Showing posts with label JUMATANO ELIMU. Show all posts
Showing posts with label JUMATANO ELIMU. Show all posts

Wednesday, May 16, 2012

Wanafunzi wanasomea vibanda vya nyasi!!

Ni ile JUMATANO YA KIPENGELE CHA MARUDIO NA LEO NIMEONA TUTEMBELEE WILAYANI NAMTUMBO.ELIMU NIMEIPATA HABARI HII  Albano Midelo Haya KARIBUNI. 



 Wanafunzi wa darasa la tano katika shule ya msingi
 SelousWilayani Namtumbo wakiwa darasani.

WANAFUNZI wa shule tatu za msingi zaidi ya 500 katika kata ya Rwinga wilayani Namtumbo mkoani Ruvuma wanasomea kwenye madarasa yaliojengwa kwa miti na kuezekwa kwa nyasi.
Uchunguzi uliofanywa katika shule tatu kati ya saba zilizopo kwenye kata hiyo ambayo ipo mjini Namtumbo umebaini kuwa katika shule ya msingi Rwinga wanafunzi 296 wanasomea kwenye vibanda vya miti vilivyoezekwa kwa nyasi.
.
Mwalimu wa taaluma katika shule hiyo Onesmo Mbawala alisema idadi kubwa ya wanafunzi katika shule hiyo wanasomea katika vibanda vya nyasi kutokana na shule hiyo kuwa na upungufu wa vyumba 12 vya kusomea ambapo vyumba vilivyopo ni vinne tu na kwamba shule hiyo iliyoanzishwa mwaka 1975 ina jumla ya wanafunzi 592.
Katika shule ya msingi Selous jumla ya wanafunzi 108 wa madarasa ya tano na sita wanasoma kwenye vibanda vya nyasi hali ambayo walimu wanasema inachangia kushusha taaluma kwa wanafunzi.
Mwalimu wa taaluma katika shule hiyo Sheweji Simba alisema shule hiyo iliyoanzishwa mwaka 2007 ina jumla ya wanafunzi 477 huku ikiwa na vyumba vinne tu vya madarasa kati ya mahitaji ya vyumba nane hali ambayo imesababisha baadhi ya wanafunzi kusomea kwenye vibanda vya nyasi .
Katika shule ya msingi Mkapa ambayo imepewa jina la aliyewahi kuwa kiongozi mkuu wa nchi Rais mstaafu Benjamin Mkapa pia kuna wanafunzi wanaosomea kwenye vibanda viwili vya nyasi kwa kuwa shule hiyo ina vyumba vinne tu kati ya mahitaji ya vyumba nane.
Mkuu wa shule hiyo Hans Mwailima alisema shule hiyo yenye wanafunzi 306 madarasa matatu yanasomea katika chumba kimoja ambapo kuanzia darasa la tatu hadi la sita wanasomea kwenye vibanda vya nyasi kwa zamu .
“Unajua wanafunzi wana tabia ya kutaniana hivyo endapo darasa moja wakisoma kwenye vibanda vya nyasi kila siku wenzao wanawatania hivyo kukata tamaa na wengine kuwa watoro hivyo tumeamua wote wawe wanasoma kwenye vibanda vya nyasi kwa zamu ili kujenga mvuto wa mazingira ya kusomea’’,alisema.

Wanafunzi wa shule ya msingi Mkapa Wilayani
Namtumbo wakiwa darasani na mwalimu wao.

Mratibu elimu kata ya Rwinga Thomas Komba amekiri shule tatu kati ya saba katika kata yake ambazo ni Rwinga,Mkapa na Selous wanafunzi kusomea katika vibanda vilivyojengwa kwa miti na kuezekwa kwa nyasi na kusisitiza kuwa shule za Minazini,Kidagulo,Migelegele na Mandepwende ndizo shule pekee katika kata hiyo ambazo hazina vyumba vya madarasa vilivyoezekwa kwa nyasi.

“Shule zangu tatu za Rwinga,Mkapa na Selous katika kata yangu zinakabiliwa na upungufu mkubwa wa vyumba vya madarasa hali ni mbaya tunafanya jitihada za kuhamasisha jamii ili waweze kujitolea kufyatua tofali kuzichoma kwa kushirikiana na serikali ili kupata vyumba zaidi na kumaliza kero hii ya aibu’’,alisisitiza.
Makamu mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo Kasimu Ntara alidai kuwa kuwa kuwepo kwa madarasa yaliojengwa kwa miti na kuezekwa kwa nyasi katika wilaya hiyo kunatokana na kuanzishwa shule nyingi za msingi .
“Mpango wa uboreshaji wa elimu ya msingi MEM nchini ulisababisha kuanzishwa kwa shule nyingi hivyo baada ya kuondoka kwa MMEM serikali imeshindwa kumudu ujenzi wa vyumba vya madarasa jitihada zinaendelea kufanyika kukabiliana na upungufu wa vyumba vya madarasa’’,alisisitiza.

TUKUTANE TENA JUMATANO IJAYO KWA JINGINE LA ZAMANI!!

Wednesday, September 28, 2011

MASUALA YA UBAKAJI NA KUPIGA WANAWAKE LINAZIDI KUWA KUBWA

Kama kawaida kile kipengele chetu cha marudio ya Makala/mada, picha au kwa ujumla tusemematukio mbalimbali kitujiacho siku ya kila siku ya JUMATANO ungana nami kujadili jambo hili.Ukitaka kusoma maoni yaliyotolewa na wasomaji mara ya kwanza bonyeza hapa.
Kweli huu ni ubinadamu jamani?
Dunia imeharibika watu wanazidi kupotoka, angalieni haya mambo yanavyozidi kuenea. Mambo kama vile unyanyasaji, kuna ukatili mwingi sana hapa duniani ambao zaidi ni juu ya wanawake na watoto. Hao ndio wanaopata shida zaidi. Ukatili ni kinyume na haki za binadamu na uko ukatili wa aina mbalimbali. Kuna vipigo, matusi, kulazimishwa kufanya mapenzi, kuna baadhi ya mila potofu kama vila ndoa za lazima, kuolewa ukiwa na umri mdogo, kurithi wajane nk.
Bado sijaelewa ni kitu gani kinawafanya wanaume wengine wawapige wanawake. Kwanini umpegi mwenzi wako? Je usipompiga uanaume wako utapotea? Na kuna raha gani kumpiga mwenzako kama mnyama? Na hata mnyama hairuhusiwi kumpiga. Hili suala la kubaka utasikia raha gani wakati mwenzako anapata maumivu yasiyo kifani. Na pia hajapenda.
Je? Mnafikiri hii inaweza kutokana na wengi wanaume wanafikiri wao ndio waamuzi wa kila kitu ndani ya nyumba? Na kwa nini watu wawili waliooana wasikaa chini na kujadiliana na kuona kosa liko wapi. Je? Ingekuwa kinyume ingakuwa sawa?

Au labda wengi wanafuata maandishi haya:- Mwanzo 3:16 Akamwambia mwanamke, Hakika nitakuzidishia uchungu wako, na kuzaa kwako, kwa uchungu utazaa watoto na tamaa yako itakuwa kwa mumea, naye atakutawala.
Ndugu wasomaji/wanablog naomba mnisaidie kunipa jibu.

Wednesday, September 21, 2011

YASINTA NGONYANI NA JOHARI YA MATUMAINI

Kama kawaida kile kipengele chetu cha marudio ya Makala/mada, picha au kwa ujumla tuseme matukio mbalimbali KUTOKA BLOG HII YA MAISHA NA MAFANIKIO NA BLOG NYINGINE MBALIMBALI. Ni kipengele kitujiacho kila siku ya JUMATANO. Leo nimefanya upekuzi na nimekukutana na simulizi hii kwa vile inanihusu nimeona ni vema niiweka hapa kama kumbukumbu/mkusanyiko. Ukitaka kusoma maoni yaliyotolewa na wasomaji mara ya kwanza bonyeza Nyasa. karibuni sana.
Nafungua anuani pepe nakuta ujumbe, najiuliza kulikoni ni nani huyu? Alaah kumbe mwana wa nyasa, aliye ughaibuni? Ni mwanzo wa kumbukumbu, furaha na burudani. Mzaha wa hapa na pale kustawisha gumzo. Mtandaoni kwa saa nyingi mazungumzo yasokwisha hamu? Hatimaye ndiyo huyu tupo uso kwa uso tunazungumza tunapiga gumzo hapa na pale najiuliza maswali kadhaa kuhusu huyu mtu lakini najua ni mungu ajuaye mengi.
Mawazo yangu yaavaa uhodari wa kujua na kutaka kuona kile ninachoamini. Siku zinapiga miezi, mwaka na saa zote. Nipo ghorofa ya pili, nasoma ghafla ujumbe mfupi unaingia katika simu, salamu toka ughaibuni, najiuliza nitende vipi kwa mwandada huyu? nafunika vitabu na daftari, namtazama mwenzangu pembeni ananikodolea macho anashangaa vipi naacha kusoma halafu nachezea simu? Namweleza kuna jambo, nataka kuongea na mtu kwanza.Tayari tunajadili hili na lile najadili mambo kadhaa yenye maudhui ya nyasa, halafu tunakumbushana mambo ya Lundo na maisha kwa ujumla.
Inawezekana usinielewe msomaji wangu mpendwa, lakini mantiki yangu ni kukupa mwanzo wa YASINTA NGONYANI na MARKUS MPANGALA. Ni kama andiko la wakristo la yesu alivyowaambia msihangaike kwa lolote wala msibebe vyakula bali mwendako mtajaziwa. YASINTA ni kiumbe mwenye sifa ambazo kila siku naziwazia, najaribu kutafakari, nakumbuka stori zetu za hapa na pale, nakumbuka yale mambo ya WAOOOOOOOOOOO!!!!1 Hee kumbe hatuko peke yetu, tunatulia na kutafakari, tunaleta mzaha kidogo na kustawisha gumzo, mambo ya hapa na pale. Usisahau tupo umbali wa maili nyingi lakini ikawa dakika kuwepo ana kwa ana.
Mimi sinywi soda, situmii pafyumu, wala mafuta makali, siweki dawa nywele zangu daima ni rasta. Nauliza swali aaaahh ndiyo maana Erick naye anapenda sana Rasta siyo? Kicheko kidogo..., namtazama kwa shauku ya kujua mengi....LAKINI nagundua kama kile alichosema Koero kuwa YASINTA NGONYANI ni binti wa kitanzania. Sifa moja kubwa aliyonayo ni MAZOEZI na ukimtazama ni unaweza kubabaika ukasema umri wake ni 23 au 26 hivi kumbe huyooooo.
Hapa nyumbani nina bustani ya matunda na mambo mengi ya nyumbani wala siwezi kubabaikia hayo mambo ya wazungu. Mi hee unaweza kudhani mtu unayezungumza naye anatania lakini kukweli ni binti mwenye itikadi msimamo mkali. Nakumbuka nipo Mbeya, nikabandikwa maaswali lukuki, stori nyingi lakini kikubwa ni faraja za hapa na pale.Msomaji wangu, huyu Yasinta nina mengi ya kumwelezea lakini nafupisha na kutoa vipande ili upate msingi kamili. Hata hivyo nimemlazimisha kucheza muziki wa KWAITO anacheza usipime kabisaa, majuzi nikamwambia ebu selebuka na MYEKE BABA ya Mandoza... akacheka kidogo.
Nikumbushe msomaji YASINTA ni mkarimu, mtulivu, mkali, mwenye upendo, smikivu, mdadisi ndiyo maana nilimwita Mama Maswali magumu, mchokonozi. Nakumbuka kuna kitu alinichokonoa lakini nikajua udadisi ukaanza.... tusijali hayo lakini nakwambia kama huwezi kuishi na YASINTA basi wewe ni kiumbe wa ajabu. Mara nyingi utamsikia Markus mdogo wangu unatakiwa kujali muda wa kupumzika, utulivu na kujenga afya kwa kufanya mazoezi....Wakati mwingine inakuwa kama unaota kulala gizani na kulamba mchanga halafu huchafuki kumbe upo ukwelini na unawaza ukweli uleule wa siku zote.
Sikiliza mimi nataka kufanya kitu fulani katika blogu, nifanyeje? Ahh tunachapa gumzo tunafundishana haya na yale. Na fundsho letu kuu la mwisho lilikuwa pale ufkweni kuhusu NeoCounter. Ni mambo matamu ya teknolojia.SWALI UNAJUA ALIANZAJE KUBLOGU NA KUIJUA BLOGU YA KARIBUNI NYASA?Kuna kisa cha YASINTA katika blogu yangu hii ambayo naomba msomaji ukitafute. na mara nyingi amenihimiza kuandika tena kwani amevutiwa nacho.Kumbe kuna siku alikuwa akitafuta akina YASINTA wenzake wapo wangapi duniani, .... ndiyo hapo akutana na KARIBUNI NYASA na kisa kile cha Yasinta mwenzake. vilevile nilimpatia kazi ya kuchoma samaki kama unakumbuka msomaji kuna TANGAZO LA KAZI NYASA, yeye ndiye alishinda. Ila anapenda sana kula MAEMBE halafu na tabia yake ya KUNYWA CHAI ISIYO NA SUKARI yaani CHINGAMBU ni moja ya vionjo vyake na ambavyo nakiri ni MTANZANIA.Nikamwambia niseme au nisiseme kile kitu fulani....... aaaah Msomaji wangu utanichoka nadhani unaweza kudhani nafanya mzaha. Lakini kiini chake ujue tu ni binti ambaye naona tofauti yake na wengine ni mtazamo na misimamo yake isiyotetereka. Ni mdadisi sana huyu kiumbe, hachoki kujifunza kila mara lakini ndoto yake ilikuwa SISTA yaani wale watawa... utakumbuka ndoto yangu ilikuwa kuwa Padre lakini yamepita...SAHAU. Nakumbuka nikawa namlazimisha kumsoma kaka Ansbert Ngurumo....
Upendo wake na namna anavyoweza kujadili na watu ni kitu ambacho kinanifanya wakati mwingine nimwambie nina wivu sana, na hilo sifichi na nimesema daima ana anajua hilo. Mungu kamleta kwa kusudio la kupendwa na watu wala hana mengi. JE UNATAKA NIKUWEKEE PICHA TULIZOPIGA? aaaaaaahh msomaji nadhani hii stori ndogondogo ni habari kamili ingawaje imekaa mshazari. mtanisamehe kwa kutoweka picha tulizopiga.....Watoto wake anawaeleza kabisaaa..... nakumbuka anasema na Camilla.... mwanangu funga kanga , lazima kutii utamaduni wetu sawa? Camilla huyoooo anatoka ndani ya bwawa... anaiendea kanga.... mrembo huyu anachukua na kuifunga mwendo wake wa maringo taratibuuu kama twiga najongea mezani. Pembeni Erick sijui kiswidi chao wanasema Irik au? Kijana mpenda mazoezi kama mamake... anafuga rasta.... lakini siku hizi kazinyoa bwana...... a ha ha ha ha!
YASINTA GERVAS NGONYANI.... ngoja nikutaji jina leke jingine..... aaaah hapana siyo ruksa ni mimi tu nalijua au vipi usitake kujua sana. Ni kweli Yasinta mpenzi wa lugha ya nyumbani na bahati nzuri ni mtundu wa kujua lugha za wengine, najua ni wachache wanamudu hilo... lakini ameweza kujifunza lugha za wanyasa wale wanaongea kama wamalawi.... zile MULIBWANJI.... halafu tunahamia mazungumzo katika kimatengo... kingoni chenyewe, kimanda, kimpoto.... kinyakyusa..... nk. ukitaka kufanikiwa maishani ni lazima ujue utamaduni wako na kuheshima na utajua wapi unatoka.....YAKO MENGIIIIII SAANAAAAAAA............................... tutahabarishana siku nyingine.... manake kuna siri, mafanikio, shubiri na mwenendo mzima wa maisha yake.... harakati zake........ NITAKUMEGEA MAMBO MSOMAJI WANGU, na usisahau kumsoma pale kwa dada Koero( huyu naye subiri simulzi zake nimekuandalia ndugu msomaji na nitajibu maswali ya wanablogu fulani walioniuliza kuhusu YASINTA na hata huyu Koero) sawa? we tulia tuuuuuu Mwisho wa juma mwema!!! NA TUONANE TENA JUMATANO IJAYO!!!!

Wednesday, September 7, 2011

Moyo wangu!!

Kama kawaida yetu na bila kusahau leo ni ile siku ya KIPENGELE chetu ambayo hutujia kila JUMATANO na leo siku hii inawapelekeni mpaka hapa kwa diwani ya fadhili....karibuni sana..


Usiuache mpweke, maumivu kuufika,
Siufanye uteseke, machozi yakanitoka,
Ufanye ufarijike, upe moyo uhakika,
Moyo wangu.

Upatie unafuu, upunguzie mawazo,
Uweke daima juu, sikalie matatizo,
Siupige kwa miguu, na kuupa mizevezo,
Moyo wangu.

Uondolee karaha, siuweke taabuni,
Ufanye kuwa na raha, sizamishe majonzini,
Utawalwe na furaha, cheko tupu maishani,
Moyo wangu.

Usiutendee hivyo, moyo wangu taumia,
Ukitenda ndivyo sivyo, kitanzi utautia,
Vyovyote vile iwavyo, elewa wakuzimia,
Moyo wangu.

TUKUTANE TENA JUMATANO IJAYO KATIKA KIPENGELE CHETU HIKI.....KILA LA KHERI.

Wednesday, June 15, 2011

NDOA YA MALAIKA HAIJAWAHI KUWEPO DUNIANI!!!

Kama kawaida leo ni jumatano ambayo ni siku ya kile KIPENGELE CHETU CHA MARUDIO haya karibuni tujumuike nami!!!!!





Wakati mwingine misukosuko ya ndoa huwaliza wanawake,


lakini hizo zote ni changamoto !


Kuna kudanganyana kwingi kuhusu ndoa pale mtu anaposhindwa kuwa mwangalifu sana kwa kauli za wengine walio kwenye ndoa. Hii hutokana na ukweli kwamba kuna kujumuisha kwingi sana. Kuna wakati huwa tunasikia au kuambiwa kwamba ndoa ni sawa na jehenamu. Baadhi ya watu walio kwenye ndoa kuna wakati huzungumza kwa njia ambayo hutufanya tuamini kwamba kuoa au kuolewa ni jinai. Ndoa ni ujinga mtupu haina maana, mtu anaweza kusema. Wasemaji hawa wanaweza kuwa ni watu tunaowaamini sana kama wazazi wetu na wengine wa aina hiyo.
Baadhi ya watu badala ya kuponda na kubeza kuizungumzia kama kitu kizuri sana kisicho na doa wala chembe ya usumbufu. Inawezekena kabisa nasi tukawaamini wazungumzaji hao, hivyo kuamini kwamba, ndoa hazina usumbufu.
Inawezekana dhana hii ikaingizwa vichwani mwetu wakati tukiwa wadogo au hata tukiwa watu wazima. Hebu fikiria juu ya mtu ambaye anajisifu kwamba ndoa yake haina hata chembe ya mkwaruzo. Ambaye anaieleza ndoa yake kwa njia yenye kushawishi kuwa, kumbe ndoa zenye matatizo siyo ndoa bali kisirani kitupu. Kama nawe uko kwenye ndoa na ndoa hiyo ina matatizo hata madogo unaweza kudhani kwamba ulikosa kuoana na huyo mwenzako. Dhana hiyoinaweza kuchipuka kutokana na kauli kama hiyo inayoelezea ndoa kama kitu kisicho na mikwaruzo hata kidogo.
Kama usipokuwa mwangalifu unaweza kuacha kuchukua hatua za kujaribu kuondoa tofauti zilizo kwenye ndoa yenu. Utaacha kufanya hivyo kwa sababu mtu fulani atakuwa tayari ameingiza kichwani mwako uongo kwamba ndoa ni “asali” na “maziwa” matupu. Ni uongo kwa sababu hakuna ndoa isiyo na mikwaruzo.
Tunatakiwa kujua kwamba lengo la ndoa siyo kuepuka kukorofishana , hapana . Ukweli ni kwamba kukorofishana kunapotumiwa vema huweza kujenga uhusiano mzuri na imara sana. Kwa sababu kukorofishana hakuwezi kuepukika kwenye ndoa kunatakiwa kutumika kama shule na dawa ya kuimarisha ndoa.
Bila kukwaruzana kwenye ndoa zetu inaweza ikawa vigumu sana kwetu kubandua tabaka la uongo lililotufunika ambalo humfanya kila mmoja kati yetu kushindwa kuona na kumfahamu mwenzake katika tabia yake halisi.
Bila kukwaruzana, kila mmoja wetu atajidanganya kwamba anamfahamu mwenzake kama alivyo wakati siyo kweli. Tunapokwaruzana tunapata nafasi ya kufahamiana vizuri katika hali halisi.
Mwanamke mmoja maarufu aliwahi kuulizwa kama huwa anakwaruzana na mumewe. Alikiri kwamba huwa wanakwaruzana kwa kusema , “ndiyo tunakwaruzana, vinginevyo tungekuwa hatuna tofauti, na hapo bila shaka ndoa na maisha vingekuwa vimepooza sana”. Huo ndiyo ukweli wenyewe, kwamba bila kukwaruzana hatuwezi kufahamiana vema na kujua kwa undani tofauti kati yetu na wenzetu.
Inabidi tujue kwamba hakuna binadamu aliyekamili, yaani asiyekosea, kama ilivyo dunia yenyewe. Kwa hali hiyo hakuna ndoa ambayo haina makosa, kwa sababu ndoa ni binadamu hao ambao siyo kamili. Kwa hiyo, mtu anapotarajia kuwa au kuishi kwenye ndoa isiyo na kukwaruzana, ni sawa na mtu huyo kutarajia kukutana na binadamu ambaye ni kamili, yaani asiyekosea.
Kutarajia kuwa na ndoa ambayo haina kukwaruzana kunaelezwa kuwa ni chanzo kizuri sana kwa ndoa nyingi kulegelege au kuanguka kabisa. Mtu anapoingia kwenye ndoa akitarajia kwamba huko hatapambana na maudhi au kero za aina fulani, ni lazima ajue kwamba, hatadumu kwenye ndoa yake kwa sababu ndoa hiyo anayoitarajia haipo.
Mtu ambaye hakubali au angalau hataki kuelewa kwamba, ndoa ni lazima iwe na mikwaruzo anaweza kukabiliwa na tatizo lingine baya zaidi kwenye ndoa yake. Kwa kutokujua au kuepuka kukwaruzana, hawezi kuwa tayari kukubali kujadili migogoro ya kindoa ili kupata ufumbuzi. Hawezi kulikubali hilo kwa sababu haamini kwamba ndoa yenye kukwaruzana ni ndoa.
Wakati mwingine rafiki, ndugu au jamaa zetu hutusimulia jinsi ndoa zao zisivyo na kukwaruzana kama kwamba ni za malaika watupu. Bila kujua, huwa tunajikuta tumewaamini. Tunapowaamini huwa tunachukulia kukwaruzana kuliko kwenye ndoa zetu kama jambo au kitu ambacho hakikutakiwa kuwepo. Hapo hujikuta tukitamani kuondoka kwenye ndoa hizo kwa matarajio kwamba tunaweza kukutana na “malaika” ambao tutajenga nao ndoa zisizo na doa.
Hata pale ambapo tunasema wanandoa wanapendana sana, bado ndoa yao ni lazima itakuwa na kukwaruzana. Lakini wanachofanya hawa na ambacho huenda wengine hawafanyi ni kujadili tofauti hizo sawia na kuamua kuzisahau na hapo wote kukubali kujifunza kutokana na tofauti hizo.
Wale walio tayari kujadili tofauti zao sawia ndiyo ambao ndoa zao huwa na afya sana hadi wengine kushangaa kama siyo pamoja na kuona wivu. Wale wanaodhani ndoa ni mahali pa kila jambo kwenda kama mtu atakavyo, ndoa zao hupogoka vibaya na kufa kwa kishindo........

Makala hii nimeitoa katika Gazeti la Jitambue la hayati Munga Tehenan.

TUONANE TENA JUMATANO IJAYO PANAPO MAJALIWA!!!