Tuesday, May 28, 2013

TUSISAHAU HADITHI ZETU:- HARUSI YA MASHAKA!!!

Hii ni hadithi ya wanaume wawili. Kazi yao kubwa ilikuwa kulima, pia walikuwa wawindaji wazuri mno.  Wote wawili walikuwa wameoa, na wote walikuwa wambeya. Walikuwa hutaka kujua kila wanachofanya wake zao. Wote walitambua maneno ya zamani: "WANAWAKE SI WATU KAMILI"
Siku moja hawa wanaume walipokwenda kuwinda pamoja, walianza kuizungumza ile methali. Hapo hapa mmoja kati yao alimuambia rafiki yake kuwa yeye angependa kumjaribu mkewe.
Alimuua njiwa na kumkata vipande. Baadaye akaweka vile vipande vya nyama ya huyo njiwa, vilokuwa vikitoka damu, mguuni kwake, na akachukua kitambaa na kuufunga mguu wake, hapo ilionesha kama kaumia mguu, hasa ilivyokuwa damu ikitokeza kwenye hicho kitambaa mguuni kwake.
Walipokaribia nyumbani, alimuomba rafiki yake ambebe mgongoni. Hapo ilioonyesha kama mtu aliyeumia sana.
Baada ya wiki moja hivi, kidonda chake kilikuwa bado kikitisha , na kilikuwa kikinuka kupita kiasi. Huyu bwana alijifanya kuwa hawezi kusimama kabisa. Mkewe alipata kazi zaidi kutokana  na hali ya mumewe. Hili lilikuwa tatizo kubwa kwa mkewe, na aliamua kumkimbia mumewe na kurejea kwa wazee wake. Kabla ya kuondoka alimuomba rafiki yake mumewe amuangalie mumewe. Alipoondoka tu marafiki walikwenda kwenye mto. Hapo mgonjwa akaoga na kuosha nguo zake zilizokuwa chafu.
Mkewe aliondoka siku nyingi. Baada ya muda alisikia kuwa mumewe kapona tena. Hapo alirejea haraka kwa mumewe.
Baada ya mikasa hii yule rafiki mtu naye akataka kujua vipi tabia ya mkewe. Siku moja alijifanya mgonjwa sana, na siku nyingi zilizofuata alikataa kula. Siku moja alimuomba mkewe amtengenezee chakula kizuri, halafu akamwambia ampatie asali kidogo.
Mkewe alifanya kama alivyoomrishwa. Chakula kilipokwisha tu huyu bwana alijifanya kuwa kazimia. Baadaye alijifanya kuwa kufa.. Wakati mkewe akishughulika kujua lililotokea, aliwaza nini la kufanya. "Sijui niite msaada, au sijui nile kwanza?" aliamua kula kwanza.
Wakati alipokuwa akila alikumbuka asali ambayo alisahau kumpa mumewe. Asali ilikuwa kwenye chupa iliyokuwa juu ya kitanda. Alijaribu kuiteremsha  chupa, lakini hakuweza kuifikia.
Hapo ilimbidi amkanyage mumewe mgongoni ili kuifikia hiyo chupa. Alipomaliza tu kula alitumia njia hiyo hiyo kuirejesha hiyo chupa. Baadaye kidogo aliosha sahani na hapo ndio akaanza kulia na kuwaita watu. Watu kijijini walikuja, na kati ya hao alikuwa rafiki yake mpenzi. Rafiki yake alianza hapo hapo matayarisho ya maziko. Ghafla maiti ikapiga chafya: "Aaccha!!" Watu walimkimbilia maiti na kumsaidia. Baadaye watu wote waliondoka wakiwa na furaha.

Hadithi  hii inatufundisha kuwa ikiwa mtu anataka kujua kila kitu cha mwenzako, utavunjika moyo bure....Je? wewe umejifunza kitu hapa? Ni hadithi kutoka kitabu kiitwacho HADITHI NA VISA KUTOKA TANZANIA..TUTAONANA TENA PANAPO MAJALIWA!!!!

2 comments:

ray njau said...

Asante kwa hadithi ndani na hadithi na ndoa inahitaji wawili walioamua kuishi pamoja wa nia moja katika masika na kiangazi.

Yasinta Ngonyani said...

Hadithi hii imenifanya nicheke ...hasa huyu mume anapokubali hadi kunuka....na huyu mke abargubutu kumganyaga mumewe. ..na zaidi mume anajitahidi kujifanya kafa...kaaaaazi kwelikweli