Wednesday, August 1, 2012

TUNAJENGA TAIFA LA WALEVI?


Ni ile JUMATANO YA KIPENGELE CHA MARUDIO YA MATUKIO MBALIMBALI NA LEO NIMETEMBELEA HAPA NA KUKUTANA NA HII HABARI NIMEIPENDA NA NIMEONA TURUDIE ILI KUJIFUNZA ZAIDI.

Mtu mmoja akiwa amelala porini baada ya kuzidiwa na kilevi

Pombe ni kiburudisho muhimu sana kwa walio wengi. Mamilioni ya wanaume na wanawake ulimwenguni wanatumia au wamewahi kutumia pombe wakati fulani katika maisha yao.

Umaarufu wa pombe bila shaka unatokana na uwezo wake katika kumfanya mtumiaji ajisikie vizuri na kusahau matatizo yanayo mkabili japo kwa muda. Pombe huondoa aibu, huufanya mwili kusisimka na kuleta furaha.

Kwa sababu hiyo pombe ni kimbilio la watu wengi wenye furaha, na wenye matatizo na shida za aina mbalimbali. Kwa mtazamo wa haraka haraka tunaweza kusema pombe ni nzuri na inafaa kutumiwa kama kiburudisho endapo mtumiaji atakuwa na kiasi na kuitumia kwa namna inayofaa.

Kwa upande mwingine pombe ni kitu kibaya sana kwani madhara yake yanazidi faida na hasa kwa kuzingatia kwamba ni watu wachache sana wanaoweza kufuata mashalti ya utumiaji kileo kama inavyotakiwa. Leo hii pombe ni chanzo kikubwa cha ajali za barabarani zinazo sababisha mauaji ya maelfu ya watu wasiokuwa na hatia.

Pombe ni hatari kwa wajawazito
Pombe pia ni chanzo kikubwa cha matatizo ya kijamii ikiwa ni pamoja na kusambaratika kwa familia, na ongezeko la talaka jambo linalosababisha mateso makubwa kwa watoto.

Aidha, pombe inachangia sana katika kuleta umaskini kwa mtu binafsi, familia na hata taifa. Pombe husababisha uzembe kazini, kupunguza uwezo wa kufikiri na kutoa maamuzi na kusababisha madhara katika ubongo hasa kwa watumiaji wenye umri mdogo (watoto).

Pombe pia husababisha matatizo ya kiafya kwa watoto walioko tumboni (ambao hawajazaliwa). Wanawake wajawazito wanaotumia pombe hujiweka katika hatari kubwa ya kuharibu akili (ubongo) za watoto wanaowabeba matumboni mwao.

Ni kwa sababu hiyo nchi zilizoendelea (kama Marekani na baadhi ya nchi za ulaya) zimepiga marufuku uuzaji wa pombe kwa vijana wenye umri chini ya miaka 18, na zinaendesha kampeni za kuwaelimisha akina mama kuepuka matumizi ya pombe katika kipindi chote cha ujauzito.

Pamoja na madhara makubwa yanayoletwa na unywaji wa pombe, ni ajabu kwamba nchini mwetu pombe tumeigeuza kuwa sehemu ya maisha. Watu wengi wenye kipato cha kawaida hujiingiza katika unywaji pombe wa kupindukia kutokana na kasumba iliyojengeka nchini mwetu kwamba watu wanaokunywa pombe kila siku wana pesa nyingi. Watu wanaojiingiza katika ulevi hufanya hivyo kwa kudhani wanainua 'status' zao.

Wengi wa walevi hawa hujikakamua kununua pombe zenye bei kubwa zaidi ili kuonesha kuwa wana pesa na kuwakoga wasiokuwa nazo. Baadhi ya wanywaji hufikia hatua ya kuweka bili katika mabaa na store zinazouza pombe ili waweze kunywa pasipo kukosa hata kama hawana pesa (na kulipa mwisho wa mwezi) jambo linalowaingiza katika umaskini wa kujitakia pasipo kujua.

Ni kutokana na ongezeko kubwa la wanywaji wa pombe makampuni mbalimbali yanayo tengeneza na kusambaza vileo yameivamia Tanzania kwa nguvu na kumwaga pombe za kila aina mitaani. Makampuni haya hujitengenezea faida kubwa isiyoelezeka.

Aidha wafanya biashara wengi nchini wameacha kuwekeza katika vitega uchumi vingine vya kimaendeleo kama kilimo, ufugaji, viwanda vidogo vidogo, elimu n.k na kugeukia biashara ya pombe ambayo inaelekea kutokuwa na mpinzani katika kuingiza faida. Si ajabu kwamba katika miji yetu kuna baa katika kila kona.

Mbaya zaidi ni kwamba serikali haifanyi jitihada zozote kudhibiti uuzaji na matumizi ya kileo katika nchi yetu (pengine kutokana na kodi kubwa inayokusanya kutoka katika biashara ya vileo). Matokeo yake pombe huuzwa kwa mtu yeyote bila kujali umri wake, muda wala mazingira inapouzwa pombe hiyo.

Leo hii makampuni makubwa yanayouza vileo ikiwa ni pamoja na kampuni ya TBL yanafanya matangazo mengi ya kuwashawishi wananchi kunywa pombe bila kujali matangazo hayo yanawavutia watoto wadogo. Hebu fikiri yale magari yanayotangaza bia mitaani kwa kupiga muziki huku kina dada warembo wakicheza mayenu na kugawa zawadi za bia kwa wananchi waliokusanyika.

Ni hivi juzi tu kampuni maarufu ya bia nchini iliendesha tamasha kubwa la muziki ambapo kiingilio ilikuwa kopo la bia ambayo mteja alipaswa kuinunua uwanjani hapo. Katika tamasha hilo washiriki wengi walikuwa vijana wadogo wenye umri chini ya miaka 18 ambao waliuziwa pombe bila hofu wala aibu.

Ni lazima tukubali ukweli kwamba pombe ni hatali kwa afya na maendeleo. Ndio maana nchi zilizoendelea (Marekani, Ulaya na hata baadhi ya nchi za kiarabu) zimeweka taratibu kali za kudhibiti matumizi ya vileo ikiwa ni pamoja na kuzuia uuzaji wa pombe kwa vijana wenye umri chini ya miaka 21 (kwa USA), kuzuia unywaji wa pombe hadharani, kupanga masaa maalum ya uuzaji wa pombe na kuzuia aina zote za matangazo ya pombe yanayo walenga vijana wadogo.

Ni jambo lililo dhahiri kwamba ulevi ni adui wa maendeleo na hivyo kuendelea kujenga taifa la walevi ni hatari kwa maendeleo, afya na usalama wa jamii yetu. Ni kwa sababu hiyo tunaishauri serikali kutoa elimu kwa umma kuhusu madhara ya utumiaji vileo.

Aidha ni vema serikali ikatunga sheria kali za kudhibiti uuzaji holela wa vileo ikiwa ni pamoja na kupiga marufuku uuzaji wa pombe kwa watoto wenye umri chini ya miaka 18.Ni muhimu sheria hizo pia zifafanue aina ya matangazo ambayo makampuni ya uuzaji vileo yanaruhusiwa kufanya ili kudhibiti matangazo yanayowalenga vijana wadogo, na pia kutamka maeneo na muda unaoruhusiwa kuuza vileo kisheria.

Kama serikali isipochukua hatua za haraka kudhibiti ongezeko la walevi nchini, si ajabu nchi yetu ikaendelea kudidimia katika wimbi kubwa la umaskini wa kujitakia. Na watu wengi wataendelea kuamini kuwa serikali inaendekeza ulevi ili wananchi wengi wasione hali ngumu ya maisha iliyoko nchini na kuipigia kelele serikali.
Na Mwana Dikala
TUONANE TENA PANAPO MAJALIWA!!!

Tuesday, July 31, 2012

MGOMO WA WALIMU NCHINI TANZANIA...BASI NGOJA MIMI NIWE MWALIMU

 Mwanafunzi anapoamua kuchukua nafasi ya ualimu. Hakika hapa ndipo inapoonekana walimu ni watu/walezi muhimu sana....
...Walimu wamegome je sisi wanafunzi tufanyeje?? Kumbukeni kuwa sisi tuna haki ya kupata ELIMU.

HAPA NI KIFUNGUA KINYWA CHA LEO CHAI KWA CHAPATI NI KAZI YA MIKONO YANGU!!!!

 Chapati zikiwa tayari kama chakula cha asubuhi ya leo ni kazi ya mikono yangu mwenyewe...mimi Nangonyani. Bahati mbaya sikuweza kujipiga picha wakati naandaa...na wengine wote walikuwa hawajaamka wakati naandaa...
......na hapa ndivyo meza ilivyoandaliwa... Chai chapati.

Monday, July 30, 2012

SIO LAZIMA UAMBIWE KWA MDOMO....

....hata kwenye kanga ni tosha kabisa...

WANAUME NA KUFUNDISHWA!!!!

Mwanamke anaweza kufikiri ataimarisha upendo kwa kumwambia mwanaume, "fedha unazopata, tungetumia sehemu na sehemu tukaweka akiba,, tukatafuta kiwanja. halafu tukatafuta sehemu kama shamba, halafu..." Anaweza kushangaa sana akiona mwanamume badala ya kushukuru kwa ushauri huo, akimwambia, "unadhani ni rahisi kiasi hicho, ingekuwa ni wewe unayetafuta fedha hizo wala usingesema hivyo. Nyie wanawake ndiyo matatizo..."
Halafu yanaweza kufuata maneno mengine ya "ajabuajabu" kutoka kwa mawamume hadi mwanamke akanywea. Mwanamke ataanza kujiuliza kosa lake kwa ushauri wake huo uliouona ni wa upendo. Ni wazi hataliona kosa lake, hivyo atajua kwamba, mumewe hampendi tena,  atajua kwamba upendo umekwisha. kama si kujua kwamba upendo umekwisha, atajua kwamba mumewe hamsikilizi wala kumjali, ni dikteta na asiyeambilika.
Ni kwa sababu tu ya kutokujua hata hivyo. Kosa la mke huyu ni kushindwa kwake kujua kwamba, yeye na mwanamume wanatofautiana. Mwanamume hataki kabisa kufundishwa, hataki kabisa kuelekezwa au kushauriwa kabla hajaomba mambo hayo kutoka kwa mkewe. Kwa asili manamume ni mbabe na angependa kuona kwamba mwanamke anamtazama kwa jicho la kuwa yeye ni shujua na anayejua kila kitu. Anaposhauriwa bila kuomba, masikioni mwake husikia kama vile anaambiwa kuwa hayuko kamili na hajimudu na hivyo analaumiwa. Katika hali hiyo hujikuta akijitetea, ambapo matokeo yake ni hayo ya kumuuliza mke kama anadhani jambo hilo ni rahisi kama anavyoliongelea. Kuuliza huku kuna maana ya kumpa taarifa mkewe kwamba siyo kuwa ameshindwa ni ka sababu jambo hilo ni gumu. Anataka kumpa taarifa kwamba, huko "kumlaumu" kwake hakuna maana yoyote. Lakini kwa upande wa mke majibu hayo hayatoi maana hiyo, hutoa maana kwamba, mume hampendi tena na hajali ushauri wake.
Wanaume siku zote wanataka kuachwa watafute suluhu wenyewe, wanataka kuona wanahangaika na kupata wenyewe ufumbuzi wa tatizo au matatizo yanayowakabili. Wakipata wenyewe ufumbuzi bila msaada wa wake zao, huhisi kuwa uanaume wao umekamilika. Wake zao wanapojipeleka kimbelembele kutaka kuwapa ushauri kabla hawajaombwa wanatafuta kukorofishana kusiko kwa lazima. Hii ina maana kwamba, wanawake wasiwape ushauri waume zao? Hapana, haina maana hiyo.
Kwa kuwa mwanamume hataki kufundishwa au kuelekezwa na mwanamke, anachotakiwa mwanamke kufanya ni kumpa mwanamume "chakula" chake, ambacho ni sifa. Aanatakiwa kuanza kwa kuonyesha kwamba mumewe amemudu au amefanikiwa katika mambo fulani kabla hajaingiza ushauri wake. Kwa mfano, Mariam anataka kumfahamisha mumewe kwamba amejisahau kuhusu maisha yao ya baadaye kwa sababu ya matumizi mabaya ya fedha. Anachotakiwa kufanya ni kutafuta yale mazuri ambayo mumewe ameyafanya au anayafanya. Inaweza ikawa kujali familia au ndugu wa mke ama kingine chochote.
Baada ya hapo ndipo anapoweza kuanza kuzungumzia kuhusu haja ya kufukiria kuhusu maisha yao ya baadaye. "Uzuri wako mume wangu ni kwamba unapenda kusikiliza na kizingatia ninachosema, wanaume wengine siyo rahisi, tunaona wanavyowadharau wake zao..., Mwanamke anaweza kuanza maelezo yako hivyo. Halafu akaendelea, "Ehe, sasa vipi kuhusu kutafuta kiwanja cha bei rahisi kwa ajili ya kuja kujenga tukiwa na uwezo baadaye. Najua sasa hivi una majukumu memngi, lakini bila shaka siyo vibaya kufukiria kuhusu jambo hilo. " Ni wanaume wachache ambao baada ya sifa kama hizo watacharuka wakielezwa kuhusu kufikiria kuhusu mustakabali wa maisha ya baadaye. Ni vizuri kwako mawamke kujaribu kufanya hivyo, ili uthibitishe kuhusu ukweli wa maelezo haya.
Chanzo:- kitabu cha Maisha na Mafanikio na Munga Tehenan.

Sunday, July 29, 2012

POLE DADA MDOGO EDNA/FAMILIA YA ÖHDMAN KWA MSIBA/WAMEPOTEZA MTOTO WAO ...

 Blog ya Maisha na Mafanikio inapenda kuungana na Familia ya Öhman kwa pigo lililowapata mwanzoni wa wiki hii inayoisha leo. Mwanablog mwenzetu Edna alikuwa anasubiri mtoto. Bahati mbaya kiumbe kime kimewatoka. POLENI SANA, TUUNGANE NAYE KATIKA KIPINDI HIKI KIGUMU..NIMEONGEA NAYE ANAENDELEA VIZURI...http://ednaohman.blogspot.se/.

BLOGG YA MAISHA NA MAFANIKIO IMEONA TUMALIZE JUMAPILI HII NA DR. REMMY ONGALA ..KILIO!!!


NAWATAKIENI KILA LA KHERI.....

TUMALIZE JUMAPILI HII YA MWISHO YA MWEZI HUU KWA FURAHA NA AMANI!!

TUMAINI huzaa FURAHA. NA FURAHA huzaa AMANI.
JUMAPILI NJEMA SANA!!!

Saturday, July 28, 2012

NDIYO NIPO NANYI ...JUMAMOSI NJEMA WANDUGU,,,!!!


Likizo hii nimeona niwe hapa hapa si kwenda mbali sana kwa hiyo hizi siku nilizopotea nilikuwa hapa summer house ni mahali pazuri kwa kupumzika na kutafakari...wavuvi hao wanakwenda kutafuta kitoweo baba na kijana wake.....
...ila inakuja wakati lazima kurudi kuvuna mavuno hapa ni mboga za maboga, Bei rahisi fungu moja mia,,,:-)


 Hapa ni ni sehemu ambayo watu wengi wanapenda kwenda na watoto wao au wao tu kufurahi. Ni Skandinavian sehemu kubwa ya "water land" SKARA SOMMAR LAND.
..Bado tulikuwa kule ilikuwa ALHASMIS ..baba na kamanda wake wakiendesha magari kama kucheza----
NAWAKUMBUKENI SANA NA TUPO PAMOJA,,,,KILA LA KHERI!!!!

Tuesday, July 24, 2012

KUADIMIKA KWA MUDA!!! LIKIZO....

 Mmmmmhh! Ngoja kwanza nikune kichwa naona kama nimeishiwa cha kusema vile..ni hivi ni raha sana kuwa na ndugu marafiki na jamaa...lakini sasa umefika muda wa kuwa pamoja na familia...niwanongóneza ni kwamba nipo Likizo...
Ila nitajitahidi kuwa nanyi pia kinamna ili tusisauliana..ila mmmhhh kuwasahau ndugu si rahisi...hapa naona kama kapulya hana furaha:-( WOTE MNAPENDWA NA TUPO PAMOJA.  MMEONA ZAWADI YANGU YA HUO UTAMADUNI/KIMASAI:-)

BIDHAA ZITOKANAZO NA UBUYU - Mafuta, Sabuni, Vipodozi, na Dawa"




Marietha Mkuya Aendesha maisha yake kwa kuuza bidhaa zitokanazo na Ubuyu
MAISHA ni kuhangaika bila kukata tamaa, kutumia kila aina ya ubunifu hasa ukiwa mjasiriamali. Hili limeonekana kwa Marietha Mkuya; mjasiriamali anayetengeneza bidhaa nyingi, zote zikitumia malighafi moja tu, Ubuyu.
Nikiwa kwenye Maonyesho ya Biashara ya Kimataifa ya Sabasaba, ndipo nilipokutana na mama mjasiriamali huyu kutoka mkoani Dodoma.
“Karibuni mjaribu bidhaa za ubuyu kutoka mkoani Dodoma.” Ndivyo alivyokuwa akiwakaribisha watu mbalimbali waliokuwa wakipita karibu na banda lake.
Anasema kama ilivyo kwa zao mhogo ambalo lina faida nyingi, ubuyu pia unafaida nyingi kiafya na kitabibu pia.
Muya anasema ubuyu unaweza kutumika kama dawa na pia kama kirutubisho cha mwili na pia unaweza kutumia ubuyu kama kipodozi.
Mama Mkuya ni mmiliki wa Kampuni ya kutengeneza vyakula ya Geitana Food Processor iliyopo mjini Dodoma,ambayo inajishughulisha na usindikaji wa bidhaa zinazotokana na ubuyu.
“Kwa takribani miaka minne sasa, nimekuwa nikijihusisha na utengenezaji wa bidhaa za ubuyu, napata malighafi hii kwa urahisi zaidi hasa ikizingatiwa kuwa Mkoa wa Dodoma unazalisha ubuyu kwa wingi.” anasema mama Mkuya.
Mjasiriamali huyu, ameweza kutengeza unga unaotokana na kiini cha ubuyu, ambao hutumika kama kiungo cha mboga kama ilivyo kwa karanga.
Pia kwa kutumia mbegu hizo za ubuyu, ameweza kutengeneza mafuta ambayo hutumika kama dawa kupunguza mafuta mwilini.
Si hivyo tu, ameweza kutumia ubuyu kutengeneza sabuni ambayo ni nzuri kupambana na aina mbalimbali za magonjwa ya ngozi.
Kwa mujibu wa Mkuya, ametengeneza dawa kwa kutumia majani ya ubuyu, dawa ambayo husaidia kupambana na maradhi sugu na kuongeza kinga ya mwili hasa kwa wagonjwa wa Ukimwi.
Akielezea jinsi alivyoingia kwenye ujasiriamali, mama Mkuya anasema ujasiriamali kwake uko kwenye damu kwani kwani alianza akiwa msichana mdogo sana, wakati huo alikuwa akiuza biashara ndogondogo gulioni.
“Nilianza kwa kuuza maji ya kunywa kwenye gulio, kisha nikaendelea na kuuza viazi, kadri siku zilivyokuwa zikienda nilikuwa nikibadilisha biashara kulingana na soko langu.” anasema.
Anaongeza kusema kuwa, kila alipoona bidhaa Fulani inasoko kubwa, basi alibadilisha na kuanza kufanya biashara hiyo.

Kuwa mjasiriamali

Mkuya anasema alilazimika kuingia kwenye ujasiriamali akiwa na umri mdogo baada ya wazazi wake kumlazimisha kuolewa baada ya kumaliza elimu ya msingi.
“Baada ya kumaliza elimu yangu ya msingi, baba yangu aliona bora aniozeshe jambo ambalo nilipingana nalo vikali.” anaongeza.
Anasema kutokana na hilo aliamua kukimbilia kanisani na kuamua kuwa Mtawa. Hata hivyo hakudumu kwenye Utawa kwakuwa familia yake ilikuwa kwenye umasikini na yeye ndiye aliyekuwa akitegemewa, alishindwa kuendelea na mafunzo ya utawa na kurudi nyumbani baada ya vuguvugu la kutaka aolewe kwisha.
“Familia yangu ilikuwa ikikabiliwa na umasikini mkubwa, hivyo nikaona ni vyema nikaingia mtaani kwa ajili ya kutafuta pesa.” anaeleza.
Mafunzo
Mkuya anasema baada ya kufanya biashara ndogo ndogo kwa muda mrefu, alibahatika kupata nafasi ya kuhudhuria mafunzo ya ujasiriamali yaliyokuwa yakitolewa na Shirika la Viwanda Vidogo (SIDO)
“Huko nilijifunza masomo kadhaa ya ujasiriamali kama vile usindikaji wa vyakula, ufungasahaji, uhifadhi na pia namna ya kutafuta masoko kwa ajili ya bidhaa ninazoweza kusindika.” anasisitiza.
Ujuzi alioupata Sido ulitosha kabisa kumfanya kuwa mjasiriamali ayekomaa kwani alianza kufanya biashara mbalimbali kama kusindika karanga na mama lishe.
“Sifa ya mjasiriamali ni kujifunza. Kila siku sikusita kujifunza vitu vipya, nilikuwa nikitamani kuingiza bidhaa mpya katika soko langu mara kwa mara, hapo ndipo niliposhawishika kuanza biashara hii.” anaeleza.
Anasema awali alianza kwa kuuza ubuyu na unga wake kwa wateja waliokuwa wakitoka Dar es Salaam.
“Wakati nikiendelea na ujasiriamali wangu,walipokuja Wajapani na kutufufundisha jinsi ya kusindika ubuyu, hapo ndipo nilipopata utaalamu wa kukamua mafuta ya ubuyu pamoja na kutengeneza bidhaa zake.” anaeleza.
Mafanikio
Anasema alianza akiwa na mtaji mdogo wa Sh50,000, lakini hivi sasa mtaji wake umeongezeka na kufikia zaidi ya shilingi milioni moja, huku akiwa ameajiri watu sita anaofanya nao kazi.
Mkuya ni mama wa watoto wawili, alizaliwa mwanzoni mwa miaka ya sabini akiwa mtoto wa kwanza kwenye familia ya watoto wanne.
Nimetumiwa na http://varsitycollegetz.ning.com Source: Mwananchi

Monday, July 23, 2012

PICHA YA MWEZI:- KUJIFUNZA MAPISHI (KUJIPIKILISHA)!!

Picha hii inanikumbusha mbali sana, jinsi ya kujifunza kupika MAPISHI. Eee bwana weee basi hapo ndiyo hapo hapo pa  kujifunza maisha baba na mama...Je wewe msomaji uliwahi kucheza mchezo huu?.

Tuendelee na ile yetu …….HADITHI HADITHI…..HAPA NI HADITHI YA MVUVI NA SAMAKI WA DHAHABU!!!



Ilipoishia ”Usiwe na hofu, baba kizee enenda kwa amani sasa.” Baba Kizee alirejea kwa mkewe mzuri. Lo! Akaona nini? Jumba zuri na barazani mkewe amesimama , amevaa vazi la maridadi la nyoya jema. Na kichwani kavaa kilemba kilichotariziwa vilivyo na vito vyema vikimning´nia shingoni. Na pete za dhahabu zilipamba vidole vyake na viatu vyororo vyekundu vikimkubali miguuni….NA SASA INAENDELEA…………
Na mbele yake watumishi wakimhangaikia, huku akiwavuta nywele zao na kuwacharaza bakora. Baba kizee akamsaili mkewe mzuri “Je, waonaje sasa mke wangu sasa roho imeridhia kibibi? Mkewe akamjibu kwa jeuri , na kumpeleka mazizini kufanya kazi za suluba huko.
Wiki moja ilipita iklifuatwa na nyingine. Na mkewe mzuri akiwa haridhiki kupita siku zote. Akamwamuru baba kizee aende tena baharini. “Enenda tena baharini ukamkabili samaki mkuu mwambie sitaki kuwa mwanamke wa basaba bora bali malkia mwenye enzi!”
Baba kizee akaona vi mno akadahili kwa nguvu. ”Nini tena, ew mwanamke! La hasha umechanganyikiwa! Kumbuka ya kuwa wanena na kutenda. Kama mke wa mvuvi utaifanya milki nzima ilemewe na kicheko!”
Mke wa mvuvi akazidi kisirani akamvuta masikio mumewe na kusema ”unathubutuje kubishana . Ewe kisonoko na mimi mwanamke wa nasaba  bora? Elekea hivi sasa baharini nakuamuru! Kama hutaki, nitakuburura hadi huko!” Baba kizee alijizoazoa na kwenda tena baharini. Bahari ile ya maji ya mbingu ikawa nyeusi tii, tena inatisha.
Akapaza sauti yake, akaita na samaki wa dhahabu akaja akiogolea. ”Ni nini tena kinachokukera. Ewe baba kizee, hebu niambie!” Kwa mwinamo wa hadhi baba kizee alijibu sawia ”ujaliwe neema Ewe Bwana wa Samaki! Mke wangu mzuri amecharuka tena safari hii ajipa wazo hatakuwa tena mwana wa nasaba bora. Yu ataka kuwa Malkia mwenye enzi.” Naye samaki wa dhahabu akajibu ”Usijali, ewe baba kizee rejea nyumbani kwa amani nawe utamkuta mkeo mzuri yu malkia!”
Baba kizee alirejea kwa mkewe mzuri na nini alikiona? Jumba lla kifalme, likimilikiwa na mwanamke wa hila akiwa ametamakani mezani. Wakuu na mabwana wakimngojelea, wakimnywesha mvinyo kwenye chombo cha dhahabu huku akividonadona vipande vinono vya nyama. Huku walinzi wenye macho makali wakimlinda pande zote wakiwa wamejihami kwa vishoka mikononi. Baba kizee akatupa jicho huku na huko. Jicho likamfeli, akagwaya! Alijiinamia hadhi ardhini mbele yake na kuweza kutoa maneno haya ”Heshima kwako na kicho Ewe malkia habe niambie sasa ikiwa moyo wako umeridhika?” Mkewe hakumthamini hata kwa mtupo wa jicho bali aliamuru watu wake kumuondolea mbali. Ndipo waungwana na wa nasaba bora wakamwelemea mbiombio wakamkwida shingoni. Na kumbeba hangahanga na mabawabu wa mlangoni wakamsindikiza nje kwa vishoka vyao.
Na halaiki yote kwa jumla yao wakajisheheni kwa kicheko. ”Hiyo ndiyo tosha yako ewe kizee mtovu wa busara! Na hilo liwe funzo lako kujijua wewe u nani siku za hapo baadaye! Na hivyo wiki ikayoyoma na nyingine ikafuata. Mama kizee akazidi utakavu, akatuma wajumbe wake kumkamata baba kizee. Walimpata, wakamleta mbele ya Malkia. Naye mke mzuri akanena kwa mumewe ”Enenda tena ukasujudu kwa samaki mkuu. Sitaki tena kuwa Malkia mwenye enzi, bali nataka kutamalaki maziwa yote na bahari na katika vina vya bahari. Nitaweka ngome yangu na huyo samaki wa dhabu atanitumikia mimi. Huku nikimtuma kotekote!” Baba kizee hakuthubutu kupinga kauli ya mkewe hivyo akaenda tena baharini na tazama! Tufani kuu ilitokea mawimbi makuu yaliinuka kumlaki, tetemeko tupu, muondoko wa ghasia, muungurumo mkuu hata hivyo baba alipaza sauti na kuita. Na samaki wa dhahabu akaja akiogelea ”kulikonit ena baba kizee njoo unieleze!” Kwa mwinamo wa hadhi baba kizee akajibu sawia ”Na ujaliwe neema Ewe Mkuu wa Samaki! Nimfanyeje huyu mwanamke? Huyu ajuza mjinga, hataki tena kuwa Malkia pia anataka kutawala maziwa na bahari. Anataka kuweka ngome zake katika vilindi vya bahari, na kukufanya wewe mwenyewe umtumikie. Na kukutuma wewe huk ona huko.” Samaki wa dhahabu alitulia tuli pasi na jibu na badala yake alipiga mkia wake majini akajerea kwenye maji makuu. Baba kizee alisimama ukingoni, akisubiri . Alisubiri kwa muda mrefu, lakini halikuja jibu. Hatimaye akarejea kwa mkewe mzuri, na tazama! Akamkuta amekaa mekoni kwenye kibanda kikongwe cha udongo na miti na mble yake kukiwa na kibeseni kilichoraruka hadi katikati. HADITHI IMEKWISHA..
Je Hadithi hii inatufunza nini? 

Sunday, July 22, 2012

NAPENDA KUWATAKIENI JUMAPILI NJEMA NDUGU ZANGUNI WOTE!!

Nachukua nafasi hii na kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunilinda, kuniongoza, kunifanya nipate chakula, na kuniepesha na yasiyo mema. Nakutumaini wewe Mungu wangu , eh Mungu, wewe ni mwamba imara katika maisha yangu ...... Pia napenda kuwaombea familia, ndugu, wazazi/walezi, marafiki, majirani, wafanyakazi wenzangu pia hata madui zangu. Mwenyezi Mungu na atushushie wote baraka na upendo pia amani ...AMINA. . NA UJUMBE WA LEO NI:- SISI SOTE NI NDUGU,WATOTO WA BABA MMOJA. 
Labda tumalizie jumapili na mwimbo huu wa Bony Mwaitege SISI SOTE.. 

JUMAPILI NJEMA SANA!!!!!

Saturday, July 21, 2012

KATIKA MAISHA KUPUMZIKA NI MUHIMU/RAHA JIPE MWENYEWE!!!!

Unapokuwa na mapumziko ya siku mbili tatu hivi kabla hujapata likizo kamili basi unakimbia na kujificha hapa (SUMMER HOUSE/SOMMARSTUGA). Mahali ambapo unaweza kupumzika tu hakuna eti ngoja niangalia mtandaoni kuna nini HAKUNA.
Na ukitokwa na jasho au ukijisikia uchovu basi ni kujitupa tu majini huna haja ya kwenda mbali kutafuta maji.......

 Ila kula ni muhimu ..akina mama wapo jikoni, na hapo ni mzee wa nyumba na pia ni raha kufikiwa na wageni aliyevaa kofia ni mgeni wetu mzee Masawe.......

 ...Wanapofika wageni ni raha kwani siku hii nilipata zawadi ambayo nilikuwa naitamani siku nyingiiiiii:-) Hiyo hapo juu UTAMADUNI !!!

 Tunapojisikia hamu ya samaki basi ni kuchukua boti na kwenda  kujaribu...wavuvi wadogo haoooo  wanakwenda kutafuta kitoweo....
Baada ya muda wanarudi mikono mitupu hakuna kitoweo...hivi ndivyo ilivyokuwa siku mbili/tatu nilipokuwa kimya...NAWATAKIENI WOTE JUMAMOSI NJEMA.....KAPULYA:-)

Friday, July 20, 2012

MSIONE UKIMYA .....NIPO KIAINA!!!

Habari za siku mbili/tatu jamani ndugu zanguni. Nimeona nikate ukimya nipo....Kesho nitawasimulia nini kisa cha kuwa kimya...IJUMAA NJEMA!!

Monday, July 16, 2012

HADITHI HADITHI…..HAPA NI HADITHI YA MVUVI NA SAMAKI WA DHAHABU!!!

Nieipenda hadithi hii na nimeona nisiwe mchoyo ni hadithi nzuri hata kwa watoto wangu wamekisoma ....nimeisoma kwenye kitabu na mwandishi ni Alexander Pushkin. Haya karibuni.

---------------------------------------------------------------------------------------------------------
Hapo zamani za kale. Palikuwepo na mzee mmoja, aliyeishi na mke wake mzuri sana kandokando ya bahari yenye maji ya rangi ya mbingu na kina kirefu. Waliishi kwenye kibanda cha udongo na miti.
Walikuwa wameishi pale kwa miaka thelathini na siku thelathini. Baba Kizee akivua samaki na bibi mzuri akifuma nguo.
Siku moja baba kizee alitupa nyavu baharini, nyavu alizivuta juu zilikuwa zimejaa uchafu wa baharini. Alitupa tena nyavu baharini, nyavu alipozivuta juu zilijaa gugu-bahari.
Mara ya tatu, nyavu zikazamishwa tena majini nyavu alipozivuta juu :- Tazama! Alikuwemo samaki mmoja. Si samaki wa kawaida, bali ni samaki wa dhahabu.
Samaki wa shahabu, akaomba msamaha. Huku akisema kwa sauti ya binadamu ”Ewe baba kizee, nirejeshe baharini nitakulipa malipo mema, nitakupatia chochote utakacho.”
Baba kizee alipigwa na mghafala. Akaingiwa na woga. Alikuwa amevua maeneo haya kwa miaka mitatu na ushee lakini hata siku moja hakupata kumsikia samaki anayezungumza.
Akamwachia samaki uhuru wake huku akisema maneno ya huruma. ”Ewe samaki wa dhahabu enenda kwa salama katika njia zako huna haja ya kunilipa fadhila. Rejea kwenye kina cha bahari na kuogelea na kupiga mikambi utakayo.”
Baba kizee alirudi kwa mkewe mzuri akamwadithia kuhusu kioja.
”Leo nilimnasa samaki wa ajabu si wa kawaida, bali wa dhahabu samaki huyo alinena lugha yetu akanisihi nimrejeshe baharini na akaniahidi zawadi maridhawa kwa kunitaka nitaje nitakacho! Nami sikutaka ujira wake nikamrejesha baharini bila malipo.”
Mke akamwambia mumewe kwa karipio ”Kefule, mjinga kichwani we! Huwezi kupata pato la samaki ukashindwa hata kuomba kibeseni cha kuogea! Tazama kile cha kwetu kilivyoraruka katikati.
Baba kizee akaenda kwenye bahari ile ya maji ya mbingu tena yenye kina kikuu, akaona jinsi bahari ilivyochafuka akapaza sauti yake, akaita na mara samaki wa dhahabu akaja akiogelea ”Kulikoni baba kizee nieleze nami nijue!”
Kwa mwinamo wa hadhi baba kizee alijibu ”Ewe mwenye rehemu Ewe mkuu wa samaki! Mke wangu mzuri ana uchungu nami haniachii kwa kutaka utakalo ataka tuwe na beseni jipya la kuogea kwa kuwa la kwetu kongwe limeraruka hadi katikati”.
Samaki wa dhahabu naye akajibu sawia ”Usiwe na hofu kamwe ewe baba kizee na enenda sasa kwa amani huko uendeko. Utalikuta hilo beseni jipya!” Baba kizee alirejea kwa mkewe mzuri na kujionea mwenyewe baseni jipya liko pale. Lakini bibie ukali akazidisha Mjinga wahedi yaani hilo ndilo ombi lako kuu hilo beseni la kuogea! Kuna faida gani kamwe” Kuwa na beseni tu la kuogea? Hebu rudi himahima enenda kwa samaki mkuu. Uende umwinamie, umwombe kijumba kizuri. Baba kizee akashika njia kwenda kwenye ile bahari ya maji ya rangi ya mbingu. Sasa bahari ilikuwa nyeusi iliyoghafilika.
Baba kizee akapaaza sauti na kuita na samaki wa dhahabu akaja akiogelea ”kulikoni baba kizee hebu uniambie hima!
Kwa mwinamo wa hadhi baba kizee akajibu ”Rehema iwe kwako Ewe mkuu wa samaki mke wangu mzuri amesawijika zaidi haniachii huru ila kuningángánia hatatulia bila kupata kijumba kizuri.” Samaki wa dhahabu akajibu sawia ” Usijali baba kizee enenda sasa kwa amani utapata takwa lako la hicho kijumba kizuri.”
Baba kizee akarejea kwenye kibanda chao kikongwe, hakuona dalili yoyote ya kibanda kikongwe. Badala yake akaona kijumba kipya, kizuri mno! Kimepakwa chokaa, kina mnara mzuri wa kupitishia moshi. Na milango ya mpingo , pia na dirisha la nakshi.
Na katika kiti cha bustanini aliketi mkewe mzuri, huku akiwa hajitambui kwa mahasira yaliyomzonga ”Kefule, pumbavu wewe usiye na kitu kichwani! Yaani hicho ndicho ulichoomba kijumba hicho cha ovyo! Rudi tena kwa samaki mkuu mwinamie na kumwambia mimi sitaki kuwa mke asiye na hadhi bali mwanamke wa nasaba bora!” Baba kizee alikwenda tena baharini. Nayo bahari ikachafuka zaidi na kusikitika. Baba kizee akapaaza sauti, akaita na samaki wa dhahabu akamjia akiogelea. ”Kulikoni ewe baba kizee, hebu niambie nami nijue!”
Kwa mwinamo wa heshima baba kizee akamjibu sawia. ”Usijali neema, ee Mkuu wa Samaki! Mke wangu, kwa roho isiyosikia kitu haniichii nikapata pumzi. Sasa ameamua hatakuwa mwanamke dhalili yeye ataka kuwa mwanamke wa nasaba bora!”
”Usiwe na hofu, baba kizee enenda kwa amani sasa.” Baba Kizee alirejea kwa mkewe mzuri. Lo! Akaona nini? Jumba zuri na barazani mkewe amesimama , amevaa vazi la maridadi la nyoya jema. Na kichwani kavaa kilemba kilichotariziwa vilivyo na vito vyema vikimning´nia shingoni. Na pete za dhahabu zilipamba vidole vyake na viatu vyororo vyekundu vikimkubali miguuni….ITAENDELEA……

TUANZE JUMATATU HII NA SALAMU/UJUMBE HUU!!!

Kuna vitu viwili mtu anaweza akafanya katika kuutafuta ukweli.
Ni:- Kutokuwa mkweli/kusema kitu moja kwa moja na kushindwa kuanza.....
JUMATATU NJEMA....

Sunday, July 15, 2012

JUMAPILI/DOMINIKA NJEMA NA WIMBO HUU WA DADA EMMY KASIGEI ALAKARA!!


Katika waimbaji niwapendao dada Emmy yupo kwenye orodha hata kama sielewi anaimba nini lakini ni raha ilioje kumsikiliza. Pia nampenda dada huyu kwa jinsi alivyo na pia mavazi yake.
JUMAPILI NJEMA SANA KWA WOTE NA YEYOTE ATAKAYEPITA HAPA ABARIKIWE SANA. AMINA....

Friday, July 13, 2012

TASWIRA YA MJI WA NJOMBE:- HAPA ILIKUWA MWAKA JANA...

Picha imepigwa nikiwa nimesimama "mtaa" uitwao KIHESA maana Kihesa ipo juu kidogo na ni karibu na Njombe girls kama sikosei....

HOMA YA NGURUWE YAUA NGURUWE ZAIDI 110 IRINGA, SERIKALI YAPIGA STOP ULAJI KITIMOTO!!!!


Mbunge wa jimbo la Kilolo Iringa Prof.Peter Msolla akitazama nyama ya kitimoto iliyokuwa ikiuzwa mnadani eneo la Nyanzwa mapema mwaka jana

SERIKALI Iringa yapiga uchinjaji na uraji wa nyama ya nguruwe (kitimoto) baada ya kuibuka upya kwa ugonjwa wa homa ya Nguruwe uliopelekea nguruwe zaidi ya 100 katika Manispaa ya Iringa na Iringa vijijini kufa kwa ugonjwa huo.
Ugonjwa huo unatishia maisha ya Nguruwe 36,179 wenye thamani ya shilingi bilioni 5, 426,850,000 kwa upande wa wilaya ya Iringa vijijini pekee huku katika Manispaa ya Iringa nguruwe 2812 zenye thamani ya shilingi milioni 421,800,000 wapo hatarini kukumbwa na ugonjwa huo.
Kaimu afisa mifugo wa wilaya ya Iringa vijijini Said Kolwa aliueleza mtandao huu wa www.francisgodwin.blogspot.com leo kuwa kutokana na kuwepo kwa ugonjwa huo katika wilaya hiyo ya Iringa tayari serikali imechukua hatua mbali mbali za kunusuru maambukizi zaidi ya ugonjwa huo ikiwa ni pamoja na kuzuia uchinjaji wa nguruwe katika wilaya nzima ya Iringa.
Alisema kuwa Halmashauri ya Iringa ilipokea tarifa ya kuwepo kwa vifo vya nguruwe katika kata ya Lyamungungwe juni 28 mwaka huu ambapo ufuatiliaji ulifanyika kuanzia Juni 30 hadi Julai 2 na kubaini kuwepo kwa ugonjwa huo katika vijiji vya Kikombwe ,Igunda hivyo kuchukuliwa Sampuli ambazo baada ya kupimwa ilibainika ugonjwa huo.
Kwani alisema katika kijiji cha Kikombwe jumla ya mazizi 5 yenye nguruwe 14 yalikuwa yameambukizwa na kati ya nguruwe 7 walikufa na kijiji cha Igunda jumla ya mazizi 10 yenye nguruwe 14 yalikuwa yameambukizwa na kati yao nguruwe 28 walikufa kwa ugonjwa huo.
Kolwa alisema kuwa ugonjwa huo unadaiwa kuingizwa na mmoja kati ya wafanyabiashara wa nyama ya nguruwe ambaye aliingiza kwa siri nguruwe katika kijiji cha Igunda akitokea kata ya ukumbi wilaya ya Kilolo ambayo imekubwa na ugonjwa huo.
Hata hivyo alisema kuwa kutokana na ugonjwa huo tayari ofisi ya mganga mkuu wa wilaya hiyo Dr .Mathias Matandala imetoa tangazo la tarantini juu ya ugonjwa huo wa homa ya nguruwe (African Swine Ferver) ikiwa ni pamoja na kuzuia biashara zote za nguruwe na nyama ya nguruwe katika wilaya hiyo pia kuingiza wala kutoa nguruwe katika wilaya hiyo.
Wakati kwa upande wake afisa mifugo katika Manispaa ya Iringa Dr .Augustino Nyeza alisema kuwa katika Manispaa ya Iringa ugonjwa huo ulibainika Juni 24 katika kata ya Mkwawa ambapo wafugaji wa nguruwe katika eneo la Don Bosco na Makanyagio ndio nguruwe zao zilianza kukumbwa ugonjwa huo na kusababisha vifo vya nguruwe 80.
Hata hivyo alisema hatua zilizochukuliwa hadi sasa ni kufunga machinjio mawili yalipo katika Manispaa ya Iringa katika eneo la Ipogolo na mjini pia kufunga vibanda vyote vya kitimoto na maeneo yote ya uuzaji wa kitimoto mjini Iringa .
Alisema kuwa mizoga yote ya nguruwe waliokufa kwa ugonjwa huo ilifukiwa chini ya ulinzi makali na mabanda 118 ya nguruwe yalipulizwa dawa .
HABARI NA PICHA KUTOKA http://francisgodwin.blogspot.se.

Thursday, July 12, 2012

NYUMBA ZA ASILI...NYUMBANI NI NYUMBANI!!!!

 KITU GOROFA SIO MPAKA MJINI SASA NI MPAKA VIJIJINI
NAWATAKIENI WOTE MEMA...

KIPANYA CHA LEO!!!

KILA LA KHERI KWA WOTE!!!

Wednesday, July 11, 2012

KWA VILE NI SIKU YA MARUDIO BASI TUANGALIA NA HAPA...HUYU NI DADA ESTER ULAYA SIJUI HILO NI SHAMBA LAKE TUJE KUCHUMA KISAMVU??!!!

Yaani hapa nimetamani hicho kisamvu halafu nimeangalia nimeona pia kama kuna mlenda pori vile. Najigamba sikuchukua mbegu za mihogo. Eti hata ule wa kutafuna tu hakuna. Safari ijayo ntajitahidi..LOL..  Ukitaka kufaidi mambo mengine afanyayo mdada huyu basi gonga hapa. Haya niwatakieni mwendelezo wa siku mwema...

NAPENDA KUWATAKIENI WOTE JUMATANO NJEMA NA UJUMBE HUU!!!

HAYA NDUGU ZANGUNI NI ILE JUMATANO YA KIPENGELE CHA MARUDIO YA MATUKIO MBALIMBALI. KWA HIYO LEO NIMEONA NIWEKE PICHA HII AMBAYO NILISHAWAHI KUIWEKA. KARIBUNI....

Macho ya huruma hufurahisha moyo, habari huburudisha mwili. Kuchukiana huendekeza fitina, kupendana husitiri makosa yote. Nilikuwa mgonjwa ukaja kuniona .Nilikuwa na njaa ukanilisha. Kumhudumia mgonjwa ni wito. JUMATANO NJEMA KWA WOTE . NA KUMBUKENI WOTE MNAPENDWA!!! NA PANAPO MAJALIWA BASI TUONANE TENA WAKATI MWINGINE.