Friday, October 19, 2012

BINTI ACHUMWA KISU NA MAMA KWA TUHUMA ZA "KUTEMBEA " NA BABA!!

Mfanyakazi wa ndani, Angel Lema (22) amechomwa kisu kwa tuhuma za kuwa na uhusiano wa kimapenzi na baba mwenye nyumba anakofanya kazi.

Angel anayefanya kazi za ndani katika kijiji cha Leganga wilayani Arumeru mkoani Arusha, inadaiwa alifanyiwa unyama huo na mama mwenye nyumba baada ya kumhisi ‘kutembea’ na mumewe.

Akizungumzia tukio hilo jana, Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Wilaya ya Meru, Dkt. Aziz Msuya, alithibitisha kumpokea msichana huyo akiwa na hali mbaya, kutokana na jeraha tumboni Oktoba 8. Dkt. Msuya alidai baada ya kufanyiwa uchunguzi, ilibainika alichomwa kisu tumboni na mwajiri wake.

“Lakini binti huyu tulipomhoji, kwanza alikataa na kudai kujichoma mwenyewe, ila baadaye ilibainika alichomwa na mama mwenye nyumba kwa hisia za kufanya mapenzi na mumewe na kumeonya asimtaje kuwa ndiye amemchoma kisu,” alidai.

Dkt. Msuya alisema kutokana na jeraha kuwa kubwa, walihofia usalama wa utumbo wake na kulazimika kumfanyia upasuaji wa tumbo ili kuangalia usalama zaidi ndani, “Tulipomfanyia upasuaji tuligundua hajaathirika utumbo na ulikuwa salama, tukamshona,” alisema Dkt. Msuya na kuongeza: “Lakini cha ajabu kidonda kikiwa kibichi, msichana huyo alitoroshwa usiku Oktoba 14, kitendo kilichotushangaza,” alisema Dkt. Msuya.

Alisema baada ya kugundua hilo, walitoa taarifa Polisi, ili wachunguze tukio hilo ili kuokoa maisha ya msichana huyo. Kamanda wa Polisi wa Mkoa, Liberatus Sabas baada ya kupigiwa simu na gazeti hili, kuuliziwa tukio hilo, alisema hana taarifa, “Mimi sina taarifa, lakini tukio hilo linaweza kuwapo… kwa kuwa niko mbali huku Moshi kwenye maziko ya Kamanda Barlow (Liberatus), bado sijapata muda wa kufuatilia taarifa za huko na kupata habari zaidi, lakini pia huku mawasiliano yanasumbua sana,” alisema.
Kamanda Sabas aliahidi kulifuatilia suala hilo mara atakapopata nafasi na kutoa taarifa.
---
Habari imeandikwa na John Mhala, HabariLeo, Arusha

6 comments:

EDNA said...

Dunia tunayoishi imejaa chuki,uonevu na unyanyasaji usio na kichwa wala miguu.
Sasa kwanini mwanaume hakuchomwa kisu? kwani uzito wa kosa si ni sawa kwa wote?

Yasinta Ngonyani said...

Edna! Yaani nimekaa siku nzima nikijiuliza je ningekuwa mimi ningefanyaje? Nasema kama wewe hapa halikuwa kosa la msichana wa kazi.. hapa kama wa kuchomwa kisu basi ilibidi baba wa nyumba. Kwa sababu yeye alijua kuwa mama wa nyumba atakuja siku moja kujua ...pole na msichana kwa kweli..

Anonymous said...

halafu kibaya zaidi msichana mwenyewe hasemi ukweli hapo tufanyeje?anamhurumia bosi wake mimi nilisha mwambia mkewangu mambo ya hausi gelo siyataki maana tutakuja kulaumiana

ray njau said...

Wanawake busara zenu zimefikia kikomo?Wasichana wa kazi mwawatafuta kwa vigelegele na kuwaaga kwa mateke kulikoni?Daima busara itangulie sheria.

Yasinta Ngonyani said...

Usiye na jina nimependa uamuzi wako. binafsi pia sijawahi na wala sitakuwa na mfanyakazi wa ndani---nikiwa naye mimi nitafanya nini? hilo ndilo swali langu kuu.
Kaka Ray! umenena la maana ..kwamba hapa msichana anapotafutwa mama wa nyumba huwa hawazi sana kuwa baba wa nyumba atamtamani

Anonymous said...

Jamani hii dunia tunapoelekea cjui hiv unakuwa na ujasili wa kumchoma kisu mtu ambae hana kosa lolote mi naona tu mwenye kosa ni mwanamme!