Monday, August 8, 2016

KUANZA KUPOTEA KWA DESTURI YA UKARIBU WA KIFAMILIA KUNAVYOATHIRI MALEZI

Malezi katika mazingira yetu ya ki-Afrika ni suala nyeti. Kwa kutambua umuhimu wa malezi katika kujenga jamii yenye ustawi, wa-Afrika tumekuwa na desturi ya kuelekeza nguvu zetu nyingi katika malezi ya wanetu. Kwa mfano, tangu mtoto anazaliwa, ilikuwa ni lazima alale kitanda kimoja na wazazi wake kwa muda unaozidi miaka miwili. Mtoto mchanga hakuachwa alale kwenye kitanda chake mapema kwa sababu za msingi zilizokubalika katika jamii zetu.


MAMA AKIWA KAMBEBA MWANAE
Aidha, mtoto daima alikulia mikononi mwa watu wazima aliowafahamu vyema. Watu hawa ama aliishi nao kwenye boma la wazazi wake au walitoka miongoni mwa jamaa inayomzunguka. Muda mwingi mtoto alibebwa mgongoni kwa mama yake au dada zake. Desturi ya kubeba watoto mgongoni ilifanya suala la ukuaji wa mtoto kufuatiliwa kwa karibu sana na imethibitika kisayansi kusaidia kujenga muunganiko wa kihisia kati ya mzazi na mtoto. Jambo hili, hata hivyo, halieleweki kwa wageni wa bara hili wanaodhani ni aina nyinine ya udhalilishaji wa mtoto.

Chakula cha pamoja ni kitamu sana

Wakati wa jioni, familia zilikuwa na desturi ya watoto kukaa na wazazi wao kijinsia. Baba aliota moto na watoto wa kiume akiwasimulia mambo mbalimbali ya kimaisha. Kadhalika, mama naye alifanya kazi za jikoni kwa ushirikiano wa karibu na watoto wa kike. Chakula kilipokuwa tayari kililiwa kwa ushirikiano. Muda wa chakula ulifahamika, na kwa kweli, kila mtoto aliwajibika kuwepo kupata chakula. Kwa kuwa chombo kilichotumika kulia chakula mara nyingi kilikuwa kimoja basi kila mmoja katika familia alilamizika kula kwa ushirikiano na wenzake.

Desturi hii ya kukaa karibu na watoto na kufanya mambo mengi kwa pamoja iliwasaidia wazazi kuwafundisha watoto maarifa na ujuzi wa aina mbalimbali. Vile vile, ukaribu huu ulikuza uhusiano wa karibu wa kifamilia. Kadhalika, karibu huu uliwahakikishia watoto usalama wao. Kisaikolojia walijua hawana wasiwasi kwa sababu baba na mama wapo na wangepigana na yeyote anayetishia usalama wao. Watoto waliwategemea wazazi wao.

Upo ushahidi wa kiutafiti kwamba kutegemewa kwa mzazi ni nguzo kuu ya malezi. Kwamba mtoto huiga mengi wa mzazi ikiwa anaamini mzazi huyo ni wa kutegemewa na yuko upande wake. Hali hii ilimfanya mtoto asiwe na wasiwasi na usalama wake pale yalipojitokeza mazingira ya kutengana kimwili na kwa hivyo wazazi kwa kweli hawakulazimika kuwa na watoto muda wote. Kama tutakavyoona katika mfululizo huu, hali hii ya mtoto kumwamini na kujisikia salama mikononi mwa mzazi inategemea sana uwepo endelevu wa mzazi kimwili na kihisia tangu siku za mwanzo za maisha ya mtoto.

Hata hivyo, kadri mwanadamu anavyozidi ‘kuendelea’ na ‘kustaarabika’, ndivyo desturi hii ya kupatikana kwa wazazi nyumbani inavyozidi kukosa umaarufu. Kwa mfano, ipo dhana inajengeka katika jamii kwamba maendeleo halisi ni vitu. Matokeo ya imani hii ni kutufanya tutumie muda mwingi ‘kuhusiana na vitu’ zaidi kwa gharama ya mahusiano na ustawi wa familia zetu.

Kadhalika, zipo changamoto nyingine za kijamii zinazotishia desturi ya familia. Kuna masuala kama kazi/ajira zinazowatenganisha wazazi na familia, misukosuko ya kimahusiano inayozaa talaka na/ama kulazimisha malezi ya mzazi mmoja, ujio wa shule za bweni kwa watoto wadogo pamoja na matatizo kadha wa kadha yanayofanya watoto wadogo wakue katika mazingira magumu yasiyo na uangalizi mzuri. Haya tutayaangalia wakati wake ukifika.

Kwa hiyo, ili kukabiliana na changamoto hizi mpya, upo umuhimu mkubwa wa kujadili tafiti zilizochunguza athari za mazingira haya mapya ya kimalezi ambayo kwa kiasi kikubwa hayakuwepo huko nyuma. Kwa mhutasari, tunaweza kutaja suala kuu linalojitokeza kwa haraka. Kwamba uhusiano kati ya mzazi na mtoto unaathiri mahusiano ya mtoto huyo na watu wengine. 

2 comments:

Nicky Mwangoka said...

Nimependa sana makala hii dada. Kweli maisha asilia ni mazuri sana na misingi yake ni mema daima, ila nasikitika yanapotea sasa kutokana na kukumbatia utandawazi

Yasinta Ngonyani said...

Kaka Mwangoka! Tupo pamoja, kwa kweli naungana nawe kwa masikitiko makubwa sana maana huwa nashangaa sana pale nionapo haya mabadiliko napatwa na hasira sana kuona watu wanaokataa utamaduni wao....aahhh wacha niache maana nahisi hasira zaidi...