Monday, April 1, 2013

MWEZI WA NNE(APRILI) NI MWEZI KUKUMBUKWA NA MUHIMU KWA HISTORIA YA NCHI YETU

Kwa watanzania wengi ambao wanafuatailia historia na kukumbuka masuala muhimu ya nchi hii mwezi huu una mambo muhimu ya kukumbukwa kutokana na matukio makuu yasiyopungua manne.
Kama ifuatavyo hapa chini.
Ø Baba wa Taifa hayati mwalimu Nyerere alizaliwa mwezi hu wa nne 13/04/19922.
Ø Muungano kati ya iliyokuwa Tanganyika na Zanzibar kuzaliwa kwa Tanzania Ulizaliwa mwezi wa nne 26/04/1964.
Ø Rais wa kwanza wa Zanzibar hayati shekh Abeid Aman Karume aliuwawa mwezi huu wa Nne tarehe 07/04/1972
Ø Aliyekuwa Waziri mkuu wa tatu wa Tanzania Hayati Edward Moringe Sokoine alifariki mwezi hu wa nne tarehe 12/04/1984.
Ø Na kwa mwaka 2013,unaongeza tukio lingine la kuanza utaratibu mpya wa kujadili na kupitisha bajeti ya Serikali kuanzia tarehe 9/4/2013.
Ø Mwaka 2014 utakuwa na tukio muhimu na nyeti litaongezeka katika mwezi huu kutokana na kuendelea kwa mchakato wa kupatikana kwa katiba mpya ya Tanzania ambayo inatarajiwa kuzinduliwa tarehe 26/04/2014,wakati muungano utakapokuwa unatimiza miaka 50.
Kutokana na matukio manne ya awali tunatakiwa kuwaenzi mzee wetu hayati Abeid Karume, Julius K Nyerere na Edward M. Sokoine ,kuna umuhimu kwa Watanzania kupewa au kukumbushwa kuhusu historia ya Viongozi hawa na tukio la muungano, viongozi hao wana michango ya aina yake katika historia ya nchi hii na kutokana na hilo tunatakiwa kujiuliza nini kama jamii tunaweza kujifunza na kuiga kutoka kwao kwa faida ya kizazi hiki na kijacho.

07/04/1972-KUUWA KWA HAYATI KARUME KWA KUPIGWA RISASI.
Mambo ya kukumbukwa aliyasimamia hayati karume.
Hayati karume aliweza kuwaongoza wazanzibar kuwaondoa watawala wa kisultani
Historia inatuonyesha kuwa karume alikuwa baharia/mvuvi. Karume alisoma mpaka darasa la nne. Kwa kusoma na kuishi darasa la nne na pia kwa kuwa baharia inamaanisha kuwa kiongozi bora na jasiri hakuhitaji kwenda shule kubwa,Uongozi ni kipaji/kujitolea na kujituma. Kiongozi anatakiwa kuongozwa na Uzalendo na siyo ubinafsi kama ilivyo kwa viongozi wengi.

Karume kutokana na kuongozwa na kanuni ya maadili ya asili aliweza kufanya maamuzi ya kijasiri bila ya kujifikiria yeye kwanza pale alipokubali kuunganisha Zanzibar na Tanganyika na kuzaliwa Tanzania,Inasadikiwa kuwa kabla ya Tanganyika kuungana na Zanzibar Mwalimu hayati JK Nyerere alitaka tuungane na Kenya Kenyatta akakataa. Kwa kukubali kwake kuungana na Tanganyika alipoteza sifa ya Ukuu wa Nchi na kuwa Makamu wa Rais kitu ambacho kama hakuwa anaongozwa na uzalendo asingekubali pamoja na kuwa kulikuwa na sababu zingine za kiusalama na za kuharakisha uhuru wa nchi zingine za kiafrika bado kwa uamuzi wake anaingia katika viongozi waliotanguliza uzalendo kwanza kabla ya ubinafsi.

Kutokana na kukubali kwake kuungana na Tanganyika Muungano huu umekuwa wa kuigwa na unaendelea kudumu pamoja na kasoro za hapa na pale. Kuna nchi nyingi za Afrika zilijaribu kuungana lakini kutokana na ubinafsi wa viongozi wa nchi hizo muungano wao haukudumu mfano Senegambia muungano kati Senegal na Gambia.

Karume alikuwa mtu wa vitendo kiongozi anayeonyesha kwa mifano halisi na hai ya kuwatumika wananchi alianzisha wazo la kujenga nyumba za kuishi watu wa maisha ya kawaida Michenzani.

Karume pia aliweza kutoa maamuzi ambayo yanaweza kufananishwa na mzazi katika familia kwa kumteua Dkt Salim A.Salim kuwa balozi mdogo wa Tanzania nchini Misri akiwa na umri wa miaka 22,ambapo katika hali ya kawaida Dkt Salim alikuwa anaonekana mchanga na mdogo na kwa mazoea ya viongozi hata katika ngazi ya familia angeweza kusema huyo ni Taifa la kesho au kiongozi wa kesho. Kwa kumteua Dkt Salimu karume alidhihirisha kuwa ni kiongozi ambaye anaamini kuwa hata vijana wanaweza kusimamia majukumu katika ngazi mbalimbali pale watakapokabidhiwa madaraka hayo kwa nia njema. Kudhihirisha kuwa chaguo lake halikuwa la kubahatisha Dkt Salim alipanda hadi kufikia kutaka kuwa katibu mkuu wa Umoja wa mataifa kama kusingekuwa na mizengwe ya mataifa makubwa. Ikubukwe kuwa dkt Salim ni mmoja kati ya makatibu wakuu wa uliokuwa umoja wa nchi huru za Afrika OAU kwa sasa AU ambaye ametumikia cheo cha ukatibu Mkuu kwa muda mrefu..

Hayati karume anatufundisha kuwa wazazi na viongozi wanatakiwa kuwaamini na kuwajengea moyo wa kujiamini na kujitumia vijana watoto wao ili waweze kusimamia na kutekeleza masuala mbalimbali. Fundisho kubwa tunalolipata kutokana na suala la KARUME kumteua Dkt salim kwa umri wa miaka 22,kuwa kuna umuhimu wa kuwaandaa vijana kuwa viongozi na wasimamizi katika ngazi ya kuanzia katika familia. Mfano tunatakiwa kuhakikisha kuwa tunawashirikisha vijana katika masuala ya utunzaji wa mali na rasimali katika ngazi ya familia na jamii.

Karume ametuachia changamoto kubwa ya kuifanyia kazi katika masuala yanayohusiana na pale tunapotakiwa kufanya maamuzi yanayohusiana na masilahi ya umma na kwa manufaa ya walio wengi. Swali wewe kama kiongozi unajilinganishaje na Mzee huyu ambaye hatuko naye kimwili lakini ambaye anaonekana bado yu hai na ataendelea kuwa hai.

Unajengaje uzima wa milele wa jina lako katika ngazi ya familia na jamii kama viongozi waliotangulia mbele ya haki?

TAREHE 12/04/2008
SOKOINE.
Historia inaonyesha kuwa Sokoine alikuwa ni waziri Mkuu wa tatu wa Tanzania alitanguliwa Nyerere,Kawawa. Alikuwa waziri Mkuu kwa vipindi viwili 1977-1981 na 1982-1984.
Sokoine alikuwa jasiri na alifanya kwa vitendo/alithubutu na aliweza. Kwa kifupi Sokoine alikuwa ana mtazamo wa kufanya kwa mkabala wa kuweza.

Kutokana na ujasiri aliweza kuthubutu na kutenda,Sokoine aliweza kuthubutu na kumshawishi mwalimu nyerere kupunguza baraza la mawaziri wakati huu baraza la mawaziri lilikuwa na mawaziri wapatao 26,alilipunguza na kuwa na mawaziri 13.

Sokoine ndiye muasisi wa kitu kinachoitwa daladala katika miaka ya 1980 lilikuwa shirika la usafiri Dar lilielemewa na idadi ya wakazi jijini Dar na kushindwa kuhimili wimbi hilo sokoine akaamuru kuanzishwa kwa usafiri wa watu binafsi ikumbukwe kuwa wakati huo suala la makapuni na biashara binafsi hazikuwa zinaruhusiwa daladala za mwanzo kabisa zilikuwa canter na zilijulikana kwa jina maarufu (Chai maharage) kutokana na kuwa na viti vya mbao mabenchi ambayo yalikuwa yanatumika sana katika migahawa na ambayo watu wa kipato cha chini hasa kwa jiji la Dar asubuhi walikuwa wanapata kifungua kinywa chai kuchanganya na maharage na maandazi au kitumbua na mkate.

Sokoine ndiye muasisi wa sheria ya nguvu kazi ambayo iliwezesha nchi hii kuwa na uzalishaji wa chakula cha kutosha kutokana na kuisimamia sheria hiyo ya nguvu kazi,Chanzo cha kijiji maarufu cha GEZA ULOLE.
Sokoine kam kiongozi wa kusimamia shughuli za Serikali aliongoza na kusimamia vita dhidi ya wahujumu uchumi (Tunaweza kusema yeye ndiye muasisi wa kweli wa kupiga vita hiki kitu kinachoitwa ufisadi.) pamoja na kuwa katika vita hiyo imeacha makovu lakini funzo tunalolipata ni kuwa Sokoine alijitolea kuwahudumia wanyonge wananchi waliowengi ambao kutokana na matokeo ya vita ya kagera makovu na machungu ya vita hiyo ilisababisha uchumi wa nchi kuyumba na baadhi ya wafanyabiashara kuitumia nafasi hiyo kwa manufaa yao kwa kuamua kuficha bidhaa muhimu ili ziuzwe kwa bei ya kulangua ( Kuliibuka biashara ya ulanguzi kurusha/Sukari, sabuni, hata sigara kwa wanaokumbuka vizuri kipindi cha miaka ya 1980) Vijana wengi wa wakati huo waliacha kusoma(shule za Msingi na sekondari) na kujiingiza katika biashara ya ulanguzi kurusha vitu muhimu ili kujitajirisha. Katika vita hiyo ya wahujumu uchumi Tanzania kwa mara ya kwanza iliweza kushuhudia wafanyabiashara wanatupa mali zao ikiwemo fedha kutokana na jinsi Sokoine alivyosimamia zoezi hilo. Historia inaonyesha kuwa wafanyabiashara wengi wanaongozwa na ubinafsi na kwa maana hiyo hawako tayari kupoteza hata senti tano,lakini waliweza kutupa mali zao.

Tunatakiwa kumkumbuka SOKOINE kwa kuangalia na kusoma yale yote aliyataka kuyafanyia kazi. Mfano hata wazo la kuwa na Usafiri wa treni Dar, (Maarufu treni ya Mwakyembe) ni moja ya masuala aliyokua anafikiria k uyafanyia kazi

SOKOINE KAMA KIONGOZI
Aliongoza kwa maslahi ya wengi wananchi aliokuwa anawatumikia
Alikuwa na sifa ya UJASIRI,KUJITUMA KUWAJIBIKA kwa vitendo.
Wewe kama kiongozi wa kisiasa au mtumishi wa umma unajipima vipi na Hayati SOKOINE jikague ili uone kama unaweza kuvaa viatu vya marehemu sokoine hata kama au kukubana?

13/04/1922-KUMBUKUMBU YA KUZALIWA KWA HAYATI BABA WA TAIFA.
Historia inatuambia kuwa mwl alizaliwa mwaka 1922 kijiji butiama katika wilaya ya musoma Mkoani mara,alianza shule akiwa na miaka 11,baada ya kuwa mchungaji wa mifugo hasa ng
ombe. Mwalim alisoma shule ya msingi inayoitwa mwishenge na baada ye kuendelea na masomo ya sekondari katika shule ya sekondari Tabora ,mahali alikoanza kuonyesha au kujipambanua kuwa yeye ana sifa za kuwa kiongozi kwa kuwa kiongozi wa serikali ya wanafunzi na alikuwa anasifa ya kutetea wanafunzi wake, sifa nyingine alikuwa na mtazamo wa kimapinduzi/ukombozi hasa katika michango yake aliyokuwa anaitoa katika debeti (Mijadala iliyokuwa inaendeshwa katika shule enzi hizo ambayo ilikuwa inahusisha na kuchambua mada mbalimbali hasa katika masomo ya historia na kiingereza.

Mwalimu aliendelea na harakati za masuala ya ukombozi hata alipokuwa katika chuo Makerere nchi Uganda.
Baada ya kumaliza masomo ya chuo kikuu mwalimu aliaajiriwa kama mwalimu katika shule ya sekondari pugu na kuendelea na harakati za ukombozi kwa kushiriki katika kuasisi uanzishaji wa chama cha Tanu Mwaka 1954 kutoka TAA. Ili kuonyesha kuwa mwalimu alikuwa amejipambanua kuwa ni mwalimu na mwalimu ni kioo cha jamii alikubali kuacha kazi ya ualimu na kuendelea na masuala ya ukombozi wa watanganyika (Kuthamini maslahi ya wengi na siyo ubinafsi). Mwalimu wakati anajikita katika masuala ya siasa ili kupigania uhuru alikuwa na miaka 32 tu,umri ambao katika hali ya kawaida katika miaka ya sasa hivi unachukuliwa kama kijana hajakomaa kuwa katika masuala ya uongozi wa kitaifa wakati si kweli.

Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ni nani katika historia ya Tanzania,Afrika na Dunia kwa ujumla?
Mfano:-  Mwl.  Nyerere alikuwa kama taasisi ya kutuwezesha kupata viongozi kwa mfumo aliuenzi-Mwinyi na Mkapa ni matokeo ya mwalimu kuwa kama taasisi.
Mwalimu alikuwa kiongozi anayeongozwa na UTU na kujali maslahi ya wengi,alikuwa Muasisi na kukubali DSM kuwa makao makuu ya kamati ukombuzi wa Nchi za kusini mwa Afrika na yeye kuwa kiongozi wa Nch zilizokuwa mstari wa mbele katika mapambano ya ukombozi wa Nchi za kusini mwa Afrika, Msumbiji, Angola, Namimbia, Zimbabwe na Afrika ya Kusini.
Mwalimu alikuwa kiongozi wa wanyonge kumbuka mwalimu alikuwa Mwenyekiti wa kamati ya SOUTH SOUTH Commision,Kamati iliyoundwa na Nchi zinazoendelea kuangalia na kupendekeza mfumo wa Uchumi mara baada ya kwisha kwa vita baridi iliyokuwa inaongozwa na Nchi za Urusi na Marekani.

Pamoja na mapungufu yake kama binaadmau bado anabaki kuwa kiongozii wa mfano aliyepata kutokea katika Nchi yetu, Bara la Afrika na Dunia.
Mwalimu anatuonyesha kuwa Uongozi ni suala la kujitolea kwa maslahi ya walio wengi na si suala la kujinufaisha. Kiongozi unatakiwa kuwa na msimamo thabiti na usio yumba,kumbuka mwalimu alipewa jina la utani la HAAMBILIKI kutokana na kusimamia katika kile anachoamini.
Mwalimu alikuwa kiongozi mwenye maono,SIASA YA UJAMAA NA KUJITEGEMEA,pamoja na mapungufu yaliyojitokeza katika utekelezaji wa siasa ya Ujamaa na kujitegemea ,suala la kujitegemea katika familia na kama taifa halina mjadala, na kuamini kuwa binaadamu wote ni sawa kwa maana katika hali ya kawaida sisi binaadamu thamani yetu ni huo UBINAADAMU na si kile unachomiliki.

 26/04/1964 NI SIKU YA MUUNGANO WA ILIYOKUWA TANGANYIKA NA VISIWA VYA UGUNJA NA PEMBA(ZANZIBAR NA KUZAA TANZANIA)
Muungano wa Tanganyika na Zanzibar pamoja na sababu nyingi zinazotolewa za masuala ya kiulinzi na usalama na undugu wa asili kutokana na watu wa kutoka Tanganyika wengi kulowea katika visiwa vya ugunja na pemba kufanya kazi za manamba katika mashamba ya mikarafuu,kazi za ulinzi na uvuvi. Sababu kubwa ni kutaka kurudisha udungu huo na pia kuhakikisha kuwa wazo la kuwa na Afrika moja linatimia kwa kuunganisha nchi na kanda na baadae kuwa na muungano wa Afrika ambao utakuwa umejengwa kwa misingi ya kueleweka miongoni mwa mataifa ya Afrika na ikumbukwe kuwa huu ndio ulikuwa mtazamo wa baba wa taifa katika suala la kuwa na muungano wa Nchi za Afrika kwa lengo la kuwa na Sauti ya pamoja katika masuala mbalimabali ya kiuchumi kijamii,kisiasa na kiutamaduni. Nini kimetokea na nini kinaendelea ni suala la kulijadili na kuliangalia kwa mapana bila ya kuwa na mtazamo wa nani anapata nini na nani anakosa nini. Je muungano huo unaweza kuwa soma kwetu katika kufikiria mustakabali wetu kama Taifa na hasa katika kipindi hiki cha viguvugu la katiba mpya. Wewe unasemaje.
Vipi suala la muungano katika familia zetu linadumishwa au ndo kila siku migogoro. Tujadili kwa pamoja.

 

3 comments:

emuthree said...

Mhh, kumbe mwezi wa nne ni muhimu sana japokuwa wengine wanauenzi kwa mzaha(April fool)...tunashukuru mpendwa kwa historia hiyo, itawasaidia sana vijana wetu, kujua wapi walipotoka na ni nini muhimu kwenye mwezi huu kwa kumbukumbu zetu.

ray njau said...

Kadiri kila mshiriki wa familia anavyomtendea mwingine kwa heshima na staha, ndivyo kunavyozidi kuwa na mawasiliano mazuri. Mwandishi William Prendergast anasema: “Wazazi wote wanapaswa kuwa na mawasiliano ya karibu, ya kila siku kwa kawaida na watoto au vijana wao.” Anaongezea: “Inaonekana kwamba hilo ndilo suluhisho bora zaidi kwa tatizo la kuwatendea watoto vibaya kingono.” Kwa kweli, Biblia inapendekeza aina hiyo ya mawasiliano ya kawaida na ya upendo. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7) Mwongozo huo unapotumiwa, nyumbani panakuwa pahali ambapo kila mshiriki wa familia anaweza kuzungumza kutoka moyoni kwa uhuru na kwa usalama.

Rachel Siwa said...

Kachiki Alifiwa na baba yake Mzazi tarehe..23/04/1994...na siku hiyo kaka yake mdogo..kwa wanaume ndiyo wa mwisho..Alizaliwa..23/04/1985....