Monday, May 17, 2010

Tatizo la mimba kwa wanafunzi bado ni kubwa

TATIZO la mimba kwa wanafunzi wa shule za msingi na sekondari bado ni kubwa kwa wilaya ya Songea hali ambayo imewafanya wadau wa elimu pamoja na viongozi wa ngazi za juu serikalini akiwemo mkuu wa wilaya ya Songea Thomas Sabaya kuwachukulia hatua kali za kisheria wazazi na wanafunzi waliopatiwa ujauzito kwa kulazimishwa kuwataja watu walio wapatia ujauzito ili waweze kufikishwa katika vyombo vya sheria.

Hali hiyo imechangiwa na tabia ya baadhi ya wazazi kupatana na watu ambao wamewapatia mimba watoto wao kwa kupatiwa fedha na kumalizana nao kinyume na sheria hali ambayo imechangia tatizo la wanafunzi wengi kupewa ujauzito.

Hivi karibuni Makamu wa Rais Dk Ali Mohamed Shein alipofanya ziara mkoani Ruvuma alionyeshwa kuchukizwa na vitendo vya baadhi ya watu ambao wanapita na kuwarubuni wanafunzi na kuwapatia mimba na hivyo kuwafanya washindwe kuendelea na masomo kutokana na ujauzito.

Akiwa wilayani Songea Dk Shein alifanikiwa kuzungumza na wananchi wa kata ya Matogoro Manispaa ya Songea na kuwaeleza jinsi anavyochukizwa na baadhi ya watu ambao wanapita na kuwarubuni wanafunzi na kuwapatia mimba na kuwaonya waache tabia hiyo mara moja kwani serikali haitasita kuwachukulia hatua kali za kisheria.

Dk Shein anasema bado tatizo la mimba ni kubwa katika baadhi ya mikoa na kuwataka viongozi kuwachukulia hatua za kisheria watu ambao wanawakatisha masomo wanafunzi kwa kuwadanganya na kuwapatia ujauzito, hivyo kuwafanya washindwe kuendelea na masomo yao.

"Bado kuna baadhi ya watu wanaendelea kuwarubuni wanafunzi na kuwapatia ujauzito hivyo naomba muendelee kuwashugulikia watu hao na muwafikishe katika vyombo vya sheria ili waweze kuchukuliwa hatua zaidi," anasema Dk Shein.

Pamoja na hayo Makamu wa Rais amevutiwa na jitihada mbali mbali zinazofanywa mkoani Ruvuma hususan wilaya ya Songea ili kuinua kiwango cha elimu katika mkoa wa Ruvuma kwani, wilaya hiyo imefanya vizuri kwa kufanikiwa kutekeleza mpango wa Serikali kwa kata zote kuwa na shule za sekondari ambazo zitachukua wanafunzi na kuna baadhi ya kata zimekuwa na shule zaidi ya mbili.

"Napenda kuwapongeza wabunge Dk Emmanuel Nchimbi na mwenziwe Jenista Mhagama kwa jitihada kubwa walizofanya katika kushughulikia kuinua elimu katika wilaya hii , wamefanya kazi kubwa na wanastahili pongezi ambapo Dk Nchimbi pekee amechangia Bati 5,096,kofia za bati 2,050,fedha taslimu milioni 13 na misumari kilo 87 vyote vikiwa na thamani ya shilingi milioni 103," anasema Dk Shein.

Dk Shein amewataka wanafunzi kuwaheshimu wazazi wao na kujali masomo kwa kusoma kwa bidii na kufata yale mema ambayo wanaelekezwa na wazazi wao ili waweze kufikia ndoto zao za baadaye badala ya kukubali kurubuniwa na wanaume ambao wanania mbaya ya kuwakatisha masomo.

Aidha ameahidi kuwa serikali itaendelea kuzisaidia shule hizo kutatua changamoto mbali mbali zinazowakabili ikiwemo ya upungufu wa nyumba za walimu, madawati, maabara, pamoja na walimu.



Akitoa taarifa ya Wilaya ya Songea kwa Makamu wa Rais, Mkuu wa Wilaya ya Songea Thomas Sabaya alisema katika kipindi cha mwaka 2008 wanafunzi 128 wa shule za sekondari walipata mimba na mwaka 2009 wanafunzi 73 walipata ujauzito na kukatisha masomo yao. ambapo katika kipindi hicho hicho wanafunzi 45 wa shule ya msingi nao walipata ujauzito ingawa tatizo hilo limepungua ambapo mwaka 2009 wanafunzi waliopata mimba ni 16 wilaya nzima.

Amesema, tayari mikakati mbali mbali ya kuthibiti mimba kwa wanafunzi imefanywa ambapo wilaya imewapeleka wanafunzi na wazazi mahakamani ili wawataje watuhumiwa hatua ambayo imesaidia baada ya watuhumiwa 25 kuadhibiwa.

Aidha, wilaya imeanzisha utaratibu wa upimaji mimba kwa wanafunzi kila baada ya miezi mitatu hali ambayo imesaidia kupunguza mimba mashuleni.

Na Joyce Joliga wa Gazeti la Mwananchi

11 comments:

Bennet said...

Hii huchangiwa zaidi na umasikini ndio maana wanafunzi wa kike wengi wao inakuwa rahisi kurubuniwa na wanaume wakware kisha wakaingia kwenye mapenzi tena yasiyo salama na mwisho wake ndio wanapewa mimba na ukimwi juu yake.

kwa hili serekali yetu inabidi ijipange sana, kuna baadhi ya njia kama kuwa na shule za bweni ambazo zina ulinzi wa kutosha

Unknown said...

Mbali na umaskini wa wananchi, pia utendaji mbovu wa serikali na ufuatiliaji duni wa sheria ambazo tayari zipo kwa kutoa adhabu kali kwa wakware ni sababu pia. Wengi wakishajua adhabu ni kali na zitafuatiliwa vitendo hivi vitapungua.

Simon said...

serikali ndio hasa inatakiwa kuwajibika kutokana na tatizo hili la mimba kwa wanafunzi wa kike.Laiti sheria zingekuwa zinafanya kazi ipasavyo.Pia wazazi nao wanahitajika kuwaelimisha watoto wao umuhimu wa shule na sio starehe,Vitoto vya shule vya kike navyo vinapenda sana dezo dezo kumbe havijui kuwa vita pay the price.

Yasinta Ngonyani said...

Naweza nikakubaliana kidogo kuwa umaskini unachangia swala hili. Lakini hivi wanaume hawana macho kuona ni watoto wa shule? Na kama wanataka basi kwa nini kuwapa mimba? kwanini wasifanye mapenzi salama?
Pia kuhusu serikali ndio, wao wanawajibika 100% kabisa. Ni kweli inahitajika wlimu mashuleni. Lakini pia kama wanaume wanajua wasichana hao ni wananfunzi kwa nini kuvunja sheria au niseme kwanini kuwatamani na kuwadanganya na vitu vizuri. Hivi wanaume hawafikirii huyo binti angeweza kuwa binti yae? je? wewe/wanaume ungeona raha bintiyo siku moja anarudishwa nyumbani kapata mimba na baba mwenye familia? ngoja niache maana naona hasira zinapanda hapa.....

Anonymous said...

wanaume ndio wanaowadanganya wasichana wadogo,inachotakiwa wahusika wasimamie sheria kisawasawa.hakuna kuwaonea huruma,mbona wao wanaharibu maisha ya wasichana masikini,tupa jela iwe kundisho kwa wengine

Anonymous said...

wanaume ndio wanaowadanganya wasichana wadogo,inachotakiwa wahusika wasimamie sheria kisawasawa.hakuna kuwaonea huruma,mbona wao wanaharibu maisha ya wasichana masikini,tupa jela iwe kundisho kwa wengine

Upepo Mwanana said...

Viongozi wa serikali tena mazee ndio ya kwanza kutafuta dogodogo, halafu hayo hayo unayaambia yahamasishe watu kuacha ulaghai, yaani ni sawa na kumpa simba mwenye njaa mwana kondoo

Mija Shija Sayi said...

Ishu hii ni ngumu, nakubaliana na upepo mwanana kabisa, viongozi badala ya kukemea ndio wanachochea.

Kakangu Bennet, shule za bweni hataziwe na ulinzi gani haitasaidia maana waalimu na wapishi huwa ni kazi yao kuwalaghai wanafunzi kwa mikate na chakula cha nyumbani. Nimesoma boarding nimeona hilo, mwanafunzi anamkubali mwl kwa sababu atakuwa anaweza kwenda nyumbani kwa mwl na kula atakavyo, anamkubali mpishi kwa vile mpishi atakuwa anampa shea kubwa ya mikate na anakuwa haishiwi sukari. Matokeo yake mimba. Nakumbuka tulipokuwa form four wiki moja kabla ya kufanya mitihani ya taifa dada mmoja alijifungulia bwenini na kwa kiwewe akaanza kukimbia huku na huko huku kamkamatia mtoto chinichini maana alikuwa hajakatwa kitovu. Cha kujiuliza binti huyo alifikishaje miezi tisa bila waalimu na nesi kujua?
Ndiyo hapo ujue uzembe upo kila mahali.

Mimi ninachoona cha muhimu ni kuwa karibu na watoto wetu na kuwafundisha kujisimamia wenyewe vizuri bila kutegemea misaada ya pembeni. Tukiwapa msingi mzuri hata kudanganyika kwa mikate, chakula na vipesa inakuwa ni ngumu.

Mheshimiwa mbunge Yasinta naomba kuwasilisha.

Yasinta Ngonyani said...

Nikiwa kama mheshimiwa mbunge kama Da Mija alivyosema nakubaliana kabisa nawe yaani msingi wa mafunzo uanze nyumbani kwa sisi wazazi. Mija hiyo habari ya kuzalie bwenini duh! sijui walimu na manesi walikuwa wapi?

Mfundishi said...

Tunaendelea kufanya makosa, tunafikiri elimu hutolewa shuleni na kusahau watu wasio katika mikondo rasmi. Mzazi anawezaje kutoa elimu (ya malezi) ambayo huna? tuwarudishe watu wetu madarasani, wasome (kisomo cha watu wazima), kuwe na mipango kabambe ya kuelimisha. Mzazi akiwa na elimu (hasa afya ya uzazi) tosha hasa akina mama watoto nao watakuwa na elimu. Kupata mimba za mapema ni heri, lakini vvu tutakemeaje?

o'Wambura Ng'wanambiti! said...

na hao madada kukubali wakishashawishiwa inahusu?

Kwani akikataa itakuwaje? Tusiwalaumu wababa/wakaka na wadada nao wana 50% yao ya ushiriki :-(