Monday, June 6, 2011

Mungu wa Kimasai adhaniwaye kuwa na nyuso mbili


NI pembezoni mwa jiji la Nairobi, Kenya, watu wa kabila hili wametengeneza duara, mmoja anaimba kwa sauti ya mtetemo mfano wa zeze na wengine wanaitika kwa sauti mchanganyiko nyembamba na nzito, kisha mmoja mmoja anaingia kati na kuruka juu akiwa amenyooka mithili ya nguzo.

Shuka zao zenye mchanganyiko wa rangi zinasalimu amri kwa kupepea kila warukapo juu, hali kadhalika vito vyao miguuni na mikononi hata shingani vinatoa sauti na kutengeneza mapigo kama ya ala za muziki. Hao ni Wamasai, watu wanaosifika ulimwenguni kote kwa kutunza tamaduni zao.
Zimekuwepo dhana na hadithi mbalimbali kuhusu mila na taratibu zao, baadhi zimesifiwa, nyingine zimekuwa zikipigwa vita na baadhi yake zinashtusha na kuacha simulizi la kushangaza.

Lakini, ukweli unabaki palepale kuwa kabila hili ni kivutio kwa wengi na ni miongoni mwa machache yaliyoweza kuhifadhi na kuheshimu mila zao, licha ya maendeleo ya sayansi ya teknolojia.
‘Enkai’ au Mungu wa Kimasai
Wao huabudu, wanamwabudu mungu mmoja, ‘Enkai’ au Engai ambaye si mwanamke wala si mwanaume. Lakini, mungu huyu amegawanyika katika sura mbili tofauti, upande mweusi(engai narok) na mwekundu(engai nanyokie). Upande mweusi ni mwema na wenye upendo na mwekundu ni wa kishetani na usio na chembe ya huruma.

Wanaamini kuwa, sauti ya radi ni dalili ya pande mbili za ‘Enkai’zikigombana, ambapo upande mweusi unataka kutoa mvua kwa ajili ya mifugo na watu, na upande mwekundu unataka mvua isinyeshe na wamasai pamoja na mifugo yao wapoteze maisha.

Wanaume husuka, wanawake hunyoa vipara
Kimila, wanawake kunyoa vipara na wanaume kusuka rasta ni baadhi ya taratibu za kipekee kwa kabila hili, si hivyo tu, bali wanawake ndiyo hujenga nyumba ya familia, tofauti na makabila mengi ya Afrika Mashariki ambapo wanaume wanawajibika katika ujenzi wa nyumba na wanawake wakiwa na jukumu la ulezi na si ujenzi.

Dhana ya kuchomeka mkuki
Imekuwepo hadithi ya kwamba, mwanamke wa Kimasai anamilikiwa na ukoo wote, kwa hilo, kila mwanaume hushiriki kitanda na wanaume wengine.
Anachofanya ni kuchomeka mkuki mbele ya nyumba (boma) na kisha kuendelea na shughuli iliyomfikisha mahali pale.
Hivyo basi, yeyote atakayekuja na kukuta mkuki huo mbele ya nyumba, hatakiwi kuingia ndani, bali kusubiri, na kuwa mvumilivu. Wivu hautakiwi kwao.

Kwa mujibu wa Simeon ole Serere, dhana hiyo ipo mbali na ukweli, kwani, mkuki huo unamaanisha kujisalimisha na hana nia ya kudhuru, hivyo mwenyeji atakaporejea asiwe na shaka kwani silaha ipo nje.

Laana ya kukata misitu
Hadi leo, Wamasai wamezungukwa na mimea katika mazingira yao, kwa mfano kuna msitu karibu na kijiji cha Mau unaoitwa Medung’i, ukimaanisha ‘Maa’ yaani ‘ usikate’. Inaaminika kwamba, ukikata miti katika eneo hilo, damu itatiririka kutoka humo na kukulaani.
“Mila hizi ndizo zilizowezesha uoto asilia kustawi katika mazingira yetu, tumeweza kuhifadhi Masai Mara, Amboseli na hifadhi za wanyama za Serengeti kwa kuwa hatuli wanyama pori,” anasema ole Kulet, mwandishi wa riwaya nane kuhusu mila za Wamasai.

Hakuna kilio, wala hisia za maumivu
Vijana wa Kimasai wanapofikia umri wa kubalehe, hutakiwa kupitia hatua ya tohara, hii huwajumuisha vijana wote wenye umri wa miaka 12 hadi 25. Kitendo hicho hufanyikaa bila ganzi na inasemekana kuwa wakati wa tendo hilo hutakiwi kulia au hata kukunja sura kuonyesha unahisi maumivu, kwani kufanya hivyo kunaonyesha udhaifu na ni aibu kwa ukoo wako.

Lakini pia, kutikisika au kukunja sura kunaweza kusababisha makosa katika ukataji wa ngozi ya uume na kusababisha kovu la kudumu au kilema cha aina yoyote ile.
“kupona kunachukua miezi mitatu hadi minne, kipindi ambacho vijana hupata shida kujisadia haja ndogo huku kukiambatana na maumivu makali. Vijana hao hutakiwa kuvaa mavazi meusi kwa kipindi cha miezi minne hadi minane,” anasema Laizer Selelii, mlinzi katika ghala moja la mazao jijini Nairobi.

Wanawake pia hufanyiwa tohara au emorata tendo hilo limekuwa likipingwa vikali na wanaharakati na wanawake ambao wamefanyiwa, kama Agnes Pareiyo.
“Usipofanyiwa tohara unaweza kukosa mume, ni kitendo kinachochukuliwa kama cha thamani na sifa kwa mwanamke, wakati mwingine, mahari yako huweza kuwa ni ng’ombe wachache kama usipopitia hatua hii,” anasema Pareiyo. “Lakini, madhara yake ni makubwa wakati wa kujifungua.”

Uchumba wa mimba
Inasemekana kuwa, wanaume wa kimasai huchumbia mimba na kuitolea mahari endapo mtoto atazaliwa wa kiume mahari ile hurudishwa.
Mila hii ndiyo inayosababisha mabinti wa kabila hili kuolewa wakiwa na umri mdogo wengine hata miaka kumi hadi kumi na mbili.
Ole Serere, anasema, suala la wao kuchumbia mimba lilikuwepo zamani ingawa sasa halifanyiki sana.Anakiri kuwa, mabinti wa Kimasai huchumbiwa wakiwa na umri mdogo kwa sababu hawaendi shule.

Ung’oaji wa jino la chini
Utafiti uliofanywa mwaka 1991/92 na kuhusisha watoto tisini na tano wenye umri wa kati ya miezi sita na miaka miwili uligundua kuwa wameng’olewa meno ya chini.

Wakati wale wenye umri wa miaka mitatu hadi saba, asilimia 72 ya watoto 111 walionekana hawana jino moja au mawili ya chini.
Utafiti huo uligundua kuwa, meno hayo hutolewa kwa ajili ya kupitisha maziwa endapo mtu amekunywa sumu au anaumwa mahututi.
Baadhi yao wanasema, kitendo hicho hufanywa wakati wa utoto ili kuondoa meno hayo ya plastiki yenye minyoo ambao husababisha watoto kuharisha na kutapika.

Kutowazika maiti
Wamasai wanaamini kuwa kila binadamu ana malaika wake mlinzi ambaye mtu akifariki humbeba na kumpleka sehemu mbili kati ya hizi, aidha jangwani kama mtu huyo alitenda maovu au katika rdhi ya utajiri wa ng’ombe kama alitenda mema.

Hata hivyo, hawatamki hata siku moja kuwa mtu amefariki, kama ni mtoto husema amepotea na kama ni mtu mzima hutajwa kuwa, amelala.
Hawawaziki wafu, bali baada tu ya kifo,mwili hutupwa porini ili uliwe na fisi. Katu hawachimbi kaburi, kwani wanaamini ardhi imebarikiwa kwa ajili yao, endapo wataichimba watalaaniwa.

“wakati mwingine tunahama kabisa makazi ambapo mtu amefariki, kwani nyumba hiyo yote huwa na mizimu,” anaeleza Serere.
Katika miaka ya hivi karibuni, wameanza kubadilika, kwani sasa hivi hulima, hufanya biashara na wapo wasomi, wake kwa waume.
Hata hivyo, hiyo si sababu ya wao kuacha baadhi ya mila zao muhimu na zenye manufaa kwao. Bado wangali wamebeba fimbo na sime, kama alama ya ushujaa wao.
Na Florence Majani wa Gazeti la Mwananchi

7 comments:

Goodman Manyanya Phiri said...

Asante sana, Dada!

Mimi nimeangaza macho yangu juu ya kipengele chenye mazungumzo ya kuhifadhi mimea, tena nanukuu:


'Hadi leo, Wamasai wamezungukwa na mimea katika mazingira yao, kwa mfano kuna msitu karibu na kijiji cha Mau unaoitwa Medung’i, ukimaanisha ‘Maa’ yaani ‘ usikate’. Inaaminika kwamba, ukikata miti katika eneo hilo, damu itatiririka kutoka humo na kukulaani. “Mila hizi ndizo zilizowezesha uoto asilia kustawi katika mazingira yetu...,” anasema ole Kulet'


Kusema ukweli, maisha ya kisasa na teknolojia yake ndio yatupoteza kwa upande mwingine. Kuhusu miti hiyo, niliwahi kusoma pahala eti enzi za kale Afrika Kusini (kabla ya ukoloni) marehemu walizikwa kwa namna nyingi. Moja yake nikuingizwa chini ya ardhi baada ya kupasuliwa tumbo na mti kupandwa juu yako.


Hiyo nayo ilisaidia ku hifadhi miti kwani watu walipata heshima fulani juu ya miti. Badala ya kwenda makaburini ulijikuta unakwenda msituni!!!


Hadi leo, mtoto akizaliwa katika makabila fulani hawatupi tovu (NAVEL) pamoja na takataka ya hospitali, bali wanakwenda kupanda mti pamoja nayo. Na Mzulu akisema "Inkaba yami iseKijitonyama" (YAANI: "TOVU YANGU IKO-KIJITONYAMA")= inamaana alizaliwa huko Kijitonyama na ukifika naye sehemu hiyo atakuonyesha kabisa mti uliepandwa hapo baada ya tovu "kuzikwa" hapo.

Koero Mkundi said...

@Goodman...
Una simulizi nzuri ajabu..

@Dada Yasinta,
Ahsante kwa habari hii yenye kuelimisha.

Penina Simon said...

Hii nayo kali, Thx mengine nilikuwa siyajui eg, wamasai wana Mungu wao, na juu ya mambo ya kifo

Raymond Mkandawile said...

Kwakweli wa Kapulya una mambo na ukapulya wako unasaidia kwani tunapata habari na simulizi nzuri kutoka sehemu mbalimbali.
Hawa wamasai kwakweli naomba niwasifie kwa ujasiri wao na hasa kwenye kulinda mila na desturi zao japokuwa kuna ambazo zimepitwa na wakati na zinatakiwa kuondolewa kwa mfano tohara kwa wanawake,kutosomesha watoto wao na mangine yanayofanana na hayo.
Nimekuwa shahidi wa ninalolisema kwani hawa wamasai hata wasome na wawe na vyeo vikubwa aina gani au wawe nje ya nchi bado utawaon na mavazi yao asili (hawaoni aibu kutukuza asili yao)Kwaakweli wanastahili pongezi na kuwa mfano wa kuigwa ktk hilo.
Asante dada kapulya kwani nimejifunza mengi sana kutokana na story hiyo..

Anonymous said...

Bwana mkandawile,nikweli unachosema kuhusu kutoona haya na asili yako,hasa mavazi.Lakini mimi na wewe ambao sina uhakika na vazi la kabila letu, haimananishi hatu thamini asili yetu. yawezekana tuka wa wazuri sana katika kutukuza majina yetu ya kiasili,hasa kwa watoto wetu.badala ya kumwita John. una mwita Mkandawile. nk. nakwazwa sana na neno asili.mfano mavazi? nitaongea zaidi kuhusu hawa jamaa na uvaaji wao(wamasai siku nyingine).kaka s

Yasinta Ngonyani said...

Kaka Mkandawile! Yaani kuwa Kapulya ni kitu kizuri sana hupitwi na chochote:-) Kuhusu mavazi ya asili naweza nikakubaliana na kaka S kidodo:- Mavazi ya asili kama uki/tukiongelea kwa undani/kihistoria zaidi ni kwamba enzi za zamani za mababu na mababuzi nikumbukvyo mimi ni kwamba walikuwa wakitembea uchi na baadaye wakagundua vazi la mabanzi ya miti na baadaye ikaja wakagundua vazi la NGOZI YA WANYAMA. Sasa hapa sijui VAZI LA ASILI LA MWAFRIKA NI LIPI?

Raymond Mkandawile said...

Kaka "S" sikuwa na maana ya kwmba wengine hatuthamini asili zetu la hasha....bali nilizungumzia kwa hawa wenzetu wamasai ambao tamaduni zao zimeonekana kuwa na nguvu sana ktk kila kitu kwa mfano kama ulivyosema majina,mavazi, chakula na hata stail zao za kimaisha.
Ila ni wazi kwamba kila mtu kwa asili yake na tamaduni zake anafanya awezavyo ili kuendeleza walau kimoja wapo ili kudumisha mila.
Neno Asili lina maana kubwa sana ambayo kama tutataka kuiwekea majadala basi hautokwisha ila kama ulivyo ahidi kaka tunasubiri hayo unayotuandalia kuhusiana na hiyo maada inayohusu Asili...tupo pamoja kaka S,na nashukuru kwa changamoto yako.