Friday, April 28, 2017

NENDA KAMPENDE MKE WAKO

Nimetumiwa na simulizi hii na rafiki binafsi imenigusa sana nikaona niiiweka hapa kama kawaida nisemavyo sipendi kunyimana elimu. KARIBUNI!

Kijana mmoja alikua akimpenda sana Mama yake, kwakua Mama yake almlea kwa shida sana tena kwa upendo wa hali ya juu kijana yule alilipa fadhila kwa kuhakikisha kua Mama yake hakosi kitu chochote.

Baada ya kuoa yeye alihama nyumbani kwao na kwenda kuishi mbali kidogo na Mama yake, lakini katika mji uleule. Pamoja na umbali huo lakini kila siku alienda kumsalimia Mama yake na wadodgo zake.

Alikua akiwapelekea zawadi na fedha za matumizi. Mara nyingi akitoka kazini alikua akitumia muda mwingi nyumbani kwao na wakati mwingine hata chakula cha usiku alikula kule na kurudi nyumbani akiwa maeshiba.

Hali hiyo iliendelea kwa muda na hata walipobarikiwa kupata mtoto bado aliendelea kuwapenda ndugu zake na kutumia muda mwingi wa ziada akiwa nyumbani kwao kuliko nyumbani kwake.

Ingawa hakua akimdharau mkewe wala kumnyanyasa lakini alimpenda Mama yake zaidi. Siku moja jioni akiwa ametoka kazini, alifika nyumbani kwa Mama yake.

Aligonga mlango na kwa bahati nzuri Mama yake alifungua mlango. Lakini wakati akitaka kuingia akiwa na kapu la zawadi mkononi Mama yake alimzuia na kumuambia kuwa hakuna kuingia.

Kijana alishangaa akidhani kua ni utani lakini Mama alikataa katakata na kumuambia. “Mwanangu najua unanipenda sana lakini sasa ni zamu ya mkeo. Wewe ushakua mkubwa umeoa unafamilia yako, nenda kampende mkeo”.

Kijana alishangaa kwani yote aliyokua akiyafanya ni kwakua Mama yake aliteseka kwaajili yake. “Najua unayafanya yote kwa upendo ila mkeo anahitaji upendo pia. Mimi ni Mama yako, ni mtu mzima, lakini yule mkeo, bado ni binti lakini mna mtoto mdogo.

Kama unavyonipenda mimi mama yako nenda kampende Mama wa watoto wako ili aweze kuwalea watoto wenu waje kuwa na upendo kama wewe. Upendo unaonionyesha nikwakua Baba yako alinionyesha upendo wa hali ya juu.

Baba yako alinipenda sana, akanionyesha upendo, moyo wangu ukawa na amani nikawa na kazi ya kuwalea nyinyo kwa furaha. Sasa na nyinyi mna furaha unanihudumia.

Lakini wewe muda mwingi unautumia hapa, mkeo unamuacha peke yake mpweke. Mwanamke akiwa mpweke anakua na kisirani, akishakua na kisirani anakua na hasira na akiwa na hasira basi hutafuta sehemu ya kuzipeleka na anaweza kuzipeleka kwa watoto.

Akizipeleka kwa watoto watalelewa vibaya na hawatakuja kuwa watoto wazuri kama wewe. Nakupenda lakaini sikutaki tena kwangu, nenda kampende mkeo, tengeneza familia yako, hii ni ya kwangu na nishaitengeneza.

Mwanangu unanipenda sana lakini ipo siku nitakufa kama Baba yako, usihuzunike lakini ipo siku hawa wadogo zako wakiume wataoa, hawatakua na muda tena na wewe. Hawa dada zako wataolewa na kuwa na familia zao.

Watakua bize na familia zao kiasi kwamba hamtaonana, hiyo haimaanishi kuwa hawatakua wanakupenda, hapana watakupenda lakini maisha ndiyo yalivyo. Kama ambavyo mimi nilikua na Kaka zangu na Dada zangu.

Kama ambavyo Baba yako alikua na Kaka zake na Dada zake waliokua wakipendana lakini sasa kila mmoja ana familia yake. Wewe utabaki na mkeo na wanao, hao ndiyo watakua familia yako kama ambavyo Baba yako alibaki na mimi na nyinyi.

Sasa kama hukumuonyesha upendo mkeo sasa hivi unafikiri utaishi naye vipi ndugu wakikutelekeza kwasababu ya majukumu yao. Nenda kampende mkeo, mpeleke zawadi.

Kwangu utakuja mara moja moja nikikuhitaji, utakuja ukisikia naumwa na utanitumia matumizi mwisho wa mwezi. Katengeneze familia yako, nenda kanitengenezee wajukuu wazuri, wenye upendo kama ulivyo wewe Baba yao.

Mama alimaliza na kabla kijana hajasema chochote alifunga mlango na kuingia ndani. Kijana alilazimika kurudi nyumbani, alimkuta mkewe kanyongonyea.

Alimkabidhi lile kapu la zawadi na kumuambia zawadi zako hizi. Mke aliruka kwa tabasamu akimshukuru mumewe kwa zawadi ile, kwani muda ulikua umepita bile kupeleka zawadi nyumbani wala kuwahi vile.

****MWANAUME; Wapende ndugu zako lakini jua mwisho wa siku mtu pekee ambaye mtazeeka pamoja ni Mke wako. Kama huamini hembu muangalie Baba yako kule kijijini vipi bado anaishi na shangazi yako?

Lakini hembu muambie Bibi na Babu yako, si wako wawili tu, tena mmewatafutia na mfanyakazi ili awasaidie. Ndiyo huyo mwanamke unayemnyanyasa leo anathamani kuliko huyo Dada yako anayemtukana mkeo kila siku na wewe unachekelea.

2 comments:

ray njau said...

Ni hadithi ndani ya hadithi.
Asante sana dada Yasii.

Yasinta Ngonyani said...

Kaka Ray...hakika ni kweli...