Thursday, February 15, 2018

TAULO ZA KIKE!...........


































NIMEKUTANA NA HII MADA  IMENIGUSA SANA EBU KUWA SAMBAMBA NAMI....
LEO nimekumbuka moja kati ya matukio yaliyopata kuniumiza sana hapo zamani. Nakumbuka nilikuwa darasa la sita, Shule ya Mazoezi Mwenge, mkoani Tabora.
Siku hiyo, nikiwa nimeketi dawati la mbele kabisa darasani, lilizuka kama zogo maeneo ya katikati ya darasa; wanafunzi wakawa wamesimama; wengine wakicheka, wengine wakionekana kufadhaika. Kusogea eneo la tukio, nikamwona binti mmoja (jina ninalihifadhi) akiwa ameketi juu ya dawati ilhali wenziye wakiwa wima wamemzunguka.

Nikiwa sijatanabahi juu ya kilichotokea, baadhi ya wasichana wakamwinua mwenzao, kisha wakamfunga sweta kiunoni ili limsitiri sehemu ya nyuma. Aliposimama, ndipo nikaona kilichotokea. Damu ilienea kwenye sketi yake huku nyingine ikibaki kwenye dawati. Wenziye kadhaa wakaungana naye kumsindikiza nje ili kumpa nguvu. Lakini mambo ya kitoto, bila kujua hofu na fadhaa vilivyomuathiri kisaikolojia mwenzetu, baadhi (hususan wavulana) wakawa wakishangilia na kumcheka.

Siku kadhaa zilipita bila msichana yule kurudi shuleni. Baadaye tulikuja kujulishwa kuwa, aligoma kurudi kwa aibu na fadhaa. Alipoteza kabisa hali ya kujiamini, akawa anawataka wazazi wake wamuhamishe shule.

Kimsingi, wanapokuwa katika hali kama hii, watoto wa kike hudhalilika na kufadhaika mno. Na hata wanapowahi kujitambua, bado wanakosa namna bora, yenye heshima na staha katika kujistiri. Inafikia pahala, mtoto wa kike anashindwa kusaidia kazi nyumba na anakosa kwenda shuleni kwa kushindwa kumudu gharama za taulo za kike (pedi) ili kudhibiti hali hiyo na kuwa huru. Kama taifa tunashiriki kumfelisha mtoto wa kike kwa kujua ama kutokujua.

Leo ninapoikumbuka kadhia hiyo, niliyoishuhudia nikiwa mdogo shuleni, nabaki nikistaajabu kusikia ati kuna wanaojiita viongozi, halafu wanazuia na kukwamisha hoja ya kuitaka serikali itoe ruzuku ili wanafunzi wa kike wagawiwe taulo hizo bure mashuleni au walau kwa bei ya chini. Leo hii, imefikia mahala huko vijijini, kwa uhaba wa taulo za kike, mtu akibahatika kuipata anatamani aivae hata mwezi mzima bila kuivua.

Tazama maajabu sasa, kondomu zinapatikana kwa bei chee na wakati mwingine kugawiwa bure kabisa, kwa sababu zinapewa ruzuku na serikali ilhali kufanya au kutokufanya ngono ni uamuzi wa mtu. Lakini linapokuja suala la taulo za kike ambapo, hakuna msichana anayeweza kuamua kutopata hedhi, unasikia watu wanaamua kuzuia hoja ya kutolewa ruzuku. Aibu gani hii - ujinga gani huu.
Mmnfyuuuuuuuuu


Maundu Mwingizi (MwanaBalagha),
Dar es Salaam.

1 comment:

ray njau said...

Kukabiliana na Matatizo ya Kukoma kwa Hedhi

“Ghafula nilihisi nimelemewa na huzuni bila kujua sababu. Nililia na kuanza kujiuliza ikiwa ninarukwa na akili.”—Rondro, * mwenye umri wa miaka 50.

“Unaamka asubuhi na kupata nyumba yako ikiwa shaghalabaghala. Huwezi kupata kitu chochote unachotafuta. Mambo ambayo ulikuwa ukifanya kwa urahisi, sasa yanaonekana kuwa magumu sana, na hujui ni kwa nini hali iko hivyo.”—Hanta, mwenye umri wa miaka 55.

WANAWAKE hao si wagonjwa. Wanapitia tu kipindi cha kukoma kwa hedhi, ambacho ni badiliko la kiasili katika maisha ya mwanamke anapoacha kuwa na uwezo wa kupata watoto. Ikiwa wewe ni mwanamke, je, unakaribia kipindi hicho? Au je, unapitia kipindi hicho sasa hivi? Vyovyote vile, kadiri ambavyo wewe na wapendwa wako mnajifunza kuhusu kipindi hiki cha mabadiliko, ndivyo mtakavyoweza kukabiliana kwa njia inayofaa na matatizo yanayohusiana nacho.
Kipindi cha Kukoma Hedhi

Wanawake wengi huanza kipindi hicho wakiwa na umri wa miaka 40 na kitu, lakini wengine huanza wakiwa wamechelewa wakiwa na miaka 60 na kitu. * Kwa wanawake wengi, hedhi hukoma hatua kwa hatua. Kwa sababu ya kubadilika-badilika kwa kiwango cha homoni kinachotokezwa, huenda mwanamke akakosa kupata hedhi pindi kwa pindi, akapata hedhi wakati ambao hakutarajia, au akavuja damu nyingi isivyo kawaida wakati wa hedhi. Wanawake wachache hukoma kupata hedhi ghafula, yaani, wanakosa hedhi mwezi mmoja na huo unakuwa mwisho wa kuipata.

Kitabu kuhusu kukoma kwa hedhi (Menopause Guidebook) kinasema: “Kipindi hicho huwa tofauti kwa kila mwanamke.” Kitabu hicho kinaendelea kusema hivi: “Matatizo ya kawaida yanayohusiana na kipindi hicho ni kupata joto la ghafula mwilini,” ambalo huenda likafuatwa na kuhisi baridi. Dalili hizo zinaweza kumfanya mtu akose usingizi na kuishiwa na nguvu. Matatizo hayo huendelea kwa muda gani? Kulingana na kitabu hicho, “wanawake fulani hupatwa na joto la ghafula mwilini kwa mwaka mmoja au miwili wakati wa kipindi hicho cha kukoma kwa hedhi. Wengine hupatwa na hali hiyo kwa miaka mingi, na wachache sana husema kwamba wao hupatwa na joto la ghafula mara kwa mara maisha yao yote.” *

Kwa sababu ya kubadilika-badilika kwa kiwango cha homoni, huenda mwanamke akashuka moyo, hisia zake zikabadilika-badilika na hilo linaweza kumfanya alielie bila sababu, na pia asiwe makini sana na asahau mambo. Licha ya hayo, kitabu The Menopause Book kinasema kwamba “kuna uwezekano mkubwa kwamba mwanamke hatapatwa na mambo hayo yote.” Kwa kweli, wanawake fulani hupata matatizo machache sana na wengine hawapati matatizo yoyote wakati wa kipindi hicho.
Jinsi ya Kukabiliana na Kipindi Hicho

Kubadili mtindo wa maisha kunaweza kupunguza baadhi ya matatizo hayo. Kwa mfano, wanawake wanaovuta sigara wanaweza kupunguza mara ambazo wanapatwa na joto la ghafula kwa kuacha kuvuta sigara. Wanawake wengi hunufaika kwa kubadili mazoea yao ya kula kama vile kupunguza au hata kuacha kunywa kileo, vinywaji vyenye kafeini, na vyakula vyenye sukari au vikolezo ambavyo vinaweza kusababisha joto la ghafula mwilini. Bila shaka, ni muhimu kula vyakula mbalimbali na vyenye lishe.

Kufanya mazoezi husaidia sana kupunguza matatizo yanayohusianishwa na kukoma kwa hedhi. Kwa mfano, mazoezi yanaweza kupunguza kukosa usingizi na kusaidia kuboresha hali ya kihisia na pia kuimarisha mifupa na afya ya mtu kwa ujumla. *
Eleza Mambo Waziwazi

Rondro aliyenukuliwa mwanzoni mwa makala hii anasema hivi: “Usiteseke kimyakimya. Ukiwaeleza wapendwa wako mambo waziwazi, hawatakuwa na wasiwasi kuhusu hali yako.” Jambo hilo linaweza kuwafanya hata wakuonyeshe subira na huruma zaidi. “Upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili,” linasema andiko la 1 Wakorintho 13:4.

.------------------
--------------
chanzo:www.jw.org/sw