Wednesday, October 6, 2010

WANANDOA NA KAULI HIZI: HATA VIKOMBE KABATINI HUGONGANA, ITAKUWA SIE?

Ndugu wasomaji, Habari hii nilishawahi kuivuka hapa MAISHA NA MAFANIKIO. Binafsi imenivutia sana na nimeona tuirudie tena kwani KURUDIA KITU ni KUJIFUNZA ZAIDI. KARIBUNI UNGANENI NAMI.
------------------------------------------------------------------------------------------------

Je unadhani au kuamini kwamba kuna ndoa ambazo wanandoa wake hawagombani kabisa? Kama unaamini hivyo, basi unajidanganya na labda unaishi katika dunia ya peke yako.

Ni jambo lenye ukweli wa kutosha kabisa kwamba wanandoa wote duniani hutokea kugombana, lakini kugombana huko hutokana na migongano au mizozo ya muda tu ambayo huweza kutatuliwa na pande mbili kama wakiamua kufanya hivyo.

Wewe unayesoma hapa, napenda kukuambia ukweli kwamba usiogope migogoro ya ndoa, kwani hicho ni kitu ambacho kamwe huwezi kukiepuka. Kuna msemo mmoja unatumika sana huko nyumbani usemao, " hata vikombe kabatini hugongana itakuwa wana ndoa?" Hii ina maana gani, ina maana kwamba haiwezekani watu kuishi pamoja halafu msiwe mnatofautiana, na kama ukiona hivyo, jua kwamba hiyo ndoa si salama kwani siku yoyote bomu litapasuka na madhara yake yatakuwa ni makubwa kuliko kawaida.

Kuna watu ambao hata kama wamekosewa na wenzi wao hunyamaza kimya na kumeza hasira zao, wengine huogopa kuwakabili wenzi wao na kuzungumzia jambo linalowakera kwa kuhofia kuonekana kama wana kasoro au ghubu. Jambo hili ni hatari sana.

Kumkabili mwenzi wako na kumwambia hisia zako kama amekukosea au amekwenda kinyume na matarajio yako ni jambao la maana sana katika kudumisha uhusiano. Lakini naomba nitahadharishe kwamba, ni vyema kufanya hivyo bila kumshusha, kubeza au kusimanga kwani hiyo sio dalili nzuri ya upendo.

Inashauriwa kwamba wanandoa au wapenzi wanapokwaruzana inabidi wajadili tofauti zao bila kusigishana, kila mmoja akitaka kuwa mshindi, hiyo haitasaidia kuimarisha ndoa bali itaongeza tatizo. Ni vyema upande unaohusika na tatizo, uwajibike na kuomba radhi kwa ustawi wa ndoa, huo ndio ukomavu.

Kutojadili mgogoro kwa wanandoa na kuupatia ufumbuzi wa tatizo huwafanya wandoa kuwa mbali kihisia, na athari zake ni kuwakuta wanandoa wakiwa wageni wa kila mmoja kwa mwenzake, yaani hakuna mawasiliano, kila mtu na lwake.

Jambo la msingi kwa wanandoa ni kujadili tofauti zao pindi linapojitokeza jambo linalomkera mmoja wa wanandoa, kwani hakuna jambo linaloweza kujitatua lenyewe bila kutatuliwa na wandoa husika. Kuacha jambo lolote bila kulitafutia suluhu ni sawa na kutega bomu, ambapo siku likilipuka madhara yake ni makubwa sana.

Unaweza kukuta mwanandoa anakereka na mambo madogo madogo ya mwenzi wake lakini hasemi, ingawa yanamkera kupita kiasi akitegemea huyo mwenzi wake atajua na kuacha, thubutu…..inapotokea siku yeye amekosa jambo dogo tu na huyo mwenzi wake akamsema, basi atatumia fursa hiyo kuanza kujibu mapigo kwa kueleza yale yanayomkera kutoka kwa mwenzi wake, na hapo itakuwa kila mtu anavutia kwake kama mwamba ngoma………na aamini nawaambia kuwa kamwe hawezi kupatikana mshindi katika jambo hilo, kwani mjadala huo unaweza kutoka nje ya mada kila mmoja akijitahidi kutafuta makosa ya mwenzi wake hata yale yaliyotokea wakati wa uchumba wenu ili mradi vurugu tupu.

Inatakiwa wanandoa wajadili kila jambo linalojitokeza hadi kulipatia suluhu, vinginevyo ni kuichimbia ndoa yenu kaburi la mapema. Wakati mwingine unaweza kukuta mwanamke analalamika juu ya kutoridhishwa kwake na matumizi ya mumewe, na hapo mume naye ataanza kukumbusha juu ya matumizi yasiyo ya lazima yaliyofanywa na mke huko nyuma. Mke naye hataridhika atakumbushia jambo lingine na lingine hadi hata mada iliyokuwa ikijadiliwa inasahaulika.

Jambo lingine ni kujumuisha mambo, matumizi ya maneno kama, mara nyingi, kila wakati au mara kwa mara si mazuri sana. Unaweza kukuta mtu mwenzi wake amekosea jambo halafu mwenzie anamwambia “Kila mara huwa unafanya hivi” au mara nyingi huwa unafanya hivyo…..Hii ni hatari kwa ustawi wa wanandoa, kwani kwa kujumuisha ni sawa na kumwambia mwenzi wako kuwa kila mara yeye ndiye mkosaji.

Kwa haya niliyoyaeleza hapa sina maana kwamba huu ndio muarobaini pekee wa kuimarisha mahusiano kwa wanandoa, bali ni moja ya mambo muhimu kati ya mengi ambayo yakizingatiwa na wanandoa wote basi ndoa yao itakuwa imara Tujadili pamoja………..

Na hapa yalikuwa maoni ya baadhi ya wasomaji......

James Adolwa said...
Kweli unavyosema kuwa maranyingi mzozo ukidhihirika ni kwasababu kuna kero lililo fichika ama kufunikiwa. Swala lingine ambalo watu wanatakikana kuzingatia....wacha nitumie kiingereza kidogo....One needs to consider what one keeps steaming under the lid of the cooking pot. If you spend your time and energy focusing on the weaknesses or faults of another then all that you will see in the other person are weaknesses and faults...and you will end up cooking up a foul tasting broth that will spill over and put out the flame of your relationship.

Instead try and focus on the strengths and virtues of your partner and in the end you will find that you keep seeing more and more good things. This is not to say that all the experiences will be pleasant but rather all the bitter, sweet, sour and salty experiences work out together such that the sum total ; the big picture, the essence of the whole experience works out to be a pleasant experience for both. I am no expert but these are the thoughts that flowed from my soul.

October 12, 2009 8:34 PM
Ramson said...
Dada yangu hapo umenena, kaka James, naona imebidi kuandikwa kwa kiingereza ili kuweka msisistizo....kaaaazi kweli kweli.

Dada Yasinta hili ni darasa tosha kwa wale wanandoa ambao hawakubahatika kujifunza namna ya kutatua migogogro ya ndani katika uwanja ulio sawa. Unajua wazee wetu walipokuwa wakituambia kuwa ndoa ni kuvumiliana wengi walitafsiri vibaya, walijua kuwa ni kumeza hasira zetu pindi tunapokosewa na hii ilitumiwa vibaya zaidi na wanawake, lakini siwalaumu bali mfumo dume ndio uliowafundisha.......
Inaposemwa kuwa ndoa ni kuvumiliana maana yake ni kujadiliana kwa uwazi pale tatizo au kunapozuka kutoelewana juu ya jambo fulani na uzingativu uwekwe kwenye kutatua tatizo sio kubishana kwa ajili ya kumtafuta mkosaji. Tumelelewa katika familia tofauti, kuna baadhi ya wanume wamefundishwa kuwa hawapaswi kuwaomba wake zao radhi hata kama wamekosa,,,,,inabidi mke awe makini kama akishajua kuwa mumewe ni wa aina hiyo.....


Anonymous said...
Darsa hilo Yasinta, safi sana, umemaliza yote hata cha kuongeza sina kwa leo labda kifupi sana wanasema katika maandiko matakatifu kwamba "upendo huvumilia, hauhesabu mabaya na kadhalika..." basi kama tafsiri sahihi ya upendo ikiwepo miongoni mwa wana ndoa basi mchezo umeisha, du ni hivi jioni hii nilikuwa nasikiliza kipindi cha maridhiano kupitia redio Maria Tanzania du, niliyoyasikia huko yanatisha kisa kusaka mtoto sijui ujiko kwa mwanaume! na kisa kingine kilikuwa wiki iliyopita ambapo mwanaume alienda kuazima dume ili limzalishie watoto, huko kote mwanamke alikuwa anashinikizwa lazima afanye mapenzi na hilo beberu!!

SIMON KITURURU said...
Bomba la somo hili Dada Yasinta!

Lakini sijui kwanini huu msemo wa kuwa Vikombe hugongana kabatini huwa na wasiwasi nao kwa kuwa nashindwa kuwa na uhakika kuwa kihalihalisi labda VIKOMBE hugonganishwa na HAVIGONGANI tu kienyeji ndani ya KABATI.


Anonymous said...
My sista unanikuna jamani hilo ni kweli my sista kwani kila mtu kalelea kivyake na malezi yake just meet with her /him ukubwani ni lazima kuwe na migongano ya hapa na pale nduguyo tu mwajibizana sembuse mtu baki ooh please Kaka Simon Kitururu kwani utakuta wewe ukisusa wenzio wanakula food yote lkn familia nyingine ukisusa watu hawali mpaka ujongee mezani,Kuna wengine hata hajui kumheshimu dadaake or kakaake yote ni malezi hp umeelewa brother from anaother mother meanz ya vikombe kugongana ni misemo ya mafumbo ya mababu zetu soo Open ya Eyes oky!!!!

chib said...
Big up Kitururu, huwa naupinga msemo huo wa vikombe kabatini kugongangana, ukweli kama kabati imetulia, vitagongana vipi, ni wale wenye mafujo tu ndio huvigonganisha, au kama unakaa Sumatra ambako matetemeko ya ardhi hayaishi, hapo ndio vitagonganishwa na tetemeko. Ypte kwa yote, somo hilo ni zuri kabisa kwa watu wote wenye ndoa na watarajiwa.

SIMON KITURURU said...
@Anony: nankunukuuu ``ooh please Kaka Simon Kitururu kwani utakuta wewe ukisusa wenzio wanakula food yote......''

Hapo si kunauwezekano kiwagonganishacho ni FUDI?:-)

Nimekuelewa lakini MKUU na pointi yako nimeipata.

@MKUU CHIB: Hapo kwa mtazamo wangu umemaliza NUKTA


Markus Mpangala said...
Ni MSARAGAMBO hapo

Yasinta Ngonyani said...
Nachukua nafasi hii kuwashukuruni wote kwa maoni yenu kwani huku ndio kujifunza. Maana kila mtu anajifunza toka kwa mwingine. Ila sifungi mjadala karibuni kujadili zaidi

1 comment:

emu-three said...

Wanasema migogoro katika ndoa ndiyo inayojenga ndoa kuwa imara kwa wenye kuelewa. Lakini wengine wanapokutana na migogoro hiyo wanakosa subira na kuishia kuachana, sio vyema kabisa!
Wanandoa wengi wanaridhika kwa kuwa ndoani, lakini hawataki kuiboresha ndoa yao kwa kujifunza, kutafuta na kuelekezana yale yatakayojenga ndoa ndoa yao. Hili ni tatizo pia, kama vitu vingine ni lazima kila mara kutafuta vitu gani vipya vya kuongezea ili ndoa isichuje!
Umri unapokwenda wengi husema aaah, sasa kuna nini tena, tukae tusubiri wajukuu basi, hapana, ndoa kila hatua inahitaji iuboreshai wake, ili kukwepa migongano. Jifunze kwanini ikifika umri fulani hali za kimwili zinabadilika, je hakuna jinsi ya kuiweka hiyo hali kama mwanzo...ipo jamani, someni na ulizeni wajuzi watawaelekeza.
Migongano katika ndoa itakwepwa pale wanandoa wenyewe watakapoichukulia ndoa kama kituu muhimu sana katika maisha yao na kama ni kitu muhimu, basi kipewe kipa umbele, kwa kutafuta kila namna ya kuiboresha. Kukwazana iwe chachu ya kuiboresha ndoa na isiwe kisingizio cha kuivunja ndoa!