Thursday, August 11, 2011

NILIPOKUWA NYUMBANI SONGEA/RUHUWIKO:- NILIPATA BAHATI SIKU HII MTAANI PALIKUWA NA HARUSI YA KIISLAM!!

Hapa bibi harusi ni huyo aliyejitanda kanga yaani wa pili. Hapo tayari amekwisha funga ndoa/harusi na sasa akisindikizwa kwa mume wake. Nilivyosikia ni kwamba, bibi harusi inabidi siku ya harusi anafungia hiyo ndoa/harusi nyumbani kwake na baadaye ndio aenda kwa mume wake. Ila hapa kwa mimi inanitatanisha kidogo. Kwa sababu utawezaje kufunga ndoa bila bwana kuwa pembeni? Niliuliza lakini sikupata jibu kamili. Naamini hapa kibarazani nitasaidiwa kupata jibu.



Safari inaendelea ....na hapo kulia ndio ilipo nyumba yetu...bahati mbaya sikualikwa kwenye sherehe yenyewe :-)



9 comments:

Unknown said...

swali zuri dada. Ngoja tuone wataalam watanena nini!

Raymond Mkandawile said...

Well come back dada YAsints AKA KApulya mdadisi...nilikumiss sana na sina shaka hata wadau wengine pia ilikuwa hivyo...Ni imani yangu kuwa umefarijika vya kutosha na pia kupunguza stress za Europe kwa kipindi fulani na sasa upo tayari kutupa uhondo ule tuliokuwa tunaukosa kwa takribani mwezi mzima..Karibu sana...

Anonymous said...

harusi ya mkiristo na muislamu wanaoishi kijiji kimoja nchi moja mkowa mmoja haiwezi kuwa na tofauti tofauti ni harusi ya mzungu na mmatumbi mila na tamaduni na ustarabu ni tofauti hata harusi huwa na tamaduni za ajabu nawengi wao huishi kama wanyama bila ya ndoa

Anonymous said...

yasinta ndoa ya kiislam ni kwamba inafungiwa nyumbani kwa baba wa bi harusi baada ya hapo bwana na bibi harusi wanaenda kwa mume au bwana harusi anamchukua mkewake.yaani ndo uzuri wa harusi za kiislam hazitaki magarama makubwa

emu-three said...

Ilivyo ni kuwa binti wa Kiislamu haruhusiwi kuonana na mumewe mtarajiwa mpaka ndoa ifungwe, ndio maana ndoa inafungwa nyumbani kwao, ili akitoka kwao kwenda kwa bwana harusi wake inakuwa ruhusa kama mke wa mtu.
Inakuwa hivi, muoaji, atakuwa keshakubaliana na muolewaji,...na mipango inakuwa imeshakamilika, kwa taraibi zote zijulikanazo, na siku ya ndoa bwana mtarajiwa na kikundi chake watakwenda nyumbani kwa bibi harusi, wakifika, wanakaa sehemu walipotayarishiwa,(pia inawezekana ni msikitini) na hapo yeye haruhusiwi kabisa kumuona bibi harusi mpaka ifungwe hiyo ndoa ina maana kiapo kinafanyika wakati bibi harusi akiwa ndani kwao,
Kwanza anaulizwa bwana harusi kuwa kaukabli kumuoa binti fulani kwa maharii fulani akiwa na muwakilishi wake...anaulizwa mara tatu,mbele ya mzazi wa binti, halafu shekhe anaondoka na mzazi wa binti hadi ndani alipo binti anaulizwa hivyo hivyo, akikubali `vigelegele'...na hapo bwana harusi anapewa nafasi ya kwenda ndani kukutana na bibi harusi...inakuwa halali kwake sasa kumuona.
Nafikiri wataalamu wapo wanaweza kuliweka hili sawa ki-imani na kwanini inafanyika hivyo
Ni hayo nijuayo kwa kifupi

Simon Kitururu said...

Mmmh!

Anonymous said...

mwoaji hukubaliana na mwolewaji kwa njia gani?mshenga?Marafiki? wazazi?Mume mtarajiwa huwa hajawahi kumwona mke mtarajiwa?

Anonymous said...

Maisha na mafanikio kwa mwanadamu ni kuoa na kuolewa.Hii ni sehemu muhimu sana katika maisha na kila mdau anapaswa kumuomba na kumshukuru Mungu kumfikisha kwenye mafanikio.Jambo kuu hapa si wanandoa wameunganishwaje kwenye mpango bali mioyo yao inahisi na kufahamu thamani ya mpango huu ambao mwanzilishi wake ni Mungu?
Angalizo kwa wanandoa wote:
[Ndoa na iheshimiwe kati ya wote, na kitanda cha ndoa kiwe bila unajisi, kwa maana Mungu atawahukumu waasherati na wazinzi._WAEBRANIA 13:4]
-----------------------------------
R.E.Njau
Dar es salaam.

Bi Mkora said...

Emu Three hayo uliyataja yote ni sawa ila umekosea kidogo tu kwenye mpangilio. Nao ni huu, muoaji kwanza hutafuta consent ya mzazi au walii wa muolewaji huyu ndiye msimamizi wa binti na hili suala wote wanalifanya halijalishi dini, kabila wala rangi, huwezi kukurypuka tu eti mnaoana bila ridhaa ya wazazi.

Pili taratibu hufanywa za mahari na kiislamu mahari ni ya muolewaji si ya walii wala wazazi wengine na ni haramu kwao kuila hiyo mahari naye muolewaji hupanga mahari aitakayo. Hapa stage hii ndiko consent ya muolewaji hupatikana maana ni kama husema mimi ili nikubali hii ndoa nipatiwe labda dhahabu, Quran tukufu, kiasi cha pesa, au kitu chochote kile akipendacho. Lakini hapa watu wengine huingiza mambo ya mila pia kama mkaja, kilemba, blanketi la bibi nk. Lakini kiislamu kinachotakiwa ni mahari tu ambayo hupewa muolewaji.

Siku ya ndoa, kabla ya kuulizwa bwana harusi, mfungisha ndoa huenda ndani alipo bi harusi akiwa na mashahidi pamoja na walii na kumuuliza mara 3 kama amekubali hiyo ndoa kwa kiasi cha mahari walichokubaliana, hapo anaweza kukubali au kukataa, akikubali mara zote 3 basi ndipo hutoka kwenda nje na kuendelea na ufungishaji ndoa kwa kumuuliza bwana harusi naye mara 3 maswali kama aliyoulizwa bi harusi.

Baada ya bwana kukubali mara 3 ndipo ndoa inafungwa kwa kusoma aya za Quran. Tena ikishafungwa basi bwana harusi anakwenda kumuona mke wake na anaweza kumchukua akaondoka nae, na anakuwa na haki zote za mume kwa mke na mke nae anakuwa na haki zote zinzostahili. Na anamchukuwa mkewe na kwenda naye kwake kwa ajili ya karamu ya harusi kama ana uwezo nayo huitwa Walimatul harusi. Yaweza kuwa na chakula chochote alichojaaliwa bwana harusi kutoa sadaka ikiwa ni yeye na jamaa zake wameandaa.

Kitu kingine nilitaka kusahau kisheria ni mume peke yake ndio mwenye kutakiwa kuingia kwenye chumba cha bi harusi na si kama ilivyo sasa wanaume wengine eti wanamsindikiza. Na pia wakati wa uchumba wanaruhusiwa kuonana lakini lazima kuwe na mtu wa tatu kati yao maana tunaambiwa wakiwa watu wawili wa jinsia tofauti mahala faragha basi ibilisi ni wa 3 wao. Hivyo mchumba anaruhusiwa kuonana na mwenzio lakini sio faragha. Na baada ya ndoa ili iikamilike iwe ndoa lazima tendo la ndoa lifanyike na si mambo ya kutia saini kwenye makaratasi tu. (kuna vyeti vya ndoa ya kiislamu achilia mbali vile vya serikali).

Hili la mke kubaki nyuma na kupelekwa na kinamama ni la kimila zaidi na si la kidini.

Tofauti iliyopo na ndoa nyingine ni kutochananyika kati ya wanawake na wanaume, kwani ndoa ni sehemu ya ibada na katika ibada za kiislamu wanawake na wanaume hawachanganyiki ili kuondoa fitna ya ibilisi.

Na ndoa ya kiislamu ni mkataba ambao husimamiwa na utekelezaji wa mkataba huo kwa pande zote mbili. Kukiukwa masharti ya mkataba huo kunaweza kupelekea ndoa hiyo kuvunjika. Hii ni mada nyingine kabisa siku nikipata nafasi nitawaambia ni yepi ambayo yamo ndani ya huo mkataba kidini maana wanawake wengi wa kiislamu hawalijui hili na hawajui kuwa kupika na kufua si sehemu ya mkataba wa ndoa zao!

Bi Mkora