Saturday, September 12, 2009

HADITHI YA DOA JEUPE

Nadhani wengi tumewahi kuisikia hadithi hii kama hujawahi basi soma hapa na ufurahi au usikitike.

Hapo zamani, alikuwwepo mfalme ambaye hakupenda kabisa watoto wa kike. Akamwonya vikali mkewe kuwa akizaa mtoto wakike, atamuua.

Mke wake alijaribu kumsihi kuhusu swala hilo, kwa kumueleza kwamba watoto, wawe wa kike au wa kiume ni riziki ya Mungu. Vile vile mtoto wa kike, atamsaidia sana mama yake kwa mambo mengi, hasa shughulu za kika siku za nyumbani. Lakini, yote aliyozungumza mkewe, ilikuwa kama kuzungumza na kiziwi.

Wakati huo, mke wa mfalme, alikuwa na mimba, na siku zilikuwa zimewadia kuzaa. Mfalme, akasisitiza kuwa huyo mtoto ambaye yu njiani kuzaliwa ataishi iwapo atakuwa wa kiume. Mkewe akazaa mtoto, mtoto wa kike. Mfalme bila huruma akamuua yule mtoto.

Mkewe akabeba mimba tena, mara ya pili, vile vile akazaa mtoto wa kike. Mambo yakawa yale yale, mtoto akauliwa.

Mimba ya tatu, mfalme alikuwa safarini. Safari hiyo, ilichukua muda mrefu sana. Huku nyuma mkewe akajifungua mtoto wa kike tena. Kwa kuhofia mumewe kumuua yule mtoto, akaamua afanye kila aliwezalo yule mtoto aishi, kwa maana mumewe alikiwa hayupo. Alimchukua porini asijue la kufanya, akahangaika huku na huku. Hatimaye njiani, akajigonga na jiwe. Jiwe hilo halikuwa la kawaida, lakini yeye hakufahamu. Ghafla, baada ya kujikwatua kwnye ilele jiwe, mbele yake alisimama bibi kizee. Akamuuliza zote mkw wa mfalme kama ana matatizo. Bila kusita, yule mke wa mfalme akamueleza yote yaliyotokea kwa mimba zake za awali na akamueleza pia, alikusudia kumfanya nini huyu mtoto wa tatu aliyekuwa mikononi mwake. Isipokuwa hakufahamu afanye nini, na nani atamsaidia.

Baada ya yule bibi kizee kusikia hayo, akaamua kumsaidia mke wa mfalme, akamwambia:”Nitakusaidia, unaweza kuniachia mimi mtoto huyu. Nitamtunza, lakini ni lazima tupeane ahadi. Utakuwa unakuja kumuangalia wakati mume wako yupo safarini. Hata kama hatosafiri kwa muda mrefu, subiri mpaka asafiri, ni lazima uweke hiyo ahadi. Ikiwa mtoto wako ataugua, nitakuja kwenye ndoto zako. Kwa sababu ya doa jeupe kwenye goti lake, tutamwita Doa Jeupe.”

Wakakubaliana na kuwekeana ahadi. Mtoto akachukuliwa na bbi kizee, mke wa mfalme akaanza rahaa safari ya kurudi nyumbani. Njiani akawaza kwa furaha:- “Hatimaye, nimepata mtoto ambaye ataishi. Niliamini kuwa nitakufa bila ya furaha kama hiyo!”

Mfalme, baada ya siku kadhaa, alirejea toka safarini, kitu cha kwanza, akamwuuliza mkewe kuhusu hali yake. Mkewe akajibu: “Nilizaa mtoto ulipokuwa safarini, lakini aliktoka kabla ya wakati wake kwa hiyo hakuishi nikamzika.” Mfalme akampa pole mkewe kwa masikitiko ya kupoteza mtoto.

Wiki, miezi ikapita mkwewe akaomba sana mume wake asafiri tena, ili akamwone mtoto wake anaendelea vipi. Lakini mfalme, hakusafiri.

Siku moja, mfalme akachukua bundiuki yake akamuaga mkewa kwamba anakwenda mawindoni, siku nzima. Hata hivyo mkewe asingeweza kufanya lolote maana ulikuwa ni muda mfupi kwake. Mfalme akajitayarisha na kuondoka. Njianai kuelekea mawindoni, mfalme akakutana na Doa Jeupe. Kwa uzuri wake alivyoumbika, ingawa alikuwa bado msichana mdogo,mfalme akamfuata alipokuwa akielekea, mpaka kufika kwenye nyumba ya yule bibi kizee na akamwona Doa Jeupe anaingia ndani Akabisha hodi, hapo nyumbani kwa bibi kizee. Mfalme akamwuuliza bibi kizee:- “Huyu mtoto wa nani?” Akajibu: “ Huyu mtoto ni wangu wa kuzaa mwenyewe!” Mfalme akauliza tena: “Anaitwa nani?” “Doa Jeupe;” akajibu bibi kizee. Mfalme akajaribu sana kuzungumza na yule msichana, lakini Doa Jeupe akabaki akimwangalia bila kusema lolote! Mfalme mwishowe akasema : “nataka kumwoa huyu mtoto wako!” Bibi kizaa kwa heshima, akajibu: “ Unavyotaka mtukufu.”

Aliporejea nyumbani, akamweleza mkewe kwamba amekutana na msichana mzuri asiye mfano na angependelea kumwoa akifikia umri wa kuolewe.

Huku nyuma bibi kizee alipata ndoto usiku ule. Ndoto hiyo ilimuonyesha nyumba yake mwenyewe. Nje ya nyumba barazani, aliona alama za mihuu ambayo alifanana na ya mfalme. Kutokana na ndoto hiyo. Akafahamu kwamba mfalme atarudi tena kwa sababu ya Doa Jeupe.
Kwa hiyo akamwambia Doa Jeupe asubuhi yake: “Mwanangu, mimi nina safari ndogo nitakapokuwa sipo, na yule mfalme akija, usimruhusu ndani ya nyumba. Na ukikutana naye nje, usishawishike kumfuata!” Doa Jeupe, akaahidi atafanya alivyoelezwa. Asubuhi, bibi kizee akaondoka. Baadaye kidogo, mfalme akaja muangalia aliyetegemea kuwa mkewe wa maisha ya baadaye. Alibisha hodi, lakini hakuna aliyefungua. Ikabidi aondoke bila mafanikio yo yote. Hayo, yalitokea mara nyingi na ukafika wakati mfalme akakata tamaa kbisa. Hivyo akachukua uamuzi wa kutafuta msichana mwingine, awe mkewe wa pili. Haikuchukua muda akaoa mke wapili. Akamwelezea kuwa :- “Nimekuoa wewe , kwa sababu sikuweza kumpata Doa Jeupe!”

Mkewe mfalme wa pili, kazi yake ilikuwa mkata kuni. Katika mojawapo ya safari mwituni kufuata kuni, alikutana na msichana mzuri sana. Aliporudi nyumbani, akamweleza mume wake kwamba amemwona msichana aliyemzungumza. Mfalme kusikia hivyo, akapata ari na hamu kubwa ya kwenda kumtafuta tena Doa Jeupe. Kweli alipofika ile sehemu mkewe alipomuona, alikuta nyayo za miguu ya Doa Jeupe,zikielekea nyumbani kwa bibi kizee. Akaenda moja kwa moja mpaka mlangoni akabisha hodi. Hakuna aliyemfungulia. Kwa masikitiko, akarudi kwake. Akajaribu tene na tena, mambo hayakubadilika.

Bibi kizee akaanza kuingiwa na wasiwasi, kwa hivyo akamfuata mke wa kwanza wa mfalme. Akameleza nini mumewe anachotaka kufanya kuhusu Doa Jeupe. Mamaye Doa Jeupe, alishtuka sana aliposikia hayo: “Haiwezekani”! alisema. Wakaja na wazo zuri pamoja kwamba yeye bibi kizee na Doa Jeupe wahamie porini zaidi. Wakafanya hivyo siku hiyohiyo.

Mfalme akakata tamaa kabisa, hasa baada ya Doa Jeupe na bibi kizee kuhama walipokuwa wakiishi zamani. Kwa sababu hiyo, Doa Jeupe na bibi kizee waliishi kwa amani miaka mingi bila kubughudhiwa.

Doa Jeupe, akawa msichana mzuri wa ajabu. Siku moja , bibi kizee, ilibidi asafiri kwenda kuangalia ukoo wake. Hivyo akamuacha Doa Jeupe peke yake pale nyumbani. Nyumba yao mpya, ilikuwa karibu sana na mto. Ambapo ndipo walipokuwa wakioga, kufua na kuchota maji. Doa Jeupe, siku hiyo akaenda kuoga peke yake. Wakati huo huo mfalme alikuwa katika moja ya safari zake. Njiani ilimlazimu avuke mto huo huo ambao Doa Jeupe alikuwa akiutumia. Dakika chache baada ya Doa Jeupe kumaliza kuoga na kurudi nyumbani, mfalme naye, akafika sehemu ile ile. Wakati akisubiri mtumbwa wa kumvusha alikaa juu ya jiwe, miguuni kwake, aliona unywele umejisokota katika mguu mmoja wapo . Alishangaa sana maana hajawahi maishani mwake kuona unywele mzuri kama huo. Akaamuru waja wapo wafanyakazi wake wamtafute mwenye unywele huo.

Haikuwa kazi rahisi. Waliendelea kufanya hivyo kwa siku nyingi. Hatimaye wakampata msichana mwenye unywele ule, ambaye alikuwa ni Doa Jeupe! Alipokuwa akioga, unywele ulitoka. Wakamlete mbele ya mfalme. Afurahi kupita kiasi kumuona amekuwa msichana mzuri aliyeumbika vizuri ajabu. Hatimaye, mfalme akafikiri, kuwa amampata msichana ambaye atakuwa mke wa tatu. Hakuwa na hamu ya kuishi na wake zake wawili.

Bibi kizee kupata habari hizo, akafunga safari kurudi kuja kumtaharisha Doa Jeupe asimwoe yule mfalme ambaye ni babake! Akamweleza ukweli wa mkasa wote toka mwanzo mpaka mwisho. Akasisitiza kwa kumwambia; “Usisahau kuwa, mfalme anataka kukuoa kwa sababu wewe ni mwanamke.

Alipomaliza kusema hayo, bibi kizee akaondoka tena: Doa Jeupe alipata uchungu baada ya kuambiwa ukweli wa visa vya baba yake. Mfalme akarudi kumwomba Doa Jeupe amwoe. Doa Jeupe akamjibu: “Usisahau kuwa, mimi ni mwanamke, kama unavyofahamu wanawake hawana faida. Hufahamu kama wanawake ni hatari? Wanaweza kukuua?
Mfalme akahamaki: “Nani kakuambia upuuzi huo?”
Doa akamwambia: “Babu zangu ndio walioniambia, wewe uliyesafiri karibu ulimwengu wote, umeshawahi kuona mwanamke mzuri kama mimi? Nataka nikueleze kuwa, mimi nimetumwa hapa duniani kuangalia mazuri na mabaya niko tofauti na wanawake wengine!”

Mfalme hakuweza kuelewa lo lote. Akabaki akimuangalia tu. Doa Jeupe akaendelea: “Sikia! Mimi ni Doa Jeupe, yule ambaye miaka mingi iliyopita, ulimwona kama msichana mdogo. Ukasema akikua ungependelea kumwoa. Mimi ni binti wa mke wako wa kwanza. Wewe ambaye uliwaua dada zangu wawili wa kwanza na wa pili mara baada ya kuzaliwa, na kusema kuwa hawana faida kwako, unataka kunioa?

Lazima ufahamu kwamba mimi naishi dunuani leo, kwa sababu mama alinizaa ulipokuwa safarini, kuhofia kwamba na mimi yangenikuta yaliyowatokea dada zangu, akanificha kwa bibi kizee. Hivyo, siwezi kuoana na baba yangu!”

Mfalme akakataa kata kata, kuamini aliyokuwa akisikia akauliza ; “ Unaweza kunihakikishia vipi, kuwa wewe ndio yule msichana niliyemuona miaka mingi iliyopita?” Doa Jeupe alkamwambia : “Muulize mke wako wa kwanza ambaye ni mama yangu naye, atahakikisha!”
Mkewe mfalme akaitwa na akaeleza yote yaliyotokea wakati mumewe yuko safarini. Mfalme akamwuuliza; “Ni kweli kwamba ulizaa mtoto wa kike ukamficha nisimwone?” Mkewe akakubali. Mfalme akaendelea kusema: “Unaweza kunihakikishia kuwa msichana mzuri hivi, ni binti yako?” Mkewe akasema: “Nilimwita Doa Jeupe, sababu alizaliwa na kovu jeupe kwenye goti lake!”

Kila mmoja akawa akimwangalia Doa Jeupe ambaye alikuwa akionyesha lile doa kwenye goti lake! Huo, ulikuwa ushahidi wa kutosha! Mama na mtoto kwa furaha ilioje, wakaangukiana na kukumbatiana, wakimwacha mfalme amejaa aibu tele.

HADITHI HII INAWAKUMBUSHA AKINA BABA WENYE UROHO WA WANAWAKE WA WENZAO, KWAMBA WANAWAKE WAMEZALIWA KAMA WASICHANA WADOGO. HIVYO WASITAMANI VYA WENZAO, VYAO WAKAVICHUKIA.
Hadithi kutoka kwenye kitabu cha HADITHI na via kutoka Tanzania.

6 comments:

Faith S Hilary said...

Nimesoma kila neno ya hii hadithi maana nina weakness ya kusoma vitu vyenye maneno mengi kama hivi ila I managed lol. Hadithi ya kusisimua na vile inafushinda na hio ndio maana ya hadithi...nawaachia "wanaume" uwanja waseme...hehe

Fadhy Mtanga said...

Wanaume awenyewe nd'o sisi? Tusemeni? Hadithi tamu na yenye elimu ya uzamivu katika muktadha wake.
Ni hayo tu!

Anonymous said...

no comment, hadithi nzuri sana na fundisho maridhawa. Lakini tuacheni matani, kuwa na mabint home yataka moyo!!

Albert Kissima said...

Hadithi hii ni nzuri,
inatoa funzo kuwa binadamu wote wanahitaji kuthaminiwa, wanaume kwa wanawake.
Watu wa india kipindi fulani walikuwa na tabia hii ya kutopenda watoto wa kike,kama hali hii bado ipo hadithi hii itawafaa sana.

Bennet said...

Hii hadithi imenikumbusha vitabu vya alfu lela ulela, mule kuna hadithi inataka kufanana na hii kidogo lakini katika maudhui mengine kabisa

Yasinta Ngonyani said...

Candy1, Hii hadithi mwenzako naipenda kweli ingawa inahuzunisha kuna kitu inafunza.

Fadhy ni kweli ni hadithi tamu na ya kusikitisha pia.

Usiye na jina je umejifunza nini? Na asante pia kwa kutembea hapa kibarazani kwangu:-)

Kissima, Natumaini watu wa India wamesoma la sivyo itabidi niwapelekee:-)

Kaka Bennet!
Nashukuru kama hii hadithi imekukumbisha hadithi nyingine.

Ahsanteni sana wote kwa kutochoka kutambelea blog ya MAISHA.