Tuesday, January 12, 2010

SITARAJII KUWA MWANAHARAKATI

Nimekuwa nikipokea email kutoka kwa baadhi ya wasomaji wa blog hii ya MAISHA wakinitaka nijiunge na Organization za kutetea haki za wanawake za huko nyumbani au nianzishe NGO yangu ya kutetea haki za wanawake na watoto. Ni email ambazo zimenitia moyo, kuona kuwa kumbe kile ninachoandika kinaigusa jamii, na huenda kuna wasomaji wengi hujifunza kupitia maandishi yangu hayo.

Watumaji wengi wa email hizo wamekuwa wakinipongeza kwa kuwa mwanaharakati wa kutetea haki za wanawake, lakini pamoja na kunipongeza pia wamenipa ushauri huo wa kunzisha NGO yangu au kujiunga na NGO za huko nyumbani ili kupigania haki za wanawake hapo nyumbani au hata ulimwenguni kote.

Bila shaka hata wewe unayesoma hapa huenda pia ulikuwa na wazo kama hilo la kunishauri nianzishe hicho kinachoitwa NGO, kwa kuona kuwa nimekuwa mwanaharakati kutokana na kuzungumzia sana habari za manyanyaso ya wanawake hapo nyumbani Tanzania.
Sitaki niwakatishe tamaa, lakini ni vyema nikaweka bayana kuwa lengo la kuandika makala za kutetea haki za wanawake sio kwamba ninayo dhamira ya kuanzisha NGO, sijawahi kuota na wala kuwaza kufanya kazi hiyo. Binafsi naamani kwamba, kuwa mwanaharakati haimaanishi kuwa na Organization. Kwamba huwezi kuwatetea wanawake na watoto isipokuwa mpaka uwe na NGO. Mimi siamini hivyo, bali naamini kuwa mtu yeyote, akiwa mahali popote kwa utashi wake anaweza kuwa mwanaharakati wa kutetea haki, ziwe ni za wanawake, watoto au hata jamii kwa ujumla, na sio lazima mtu huyo awe na Organization.

Naamini kuwa ile kuandika makala tu, iwe ni kupitia magazetini , ukurasa binafsi, yaani Blog au kuzungumza redioni au hata katika luninga inatosha kabisa kuwa mchango katika kuibadilisha jamii kimtazamo.
Nimelizungumza hili maana nadhani kuna baaadhi ya wasomaji wa blog hii wanadhani kuwa huenda ninavyoandika makala za kutetea haki za wanawake ni kamchakato kangu ka kuelekea kuanzisha Organization yangu nitakaporeja nchini.
Kusema kweli sina wazo hilo kwa sasa, bali nafurahia sana, kile ninachoandika na jinsi wasomaji wanavyotoa maoni yao huku kukiwa na tofauti za kimtazamo. Kusema kweli huwa najifunza mengi kupitia changamoto za wasomaji wa blog hii.

Labda ingekuwa ni vyema nikaweka bayana kuwa, mimi nimfuatiliaji wa habari za hapo nyumbani Tanzania, kupitia magazeti na mitandao tofauti tofauti, na hata ninapokuwa nyumbani Tanzani huwa nanunua vitabu na nasoma sana magazeti mengi ikiwa ni pamoja na kuzungumza na watu wa rika tofauti na kada tofauti ili kupata uzoefu wao juu ya kile ninachokisoma kupitia vyombo vya habari vya nyumbani.

Mimi nimezaliwa kijijini huko Lundo Nyasa na nimekulia kijijini kabisa Kingoli au Litumbandyosi mkoani Ruvuma, nimekulia kijijini kabisa, nafahamu maisha halisi ya mwanamke wa kijijini, kuanzia kulima, kukata kuni, kupika, na shughuli ndogo ndogo zinazofanywa huko vijijini. Pia nafahamu juu ya ndoa za mapema kwa wa watoto kike na athari zake kwa kuwa nimezishuhudia, nimeona wanawake wanaonyanyaswa na waume zao, nimesikia habari za wanawake kubakwa, kwa hiyo ninapoandika habari yoyote juu ya madhila ya wanawake, ni kutokana na uzoefu wangu, maana ninajua ninachoandika.

Huku ughaibuni nilipo kuna visa na mikasa mingi sana, kuna mitandao mingi ya habari na vyanzo vya habari pia ni vingi, ninaweza kuandika habari za huku na zikavutia, kwani nimeshajaribu mara kadhaa, lakini kwanini niandike habari zao? Nimeona ni vyema nikiwa naandika habari za huko nyumbani kwa wingi ili jamii itambue kuwa japo niko huku ughaibuni lakini nayafahamu madhila yao, na niko tayari kuyakemea japo niko mbali.
Hata hivyo naomba nikiri kuwa nimevutiwa sana na wale wanaoniunga mkono kataka makala zangu. Nawashukuru sana na ninaomba msiache kunipa changamoto pale ambapo mtaona labda nimekosea au nimeteleza, kwani mimi sio mwanahabari bali ninapenda sana kuandika na ninafurahia kuandika yale yanayoigusa jamii kwani huo ndio mchangao wangu, pamoja na hayo sitaacha kale katabia kangu ka udadisi, yaani UKAPULYA, kwani huwa sioni haya kuuliza pale ninapokutana na jambo nisilolifahamu au lililonipitia kushoto.
Tuko pamoja
Mungu awabariki wote!!

17 comments:

Chacha o'Wambura a.k.a Ng'wanambiti! said...

Na katika uanaharakati huo waweza kuta ushaanzisha NGO ya wanaharakati ijulikanayo kama ruhuwiko.blogspot.com a.k.a Maisha :-(

una hakika huna NGO mpaka sasa?

Upepo Mwanana said...

UKAPULYA, inafurahisha sana.

Mimi sina kipaji kama chako, wewe ndio kipaza sauti chetu. Tupo pamoja dada

Yasinta Ngonyani said...

Chacha Wambura! kuwa kama nina uhakika kuwa nina NGO mpaka sasa? kwa kweli sijui kama elimu hii inawafikia watu wote mpaka vijijini kabisa. Kwani nadhani wao ndio wanaopata shida zaidi Au?

Na upopo Mwanan:- nashukuru kama umefurahi kwa neno KAPULYA.Na nashukuru kama Tupo pamoja.

Koero Mkundi said...

Hivi huwezi kutetea haki za wanawake na watoto au jamii kwa ujumla mpaka ujiunge na NGO au kuanzisha NGO?
Dada Yasinta kwa taarifa yako kuwa na NGO kwa hapa nchini ni kama kamradi ka kujitengenezea vimilioni kadhaa, huku wale walengwa wakiendelea kutumiwa katika kuombea mkwanja kwa wafadhili lakini wakiachwa katika lindi la umasikini.
NGO nyingi hapa nchini zimekaa kifisadi sana na zinatumiwa na wamiliki wake katika kujitengenezea kipato kwa kuwatumia waathirika kuombea misaada na wakipata wanajiangalia wao tu.
Eti Chacha Wambura si unajua mambo ya write up, unaandika kamradi kako na kuambatanisha na picha kadhaa za maigizo ulizowapiga watu uliowatengeneza halafu baada ya hapo unaipeleka kwa wafadhili. Ikikubaliwa na pesa ikitoka, ndio imetoka hiyo, ponda mali kufa kwaja.
Dada yangu Yasinta nakutahadharisha kuwa hao waliokushauri wanataka kukutumia kwa kuwa uko huko ughaibuni, watajidai kutaka kujiunga na wewe ili kuanzisha hiyo NGO, kwa kuwa wanajua itakuwa ni rahisi kwako kutafuta wafadhili wa huko, na pesa ikitoka hutawaona, watakuchafulia jina lako.
Wewe kuwa tu mpiganaji wa mtandaoni inatosha kwani haya maandishi iko siku yatawafikia wananchi walio wengi kwa jinsi teknolojia inavyozidi kukua.

Mija Shija Sayi said...

yasinta mbona wewe ni mwanaharakati tayari!

Na mimi nachukua nafasi hii kumuomba Chacha o'Ng'wanambiti afungue blogu au mnasemaje wadau wengine?

Chacha o'Wambura a.k.a Ng'wanambiti! said...

Da Yasinta: tayari unayo constituency katika Jimbo la uchaguzi la 'Nangonyani' :-) Hivo usiwe na shaka kuwa ujumbe wako hauwafikii watu wa vijijini.

Una uhakika unajua maana ya kijiji? :-(
Je kijiji lazima kiwe kijijini na siyo mjini :-(

Da Koero: hilo nalo neno :-( lakini subject to discussion, ha!

Da Mija: Duh! ati Mkurya awe na blog! :-) Kuna sababu zozote za msingi za mimi kuwa na blog? Je yawezekana na-miss baadhi ya vitu kwa kutokuwa na blog? :-(

najua kitu ninachomiss ni kutokuwa na access ya ku-comment katika baadhi ya blogs kama ya Koero mpaka wakati mwingine (hapo nyuma) nililazimika kumtumia komenti zangu kwa email kitu ambacho wakati mwingine sijisikii kuwa huru kwa kujinadi kama hapa ninapotoa comment live :-(

Christian Bwaya said...

Kati ya kundi la watu nisiowapenda ni hawa wanaharakati. Wanafiki. Wanatafuta ulaji kwa mgongo wa kutetea haki za wengine. Nitakuja kulieleza hili siku nyingine nipatapo fursa nzuri zaidi. Ila sidhani kama tunawahitaji watu hawa.

Christian Bwaya said...

Niliandika kwa spidi bila kusoma maoni. Kimsingi nakubaliana na anachosema Koero. Profesa Chachage aliwahi kuziita hizi NGOs kama Nothing is Going On. Hakuna cha kutetea watu kinachotafutwa na ndicho labda kinachoendelea ni mlo. Nukta.

Kuna watu wanatumia matatizo wetu kwa faida yao.

Chacha o'Wambura a.k.a Ng'wanambiti! said...

Kaka Bwaya: kama wanasiasa? :-(

chib said...

Katika mambo ya blogu, kuna wamiliki, wasomaji na wachangiaji. Chacha naye ana nafasi yake. Huenda mkimwambie aanzishe blogu, atajikuta naye anachangia mada yake kwa kujisahau :-)

Ila nina imani akianzia, siku ya kwanza atapa followers kama 50 hivi

nyahbingi worrior. said...

Dada,ngoja nirudie tena kusoma makala.

Christian Bwaya said...

@Chacha: bora wanasiasa tunajua wanatafuta shibe ya matumbo yao. Hawa wanaoitwa wanaharakati ni wanafiki.

Kwenye shughuli zisizo na ulaji hata kama zina manufaa kwa jamii hawaonekani. Chunguza uone.

Ramson said...

Duh! Dada Yasinta naona umeniwahi, hivi hatuwezi kuanzisha ka NGO ketu huku Ughaibuni na sisi tutengeneza Vijisenti vyetu. Nilikuwa na hili wazo siku nyingi na nilitaka nikushirikishe au?........!!!!?...LOL

Teh teh teh teh…..Koero mtoto una hatari wewe, hivi kwa nini unasema siri za watu, hujui kuwa hiyo ni miradi ya watu na wanasomesha watoto wao nje ya nchi kwa huto tumiradi twa NGO, halafu wewe unamwaga mambo hadharani …..Kwani hujui kuwa Kamala na Chacha Wambura wana ka NGO kao ka kuhamasisha vijana kuoa kungali mapema ili kuepuka janga la Ukimwi na kwa kuanzia Kamala kaona na picha za harusi yake zitatumika katika kusapoti write up yao…..LOL

Nakumbuka nilipomaliza kidato cha sita, niliungana na wenzangu watatu tukajidai kuanzisha kamradi ketu eti ka kupambana na Ukimwi, Duh! Tukaandika write up , tena ilitugharimu kweli maana Hapo Dar, kuna watu kazi yao ndiyo hiyo kuandika write up kwa malipo na wana pesa kweli , Basi tukaenda USAID tukakuta masharti magumu, tukageuza kibao tukaenda DANIDA, nako duh! Masharti magumu. Nikaona ujinga huu, nikajitoa na kufanya mipango ya kuja ughaibuni kuendelea na masomo.
Yule mwenzetu mmoja akakomaa, na sijui alipitia mlango gani, niliporudi nchini mwaka jana nikamkuta mambo yake saaafi anazo Toyota balloon na Rav 4 kadhaa, mambo yamemnyookea. Ama kweli kufanikiwa Bongo, yahitaji uwe msanii kweli kweli, huyu jamaa keshatoka kwa fedha za wafadhili,……Teh teh teh,,…….asije akanisoma hapa akani mind ….LOL

Chacha o'Wambura a.k.a Ng'wanambiti! said...

Naona mjadala unaelekea kwingine kama sijakosea. sina hakika lakini labda swali litakuja:

Je NGOs ziko kwa ajili ya watu ama kwa ajili ya walozianzisha?

nadhani ni kamjadala kazuri ambako kanaelimisha. kwa maelezo ya wengi hapo juu inaonesha kuwa ni kwa ajili ya walozianzisha.
na tukianzia hapo kama Kaka Bwaya alivosema ni wanafiki sina hakika kama ni generalization ama ni specific ishu.

Kuna nadharia mbalimbali kuhusu haya mambo. Na unapoliangalia swala hili utaona kuwa lina sababu zake. Mojawapo ni structural Adjustment programs za bretton woods institutions kama world bank, imf nk. Hawa jamaa nnavoona hakuna maendeleo wanayoyatetea bali ajira na faida/biashara kwa nji wanazozitetea ama zinazowafuga.

kuna wakati huwa najiuliza mfadhili kutoa kwa jamii $5,000 kwa ajili ya mradi halafu anatumia $15,000 kwa ajili ya kuja kufanya monitoring na evaluation :-(

Halafu utasikia zimetolewa bilioni za dola, asilimia 85 ya msaada huo ni technical support ambapo wanaotoa hiyo tekniko sapoti ni wao haohao. Kwa hiyo utaona kuwa kuna mlolongo wa unafiki toka kwa watoao mshiko mpaka wanaotumia :-(

Nadhani kuna matatizo ya kimfumo. Nasikia wengi wa wenye NGOs ni wazee hasa wastaafu na walopitiwa na ridandansi ya world bank's SAP :-(

kwa vijana inakuwa ngumu kwa kuwa elimu yetu haitufundishi kujiajiri badala yake utasikia kijana amemaliza bussiness administration anazunguka mitaani kutafuta ajira mpaka kisigino ya kiatu inaisa kabisaaa :-( Na wale wajanja wenye kujua tokana na kuelimishwa wanaingia kwenye ajira hata ambayo hawakuitaka kwa kuwa ati kuna maslahi.


Kwa ujumla, kama ilivo siasa, sekta ya NGO imevamiwa na manyang'au nikiwemo mimi na Kamala :-)

naona naanza kuhubiri na Mt simoni anaweza kunifukuza sasa hivi :-( Ndo sababu nkasema tuahitaji mada hii kujadiliwa kwa saidi kwa sababu CBO/NGO yenye kujali maslahi ya wananchi haianzishwi toka juu bali toka CHINI :-)

kamala Lutatinisibwa Lutabasibwa said...

NGOZ za wanawake hapa nchini ni wizi, utapeli na ubakaji. ebu tembelea kazi za TGNP uone mambo ya ajabu eti wanamtetea mwanmama

DUH

nilimwambia chaha aanzishe bulogu akasema hana cha kutundika humo!

eti NGO yako??? kuna NGO ya mtu? kwa ni kammpuni?

Yasinta Ngonyani said...

Koero usiwe na wasiwasi sitaanzisha NGO.

Da mija asante kama unaona tayari nimesha anzisha moja.

kaka Bwaya karibu tena kwani ulikuwa umpotea kidogo

Ramson naona umesikitika kuwa nimekuwahi...lol pole sana na labda afadhali nimesema hili kwani ungeniwahi labda ningekubali na haliafu ingekuwa kama Koero alivyosema...lol

Kamala! ni kweli kwa nini mtu uwe NGO yako na halafu kumbe kuwadangaya wtu tu. Naomba mjadala uendeleeeeeeee

Markus Mpangala. said...

nipo bize na michuano huko ANGOLA