ambao pengine kwa kutofahamu hupenda kutamka maneno kama haya mbele ya watoto, ‘bila fedha dunia hii nani atakujua, ni nani atakuthamini,’ watoto waliolelewa wakiyasikia maneno au kauli kama hizi mara kwa mara ndio wale watu ambao leo hawawezi kuthamini mtu mwingine hadi mtu huyo awe na fedha. Ndio wale ambao leo wanapoona mtu ana fedha hata akiwatemea machoni hufurahi na kuona fahari, wale ambao hujipendekeza kwa watu wenye fedha ni sehemu muhimu ya maisha yao.

Hawa ndiyo wale watu ambao wanapokosa fedha huwa kama wagonjwa, ndoa zao huwa ngumu, uhusiano na wenzao huwa mgumu na kukata tamaa huwafikia haraka. Hii ni kwa sababu wazazi wao waliingiza akilini mwao imani hii ya kwamba mtu kutokuwa na fedha si lolote si chochote na kwamba mtu mwenye fedha ndiye binadamu zaidi na anastahili kunyenyekewa kwa sababu thamani yake ni kubwa.

Kuna wakati wazazi huwa wanaamini kwamba mtoto hapaswi kuambiwa hapana kwa kila anachokihitaji kama uwezo wa kumpa kitu hicho upo. Wazazi hawa humpa mtoto kila anachokitaka bila kujali kama kinamsaidia katika makuzi yake au hapana.

Tabia hii ni mbaya na ya hatari sana katika makuzi ya mtoto, kwani mtoto anayelelewa katika mazingira haya huja kuwa na wakati mgumu sana maishani kuhusiana na fedha. Bila shaka umeshawahi kusikia kuona watu ambao hawako tayari kusikia neno ‘hakuna’ hasa kuhusu fedha.
Hawa ni wale watu ambao walipokuwa watoto hawakunyimwa kitu, walipewa na wazazi kila walichohitaji. Kwa sababu hiyo wakakua wakiamini kwamba binadamu anapaswa kupata chochote kila anapokihitaji.

Hebu fikiria kuhusu mtu ambaye anaamini akilini mwake kwamba kila anachohitaji ni lazima kipatikane. Lakini siyo kuhitaji kutoka kwake mwenyewe, la hasha bali kuhitaji kutoka kwa mwingine.
Kuna watu ambao wanapokuomba kitu au fedha na ukawaambia huna, inakuwa tayari umeshajenga uadui mkubwa nao kwa sababu wao hawajui neno ‘hapana’. Wakati wanapohitaji kitu, wazazi wao waliwajaza akilini mwao dhana kwamba mtu ni lazima apate kila anachokiomba au kukitaka kutoka kwa mwingine.

Kama ni ndani ya ndoa wanawake waliopata malezi haya huwa wanasaidia sana kuzilegeza au hata kuzivunja ndoa zao. Kwa kuwa wamelelewa kwa kupewa kila walichokihitaji.
Wanapoolewa huwa hawategemei hata siku moja waume zao kuwaambia ‘sina’. Wanapoambiwa ‘sina’ na waume zao, wanatafsiri kauli hiyo kama ukosefu wa upendo. Kwani wazazi wao waliwapa kila kitu kwa sababu waliwapenda. Hivyo wao wanavyoamnini ni kwamba upendo ni sawa na kutoa kila kinachoombwa na mwingine.

Bila shaka umeshawahi kusikia jinsi baadhi ya watu wanavyolalamika wanaponyimwa kitu walichoomba kutoka kwa mwingine. Hata ukiangalia mtindo wao wa kuomba ni kama vile wanatoa amri au kulazimisha wapewe, iwe ni haki yao au siyo haki yao. Hii ni kwa saabu katika makuzi ao hawakufundishwa kutofautisha kati ya utashi na hitaji.

Ili kupunguza watu wa aina hii katika jamii inabidi wazazi wawe makini sana katika malezi ya watoto wao kuhusu fedha. Mtoto ni lazima aonyeshwe kwa upendo kwamba kuna wakati hawezi kupewa kila anachohitaji. Kuna wakati ni lazima anyimwe kwa upendo kitu anachohitaji hata kama wazazi wana uwezo wa kukipata kirahisi. Kunyimwa huku kutamfanya mtoto aingize akilini dhana kwamba katika maisha siyo lazima tupate kila kitu tunachokihitaji.

Mtoto ni lazima aonyeshwe tofauti kati ya utashi na mahitaji. Kuna mahitaji ya msingi ya binadamu ambayo ni lazima mtu ayapate. Lakini kuna tamaa ya kimwili ambayo humpelekea kutaka kila anachokiona. Ni lazima mtoto aambiwe ni kwa nini inabidi mtu afanye uchaguzi wa kupata mahitaji kwanza na baadae ndiyo afikirie kupata utashi.

Mtoto asipofundishwa kwa vitendo au hata kwa kuelekezwa kuhusu ukweli huu ndipo pale anapokuja kuwa mkubwa hushindwa kujua anunue au atafute nini kwanza na nini baadae katika mahiaji yake. Unaweza kukuta mtu ana gari la bei mbaya asana lakini mahali pa kulala ni tabu. Unaweza kukuta mtu anavaa nguo za bei mbaya sana, lakini kwake hata mahali pa kukaa hakuna. Watu kama hawa hawazuki tu, bali huzushwa na malezi haya mabaya.

Malezi mazuri ni yale ambayo mtoto hupewa au huonyeshwa upendo kukubaliwa na kuungwa mkono kwenye mambo anayoyafanya na siyo yale ya kupewa fedha badala ya mambo hayo. Fedha ikichukua nafasi ya mambo hayo mtoto anapokuja kukua atashindwa kutofautisha kati ya fedha na upendo au mapenzi.

Kama ni mtoto wa kike ndiyo wale ambao hawawezi kukaa na mume ambaye hana fedha. Hawawezi kwa sababu pasipo na fedha hakuna mapenzi au upendo kama walivyolelewa kwa kuamini hivyo.

Monday, August 8, 2011

"KAPULYA" BLOG YA MAISHA NA MAFANIKIO:- INAPENDA KUMSHUKURU MUNGU KUWA TUMESAFIRI SALAMA...MENGINE YANAKUJA BAADAYE:-) NIMIRUDIIII





Nimefika jana jioni .Hapa ni Jumamosi ya tarehe 6/8 nikiwa Silver Sand Dar Es Salaam.......Kapulya huyooooooo!!