Saturday, December 1, 2012

Neno La Leo: Fikiri Kuwa, Sayari Tunayoishi ( Dunia) Ni Jehenamu Ya Sayari Nyingine..​.!

Ndugu zangu,

Kwamba kuna viumbe kwenye sayari nyingine wenye kukesha wakiomba kwenye nyumba zao za ibada, kuwa Mungu wao awaepushe na balaa la kuwaleta kwenye sayari dunia. Dunia iliyo zaidi ya tambala bovu. Dunia iliyojaa wanadamu wenye roho za wivu, kinyongo, inda, husda na nyinginezo. Wanadamu wenye kutakiana mabaya badala ya mema.

Na mfano ni huyu aliyeomba sana kwa Mungu ashushiwe rehma. Siku moja akashukiwa na malaika. Akaambiwa, kuwa Mungu amepokea maombi yake. Kwamba anamtaka mwanadamu huyu achague jambo moja ili ashushiwe. Na akishachagua moja, basi, Mungu atampa jirani yake mara mbili ya kitu alichochagua.

Mwanadamu yule akamwambia malaika; " Basi, niache kwanza nitafakari". Baada ya kutafakari kwa muda,mwanadamu yule akatamka; " Namwomba Mungu anipe chongo!" Kwamba kwa vile alimwonea kinyongo jirani yake apate mara mbili ya atakachokipata, mwanadamu yule aliona ni heri Mungu amtoboe jicho lake moja, awe chongo, na jirani yake atobolewe mawili, awe kipofu!

Naam, fikiri kuwa sayari tunayoishi yaweza ni jehenamu ya sayari nyingine. Kumbuka, nimesema fikiri, hivyo basi fikiri kwa bidii...yaweza kukusaidia kupata jibu la kwanini nchi yetu ni masikini, na watu wake pia.

Na hilo ni Neno La Leo.

Maggid Mjengwa
Iringa.
0788 111 765
Nimetumiwa na http://mjengwablog.com.

No comments: