Tuesday, March 29, 2011

SHUKRANI ZA DHATI TOKA KWA FAMILIA YA MZEE NGONYANI/K​LAESSON!!!


Familia ya mzee Ngonyani 2008-2009 Ruhuwiko-Songea
Kwa niaba ya wanafamilia jamaa na marafiki wote. napenda kutoa shukrani za dhati kwa kuwa nasi bega kwa bega tangu 23/3/2011 siku ya Jumatano mpaka hivi leo. Kwa kweli ninyi ni NDUGU wa kweli kabisa hamkuwa nyuma hata mara moja. Nilipopata tu habari hii nikajikakamua ili kuwahabarisha. Hazikupita sekunde baada ya kuweka tangazo mara nikaona maoni yananza kutiririka. Nikawa mchovu nikaenda kulala, kuamka asubuhi naangalia nakuta Mawazoni nako tangazo lipo. Dakika hazipiti mara naona tangazo jingine kwa mdogo wangu kwa mama mwingine Vukani naye ameweka na pia kashikwa na mshangao wa kutoweka kwa ndugu yetu mpendwa Asifiwe. Mara nasikia simu yangu ya kiganjani inaita napokea nasikia sauti ambayo sijawahi kusikia sio mwingine tena bali ni yeye mwenyewe Mwanamke wa shoka. Dada huyu amekuwa akinipigia simu kila siku kutujulia hali. Na pia bila kusahau tumekuwa tukitumiwa barua pepe nyingi nyingi mno pia ujumbe wa simu ya kiganjani. AHSANTENI wote na mwenyezi mungu awazidishia mara dufu kwa wema wenu. Hakika kwa msaada/ushirikiano wenu wa kueneza habari na wengi wakiwemo wanafamilia kuweza kupata habari kwa njia hii tunawashukuru sana. Watu wengi wameguswa sana na kifo cha ndugu yetu Asifiwe, sina la kusema zaidi ya AHSANTENI SANA. Kuhusu kumuenzi Asifiwe hakukuishia hapo naye Swahili wa Waswahili akaongeza mchango wake. Habari zikazidi kuenea na watu wakawa wanazidi kutufariji. Kwa kweli hapo ndipo nilipojikuta najisemea, kweli kublog si kublog tu bali ni mahali ambapo hukutanisha watu na kuwa NDUGU. Muda ukapita nikaona Kazi yako ni jina lako naye kaweka tangazo nikapiga magoti na kushukuru jinsi habari zinavyoenea kwa haraka. Hapa bado ni siku ya Alhamisi 24/3/2011 mara nikaona Mwananchi mimi kaandika kitu pia wakiwa wawili zaidi yaani kaka Shabani Kaluse na Chacha o`Wambura. Na hapo hapo nikawa napokea simu, watu wakitupa pole kwa msiba nikajikuta kama nipo hapa nyumbani na watu 500 kumbe hapana. Matangazoyakazidi kuongezek na watu kupata habari kona zote kwani naye Nyahbing worriors hakuwa nyuma. Ijumaa tarehe 25/3/2011 Diwani ya fadhili akasema hapana ni lazima niweka kitu, kwa kweli nasema kama mdogo wangu Koero Mkundi alivyosema kuwa msiba huu si wangu tu ni wa wote ni kweli kabisa. Kufumba na kufumbua barua pepe zikawa nazo zinamiminika kutoka sehemu mbalimbali. Wote mliotuma msione kimya tumezipata pole zenu ila ni kutingwa tu. Mwenyezi Mungu na awe nanyi. Kweli aliyeanzisha kublog na apongezwe sana. Habari ya msiba wa Asifiwe haikuishia hapo kwani Mzee wa Lundu Nyasa naye akaibuka kutoka ziwani. Lakini hata hivyo kama waswahili wasemavyo hakuna kuchelewa naye Mzee wa Changamoto akaona naye ni lazima atoe aliyo nayo moyoni. Halafu napenda kumshukuru BOSI wangu kwa kunipa ruhusu ya kuwa nyumbani kwa nyumbani kwa kipindi hiki kigumu. Bila kuwasahau WAFANYAKAZI WENZANGU ambao wamekuwa wakipiga simu na kunipa pole. Kwa kweli zimekuwa siku za machungu, pigo pia tumeachiwa pengo ambalo halitazibika kamwe. Tarehe 26/3/2011 ndio ilikuwa siku ya mazishi niliendelea kupokea simu kutoka sehemu mbalimbali na pia nikiwa nawasiliana na Ruhuwiko. Kwa kifupi mazishi yalifanyika kwa utulivu mkubwa, watu walifurika kama utitiri kiasi kwamba Kanisa la Ruhuwiko likawa ndogo . Kwa niaba ya wanandugu, tunawashukuruni sana wote walioshiriki wakiwa karibu au wakiwa mbali kwa kumsindikiza Asifiwe katika safari yake ya mwisho. AHSANTENI SANA WANABLOG/WASOMAJI WANANDUGU WOTE. TUNASHUKURU KWA USHIRIKIANO WENU WA HALI NA MALI. BILA NINYI SIJUI INGEKUWAJE? PAMOJA DAIMA!!!

20 comments:

Rachel Siwa said...

AShukuliwe Mungu wetu!Nasi tunasema asante kwa Mungu wetu!kwa maana fadhili zake zadumu milele na milele Amina!!
pia naona kidogo umeaanza kupata nguvu dada Yasinta Mungu anamakusudi yake kukuunganisha na watu!.

Mbarikiwe sana!.

Baraka Chibiriti said...

Pole sana Dada, tupo pamoja nawe katika kipindi hiki kigumu, kwa maombi na sala zangu/zetu, ili Mwenyezi Mungu ampokee mpendwa wetu Asifiwe na kuwapa nguvu tena ya kuvuka wakati huu mgumu nyinyi wana familia.

Mwanasosholojia said...

Tunashukuru kuona unafarijika da'Yasinta, tuko pamoja!

Unknown said...

Ni kipindi kigumu sana, Mungu anaweza kukufariji kwa ndani kabisa ya moyo wako kunako hitaji faraja kubwa kwa sasa,Mungu azidi kukupa faraja,tuko pamoja,umoja ni nguvu.

Mija Shija Sayi said...

Nami kama wengine, tunashukuru kuona unafarijika dada, asante kwa shukrani zako na Mungu azidi kuwa nanyi.

Bwana awatie nguvu.

**Aisee makala umeiandika kwa ustadi ile mbaya...

Anonymous said...

we poa tu mbona mimi umenisahau,natafuta kamba! usikonde,niuungwana unapo washukuru walio kufariji,umefanya la mbolea sana.mungu akae nawewe. mmependeza wenyewe wangoni.kaka s

Masangu Matondo Nzuzullima (MMN) said...

Kifo kweli ni kiboko yetu sisi tuliozaliwa. Juzi hapa binti yangu wa miaka mitano akanipiga swali eti: Dad, why do old people die?

Nilitaka kumwambia kwamba si old people peke yake. Hata watoto kama yeye wanaweza kuondoka kama siku ikifika.

Yote kwa yote, Mungu Asifiwe na Mapenzi yake daima yatimizwe. Asifiwe - pumzika salama !!!

o'Wambura Ng'wanambiti! said...

Tuko pamoja Da Yasinta!

kamala Lutatinisibwa Lutabasibwa said...

ole wangu nisiyetoa pole!

emu-three said...

Usijali sana huo ndio ujirani, ujirai mwema ni pamoja na kufarijiana,kwani akufaanye kwa dhiki ndiye rafiki wa kweli.

Penina Simon said...

Mungu azidi kuwatia nguvu na kuwapigania na kuwashindia kila siku.

Simon Kitururu said...

Asifiwe R.I.P !
Yasinta -
Tuko Pamoja!

ADELA KAVISHE said...

Mungu azidi kuwatia nguvu Tuko pamoja sana Yasinta

Ndugu Nkwazi N Mhango said...

Da Yacinta makiwa kwa kuondokewa na dadako mpendwa na Mungu ampumzishe mahali pema peponi. Vibaya ni kutangulia lakini wote tunaelekea huko na hatujui ni lini na kwa namna gani.
Hiki ni kipindi kigumu kwako. Lakini ndicho kilimwengu na huu ndiyo ukubwa.
Mungua awaongezee nguvu kulivuka hili.
Kila la heri.

Koero Mkundi said...

Ni msiba mzito uliomgusa karibu kila mtu aliyepata kufahamu habari za ugonjwa wa Asifiwe.

Nimesoma waraka wako wa shukrani nikiwa na picha tofauti kabisa, kwani umeuandika kwa umahiri mkubwa na nimevutiwa na namna ulivyopangilia maneno yako kwa ustadi.......

Ni jambo la busara kurudisha shukrani kwa wale walioungana na wewe katika kipindi chote cha simanzi tangu tulipoondokewa na mdogo wetu Asifiwe.

Japokuwa ilikuwa ni vigumu kwako kuamini kile kilichotokea, lakini naona ni vyema tukubaliane na mapenzi ya mungu ili maisha yapate kuendelea. Waswahili wanasema yaliyopita si ndwele..........

Mwisho kabisa nakutakia wakati mzuri wewe na familia yako.

Yasinta Ngonyani said...

Naamini nikweli kwamba Mwenyezi Mungu ana makusudi yake kutuunganisha . Nona nimekwisha sema mengi kwenye makala na hapa nataka tu kusema. TUWE PAMOJA SIKU ZOTE ZA RAHA NA TAABU. WOTE MNAPENDWA SANA.

Raymond Mkandawile said...

Naomba kuchukua fursa hii kukupa pole sana dada yetu,mpendwa wetu na mwana blog mwenzetu kwa msiba mkubwa uliokupata wa kupotelewa na dada yako/yetu Asifiwe.
Tunatambua jinsi msiba huu ulivyokuathiri lakini tunakuombe sana Mungu akujalie na kukutia nguvu zaidi katika kipindi hiki kigumu cha majonzi.
Mimi Raymond kwa niaba ya crue nzima ya;www.mkandawilejr.com
Bwana alitoa na bwana ametwaa jina lake libarikiwe.

Nampangala said...

Pole sana mlongo wangu kwa kipindi hiki kigumu sana kwako na familie yako. Mungu awape nguvu na ushilikiano kwanu. Mungu amlaze mahali pema peponi, na mwanga wa milele aangaziwe katika safari yake ndefu.

ray njau said...

Poleni sana ndugu zetu na kumbukeni kuwa kifo ni adui wetu sote.

Anonymous said...

Excellent article. Keep posting such kind of information on your site.
Im really impressed by your blog.
Hey there, You've performed a fantastic job. I'll definitely digg it and personally suggest
to my friends. I am confident they will be
benefited from this site.

Have a look at my blog post :: how To eat paleo in college