Tuesday, August 23, 2016

SENENE NI WADUDU WANAOTUMIKA SANA NA KABILA LA WAHAYA MKOANI KAGERA KAMA KITOWEO.....

Senene (Ensenene, kwa Kihaya) ni miongoni mwa wadudu wanaotumiwa sana na kabila la Wahaya mkoani Kagera kama kitoweo, pengine kuliko kabila lolote tangu enzi za mababu.
Pamoja na wadudu hao kuheshimika katika kabila la Wahaya, historia kamili ya asili ya wadudu hao bado haijulikani.
Mwanzoni senene waliliwa na wanaume peke yake. Wanawake walionywa wawe na haya siku zote na wasivunje mwiko kwa kula senene na vitu vyote vilivyokatazwa. Wanawake wote walikuwa na utii wakiheshimu mila na desturi za kabila lao hivyo kutokana na haya hiyo waliitwa “WAHAYA”. 
Wasichana walipeleka zawadi ya senene kwa wachumba wao kama ishara ya kuonyesha upendo na utayari wa kuolewa na mchumba huyo. Msichana ambaye hakufanya hivyo uwezekano wa kuolewa na mchumba wake ulikuwa mdogo, hivyo senene walitumika kama ishara ya upendo na uaminifu.
Zipo aina nyingi za senene lakini wale wanaozungumziwa hapa wamegawanyika katika kundi lijulikanalo kama Orthopterous. Hawa ni jamii ya panzi wapole ambao hawana tabia ya kuharibu na kuteketeza makazi yao kwa chakula kama walivyo nzige wengine. Senene huzaliana kwa wingi katika mwambao wa maziwa makuu baada ya kutaga mayai yao ardhini kipindi cha kiangazi.
Baada ya kutaga mayai na kuangua mzunguko wa maisha yao huishia kati ya mwezi Oktoba na Desemba ambapo kipindi hiki huwa ni msimu wa mvua za vuli zijulikanazo kwa wahaya kama Omusenene. Hiki ni kipindi ambacho senene huruka wakiwa katika makundi wakihitimisha safari ya maisha yao.
Pamoja na kutumika kama kitoweo pia jamii imeanza kufaidika na senene kama chanzo cha kujipatia kipato, jambo ambalo limeufanya mkoa wa Kagera hasa Bukoba kujulikana sana kitaifa na kimataifa, pia kutokana na uchunguzi wa madaktari imeonekana kuwa senene wanaongeza vitamin “C”