Monday, March 22, 2010

Aliyedaiwa kufa na kuzikwa aibuka hai!!!

MKAZI wa mjini Mafinga ambaye alidaiwa kufa na kuzikwa mwezi Oktoba mwaka jana, amerejea kwao akiwa hai na kusema"sikumbuki kama niliwahi kufa".
Kijana huyo, Nickson Kabonge, 23, aliwasili nyumbani kwao juzi mchana akitokea msitu wa Kihanga ulio Mafinga ambako amedai alikuwa akifanya shughuli za kupakia mbao na magogo kwenye magari.
Wakati familia yake, na hasa baba ikiamini kuwa alishafariki na ilishiriki kumzika, kijana huyo aliiambia Mwananchi kuwa aliamua kurejea kwao baada ya kuota kila mara kuwa baba yake amefariki.
Kurejea kwa kijana huyo kulizua yaharuki kwa wakazi wa mjini hapa ambao walifurika nyumbani kwao kumshangaa, wakionekana kutoamini kuwa aliyerejea ni kijana waliyemzika na badala yake kumchukulia kuwa ni msukule.
Pamoja na kurejea kwao, baba wa kijana huyo, Boniface Kabonge alisema kuwa mwanaye Nickson alifariki dunia Oktoba 6 mwaka jana na kuzikwa kwenye makaburi ya Mufindi.
"Nilishtuka mwanangu alipobisha hodi na kuingia ndani wakati najua alishakufa na tulimzika, sijui imekuwaje hadi aliyekufa arejee nyumbani,"alisema
Alisema kabla ya kifo chake kijana huyo alikuwa akifanya kazi ya kupasua mbao kwenye msitu huo wa Kihanga, lakini alifariki baada ya kuangukiwa na gogo ambalo lilimjeruhi vibaya kichwani.
Alisema mwili wa kijana huyo ulipelekwa Hospitali ya Wilaya ya Mufindi na kuhifadhiwa katika chumba cha maiti hadi siku ya pili ulipopelekwa nyumbani kwao kwa ajili ya kuagwa.
"Mimi ndiye niliyemuosha mwanangu kutokana na mila zetu, tulimpeleka nyumbani watu waliaga kama kawaida na baadaye tulimzika kwa sababu kila mmoja alijiridhisha na kifo chake," alisema
Akizungumza na Mwananchi kijana huyo alisema hafahamu habari za kifo chake.
"Nashangaa wanaponikimbia ila sikumbuki kama niliwahi kufa, nachojua nilikuwa nikiishi na wenzangu kumi katika msitu wa Kihanga ambako tulikuwa tukila pumba na maji,"alisema
Alisema kuwa kilichomrejesha nyumbani kwao ni ndoto alizokuwa akiota kuwa baba yake amefariki hali iliyomlazimu arudi kuhani msiba.
"Kila nikikaa mwili wa baba yangu ulikuwa ukipita mbele yangu kwenye jeneza huku ukiwa umefunikwa kitambaa chekundu, ndio maana nikaamua kuja kumzika.
Nashangaa nilipofika hapa nikaambiwa kuwa mimi ndio nilikuwa nimekufa,†"alisema.
Kijana huyo alishangaa zaidi baada ya kuonyeshwa kaburi ambalo mwili wake umezikwa na akataka lifukuliwe kukujua ulizikwa mwili gani.
Jeshi la polisi limethibitisha kupokea taarifa za kurejea kwa kijana huyo ambaye mwili wake ulihifadhiwa katika Hospitali ya Mufindi kabla ya kuzikwa.
Mganga msaidi wa hospitali hiyo, Meshack Mlyapatali alisema wapo tayari kufanya uchunguzi wa kisayansi wa tukio hilo, lakini wanasubiri agizo kutoka serikalini au Jeshi la Polisi.
Baba yake alisema kija huyo amebadilika kwa kuwa siku hizi anazubaa na kujikunyata na kuwa wakati mwingine amekuwa akiweweseka kuwa anaona jeneza likipita mbele.

Nimeona si vibaya nikiweka habari hii hapa kibarazani kwangu kwani wote tuna nia moja ya kuhabarisha jamii.
Imeandikwa na Tumaini Msowoya, Mufindi


7 comments:

John Mwaipopo said...

habari hii imekuwa ikijaza kurasa za vyombo vya habari pasi na sababu. mie ni miongoni mwa tunaobisha. kanisa moja la 'upako' iringa ndilo linalojidai kumrejeshea uhai huyu mtu. swali langu hapa ni; hivi kufa sio mpango wa mungu. mpaka leo hawajafukua kaburi alimozikwa huyo mtu. ni hadaa za kanisa za kutaka kupata 'wateja' wengi.

Mija Shija Sayi said...

Makubwa! Hapa najiuliza vipi kama yule aliyekufa ni wa kweli na huyu aliyefufuka ndio wa bandia, mwanawane kizaazaa chake sipati picha.

Anonymous said...

wakishafukua kaburi ndio tutajua kweli mie naogopa mambo ya bongo jamani ndio nini hiyo, mzidi kutupa habari nasi tujue kitakachoendelea, asante dada kwa habari hiyo mie kwanza ndo nimeisoma hapa kwa blog yako.

MARKUS MPANGALA said...

abrakadabra za makanisa ni nyingi tu. Hii ikiwemo
kaka Mwaipopo pale kwetu Lundu kuna jamaa alizama ziwani yaani alikufa maji, lakini hadi kesho anaonekana nchi kavu.
kuna jamaa mmoja alikuwa anabisha sana basi kuna siku akamtokea yaani yule jamaa alionekana mbele yake yapata muda wa saa 12 jioni. sasa sijui hii imekaaje.

LAKINI hizi za makanisa ni WIZI MTUPU ni wachawi wa freemasons hakuna neno la mungu hapo, si unakumbuka KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MENGI YANATENDEKA?
rejea kitabu cha DAVID YALLOP cha IN GOD'S NAME.
Lol..... makanisa ya sasa kama tu ngome za wajinga

chib said...

Mimi naona hizi ni porojo tu za kutafuta biashara. Maana makanisa mengine siku hizi ni biashara tu, na wengine wanasemekana kutumia nguvu za giza kupata wafuasi.
Ulishasikia wapi kanisa ati muhubiri ni mmoja tu, akisafiri basi mnasikiliza kanda za mahubiri yake......

EDNA said...

Mmmmh no comment,

Yasinta Ngonyani said...

Mimi siamini kama ni kweli kwani kuna akina YESU wangapi sasa? Hizo ni imani tu za watu unajua kila mtu akiamini kitu basi kinaweza kuwa kweli. Kwanini wasifukue kaburi ili kuhakikisha?