Wednesday, January 11, 2012

Ndoa ni ninyi wenyewe, Siyo watu wa nje

TULIKUWA TUMEPUMZIKA KIDOGO NA KIPENGELE CHETU CHA MARUDIO KILA SIKU KAMA HII YA JUMATANO. NA LEO KATIKA UPEKUZI WA KAPULYA AMEKUTANA NA MAKALA HII NA AMEONA SI MBAYA KAMA WENGI TUKIJUA KWANI KAMA NISEMAVYO KURUDIA SOMA NDIO MTU UNAPOELEWA ZAIDI. MAKALA HII NIMEIKUTA HAPA. KARIBUNI.
---------------------------------------------------------------------------------------------
SIRI moja kubwa ya kuwa na ndoa nzuri ni wanandoa wenyewe kujitambua kuwa wao ndiyo wenye deni la kuimarisha uhusiano walionao.

Ndiyo kusema kuwa kila siku katika maisha yako, unapaswa kutafuta mbinu za kufanya ili uhusiano wenu uendelee kuwa mzuri.
Siku moja nilikuwa napita Sinza (Dar es Salaam), nikamsikia dada mmoja akijibizana na mwenzi wake kwenye simu; Aah! kwani wewe unataka muda huu niwe wapi? Haya basi niko chooni.

Hayakuwa majibu mazuri, kiasi dada mwingine aliyekuwa karibu, akamsihi mwenzake asizungumze vile.Watu wengi wanapenda kuwa na ndoa nzuri, lakini wao hawajui kuwafanyia mazuri wenzao. Utakuwaje na ndoa nzuri wakati kauli zako ni chafu?

Jitahidi kuwa na kauli nzuri kwa mwenzi wako. Hata pale mwenziyo anapokukosea, zungumza naye kwa njia ya kuondoa kasoro, si kutukanana. Siku zote waza namna ya kuujenga uhusiano wenu. Usidhani ndoa nzuri za wenzio ni jambo linaloshindikana kwako, hapana. Ndoa haijengwi kwa matofali, bali kauli njema na matendo mema.

Kumbuka hakuna mtu aliyezaliwa aje kuiimarisha ndoa yako, ni wewe mwenyewe unapaswa kufanya kazi hiyo. Anza leo kuchukua hatua kama ndoa yako ina walakini huo, utashangaa utakavyokuwa na ndoa nzuri. Katika maisha hakuna lisilowezekana. Kwanza weka lengo, kisha chukua hatua, utafanikiwa.

Ni muhimu kujifunza masuala haya kwani elimu haina mwisho. Wengi wakishaingia kwenye ndoa, basi hudhani wameshamaliza kila kitu. Ni makosa makubwa, unapaswa kuendelea kutafuta mbinu mpya kila siku ili mfaidi raha za ndoa.

Kuna mengi ya kujifunza:
Katika ndoa kuna mengi ya kujifunza, mojawapo ni kujua mwenzi wako anapenda nini. Kwa mfano wanaume wengi wanapenda wake zao wawe na utayari katika mahusiano.Unaweza kushangaa, lakini ni ukweli. Tafiti zinaonyesha watu wasio kwenye ndoa hukutana kimwili mara nyingi zaidi kuliko walio kwenye ndoa, licha ya kuwa wanalala kitanda kimoja.

Watu wakishaingia kwenye ndoa, hufanya tendo hilo kwa muda mfupi zaidi kuliko ilivyokuwa kabla hawajaoana, unajua ni kwa nini? Utayari huwa matatizoni. Sababu ziko nyingi, lakini mojawapo ni wanaume wengi kurudi majumbani wamelewa chakari, wananuka pombe na wake zao wanalazimika tu, wafanyeje.

Lakini wakati wa uchumba, wanaume hao huenda kwa wapenzi wao wakiwa hawajalewa.
Ndiyo ukweli. Kimsingi wanandoa kila mmoja anatarajia kuona mwenzi wake anamjali na anamsikiliza. Kufanikiwa hili, lazima kutumia akili.

Kuna ambao licha ya kuwa tayari kaingia kwenye ndoa, lakini kwa upumbavu, anazungumzia habari za mpenzi wa zamani.

Pia kuna walio kwenye ndoa, lakini wanajali zaidi watu wengine wa nje au kuwasikiliza zaidi wazazi ambao mara kadhaa wamekuwa chanzo cha ndoa kuvunjika.
Jamani hata Biblia imeandika;
Mtu atawaacha wazazi wake na kuandamana na mkewe, hao wawili watakuwa mwili mmoja.

Wengine wako katika ndoa lakini wana lundo la wapenzi nje. Hapo ndoa yako ikiyumba utamlaumu nani? Fanya jitihada kuipa uhai ndoa yako, iwe paradiso ya kweli.Kuna ambao badala ya kutamani kurudi nyumbani, wao hutamani kuchelewa, maana nyumbani hakukaliki.Yaani hakuna mapenzi, hakuna kinachovutia. Mume au mke hapendi kujifunza mambo zaidi.
Ndugu yangu rekebisha ndoa yako, uishi kwa furaha.

Dismas Lyassa ni mtaalam wa mahusiano, wasiliana naye kwa simu 0754 498972 au 0786 148105.
TUKUTANE TENA WAKATI UJAO AU NISEME JUMATANO IJAYO.

14 comments:

sam mbogo said...

Nahilo ndo jibu,ndoa ninyie wenyewe na wala siyo watu,kwamsisitizo (watu wanjee). kaka s

Rachel Siwa said...

Haswa Ndoa ninyi wenyewe,baraka kwa woootee!kaka wa mimi Sam mwana wa mbogo ujambo?

sam mbogo said...

Dada yangu,seydinawangu, laazizi, nyongo mkaliini,bisikuti yangu dear wangu Rachel,mimi mzima tu,za mwaka mpya?ila swali la kizushi ,ndoa ya mbongo kwa mbongo kwa mwanaume wa kibongo ni rahisi kidogo kuimudu!!?? mnasemaje tofauti na mwanaume wa kibogo ukijichanganya na mdada ambaye si mbongo? kaka s

Mija Shija Sayi said...

Kaka Sam hayo majina uliyomwita rachel unamwitaga wifi lakini au uanyatajia nje tuu...ila hilo la bisikuti yangu nimelipenda sana.

Kuhusu swali lako nadhani inategemeana na tabia ya mtu, unaweza ukawa na mwenza asiye mbongo na ukataabika vilevile kama tabia yako haina utu ndani yake..

Yasinta Ngonyani said...

Kaka Sam, da´Rachel na da´Mija! ahsanteni sana kwa kupita hapa na kuacha chochote mbarikiwe sana.
Ndoa ni sisi wenyewe na sio watu wa nje...lakini ndani ya ndoa kuna vishawishi vingi mno ambavyo vinahitaji uvumilivu mkubwa sana. Tamaa, Tamaa ndio kitu ambacho kinafanya ndoa nyingi kutoheshimika,kutokuwa na uvumilivu, kutokuwa na mawasiliano nk. nk....kwani kuna vitu vingi sana nikianza kusema hapa itabidi niwe na daftari nzima...

Rachel Siwa said...

Ahsante sana kaka wa mimi Sam mwana wa Mbogo,Chocolate,Haluwaa wangu, hahahahha da'Mija dada ndiyo wa kwanza jamani mke si wamekutana Ukubwani? au.....Tena hatuombei hivyo lakini ndoa kama ikiisha undugu hauishiii, na ukiona hivyo Wifi maneno anayopewa weacha tuu,@kaka Sam kwenye mapenzi/ndoa hakuna cha Mbogo kwa Mbogo wanaweza wakawa mizinguzii tuu na Mbogo kwa Mtu mwingine ikadumu!!Mapenzi ni Mapenzi......siku nyingine nitakuwekea Nasaha za mama Rachel alizotoa kwenye kuniaga, hahaha alimwaga kwa kiung'eng'e ilikuweka msisitizo.
Da Yasinta ubarikiwe kwa somo hili na wooootee.

Mija Shija Sayi said...

Wee Da'Rachel mi dadako unajua!!

Da Yasinta hebu fafanua zaidi hilo la tamaa..

Yasinta Ngonyani said...

Mija! kuhusu TAMAA: NI KWAMBA MTU LAZIMA uchunge tamaa. tamaaa mbaya…utakuta mtu una mke/mume lakini bado unataka mwingine wanini? macho sifa yake ni kuona yaani kutazama kinachoonekana. Ila sio kila unachokiona ukazani kupata inawezekana. Bora kuishia kutazama kuliko kujifanya unaweza sana.

sam mbogo said...

kwenye ndoa, tamaa ipo,ambayo kwaharakaharaka unaweza kusema kama ulivyo/alivyo fafanuwa binti wa kingoni mama ka/camila(sijuwi nimepatia). vilevile wakati mwingine siyo tamaa,bali ni matatizo yaliyomo ndani ya ndoa.mfano mume/mke hakupi chakula cha usiku(yaani hamgonishani, amriya sita haivunjwi) inaweza kumpelekea mwenzi wako awe mke/mme kutamani nje. labda huu mfano mwingine anaweza kusema hauna nguvu ,kitamaa.mfano huu ni hitimisho katika mikwaruzano na migongano mingi tu kwa wana ndoa ambapo msipo kuwa na misingi mizuli na utaratibu mzuri wa kuyazungumza na mkayamaliza nyinyi wenyewe, hitmisho langu laweza kuwa sahihi kimaamuzi na hatimaye mume/mke kutamani nje. kaka s

Yasinta Ngonyani said...

kaka Sam! Nimekupata sana...na wala sipingi kwa vile tamaa ndio mbolea katika ndoa. ila sasa hapa hiyo ya kutoka nje inatokana na kutopata chakula cha usiku siku moja au siku ngapi? Maana utakuta wengine wana mke/mume mzuri na kila kitu wanacho ambacho kinatakiwa wawenacho lakini bado ana nyumba ndogo sasa hii ni nini?

sam mbogo said...

kwanza kabisa,kutoka nje si kuzuri.nyumbandogo pia si nzuri. lakini tunao rafikizetu,kaka zetu,hata wajomaba zetu,baba zetu wadogozetu,wenye kutoka nje ama kuwa na nymba ndogo. kinacho watoa nje ni hicho chakula cha usiku. iwe maramoja au kilasiku. sasa swali lako ni kilasiku mtu anatoka nje,wakati ana mke mzuri tu,. jibu hapa nikwamba ndani ya ndoa kila mtu ana kuja na tabia yake,ambayo yawezekana kakuwanayo,ama karithi? sasa mtu huyo inategemea na mazingira ya nayo mzunguka. wengi ndoa kwao ni sifa nikitu ambacho,hukichukulia kama ni utaratibu walio ukuta,kiundani kuna maswali mengi ya kujiuliza,kabla ya kuoa na kuolewa,mfano je nikotayari kuoa au kuolewa. je kuna msukumo wa mtu,familia dini,rangi,au hata uwezo kifedha. sasa wengi wetu huwa hatupati muda wa kujiuliza yote haya,na nikweli ina hitaji ufahama wa hali yajuu hasa ukizingatia wengi wetu huamimini ndoa ni bahati,kituambacho kina funga na kuziba nafasi ya kuweza kujiuliza maswali hayo hapo juu. kwa hiyo tabia ya mtu, kwa wana ndoa nikitu muhimu sana kukiangalia hasa sisi wanaume ndomaana unakuta wengi wanatoka nje nahili ndo sababu kiukweli ukiangalia katika familia zetu tunazo toka,lazima utakuta baba alizaa nje, kwa hiyo unategemea mtoto wakiume ndani ya familia hiyo aka pona na katabia hako japo si wote lakini hili lina madhara yake chunguza utakubaliana na mi..kaka s.

Yasinta Ngonyani said...

Kaka Sam! hakika kila neno ulilosema ni kweli kabisa kwani kujiuliza HILO NDIO MUHIMU SANA KATIKA YOYE. Yaani je nipo tayari? nampenda huyo mtu kama alivyo au? Natamani kama ningekutana nawe tena na kuongelea jambo hili:-) Halafu hilo la kusema kuolewa ni bahatio yaani ..basi tu nina mengi sana ya kusema ila nikianza kitakuwa kitabu. UPENDO, UVUMILIVU NA USIKIVU ni muhimu sana katika ndoa. Ahsante kwa mifano uliyotoa..nimeipenda.

Rachel Siwa said...

da'yamimi Mija mama ya MMM, najua na nakuhusudu sana dada wewe!pia Asannte kwa kuchokonoa somo liendelee naona tumepata faida zaidi,da'Yasinta na kaka Sam ahsanteni sana kwa somo!!!

Mija Shija Sayi said...

Kaka Sam Una pointi. Ni kweli tunajisahau tu ila suala la ndoa lilitakiwa liwe na mafunzo yake tena mengi tu, ikiwezekana hata mashuleni. Watoto wanatakiwa waanze kujua polepole maana ya ndoa ili wanapofikia umri huo wa kuoa wawe na macho ya uchunguzi kulingana na msingi waliopewa huko mafunzoni. Sishangai kwa nini watu tuna mtazamo wa 'ndoa ni bahati', hii ni kwasababu ndivyo jamii inavyotufundisha. Tusisahau You are what you see and perceive.

Ni hilo tu wandugu.

Rachel cha utundu nasubiri maoni yako.