Friday, February 26, 2010

HII NDOA AU NDOANA: KAMA UNATAKA KUJUA CHANZO, BASI SOMA HAPA.

Wadau,

Nimepata maelezo ya ziada toka kwa kaka Mlachaombwani baada ya kuona kuwa wengi wenu mmekuwa na maswali mengi sana kutaka kujua ni nini chanzo cha mtafaruku huo. Majibu yake ni haya kwa ufupi:

Mwaka 2001 wakati wakiwa na mtoto wao wa kwanza (akiwa na umri wa chini ya miezi 3) mume alimuomba mke akakae kijijini kwa mume ili wazee wamwone mtoto na pia kumpa jina. Mke alikwenda huko ukweni na alikaa kwa muda wa miezi mitatu.

Kwa mujibu wa maelezo ya mke mara baada ya kurudi kutoka ukweni, alidai kuwa alipokuwa huko kwa huo muda wa miezi 3 aliteswa sana na mama mkwe wake kwa sababu si wa kabila la mume kwa kuwa mume hakuoa mke toka kwa kabila lao.

Awali wazazi wa mume walimtafutia mume mke wa kabila lao lakini huyo mchumba alimtosa kaka wa watu kwa kigezo kuwa ‘hawezi kuolewa na mtu ambaye kwao hakuna hata kuku’ na ‘mtu ambaye jogoo hawiki’ (stori ya ‘jogoo hawiki’ ilikuwa kwamba kaka Mlachaombwani, kutokana na malezi aliyopata hakuamini katika kuonjana kabla ya ndoa hivyo kila mchumba alipotoka naye alitegemea kumegwa na kwa kuwa alikuwa hamegwi basi akadhani jogoo hawiki kumbe jamaa anaitunza kwa ajili ya ule wakati mzuri wa –Bwana na Bibi arusi sasa wanakwenda kujipumzisha)

Hivyo alipompata huyu mke aliye naye, hakufanya ajizi akaingia kichwa kichwa na kumtundika mimba iliyopelekea binti kuondoka kwao na kwenda kuishi na kaka Mlachaombwani ili kuepusha vurumai na rabsha zaidi kutoka kwa wazazi.
Na inavyoonekana wazazi wa kijana hawakupendezwa na hilo.

Kwa hiyo kutokana na makosa hayo ya mama mkwe ya kumtesa (mke anadai kuwa wakati mwingine alikuwa analazwa njaa ilhali ananyonyesha na pia kufuata maji na kuni umbali mrefu-zaidi ya km 5- wakati mgongo ulikuwa haujakomaa).

Hapo mnamo mwaka 2003 kama alivyosema ndipo jinamizi la kunyimwa unyumba lilipoanza kwa kile kilichoelezwa kuwa ‘mke hajisikii’ na kumuuliza mume kuwa ‘kwani huwezi kuishi bila kuonja’. Kaazi kwelikweli!

Katika kutafuta faraja, nadipo akajikuta akiwa na watoto nje ya ndoa kitu ambacho haikuwa ni dhamira yake. Saswa hivi chuki imekuja kuwa kubwa baada ya wazazi kumpokea mmoja wa watoto wa kaka Mlachaombwani na pia kuuliza kwa nini hakai na watoto wake (waliozaliwa nje ya ndoa) nyumbani kwake.
Mbali na hayo, haelewani na shemeji zake kwa sababu zisizoeleweka.

Kaka Mlachaombwani anakiri kuwa yeye ndiyo chanzo kwa kuwa, kama asingempeleka mkewe kijijini pengine kusingetokea hayo yote. Lakini anashangaa kuwa pamoja na kutumia wasimamizi wa ndoa na viongozi wa dini MKE hataki kuwasamehe wazazi na ndugu zake kwa kile alichosema mwenyewe kuwa AMEWA-DELETE kwa hiyo, hakuna msamaha kwa yeyote yule.

Kaka Mlachaombwani anabainisha kuwa mkewe huyo hataki apeleke matumizi kwa wazazi wake na hata wakiwatembelea nyumbani kwao, kama mume hayupo basi hawatakarimiwa.

Kwa maelezo ya kaka Mlachaombwani, ndiyo anataka kuachana na huyo mkewe lakini watoto wao ndiyo kikwazo kwa sasa. Na anakiri kuwa anampenda sana mkewe lakini cha kushangaza mkewe anamchukia saaaaaana! Na kutokana na hilo anajikuta wakati mwingine anachuki na kila mwanamke anayekutana naye njiani kwa kuwa anadhani wanawake wote wako hivyo.

Hataki kuoa tena na anasema mipango yake ikifanikiwa ataondoka na kumuachia huyo mkewe kila kitu na kuanza upya kwa kuwa anajua alipoanzia huku akiishi na wanawe wote.

Vipi hapo? Je kuna msaada wa ushauri kwa kila mmoja wa hao wanandoa? Mnadhani kuondoka na kumuachia kila kitu ni suluhisho au ushauri wa Dada Koero kuwa amfukuzie mbali ndio mzuri zaidi?

13 comments:

Mija Shija Sayi said...

Unaona sasa, angalau tumepata picha.

Kabla sijaendelea naomba kuuliza Je wazazi wa Mlachaombwani wamemsamehe na kumpenda mkwe wao? Maana tusilazimishe Mrs Mlachaombwani kuwasamehe wakwe zake wakati wenyewe hawajamsamehe Mrs Mlachaombwani.

Halafu kwa nini wenyewe ndio walazimishe watoto wa nje waje ndani?

Kwa mtizamo wangu ndugu wa mume ni wakorofi, wangewaachia wenyewe watatue matatizo yao.

Unknown said...

Hapo umenena dada Mija.
Mwanzoni nilishindwa kutoa ushauri kutokana na kutojua chanzo ni nini, lakini kwa simulizi hii ya pili, nimepata mwanga angalau.

Nadhani swala hili linatakiwa litatuliwe kati ya pande mbili kwani kuna ukweli umeshajulikana kuwa wakwe ni wakorofi na hivyo wao ndio wanatakiw kumuomba radhi mkwe wao yaani mke wa MLACHAOMBWANI, ili moyo wake uwe safi.
Ni suala ambalo bwana mkubwa anatakiwa kulisimamia mwenyewe ili kunusuru ndoa yake.

Niwaanchie na wengine watoe maoni yao.

Bennet said...

Duh! kumbe huyu mke wa mlachaombwani na yeye alifanyiwa mabaya na Mama mkwe ndio maana na yeye akaamua kuwachukia kabisa
Lakini tatizo kwa nini anamnyanyasa na mumewe wakati hana kosa?

o'Wambura Ng'wanambiti! said...

Nadhani sasa kila mtu atakayekuja atasema kuwa 'UNAONA SASA!'

Da Mija: nakubaliana nawe kwa asilimia 100 kuhusu hao wazazi wakorofi. Sitazungumzia kuhusu wamemsamehe ama la lakini mie ntazungumzia suala zima juu ya upendo!

Samahani kama ntaonekana kuwa mhubiri wa upendo lakini naomba nifanye hivo kwa ufupi kwa kuwa nilinusurika kuwa padre...lol

Da Mija, tufanye kuwa hawajamsamehe huyo mkazamwana wao. Natufanye kwamba hawajalazimisha wana wa nje waje ndani bali wameuliza.

Nijuavyo mimi upendo ni KUTOA na si kupokea. Na kutoa maana yake ni ku-sacrifice hata yale ambayo hayawezekani; si lazima utoe kikubwa bali hata kiduchu tu uonacho kuwa hakiwezekani.

Kwamba unapaswa kumpenda mumeo ama mkeo hilo halina mjadala. Kuna baadhi yetu tumeoa ama kuolewa na machaguo yasokuwa yetu na tumejifunza kuwapenda wenzi wetu hao on the way. Na kwa kweli suala la kumpenda ambaye hakuwa chaguo linataka moyo na sadaka ya uhakika, pengine ya kushinda ya BWANA MKUBWA mtini :-( (imagine mtu hakuzaliwa tumbo moja nawe halafu wenda ama aja kushea shuka moja nawe kwa miaka zaidi ya miaka 60 ya maisha ya hapa duniani, ati kwa jina la kupendana!)

Turejee pale kuwa wazazi hawakutaka mwana wao kuoa ambaye si kabila lao. Kuna mengi yanayotokea linapotokea jambo kama hilo. Almanusura nami linipate kama hilo wakati fulani. Lakini pia halikuwa na maana sana kwangu kwa kuwa nakumbuka hata mama yangu hakuwa chaguo la baba (baba alichumbia dada wa mama ila akawahiwa na tajiri ambaye alitoa ng'ombe 58 wakati baba yangu alikuwa na ng'ombe 45!) na mama alikuwa akichukiwa sana na mawifi zake na nakumbuka kwamba hawakuwa in good terms na bibi (mama mkwe wa mama) (hawa ni wa kabila moja remember).

Kwa hiyo suala la kaka Mlachaombwani si la leo na kwamba yeye si peke yake kwani walishayapitia masahibu kama hayo wengine (nimewapa uzoefu wa kwetu). huyo mwana mama ana tatizo....

Samahani kwa kuhukumu lakini naweza kusema kuwa kwa kutumia kanuni ya upendo ANA TATIZO. Kama anadai kuwa yuampenda mumewe basi hana akili nzuri. Pengine hajui maana ya upendo ama kadanganywa. Sina hakika kama methali za wahenga kuwa 'ukipenda boga...'

Ninachojua ni kuwa ili uweze kuishi vema na kwa raha mstarehe kanuni inayoweza kukusaidia siku zote in Love, love, love and love! (bwana mkubwa alisema kuwa MPENDE JIRANI YAKO na MPENDE ADUI YAKO).

Na nyingine ni SAMEHE NA SAHAU! (FORGIVE and LET GO). Kama usipotumia mbinu hizo utajikuwa unaishi maisha magumu sana hapa duniani. Sina hakika na Kaka Mlachaombwani ana mtizamo gani lakini mie ningeona kama maigizo vile kwa kuwa huyo mamsapu wa Mlachaombwani hajui alitendalo.

Kwamba wazazi wa mume wanamchukia haina mashiko sana, maadam mumewe anampenda ANAPASWA KUWAPENDA WOTE BILA UBAGUZI. Pengine hatujajua kama ndugu wa mke wakija wanashughulikiwa namna gani na kama ana ubaguzi pia ni tatizo.

Nachelea kusema kuwa kama wazazi hawawezi kumwomba msamaha mkwe na mama anasema kuwa amewa-delete kwenye operation system yake hakuna atakayeshinda katika vita hivo na kwamba muumiaji ni MKE kwa kuwa wazazi hao wanapita na kwamba hao wanandoa wanapaswa kujiongeza wenyewe kama kaka Kaluse alivosema.


Kuhusu watoto nadhani ni ujinga kumzuia mume kuwatunza watoto kwa kuwa kama mume hana mahusiano tena na aliyezaa naye anafanya kosa kubwa. Kama ni suala la kuwaleta watoto hao nyumbani linazungumzika na kama ni kufuata mfumo wa dini (atleast kwa Wakatoliki) najua kuwa mume hawezi akaleta watoto alozaa nje bila ya mke kukubali lakini MATUNZO ni haki ya watoto.


Niwaachie wengine waendelee na mahubiri...lol

Mija Shija Sayi said...

Hakuna haja ya kuachana hapa, Kuna msemo usemao EVERY DISAPPOINTMENT IS A BLESSING. Huwezi kujua kikwazo hiki kinakuja na baraka gani utakapo kishinda.

Kaka Kaluse kasema, maadam umeshajua tatizo lilianzia wapi basi ni jambo la wewe kulisimamia ili kuinusuru ndoa yako. Tengeneza urafiki naye upya, jishushe, msikilize, nendeni holiday peke yenu, nakuhakikishia siku moja ataona haina maana kugombana na mtu asiyerudisha ugomvi.


Ng'wanambiti kaongea jambo la msingi sana juu ya UPENDO, namnukuu....."Nijuavyo mimi upendo ni KUTOA na si kupokea. Na kutoa maana yake ni ku-sacrifice hata yale ambayo hayawezekani...."

Sasa Mlachaombwani inabidi usimamie katika kauli hiyo ya Ng'wanambiti wakati huo huo ukijaribu kuangalia na upande wa pili kama kuna vizabizabina wanaompa kichwa Mrs wako, maana huwezi kujua labda mashoga au ndugu zake wanampa nguvu ya kukufanyia anayokufanyia.

watila said...

UNAONA SASA
MIMI NATILIA NGUVU SANA MAWAZO AU FIKRA ZA NDUGU CHACHA PALE ALIPOSEMA KUWA

Nijuavyo mimi upendo ni KUTOA na si kupokea. Na kutoa maana yake ni ku-sacrifice hata yale ambayo hayawezekani; si lazima utoe kikubwa bali hata kiduchu tu uonacho kuwa hakiwezekani.

pia ninavoona mimi kuwa penye kila tatizo pana suluhusho
kwahi bado kuna uwezekano wa tatizo kutatuka waswahili wanasema

na inawezekana tatizo likaisha na na wakaa kaa pamoja kama zamani

na haitokuwa ni miracle ni miujiza yapo matatizo mazito kushinda hayo yametatuliwa na mke na mume wanasahau kabisa ule ugonvi wanafunguwa chapter nyengine
haina haja kuwa delete kwenye system wakweze pia

Koero Mkundi said...

.
Naamini wengi walinielewa vibaya kuwa siitakii mema ndoa ya kaka Mlachaombwani, lakini halikuwani lengo langu kutaka ndoa ile ivunjike, bali kutaka kila mtu awajibike ili kuinusuru ndoa yao.

Inawezekana namna nilivyowasilisha maoni yangu, kulikuwa na hisia za chuki zilizo wazi dhidi ya mwanamke anayetuhumiwa kutotoa unyumba, lakini lengo langu halikuwa ni kumkandamiza mwanamke huyo.

Nililotaka kusema hapo ni kuonyesha kuwa, aina ya maisha wanayoishi wandoa hao ni hatari kwa ustawi wa familia yao hususan watoto wao ambao kwa kiasi kikubwa wanahitaji upendo wa wazazi wao.

Haiwezekani watu wagombane mpaka kufikia kunyimana unyumba na kutukanana mbele ya watoto bila hata ya aibu halafu tuseme kuna ndoa hapo? Basi huo utakuwa ni uenda wazimu.

Waliomkosea ni wakwe, na sio mumewe, na kama ni kuolewa hakuolewa na wakwe aliolewana mume, kumhukumu mume kwa makosa ya wazazi wake ni kumuonea.

Hivi watoto watakuwa wamejifunza nini kutoka kwa wazazi wao? Naamini watakuwa wamejifunza kuwa maana ya ndoa ni kugombana na kutukanana mbele ya watoto, na hata wao watatumia walichokiona kutoka kwa wazazi wao watakapokuwa wakubwa na ndoa zao kamwe hazitakuwa na amani, iweje ziwe na amani ilhali wazazi wao hawakuwahi kuwa na ndoa yenye amani kamwe?

Jambo lingine ni kumnyima mume unyumba bila sababu ya msingi, unajua kuna baadhi ya sisi wanawake tunadhani kuwa bakora ya kumchapa mwanaume ni kumnyima unyumba, hilo ni kosa kubwa sana. Sasa unamnyima unyumba ili iweje?

Siku hizi, jamani mambo yamebadilika. Huko nje kuna mabinti ambao ni wawindaji haswa. Wako tayari muda wote, wewe ukisema wa nini wenzio wanasema nitampata lini…..na wanaume wa siku hizi hawajui kubembeleza kama wa zamani, wewe ukisema “Sikupi basi” unafikiri atakwambia nini, atakucheka tu!
“Wewe unaniambia mimi hivyo?, Subiri kama nitakuomba tena!” Atakuona umpumbavu tu, wewe unamwambia “sikupi basi” na huko nje anawaona wenzako wanavyojigonga gonga kwake, unafikiri atahangaika na wewe wa nini? Dhubutuuu…..kama sio ukimwi atakuletea watoto wan je ya ndoa, utamfanya nini?

Mtu anaweza kusema kuwa hata wanaume pia nao wako wengi na hata mwanamke naye anaweza kutoka nje ya ndoa akapata ridhiko.Ni sawa, lakini je, kutokana na mfumo dume uliotamalaki katika jamii yetu, unafikiri ni nani atakayeonekana kajidhalilisha?
Wenzetu wao wanaamini kuwa mwanaume kufumaniwa ni kudhihirisha kuwa yeye ni rijali na kidume, lakini kwa mwanamke je? Mtajaza wenyewe….

Mwisho wa siku mtaleteana Maukimwi na kupoteza maisha bure kwa jambo ambalo wote mngeweza kuliepuka kama mngetumia busara kidogo tu.

Katika biblia tumesoma kuwa mwanamke mpumbavu huvunja ndoa yake kwa mikono yake mwenyewe. Nimetafuta katika biblia hiyo hiyo mahali pameandikwa neno hilo hilo likimlenga mwanaume lakini sijapata. Hii ina maan gani? Ina maana kwamba mwanamke analo jukumu kubwa la kuilinda ndoa yake ukilinganisha na mwanaume.

Mara nyingi wanawake, husifika kwa kuwa na busara na uvumilivu, hawa wanaume ni sawa na watoto wetu wakubwa, namna tunavyowalea watoto wetu na kuwatunza, hata wanaume huhitaji huduma hiyo hiyo, tena wakati mwingine huhitaji upendeleo zaidi ya watoto.

Nimejifunza mengi kutoka kwa wazazi wangu na hapa nilipo najua majukumu yangu kama mwanamke.

Naona nimekuwa mhubiri hapa, ngoja niwahi zangu kanisani kwani leo ni SABATO…..LOL

Ramson said...

Sasa mimi niseme nini, maana naona kaka Chacha o'Wambura na Koero Mkundi wamemaliza kila kitu.

Yaani karibu watoa maoni wote wameonekana kuitakia mema ndoa ya kaka Mlachaombwani.

Sasa ni jukumu lake yeye na mwenza wake kukaa chini na kuyafanyia kazi yote mazuri yaliyosemwa na wachangiaji.....

Mrs Haule said...

Mume hapa ndio mwenye kosa, inaelekea mara ya kwanza alijisahau hadi akawafanya ndugu zake kuingilia ndoa yake.

Itakuwaje ndugu zako wawe na uamuzi kuhusu hao watoto wako wa nje? Hapo inaonyesha kabisa wewe unasikiliza ndugu zako kuliko mkeo, ndio maana mkeo sasa kakuchukia wewe pamoja na ndugu zako maana wote lenu moja.

Vile vile ilikuwaje umuache mkeo akakae kwenu miezi 3 yote hiyo anafanya nini? Ukweni ni kwenda tu kukaa siku mbili tatu na kugeuza,ukikaa sana ndio mambo kama haya huwa yanajitokeza. Hivyo hapa wewe mwenyewe mume ndio ulitafuta matatizo.

Ndugu zako ni wakorofi na wewe unawasikiliza, ukisikia ndugu wa mume wanabomoa ndoa ndio kama hivi ndoa yako sasa ipo matatani kwa kusikiliza ndugu.
Unataka kumuacha mkeo hebu fikiria tabu watakazopata watoto wako bila malezi ya baba na mama,nadhani hao watoto bado wadogo tu wanahitaji malezi yenu nyote wawili.

Mie sikushauri umuache mkeo, ila jitahidi kurudisha upendo, maana hapa chanzo haswa ni ndugu zako. Hivyo jitahidi kutosikiliza ndugu zako na fanya jitihada za kumrudisha mkeo katika njia iliyonyooka.

Hebu muonyeshe mkeo upendo wa dhati na kuwa karibu na mkeo atarudi tu katika hali yake ya kawaida kama ilivyokuwa zamani.

Jacob Malihoja said...

Mhhhhhhhh! Hatari! Hatari! Mama anahasira huyo! Wakwe nao ni ishu! huyo jamaa nae ni wa kumtafakari!!!! sijabahatika kupitia maoni ya wadau wote,sijui nitarudia?, yote heri hata kama nitarudia maoni ya mtu!

Jamani! Lakini ni kweli chanzo ni hao wazazi peke yao? ni ukweli usiopingika wanaume tunaongoza kuwasaliti wanawake, ila tunakwepa hatia tulizonazo na kuzirushia kwa wanawake wenyewe au watu wengine mambo yanapoharibika. Hii hutokea kwa waliooa na kwa wale ambao wako kwenye mahusiano tu.

Ukweli kabisa kama jamaa anampenda mke wake ni vema kwanza akili udhaifu uiofanywa na wazazi na ndugu zake kwa mkewe, na akili udhaifu alioufanya yeye. Pili awaelimishe wazazi wake kwa utulivu na upendo, na kisha awakalishe wazazi wake na mkewe wayamalize na kusameheana. Kabla ya kuwakutanisha anatakiwa akishaongea na wazazi wake wakayaweka sawa, arudi kwa mkewe na kumlainisha kulingana na alivyoongea na wazazi wake ili watakapokuwa na kikao cha pamoja mkewe awe amekwenda pale tayari amelegeza hasira alizonazo kwa wakwe.

Kuhusu kunyimwa, Hapa huyu jamaa atueleze ukweli, maana sipati picha unoko wa mama kijijini, huku mjini daftari lifungwe! Kwani mama ndiye anayeandika? hapa kuna kitu cha ziada! Lakini huyu jamaa amenishangaza sana, yani pamoja na kelele zote hizi na Ukimwi amethubutu kutoka nje ya ndoa kavu kavu! hii ni hatari!

Diplomasia ni muhimu, kumwacha huyo mwanamke sio suluhu, maana anaweza kupata mwingine ikatokea shida nyingine, itakuwaje? Kujishusha ni moja ya hatua muhimu sana na maridhiano ya kidiplomasia!

kamala Lutatinisibwa Lutabasibwa said...

""""Saswa hivi chuki imekuja kuwa kubwa baada ya wazazi kumpokea mmoja wa watoto wa kaka Mlachaombwani na pia kuuliza kwa nini hakai na watoto wake (waliozaliwa nje ya ndoa) nyumbani kwake.
Mbali na hayo, haelewani na shemeji zake kwa sababu zisizoeleweka."""""""

mwisho wa kunukuuu.

siku zoote nasema ni upuuzi mkuubwa saana kuacha wazazi waingilie ndoa zenu. ni vigumu kwa wamama wetu wakibongo kuwapenda wakamwanawao, siuko zoote wana wivu.

kwa hiyo nisawa kisaikolojia kwa huyo mke wa mlama.... kumchukia mumeo kutokana na vituko vya mamamkwe kwa sababu huyu mke anamchukia mama mkwe wakati huyu mume anampenda mamaye! a mess

harafu utampelekaje mkeo akakae na wazazi eti watafutie jina?? kwani majina yanapatikana wapi??

baba yangu alifanya huu ujinga wa kumwendekeza mamayake (bibi yangu) na mawifi, kilichotokea walimfukuza mke wake wa kwanza (mamangu wakambo) na mke wa pili (mamangu) baba akaishi singo, sisi tukalelewa na bibi na mashangazi waliotutenda vya kutosha! mama aliharibika kisaikolojia kiasi kwamba hampendi mwanae hata mmoja na baba alikufa frustrated pamoja na kwamba alikuwa na mali nyingi

mpaka sasa wanatuzingira na kungangania urithi aliotuachia baba na mambo ya kishirikina,

sasa nilipokutana na wife nikamuonya asijejishughulisha kwa chochote na familia yangu, alinibishia na kuniona roho mbaya, alikini baadaye aliklubali mwenyewe.

naishi maisha yangu, simpeleki wife kwa mtu wala hakuna wa kunitafutia jina la mtoto

hili ni tatizo kubwa la huyu jamaa japo mbishi.

mke wake amehathiriwa kisaikolojia kiasi kwamba hata kama mume wake kafanana na wazazi anaitumia hiyo kuzidi kumchukia inahitaji kazi kubwa, ila kuachana na mke au kumkimbi italeta matatizo makubwa sana, inabidi awe makini sana

Anonymous said...

yaani haya matatizo ya ndugu wa mume yamekuwa kama nyoka wa sumu ktk ndoa. kaka tumia akili mama yako hawezi kuwa nafasi ya mke wako. yeye atabaki kuwa mama na mke ni mke.Sasa basi nawashauri pia mkapime afya zenu maana huko ulirukaruka usije leta na ukimwi kwa mkeo bure watoto wakakosa wa kuwalea

Anonymous said...

Nakushauri kaka usimuache mkeo sababu anakupenda sana, tatizo kaathirika kisaokolojia tangu mwanzo pale ulipompeleka kijijini kwa mama akajifungue na kwa sababu ya ugeni na jinsi walivyomtenda na akakuambia ukashindwa kumtoa haraka kuonyesha unamjali yeye na mtoto.Amejenga hisia ya ukatili wa familia yako na wewe ukihusika na hiyo sumu imemla mpaka malipizi yake ndio hizo action , mwengine angetafuta mapozeo ya nje au kuondoka kabisa ila huyo wako ndio action yake. Cha muhimu jaribu kumshirikisha mungu katika ndoa yenu nikimaanisha mpende mkeo kama vile ndio unaanza uchumba leo nae atakutii tu. Na jaribu kumtoa out sehemu tulivu mbali na nyumbani ikiwezekana mkalale nje ya nyumbani kwenu w'end nzima kisha umuweke kwenye mazingira ya kukusikiliza umuambie maisha unayotamani kuishi nae.Hapo utatibu mawazo ya ndoa ni wewe na yeye ukifanikiwa hivyo endelea kujitahidi kuonyesha kwa matendo bila kusahau uwepo wa mungu, Jaribu kumshirikisha mkeo kila jambo lako linalohusu familia na kwa sababu anachuki na familia yako plz usipende kwa sasa kuwazungumzia sana ktk mazungumzo yako na mkeo au kumjulisha ishu ambazo unazitekeleza huko nyumbani kwa mama sababu ugomvi wa mama na mkeo bado unaendelea sio tu mkeo hawapendi tu ndugu zako kuna sababu ambazo wewe unatakiwa uzitafute na kuzitatua na ndugu ndio wanazidisha ugonjwa kwa wewe kuzaa nje ya ndoa na familia yako kuingilia kati kuidhinisha kuwa umefanya sawa hilo ni tatizo tena na inawezekana mama kuwachukua watoto wa nje ni kwa nia ya wewe kupeleka mahitaji na kuzidi kumsakama mkeo kuwa hana mapenzi na watoto wako au anakuzuia usiwalee. Plz onyesha kipaumbele kwa mkeo, MAMA YEYE AMEISHAKULA RAHA ZAKE NA NDOA YAKE NA WEWE TAFUTA RAHA YA NDOA YAKO. Wewe unanafasi kubwa ya kumponya mkeo mkaushi kwa raha , huo ni ugonjwa kiakili umeathiri fikra na sasa umetoka kimatendo na tabibu ni yule aliyeusababisha ambae ndio wewe.na kumbuka NDOA NI PARADISO YA DUNIANI NA SIO NDOANO.