Sunday, July 5, 2009

SALA YA MKE KUMWOMBEA MUMEWE

Nimeona si vibaya kama tukirudia hii sala tena na tena

Ee Bwana , ni ajabu,
Jinsi fikra zangu zinavyomrudia kila mara
Huyu, mume wangu,
Mwenzi anayeshiriki maisha yangu kwa namna ya pekee.
Ninapofagia nyumba na mazingira yake,
Nataka kutengeneza nyumba nzuri kwa ajili yake.
Ninapopika chakula vizuri,Napenda kumfurahisha.
Ninaponunua nguo mpya na kujaribu kuonekana mrembo,
Ni kwa ajili yake tena, Ee Bwana.

Na ninaweza kukuambia kwamba
Ninamwonea fahari,
Anafanya kazi kwa bidii ili kupata riziki yetu;
Ni mtu mwenye haki, mwadilifu,
Naye hujitahidi kutufurahisha.
Kwangu, yeye ni mpole na mwangalifu.
Hunijali na kuonyesha kweli kwamba anajali.
Hunifanya mimi nijiamini mwenyewe,
Anajua jinsi ya kuondoa hofu zangu,
Hunipatia usalama na upendo ambao nahitaji sana.

Ee Bwana, ninakuomba,
Umbariki na umlinde.
Katika safari zake, umfikishe salama.
Kazini mwake, umpe fanaka
Na hapa, nyumbani petu naomba apate amani na heri.

Bwana, unisaidie mimi pia
Niweze kuwa yule mke anayehitaji.
Unifanye niwe mtu anayeweza kumwamini daima,
Mwanamke ambaye anaweza kumfurahia,
Niweze kumsaidia asahau matatizo yake,
Niweze kuondolea mbali hofu zake na kupunguza uchungu wake.

Bwana, Wewe ndiwe uliyenipa mume huyu,
Na katika yeye,Umenipatia sehemu ya nafsi yako mwenyewe.
Ninakusifu kwa ajili yake, Ee Bwana.

Napenda kuwatakieni wote Jumapili Njema.

11 comments:

Fadhy Mtanga said...

Ahsante sana.
Nakumbuka mwaka jana kwenye mwezi Novemba kama sikosei, ulipoitoa hii sala. Ni sala nzuri sana. Si kwa mwanamke tu kumwombea mumewe, bali pia kwa mwanaume kwa mkewe. Vivyo hivyo iwe watoto kwa wazazi wao, wazazi nao kwa watoto. Iende hata kuwaombea marafiki zetu. Zaidi maadui wetu na wale wote wanaotuudhi.
Ubarikiwe kwa kutukumbusha.
Ni hayo tu!

Simon Kitururu said...

Sijui kwanini miye sio mme wako kama maswala yenyewe mpaka unayasalia!:-(

Mzee wa Changamoto said...

Nimemwamsha mke wangu kumkaririsha hii sala. Naamini atakuwa akiniombea kila wakati. Hivi utaweka ya mume kumuombea mkewe? Lol
Asante tena na tena na Jumapili njema

www.tanzaniasports.com said...

Wee dada, mkali kila kitu ni sala.....Naungana na Kitururu..inaelekea umebarikiwa kuliko wanawake wote...sala..sala..sala...amina

Nicky Mwangoka said...

Ni sala nzuri kweli. Kweli hapa kina mama washindwe wenyewe kuwaombea waume zao. NI baraka tele.Asante kwa mwelekezo kwani nasi wanaume tunapaswa kuwaombea wanawake ambao ni nguvu muhimu sna kwenye maisha.
Ni muhimu kujenga moyo wa sala.

chib said...

Nimemtumia mke wangu sala hii

kamala Lutatinisibwa Lutabasibwa said...

sitaki mke wangu aniombee sala hii wala nini kwa sababu ni ya Yasinta kwa mumewe na sio mke wangu kwangu

kama mke wangu anaona umuhimu basi anitungie ya kwake na sio kopy n pest inayoharibu maendeleo ya waafrika wengi. AMINA

Yasinta Ngonyani said...

Asanten wooote kwa maoni yenu naona wengi wanataka na sala ya mke kumwombe mkewe sawa subirini.

Na Kamala nimesema sala ya mke kuwombea mumewe. Nina maana mwanamake yeyote yule sio mimi tu kumwombea mume wangu.

Mzee wa Changamoto said...

Hahahahaaaaaaaaaaaaaaa Kamala. Kweli kumekucha

Mija Shija Sayi said...

Yasinta wewe mwisho..duh, asante kwa sala nzuri, hivi hapo sasa unamjibuje Kitururu?

Anonymous said...

Ubarikiwe sana.