Monday, May 12, 2014

HIVI UNADHANI UMELETWA DUNIANI KUFANYA NINI?

Mama Theresa: Alitoa kila alichokuwa nacho kwa ajili ya masikini.

 Nimeakuwa nikiwaza sana kuhusu huyu mama Therese, nikawa najiuliza hivi ile ndoto yangu ya kuwa sista  kama kweli ningefanikiwa je? ningekuwa kama yeye? au je yeye alikuwa hivyi kwa vile alikuwa kama alivyo? au je? kuna mtu mwingine tena kama Yeye? Kama tujuavyo mtu ukipata cheo, au kubahatika kuwa na hali nzuri. Huwa hawawajali kabisa wenzao lakini labda mafanikio yako ni kwababu yao kimalezi na mawazo. Kidogo ulicho nacho gawana na wenzako na Mungu atakujalia..... baadaye nikakumbuka nilisoma sehemu habari ya mama Theresa HAPA...Ebu msoma Mama Theresa.... 
-------------------------------------------------------------------------------------------------------
Maisha. Kila mmoja anaweza kuwa na fasihi yake kuhusu maisha. Wale wanao yafasihi maisha kwa kufuata mafundisho ya imani zao wana fasihi yao wanasayansi wana fasihi yao, na wengine wengi wana fasihi yao, huku pengine kila mmoja pia akiwa na fasihi yake.
Lakini swali hilo nalo je; binadamu amekuja hapa duniani kufanya nini? Huenda hili ndilo ambalo litapata majibu tofauti kupita kiasi. Litapata majibu tofauti kwa sababu kila mtu huamini au kudhani amekuja kuishi hapa duniani ili kutafuta ustawi. Kwa bahati mbaya ustawi wenyewe nao unapimwa kwa kiwango cha fedha na mali mtu alizozipata.

Hebu tujiulize wale wenye fedha kupindukia hawahangaiki hata kuliko wale ambao hawana hata senti ya kula kesho? Bila shaka ni kuwa wanahangaika sana. Hii ina maana kwamba kama binadamu angekuja hapa duniani ili kutafuta ustawi wa fedha na mali watu hawa wasingehangaika kiasi hiko kwani tayari wangekuwa wamepata hicho ambacho kimewaleta.
Kuhangaika kwao kuna maana kwamba binadamu hakuja hapa duniani kutafuta usitawi wa fedha au mali. Kama ni hivyo binadamu amekuja kutafuta kitu gani basi? Ni swali gumu sana na siyo wengi ambao wametafuta jibu wamefanikiwa kulipata.
Ili mtu aweze kujibu swali hili karibu na usahihi inambidi kwanza ajue yeye ni nani. Bila kujua yeye ni nani mtu hawezi kujua kwamba amekuja au kuletwa hapa duniani kufanya nini.
Kwa lugha rahisi na ya kawaida sana binadamu ni mwili na roho yake. Kazi ya mwili ni kuhifadhi roho yake yaani mawazo na uwezo wote unaotokana na kufikiri. Iwe ni kwa imani au sayansi. Binadamu anagawanyika rahisi sana kwa njia au maelezo hayo tu.
Binadamu huzaliwa kukua na badae kufa. Kama kifo ndiyo mwisho wa binadamu basi ni rahisi sana kusema binadamu amekuja hapa duniani kufanya nini lakini kama kifo siyo mwisho wa binadamu kuna ugumu kidogo katika kueleza lengo la binadamu hapa duniani.
Kama kifo ndiyo mwisho wa kuwepo binadamu ina maana kwamba binadamu anapaswa kujitazama kama mwili zaidi kuliko kama kitu kingine. Hii ni kwa sababu kufa kwa mwili wake kutakuwa na maana ya kumalizika kwake. Ukiacha imani inayotokana na mafundisho ya dini zetu wengi wetu huwa tunaamini kwamba binadamu ni mwili na anapokuwa amekufa huwa ndiyo mwisho wake. Imani hii hujitokeza sana kwenye matendo yetu.
Lakini ninavyofahamu mimi ni kwamba maisha ni zaidi ya mwili. Ni katika mkabala huo ambapo tunaamini kwamba binadamu hakuja hapa duniani kukamilisha majukumu ya kimwili na matamanio yake bali amekuja hapa duniani kwa sababu nyingine zaidi.
Wengi wetu tunaamini kwamba tumekuja hapa duniani kwa ajili ya kutafuta fedha pamoja na ‘kutanua’ tunaamini kwamba tumekuja hapa duniani kutafuta vyeo na kuwakanyaga wengine na tunaamini kwamba tumekuja hapa duniani kutafuta umaarufu. Lakini historia haituonyeshi hivyo haikubaliani na imani hiyo ingawa tunajaribu kuikumbatia isituponyoke.
Badala yake ingetakiwa kuanza kujiuliza maswali hayo; baada ya kupata mali na ‘kutanua’, baada ya kupata madaraka na kuwakanyaga wengine na baada ya kupata umaarufu halafu kitafuata kitu gani? Jibu ni rahisi kwamba kutafuata utupu. Ni wengi sana ambao walijidanganya kwamba wamekuja hapa duniani kutafuta vitu hivyo na baada ya kuvipata wakagundua kwamba sivyo walivyovifuata.
Kwa maelezo mafupi na ya moja kwa moja ni kwamba binadamu amekuja duniani kutoa. Kwenye imani ya dini nyingi inaelezwa kwamba binadamu amekuja hapa duniani kumwabudu Mungu. Kuabudu mana yake kufanya ibada na ibada ina maana ya matendo yetu yote mema kuanzia asubuhi tunapoamka hadi tunaporejea tena kitandani.
Binadamu ameletwa duniani kuifanya dunia kuwa mahali pazuri panapofaa mtu kuishi na baadae kuondoka akiwa ameiacha dunia ikiwa salama zaidi kwa wengine. Wale wote walioishi miaka 150 tu iliyopita wameondoka. Wengi wameondoka kama mawe yanavyoondoka kwa kubanduliwa na misukosuko ya jua na mvua, lakini wengine wameondoka na kuiacha dunia mambo ambayo yamefanya maisha yetu kuwa bora zaidi. Hawa ndiyo ambao wangefanya kile ambacho kimemleta binadamu hapa duniani.
Kila mtu anacho kitu cha kutoa. Lakini ni vigumu kwa mtu kuwa na cha kutoa kama mtu huyo hafanyi ibada, yaani hatendi mema. Kama mtu ametawaliwa na mwili ni vigumu kwake kutenda mema, hivyo kuwa vigumu kwake kujua kile ambacho kimemleta binadamu hapa duniani.
Ili kuthibitisha kwamba binadamu ameletwa hapa duniani kwa ajili ya kutoa unaweza kutoa kuanzia leo, hebu jaribu kutoa ili uone matokeo yake, toa kidogo katika ziada uliyonayo kwa wosia nayo, toa upendo kwa wanaoukosa, toa huruma kwa wanaohitaji toa chochote unachoweza kukitoa kwa wanaokihitaji. Bila shaka ukiweza kufanya hivyo, utagundua siri ni kwa nini binadamu aliletwa hapa duniani..

2 comments:

Ndugu Nkwazi N Mhango said...

Mimi sidhani bali najua na kuamini kuwa nililtetwa hapa duniani kuwa mimi tena mimi mimi. Je nimetoa mchango gani kwa jamii? Nimezaa wanangu na kuwalea. Nimelalamika sana kuhusiana na ufisadi. Nimetunga vitabu japo si vyote vilivyochapishwa. Nimepiga shule kama sina akili nzuri. Nimewasaidia maskini wengi hata wengine wakataka kunitoa roho na siwataji. Nilijitahisi kuwapenda watu wote ingawa wengi waliniumiza japo sina kinyongo nao. Nimeletwa kufanya mengi katika machache niliyoweza. Sijutii nafurahia na kuridhika ingawa sitosheki na matendo yangu.

Yasinta Ngonyani said...

Mwal. Mhango! Nimependa ulichosema---kwani kila mtu aliletwa hapa duniani awe kama alivyo yaani na vipaji vyake kwa hiyo ukiona unafanya kitu na hakiwi kama utakavyo labda ni kuanza kufikiri kuacha... na ni kweli hakuna anayetosheka ndio..Ahsante