Monday, January 24, 2011

UKIKUTA MANYOYA, UJUE KESHALIWA!!!

Utotoni kuna michezo mingi ya kukumbukwa
Habari/kisa hii/hiki nadhani wengi mnakikumbuka niliandika mwaka jana katika pitapita zangu nimekutana nacho hapa kibarazani na nimekipenda na nikaona si mbaya kama tukipitia tena kama nilivyozoe kusema kurudia kitu/kusoma ndio kujifunza. Haya karibuni .....
-------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------
Wakati wa utoto wetu yapo mambo mengi ambayo tumeyapitia, ambayo huwa wakati mwingine ukiyakumbuka unatamani sana kurejea utotoni.

Hivi karibuni mdogo wangu Koero aliweka mada yake aliyoipa kichwa cha habari kisemacho, ‘anaposema mwendawazima’.
Katika makala yake hiyo kuna kipengele alizungumzia kuhusu kuteka maji kisimani na jinsi yeye na bibi yake walivyowakuta mabinti wa pale kijijini kwa bibi yake walivyokuwa wakicheza na wavulana pale kisimani badala ya kuchota maji na kupeleka nyumbani.

Pamoja na kukemewa na Bibi Koero, lakini walimdharau ma kuendelea kucheza michezo yao na wavulana wale, bila kujali onyo la Bibi Koero, isipokuwa binti mmoja ambaye alimsikiliza bibi Koero na kuondoka kurejea nyumbani akiwaacha wenzie wakiendelea kucheza pale kisimani. Kama ungependa kujikumbusha makala hiyo unaweza kubofya hapa.

Kipengele hicho kilinikumbusha wakati wa utoto wangu kule kijijini Litumbandyosi/Kingoli wakati ule nikiwa darasa la nne.
Wakati huo tulikuwa tukienda kisimani kuteka maji na huko tulikuwa tukicheza michezo mingi ya kitoto.

Nakumbuka nilipokuwa likizo nyumbani mwaka jana, nilipokuwa naelekea sokoni, njiani nilikutana na kijana mmoja ambaye ningependa kumwita Mpetamanga (Sio Jina lake) kwa kweli nilikuwa nimemsahau, sijui ndio uzee unaninyemelea, maana nilishangaa alinikumbuka vizuri sana tofauti na mimi ambaye nilikuwa nimemsahau.

Mpetamanga nilisoma naye darasa moja na nakumbuka baadae familia yao ilihama pale kijijini na kuhamia kijiji cha jirani na huo ukawa ndio mwisho wa kuonana na kijana huyu.
Kukutana kwetu pale njiani kulitukumbusha mambo mengi sana ya utotoni ikiwemo ile michezo tuliyokuwa tukicheza kule kisimani tulikokuwa tukichota maji.
Mpetamanga alitumia muda huo kunikumbusha mambo mengi ya utotoni ikiwemo hiyo michezo tuliyokuwa tukicheza kule kisimani.

Kwa kuwa nilikuwa na haraka nilimuaga, lakini nilimkaribisha nyumbani, kisha tukaagana na nikaondoka kuelekea sokoni kununua mahitaji yangu.
Siku iliyofuata nikiwa nyumbani na mwanangu Erik, kwani Camilla alikuwa ametoka na baba yake kwenda mjini kununua mahitaji mengine ya pale nyumbani, nilisikia mtu akibisha hodi, nilipokwenda kufungua mlango alikuwa ni Mpetamanga.

Nilimkaribisha ndani kwa bashasha na kisha tukakaa sebuleni kwa mazungumzo.
Nilimwita mwanangu Erik na kumtambulisha kwa mgeni.
Mpetamanga alishtuka sana, na kuniuliza kwa hamaki, ‘Yasinta umeolewa?’
Nilimjibu kuwa nimeolewa na nina watoto wawili. Nilimjulisha kuwa ninaishi nchini Sweden na familia yangu, na pale nyumbani niko likizo tu.

Alishtuka sana na nilimuona dhahiri akiwa amenyong’onyea kabisa. Alinijulisha kuwa alipomaliza shule alikwenda nchini Malawi kundelea na masomo na amekuwa akiishi huko tangu alipoondoka nchini.
Na yeye kama ilivyo mimi aliamua kurudi nchini kuwasalimia ndugu zake na safari hiyo ilimlazimu kufika Ruhuwiko kumuona mjomba wake, lakini pia akiwa na hamu ya kuniona kwani aliambiwa kuwa familia yetu ilihamia Ruhuwiko siku nyingi.

Na pale tulipokutana ndio alikuwa amefika Ruhuwiko.
Aliniambia kuwa, nilipomkaribisha nyumbani alifurahi sana na alijua huo ndio wakati muafaka wa kuzungumza nami kwani ni muda mrefu alikuwa akiniwaza, na lengo lake ilikuwa kama akinikuta sijaolewa basi azungumze nami ili alete posa.

Nilicheka sana na kumwambia kuwa amechelewa kwani mie niliolewa na kuondoka nchini na kuhamia Sweden.
Nilimchekesha pale nilipomwambia, ‘Ukikuta manyoya basi ujue ndio keshaliwa’
Alicheka sana na kuniuliza kama nina maana gani, na ndipo nilipomfafanulia kuwa mpaka amekuta watoto basi ajue kuwa ndio nishaolewa hivyo……..

Lakini kitu kingine kilichomshangaza zaidi ni kuona jinsi ninavyozungumza kingoni na Kiswahili kwa ufasaha pamoja na kuishi nje ya nchi kwa muda mrefu, kwani hata nilipomweleza kuwa nimeolewa na ninaishi nchini Sweden alidhani namtania, hadi nilipomuonesha picha za familia yangu.


Hata hivyo Mpetamanga alikubali matokeo, na kuridhika na maelezo yangu.
Kusema kweli kila niwapo likizo nyumbani nakutana na visa na vituko vingi vya aina hii na haviishii hapo, hata mtandaoni nako kuna visa vyake, hili sitalizungumza kwa undani maana mdogo wangu Koero amelizungumza hili kwa kirefu katika makala yake aliyoipa kichwa cha habari kisemacho, ‘Dalili hizi sio za kweli’ unaweza kubofya hapa kumsoma.

Kuna wanaume wakware ambao hawakubali kushindwa. Hata wakute manyoya lakini bado watapekuwa weeeee! wakiamini kukuta minofu. Jamani mmeshachelewa ndio keshaliwa huyoo…….LOL

10 comments:

o'Wambura Ng'wanambiti! said...

wengine wanapenda mifupa na si nyama ati!

Rachel Siwa said...

hahaaha Mpetamanga mezea kwa maji tuu MSWIDISH amekuwahi wewe ulikuwa unaremba ehhe!
Aksante da Yasinta!

emu-three said...

Mhhh, rafii yangu anayetokea huko, akanikumbusha kuwa `wao, wakikabidhiwa mzigo wanaufikisha kwa mwenyewe bila mapungufu, lakini wakikabidhiwa nanihii, ni nadra kufikisha...mmmh, naogopa kuongea zaidi.
Najaribu tu kudodosa huu usemi wako wa mwisho ulisoema hivi:-Kuna wanaume wakware ambao hawakubali kushindwa. Hata wakute manyoya lakini bado watapekuwa weeeee! wakiamini kukuta minofu....
KWAMBA Usijiamini moja kwa moja kuwa kuku keshaliwa, ..wewe kuna vichwa ngumu dada'ngu!

ADELA KAVISHE said...

hahahahahaha umenikumbusha mbali sana my dear

Goodman Manyanya Phiri said...

Dada Adela Dally Kavishe, mlikuwa mnataka nini “huko mbali” na wanaume wenye kupenda kuwatongozeni? Mpetamanga twatakiwa tumjadili au tumhukumu Mngoni wawatu?

NAMNUKUU DADA YASINTA:

“Kusema kweli kila niwapo likizo nyumbani [UNGONINI]nakutana na visa na vituko vingi vya aina hii na haviishii hapo, hata mtandaoni nako kuna visa vyake..."


Wacheni Dadazetuni kutunyanyasa sisi kaka zenu! Mnataka tuwatongoze nyani? Au mnataka kutongozwa na wanawake wenzenu tu na sio pia na sisi wanaume? Au mnajiona kushuka ngazi mkitongozwa na aina fulani ya wanaume? Twambiane kinaganaga tu kila tunapowatongozeni na tutaacha kuwapeni burhudhani zetu: sisi hatukuwa namaana mpate ugonjwa wamoyo bure juu ya hilo, kumradhi!



EUROPEAN SCENARIO


Hata huko ng’ambo mwendesha-barua (POSTMAN) atashtuka naku staajabu (kwa furaha lakini) kutoka kichwani mpaka chini akikaribishwa ghafla ndani na mwanamke nayeye huku alikuwa pilikapilika na shughuli sugu za wingizaji-barua huko mitaani.


Nikwambie, baada ya kufunguliwa huo mlango na huyo bibi, anaweza kabisa akafikiria mambo ya kumwoa huyo mwanamke kama yeye POSTMAN bado kuoa.


Na kama huyo mwanamama je anamtoto ndani ya nyumba?

Mtoto sitatizo kwa POSTMAN kwani atafanya ADOPTION tu, tena ni dalili nzuri kwamba POSTMAN amekutana na jike halisi...labda liliopewa mimba na kisha bahati mbaya kutelekezwa na dume fulani!


Kwanini POSTMAN asishtuke "nakujaza mwenyewe huyo mwanamama anamtoto inamaana keshaolewa POSTMAN kaa mbali”?

Hilo swali litakuwa ni swali la unafiki tu kwani asilimia kubwa ya watoto wenye baba-walezi utakuta baba haohao sio tena baba-wazazi na labda zaidi ya nusu ya watoto wote duniani hawana baba-mzazi mwenye msaada kutokana na talaka, kutojitokeza kwa baba huyo, au kufiwa naye baba-mzazi, WALA HAO WATOTO HAWANA HATA BABA-MLEZI!



Nimesema mengi na sifichi nataka jibu kutoka kwa akinamama. Lakini, cha kumtetea Dada Yasinta binafsi hapa kwenye posti yake ni kwamba “karibu-Mpetamanga” yake haikuwa kabisa sawasawa na “Karibu-POSTMAN” ya maana hapo juu huko Ulaya, kwani Yasinta naMpetamanga walicheza pamoja michezo kama watoto huko visimani vya Ungonini. Tena nasikia kisauti kinachosema: “Toa mfano unaohusiana na mazingira yaAfrika, Bw Phiri uwache mifano kama 'POSTMAN'”.



AFRICAN SCENARIO


Nianze kwa kunukuu maelezo ya Dada Yasinta:

“[Mpetamanga] alicheka sana...na ndipo nilipomfafanulia kuwa mpaka amekuta watoto basi ajue kuwa ndio nishaolewa hivyo….”


Nami nikiwa Manyanya nilicheka kama Mpetamanga niliposoma sehemu hiyo yako ya maandishi! Dada wee, manyoya sikanga kabisa! Na kanga huyo au mnyama yoyote yule anaweza akatolewa manyoa yote huku akiwa bado yuhai nakuja kuotesha manyoa mengine hapo baadaye.


Je, tunakubaliana?


Sasa, kama humtafuti palepale ulipokuta manyoa yake, je utajuaje kama kweli keshaliwa? Maana yake inawezekana kabisa ikawa manyoa ni dalili tu jinsi alivyopigana na kujitetea kwa adui yake mpaka pale alipoponea chupuchupu!


Dadazanguni Yasinta nawe Koero, Mkumbuke basi tunaweza tukacheza mchezo mmoja tukiwa watoto namimi Mpetamanga mchezo huo nikachukulia kama “mie ni mume wako nawe ni mke wangu” (PLAYING HOUSE) wakati wewe Yasinta/Koero ni bado mchanga zaidi kuyatafakari kwa undani ninayeyatafakari mimi juu ya ugali wako huo wa udongo “ulienipikia kama mimi mume wako wa ukweli pale baadaye ukubwani”. Na tunapokutana baada ya miaka 25 nawe kusema “karibu Mpetamanga”, najua kabisa MUNGU ATUKUZWE KWANI NDOTO YANGU YA UTOTONI INAANZA KUTIMIA!



KWA KUMALIZA



Turejee basi katika mjadala tuliopewa leo. Mimi najua ilikuwa utundu tu kwa Dada Yasinta (au niseme usahaulifu kidogo kwa upande wake) lasivyo ilikuwa kosa kabisa kusema:


“[Kaka Mpetamanga, Karibu nyumbani]”....


...bila kumtahadharisha papo hapo kwamba:
“Lakini ujuwe mwenzangu ya utoto wetu pale kijijini yamekwisha sasa tuko ukubwani na mimi mwenzio tayari kuolewa, na mume wangu yupo nyumbani:”.

Upepo Mwanana said...

ha ha haaa Chachaaaaa

Simon Kitururu said...

Kwenye MANYOYA YA KUKU bado ni kweli pia kuwa,...
... labda KUKU alifanikiwa KURUPUSHANI na akakimbia na minofu yake LAKINI!:-(

Ndugu Nkwazi N Mhango said...

Je kama hana manyoya akiliwa utajuaje? Na je anayefuatilia kama ni fisi au mbwa unategemea nini? Je kama ni sisimizi huoni kuwa manyoya bado ni dili?

emu-three said...

Mhhh, hapa kuna kaporojo kazuri, ngoja nikae, angalau nisikie harufu ya manyoya yaliyobakia, ...na na..wanasema kuku akiatamia anawacha manyoya, labda haya manyoya ni ya kuku alikuwa anaatamia, katoka kidogo, ...lakini...hahah, naongezea utamu wa kijiwe jamani, naona kimefika kwa wenyewe!

Unknown said...

Hii kama sio zubaa uone basi ni isha kuwa hivyo ilivyosemwa.