Tuesday, December 16, 2008

KAPULYA MDADISI+(YASINTA MDADISI) =MAISHA

Mwenzenu nimekuwa nimeitafuta hadithi hii muda mrefu sana kwani nakumbuka niliisoma shule ya msingi . Sababu kubwa ya kuitafuta ni kwamba watu wengi wamekuwa wakinipachika majini kutokana na udadisi wangu , wengine wananiita mdadisi, maswali magumu, dada mwenye nguvu, na wengine Kapulya ndio maana naiandika leo. Nadhani wengi tunaikumbuka sana hadithi hii:-

Mzee Mwembe alikuwa mwenye nguvu nyingi na hodari sana wa kufanya kazi za mikono. Aliishi katika kijiji cha mdulo, Wilaya ya Rungwe.

Siku moja baada ya shughuli nyingi za mchana kutwa, Mzee Mwembe alijipumzisha kivulini huku akibugia bwimbwi la mahindi. Karibu naye alikuwepo Kapulya, mtoto wake wa kiume wa kwanza. Kapulya alikuwa mdadisi sana alipenda sana kuuliza maswali. Baba yake alimpenda kwa kuwa maswali yake yalikuwa na busara. Alipomwona baba yake awtulia, kamwuliza, “Baba, babu zetu waliwezaje kuishi na kupata chakula chao bila majembe, mikuki, mapanga na miundu?” Tatizo hili lilikuwa likimsumbua sana kichwani mwake kwa sababu alikwisha sikia kwamba vifaa hivi havikuwepo siku za kale. Mzee Mwembe akachukua bilauri ya maji akayanywa na huku akimsikiliza sana mwanawe. Baada ya kukohoa mara mbili hivi akamweleza, akisema, “siku hizi tunasikia katika mikutano ya siasa maneno mengi sana. Kwa mfano, mawazo ya kujitegemea yanatufundisha tusiwe wanyonyaji au makupe. Katika kujitegemea yatupasa kufikiri na kuvumbua vitu vyetu wenyewe ili kuyafanya maisha yetu yawe rahisi. Hivi ndivyo wazee wetu wa zamani walivyoishi. Pengine utasema kuwa maisha yao yalikuwa magumu lakini wao waliyafurahia. Kila kitu walikipata kwa kukifanyia kazi. Mtu goigoi na mnyonge aliishi kwa taabu na dhiki. Hii yote ilisababishwa na uhaba wa vifaa bora vya kufanyia kazi. Hapakuwepo na majembe, miundu, wala mikuki iliyotengenezwa kwa chuma kama ilivyo sasa. Hata hivyo kila mtu mwanaume aliweza kujitegemea kwa kutumia vifaa vyake vya kumsaidia kuendeshea maisha yake. Ilibidi kutengeneza vifaa hivi kwa kutumia miti. Miti yenyewe ilikuwa ni ile iliyochaguliwa maalum kwa kazi hii. Miti iliyokuwa inafaa ilikuwa ni ile iliyoweza kudumu muda mrefu bila kuharibika.

Matumizi ya vifaa hivi yalikuwa ya aina nyingi. Watu walitumia mikuki kwa kuwindia na kama kinga yao wakati wa safari. Majembe yalitumika kwa kazi ya kulimia na mashoka yalitumika kwa kupasulia kuni”

Kapulya alivutwa sana na maelezo hayo. Akabaki akimsikilza baba yake kwa makini sana. Mzee Mwembe hakukomea hapo, bali aliendelea kusimulia kwamba watu wa zamani walikuwa na tabia nzuri sana. Baadhi ya vitu vingi walivyogundua walivitoa vitumike kwa faida ya wote. Kwa njia hii maarifa ya uvumbuzi yaliendelezwa vizazi hadi vizazi. Kwa kutumia maarifa ya vizazi vilivyotangulia nasi pia tunaweza kuvumbua vitu vipya. Hivyo maisha ya binadamu huendelea kuwa bora na yenye manufaa.

Kapulya alipenda kujua pia jinsi watu wa kale walivyopata moto kwa kupikia vyakula vyao. Alikwisha sikia kuwa hawakuwa na mitambo ya kutengeneza vibiriti kama tuliyo nayo sasa. Hapo Mzee Mwembe hakutaka kmweleza kwa maneno tu. Akamwambia, “Chukua hicho kijiti kilicho hapo nyumba yako. Kichonge kidogo kwa kisu mpaka kipate uso uliosawazika.” Kapulya akafanya kama alivyoagizwa.

Kisha Mzee Mwembe aliendelea kusema. “Sasa tafuta kijiti kingine chenye unene wa kidole chako cha mkono. Halafu kikate kiwe na urefu wa kutosha. Baada ya Kapulya kukusanya vitu hivi Mzee Mwembe akamwelekeza atengeneze kijishimo karibu na ncha ya kile kijiti cha kwanza. Akafanya hivyo. Kisha baba yake akamwambia, “Sasa chukua kijiti chenye kishimo na kiweke juu ya majani makavu yaliyo laini.” Halafu baba yake alimwambia apekeche kile kijiti katika kile kishimo. Akafanya hivyo kwa nguvu sana. Basi akaona vumbi lenye moto sana likianguka juu ya yale majani makavu. Hapo aliona moshi ukitoka. Akazidi kupekecha kwa nguvu zaidi. Baba yake akamwambia, “Sasa chukua hayo majani yanayotoka moshi. Yapulize taratibu.” Akafanya hivyo na mara akaona moto ukiwaka Kapulya akawa amagundua njia ya kupatia moto. Uso wake uliwaka kwa furaha. Akaongeza majani. Halafu alichochea kuni ndogo ndogo na mwishowe akaongeza kuni kubwa. Akakata mahindi akayachoma.

Kwa njia hii ya kuuliza maswali na kwa tabia yake ya kujaribu kugundua vitu vipya Kapulya amejifunza mambo mbalimbali. Haoni haya kuuliza maswali kwa sababu anajua ya kuwa “kuuliza si ujinga.”

SWALI langu kwa ninyi mlionipachika hayo majina:- Je kweli nastahahili kuitwa hayo na kweli nipo sawa na Kapulya? Ni hilo tu.

9 comments:

Simon Kitururu said...

@Yasinta.Kwa bahati mbaya au nzuri mimi sikuuliza hilo swali. Lakini kutokana na kukusoma hapa kijiweni najua wewe ni mdadisi na maswali yako ni magumu kuliko ya KAPULYA.Wewe hauko sawa na Kapulya ukiniuliza mimi. Wewe ni Yasinta! Kuuliza si ujinga lakini! Wewe unafikiri uko sawa na Kapulya?

Christian Bwaya said...

Mie napita tu jamani nilikuja kuchota mawazo humu ndani....!

Uwezo wa Yasinta naukubali. Hongera dada.

Unknown said...

NA KWELI NAUNGANA NA BWANA KITURURU, KUSEMA KWELI DADA YASINTA WEWE NI ZAIDI YA KAPULYA!!!!

MARKUS MPANGALA said...

Aaaaah ha ha ha ha ngoja nicheke kwanza, halafu nipumue huuuuuuuuuuuuu oooooohh okkkkkk. nilikuwa nangojea falsafa za kaka Simon sasa nimezipata lakini hata kaka Sahaban sijui kama umeipata vema hii falsafa yake ninukuu "wewe hauko sawa na KAPULYA ukiniuliza mimi. Wewe ni Yasinta! kuuliza si ujinga lakini! Wewe unafikiri uko sawa na Kapulya"? duuuh Mkuu Kitururu wewe ni mwanafalsafani, hii falsafa sijui wenzangu mmeielewa vema. sifafanui tafakarini wenyewe. NDIYO aliyembatiza jina la MASWALI MAGUMU ni mimi mnyasa tena sana nikasema duuuh dada Yasinta wewe unakuwa kama kaka Ansbert Ngurumo kwa maswali yako maana much respect huyu kaka. Lakini nimesoma kisa hiki na kukikumbuka nikasema Kapulya ni yeye na Yasinta ni yeye kila mmoja ana umahiri wake lakini kila mmoja atabaki na umahiri wake vinginevyo turudi katika falsafa za kaka Simon hapo hebu someni kwa undani halafu pasueni vichwa mpate majibu. hakuna ubishi Yasinta ni mwisho wa Reli kwa maswali ukikasirika poa tu mkubwa wangu haina noma. ila unauliza kwa nia njema tu kama Kapulya lakini je Yasinta ni nani na Kapulya ni nani. jibu analo kaka Simon hapo someni

Fadhy Mtanga said...

Niseme kitu?
Lakini wakubwa zangu,
wamesema yote.
Msisitizo unaruhusiwa? Tufanye jibu liwe ndiyo.
We ni zaidi ya Kapulya.
Si ndiyo hapo?
Sasa je?
Unastahili pongezi.
Nani anabisha?
Ajitokeze,
Nasi tumwone!

Unastahili sana,
Hizo pongezi.
Wala si urongo!

Nimemaliza,
Kusema
Niliyonayo,
Kwa leo.

Yasinta Ngonyani said...

Asanteni sana kaka zangu kwa maoni yenu mazuri. Ila nawaomba msifikiri ya kwamba niliandika hii hadithi au hilo swali Kwa sababu ya kutaka SIFA. Hapana sina tabia hiyo:- Karibuni tene na tena ktk kijiji hiki cha Ruhuwiko

MARKUS MPANGALA said...

haaa kumbe jibu NDIYO weweeee nimeshinda alah kumbe ni mimi au Yasinta. lakini hitimisho lanipa simanzi looo kumbe nina furahia hata gego linaonekana kwaheriii wakuu

Vimax Asli said...

i like this blog, thanks you

Anonymous said...

Kapulya naye kwa kipindi hicho alitupa hamasa sana ya kupenda kujua uhalisia wa maisha kuto ogopa kutaka kujua vitu, ahsante sana kwa tukumbusha matini hii ama kwa hakika wewe na kapulya ni sawa kabisa.