Tuesday, February 1, 2011

KWA NINI WANAUME/AKINA BABA WENGI WANAFIKIRI WAO NDIO WAAMUZI/WAFALME WA NYUMBA?

Suala hili limekuwa likinikera sana akilini mwangu kwa miaka mingi. Ya kwamba akina baba/wanaume wao wanafikiri kazi yao kubwa katika nyumba ni kuwa MUME/BABA basi. Mara nyingi utasikia wanasema mimi ndio mkubwa wa nyumba. Na kama wanafanya kazi za ofisini basi ndo itakuwa kero mno. Kwani hapa atataka anaporudi toka kazini akute chakula mezani, maji ya kuoga bafuni tena ya moto, nguo zmepigwa pasi n.k. Na kinyume kama hana kazi basi atakuwa anashinda kilabuni(UGIMBI) na akirudi toka huko basi ni kelele tu, hakuna amani wala maelewano

Bado naendelea, kuna wengine wanaona kupika, kulea watoto, kutafuta chakula ni kazi ya wanawake. Yaani hawawezi hata kujipikia chai kwa vile wao ni wanaume au hata kumbadili mtoto nepi, Mtoto amabaye ni wake. Kikubwa wanachofanya ni kukaa kitini/sofani na kuletewa kile wanachotaka. Wanasahau kabisha jambo la USAWA.

Bado wanaishi dunia ya mababu, mababu na mababuzi. Tuache UBINAFSI tuishi kwa kushirikiana/kusaidiana kwani wote ni SAWA. Nasema tena tuishi kwa kusaidiana hapo wote tutafurahia maisha. Tuache mambo ya UTUMWA

18 comments:

Anonymous said...

Dada Hyacinta asante kwa habari yako nzuri ya kufikirisha. Huko nyumbani kwako salama lakini ? Mume na watoto wote wanaendelea vyema ? Basi nakutakia maisha na mafanikio mema. !!

Yasinta Ngonyani said...

usiye na jina ahsante kwa kuipenda habari hii. Na ahsante kwa kuuliza hali zetu wote salama tu nawe nakutakia yote mema.

kamala Lutatinisibwa Lutabasibwa said...

wanaume ni kama watoto, tunahitaji kujaliwa, kuangalia, kupetwa petwa na hata kubebwa migongoni

Anonymous said...

Hapa yamechanganywa mambo mengi mno katika kapu moja.Yasinta kama unataka tufike huko unakotaka tufike chukua kipengele kimoja tu na kukichanganua hicho na kukishikilia hadi uone utekelezaji wake.Mambo mengi pamoja utashangaa hakuna hata moja litakalotekelezwa hadi siku hiyo jua litakapozama mara ya mwisho

Simon Kitururu said...

Kuna mambo mengi yanasababisha wanaume wawehivyo!

Kiasili kuna wakati MWANAUME ndio alikuwa mtafutaji wa kila kitu cha nyumbani hasa kipindi MWANAMKE kajifungua tukiachilia mbali enzi za kuwinda kwa mishale butu ya miti nk.


Kibaolojia na KIASILI mwanamume ndio mweny bonge la misuli kutokana na jamii enzi hizo ya kujichanganya msitu huohuo na SIMBA na chui mwanamume akawa mlinzi na muamuzi wa mengi ya mpaka ulinzi wa FAMILIA.

KIUCHUMI na kiasili: Binadamu walipo anza kuishi katika vijiji na sio kuhamahama shughuli za ulinzi wa eneo kutoka kwa binadamu wengi ne likazidi kuwa ni la wanaume ambao kabla ya mabunduki bado kimkong'oto walikuwa wanaweza kushusha zaidi kuliko wanawake kitu kilichofanya mpaka kufikia kuwa ni MWANAMUME ndio mwenye ardhi kwa kuwa ndio ailindaye hata wakati mwanamke hajiwezi kutokana na ujauzito , watoto wadogo na kadhalika. Na aliyemiliki ardhi akawa ndio muamuzi .

Ukifuatilia kazi gani zilienda zaidi kwa wanawake na zipi kwa wanaume utagundua ni mchanganyiko wa MAUMBILE kibaolojia na mpaka kiuchumi nani alilinda na kuwezesha familia kuishi salama salmini. Na kwa ujumla fuatilia tu historia ya binadamu na utajua ni kwanini tumefikia hapa.

Na ukiangalia jinsi gani MORANI wa KIMASAI hawana kazi siku hizi za KIMORANI kwa kuwa jamii imebadilika. Utagundua kuwa tatizo hilo haliwagusi MAMORANI tu wa KIMASAI ambao ni wapiganaji vita na hakuna vita wahusishwavyo. Jamii imebadilika kote na siku hizi kazi ya mtu haijali sana JINSIA ya mtu ingawa kwa kuwa JAMII ni vigumu kubadilika kirahisi. Bado WANAUME wanacheza role walizocheza tokea enzi za mababu tatizo tunaishi katika ulimwengu wa DOT.COM

Kwahiyo DA YASINTA:
jibu la swali lako ni kwamba MAZINGIRA yamebadilika ila WANAUME hawajabadilika haraka kufikia ilipo dunia ya sasa ambayo kiongozi wa nchi na sekretari wa mjumbe wa nyumba kumikumi wote katika kazi zao wanatumia misuli sawa kudokoadokoa KEY BOARD ya COMPUTER.


NI MTAZAMO TU!

Goodman Manyanya Phiri said...

Vumilieni tu, Dada zetu. Kwa utafiti wakisayansi kabisa sisi tutakwisha duniani nanyi mbakie.Mtakuja kutukumbuka tukishatolewa hapa ardhini!

http://www.examiner.com/sex-relationships-in-newark/men-will-be-extinct-appreciate-them-now

chib said...

Kama vile nakubaliana kubaliana na Kitururu. Kuna suluba nyingine wanawake wao wenyewe husema hizo ni kazi za wanaume, labda wakiondoa hiyo dhana, kunaweza kukaja mabadiliko mengine ikiwamo na kibayolojia!
Mjadala zaidi unahitajika

Anonymous said...

Wanawake wenyewe wana jukumu kubwa kwa nafuu yao wenyewe. Hivi, bila kuwa na jazba lolote bali kwa upendo wote:
1.Wapendane na wasaidiane wao wenyewe
2.Wachangamkie mambo yenye tija mfano elimu, wasome kwa bidii bila kutegemea upendeleo
3.Watekeleze vema na kwa ufanisi majukumu yawapasayo, mfano wabunge wanawake wawasaidie wanawake wenzao hasa wa vijijini.

Anonymous said...

Laiti ningeiona hiyo siku ambapo watabakia wanawake tu ulimwenguni! Kutakuwa na amani kweli?

Mija Shija Sayi said...

Yasinta hiyo tabia ilikuja polepole wanawake tukaikubali na kuona sifa. Tuliona sifa kumshughulikia mume kwa kila jambo, tuliona sifa kumuachia baba atoe maamuzi yote kwa vile tu ana misuli na pia kutafuta kupendwa zaidi na mume. Sasa wanaume wamezoea inakuwa ngumu kujishusha.

Kama tukitaka kuiua tabia hiyo ni lazima wanawake tubadili mtazamo wetu wa maisha, ni lazima tuamini tunaweza kutoa maamuzi bila msaada kutoka kwa mwanaume na si kuamini tu bali na kutenda pia.

Goodman Manyanya Phiri said...

Nao utafiti unatuletea habari mpya kweli ya kwamba

["wale wanaume wenzetu wenye 'ustaarabu' wakuwasadia wake zao shughuli zote zile za wanawake 'kidesturi' hasa katika mambo ya kulea watoto, INAWEZEKANA KABISA WANACHEZEA MOTO KAMA SIYO KULILIA WEMBE NDOANI"]

Toleo la mwezi wa January 2011 la gazeti (JOURNAL) liitwako: DEVELOPMENTAL PSYCHOLOGY ndio linatupasha hizo habari kwa kupitia mmoja wa waandishi juu ya huo utafiti (kutoka Chuo Kikuu cha Dola Ohio), Ms Sarah Schoppe Sullivan.


Utafiti unapendekeza:

"BABA, CHEZA NA MTOTO TU BASI! KUMWOGESHA, MARA UNAMWANDALIA MTOTO CHAKULA NA MAMBO KAMA HAYO, ACHIA MKEO AFANYE NA AMANI MNAYO KATIKA NYUMBA YENU NA MSAIDIE MKEO MTABISHANA BURE JUU YA HUYO MTOTO!"


http://blogs.forbes.com/meghancasserly/2011/01/27/university-of-ohio-parenting-father-involvement-coparenting/

o'Wambura Ng'wanambiti! said...

Duh!

emu-three said...

Miminashindwa nisemeje, kwasababu najiuliza `kwanini...kama ndivyo ilivyo...'
Nafikiri ili kwanini `iondoke' ni lazima hatua ichukuliwe...kwanza angalia nini mwanaume anafanya na wewe fanya hivyo...mume wako ni mjenzi, ni msukuma mkokoteni, ni nani vile, basi fanya afanyavyo, halafu mwisho wa siku unamwambia siumeone, nimefanya yako yote sasa ni zamu yako kufanya yangu! KIVITENDO TUTAWEZA, LAKINI KIMANENO TUTABAKAI KULUMBANA...
Ni wazo tu dada yangu!

Rachel Siwa said...

mmmhhhh mimi nashindwa nasiye wanawake nao mmhh baba mmoja wanawake ameoa na ni wake zake zaidi ya mmoja,achana na nyumba ndogo,Na hao wanawake wanawachukulia wanawake wenzao,ukimuuliza umeolewa hapana ila ninashea!!!!!!!wanaume watazidi kuwajuu maana kama mko wanawake 3 wewe ukataka huo usawa na wenzio hawataki,wao wanafanya kama anavyosema kaka KAMALA JE Wataacha kuwa Wafalme wa Nyumba?

Yasinta Ngonyani said...

Napenda kuchukua nafasi hii na kuwashukuruni wote kwa michango yenu mizuri na ya kuelimisha. Na ni ruksa kuendelea na mjadala....

Mtesuka said...

Dada Yasinta, kwanini umefikiri hivyo? Je historia yetu inatuambia nini juu ya hilo? Na wanatasnia ya -ke, wanasemaje? naomba unisadie hapo!

Yasinta Ngonyani said...

Kaka Mtesuka kwanza za magono!!
Nimesema hivi kwasababu ni muda mrefu nimekuwa nikilitafuta jibu kwanini ipo hivi na isiwa kinyume, kuwe na UMOJA. Na kuhusu historia yetu inasema nini usifikiri sijui. Lakini kuna vitu/vijambo vingine mwanamume anaweza kujituma na kumsaidia mwanamke ili mke asiwe mchovu. Na kwa vile wanawake tumeikubali hali hii na kuona sifa basi ndo maana ipo hivyo. UMOJA NI NGUVU.Na naamini wanawake nao wanaweza haswaa kufanya maamuzi peke yao au kwa pamoja.

Penina Simon said...

Biblia husema wazi kuwa mwanaume ndio kichwa cha nyumba, kumbuka hata makanisani wamezuiliwa kusema, lakini mabadiliko yanavyokuja katika ulimwengu huu wanawake hawataki kuwa nyuma tena, wala kusubiri ruhusa kwa waume zao.wanataka kuondoa huo mfumo. lakini Mwanaume ndiye aliyeumbwa wa kwanza, na mwanamke kumegwa kutoka kwake ikionyesha kuwa ni lazima awe sehemu ya mumewe.