Monday, October 8, 2012

HEBU FIKIRIA KIDOGO KUHUSU HILI!!!

Tafiti nyingi zinaonyesha kwamba, ndoa sita katika kila kumi huvunjwa na wanaume au wanawake kutoka nje. Lakini inaonekana pia kwamba, wale wanaotoka nje ya ndoa zao, wengi ndiyo ambao huacha au kuachwa. Ni karibu ndoa nane katika kila kumi, ambazo hufikia ukomo kutokana na kutoka nje.
Wanawake ambao wako chini ya umri wa miaka 30, hutoka nje kwa kiwango karibu sawa na wanaume. Umri huo ndiyo hatari sana kwa wanawake kutoka nje.
Inaonyesha kwamba, bado dini haiogopwi sana linapokuja suala la kutoka nje. Waumini na viongozi wengi wa dini mbalimbali wanadaiwa kutoka nje kwa kiwango kikubwa kuliko inavyodhaniwa.
Karibu wanawake wawili katika kumi na wanaume watatu katika kumi, huwa wametoka nje ya ndoa zao katika maisha yao hapa duniani.
Uhusiano mwingi wa kiuzinzi hudumu kwa miaka mitatu tu na wapenzi huachana au kuachanishwa kwa kufumaniwa. Lakini mwingine hudumu maisha, ingawa na madhara yake nayo hudumu maisha.
Ni mwanamume mmoja kati ya kila kumi, ambao huwaacha wake zao na kuoa nyumba ndogo. Wengi hubaki na wake zao huku wakiwa na nyumba ndogo, au kuwaacha wake zao, lakini hawaoi nyumba ndogo.
Hata hivyo, wanane kati ya kumi miongoni mwa wale wanaowaacha wake zao na kuoa"nyumba ndogo," nao huja kuachana na nyumba ndogo hizo. Kwa hiyo, ni wawili tu kati ya kumi ambao hudumu na "nyumba ndogo" walizozioa baada ya kuachana na wake zao kwa sababu ya "nyumba ndogo" hizo.
Halafu wanane kati ya kumi ya kila aliyevunja au kuvuruga uhusiano wake na mume au mke kwa sababu ya hawara, huja kujuta baadaye. Ni wawili tu kati ya kumi, ambao uvurugaji wa uhusiano wake kwa sababu ya hawara, hawaji kujuta. Hawa ni wale ambao ndoa zao zilikuwa tayari na mashaka makubwa.
Huchukua mwaka mmoja hadi mitatu kwa ndoa ambayo imeingiliwa na fumanizi, wanandoa kuanza kuelewana tena kama awali. Hapo uhusiano huwa imara kuliko awali, au huingia mashaka ya sirisiri.
Chanzo:- kitabu Mapenzi kuchipia na kunyauka na Munga Tahenan.

9 comments:

Emmanuel Mhagama said...

Nina wasiwasi kwamba hali halisi ya jambo hili ni mbaya kuliko matokeo ya utafiti huu. Ni kitu cha kushangaza kwamba watu wanapata ujasiri hata wa kujidai mbele ya wenzao juu ya usaliti wanaoufanya kwa ndoa zao. Hivi kama unaona maisha ya kuruka ruka ndiyo yanayokufaa, kitu gani kilikufanya umwingize mwenzio kwenye kifungo cha maisha huku ukijua kwamba wewe hayo maisha huyataki au huyawezi? Inanikera mimi!!

Yasinta Ngonyani said...

Kaka Mhagama! hakika umeneno...ni kweli kama uliamua kufunga ndoa na huyu mtu iweje leo unatoka nje? ana kasoro, au amebadilika nini? kwa hiyo unapoamua kufunda ndoa/kuishi na mtu inabidi UFIKIRI SANA sio tu kufunga....

Emmanuel Mhagama said...

Shetani ametusizi speed. Kila mahali anatudanganya tu. Ametujaza tamaa za mbuzi za kuona kila kitu kilicho mbali ndo kizuri. Mke mzuri wa jirani, wa kwako mbaya. Mume mzuri wa jirani, wa kwako mbaya. Nyumba nzuri ya jirani, ya kwako mbaya. Gari zuri la jirani la kwako baya. Watoto wazuri wa jirani, wa kwako wabaya hadi unawaita mbwa. Mwee!! kwali mavene.

ray njau said...

Epuka kukosa uaminifu katika njia yoyote.
• Yesu Kristo alisema: “Kila mtu ambaye anaendelea kumtazama mwanamke na kumtamani tayari amefanya uzinzi pamoja naye moyoni mwake.” (Mathayo 5:28) Mtu anapofanya ngono nje ya ndoa, yeye analeta pigo kubwa kwa muungano huo, na Biblia inasema kwamba kufanya hivyo ni msingi wa talaka. (Mathayo 5:32) Hata hivyo, maneno ya Yesu yaliyonukuliwa hapo juu yanaonyesha kwamba tamaa mbaya huwa katika moyo wa mtu hata kabla hajafanya uzinzi. Kwa kweli, kukuza tamaa hiyo mbaya ni kumsaliti mwenzi wako.

• Ili kuwajibika sikuzote katika ndoa yako, azimia kabisa kutotazama ponografia. Tofauti na maoni ya watu wengi, ponografia ni sumu katika ndoa. Ona jinsi mke mmoja anavyoeleza hisia zake kuhusu mazoea ya mume wake ya kutazama ponografia: “Mume wangu anasema kwamba kutazama ponografia kunachochea hisia zetu za kimahaba. Lakini hilo linanifanya nijihisi sifai na simtoshelezi. Mimi ninalala nikilia anapotazama ponografia.” Je, ungesema kwamba mwanamume huyo anawajibika zaidi kwa ndoa yake au kuwajibika kwake kunazorota? Je, unafikiri kwamba anafanya iwe rahisi kwa mke wake kuendelea kuwajibika kwa ndoa yao? Je, anamtendea kama rafiki yake wa karibu zaidi?

• Mwanamume mwaminifu Ayubu alieleza kuhusu uwajibikaji wake kwa ndoa na kwa Mungu kwa kufanya ‘agano pamoja na macho yake.’ Aliazimia ‘kutokaza fikira kwa bikira.’ (Ayubu 31:1) Unaweza kumwiga Ayubu jinsi gani?

• Zaidi ya kuepuka ponografia, unahitaji kulinda moyo wako usipendezwe kwa njia isiyofaa na mtu wa jinsia nyingine. Ni kweli, wengi wanahisi kwamba kucheza kimapenzi na mtu wa jinsia tofauti hakuwezi kudhuru ndoa. Lakini Neno la Mungu linatuonya: “Moyo ni wenye hila kuliko kitu kingine chochote nao ni hatari. Ni nani anayeweza kuujua?” (Yeremia 17:9) Je, moyo wako umekudanganya? Jiulize: ‘Mimi ninapendezwa na nani zaidi, mwenzi wangu au mtu mwingine wa jinsia tofauti? Mimi ninamwambia nani kwanza habari njema, mwenzi wangu, au mtu mwingine? Mwenzi wangu akiniomba niache kushirikiana na mtu fulani wa jinsia tofauti, nitatenda jinsi gani? Je, nitakasirika, au nitafurahi kufanya mabadiliko hayo?’

Emmanuel Mhagama said...

Kaka Ray, hili GOSPEL nimelipenda sana. Mwenye masikio ya kusikilia na asikie Neno hili.
Stay blessed in Jesus' Name.

Anonymous said...

mimi niko mje kidogo ya mada mimi naomba nimuulize huyo ray maana naona anijua sana biblia mbona katika walawi inasema mtu akitembea na mama yake au baba yake auwawe na mru aiwa na mapepo au mchawi auwawe hii imekaje maana tunaambiwa usihuku usije ukahukumiwa

Anonymous said...

Ngoja nimsaidie kaka Ray. Mungu amejifunua kwa wanadamu hatua kwa hatua. Kwa mfano unapoambiwa umwombee adui yako naa umbariki anayekulaani, siyo jambo jepesi kwa mwanadamu wa kawaida. Zamani zile katika jambo lile lile waliimbiwa jino kwa jino. Neema tuliyo nayo sasa inatutosha kusamehe bila kujali tumekosewa kiasi gani. Kifupi ni hivi, aliyesema wale wauawe wakati ule ndiye huuo huyo anayesema sasa usihikumu usije ukahukumiwa. Katika hali ya kawaida unapopewa magizo na juu ya jambo moja na mtu huyo huyo mmoja, kwa vyovyote utachukua maagizo ya hivi karibuni, siyo ya zamani. Yeye aliye na Ujuzi wote na Ufahamu wote anajua kwa nini nyakati zile alisema vile na nyakati hizi anasema hivi.

ray njau said...

Kwenye Mlima Sinai, Yehova alieleza kwa mdomo yale aliyotarajia watu wake wafanye. Baadaye, Musa alipokea mabamba mawili yaliyokuwa yameandikwa zile Amri Kumi. Aliposhuka kutoka mlimani, aliwaona Waisraeli wakiabudu ndama ya kuyeyushwa, na kwa hasira akayatupa yale mabamba chini, na kuyavunja-vunja. Yehova aliandika tena zile Amri Kumi kwenye mabamba ya mawe ambayo Musa alichonga._[Kutoka 32:19;34:1] Amri hizo hazikuwa zimebadilika tangu zitolewe mara ya kwanza. Musa alipaswa kuzifuata. Pia Mungu alimweleza Musa Yeye ni mtu wa aina gani, na kumwonyesha jinsi alivyopaswa kujiendesha akiwa mtumishi wake. Wakristo hawako chini ya Sheria ya Musa, lakini yale ambayo Yehova alimwambia Musa yana kanuni nyingi za msingi ambazo hazibadiliki na ambazo bado zinawahusu wote wanaomwabudu Yehova.[[Waroma 6:14,13:8-10]

ray njau said...

Hata hivyo, kabla ya ile imani kufika, tulikuwa tukilindwa chini ya sheria, tukiwekwa pamoja kifungoni, tukiitazamia imani iliyokusudiwa kufunuliwa.Kwa sababu hiyo Sheria imekuwa mtunzaji wetu kutuongoza kwa Kristo, ili tutangazwe kuwa waadilifu kutokana na imani.Lakini sasa kwa kuwa imani imefika, sisi hatuko tena chini ya mtunzaji._Wagalatia 3:23-25