Showing posts with label serikali. Show all posts
Showing posts with label serikali. Show all posts

Thursday, January 31, 2013

Neno La Leo: Mwaka Ni Kama Noti Ya Elfu Kumi Ya Bongo, Ukiichenji​, Inapukutik​a!



Ndugu zangu,
Leo ni mwisho wa mwezi wa mwaka mpya. Na mwaka ulivyo ni kama noti ya shilingi elfu kumi ya Bongo. Ukiichenji tu, utashangaa inavyopukutika!
Ukae sasa ukijua, kuwa kesho ndio Februari Mosi. Hivyo, mwaka mpya wa 2013, kama ilivyo kwa noti elfu kumi, ndio tutakuwa tumeuchenji. Subiri sasa uone siku, wiki na miezi inavyopukitika. Fumba na kufumbua utasikia tumeshaingia Juni tunaelekea Bajeti ya Serikali ya Julai, na ukitoka hapo utafikiri mwaka unateremsha milima ya Kitonga.
Inatukumbusha nini?
Umuhimu wa kupanga mambo yetu. Inahusu muda na matumizi ya muda. Na mwanadamu usipokuwa makini na muda, itakuwa sawa na kisa kile cha mzazi aliyeulizwa na wanawe; " Mbona nguo za Krismasi hatujanunuliwa?"
Mzazi akawajibu wanawe; " Jamani, Krismasi ya mwaka huu imekuja ghafla sana!"
Kana kwamba hakujua, kuwa kwenye kalenda ya mwaka tarehe ya Krismasi imeshawekwa, Desemba 25!
Ndio, Afrika mvua hainyeshi ghafla, huwa kuna dalili zake. Na katika maisha, mambo mengi hayaji ghafla, bali hutukuta tukiwa hatujajiandaa. Jiandae na mwaka unaoanza kupukutika kuanzia kesho, kama noti ya shilingi elfu kumi. Kila la kheri.
Nimetumiwa na kaka Maggid Mjengwa.

Monday, July 9, 2012

Neno La Leo: Vita Hii Ya Serikali Na Madaktari Ikome Sasa!!!!


Ndugu zangu,
NCHI yetu ingali katika huzuni ya uwepo wa mgogoro kati ya madaktari wetu na Serikali yetu. Ni huzuni iliyochanganyika na hofu na mashaka.  Suluhu ya kushikana mikono haijapatikana.
Inasikitisha, maana, hii ni nchi yetu, wanaogoma ni madaktari wetu na inayogomewa ni Serikali yetu. Ni wananchi wa nchi hii wenye kutaabika na hata  kupoteza maisha yao kutokana na mgomo huu. 
Hili ni jambo la kuhuzunisha sana. Ni jambo lenye kuitia doa nchi yetu. Huko nyuma kuna tuliosisitiza, na hapa narudia kusisitiza msimamo wangu kama Mtanzania ninayeipenda nchi yangu, kuwa hakuna njia nyingine ya kuumaliza mgogoro huu bali ni kwa njia ya mazungumzo ya kindugu na kirafiki. Wahusika wana lazima ya kukaa kwenye meza moja kama Watanzania na kuitafuta suluhu ya mgogoro huu kwa manufaa ya nchi yetu na watu wake.
Kwa sasa kila upande unamwona mwenzake ndiye mwenye makosa. Hivyo, kila upande umejichimbia handakini na kuendeleza ' vita vya kuviziana'. Ukweli, katika vita hivi hakutakuwa na mshindi, maana, kama taifa, sote tumeshashindwa. Na tunaendelea kushindwa zaidi, maana, watu wetu wanaangamia kwa kukosa tiba ya uhakika.
Kimsingi madai ya madaktari ni ya msingi na yanazungumzika. Na hoja za Serikali ni za msingi na zinazungumzika. Hivyo, pande zote mbili zinaweza kuzungumza na kufikia muafaka. Si jambo la hekima kwa sasa kwa madaktari kuendelea na mgomo wao wakati milango ya mazungumzo haijatiwa komeo la shaba, na si hekima vile vile kwa Serikali ' kugomea' kuzungumza na madaktari kwa kisingizio kuwa suala hilo liko mahakamani.  Naungana na viongozi wa kidini walioisihi Serikali kufuta shauri hilo  na kuimaliza kadhia hii kwenye meza ya mazungumzo.
Ni vema na ni busara sasa kwa madaktari wakatangaza, kwa manufaa ya nchi  yetu, kuahirisha mgomo wao mara moja na kurudi kazini  kuwahudumia Watanzania kwa moyo wote. Wafanye hivyo  hata katika mazingira magumu waliyonayo,  wakati juhudi za kufikia muafaka na Serikali zikiendelea.
Maana, mgomo wowote ni jambo la hasara. Kila siku inayokwenda kukiwa na mgomo ina maana ya hasara kwa nchi na watu wake. Ni hasara ya fedha na uhai.  Ndio maana ya pande zote mbili zinapaswa kuhakikisha zinakutana na kutafuta suluhu ya kushikana mikono.
Na huko twendako, endapo kutatokea hali ya kutoelewana baina ya Serikali na madaktari, basi, Chama cha Madaktari kianze sasa kufikiria namna njema ya kuendesha migomo tofauti na hii ya sasa. Mathalan, katika kuishinikiza Serikali ingewezekana kuanza na mgomo kwa Hospitali moja na si nchi nzima. 
Ingewezekana pia isiwe kwa hospitali nzima bali vitengo kadhaa huku huduma kwenye vitengo vingine zikiendelea. Hata hilo pia lingewaletea usumbufu wananchi na kufikia kuishinikiza Serikali kwenye kujadiliana na madaktari  katika kuboresha maslahi yao. 
Lakini hili la ' Wild Strike' kwa maana ya mgomo wa nchi nzima lina' hatari ya kiafya' kwa taifa.  Tusifike mahala tukachangangia kuifanya nchi yetu wenyewe iende kwa kutambaa kutokana na migomo. 
Nimepata kuandika, kuwa katika  nchi zetu hizi, mganga wa tiba aliyesomeshwa kwa fedha za walipa kodi  na kwa miaka mingi anahitajika sana. Mganga wa tiba msaidizi anahitajika  sana. Na hata kama angelikuwapo Msaidizi wa Mganga Msaidizi wa tiba ,  naye angehitajika sana. Vivyo hivyo kwa wakunga wakuu na wasaidizi,  wauguzi wakuu na wasaidizi wao. Wote hao anahitajika sana.
Na  katika nchi zetu hizi, Serikali hazipaswi kufikia hatua ya kuwatisha na  hata kuwafukuza kazi madaktari. Hilo la mwisho lifanyike tu pale ambapo  njia nyingine zote za kumaliza tofauti na kusuluhisha migogoro na  madaktari zitakapokuwa zimeshindikana. Na kwa nini ishindikane?
Naam, Watanzania tungependa kuona vita hii baina ya Serikali na madaktari ikimalizwa haraka kwa kutafutwa suluhu ya kushikana mikono. Inawezekana.
Habari hii nimetumiwa na Mwenyekiti Mjengwa......

Thursday, September 1, 2011

Baada ya miaka 50 ya uhuru wa Tanganyika​, je Tanzania inakuhitaj​i?

Mwaka 2011, Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inasherehekea miaka ya uhuru wa serikali ya Tanganyika, taifa lililomezwa April 26, 1964 baada ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar. Kwa hesabu za haraka haraka utaona miaka hamsini ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itaadhimishwa April 26, 2014. Muungano wa Tanganyika na Zanzibar una faida na kasoro zake, lakini leo nitajadili mada inayouliza kuwa “baada ya miaka 50 ya uhuru wa Tanganyika, je Tanzania inakuhitaji?”.

Magwiji na wataalamu wa falsafa ya imani duniani, wanatuaminisha kuwa hakuna nguvu inayozidi upendo, wakidadavua zaidi husema kuwa penye upendo uliopea Mungu yupo. Hata ukitafakari maisha ya mahusiano tunayoishi, huna budi kumpenda mtu kwanza kabla hujaenda mbele zaidi kumpa nafasi ya kuwa mwenzi wako wa ndoa, katika muktadha huo ni kawaida kumwona kijana mwanamke akitoka bara la Amerika kufunga ndoa na kijana mume toka Mwanza, vivyo hivyo haishangazi kuona vijana wakivuka bahari na mito, milima na mabonde kutoka bara moja kwenda bara jingine kutafuta mapenzi yanayojengwa na upendo.

Hakika upendo ni nadharia ambayo hakuna maelezo yanayotosha kuidadavua kwa kilele chake. Bila shaka yoyote upendo miongoni mwa Watanganyika na Wazanzibar ndio uliozaa taifa la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa mtazamo wangu, upendo ule uliozaa muungano hapa Tanzania miaka 47 iliyopita, naona umepoa kama sio kufifia na kuchuja. Makala hii haitojadili nani amefifisha upendo huu hapa Tanzania.

Nakumbuka siku ile, taifa lilipotangaziwa kuhusu afya ya baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere, kuwa hali yake sio nzuri, Watanzania tuendelee kumuombea, mwili ulinisisimka kwa hofu. Nikapata baridi na hofu kuu, maswali mengi yalinikaba hasa nikijiuliza, itakuwaje nchi yangu bila “a great man, father of the nation?”. Hakika Mwalimu Nyerere alikuwa “great man”. Hata viongozi waliomzunguka wao pia walikuwa “great people”. Watanganyika hawa “great people” kizazi chao shurti kiwe “great generation”.

Wahenga walipata kusema kuwa “macho ni dirisha la fikra na ujasiri alionao mtu”, ukweli huu nauona kila ninapowatazama machoni Watanganyika nami nawaona kuwa na “great people”. Ujasiri huu tulionao hausemwi sana siku hizi, hivyo ipo haja ya kufanya kampeni ya makusudi miongoni mwa vijana wa Kitanganyika, hivyo upatapo fursa ya kushikana mkono na rafiki yako, vema ukamtazama machoni kwa walau dakika moja, kisha umwambie “you are a great person” kwa vile kila Mtanganyika ni kizazi cha “great people” ambacho ndio kiliasisi taifa la Tanganyika linalotimiza miaka 50 ya Uhuru tarehe 9 Desemba mwaka 2011.

“Great people” wale wakiongozwa na “great man” Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere walifanikisha kujenga misingi ya Taifa la Tanganyika na kufanikisha Muungano wa Tanganyika na Zanzibar mwaka 1964, kwa vile upendo baina yao ulipea, vivyo hivyo waliipenda nchi yao na watu wake. Ukweli ni kuwa Watanganyika ni "great people", japo utamaduni wa kuambiana ukweli huu haupo tena nchini Mwetu. Nasisitiza kuwa Watanganyika ni kizazi cha “great people” kwa vile Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere aliweza kuwakaripia viongozi wa mataifa yenye nguvu za uchumi kama Amerika na Uingereza haya Israel pale alipoona matendo ya mataifa hayo yanaathiri kwa makusudi ustawi wa nchi zenye uchumi mdogo, kwa Mwalimu, kigezo cha ubinadamu hakikuwa uchumi bali ubinadamu wenyewe.

Mwalimu Nyerere hakuishia kukemea mataifa makubwa pekee, bali alikemea pia viongozi wa ndani ya Tanganyika ambao nia zao binafsi zilikuwa zinakinzana na maendeleo ya nchi yetu. Mwalimu hakusita kuanika udhaifu, uchafu na tamaa za viongozi hao na akasisitiza kuwa watu hawa wasipewe uongozi kwa hawana nia thabiti ya kuweza ustawi wa jamii ya Mtanganyika. Bila shaka yoyote, msimamo huu wa Baba wa Taifa ndio ulikuwa msimamo wa serikali yake yote, ndio ulikuwa msimamo wa viongozi wengine wote, Mwalimu Nyerere amekuwa “father figure” kwa viongozi wengi wa Tanganyika kwa kuwa na maneno machache na matendo mengi, nakumbuka tulipata kuwa na wimbo wa kusifia matendo ya Baba wa Taifa kuwa “Raisi wetu hapendi kusema, raisi wetu Nyerere baba, anaonesha mfano kwa vitendo”.

Mwalimu Nyerere alikuwa na shamba lake kule Butiama, shamba la Mwalimu lilikuwa mfano kwa wanakijiji wenzake, ukubwa wa shamba hili la Mwalimu haukuwa nusu ya ardhi ya kijiji, bali alichukua sehemu kidogo ili kila mwanakijiji mwenye nia ya kufanya kilimo naye apate ardhi. Hapa utaona fahari ya Mwalimu Nyerere haikuwa kujilimbikizia mali, ndio maana uwepo wa Tanzania ulimhitaji sana Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere. Swali linabakia, je baadhi ya viongozi tulionao ambao kujilimbikizia ardhi na mali kwa njia za ufisadi na kuuza mali asili zetu, Tanzania inawahitaji?

Kwa vile utamaduni wa kuambiana kuwa “sisi ni great people”, imekuwa kawaida kuona Watanganyika wa leo tunaishi kama pimajoto -thermometer- ambayo inabadilisha kizio cha joto kadiri unavyoiweka kwenye nyuzi joto tofauti. Ni kawaida kwa pimajoto kusoma nyuzi joto za juu ukiiweka kwenye mazingira yenye joto la juu, pia ni kawaida sana ikiwa pimajoto itatolewa kwenye mazingira ya nyuzi joto la juu na kuwekwa kwenye barafu itasoma nyuzi joto sifuri ama chini ya sifuri. Mfano huu unamaanisha kuwa Pimajoto inaathiriwa na mazingira, hali inayotokea sana kwa Watanganyika wa leo bila kujali elimu zetu, vipato vyetu ama namna yoyote ya uelewa uliokolea, tumekuwa tunaathiriwa sana na mabadiliko ya agenda ama mazingira, kwa mfano bei za bidhaa zinapopandishwa kiholela tunalalamika lakini hatuchukui hatua kukemea na kukomesha hali hiyo, zaidi tumekuwa ni walalamikaji tuliojaa woga wa kuuliza kwa nini hali ipo hivi, nashangaa sana tumekuwa sio “great generation” tuliozaliwa na “great people” chini ya uongozi wa Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere ambaye agenda yake ilikuwa kukemea uoza huu.

Mwalimu Nyerere na Waasisi wa Taifa letu hawakuishi kama Pimajoto, fikra zao hazikubadilishwa na mazingira kama ilivyo Pimajoto bali wao ndio walipambana kubadilisha mazingira magumu waliyokuwa nayo wakati huo hawakukubali chochote kilichodhalilisha utu wao, kilichobeza ubinadamu wao ama kilichodidimiza ustawi wa Tanganyika ama Watanganyika. Kwa kutunza heshima na utu wa Mtanganyika walisisitiza sana elimu ya ujamaa na kujitegemea. Ukitazama wengi wa viongozi tulionao Tanganyika ya leo wengi wanaishi maisha ya Pimajoto, wanabadilika badilika ili kufanikisha nia zao binafsi zinazokinzana na mahitaji ya mustakabali wa Taifa letu Tanganyika, baada ya miaka 50 ya uhuru wa Tanganyija, Watanganyika tunaoishi maisha ya Pimajoto, Tanzania inatuhitaji?

Miaka 50 ya uhuru wa Tanganyika imeshuhudia awamu nne za maraisi wa Tanganyika, huku awamu ya kwanza ikiongozwa na Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere, awamu ya pili Mzee Ali Hassan Mwinyi, awamu ya tatu iliongozwa na Mzee Benjamini Mkapa na awamu hii ya nne usukani umeshika na Raisi Jakaya Kikwete. Katika awamu zote nne, serikali imepambana na changamoto mbali mbali za maendeleo, pia imetumia fursa nyingi za maendeleo ili kuwezesha maendeleo ya kiuchumi, kisisasa na ustawi wa jamii. Yatokanayo na jitihada hizi na changamoto zake sio muktadha wa makala hii.

Kwa makala hii, miongoni mwa maswali ya kujiuliza ni:- je serikali ikiwa ni mzazi wa kila Mtanganyika, inawapokea Watanganyika na matatizo yao na kuwaongoza kutatua shida zao? Kwa maana jitihada zilizofanywa na awamu zote, miaka 50 baada ya uhuru wa Tanganyika zimefanikiwa kiasi gani kutatua matatizo yanayokabili ustawi wa jamii ya Mtanganyika? Je, miaka 50 inatosha tu inaalika sherehe na karamu ya kujivunia uhuru ama ni fursa kwetu kutafakari wapi tulipojikwaa kama Taifa badala ya kulalamikia wapi tulipoangukia? Maana miaka 50 ya uhuru wa Tanganyika haijatosha kutatua shida za msingi kama uhaba wa madawati mashuleni, uhaba wa madawa, vitendanishi tiba na watumishi hospitalini, kukosekana kwa nishati ya umeme ya uhakika na mambo mengine mengi.

Kwa bahati mbaya sana miaka 50 baada ya uhuru wa Tanganyika , taifa letu linashuhudia matumishi ya ujuzi na utaalamu wa baadhi ya viongozi wenye tamaa, ulafi na ubinafsi vikitumika kuzidisha umaskini miongoni mwa jamii kubwa ya Watanzania, je, Tanzania itakapofikisha miaka 50, hapo tarehe 26 April 2014 itakuwa bado inahitaji viongozi wa namna hii?

Nihitimishe kwa kusema kuwa, kila tunapotazama tulipotoka, hasa baada ya miaka 50 ya uhuru wa Tanganyika, vema tukijua kuwa sisi Watanganyika ni “great people” mambo yaliyofanywa na waasisi wa Taifa letu ni mfano hai wa hiki ninachosema. Changamoto tuliyonayo leo hii ni kuishi maisha ya Pimajoto, ambayo ni kinyume na silika ya “great people” maana “great people” wote huwa wanabadilisha mazingara yao na kuyafanya kuwa bora zaidi kwa ustawi wa taifa lao na vizazi vijavyo. Serikali haina budi kusimamia sheria zake ili wajanja wachache wasitumie maarifa waliyoyapata kuihujumu serikali, badala yake wataalamu hawa watumike kusaidia kusukuma mbele gurudumu la maendeleo ya Taifa, tukifuata njia hii ndiposa tutajibu hoja ya Miaka 50 baada ya uhuru wa Tanganyika, je Tanzania inanitaji?
Imeandikwa na,
Barnabas Mbogo.
Nyamagana, Mwanza
.

Saturday, August 20, 2011

WILAYA MPYA YA NYASA YAKABILIWA NA CHANGAMOTO ZA AFYA KWA WANAWAKE

Hili ni gari la wagonjwa lililotolewa na kamanda wa vijana wa CCM na mbunge wa Ludewa Deo Filikunjombe kituo cha Manda Ludewa.

Baada ya kupumzika jumamosi hii ya leo nikaona si vizuri nikipitia badhi ya vibaraza na kusafisha macho kidogo. Na kweli nimekutana na habari ambayo imenigusa sana hasa ukizingatia nimekwisha wahi kuishi katika mazingira haya. Lundo ndicho kijiji nilichozaliwa binadamu mimi kwa hiyo nimeona nami niweke hapa ili habari iweze kuenea na wengi walijue hili jinsi wanawake tunavyopata taabu. Habari hii nimeipata hapa.

-----------------------------------------------------------------------------------------------
SEKTA ya afya katika nchi yoyote duniani ina umuhimu mkubwa sana katika kuleta ustawi wa jamii na kwamba ili jamii iweze kujitegemea kielimu,kisiasa,kiuchumi ni lazima iwe na afya bora itakayowezesha nchi kupiga hatua kusudiwa
Uchunguzi uliofanywa na mwandishi wa mtandao wa TGNP na mtandao huu Stephano Mango kutoka Nyasa umebaini kwenye wilaya mpya ya Nyasa Mkoani Ruvuma katika shughuli za kiuandishi kufuatilia hali ya huduma ya afya ya uzazi kwa wakazi wa wilaya hiyo iliyopo mwambao mwa Ziwa Nyasa
Nilibahatika kufika huko kwa ufadhiri wa Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP)na kuweza kufanikiwa kutembelea kata sita za Lituhi,Mbaha,Kihagara,Mbambabay,Chiwanda na Kilosa katika wilaya hiyo
Katika shughuli zangu za uandishi nilibaini mambo kadhaa yanayowakumba akina mama wajawazito kabla na baada ya kujifungua wakati wa kwenda katika vituo vya afya na Zahanati kupata huduma ya afya ya uzazi na mtoto
Miongoni mwa mambo hayo ni umbali mrefu kutoka kwenye makazi hadi kufika katika vituo vya afya ili kuweza kupata huduma ya kliniki kwani akina mama wengi wajawazito wamekuwa wakitembea umbali mrefu pekee yao bila hata kusindikizwa na wenza wao
Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili kutoka katika vijiji vya
Chimate,Mtupale,Chinula,Ndengele na N’gombo umebaini kuwa akina mama wengi wajawazito wamekuwa wakikumbana na kero kubwa ya usafiri wa kutoka kwenye vijiji wanavyoishi hadi kwenye vituo vya afya kufuata huduma za kliniki ya mama na mtoto
Imebainika kuwa akina mama hao wajawazito wamekuwa wakichelewa kufika katika vituo vya afya na wakati mwingine kukosa kabisa huduma muhimu ya afya ya mama na mtoto kutokana na adha kubwa ya usafiri jambo linalopelekea kudhoofika kwa afya zao kabla na baada ya kujifungua
Baadhi yao kutoka katika Vijiji vya Mtupale,Mtipwili,Chiulu,Kwambe,Mbaha na Kingirikiti wakizungumza na gazeti hili walisema kuwa kutokana na umbali mrefu uliopo toka wanakoishi hadi kwenye vituo vya afya wamekuwa wakishindwa kuhudhulia kliniki kabla na baada ya kujifungua kwani wakina mama hao wamekuwa wakilazimika kujifungulia majumbani kwa sababu ya kukosa nauli na wakati mwingine usafiri wa kuwafikisha katika vituo hivyo
Walisema kuwa hali hiyo licha ya kuwa ni hatari kwa afya zao lakini wamekuwa wakilazimika kufanya hivyo kutokana na mazingira magumu waliyonayo katika maeneo wanayoishi na kwamba Zahanati nyingi zilizopo kwenye maeneo jilani wanayoishi zimekuwa zikikosa dawa,wataalamu pamoja na vifaa tiba
Uchunguzi huo umebaini kuwa Wilaya mpya ya Nyasa ina vituo vya Afya Vitatu ambavyo ni Lituhi kinachomilikiwa na Kanisa Katoliki Jimbo la Mbinga,Liparamba na Mbambabay pamoja na Hospitali ya Liuli ambayo inamilikiwa na kanisa la Anglikana Dayosisi ya Ruvuma pamoja na Zahanati nyingi ambazo huduma yake ni duni
Imebainika kuwa wakina mama wajawazito kutoka kijiji cha Mango hadi kituo cha afya cha Mbambabay wamekuwa wakitembea kwa miguu umbali wa kilometa 43 na wakati mwingine wamekuwa wakitumia usafiri wa Yeboyebo(pikipiki) kwa nauli ya shilingi elfu 9,500 ambako kwa gari ni shilingi elfu 3000
Aidha imebainika kuwa gharama za matibabu ni kikwazo kwa akinamama hao kwani wamekuwa wakichangia huduma za kliniki na matibabu kati ya shilingi 2000 na shilingi 6000 kila wanapohitaji kupata huduma kinyume na sera ya taifa ya matibabu bure kwa wajawazito na watoto chini ya miaka mitano
Wakizungumza kwa nyakati tofauti na gazeti hili katika kata ya Lundo akina mama hao walisema kuwa Serikali imekuwa ikisema akina mama wajawazito na watoto chini ya miaka mitano wanatakiwa kupata huduma ya afya bila kuchangia malipo lakini wao wamekuwa wakichangia fedha nyingi
Kutokana na kuchangia gharama hizo ambazo kwao zimekuwa kero kubwa wamekuwa wakilazimika kwenda kliniki wanapokaribia kujifungua tu ili kuweza kukwepa gharama zinazotozwa mara wanapofika katika Zahanati na vituo hivyo kutokana na ugumu wa maisha
Walisema kuwa katika kata hiyo kuna Zahanati ya Lundo ambayo mara nyingi imekuwa ikikosa dawa muhimu za wajawazito na wahudumu wake wamekuwa na lugha chafu kwa wagonjwa hali inayopelekea akina mama wengi kutohudhulia Kliniki kwa kuhofiwa kutukanwa na kupoteza muda wa kufanya kazi zao za kujitafutia ridhiki
Mary Haule mkazi wa kata hiyo ambaye anaujauzito wa miezi saba alisema kuwa kutokana na hali hiyo amekuwa akienda kupata matibabu katika Kituo cha Afya cha Mbambabay kwa kuhofia usalama wake wakati wa kujifungua
Haule alisema kuwa wajawazito wengi wamekuwa wakinyanyaswa sana pindi wanapofika katika Zahanati kwa ajili ya kupata huduma za matibabu jambo ambalo linaonyesha uzalilishaji wa hali ya juu kwa wanawake
Uchunguzi uliofanya na Gazeti hili umebaini kuwa Zahanati nyingi za Mwambao mwa Ziwa Nyasa zimekuwa zikikosa dawa muhimu kwa ajili ya wajawazito na watoto chini ya miaka mitano kutokana na mgawanyo usio wa uwiano unaotolewa na Bohari ya Madawa Nchini(MSD)
Aidha kutokana na ukosefu huo wa dawa uchunguzi umebaini kuwa wahudumu wa Zahanati hizo wamekuwa wakiwauzia dawa na vifaa tiba wajawazito kwa bei kubwa hali inayopelekea unyanyasaji mkubwa kwa akina mama hao ambao wanatoka umbali mrefu kwa ajili ya kupata matibabu stahiki
Gazeti hili lilishuhudia baadhi ya wajawazito 3 katika Kituo cha Afya cha Mbambabay wakitokea Kata ya Tumbi umbali wa kilometa 43 ambapo wamekuwa wakitembea kwa miguu na wakati mwingine kwa pikipiki kwa kutozwa nauli kubwa kwenda kuhudhulia Kliniki
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga ambaye pia ni Diwani wa Kata ya Chiwanda Oldo Mwisho aliliambia gazeti hili kuwa kufuatia adha wanazopata wakina mama wajawazito alisema kuwa Halmashauri yake inazitambua adha hizo na kwamba sera ya afya ya Serikali imetamka wazi kuwa kila kata ni lazima ijenge kituo cha afya ili kukabiliana na adha hizo na kila kijiji ijenge Zahanati
Mwisho alisema kuwa kutokana na hali wananchi wamekuwa wakihimizwa ujenzi wa vituo vya afya kwenye kata zao ambapo changamoto kubwa inayoikabili Serikali ni ubovu wa miundombinu, upungufu wa wataalamu wa afya,dawa na vifaa tiba
Akizungumza na gazeti hili Mbunge wa Jimbo la Mbinga Magharibi Kapteini John Komba alisema kuwa Wilaya ya Mbinga ina eneo kubwa la kiutawala hivyo ilikuwa imezidiwa uwezo wake wa kutoa huduma kwa jamii kwani ilikuwa ina hudumia wakazi wa majimbo mawili ya uchaguzi la Mbinga Magharibi na Mbinga Mashariki
Komba alisema kuwa Serikali kuu kwa kutambua ukubwa wa eneo hilo imeamua kuyagawa majimbo hayo katika Wilaya na kupata Wilaya ya Mbinga na Wilaya mpya ya Nyasa ambayo inaanza rasmi katika kipindi hiki cha bajeti ya mwaka wa 2011/2012 hivyo mara itakapoanza itapunguza adha hizo za wajawazito kwa kiasi kikubwa
Alisema kuwa mara nyingi amekuwa akipigania ustawi wa afya za akina mama wajawazito anapopata wasaa wa kuchangia bungeni akiwa mwanasiasa aliyepewa dhamana na wananchi katika kushirikiana nao kujiletea maendeleo kusudiwa katika jimbo hilo.

Monday, February 7, 2011

WIZARA YA MALIASILI NA UTALII YAPATA MKURUGENZI MPYA WA IDARA YA UTALII


Na Tulizo Kilaga wa Wizara ya Maliasili na Utalii
Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii amemteua Bw. Ibarahim Mussa kuwa
kuwa Mkurugenzi wa Idara ya Utalii kuanzia tarehe 01 February 2011.

Uteuzi huo ameufanya kwa mujibu wa kifungu cha 6 (1) (b) cha Sheria ya
Utumishi wa Umma Na. 8 ya mwaka 2002.

Ibrahim A. Mussa (53) ni mtumishi wa Wizara ya Maliasili na Utalii tangu
mwaka 1982 hadi sasa ambapo alifanya kazi katika ngazi mbalimbali, katika
Idara ya Misitu na Idara ya Utalii.

Kabla ya kuteuliwa kuwa Mkurugenzi wa Utalii, Ibrahim A. Mussa alikuwa
Mkurugenzi Msaidizi anaesimamia Utafiti, Takwimu na Mafunzo katika Idara
ya Utalii.

Bw. Mussa ana Shahada ya Uzamili (International Tourism Management)
aliyoipata mwaka 2005 kutoka chuo cha Sheffield nchini Uingereza

Bw. Mussa anachukua nafasi ya Mkurugenzi wa Idara ya Utalii kutoka kwa Bi.
Maria Mmari ambaye amepangiwa kazi nyingine.