Thursday, June 30, 2016

HILI NI CHAGUO LA BLOG YA MAISHA NA MAFANIKIO KUWA PICHA AZIPENDAZO NA ZA MWISHO WA MWEZI HUU WA SITA

 Huwa najisemea  mara nyingi sana hakuna kabila litunzalo mila, tamaduni kama kabila la kiMasai ebu angalia hao akina kaka mavazi yao au tu kwa ujumla jinsi uwaonavyo wanavyothaminimila/utamaduni wao

Na hawa akina dada yaani mavazi yao ni rahisi na wamependeza. Bado watu tunahangaika  na utamaduni wa watu wengine  sijui masuruali.....nk. Kwanini kuiga utamaduni wa wengine wakati wenyewe tuna utamaduni mzuri na wa kuvutia?.....

Wednesday, June 29, 2016

UKOSAPO NENO JEMA, KHERI UJINYAMAZIE.

Nakuasa usikie, usemaji ni karama,
Maneno usirukie, sema mambo kwa kupima,
Utamkapo ujue, neno halirudi nyuma,
Ukosapo neno jema, kheri ujinyamazie.

Kheri ujinyamazie, ovu huleta khasama,
Majuto yasikujia, “Laiti nisingesema”,
Mtu baa azuae, Motowe utamchoma,
Ukosapo neno jema, kheri ujinyamazie.

Ni wengi wajiponzao, kwa zao mbovu kalima,
Heshima waitakao, waseme usemi mwema,
Wale waumbukanao, ni kwa ndimi kuparama,
Ukosapo neno jema, kheri ujinyamazie.

Watazame wakuao, dunia kuwatazama,
Ni wale wapimiao, kabla ya kuyasema,
Na kimya wanyamazao, wakosapo neno jema,
Ukosapo neno jema, kheri ujinyamazie.

Neno huenda likuwe,lizidi hata vilima,
Mambo mawi liyazue, akili zende mrama,
Au mema yatukie, liwapo neno la wema,
Ukosapo neno jema, kheri ujinyamazie.

Funzo walitufunzao, wazungupule wa zama
Zama za kale na leo, walokimcha Karima,
Yawe mema tusemao, tusije zusha zahama,
Ukosapo neno jema, kheri ujinyamazie.

Mola akubarikie, na ambaye akusoma,
Na furaha ututie, uwe ni diwani njema,
Mema utuhadithie, wana kwa watu wazima,
Ukosapo neno jema, kheri ujinyamazie.

Shairi hili limetungwa na Mshairi maarufu Afrika Mashariki Bwana Amri Abedi, nami nimeona sio vibaya kulirejea ili tujifunze pamoja................. panapo  majaliwa tutaonana tena...

Tuesday, June 28, 2016

KUMBUKUMBU ISIYOSAULIKA...NIMEKUMBUKA MIAKA ILE NILIPOKUWA BINTI MDOGO NA KAZI YA KUTWANGA MIHOGO ILI KUPATA UNGA WA UGALI KULE NYUMBANI LUNDO/NYASA!

Ama kweli tumetoka mbali...nakumbuka shughuli hizi kama vile ilikuwa jana. Ila mama yangu huko aliko asterehe kwa amani. Ahsante mama kwa kunifunza hizi kazi, hata kama ilikuwa kwa mikwala:-) maana nakumbuka nilikuwa nachukua mihogo na vifaa vingine na kwenda kwa rafiki zangu Oliva,,, na huko sasa nikitoka saa nane  nyumbani kurudi saa kumbi na mbili. Kisa kucheza mipira wa kudaka(rede...redesta)...mmmmhhh we acha tu...je nawe unakumbuka shughuli  yoyote ile....

Monday, June 27, 2016

MABALAA HUMUANDAMA MTOTO WA KIKE TANGU AKIWA TUMBONI………!


Tatizo hili hufahamika kama Female Infanticide, yaani mauaji ya kukusudia yanayofanywa kwa mtoto wa kike. Achilia mbali kile kitendo cha mtoto kuuawa muda mfupi tu baada ya kuzaliwa, utelekezwaji wa mtoto wa kike mara tu anapozaliwa na kutoa mimba baada ya ugunduzi kwamba, ni mtoto wa kike, zote ni njia za kumuondoa mtoto wa kike duniani. Tatizo hili liko katika jamii zote zinazomchukulia mtoto wa kike kama balaa na yule wa kiume kama baraka kwa familia.
Kwa hapa nchini mtoto wa kike huuawa kwa njia isiyo ya moja kwa moja. Watoto wa kike hudharauliwa na kuachwa linapokuja swala la elimu katika familia. Ukichunguza hata wewe utabaini kwamba, katika familia nyingi, ambapo watoto wa kiume wamepata elimu bora, watoto wa kike katika familia hizo wamepuuzwa na hata kutopewa kabisa elimu.
Watoto wa kike, hasa wale wanaozaliwa nje ya ndoa wametelekezwa kirahisi, wamekataliwa na baba zao kirahisi, ukilinganisha na watoto wa kiume. Idadi ya watoto wa kike wanaokufa kutokana na kutelekezwa na kukataliwa na baba zao ni kubwa kuliko ya watoto wa kiume. Hata zile kesi nyingi za watoto kukataliwa na baba zao zinahusisha watoto wa kike zaidi.
Ni jambo la kushangaza kwamba ndoa ambayo ina watoto wa kike watupu hutazamwa kwa bezo na dharau ukilinganisha na ile yenye watoto wa kiume watupu. Hata wale wanawake wanaozaa watoto wa kike watupu hujihisi vibaya na kuamini kwamba walistahili kuzaa watoto wa kiume pia.
Kwa maeneo ua vijijini na katika familia masikini, watoto wa kike hutazamwa kama, ‘biashara ya kesho’ambapo watauzwa kwa njia ya mahari. Kwa hiyo thamani yao ni kuolewa, ni ile ya kibidhaa na sio kibinadamu. Na ndio maana mtoto wa kike anaposhindwa kuolewa huanza kuonekana kama mzigo usio na thamani, na hata kuzongwa hutokea.
Ili kujinasua na tatizo hili, msichana huenda kwa mwanaume yeyote kama kwa kujilazimisha. Kila mtu anajua kuhusu wazazi hapa nchini, ambao wamekuwa wakiwalazimisha binti zao kurudi kwenye ndoa za mateso kwa hofu ya kurejesha mahari. Kinachotokea ni binti hao kuuawa na waume zao. Ni wazi hii ni njia ya makusudi ya kuwapunguza wanawake, bila kujali mtu ataieleza vipi……………….
Chanzo........Jamii Forum

Sunday, June 26, 2016

JUMAPILI NJEMA.... LEO TUMETEMBELEA KANISA NDOGO LA SEMENARI YA PERAMIHO

KANISA NDOGO MPYA LA SEMINARI YA PERAMIHO
BARAKA ZA MWENYEZI MUNGU NA UPENDO ZIWE DAIMA KATIKA NYUMBA ZETU.

Friday, June 24, 2016

NAWATAKIENI MWISHO MWEMA WA JUMA ...NYASA HII! CHAKULA AKIPENDACHO KAPULYA

Ugali wa muhogo, Kisamvu, dagaa wabichi na kipande cha samaki tena kichwa...nakwambia hapo ni utamu tu....


Tuesday, June 21, 2016

ZAWADI KUTOKA KWA RAFIKI YANGU HUKO NYUMBANI....NI KISAMVU NA MIHOGO

 Nalipenda zao hili la muhogo sana kwanza unapata mboga, mti wake unaweza kutumika kama kuni...
...muhigo wenyewe unaweza kutafuna, kuchemsha na kula kwa chai asubuhi au chakula cha mchana au jioni pia unaweza kupika kama futari tena wakati huu wa mfungo wa Ramadhani  muhogo una  thamani ana. Maganda ya muhogo ni chakula kizuri sana kam unafuga baadhi ya wanyama pia samaki... hii ilikuwa  habari fupi kuhusu mihogo. Ila hii ni zawadi yangu kutoka kwa rafiki yangu. Najua kuna watu humu mmetamai:-)

Monday, June 20, 2016

SWALI KUTOKA KWA MSOMAJI WA BLOG YA MAISHA NA MAFANIKIO

Habari za leo ndugu zanguni...nimetumiwa huu ujumbe kwa barua pepe yangu..nimeona ni kheri niweke hapa kibarazani ili tusaidiani maana kwenye wengi pana mengi. Karibu tumsaidie huyo dada................................................................

Habari,  mimi ni dada ninayeishi Iringa nina umri wa miaka 18 kwa bahati mbaya mpenzi wangu amenipa mimba na kutokana namna alivyo baba yangu Naamini akifahamu kwamba nina mimba ataniua Kwani mimi ni mwanafunzi.
Nimeongea na mchumba wangu tumekubaliana tukaitoe.
Hata hivyo bado najiuliza kama kutoa mimba  ni kitu sahihi? Na je, nifanyeje Kwani nipo kwenye njia panda.

Sunday, June 19, 2016

JUMAPILI YA LEO TUPO KATIKA KIINI CHANGU NYUMBANI LITUMBANDYOSI...NA HILI NDIYO KANISA LETU

Kanisa hili ndilo alilosali babu, bibi, shangazi baba yangu na karibu wanafamilia wote wa Ngonyani husasani mimi Kapulya na  nimeshawahi kusali katika  kanisa hili na familia yangu....USISAHAU ULIKOTOKA NYUMBANI  KWA BABA YAKO NI NYUMBANI KWAKO.....JUMAPILI NJEMA KWA WOTE!

Friday, June 17, 2016

Thursday, June 16, 2016

LEO TUANGALIE METHALI ZETU ZA KISWAHILI....

1. Jirani mwema ni bora, kuliko rafiki.
2. Waarabu wa pemba hujuana kwa vilemba.
3. Usifungue duka ili kupenda kucheka.
4 Ukitaka kusaidiwa nawe, saidia mwenzako.
5. Palipo na moshi pana moto.
6. Kizuri kwako, kibaya kwa mwenzako.
7. Kaa na mwenye tabia njema, utashiriki ya heshima.
8. Baba na mtoto mwanaume, mama na mtoto mwanamke.
Kwa leo ni hizi ila nitaendelea kpekua nyingine  na kama nawe msomaji unazo mbili tatu  usisite kuendeleza orodha...WOTE MNAPENDWA!

Wednesday, June 15, 2016

NIMEOTA NDOTO NIPO LUNDO/NYASA NAKULA UGALI KWA SAMAKI NA KISAVU... MLO AUPENDAO KAPULYA...

Nilipoamka kumbe sio...maana hapa nilipo hata unga sina wa kusonga huo ugali sina. Nitabaki kula kwa macho tu......Ngoja nikatafute unga......

Tuesday, June 14, 2016

LEO TUPO KIJIJI FULANI MBAMBA BAY...

Nimeipenda taswira hii..inanikumbusha mbali sana. Hakika tumetoka mbali ...ngoja niache panapo majaliwa tutaonana tena. Kapulya.

Sunday, June 12, 2016

JUMAPILI YA LEO NIMEONA MUWE NAMI NA TUSALI SALA YA BABA YETU KWA LUGHA LUGHA YA KINGONI .....PIA KIWAHILI....

TUANZE NA KINGONI....KARIBUNI
"Hinu nyenye pemwisali, msala naha:-
CHINGONI
Dadi witu,
Witama kunani kulihundi,
Lihina laku lihyuwanike,
Ubambu waku utibwerele,
Chewifuna wenga vakiti vandu,
pamlima apa ngati chevikia kunani kulihundi,
Utiletele lelu chakulya chitu cha magono goha,
Utiwusile getihokili,
ngati tete tukuwawonela lipyana vevahoki kwa tete.
Ukotoka kutileka kulemala nichihaki,
nambu utiwusile vihaki.
(Ndava ubambu waveve na makakala na uvaha, magono gaha. Pepayi)
Mt. 6, 9-13.
......................................................................................
SALA KUU YA BABA YETU KWA KISWAHILI....KARIBUNI
Baba yetu uliye Mbinguni,
Jina lako litukuzwe,
Ufalme wako ufike,
Utakalo lifanyike , duniani kama Mbinguni.
Utupe leo mkate wetu wa kila siku,
Utusemehe makosa yetu, kama tunavyowasamehe na sisi waliotukosea.
Usitutie katika vishawishi, lakini utuokoe maovuni.(Kwa kuwa ufalme ni wako, na nguvu, na utukufu, hata milele. Amina
HII SALA IMEBEBA MAOMBI YOTE, LIKIWEMO LA KUSAMEHEWA DHAMBI NA KUOMBA RIZIKI.
UKISALI  HII , HUNA HAJA YA KUSALI VINGINE VYOVYOTE.
FANYA HIVYO KILA SIKU, KILA UPATAPO MUDA.
JUMAPILI NJEMA KWA WOTE AMANI NA BARAKA VITAWALE NDANI YA NYUMBA ZENU...  

Friday, June 10, 2016

TUANZE MWISHO WA WIKI NA MLO HUU WA NGUVU KANDE/MAKANDE..KARIBUNI....

Si mnajua mchoyo hana rafiki kwa hiyo karibuni tujumuike hapo ndo chakula huwa kitamu zaidi tukiwa wengi. NAWATAKIENI WOTE MWISHO MWEMA SANA WA WIKI. IJUMAA NJEMA!

Thursday, June 9, 2016

SKETI YA KITENGE:- HIZO NDIZO NGUO AZIPENDAZO KAPULYA ZA KUJIMWAGA.....!

Nguo za kujimwaga ni ngua nizipendazo mimi/kapulya  halafu hii sketi ni bomba sana ina mifuko pia. Kwa hiuyo hapa hakuna haja ya kuwa na pochi. Pia rangi zake ni maridadi kabisa....Vitenge tunavyo pia Kanga  za kuweza kushona, kuvaa na kupendaza sana...NIMEIPENDA MNO HII SKETI!

Tuesday, June 7, 2016

MAISHA:- WEWE NA MIMI MPAKA MUNGU ATAKAPOTUTENGANISHA....

Tulichokuwa nacho tutagawana mke wangu ...nimeipenda hii picha jinsi inavyoonyesha upendo wao. Hapo inavyoonekana wamekuwa pamoja tangu ujana mpaka hivi sasa. Sijui siku hizi .....ngoja niache na wengine mseme.

Monday, June 6, 2016

VITU AMBAVYO WATOO WA SIKU HIZI WANAVIKOSA AMBAVYO NI TOFAUTI NA EZI ZETU YAANI NI HIVI:-

Nimetumiwa hii na msomaji wa MAISHA NA MAFANIKIO nikaona niweke hapa ili na wenzangu mkumbuke na labda kuna la kuongezea...KARIBUNI

1. Unalia sababu umechapwa, utachapwa tena
2. Umechapwa hukulia utachapwa tena
3. Ukijililia tu bila kupigwa, utachapwa
4. Kusimama wakati wazee wameketi, utachapwa
5. Ukiketi wakati wazee wamesimama. utachapwa
6. Kujipitishapitisha mahali ambapo wazee wamekaa, utachapwa .
7. Kuwajibujibu watu wazima, utachapwa
8. Usipomjibu mtu mzima, utachapwa
9. Kujifanya sugu wakati unachapwa, utaendelea kuchapwa.
10. Ukitoka kuchapwa, ukaimba au kupiga mruzi, utachapwa tena.
11. Usiposalimia wageni, utachapwa
12. Ukila chakula cha wageni, utachapwa.
13. Kuwalilia wageni wanapoondoka, utachapwa.
14. Ukikataa kula, utachapwa.
15. Kuchelewa kurudi nyumbani baada ya jua kutua/kuzama, utachapwa
16. Kula nyumba ya jirani, utachapwa.
17. Kujitia kisirani, utachapwa.
18. Kujitia kujuwa juwa sana, utachapwa.
19. Ukipigana na mtoto mwenzio, akakupiga ukirudi nyumbani, utachapwa.
20. Ukikaa na kusikiliza wazee/wakubwa wanapoongea utachapwa
21. Ukiwa unakula chakula polepole, utachapwa.
22. Ukiwa unakula haraka haraka, utachapwa.
23. Ukiwa unakula sana, utachapwa.
24. Kuendelea kulala wakati wazee wamesha amka tayari, utachapwa.
25. Ukiwa unawaangalia wageni wakati wanakula, utachapwa.
26. Ukitembea na mtu mzima, ukajikwaa na ukaanguka, utachapwa.
27. Ukijamba mbele ya wakubwa, utachapwa.
28. Mtu mzima akijamba, ukamwangalia, utachapwa.
29. Ukila na wakubwa ukachukua nyama bila kupewa, utachapwa.
30. Ukinawa kabla ya wakubwa, utachapwa.
31. Ukimaliza kula ukanyanyuka kabla ya wakubwa, utachapwa.
32. Umechelewa kurudi dukani, utachapwa
33.uki...................................utachapwa tu .....................endelea na wewe mengine
PANAPO MAJALIWA TUTASEMA TENA...PAMOJA DAIMA KAPULYA!

Sunday, June 5, 2016

NAPENDA KUWATAKIENI WOTE JUMAPILI HII HII YA KWANZA YA MWEZI HUU SITA (6)

Napenda kuchukua nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutulinda wote tulioiona siku ya leo. Na pia naomba Mungu baba uyapokee maombi yangu kwa wagonjwa  na wenye shida nyingine ili wapate nafuu. Pia naomba sala zangu kwa marehemu wote zisikike kwako Baba. Amina.

Friday, June 3, 2016

LEO TUNAADHIMISHA KUMBUKUMBU YA KUZALIWA KWA KIJANA WETU ERIK KUTIMIZA MIAKA 16...HONGERA SANA KIJANA WETU.... !

  Kaka Erik Nyumbani Ruhuwiko-songea 2015
Ndugu wapendwa natumai Ijumaaa hii itakuwa njema.Mungu azidi kuwabariki/kutubarika  katika yote.Hapa kwetu Ijumaa hii ni njema kabisaa. Leo tunaungana na kijana wetu mpendwa kwa kumbukumbu yake ya siku ya kuzaliwa Siku kama ya leo Mungu alitubariki na kutujaalia mtoto wa kiume kaka Erik. Mungu anaendelea kumtunza vyema katika yote. Mungu yu mwema sana, sifa na utukufu viwe kwakwe. Tunamweka kijana huyu mikononi mwake Baba wa Mbinguni katika yote. Aendelee kuwa Baraka kwetu kama wazazi,walezi, Ndugu,Jammaa,Marafiki na Jamii yote. 
Ngoja tu tuweka na wimbo ambao kaka Erik alianza kusikiliza kwa kujifunza kiswahili ingawa nilipata swali moja kwa nini wanasema Kenya na sio Tanzania mama? na wimbo wenyewe ni huu JAMBO BWANA

HONGERA KWA SIKU YA KUZALIWA KAKA ERIK.

Wednesday, June 1, 2016

TUANZE MWEZI HUU MPYA/WA SITA KUTEMBELEA.....WANJAWA NDEGE WA SONGEA NI MIONGONI MWA VIWANJA BORA TANZANIA


SONGEA - DAR ES SALAAM
Uwanja wa ndege wa Ruhuwiko uliopo manispaa ya Songea mkoani Ruvuma ni rasilimali adimu inayoweza kusaidia kukuza uchumi wa mji wa Songea hasa kutokana na  uwanja huo kuwa ni miongoni mwa viwanja bora Tanzania. Uwanja wa ndege wa Songea ni miongoni mwa viwanja 13 bora vya ndege Tanzania kati ya viwanja karibu 50 vilivyopo nchini.Uwanja huo ambao ulijengwa kati ya mwaka 1974 hadi 1980 umewekewa lami hivyo kuwa na uwezo wa kutua ndege majira yote masika na kiangazi. Utafiti umebaini kuwa uchumi wa manispaa ya Songea umeongezeka ingawa sio kwa kiwango kikubwa baada ya kuanza safari za anga kutoka Songea hadi Dar es salaam ukilinganisha na hali ilivyokuwa kabla ya mwaka 2011 wakati mji wa Songea ukiwa hauna usafiri wa anga. Ofisa habari wa manispaa ya Songea Albano Midelo anasema Kabla ya kuanza safari za ndege
katika uwanja wa ndege wa Songea mwaka 2011,wafanyabiashara,Taasisi za kidini,
wawekezaji na wadau wengine walikuwa wanapata shida ya kusafiri kwa magari ambayo
yanachukua zaidi ya saa 15 kutoka Dar es salaam hadi Songea.
Midelo anasema safari za anga zimesaidia wadau mbalimbali kutumia usafiri wa ndege kutoka na
kwenda Dar es salaam hivyo  kuwezesha kufanya kazi zao kwa muda mfupi badala ya kupoteza saa
kadhaa barabarani hivyo kuzorotesha uchumi wa manispaa ya Songea na wa mtu mmoja mmoja.
“Licha ya kukuza uchumi,lakini usafiri wa anga katika manispaa ya Songea umerahisisha huduma za matibabu, mgonjwa anapozidiwa na kuhitaji rufaa kwa haraka anasafirishwa kwa njia ya anga kutoka Songea hadi Dar es salaam, hivyo usafiri wa anga umesaidia kuokoa maisha ya wakazi wa Songea na watanzania kwa ujumla wake’’alisema. Ongezeko kubwa la  wageni wanaosafiri kwa ndege katika mji wa Songea wanapolala katika nyumba za wageni na kukodi taksi kutoka uwanja wa ndege hadi mjini wanasaidia kuongeza pato katika Halmashauri ya manispaa ya Songea.
Hata hivyo changamoto kubwa ambayo inasababisha wakazi  wa Songea na wageni kutotumia usafiri wa ndege ni nauli kubwa ambayo inatozwa na kampuni binafsi ya ndege ya Auric Air ambayo ni kati ya shilingi 350,000 hadi 400,000 bei ambayo wengi wanashindwa kumudu kulipa.
Utafiti unaonesha kuwa nauli za ndege zikishuka watanzania wengi  wanaweza kusafiri kwa ndege kutoka Dar es salaam hadi Songea hivyo Songea itapata wageni wengi ambao watapata huduma mbalimbali za usafiri,chakula,malazi na kutembelea vivutio vya utalii hivyo kukuza pato la serikali na mwananchi mmoja mmoja. Meneja uwanja wa ndege wa Songea Valentine Fasha
Meneja wa uwanja wa ndege wa Songea Valentine Fasha  amesema licha ya changamoto ya nauli inayotozwa na kampuni binafsi ya ndege ya Auric air bado kuna idadi kubwa ya abiria ambao wameamua kusafiri kwa ndege toka Songea hadi Dar es salaam.“Abiria ambao wanatumia ndege kutoka Songea hadi Dar es salaam wanaendelea kuongezeka kwa mfano kwa mwaka 2015 pekee abiria  karibu 5000 walisafiri kwa ndege idadi ambayo inaridhisha kwa kuwa kabla ya usafiri wa anga idadi ya wageni waliokuwa wanafika Songea pia ilikuwa chini’’ ,alisisitiza.
Alisema ndege zilizokuwa zinatua kwenye uwanja huo kabla ya mwaka 2011 zilikuwa zinakodiwa kwa gharama kubwa ambapo kuanzia Oktoba 17,2011 kwa mara ya kwanza ndege ya abiria ya Auric ilianza kutoa huduma kwenye uwanja huo kuja Songea na kurudi Dar es salaam.Hata hivyo amesema serikali itakaponunua ndege ya serikali nauli ya ndege inaweza kupungua na kwamba lengo la mamlaka ya ndege Tanzania ni kuhakikisha kuwa kila mtanzania aweze kusafiri kwa ndege kwa kuwa usafiri  wa ndege ndiyo  wa haraka,salama na uhakika zaidi.
Fasha amebainisha kuwa ndege ya Auric inatoa huduma za usafiri siku tano kwa wiki ambazo ni Jumamatu, Jumanne, Jumatano, Alhamis na Jumamosi, ndege hiyo ina uwezo wa kubeba abiria 13, inatumia saa 2.15 kutoka Songea hadi Dar es salaam.Hata hivyo amesema ndege kubwa yenye uwezo wa kubeba abiria kuanzia 50 inatumia takriban saa moja tu
kutoka Songea hadi Dar es salaam na kwamba nauli kwa ndege kubwa pia inapungua ukilinganisha na ndege ndogo.
Kulingana na meneja wa uwanja huo,Mamlaka ya viwanja vya ndege Tanzania ina mpango wa kupanua uwanja wa ndege wa Songea ambapo serikali imefanya upembuzi yakinifu katika viwanja 11 Tanzania ukiwemo uwanja wa ndege wa Songea ambavyo vinatakiwa kuboreshwa ili viweze kutoa huduma bora na za kisasa na kusababisha ndege kushawishika kutoa huduma Songea.
Fasha amesisitiza kuwa uwanja wa ndege wa Songea unatarajiwa kupanuliwa na kupewa vifaa vya kisasa ili uwe  uwanja wa kisasa zaidi pia ni matarajio ya serikali kuleta ndege ya serikali ambayo inaweza kuboresha huduma za usafiri wa ndege katika safari ya Dar es salaam-Iringa hadi Songe
“Route zote za ndege katika Tanzania zina huduma za ndege isipokuwa hakuna route ya Dar es salaam, Iringa na Songea,Rais wetu Magufuli amepania kulisimamia shirika la Ndege hivyo naamini atahakikisha route yetu inafanikiwa,lengo ni kila mtanzania aweze kupanda ndege,aone dunia inavyoonekana akiwa angani,aweze kusafiri kwa haraka kwa gharama nafuu’’,alisisitiza.Amesema shirika la ndege la Tanzania likifufuliwa na kusimama utakuwa ni ukombozi kwa watanzania wote kwa kuwa sasa ndege zitaruka na kutua katika kanda zote ikiwemo ya Dar es salaam,Iringa hadi Songea  hivyo kufuta tabaka kwamba kila mmoja ataweza kupanda ndege kutokana na gharama kuwa chini.Katika bajeti ya mwaka 2016/2017, Waziri wa ujenzi,uchukuzi na mawasiliano Profesa Makame Mbarawa amesema shirika la ndege Tanzania (ATCL)limetengewa shilingi bilioni 500 kwa ajili ya kununua ndege tatu mpya.Hata hivyo Profesa Mbarawa alisema idadi ya ndege zitakazonunuliwa na bei ya kila moja itajulikana baada uya uchambuzi kukamilika. Alisema mamlaka ya viwanja vya ndege Tanzania katika bajeti ya mwaka 2016/2017 imetengewa shilingi bilioni 200 kwa ajili ya kutekeleza miradi yake ikiwemo ukarabati wa viwanja vya ndege ,usimikaji wa taa,mitambo ya kuongozea ndege na kuendeleza upanuzi
wa viwanja vya ndege.
Mwisho
CHANZO:-Stephano Mango