Thursday, June 11, 2009

MALI NA FEDHA NI KITU GANI KWA MWANAMKE?

Kuna jambo moja leo nataka kulizungumzia, nalo sio jingine bali ni hili la wanaume kutokujua hasa sisi wanawake tunawapendea nini katika ndoa au mahusiano.
Katika maisha yangu ya ndoa nimekuja kugundua mambo mengi sana ambayo huenda wanaume wengi hawayafahamu juu yetu sisi wanawake.

Kuna ujinga mkubwa sana ambao huwa unawasumbua wanaume. Wanaume wengi, sijui ni kutokana na malezi huwa wanadhani kwamba sisi wanawake tunahitaji fedha na mali ili kufurahia maisha ya ndoa au mahusiano.

Na dhana hii ambayo mimi naiona kama ni potofu, huwafanya wanaume kuamini kwamba wakiwa na fedha watakuwa wamemaliza matatizo yote ya mwanamke, na hivyo kuwa na ndoa au mahusiano yenye amani na utulivu.

Na kwa kuwa wanaamini hivyo, basi wakiishiwa ndani hapakaliki, wanahangaika kutafuta fedha ili kuzihami ndoa zao au mahusiano yao na wapenzi wao, kwani wanaamini kuwa bila fedha kutakuwa hakuna upendo tena kutoka kwa wake zao aua wapenzi wao.
Katika kipindi hicho cha ufukara ndipo mwanaume atakuwa karibu zaidi na mke au mpenzi wake kwa hofu ya kuogopa kuachwa, lakini baadae akizipata anakuwa hana muda na (bize)unajitokeza kwani wanakuwa na imani kuwa fedha ipo kwa hiyo uwezekano wa kuachwa na wake au wapenzi wao nao unakuwa haupo.

Sikatai wanaume kutafuta fedha kwa bidii ili kuondokana na umasikini na kuweza kijikimu kifamilia, lakini inapokuja kuonekana kuwa sisi wanawake tunawapenda wanaume kutokana na kuwa na fedha, hilo nalipinga kabisa.
Tuachane na zile dhana zilizojengeka siku hizi kuwa, wanawake wa siku hizi eti wanafuata pesa tu (after money) na wanathamini sana wanaume wenye fedha. Hilo inawezekana lipo lakini hebu tujiulize, hivi mwanamke anayempenda mwanaume kwa ajili ya fedha, hata akiolewa, unadhani atakuwa na amani kweli?

Kama mwanaume huyo atakuwa (bize) hana muda na shughuli zake, halafu anadai kuwa ana amani, basi labda atakuwa anaipata mahali pengine na sio kwa mume huyo, na hiyo ni hatari sana.
Kuna haja ya wanaume kujiangalia mienendo yao, je wanakuwa na muda na wake au wapenzi wao? Na wanatenga muda maalum wa kuzungumzia matatizo ya familia yao na kutafuta suluhu kwa pamoja?

Kuna haja ya wanaume kujikagua na kuangalia upya mahusiano na wake au wapenzi wao yakoje kabla mambo hayajaharibika

8 comments:

Anonymous said...

Huu japo ni ushauri wa bure, una thamani kubwa sana katika maisha ya yeyote yule anayefikiria juu ya mahusiano na maisha ya ndoa.
Watu tunatofautiana katika kipaumbele fedha kwenye mahusiano. Fedha na mali siyo jibu la moja kwa moja la kutatua matatizo, tena wakati mwingine huwa ndiyo chanzo cha wivu, maneno, ugomvi kero na matatizo chungu nzima.
Fedha inahitajika katika kuyamudu maisha lakini fedha si MSINGI mkuu wa ndoa.
Shukran Da Yasinta!

Anonymous said...

tuna lundo la mifano ya wanawake wanaopenda pesa. japokuwa sio wote lakini inaweza kuwa asilimia 80 wanaendekeza pesa katika uhusiano, ni wanawake wangapi wamewacha waume zao baada ya kupoteza kati, au kufilisika katika biashara? tafakarini, huwa wanasema samaki mmoja akioza....

Yasinta Ngonyani said...

Da Subi! hapo umesema ni kweli wengi wanafikiri wakiwa na pesa basi matatizo yote yanakwisha. Ndo kwanza yazidi kuongezeka kwani hao hao matajiri wanadiriki hata kuua ili utajiri uendelee. Kwani siku hizi hata wanaume nao wanataka wanawake tajiri. Kwa hiyo kama unataka kuoa/kuolewa usiolewe kwa ajili ya mali/fedha olewa kwa penzi la dhati.

Usiye na jina asante. Hawa wanawake basi hawakuwa na mapenzi ya dhati. Na ndio, "Samaki akioza moja wote wameoza..." basi inabidi tuwe makini ili taifa lijalo lijue kuwa penzi sio mali/fedha penzi/pendo ni kumpenda mtu kama alivyo.

Bennet said...

Ukiwa na pesa unauwezo wa kununua ngono na wala sio mapenzi, kama una mwenza na anakupedea pesa zako ujue hayo sio mapenzi kwa sababu ukifulia na yeye atatoka nje ya ndoa au kuondoka kabisa

Simon Kitururu said...

Tukiachana na swala la kuwa sina Fweza, kwangu mimi binafsi napata taabu sana kujua wanawake wanawaza nini mpaka naanza kuchukulia serious wadaio Wanaume na Wanawake hutokea sayari mbili tofauti!:-(

chib said...

Yasinta, wewe umezungumzia upendo wa kweli kutoka kwa mwanamke, lakini ukweli, kuna wanawake, tena wengi, upendo unakuja kwa kumuona mwanaume ana uwezo, na uwezo hauchukuliwi kwa kuwa unaweza kukidhi masuala ya kiunyumba, au unachapa kazi nk. Kaupendo kanakuja kwa kuangalia kama utakidhi na mahitaji yanayohitaji pesa.
Masikini dume, mara nyingi hata wanawake wanamdharau, kila mahali popote duniani.
Fuatilia uhusiano wa mapenzi kati ya m'me na m'ke kwa misingi ya genetic, utashangaa kuona jinsi wanaume na wanawake wanvyotofautiana kimtazamo. Kwa kukumegea kidogo, wanawake wana ubongo mkubwa kwa asilimia 25 zaidi kuliko wanaume, hapo kuna kitu wanatuzidi, chaweza kuwa cha maana au cha kupuuzi.
Huo ni mtazamo tu, sina ubavu wa kujibu kwa atakayeleta malumbano

kamala Lutatinisibwa Lutabasibwa said...

sio wanawake tu bali hata wanaume hupenda fedha na ndio maana huishia kuzitafuta.

mahusiano yanahitaji kuwa pamoja muda mwingi, kusikilizana, kushirikishana na kushaurina.
binadamu wa leo anajitafuta katika fedha wakati hakuja nazo na wala haondoki nazo~

Msangi, RS said...

Tatizo ni misingi ambayo wanaume wanajengewa na wanawake wenyewe. Maana asilimia kubwa ya wanawake husema na kuishi katika semi zao za kuwa wanaenda kwa wanaume kusaka maisha. Yaani wengi wa kina dada hivi sasa, wanachukulia kufunga ndoa kama sehemu ya kujitafutia maisha na sio kutekeleza maandiko, kusaka furaha ya kimoyo.... haiyumkiniki ndio maana wanaume huwekeza sana katika kusaka fedha zaidi kuliko jambo lolote lile, maana akiwa hana fedha akirejea nyumbani nako kunakuwa hakukaliki. Siku hizi wanasema hapatoshi... nitarejea baadae tena