Wednesday, October 7, 2015

SHUJAA WETU HAKUSALITI JAMAA ZAKE NA UTAWALA WAKE.....!!!!!


Nduna Songea Mbano, muda mfupi kabla ya kuuawa
Nduna Songea: Shujaa wa Wangoni aliyewapeleka puta wajerumani..SHUJAA WETU HAKUSALITI JAMAA ZAKE NA UTAWALAWAKE..!!. HUWEZI kuielezea na kuikamilisha historia ya vita ya Majimaji na ukombozi wa nchi yetu
bila kumtaja shujaa wa kabila la Wangoni, Nduna Songea Mbano ambaye jina lake lilipewa hadhi ya kuuita mji wa Songea kutoka kwenye jina la Ndonde mwaka 1906.
Kiongozi huyo alikuwa ni miongoni mwa wasaidizi ( Nduna) 12 wa Chifu wa kabila la wangoni (Nkosi) chifu Mputa bin Gwezerapasi Gama. Wasaidizi wake wengine walikuwa ni Mgendera Mawaso Gama, Kohongo Magagura, Mputa Mkuzo Gama, Magodi Mbamba Mbano, Mtekateka Muyamuya Tawete, Fratela Fusi Gama. Manduna wengine ni Maji ya Kuhanga Komba, Zimanimoto Gama, Mpambalyoto Soko Msalawani, Mtepa Hawaya Gama na Nduna Mkomanile ambaye alikuwa ni mwanamke pekee kuwa nduna.
Nduna Songea Mbano alikuwa maarufu kuliko manduna wenzake na hata chifu Mputa Gama alikuwa anamtegemea sana katika kuwaongoza manduna na wapiganaji
wa vita ya Majimaji kiujumla.  Mhifadhi kiongozi wa Makumbusho ya Taifa ya Majimaji Songea, Philipo Maligissu
akizungumzia maisha ya Nduna Songea Mbano katika viwanja vya Makumbusho hayo, anasema kuwa Nduna Songea Mbano weledi ndio uliompa umaarufu sana.
Kutokana na weledi na ushadi wake, aliwazidi wenzake 11 katika mbinu za kuandaa mikakati ya kivita, kutoa uamuzi mzito pasi na kutetereka na kusimamia utekelezaji wake kikamilifu.
Kwa umakini mkubwa, Nduna Songea Mbano aliweza kufanya kile alichokuwa akikiamini na uthibitisho wa jambo hilo ulianza kujitokeza Julai 12, 1897 katika viwanja vya Bomani kwa mkuu wa Wilaya wa Wajerumani, Luteni Engelhardt.
Maligissu anasema rekodi zilizopo zinaonesha kuwa tarehe hiyo Nduna Songea Mbano, alionekana kuwa ni mtu wa kipekee katika idadi ya manduna 11 ambao walikuwa wasaidizi
wa Chifu Mputa Gama kwa kitendo chake cha kubisha wazi wazi tamko la utawala mpya wa Wajerumani la kutaka Wangoni wakomeshe biashara ya utumwa.
Siku hiyo ilikuwa ni rasmi ambayo utawala wa kikoloni ulikuwa unaanzishwa katika mji wa Songea, wakati huo ukiitwa Ndonde na Mkoa wa Ruvuma kiujumla ukiwa chini ya Luteni
Engelhardt aliyekuwa Mkuu wa Jeshi Kanda ya Kusini.
Wajerumani walipofika kuanzisha makoloni yao katika maeneo ya ukanda wa kusini walikutana na msuguano mkubwa kutoka kwa tawala za Kiafrika, hasa tawala za Wangoni.
Maligissu anasema kuwa Wangoni walikuwa na tabia ya kwenda mikoa ya Lindi na Mtwara
kuvamia, kuchukua mateka na kuwapeleka Songea kuwafanyisha shughuli mbalimbali katika maeneo yao ya utawala wao.
Tabia hiyo ya Wangoni iliwachukiza sana Wajerumani, kwani walikuwa wanaheshimu sana makubaliano yaliyofikiwa kutoka kwenye mkutano wa Berlin wa 1884 /85.
Katika mkutano huo moja ya makubaliano ni na kila nchi yenye koloni barani Afrika ikomeshe biashara ya utumwa, hasa ikizingatiwa kwamba Wajerumani walikuwa wamejiimarisha sana.
Hivyo walipofika Ruvuma wakatoa tamko kwa Wangoni kuwa hairuhusiwi na haitaruhusiwa tena kwenda Lindi, Mtwara au kokote kuchukua mateka na kwamba mateka wote waliochukuliwa na Wangoni waachiwe huru.
Baada ya Wajerumani kutoa tamko hilo, ndipo Nduna Songea Mbano alipojitokeza waziwazi
na kusimama kujibu hoja iliyotolewa na Wajerumani kuhusu tamko hilo.
Nduna Songea Mbano alisema kuwa utawala wa kabila la Wangoni hauwezi kutekeleza tamko hilo na kwamba msimamo wao ni kutoutambua utawala mpya wa Kijerumani na tamko lao.
Kwamba ujio wa Wajerumani na tamko lao kwa Wangoni vililenga kudhoofisha utawala wa machifu na manduna katika maeneo yao kwa kufuata kanuni zao za kimila na kitamaduni.
Kuanzia hapo Wajerumani walimwona Nduna Songea Mbano kuwa ni mtu hatari sana katika utawala wao mpya, hivyo kumweka alama maalumu na kuanza kumfuatilia nyendo zake.
Alionekana kuwa kiongozi shupavu mwenye misimamo mikali na anayezingatia heshima na utu wa kabila lake bila kuyumbishwa. Alionekana kuwa pekee mwenye uwezo mkubwa wa kufanya kazi katika mazingira yoyote kwa kushirikiana na wananchi wake ambao walikuwa
wanamheshimu sana na kumsikiliza.
Maligissu anaeleza kuwa Nduna Songea Mbano alikuwa na uwezo mkubwa wa kuwaunganisha
wananchi wake na kuwa na umoja, upendo na mshikamano na kwamba alikuwa akiwaelekeza jambo wanalifanya kwa umakini na kwa ukamilifu.
Nduna Songea Mbano aliendelea kujizolea umaarufu mkubwa na baada ya kutamka kuwa yupo tayari kwa lolote lile na hawezi kukubali kuona tawala za Kiafrika zinadharauliwa na wakoloni kwa namna yeyote ile.
Wajerumani wakaamua kuwaalika machifu na manduna wote Julai 13, 1897 Bomani kwa mkuu wa wilaya na kuwaambia kuwa mtu yeyote katika eneo lake atakayekaidi amri yoyote kutoka kwa uongozi mpya wa Wajerumani atapigwa risasi, kunyongwa hadi kufa au kufungwa maisha. Siku hiyo hiyo machifu na manduna walichukuliwa hadi juu ya mlima wa shabaha wa Chandamari, katikati ya mji wa Songea na kuoneshwa nguvu ya risasi inavyoweza kufanya kazi katika mwili wa binadamu na kwamba silaha za kijadi na kimila za Wangoni hazingeweza kufua dafu mbele ya silaha hizo.
Licha ya Wajerumani kutoa vitisho vingi, Nduna Songea aliendelea na msimamo wake wa awali wa kuchukia na kuupinga utawala wa Wajerumani na kuutetea utawala wa Kiafrika mpaka ilipokuja kutokea Vita ya Majimaji. Nduna Songea alitoa ushindani mkubwa sana katika vita hivyo na kuonesha ustadi mkubwa kwenye mapigano na katika sehemu zote ambazo Wajerumani walipigana, wameandika kuwa hawakupata ushindi mkubwa kama waliopata katika mkoa wa Ruvuma, zamani nchi ya Ungoni.
Viongozi wao hawakuwa wanafiki, kwani walijitoa kikwelikweli kusaka ukombozi na hadhi ya tamaduni zao mpaka dakika ya mwisho. Ndio maana idadi kubwa ya watu walionyongwa katika historia ya Tanzania walitoka katika himaya ya Nduna Songea Mbano na ushahidi upo wazi kuwa watu 67 walihukumiwa kunyongwa hadi kufa, akiwamo Nduna Songea Mbano.
Katika kuonesha kuwa Nduna Songea alikuwa na uwezo wa kufanya mambo kwa weledi mkubwa bila kusaliti dhamira yake kuanzia mwaka 1897 aliandaa jeshi lake la kupambana na utawala wa Wajerumani.
Akaanza kuchukua watu wake na kuwapeleka juu ya mlima wa Chandamari kufanya nao mkutano, kutoa mafunzo ya kivita na kuwaelekeza kwa nini Wajerumani wachukiwe.
Katika mlima huo ndipo alipoeleza kwa kina madhara ya kuukubali utawala wa Wajerumani
na kutoa ahadi kwa wananchi wake ya kuwaondoa Wajerumani kwa lazima na kuwa eneo hilo ni la Wangoni, wamekuwa wakiishi siku zote chini ya utawala wao, hivyo haiwezekani wapelekewe utawala mpya wakati hawauhitaji.
Chokochoko hizo zilizaa vita vya Majimaji na wakati mapigano yakiendelea Wajerumani walianza kumtafuta Nduna Songea ili wamkamate na kufanya naye mazungumzo ya maridhiano.  Kumbe Songea Mbano alikuwa amejificha kwenye pango kubwa lililopo kwenye mlima wa Chandamari na usiku alikuwa akikutana na askari wake nje ya pango hilo na kuwapa mafunzo zaidi ya kivita.  Maligissu anaeleza kuwa Nduna Songea alikuwa anaishi na ndugu zake katika eneo la Mateka, leo hii manispaa ya Songea na wakati wa vita ndipo Songea Mbano alikuwa anajificha katika pango hilo ili wasimkamate mpaka atakapotimiza malengo yake.  Wajerumani walipoona wanaendelea kupata madhara makubwa kutokana na vita hivyo, waliamua kuwakamata ndugu na familia yake, Chifu Mputa Gama na manduna wengine na kuwafunga gerezani kwa lengo la kumdhoofisha Nduna Songea.
Baada ya Wajerumani kumdhoofisha Nduna Songea alipata taarifa zote na akaamua kutoka
kwenye pango hilo na kwenda kwa Wajerumani na kutaka watu wake waachiwe ili mapigano yaendelee.  Ndipo naye alipokamatwa na kuswekwa gerezani na Wajerumani wakawahukumu wafungwa hao kunyogwa hadi kufa.  Wafungwa hao waliamriwa kuchimba shimo kubwa bila kujua ndilo lingekuwa kaburi lao na ilipofika siku ya kifo chao, walinyongwa kwa zamu kwa muda wa siku mbili na maiti zao kuwekwa kwenye kaburi hilo hadi walipofikia 66 ndipo walizikwa kwa pamoja.  Walimwacha Nduna Songea Mbano ili awasaidia kutimiza malengo yao kwa wananchi, kwani waliamini akiwa kiongozi jasiri na anayependwa na watu wake angesikilizwa vizuri. Tangu siku hiyo walipomwacha bila kumnyonga, Nduna Songea aliwasumbua Wajerumani na kutaka naye anyongwe kama ndugu zake, kwani hakuona sababu ya yeye kuishi wakati ndugu zake alishauawa; akasema wasipomnyonga angegoma kula na kunywa chochote mpaka afariki dunia. Ndipo Wajerumani walipoamua kumnyonga na kumzika katika kaburi la peke yake, wakiamini kuwa ni mtu wa pekee mwenye ushujaa, uamuzi mzito na msimamo usioyumba. Walimuenzi kwa kubadilisha jina la mji wa Ndonde na kuubatiza jina la Songea, ambapo mpaka sasa linatumika kuuita mji huo wenye hazina kubwa ya historia na utalii wa kitamaduni.
KATIKA PITAPITA MTANDAONI NIMEKUTANA NA HII MADA YA KIHISTORIA YA WANGONI  NIKAONA SI MBAYA KAMA NIKIWEKA HAPA MAISHA NA MAFANIKIO UKIZINGATIA ASILI YANGU NI MNGONI....PANAPO MAJALIWA TUTAONANA TENA......NA CHILAWU MEWAWA/NA KESHO HIVYOHIVYO
 

2 comments:

Ndugu Nkwazi N Mhango said...

Hii kitu nimeipenda kwani ni darasa tosha

Yasinta Ngonyani said...

Kaka Mhango! Yaani kama vile uliyaona mawazo yangu ya kuweka hili somo hapa sikutaka kufaika pake yangu...Ahsante kwa kusema kila kilicho ndani ya roho yako. PAMOJA DAIMA:-)