Tuesday, July 14, 2009

KUMBUKUMBU+MAISHA

Nakumbuka ilikuwa mwaka 1983 nilikuwa naishi Lundo (Nyasa) wakati huo. Siku moja mchana nilikuwa naosha vyombo. Nilikuwa nasugua sufuria na vyungu hii ilikuwa kazi yangu. Kama mjuavyo Nyasa ni kula samaki sana. Kuna mtu alitupa miiba ya samaki ovyo na kwa mimi kutojua ni sehemu ile ile niliyokuwa nikiosha vyombo. Kwa bahati mbaya nilipiga magoti bila kujua napiga magoti kwenye miiba. Mmh kazi kwelikweli.

Baada ya siku goti lilianza kuvimba, nilichofanya tangu siku ile ya kwanza sikumwambia mtu nini kimenipata. Sababu kubwa ni kwamba ningeambiwa nibaki nyumbani. Sio kwenda shule ni mgonjwa. Na goti lilizidi kuvimba, lakini nilijikakamua na kuvumilia na maumivu yote. Kisa nilikuwa sitaki kubaki nyumbani bila kuhudhuria masomo.

Lakini siku moja wakati nipo shule nilikosa raha sana kwa maumivu. Rafiki yngu mmoja aitwae Claire Mputa aliona goti langu limevimba sana. Akanishauri niende hospitali naye atanisindikiza. Hata hivyo nilikataa kisa ni kile kile kuogopa kukosa masomo yatanipita. Lakini Claire aliweza kunishauri.

Ilichukua muda mrefu kufika hospitali kwani sasa goti lilikuwa limevimba mno na nilikuwa nachechemea na pia lilikuwa linauma sana, kwani kidonda kilianza kutunga usaa (infection). Kwa hiyo tulikuwa tunatembea polepole sana. Na hapo hatukuwa sisi tu kulikuwa na wanafunzi wengine pia waliokuwa wagonjwa wao walitangulia . Baada ya muda, yaani tulikuwa tunakaribia kufika hospitali tukawakuta wale wanafunzi wenzetu waliotangulia wamechepuka maporini ambako kulikuwa na miembe mingi iliyoshonana. Claire akaniambia; Yasinta twende tukaangalie wanafanya nini? Basi tukaenda kuangalia wote mie na Claire, tulipofika, tukawakuta wanafanya ule mchezo unaofanywa na wanandoa (ngono). Tulishangaa sana na kuondoka, kumbe wao walikuwa si wagonjwa walitaka tu kukwepa masomo na kwenda kufanya ule uchafu. Yaani ilikuwa kinyume kabisa na mimi, na sikutarajia kama wanafunzi kwa umri ule tuliokuwa nao wangeweza kufanya yale tuliowakuta wakiyafanya.

Haya, tulipofika hospital kama kawaida kukaa foleni. Mara ikaja zamu yangu Claire Mputa akanishika mkono na kunisindikiza ndani ya chumba ambacho kilikuwa maalum kwa mambo ya vidonda. Nakumbuka yule daktari alikuwa mzee kidogo, aliitwa Kataulaki. Alinitisha alipochukua mkisu mkubwa nilifikiri anataka kuukata mguu wangu. Lakini hakufanya hivyo alinitibu na mimi na Claire Mputa tukarudi tena shuleni.

Kikubwa ninachotaka kusema hapa ni kwamba kama Claire asingenishauri kwenda hospitali basi leo hii nisingekuwa na mguu wa kushoto. Na pia nisingeyaona yale nilioyaona kule miembeni, kwani yalinifunza kwa kiasi fulani. Napenda kuchukuwa nafasi hii kuwashukuru rafiki yangu Claire Mputa na pia yule Daktari Kataulaki
Napenda kuwaambia ahsanteni sana.

13 comments:

Anonymous said...

Du hapo walikosekana wavulana wawili! wangekuwepo hadithi ingekuwa nyingine

Albert Kissima said...

Dada Yasinta pole sana na pia nampa hongera rafiki yako huyo kwa kukupa wazo la kwenda hospitali.

Nami si vibaya nikiweka kisa changu hapa kilichonitokea nikiwa ktk shule moja huko Arusha nikiwa kidato cha sita.

Ilikuwa ni wakati wa likizo, mimi na baadhi ya wanafunzi wengine tuliamua kubaki kwa ajili ya kujisomea.

Siku moja mida ya saa nne asubuhi nilitoka bwenini na kujisogeza toilet kwa ajili ya mambo fulani.Basi nilitafuta ndoo kwa ajili ya kuingia toilet lkn sikupata(maisha ya shule haya) basi nikaishia kwenye haja ndogo. Wakati nipo nje nanawa mikono ktk sinki, nilitazama juu kwenye mti mkubwa uliokuwa kwenye kilima, si mbali na kile choo.Mti huu ulikuwa umeanza kukauka.Wakati nauangalia huku naendelea kunawa mikono, nilijiuliza kimoyomoyo, hivi siku huu mti ukianguka, aliyeko ndani ya hiki choo atapona kweli? Amini usiamini, nilipomaliza tu kujiuliza huku nautazama ule mti, niliuona unaanza kuja(hapa nilikimbia kwa kasi ya ajabu) na uliangukia kile choo na kukivunjavunja kabisa.Mpaka leo najiuliza ningepata ile ndoo, da! Ingalikuwa hadithi nyingine.


Katika shule hiyo nilishuhudia msichana aliyekuwa anatembelea mashule tofauti akitoa ushuhuda wa kukaa kuzimu miaka tisa akimtumikia shetani( hili mpaka leo siliamini) na pia nilishuhudia kijana mmoja niliekuwa naishi naye chumba kimoja akiongea mambo mengi kuanzia saa nane usiku hadi saa kumi na mbili asubuhi.(kwa mujibu wake ni kwamba maneno hayo alikuwa akiyatamka kwa kuongozwa na roho wa Mungu)

Fadhy Mtanga said...

Da Yasinta tujibie swali, ni kweli pangekuwapo vijana wengine wawili hadithi ingekuwa nyingine?

Lakini pole sana kwa usumbufu wa mguu wako. Tunashukuru uliunusuru. Pia ashukuriwe rafikiyo wa dhati kwa kuangalia mbali.

Bennet said...

Mi nilifikiri chini ya mwembe wameenda kuokota maembe kumbe wana mambo yao, hili nalo naona ni somo pia

kamala Lutatinisibwa Lutabasibwa said...

unamaanisha wale jama walifanya uchafu? mboona mimi sioni hata harufu ya uchafu? unauhakikagani kuwa mioyoni mwao hawakuwa wanandoa? mpaka pete?

utakuwa ulichomwa na samaki aliyeumwa na nyoka. vipi km ile mifupa ingechoma sehem nyet?

ni hayo tu

chib said...

Kama upo mzima kwa sasa ndio furaha ya wote, ila Kissima, mbona hujasema ulipotoka mita chooni kama taulo au chochote ulichokuwa nacho kiliponyoka au la!! :-)

Koero Mkundi said...

Kwanza dada pole sana kwa yaliyokupata, mimi naamini lililokupata, ilibidi litokee ili ujifunze jambo na kweli umejifunza maana kama usingeyaona hayo uliyoyaona pale miembeni usingejua raha na karaha zake……

Naona midume humu imeshupalia kusema kuwa, kulikosekama wanaume wawili, ili iweje? Au mnazungumzia kubaka? Hivi haiwezekani kuwa hata hao waliopelekwa miembeni walibakwa?

Kwa mazingira ya vijijini naamini hilo linawezekana maana wasichana wengi huko vijijini huingizwa katika mitego ya kuonjwa na wanaume wakware wangali wadogo huku mila zikilinda huo uchafu..

Kamala, huo mchezo ni mchafu kwa sababu haukufanywa kwa kufuata taratibu zinazotakiwa iwe ni kimila au kidini, kila jambo lina taratibu zake kwani hata wanyama wana taratibu, sasa iweje sisi wanaadamu tushindwe kufuata taratibu?
Je sisi na wanyama ni nani mwenye akili zaidi ya mwingine?

Tusishabikie ujinga, wote tunatakiwa kukemea…….ebo!!!!!!!!!!!

Simon Kitururu said...

Duh!

PASSION4FASHION.TZ said...

Pole sana Yasinta, hadithi yako ni nzuri sana imenikumbusha mambo mengi ya utotoni,unapokuwa na rafiki mzuri atakushauri mazuri,hakika ni rafiki hutakaa umsahau maishani mwako.

kamala Lutatinisibwa Lutabasibwa said...

koero siku hizi unaishi kijijini nini? du naona kama vile umetumwa!! kuna aliyajribu kukub......a......kaaaaa nini? bibi yako hajambo?

usituite midume. una uke kwa ajili ya wanaume bwana, ebo!!!!

uliwahi kuona watu wanabakwa kimya kimya au ukiwakaribia unasikia wanalia kwa furaha? kwani wanaume hawabakwi, koero bwana!!!

Fadhy Mtanga said...

Yee mweeh! Da Koero mijidume siye wala hatushabikii ujinga. Tunasema ukweli.
Sidhani kama tubinti tule tulibakwa. Naami tulikwenda with consent. Mazingira yenye yanaonesha waliridhiana that's why waliondoka shule wakisingizia waenda hospitali.
Tuliosoma shule za vidumu na ufagio tumeyaona mambo kama hayo. Watoto wa kike wanaanza kusosomolewa kitambo wangali wadogo, tena kwa ridhaa yao.
Usinikabe koo dadaangu, nisamehe kwa kusema ukweli.

Yasinta Ngonyani said...

Ahsanteni wote kwa maoni yenu nimefurahi sana na pia nimecheka sana nawapenda wote. Na nitajibu swali lenu Kwa tabia yangu niliyo nayo nasema HAPANA. Yaani kama kungekuwa na wavulana wawili sisi hatungethubutu kabisa kufanya hivyo. Kwani katika vichwa vyetu tulikuwa tunawaza tu masomo.

chib said...

Naona baraza lilikuwa moto kwa ishu hii :-0
Siju watu watasemaje kwa masuala ya ushoga, maana wanyama wanaweza kuwa bora hapo kuliko bin Adam