Sunday, April 11, 2010

Nakuomba Mola Wangu

mke mwema

Nimechoka nimechoka, nimechoka peke yangu,
Mwenzenu nataabika, nahisi dunia chungu,
Nimechoka hangaika, namhitaji mwenzangu,
Nakuomba Mola wangu, nipatie mke mwema.

Nahitaji nami oa, kwani muda umefika,
Nimpate aso doa, mke alokubalika,
Niwe nayo njema ndoa, siyo ya kukurupuka,
Nakuomba Mola wangu, nipatie mke mwema.

Binti ntayempata, ajue kumcha Mungu,
Asiwe mwenye kunata, awe'shimu ndugu zangu,
Aitike nikimwita, hata mbele ya wenzangu,
Nakuomba Mola wangu, nipatie mke mwema.

Ajaaliwe nidhamu, nidhamu ya kwelikweli,
Ajawe na ufahamu, kufikiri mara mbili,
Hekima nayo muhimu, mazingira kukabili,
Nakuomba Mola wangu, nipatie mke mwema.

Sitaki mwenye kiburi, huyo ataniumiza,
Sitoitoa mahari, mwenye kukiendekeza,
Napenda ajidhihiri, hivyo asije nitweza,
Nakuomba Mola wangu, nipatie mke mwema.

Awe amefunzwa vema, awe na njema tabia,
Yawe maisha salama, asiruke na dunia,
Mola 'tatupa uzima, tutamtumainia,
Nakuomba Mola wangu, nipatie mke mwema.

Awe na uvumilivu, majira hayafanani,
Siku tukila pakavu, asizue tafrani,
Asitende jambo ovu, kuniweka matatani,
Nakuomba Mola wangu, nipatie mke mwema.

Sitochagua kwa dini, kabila ama kwa rangi,
Nitampenda moyoni, yeyote mi' simpingi,
Anifae maishani, ndilo jambo la msingi,
Nakuomba Mola wangu, nipatie mke mwema.

Na watoto tuwazae, Mungu akitujalia,
Tasa 'simnyanyapae, dunia kuichukia,
Kwa dhiki nikamfae, apate kujivunia,
Nakuomba Mola wangu, nipatie mke mwema.

Kuna kitu namwahidi, kwake nitakuwa mwema,
Sitofanya ukaidi, nitamw'eshimu daima,
Kwani kwake sina budi, kumwongoza kwa hekima,
Nakuomba Mola wangu, nipatie mke mwema.

Nitakuwa mwaminifu, kamwe sitomwumiza,
'Tamjali mara alfu, dhikini kumliwaza,
Na watu watamsifu, maana atapendeza,
Nakuomba Mola wangu, nipatie mke mwema.

Kaditama nimalize, kwa beti zangu dazeni,
Afaaye 'jitokeze, nimweke mwangu moyoni,
Mmoja tu nimtuze, huyo huyo maishani,
NAKUOMBA MOLA WANGU, NIPATIE MKE MWEMA.
Shairi limetungwa na Fadhy mtanga nami nimevutiwa nikaona niweka hapa ili tujifunze kwa pamoja. NA NAPENDA KUWATAKIENI WOTE JUMAPILI/DOMINIKA NJEMA. NI JUMAPILI YA 15 YA MWAKA HUU!!!!


17 comments:

Fadhy Mtanga said...

We da Yasinta wewee! Mwe nashukuru sana mweeeh! Haka kashairi mwe nilikatungapo nikiwa na hisia kwa kweli....sasa mwee ndo umeniwekeapo na kapicha ka kasichana kanunu mweeh!
Amaa kanapendezaga mweeh..!

Koero Mkundi said...

Nimechoka nimechoka, nimechoka peke yangu,
Mwenzenu nataabika, nahisi dunia chungu,
Nimechoka hangaika, namhitaji mwenzangu,
Nakuomba Mola wangu, nipatie mume mwema.

Nahitaji nami olewa, kwani muda umefika,
Nimpate aso doa, mume alokubalika,
Niwe nayo njema ndoa, siyo ya kukurupuka,
Nakuomba Mola wangu, nipatie mume mwema.

Mume ntayempata, ajue kumcha Mungu,
Asiwe mwenye kunata, awe'shimu ndugu zangu,
Aitike nikimwita, hata mbele ya wenzangu,
Nakuomba Mola wangu, nipatie mume mwema.

Ajaaliwe nidhamu, nidhamu ya kwelikweli,
Ajawe na ufahamu, kufikiri mara mbili,
Hekima nayo muhimu, mazingira kukabili,
Nakuomba Mola wangu, nipatie mume mwema.

Anonymous said...

Sasa hapo ngoma draw, Mtanga anasaka demu na demu anasaka mume. Mtanga katoa sifa za mwananke anayentamani, na mwananke nae katoa sifa zile anazitamani. Na uzuri zinafanana. sasa mnangoja nini? Mtanga mbona "mzigo huo hapo" hebu kama unasukuma ntu aliyenkalewa ulanzi vile. Mie nafanya kusubiri arusi ya Mtanga na Koero! natanguliza vigelegele vyangu "lililililii! lyalyalyalya!!

Ramson said...

Jamani Koero kwani nini upate tabu wakati mie nipo.......duh!
Nina sifa kedekede yaani kupita hizo ulizozitaja hapo.....

Huyo annony hapo juu naye ana kiherehere anampigia Mtanga debe wakati amishaona zamaaaaani....

Mwaya Mchumba wangu Koero narudi mwezi wa saba huko Bongo nitajie tu mahari nikifika ndoa ya mkeka chapchap.......LOL

MARKUS MPANGALA said...

Nipe pendo lako,
langu liwe lako,
lifanye uwezavyo,
limeza upendavyo,
langu liwe lako,

bado shaka n'nayo,
huba hilo lako,
la kweli hilo,
langu liwe lako?
Ndoa inoke kwako,

kweli ni langu?
hakuna kidudu?
lisiwe la mtu?
nifaidi lidumu,


Mmmha jamniiii

Michael said...

Shairi Zurii saana,Mtanga naamini Mungu alisikia sala yako, wewe dada Yasinta Hiyo picha umeitoa wapi? naamini huyo dada moyo wake ni mzuri kama sura yake,Koero jiandae kupokea maombi, ujitahidi kujibu yote

Thanks dada Yasinta, mtanga Koero you people you made my day

Mbarikiwe

Anonymous said...

Ramson. huo mzigo ni wa Mtanga ambaye aliwahi kuomba na Koero kaja kumwaga vigezo vyake anavyovitaka na mimi nimeona vinafanana sana. Sasa yanini mateso wakati mzigo upo jirani yake kabisa, si bora ajisukumie kama anasukuma mlevi ulanzi vile.

Fadhy Mtanga said...

Koerooooooooo......!
Koero sauti yangu sikia,
Waungwana unawasikia?
Maana sifa ulizozitoa,
Ni kama ninazozililia,
Kumbe hakika umetokea,
Nami ndiye nayekufaa,
Jibu zuri ukanipatia,
Ndoto nimeliotea,
Basi siachi kukusubiria.

Njoo haraka pasi kukawia!

Koero wewe.

Yasinta Ngonyani said...

Koero kwanini usimchugua Fadhy maana hizo sifa ulizozitoa ni zake kabisa. Fanya hivyo mdogo wangu watu tucheze, kula na kucheza ile ngoma ya kibena .......nimesahau kigogo jina lake. Ntafurahi kwani ukiolewa na mtani Fadhy basi nawe utakuwa wifi yangu na pia mtani lyaa lyaaa lyaaa....

Mija Shija Sayi said...

Fadhy na Koero wanameremeta! Eeh! Mola waunganishe wawili hawa.

kamala Lutatinisibwa Lutabasibwa said...

bloger vs bloger, kazi ipo.

nikiwa bado kijana mbich, handsome nk nilisomea chuo cha ushirika Moshi kwa hiyo nilikutana na wachaga nawapare wa kutosha, onyo kwa mtanga ni kwamba hawajui kukatika wala nini harafu ni komandi kibao

unaweza dhani umepata ... labda kama koero ni mchaga / mapare wa Mujini

Jacob Malihoja said...

Mh! Du! hapa sijui nichangie nini .. lakini nimepata cha kuchangia... Haya wote na tumwombe mungu awasaidie wote waliochoka kukaa peke yao .. wako wengi mno hao.. wenye kilio kama hicho!!!! wako ambao mpaka sasa bado .. na kila mmoja ana sababu tofauti .. wengine kwasababu ya masomo .. wengine kwasabbu ya kuzunguka nchi mbali mbali kusoma na kikzi.. wengine sijui kwasababu gani .. ila kimsingi wote wakati wao umekuwa bado.. wakati ukifika kila kitu kinafunguka.. wakati ukifika jiwe lililowekwa pale mlangoni litaondoka siku ya tatu na matumaini yatarudi upya! na hivi naamini wengi kwa andiko alilotoa Koero huenda wengine wameambiwa wainuke wale na wanywe sauti ya mvua inakuja!

MARKUS MPANGALA said...

Mnahangaika bureeeeeee ha ha ha ha ha kumbe hamjui etiiiii

NGOJA hiyo ndoya Koero na Mtanga someni maoni jabali Kamala.

SASA................. hivi hamjafahamu huyo binti pichani ni nani???????? jamani njoeni Ruhuwiko mtamfahamu huyoooooooooooo kimwana anaitwa ............................ a.k.a nangonyani mdogo.
ha ha ha ooooooooooopsssssssssssssssssssiiiiii MHARUKO Koero unahangaika nini, mwenzio si huyo hapo tayariii au unaogopa vichakani kabla ya EMCHEKU???????????? Lol

o'Wambura Ng'wanambiti! said...

Ngoja nami niende vichakani nkatunge shairi la kwangu la kupata NYUMBA NDOGO NZURI....lol

Anonymous said...

Kamala unaniacha hoi kwa kucheka. Nasikia hawa watu ukiwa nae kwa kitanda, yeye anachukua gazeti na kuanza kusoma, halafu anakuambia ukimaliza niambie. na hivi Koero kawa mwanahakati si ndio kabisa? sio ajabu wewe unakatika mwenzio anawaza cha kuandika kwenye blog yake, hapo ukimuuliza kulikoni atakujibu ni haki yake usimnyasenyase. Anyway jariku kupiga Emcheku na kuvuta mzigo hivyo hivyo.

Koero Mkundi said...

Nahisi kama Fadhy Mtanga bahati imemdondokea....

KAMALA} Mhmmmm......

Hii ya annony nayo ni kali.......

"Kamala unaniacha hoi kwa kucheka. Nasikia hawa watu ukiwa nae kwa kitanda, yeye anachukua gazeti na kuanza kusoma, halafu anakuambia ukimaliza niambie. na hivi Koero kawa mwanahakati si ndio kabisa? sio ajabu wewe unakatika mwenzio anawaza cha kuandika kwenye blog yake, hapo ukimuuliza kulikoni atakujibu ni haki yake usimnyasenyase. Anyway jariku kupiga Emcheku na kuvuta mzigo hivyo hivyo."

Ha ha ha ha haaaaaaa......!!!!!

Fadhy Mtanga said...

Nahisi kama Fadhy Mtanga bahati imemdondoke....

Maneno hayo peke yake yanatosha kufanya mtu akose hata usingizi.

Maana ni bahati kwelikweli.

Najikuta nimeishiwa maneno.