Thursday, August 6, 2009

MAISHA YA UGHAIBUNI NA VIJIMAMBO TOKA NYUMBANI

Naomba nikiri kuwa tangu nianze kublog nimetokea kufahamiana na watu wengi sana, si hivyo tu bali pia nimekuwa nikipata email nyingi sana kutoka kwa wasomji wa blog hii ya maisha.

Miongoni mwa email ninazopokea zipo nyingine ambazo kwa kweli huwa zinaniacha na maswali lukuki, hata sijui nisemeje, ngoja leo niwashirikishe wasomaji wa blog hii katika kutafakari jambo hili.

Nakumbuka mwaka juzi 2007 tulikuwa nyumbani Tanzania. Baada ya wiki mbili kupita tulikwenda kumtembelea baba yetu mkubwa. Tulipokuwa pale, baada ya muda akaja mzee mmoja na kuanza kuuliza mama wa watoto yupo wapi? {Akiwa na maana ya mimi}, kisha akaendelea, "Nimesikia binti wa Ngonyani anayeishi Ulaya kaja" Baba mkubwa akamjibu akamwambia "ni huyo hapo" huku akionesha kwa kidole pale nilipokaa. Mzee kusikia hivyo akashtuka na kusema si kweli mbona yupo kama kawaida tu. Hakuamini kwa muda, ila baada ya kuniangalia sana aliona sura inafanana na ya baba yangu, ndio akaamini.

Mwaka huu katikati ya mwezi wa kwanza wakati tulipokuwa nyumbani Tanzania, nakumbuka ulikuwa ni msimu wa kulima. Siku moja tukiwa tunapumzika sebuleni. Mara tukasikia mtu akibisha hodi, tukaitikia karibu na tukafungua mlango, kumbe kulikuwa na watu watatu wanaume ambao hatuwafahamu.
Tukawakaribisha, na wakaingia ndani, wakaanza kueleza kilichowaleta. Walikuja pale kwetu kuomba hela kwa ajili ya kununulia mpira au kama tuna mpira basi tuwape.

Ninachotaka kusema hapa ni kwamba watu wa nyumbani Tanzania au Afrika kwa ujumla wanafikiri mtu kama anaishi Ulaya basi wana ile picha kuwa mtu huyo atakuwa amejiremba kwa kuweka mikorogo na vikorombwezo vingine vya ulimbwende na mavazi yake yatakuwa tofauti na watu wa pale kijijini au mjini, atakuwa anaongea kiingereza au lugha nyingine ya huko aishiko na sio kilugha kama vile kingoni. Pia wanadhani mtu huyo atakuwa anaishi kama yuko peponi na sio mtu wa kawaida kwa maana ya kwamba ana ukwasi uliopindukia, na hana shida kabisa na maisha yamemnyookea.

Ni hivi majuzi tu nimetumiwa ujumbe mfupi kupitia simu yangu ya kiganjani toka kwa mtu nisiyemfahamu akiniomba hela:- nitanukuu ujumbe huo “Mama shikamoo! Za siku nyingi? Nina ombi, ninaomba nisaidie mtaji lengo langu niweke duka la dawa za mifugo tuna shida sana na magonjwa ya mifugo. Nitashukuru sana ukinisaidia, naomba majibu asante” mwisho wa kunukuu ujumbe huo.

Kusema kweli nilishangaa sana kupata ujumbe wa aina hiyo kutoka kwa mtu nisiyemfahamu. Kwa mtazamo wa mtu huyo ambaye sijui kama ni kijana au mzee na hata sijui ni wa jinsia gani akilini mwake anadhani kwamba kwa kuwa ninaishi Ughaibuni ni lazima nitakuwa na pesa, asijue kwamba maisha ya huku ni tofauti sana na tena afadhali hata huko nyumbani Afrika unaweza kwenda kuomba chumvi kwa jirani au hata kula kwa mtu bila hata ya wasiwasi.

Swali:- Je Ungekuwa wewe ndio mimi ungefanya nini?

12 comments:

Fadhy Mtanga said...

Duh!

Mzee wa Changamoto said...

Ningempa zawadi ishindayo yooote ahitajiyo.
NINGEMUOMBEA APATE AKILI ZA KUNG'AMUA ANACHOTAKA NA KUWEZA KUFANYA NA SI KUTAKA KUFANYA KWA KUWA KUNA UHITAJI.
Hapo ningekuwa nimetatua tatizo lake na la jamii pia. Kwani kumpa mtu pesa ilhali hajui kama ataweza kuzitumia vema kufanikisha lengo ni KUMUUA yeye kama si jamii nzima.
Muombee tu abadili mtazamo na afanye kilicho ndani ya uwezo wake

mzee wa matukiodaima habari bila uoga said...

Hapa kazi kweli kweli hata sijui ingekuwaje?

Anonymous said...

Naona DADA yetu Huna kitu cha kuandika...ktk blog....kama mtu anaomba ni vizuri ukisema uwzi kusaidi..kuliko kusimanga...
Mdau Germany

Faith S Hilary said...

I agree na Mzee wa Changamoto, kama vipi mpe hali halisi na I am sure ataelewa unless akiamua ku-pretend hajaelewa.

Nicky Mwangoka said...

Naam dada hiyo ndio asilia yetu, hayo hayaepukiki, muhimu ni kutoa maelezo yakinifu kwa wahusika.Au unaonaje wewe?

Anonymous said...

Mdau Germany,I support your comment 100%.

why should someone take advantege of the ones who are inneed?

For Christ sake do we have to write what our brothers and sisters are in heed off?

My brothers and sister,do we know the diffrent between personal problems and public issues?

Shaka Zulu.

Anonymous said...

Yaani umenikumbusha nami nilikuwa napata shida kwani nimepoteza marafiki zangu wote!Wanataka niwatafutie shule na wengine wanataka sponsor au niwalipie...na hapo ndo nilikuwa nimefika ughaibuini (mwezi tu) Hivi sijui wanafikiria nini?????

Simon Kitururu said...

DUH!

Albert Kissima said...

Dada Yasinta, hizi zote ni athari za ukoloni, wakoloni walipokuja waliweka mazingira ya kuonekana wao ndio matajiri na kila kitu kinatoka kwao, na kwa sababu wakoloni walikuwa ni wazungu na leo hii unaishi uzunguni basi wanaamini kuwa na wewe tayari unauwezo kama waliokuwa nao wakoloni wa enzi hizo,kwani walikuwa wakigawa nguo hata na pesa pia.

Cha msingi ni kuwaeleza kuwa huna uwezo na kujaribu kuwapa hali halisi ya maisha ya huko.

PASSION4FASHION.TZ said...

Pole sana Yasinta hivyo ndio vijimambo sio wewe tuu.

kamala Lutatinisibwa Lutabasibwa said...

sijiu ningefanya nini kwa sababu sio mimi ila ikifika wakati nikawa mimi basi nitasema kile utakachokukisikia nijapokuwa mimi. amnia