Wednesday, February 8, 2012

Ni nani anayechangia kuvunja ndoa mke au mume?

Habari hii imenisikitisha sana na imeniuma sana nikiwa kama mwanamke. Na nimeshindwa kuvumilia kutoisambaza hebu soma mwenyewe. nimeipata hapa.

Ndugu mpendwa, nakusalimu kwa amani na upendo.

Mimi ni mmoja wa wapenzi wa blog yako, na huwa sikosi kuifungua karibu kila siku, na nikiikosa ninakuwa sina raha, na raha yangu huzidi zaidi pale ninapoona umeandika kitu , hasa kwenye visa vyako, vimekuwa kama kitu ambacho nikikikosa siwezi kuishi…umenipa limbwata la visa vyako…lol
Nimesikitika sana kuwa huna vitendea kazi au sehemu ya kujishikiza, ili uweze kutupa visa hivi ikiwezekana kia siku, maana hasa sisi tunaoishi nje, tunatamani kusoma habari za Kiswahili na hasa visa vyenye ukweli ndani yake, kama vya kwako, ambavyo ukivisoma ni sawa na mtu anayeangalia movie. Na kwanini usiweke matangazo,…mbona wenye mitandao wenine wanaweka, na utakuta mitandao yao haina mengine zaidi …sana-sana ni picha, udaku au umbeya.Mimi leo nimeamua kukuandikia jambo moja linaloninyima raha,…kama halitifaa kuliweka hewani nirudishie, na kama litafaa lipitie vyema, kama nimekosea Kiswahili nirekebishe maana tumeloea Ulaya hata lugha sasa inatupiga chenga. Kwa ujumla nimekuwa nikipitia mitandao mingi, na mingi imekuwa haielezi ukweli kuhusu mwanamke na mwanaume, hasa NDOA, Naizungumzia ndoa, kwani mimi nipo ndani ya ndoa, nana bahati ya kuishi kwetu bongo kwenye manyayaso ya hali ya juu ya ndugu na mama mkwe na pia kuja kuishi Ulaya, ambapo maisha yetu sio mabaya, tunakula ….Sasa ubaya upo wapi, najua wengi mtauliza, nakuwaza, Ubaya upo ndani ya ndoa yenyewe, ubaya upo kwenye kusikilizana, ubaya upo kwenye maisha ya mke na mume, mimi huku ni kama mfanyaakzi wa nyumbani, ninaweza kusema mimi ni mmoja wa wahanga wa ndoa,ingawaje nipo dunia ya sasa, ninaishi Ulaya na mume wangu, lakini maisha ninayoishi na mume wangu ni kama tupo ile dunia ya mababu zetu ambayo mke hana usemi. Mke ni kama bidhaa, yote nimevumilia sikujali kuwa nipo Ulaya, na kama ningeliamua kufanya lolote ningeliweza, lakini bado naiheshimu ndoa yangu. Mimi hapa nipo kama mshumaa tu, siku yoyote unaweza ukazima, na ni bora niyasema haya ili watu wajifunze na waysikie, mwanga wa mshumaa huu usiishie kwangu tu, uwamulikie na wengine wanaoteseka kama mimi.
Najua wengi mtanilaumu kuwa natoa siri yangu ya ndoa, lakini nimeona ni heri kufanya hivyo, ili iwe chachu kwa wale wanaume wengine wenye tabia kama hizi waweze kubadilika, ila kwa mume wanu imeshindikana, imekuwa kama mbuzi kupigiwa gitaa. Hapa nilipo umri umeshapevuka, siwezi kusema niachane naye, nikatafute mume mwingine, nani atanioa mimi wakati sura imeshachujuka. Sitaweza kuwatelekeza watoto wangu kwa kuabdili wanaume, hapana, ila nahitaji mawazo yenu, ….Kwanini naandika haya : Nimeamua kuyaaandika kwasababu kuna mtu aliuliza swali, je kati ya wanandoa wawili mke na mume ni nani anayechania kuvunja ndoa. Ndio sisi wanawake tunakuwa na kitu kinachoitwa kitchen party, je inatusaidiaje kudumisha ndoa zetu, huyu mtu aliuliza hivyo, nikashindwa kumuelewa kwani ndoa ni watu wawili, kama mke atajitahidi sana na mume bado haelewi hiyo ndoa, au hayo mafunzo ya kitchen party yatasaidia nini.
Nimefikiri sana, na kufanyia utafiti ukianzia kwangu mwenyewe na kugundua kuwa kati ya mwanaume na mwanamke anayechangia kwa kiasi kikubwa kubomoa ndoa,ni mwanaume ila nchi za kwetu,hasa nchi za dunia ya tatu(maskini,afrika)wanamwangalia mwanamke kama ndiye chanzo cha kuvunjika ndoa, hasa wakisema, eti wanawake wengi haweze kumtuliza mume, hawajitahidi kumshawishi mume atulie nyumbani na ndio maana wanatafuta nyumba ndogo n.k swali hapa ina maana mke pekee ndiye anatakiwa kufanya jitihada hizo?
Hebu tuziangalie jitihada za mwanamke hasa wa Kiafrika, na tujiulize mwanamume anataka jitihadi gani zaidi ya hizo, kwani,mwanamke wa kiafrika,anamoyo ule wa kuvumilia,maudhi pamoja na manyanyaso ya kila aina,anayofanyiwa na mume wk.Mfano,kupigwa, kuishi na mwanamume mlevi, kumvumilia mwanamume hata akichelewa kazini kwa visingizio mbali mbali,kuletewa watoto wa nje,au hata kuletewa nyumba ndogo au vimada nk.Lakini yote hayo,anayabeba ndani ya moyo wake,na anaona kuwa ni aibu ya ukoo,yeye kurudi kwao,kwa kisa,ameshindwa kuvumilia ndoa.Wanawake wengine,hadi wanapata vilema vya maisha,kwenye ndoa zao na bado wapo kwenye ndoa wanavumilia na kuendelea na maisha kama kawaida.Wengine,wanawafumania waume zao,lakini,wanabakia na siri na kuwatetea waume wao,kuwa hakufanya jambo lolote baya na vitu kama hivyo, je uvu,milivu gani kama huo, upendo gani kama huo, uvuto upi mnaoutaka, kucheza sebene peke yake.Hebu chukulia upande wa pili kwa mwanaume mfano mwanaume,akufumanie,itakuwaje, wewe uchelewe kurudi nyumbani itakuwaje, ….ukosee kufanya jambo fulani, na mengine mengi, mwanamke atakiona cha mtema kuni.
Kwa ujumla Ndoa,inaumiza sana kwa wanawake.Na vidonda vya ndoa au majeraha ya ndoa,ni mengi sana kwa mwanamke na hayaponyeki, kwani kila siku yanatoneshwa…Kwa ujumla mwanamke wa Kiafrika anastahili kupewa heko, na hili nimejifunza nilipokuja kuishi huku Ulaya. Huku Ulaya mwanamke ana haki zake, hayanyanyaswi ovyo,na ole wako mwanamume umnyanyase mkeo halafu alifikishe hilo swala kwenye vyombo vya sheria….sio kwamba nawasifia kwa hili, lakini kwa kiasi kikubwa limemkomboa mwanamke na kujiona kumbe na yeye ni kimumbe kama mwanaume.Mimi nimeishi maisha hayo ya taabu hata vile nipo Ulaya, nimekuwa nikiishi na mume wanu na kumfanyaia yote kama vile nipo nyumbani, lakini ….nasema lakini ni ule usemi usemao penye miti mingi hakuna wajenzi…imefikia mume wangu hawajabiki kwenye swala muhimu la ndoa yake, swala ambalo wengi wanatulaumu kuwa sisi sio wabunifu, hatujui mapenzi, lakini utajuaje kucheza mpira kama hujaingia uwanjani…hayo ni visingizio vyao na kusema ukweli kama hilo wao ndio wakulaumiwa, kwani walitakiwa kushirikiana na mkewe wakafundishana na kuelekezana sio kukimbilia vimada.
Uvumilivu una mwisho wake, na majeraha yakizidi sana mwisho wake yanaweza kugeuka kuwa kansa, ndio maana nimeandika hilo swala kwako, uliweke hadharani watu walijadili na wanaume wasema ukweli wao, ili sisi wanawake tujue ni nini hasa waanume wanakihitaji kutoka kwetu, ili tuwatimizie,… ili tukiwafanyia hivyo waweze kutulia majumbani kwao, ili mwisho wa siku ndoa ziwe na amani.Humutaamini kuwa wengine tunamaliza miezi zaidi ya mitatu hatuwajui waume zetu, waume zetu huku Ulaya wanasingizia kuwa wanachoka kwenye kubeba maboksi, je ni kweli hili au ni kisngizio cha mume wangu tu, au na wenzangu wanafanyiwa hivyo hivyo, …je huko wanaposhinda na hata kulala na machangudoa hawachoki, au wanatufanya sisi ni wajinga tu hatjui nini wanachokifanya, je hii ni ndoa kweli, je na sisi tukiamua kutoka nje ya ndoa waatsemaje, na kwa hilo ni nani atalaumiwa, lakini tunaogopa kuja kuwaacha watoto wetu mayatima kwa kuugua magonjwa mabaya.Samahani sana kama nitakuwa nimewakwaza wengine kwa hayo niliyoyaongea lakini kama ilivyo kawaida ukweli huuma, …
Mimi mwenye majeraha ya ndoa Mama Wawili.

12 comments:

sam mbogo said...

Naomba ,nianza kumpa pole.mdada huyo. natamani kama ningekuwa karibu naye nimsaidie kima wazo/kitaalam.ila muhimu nikwamba yeye ndiyo mwenye uamuzi kutokana na maelezo yake,afanye kile nafsi yake ina mtuma,sisi tutatoa maoni lakini yeye ndo mhusika mkuu na ndiye anaye sikia mateso haya na manyanyaso haya. chukua uamuzi mgumu na baadaye utaufurahiya. pia kwapande wa mume sivyema kuifikisha ndoa yako hapo kama kweli una ona mkeo ni mzigo kwako mwambie ukweli kama humuhitaji,lakini kumbuka mna watoto, mnaweza tatua swala lenu kwa faida ya watoto. pia angalia na mzingira mnayo ishi,ulaya.jaribu kuwa muwazi na mkeo kuna mambo mengine ya kiulaya nimazuri kuyafuata,mfano kutokumnyanyasa mkeo, watoto na hakizao.mwisho wa yote ikishindikana tafuteni sheria zinasemaje ili kuwasaidia. kaka s

emuthree said...

Mimi kuna mahali niliuliza swali, kwanini mtu akitaka kuwa dakitari au mwalimu au mwanasheria au mtaalamu au mjuzi wa jambo lolote, anakwenda shule, au anajifunza kwanza.
Cha ajabu na nashangaa hata wahusika ambao wanafungisha hizi ndoa hawaliulizi hili , kuwa je hawa watu wanaoingia kwenye ndoa, wanaijua ndoa vyema, wanajua maisha ya mume na mke...
Hata kama mumeoana na hamkubahatika kuisoma ndoa, kwani zipo njia nyingi za kuisoma ndoa, hata kuuliza, kwa wazee, wanataaluma, au wakuu wa dini, basi siku hizi kuna mitandao, kuna vitabu, kwanini mtu hujifunzi.
Nazungumza hivi kwasababu wanadoa wengi wamekuwa wakiingia kwenye matatizo ya ndoa zao na ukichunguza utakuta ni kitu kidogo tu, ambacho wangekaa na kusikilizana kingetatuliwa, na hili ni kwasababu ndoa imechukuliwa kama `mapokeo' mambo mengine yatajileta yenyewe.
Mambo kama haya yanajirudia rudia na kweli yapo sana, lakini mimi sikujua kuwa hata huko Ulaya mambo haya yapo , basi ipo kazi.
Mlengwa asichoke, ikibidi awahusishe watu wa dini watatoa neno ambalo linaweza kuwasaidia, lakini muhimu ni wao wawili kusikilizana.
Dada Yasinta, tupo pamoja, nashukuru kwa kuitangaza hii mada ni muhimu sana.

Rachel Siwa said...

Ahsante sana da'Yasinta kwakuleta hili swala hapa,mimi nimeshatoa maoni yangu kule,lakini kwa kuongezea,Waume wabadilike huu si wakati wa kunyanyasana,pia Wanaweke tuwe makini sana na hawa wanaume wanaweza kutugombanisha na kila mtu kwa tabia zake mbaya,nafikiri pia tuwavae hawa wanaume kwanini kila leo unaniaibisha kwa kuchukua wanawake wengine?kwani wanawake tunapenda sana kuwafichia tabia hizi mbaya za wanaume na kugombana na wanawake wengine kwanini unamchukua mume wangu,oohh yule na yule hahisi wananichukulia,kabla hatujagombana tuwaambie hivi wewe mwanaume unatatizo gani mpk unafikia kujitembeza,kutojiheshimu,kufunguafungua hiyo zipu yako?AGGHHHHH na kunidhalilisha mie pia kuniambukiza magonjwa.Labda atakuwa na sababu ya msingi kama ni mimi ndiyo sababu basi nijirekebishe. Duuhhh nitamaliza ukurasa huu,Ahsante kaka Sam mwana wa Mbogo kwa maoni yako.

Yasinta Ngonyani said...

Nakubaliana na waliotangulia NDOA wengi wanafikiri ndoa ni ile kupeana pete na kukubali ndio. Lakini ile ya kusikilizana yaani kukaa chini na kumsikiliza mwenzako mwisho wa siku ni MUHIMU SANA kwani ndoa bila mawasiliano si ndoa. Tusemapo UVUMILIVU.katika ndoa ina mipaka yake kwani mtu anaweza akavumilia na mwisho utachoka na itabidi upaze sauti. Wanawake wengi tunakubali kuteseka kwa sababu ya watoto. Kwa sababu katika ndoa mkishapata watoto na inatokea hali kama hii hakuna mtu anayeteseka zaidi ya watoto. Watoto wanakuwa na hali mbaya sana na hata kama wanakwenda shule matokeo yao ya shule hayatakuwa mazuri. Kwa hiyo hapa anayeumia ni mama na watoto lakini nakuomba wewe mama wawili jaribu kufikiria ni uamuzi gani wewe ungeuchukua uwe mgumu au mwepesi ili mradi kuwa salama. Ningejua ni nchi ipi unaishi .... Mwenyezi Mungu na akupe Nguvu dadangu

ray njau said...

KIELELEZO KWA WAKE
10 Familia ni kama shirika, na ili lifanye kazi vizuri, linahitaji kuwa na kichwa. Hata Yesu anajitiisha kwa Yule aliye Kichwa chake. “Kichwa cha Kristo ni Mungu” kama vile “kichwa cha mwanamke ni mwanamume.” (1 Wakorintho 11:3) Kujitiisha kwa Yesu chini ya ukichwa wa Mungu ni mfano mzuri kwa kuwa sote tuna kichwa ambaye tunapaswa kujitiisha kwake.

11 Wanaume wasio wakamilifu hufanya makosa na mara nyingi wao hupungukiwa katika jukumu lao la kuwa vichwa vya familia. Kwa hiyo, mke anapaswa kufanya nini? Hapaswi kudharau mambo ambayo mume wake anafanya au kujaribu kumnyang’anya ukichwa. Mke anapaswa kukumbuka kwamba roho ya utulivu na upole ina thamani kubwa machoni pa Mungu. (1 Petro 3:4) Akiwa na roho hiyo, itakuwa rahisi kwake kuonyesha utii wa kimungu hata katika hali ngumu. Isitoshe, Biblia inasema: “Mke anapaswa kumheshimu sana mume wake.” (Waefeso 5:33) Lakini vipi akikataa kujitiisha chini ya Kristo akiwa Kichwa chake? Biblia inawasihi wake hivi: “Jitiisheni kwa waume zenu wenyewe, ili, ikiwa wowote si watiifu kwa lile neno, wavutwe bila neno kupitia mwenendo wa wake zao, kwa sababu wamekwisha kushuhudia kwa macho mwenendo wenu ulio safi kiadili pamoja na heshima kubwa.”—1 Petro 3:1, 2.

Sara aliwawekea wake mfano gani mzuri?

12 Mume awe ni mwamini au la, mke hatakuwa akimvunjia heshima ikiwa ataeleza maoni yake kwa njia ya busara hata kama yanatofautiana na ya mume. Huenda maoni yake yakawa sawa, na yanaweza kufaidi familia nzima ikiwa mume atamsikiliza. Ingawa Abrahamu hakukubaliana na mke wake Sara alipopendekeza jinsi ya kutatua tatizo fulani la familia, Mungu alimwambia: “Sikiliza sauti yake.” (Mwanzo 21:9-12) Bila shaka, mume anapofanya uamuzi ambao haupingani na sheria ya Mungu, mke wake anapaswa kuonyesha anajitiisha kwake kwa kuunga mkono uamuzi huo.—Matendo 5:29; Waefeso 5:24.

13 Mke anaweza kutimiza jukumu lake kwa kutunza familia. Kwa mfano, Biblia inaonyesha kwamba wanawake ambao wameolewa wanapaswa ‘kuwapenda waume zao, kuwapenda watoto wao, kuwa na utimamu wa akili, safi kiadili, wafanyakazi nyumbani, wema, wakijitiisha kwa waume zao wenyewe.’ (Tito 2:4, 5) Mke ambaye pia ni mama anayefanya hivyo, atapendwa na kuheshimiwa daima na familia yake. (Methali 31:10, 28) Lakini kwa kuwa ndoa ni muungano wa watu wasio wakamilifu, huenda hali fulani wasizoweza kuvumilia zikawafanya watengane au kutalikiana. Biblia inaruhusu kutengana hali fulani zinapotokea. Hata hivyo, kutengana hakupaswi kuchukuliwa kivivi hivi tu, kwa kuwa Biblia inashauri: “Mke hapaswi kuondoka kwa mume wake; . . . na mume hapaswi kumwacha mke wake.” (1 Wakorintho 7:10, 11) Msingi pekee wa Kimaandiko wa talaka ni uasherati.—Mathayo 19:9.

Interestedtips said...

Pole sana dada, wengine bado tu wachanga ktk mstakabali huu wa haya maisha, ngoja nisome comments ili niweze kupanuka zaidi kimawazo, kiakili, kibusara na kihekima

Mija Shija Sayi said...

Maisha huwa hayatabiriki, mkorofi huweza kuwa yeyote tu au wote pia mama au baba. Nilichojifunza katika utafiti wangu mdogo ni kwamba, sehemu yoyote inayounda umoja Shetani haipendi kabisa na atafanya juu chini kuwavuruga au kupavuruga, kama huamini jaribu kuangalia jumuiya mbalimbali, ndoa, muungano wa nchi n.k yaani utakuta ni migogoro mitupu inatawala ambayo yote husababishwa na selfshness hakuna mtu anataka kumsikiliza mwenzie, huu ni udhaifu mkubwa kwa binadamu ambao Shetani anautumia sana kutuvuruga.

Bahati mbaya sana hakuna awzaye kumshinda muheshimiwa Shetani isipokuwa kwa njia ya maombi peke yake.

Maombi ni muhimu sana katika ndoa au muungano wowote. Piga maombi kisawasawa halafu ndo apply ideology zako basi hapo utashangaa mwenyewe.. CHEZEA MAOMBI.

Lucie Mangaza said...

pole sana Mungu atakusaidiya katika matatizo yako

Penina Simon said...

Yes wengi tumepitia maisha hayo lkn utashangaa bado tunagangamala kwenye ndoa ili kulinda watoto.
ingawa tunabeba misalaba mizito lkn hatuna jinsi.

Unknown said...

Hodi jamani!!

Nilipita tu kusalimia japo nimekuta kuna mjadala, hata hivyo kutokana na haraka za kuwahi usafiri nikaona si vyema kutoacha unyayo.

Anonymous said...

kiukweli imenigusa hit Mimi ninamtihani hunaofanana na WK inauma sana cos ni watoto

Anonymous said...

Nilikuwa natafuta kujua nani husababisha ndoa kuvunjika nikakutana na ujumbe wa huyu dada, mimi ni mhanga mkubwa, ninandoa ya kikatoliki nimeoa msabato, kazi yangu inakipato si kibaya sana na mke wangu ni mwalimu, tulikuwa na maisha ya kawaida kabisa lakini kwa Baraka za Baba yangu kutoka kwa Mungu nimebarikiwa kuwa na nyumba tumejenga wote japo mke wangu alichangia sehemu ndogo, nina gari na watoto wetu wanasoma shule jirani ya Kulipia. mke wangu hanipikii chakula, wanapika wadada wa kazi wapo wawili, mke wangu hanipokei nitokapo kazini napokewa na watoto ama wadada wa kazi, mke wangu hawezi kuninyooshea suruwali, mke wangu hawezi kunisugua mgongoni hata nikimuomba kunisaidia, mke wangu hata kupanda maua nyumbani hawezi, mke wangu hata kushughulikia kuku hawezi, mke wangu humpatia pesa 1m ya vikoba kila mwezi, mke wangu hanipikii chakula ninacho kipenda (Ftari ya mihogo, viazi, maboga na karanga) lkn alianzisha vurugu akitaka nimnunulie gari kesi ikafika kwao nilimuita baba mkwe lakini alionekana kumtetea mwanae, nilimwambia akachague gari analotaka akachagua E-Xtrail Nissani, nilimsihi achague Alex ana RUNX akakata.

sasa limeibuka kubwa zaidi nipo namuuguza mama yangu mzazi nimeamua niwapeleke watoto shuleni asubuhi kwa mguu ili kufanya mazoezi kwakuwa uzito wao ni mkubwa hataki anataka tuwapeleke watoto kwa gari lakini umbari ni wa kutembea dk 14 yaani kwenda na kurudi ni dk 28-30.

kwa sasa kesi ipo kwa mchungaji lakini mbele ya mchungaji alipopewa nafasi ya kuomba akamuomba Mungu Kumuondoa duniani kwakuwa nimekataa kupeleka watoto shuleni kwa gari. kila siku akisali ndiyo ombi lake kuu, kei imefika kazini kwake, kwa baba yake, na sasa kwa babu na wajomba zake lakini msimamo wake upo palepale.

Nachotaka kusema hakuna mwenza maalumu wa kuharibu ndoa bali aweza kuwa mwanaume ama mwanamke.

sala zenu. leo nimeitwa na mchungaji nikasikilize baada ya yeye kuongea naye.

Sala zaweza kuwa suruhisho,

watoto wanapenda kutembea kwa miguu.