Wednesday, March 21, 2018

MAONI YALIYOTOLEWA NA KAKA RAY NJAU KUHUSU TAULO ZA KIKE!


HAPA NI KAKA RAY NJAU 

Kukabiliana na Matatizo ya Kukoma kwa Hedhi

“Ghafula nilihisi nimelemewa na huzuni bila kujua sababu. Nililia na kuanza kujiuliza ikiwa ninarukwa na akili.”—Rondro, * mwenye umri wa miaka 50.

“Unaamka asubuhi na kupata nyumba yako ikiwa shaghalabaghala. Huwezi kupata kitu chochote unachotafuta. Mambo ambayo ulikuwa ukifanya kwa urahisi, sasa yanaonekana kuwa magumu sana, na hujui ni kwa nini hali iko hivyo.”—Hanta, mwenye umri wa miaka 55.

WANAWAKE hao si wagonjwa. Wanapitia tu kipindi cha kukoma kwa hedhi, ambacho ni badiliko la kiasili katika maisha ya mwanamke anapoacha kuwa na uwezo wa kupata watoto. Ikiwa wewe ni mwanamke, je, unakaribia kipindi hicho? Au je, unapitia kipindi hicho sasa hivi? Vyovyote vile, kadiri ambavyo wewe na wapendwa wako mnajifunza kuhusu kipindi hiki cha mabadiliko, ndivyo mtakavyoweza kukabiliana kwa njia inayofaa na matatizo yanayohusiana nacho.
Kipindi cha Kukoma Hedhi

Wanawake wengi huanza kipindi hicho wakiwa na umri wa miaka 40 na kitu, lakini wengine huanza wakiwa wamechelewa wakiwa na miaka 60 na kitu. * Kwa wanawake wengi, hedhi hukoma hatua kwa hatua. Kwa sababu ya kubadilika-badilika kwa kiwango cha homoni kinachotokezwa, huenda mwanamke akakosa kupata hedhi pindi kwa pindi, akapata hedhi wakati ambao hakutarajia, au akavuja damu nyingi isivyo kawaida wakati wa hedhi. Wanawake wachache hukoma kupata hedhi ghafula, yaani, wanakosa hedhi mwezi mmoja na huo unakuwa mwisho wa kuipata.

Kitabu kuhusu kukoma kwa hedhi (Menopause Guidebook) kinasema: “Kipindi hicho huwa tofauti kwa kila mwanamke.” Kitabu hicho kinaendelea kusema hivi: “Matatizo ya kawaida yanayohusiana na kipindi hicho ni kupata joto la ghafula mwilini,” ambalo huenda likafuatwa na kuhisi baridi. Dalili hizo zinaweza kumfanya mtu akose usingizi na kuishiwa na nguvu. Matatizo hayo huendelea kwa muda gani? Kulingana na kitabu hicho, “wanawake fulani hupatwa na joto la ghafula mwilini kwa mwaka mmoja au miwili wakati wa kipindi hicho cha kukoma kwa hedhi. Wengine hupatwa na hali hiyo kwa miaka mingi, na wachache sana husema kwamba wao hupatwa na joto la ghafula mara kwa mara maisha yao yote.” *

Kwa sababu ya kubadilika-badilika kwa kiwango cha homoni, huenda mwanamke akashuka moyo, hisia zake zikabadilika-badilika na hilo linaweza kumfanya alielie bila sababu, na pia asiwe makini sana na asahau mambo. Licha ya hayo, kitabu The Menopause Book kinasema kwamba “kuna uwezekano mkubwa kwamba mwanamke hatapatwa na mambo hayo yote.” Kwa kweli, wanawake fulani hupata matatizo machache sana na wengine hawapati matatizo yoyote wakati wa kipindi hicho.
Jinsi ya Kukabiliana na Kipindi Hicho

Kubadili mtindo wa maisha kunaweza kupunguza baadhi ya matatizo hayo. Kwa mfano, wanawake wanaovuta sigara wanaweza kupunguza mara ambazo wanapatwa na joto la ghafula kwa kuacha kuvuta sigara. Wanawake wengi hunufaika kwa kubadili mazoea yao ya kula kama vile kupunguza au hata kuacha kunywa kileo, vinywaji vyenye kafeini, na vyakula vyenye sukari au vikolezo ambavyo vinaweza kusababisha joto la ghafula mwilini. Bila shaka, ni muhimu kula vyakula mbalimbali na vyenye lishe.

Kufanya mazoezi husaidia sana kupunguza matatizo yanayohusianishwa na kukoma kwa hedhi. Kwa mfano, mazoezi yanaweza kupunguza kukosa usingizi na kusaidia kuboresha hali ya kihisia na pia kuimarisha mifupa na afya ya mtu kwa ujumla. *
Eleza Mambo Waziwazi

Rondro aliyenukuliwa mwanzoni mwa makala hii anasema hivi: “Usiteseke kimyakimya. Ukiwaeleza wapendwa wako mambo waziwazi, hawatakuwa na wasiwasi kuhusu hali yako.” Jambo hilo linaweza kuwafanya hata wakuonyeshe subira na huruma zaidi. “Upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili,” linasema andiko la 1 Wakorintho 13:4.
chanzo:www.jw.org/sw
Maoni yanatoka katika mada hii TAULO ZA KIKE! kila la kheri kwa wote na ahsante sana kaka RAY.


2 comments:

ray njau said...

Kumweleza Binti Yako Kuhusu Hedhi

Yaelekea wasichana ambao hawajafikia umri wa utineja wanaokaribia kupata hedhi wataelewa mambo rahisi na hususa kuhusu hedhi. Mambo hayo yanaweza kutia ndani mara ambazo atapata hedhi, muda ambao itachukua, au kiasi cha damu atakachopoteza. Hivyo, mwanzoni mwa mazungumzo yenu, ingefaa kuzungumzia mambo ambayo msichana atafanya mara aanzapo kupata hedhi. Pia, huenda ikakubidi kujibu maswali kama: Nitahisije? au Nitazamie nini?

Baadaye, huenda ukataka kuzungumzia zaidi utendaji wa mwili wakati wa hedhi. Mara nyingi, unaweza kupata vichapo vinavyozungumzia habari hiyo kutoka kwa wale wanaotoa huduma za afya au kutoka kwenye maktaba, au kwenye duka la vitabu. Vichapo hivyo vitakusaidia kueleza mambo kwa undani. Huenda wasichana fulani wakapendelea kujisomea vichapo hivyo na wengine wakataka msome pamoja.

Tafuta mahali patulivu. Anza mazungumzo kwa kumweleza kuhusu mabadiliko ambayo hutukia wakati wa kubalehe hadi anapokomaa kabisa. Huenda ukasema hivi: “Hivi karibuni utapatwa na jambo fulani la kawaida ambalo huwapata wasichana wote. Unajua ni nini?” Au mama anaweza kuanza mazungumzo kwa kutaja jambo lililompata. Anaweza kusema: “Nilipokuwa msichana kama wewe, nilianza kujiuliza mambo ambayo hutukia mtu anapopata hedhi. Mimi na rafiki zangu tulizungumzia jambo hilo shuleni. Je, rafiki zako wameanza kuzungumzia jambo hilo?” Mwulize yale ambayo anajua kuhusu hedhi na rekebisha maoni yoyote yasiyofaa. Uwe tayari kuzungumza sana mwanzoni, kwa kuwa huenda binti yako asizungumze sana au hata anyamaze kabisa.

Kwa kuwa wewe ni mwanamke, bila shaka ulikuwa na wasiwasi na woga kuhusu hedhi. Unaweza kutumia yale yaliyokupata unapozungumzia jambo hilo. Ulihitaji kujua nini? Ulitaka kujua nini? Ni habari gani zilizokusaidia? Jaribu kuwa na usawaziko unapoeleza mambo yanayofaa na yasiyopendeza kuhusu hedhi. Uwe tayari kuulizwa na kujibu maswali.

Elimu Inayoendelea

Kuwaelimisha wasichana kuhusu hedhi si jambo linalopaswa kufanywa mara moja tu, bali mafundisho hayo yanapaswa kuendelea. Si lazima ueleze kila kitu mara ya kwanza. Msichana anaweza kutatanika ukimweleza habari nyingi mara moja. Watoto hujifunza mambo hatua kwa hatua. Pia huenda ikafaa kurudia habari hiyo pindi mbalimbali. Wasichana wachanga huelewa habari zaidi kadiri wanavyokua.

Jambo lingine ni kwamba maoni ya msichana kuhusu hedhi hubadilika-badilika kadiri anavyobalehe. Mara binti yako anapozoea kupata hedhi, huenda akawa na mahangaiko na maswali mengine. Kwa hiyo, unahitaji kuendelea kumpa binti yako habari zaidi na kujibu maswali yake. Zingatia habari iliyo muhimu na inayomfaa zaidi binti yako ikitegemea umri na uwezo wake wa kufahamu mambo.

Kuchukua Hatua ya Kwanza

Lakini utafanya nini ikiwa binti yako anaonekana kwamba hapendezwi na habari hiyo? Huenda ikawa hataki kuzungumzia mambo ya kibinafsi. Au labda anahitaji muda ili ajihisi huru kuzungumzia habari hizo na kuuliza maswali. Pengine hata atasema kwamba tayari anajua kila kitu kuhusu habari hiyo.
Huenda ikakubidi wewe ukiwa mzazi, kuanzisha mazungumzo mafupi kuhusu hedhi na kuyaendeleza. Kwa kweli, hilo ni daraka lako ukiwa mzazi. Iwe atakubali kwamba anahitaji msaada wako au la, binti yako anahitaji msaada wako. Huenda ukavunjika moyo na kuhisi kuwa hustahili, lakini usikate tamaa. Uwe na subira. Bila shaka baada ya muda, binti yako atathamini jitihada zako.(Chanzo:jw.org/sw)

Yasinta Ngonyani said...

Ahsante kwa kutokuwa mchoyo wa Elimu!