Monday, July 31, 2017

TWENDE KWETU RUVUMA : JINA LA SONGEA NA UMAARUFU WAKE



NGULI WA VITA VYA MAJIMAJI 1905-1907 NDUNA SONGEA MBANO..


JINA la Songea limekuwa maarufu kiasi cha kuwafanya baadhi ya watu kudhani kuna mkoa unaitwa Songea.
Ukweli ni kwamba Songea ni wilaya iliyopo katika mkoa wa Ruvuma na jina hilo linatokana na shujaa wa Wangoni, Nduna Songea Mbano. Ni vigumu kuilezea historia ya vita ya Maji Maji bila kutaja jina la Songea, shujaa huyo wa Wangoni kutokana na mchango wake mkubwa katika kupigania haki na uhuru wa Waafrika.

Songea alikuwa mtu mwenye sifa ya kipekee kutokana na uwezo wake mkubwa wa kufanya kazi bila kuchoka na katika mazingira magumu . Aliwashirikisha wananchi wake katika kufanya maamuzi na kujijengea mazingira yaliyomfanya kila mtu amuamini, kumsikiliza na kumheshimu.

Nduna Songea Mbano alikuwa ni shujaa aliyesimama kidete na kupinga hoja ya utawala wa Kijerumani ambao ulionekana wazi unataka kudhalilisha utawala wa kabila la Wangoni. Songea alisimama kidete na kusema waziwazi kuwa  Wangoni hawawezi kuutambua utawala mpya wa kijerumani.

Hivyo kutokana na ujasiri wake, baada ya wajerumani kuwashinda vita kwa taabu dhidi ya Wangoni ,jina lake hilo likapewa hadhi ya mji wa Songea badala ya jina halisi la ‘Ndonde’ mwaka 1906. Kiongozi huyo alikuwa ni miongoni mwa wasaidizi ( Nduna) 12 wa Chifu wa kabila la Wangoni (Nkosi) Chifu Mputa bin Gwezerapasi Gama.

Wasaidizi wengine ni Mgendera Mawaso Gama, Kohongo Magagura, Mputa Mkuzo Gama, Magodi Mbamba Mbano, Mtekateka Muyamuya Tawete na Fratela Fusi Gama. Wasaidizi wake wengine wa Chifu Mputa ni pamoja na Nduna Maji ya kuhanga Komba, Zimanimoto Gama, Mpambalyoto Soko Msalawani, Mtepa Hawaya Gama na Nduna Mkomanile ambaye alikuwa ni mwanamke pekee kuwa na wadhifa huu wa Uduna.

Nduna Songea Mbano alikuwa ni maarufu kuliko manduna wenzake na hata chifu Mputa Gama alikuwa anamtegemea sana katika kuwaongoza Manduna wenzake na wapiganaji wa vita ya Maji Maji. Ofisa Elimu Msaidizi wa Makumbusho ya vita ya Maji Maji ya Songea, Erick Soko , anaelezea sifa za ziada alizokuwa nazo Nduna Songea katika kuongoza vita vya Maji Maji dhidi ya wakoloni wa kijerumani.

Soko anayaelezea maisha ya Songea kuwa alitokea kupata umaarufu mkubwa ikilinganisha na wenzake 11 kwa kuwa alikuwa na ueledi na ustadi wa kuandaa mikakati ya kivita, na kutoa maamuzi mazito yasiyotetereka na kuyasimamia kikamilifu. Umakini wake mkubwa ni kufanya kile alichokuwa akikiamini na uthibitisho wa jambo hili ulianza kujitokeza julai 12, mwaka 1897 katika viwanja vya Bomani kwa Mkuu wa Wilaya wa Kijerumani, Luteni Engelhardt.

Soko anaeleza kuwa rekodi zilizopo zinaonyesha tarehe hiyo alionekana kuwa ni mtu wa kipekee katika idadi ya Manduna 11 waliokuwa wasaidizi wa Chifu Mputa Gama . Hatua hiyo ilitokana na kitendo chake cha kubisha wazi wazi tamko la utawala mpya wa Wajerumani la kuwataka wangoni wakomeshe biashara ya utumwa.

Kwa mujibu wa Soko, siku hiyo ilikuwa ni siku rasmi ambayo utawala wa kikoloni ulikuwa unaanzishwa kwenye mji wa Ndonde , wakati huo kabla ya kuitwa mji wa Songea. Mji wa Ndonde katika mkoa wa Ruvuma ulikuwa chini ya Luteni Engelhardt wa Jeshi la Kijerumani, alikuwa ni Mkuu wa Kanda ya Kusini.

Hivyo anasema, wakati Wajerumani walipofika kuanzisha makoloni yao maeneo ya ukanda wa kusini walikumbana na msuguano mkubwa kutoka kwa tawala za Kiafrika hasa utawala wa Wangoni. Soko anasema , wangoni walikuwa na tabia ya kwenda mikoa ya Lindi na Mtwara kuvamia na kuchukua mateka na kuwaleta Songea kuwafanyisha shughuli mbalimbali katika maeneo yao ya utawala.

Hata hivyo anasema , tabia hii ya Wangoni iliwachukiza Wajerumani, ambao walikuwa wanaheshimu makubaliano yaliyofikiwa katika mkutano wa Berlin wa mwaka 1884 hadi 1885. Soko anasema makubaliano hayo yaliyofikiwa ni kila nchi yenye koloni barani Afrika ni lazima ikomeshe biashara ya utumwa na nyakati hizo Wajerumani walikuwa wamejiimarisha katika mikoa ya Lindi na Mtwara.

Hata hivyo anasema, Wajerumani walipofika Ruvuma wakatoa tamko kwa Wangoni haitaruhusiwa tena kwenda Lindi, Mtwara na maeneo mengine kuchukua mateka na mateka wote waliochukuliwa waachiwe huru ili kukomesha biashara ya watumwa. Hivyo anasema , baada ya Wajerumani kutoa tamko hili ndipo Nduna Songea Mbano alipojitokeza waziwazi na kusimama na kuipinga hoja ya Wajerumani kuhusiana na tamko hili.

“Songea alipinga hoja hiyo mbele ya utawala wa Kijerumani akisema utawala wa kabila la wangoni hauwezi kutekeleza tamko hilo na msimamo wao ni kutoutambua utawala mpya wa kijerumani na tamko lao, ”anaelezea Soko. Kwa mujibu wa Kiongozi huyu wa Wangoni ujio wa utawala wa Wajerumani ulikuwa na lengo la kudhoofisha utawala wa Machifu na Manduna katika maeneo yao.

Historia inaeleza kuwa Wangoni waliona kufuata kanuni za Wajerumani, watapoteza mila za kitamaduni za Wangoni. Kutokana na msimamo wa Nduna Songea Mbano , kuanzia hapo Wajerumani walimuona kuwa ni mtu hatari katika utawala wao mpya na walimuweka alama maalumu na kuanza kumfuatilia nyendo zake.

Misimamo yake hiyo ilizidi kujenga umaarufu mkubwa na matamshi yake mbele ya Wajerumani kuwa yupo tayari kwa lolote lile na hawezi kukubali kuona tawala za kiafrika zinadharauliwa na wakoloni kwa namna yoyote ile. “Songea alikuwa na uwezo mkubwa wa kuwaunganisha wananchi wake wawe na umoja, upendo na mshikamano na kila anapotoa maelekezo wafuasi wake wanayatekeleza kwa umakini na kwa ukamilifu,” anaelezea Soko.

Ili kuonesha alikuwa na uwezo wa kufanya mambo kwa uweledi mkubwa bila kusaliti dhamira yake , mwanzoni mwa mwaka 1897 alianza kuandaa jeshi lake la kupambana na utawala wa Wajerumani. Hatua ya kwanza aliwachukua watu wake na kuwapeleka katika mlima wa Chandamari uliopo kati kati ya mjini na kufanya nao mkutano ulioendana na kutoa mafunzo ya kivita na kuwajengea ujasiri wa kuwachukia Wajerumani.

“ Wakiwa kwenye mlima huo ndipo alipoeleza kwa kina madhara ya kuukubali utawala wa Wajerumani na kutoa ahadi kwa wananchi wake ya kuwaondoa Wajerumani kwa lazima.” Soko anaelezea . Songea Mbano aliwafahamisha wafuasi wake ya kwamba eneo hilo ni mali yao na wamekuwa wakiishi siku zote chini ya utawala wao , inakuwaje waletewe utawala mpya wa Wajerumani wakati hawauhitaji.

Hata hivyo mnamo Julai 13, 1897, utawala wa Wajerumani waliamua kuwaalika machifu na manduna wote Bomani kwa Mkuu wa Wilaya wa kwanza katika eneo la ungoni. Amri ya kualikwa kwao ilitolewa na Mkuu wa Jeshi la Wajerumani katika eneo la ungoni, Luteni Engelhardt .

Machifu na manduna wa Wangoni waliambiwa mtu yeyote katika eneo lake atakayekaidi amri yoyote kutoka kwa uongozi mpya wa Wajerumani atapigwa risasi, kunyongwa hadi kufa au kufungwa maisha . Katika kuwatisha watakaokaidi amri ,machifu na manduna walichukuliwa hadi katika mlima wa kulenga shabaha unaojulikana ‘ Mlima Chandamari’ uliopo kati kati ya mji wa Songea.

Walipofikishwa hapo Wajerumani walionesha nguvu ya risasi inavyoweza kufanya kazi katika mwili wa binadamu na kwamba silaha za kijadi na kimila za wangoni haziwezi kufua dafu mbele ya silaha zao. Licha ya Wajerumani kutoa vitisho vingi, Nduna Songea Mbano aliendelea kushikilia msimamo wake wa awali wa kuuchukia utawala wa Wajerumani na kuutetea utawala wa Kiafrika mpaka ilipotokea vita ya Maji Maji.

Wakati huo , Nduna Songea Mbano alikuwa amejificha kwenye pango kubwa lililopo kwenye mlima wa chandamari na usiku akiwa anakutana na askari wake nje ya pango hili na kuwapa mafunzo zaidi ya kivita. Hata hivyo anaelezea kuwa, wakati mapigano yakiendelea Wajerumani walianza kumtafuta Nduna Songea Mbano ili wamkamate kwa lengo la kufanya naye mazungumzo ya maridhiano.

Katika vita hii Nduna Songea Mbano alitoa ushindani mkubwa kwa Wajerumani na alionesha ustadi mkubwa kwenye mapigano na sehemu zote ambazo Wajerumani walipigana. Hivyo anaeleza kuwa, Wajerumani walipoona wanaendelea kupata madhara makubwa kutokana na vita hivi waliamua kuwakamata ndugu na familia ya Nduna Songea Mbano.

Waliomakatwa ni pamoja na Chifu Mputa Gama na Manduna wengine ambao walifungwa gerezani likiwa ni lengo la kumdhoofisha Nduna Songea Mbano. Baada ya kumdhoofisha nguvu ya jeshi lake , Nduna Songea Mbano aliamua kutoka kwenye pango alikojificha na kwenda kwa Wajerumani ili kutaka watu wake waachiwe huru.

“ Hakufua dafu katika mpango huu, naye alikamatwa na kuwekwa gerezani na Wajerumani waliamua kuwahukumu wafungwa wote kunyongwa hadi kufa akiwemo chifu wa kabila la Wangoni Mputa Bin Grazerapasi Gama,” anaeleza Ofisa Elimu huyu. Katika jambo la kusikitisha, Ofisa Elimu Msaidizi wa Makumbusho haya anasema kuwa, wafungwa hawa waliamuliwa kuchimba shimo kubwa bila kujua shimo hilo ndilo litakalotumika kuwa kaburi lao.

“ Ilipofika siku ya kunyongwa walinyongwa kwa zamu siku mbili na maiti zao kwenda kuwekwa kwenye kaburi walilokuwa wamelichimba wakiwa hai hadi wote 66 na kuzikwa kwa pamoja kwenye kaburi “ anaelezea Ofisa Elimu huyu. Hata hivyo Wajerumani walimuachia Nduna Songea Mbano aweze kuwasaidia kufikisha malengo yao kwa wananchi wakiamini kuwa yeye ni kiongozi jasiri na anayependwa na watu wake na hivyo kusikilizwa vizuri.

Kwa mujibu wa kumbukumbu za kihistoria zilielezwa na Ofisa Elimu Msaidizi wa Makumbusho haya ya Maji Maji Songea, kuwa tangu siku walipomuacha bila kumnyonga aliwasumbua Wajerumani. Kutokana na maelezo ya kumbukumbu hizo, Nduna Songea Mbano alitaka naye anyongwe kama ndugu zake kwani haoni sababu ya yeye kuishi wakati ndugu zake wamekufa.

Hata hivyo anaeleza kwa kusema “ Nduna Songea Mbano aliwaeleza Wajerumani hao kwa kusema kama hawataki kumnyonga basi hataki kula wala kunywa chochote mpaka afe. Uamuzi huo , ndio uliwasababishia Wajerumani kuamua kumnyonga na kumzika katika kaburi la peke yake .

Wajerumani wakiamini kuwa ni mtu wa pekee mwenye ushujaa na maamuzi mazito na misimamo isiyoyumba na walimuenzi kwa kubadilisha jina la mji wa Ndonde na kuuita jina la Songea. Tangu wakati huo mpaka sasa linatumika kuuita mji huu jina la Songea ambao ni wenye hazina kubwa ya historia na utalii wa kitamaduni

Katika pitapita mtandaoni nimekutana na hii nikaona si mbaya niiweke hapa kibarazani.

Wednesday, July 26, 2017

MAKABILA TANZANIA: UTAJIRI WA KUJIVUMNIA

Je? wewe kabila lako ni lipi hapo? Tujenge Taifa letu. Tutumie utajiri wa makabila yetu kuwa na Taifa imara na lenye mshikamano wa hali ya juu. PAMOJA DAIMA!

Tuesday, July 25, 2017

ELIMU:- WAZAZI TUNAFIKIRI WATOTO WANAPATA ELIMU KUMBE WANAFANYA MIRADI KUINGIZA FEDHA KWENYE MFUKO WA SHULE...

Tutafika kweli kwa mtindo huu? Nimekumbuka mbali sana wakati ule nasoma shule ya msingi, kubeba tofali, kulima mashamba, kukata nyasi, kusomba kuni nk. aise kwa kweli tumehinya sana miaka ile...

Sunday, July 23, 2017

NAWATAKIENI JUMAPILI NJEMA

......Hayo mnayajua, ndugu zangu wapenzi, basi kila mtu na awe mwepesi wa kusikia bali si mwepesi wa kusena wala kukasirika....
Yakobo 1:19..
AMANI ITAWALE NYUMBANI WENU.

Thursday, July 20, 2017

MWANZO MGUMU.... LAKINI BUSTANI YETU INAANZA LEO RASMI....

 Hatimaye bustani yetu inaanza kuridhisha. Ni mchicha,  figiri na mboga maboga
 Ukiwa  na sehemu ndogo  usikata tamaa panda kwenye makopo au ndoo...hspa ni nyanya
Na hapo ni pilipili hoho na mboga maboga  ujanja eeehhh:)

Tuesday, July 18, 2017

Friday, July 14, 2017

NGOMA YA ASILI YA LIZOMBE/KITOTO YA WANGONI SONGEA RUVUMA


NAWATAKIENI MWISHO WA JUMA UWE MWEMA MWENYE FURAHA NA AMANI....PAMOJA DAIMA!

Thursday, July 13, 2017

KARIBUNI TUJUMUIKE MLO WA JIONI HII YA LEO

Ugali, samaki wa kukangaka halafu kuungwa na tui la nazi, mboga majani kidogo na maharagwe. NAWATAKIA JIONI/AU LABDA MCHANA AU ASUBUHI....KAPULYA WENU.

Monday, July 10, 2017

TUANZE JUMATATU NA PICHA HII!

JUMATATU NJEMA IWE YENYE FURAHA NA AMANI! NALIPENDA VAZI HILI SANA....

Sunday, July 9, 2017

UJUMBE WA JUMAPILI YA LEO...KUTOKA KWA BLOG YA MAISHA NA MAFANIKIO

Sisi binadamu daima tunafanya kazi kwa kutumaini siku ya kesho itakuwa  bora lakini wakati kesho inafika badala ya kufurahi, basi sisi tuanaanza kunafikiria kesho tena itakuwa bora?  Hebu tuwe na siku ya leo sio kila wakati kufikiria ubora  wa kesho. MAISHA NI MAFUPI UPATAPO WASAA FURAHIA....JUMAPILI NJEMA

Friday, July 7, 2017

TUMALIZA WIKI NA PICHA HII

Sijui kama ningethubutu kukaa hapo juu ya mikungu ya ndizi. TUPO PAMOJA NA MWISHO WA JUMA UWE WENYE FURAHA NA AMANI.  KAPULYA. ...

Tuesday, July 4, 2017

HAPA VIPI TENA?

Sasa hapa imekaaje tena? wasomaji tusaidiane hapa. Duh kaaazi kwelikweli hapa.

Monday, July 3, 2017

BUSTANI...NILIMTEMBELEA DADA YANGU MMOJA KWENYE BUSTANI YAKO HII NZURI

MCHICHA NA MAHARAGWE
Jana nilimtembelea dada yangu kwenye bustani yake. Ana bustani nzuri sana niliipenda sana na kumwonea wivu:-)  ila kwa upendo wake alinichumia mchicha mwingi tu nilimshukuru sana. Bustani yangu mwaka huu inasuasua....ila sijakata tamaa na hivyo nimeiona ya huyu dada nimepata nguvu zaidi......karibuni mtaona bustani yangu