Friday, February 28, 2014

MWEZI WA PILI/FEBRUARI NDO UNAISHA LEO NAMI NIMEONA TUMALIZE KWA NYIMBO HIZI TATU...KUHUSU WAIMBAJI NA MIJI WALIYOZALIWA...KAPULYA NAYE ANATAKA KUIIMBA SONGEA:-)



Na hapa je?


Au labda hapa

Je? wimbo upi wewe umeufia zaidi...Mimi bwana  ningekuwa na sauti kama zao ningetunga nami Songea All Stars...Songea ...Songea ...tunayo furaha kuwa wazaa wa Songea...Mhhhh ngoja niwasake waimbaji wote kutoka Songea tuanze hili zoezi. Hivi wapo kweli?
NAWATAKIENI WOTE MWISHO HUU WA MWEZI UWE MWEMA ...TUONANE TENA PANAPO MAJALIWA MWEZI UJAO!!!!

Thursday, February 27, 2014

MAISHA NA MAFANIKIO LEO NA UJUMBE UFUATAO:-......!!!

Ishi maisha rahisi,  Onyesha mapendo/upendo kwa ukarimu wa kweli,  Onyesha upendo kwa undani na kujali, Ongea kwa huruma,  Mengine yote mwachie Mungu.
KWA UJUMBE HUU NAPENDA KUWATAKIENI WOTE SIKU NJEMA SANA!

Wednesday, February 26, 2014

LEO TUENDELEE UTAMADUNI HUU WA NYWELE..MTINDO WA NYWELE!!!!

Nimekumbuka leo mtindo huu wa nywele nadhani pia hakuna mdada/mwanamke asiyekumbuka mtindo huu wa nywele. Binafsi nakumbuka zaidi nilipokuwa shule ya msingi , ni mtindo huu tu ulikuwa unasukwa kwa wasichana kama hutaki basi kata nywele...Basi kila jumapili na jumatano ni kusuka ili nywele ziwe safi maana usiposuka mkasi unapita kichwani au wembe pia, kama vile msalaba. Nashukuru nilikuwa sina shida ya msusi, msusi wangu alikuwa mama  kama alikuwa amesafiri basi majirani walinisuka....Je? nawe ulikuwa unasuka msuko huu? na,  je? uliuitaje msuko huu? Mimi na rafiki zangu  tuliuita mtindo/msuko huu TWENDE KILIONI. SWALI JINGINE:- JE? ni kwa nini mtindo huu unaitwa Twende kilioni?.....

Tuesday, February 25, 2014

VAZI LA KANGA NI MUHIMU KWETU TUSISAHAU VAZI HILI NA TULIKOTOKA: KANGA!!

 Kanga ya kwanza imetegenezwa mwaka 1870 na mwanamke kutoka kisiwa cha Zanzibar.

Kanga ni kitambaa chenye umbo la mstatili na rangi mbalimbali. Kipimo chake cha upana ni 44 inchi hivi na kipimo chake cha urefu ni inchi 60 hivi.
Kwa watu wa Afrika ya Mashariki, hasa wanawake, kanga ni  nguo muhimu sana. Mara kwa mara, wanawake wanavaa kanga wakati wa kupika, kusafisha nyumba, kuteka maji, na kadhalika.
Tena, kanga zinavaliwa na wanawake kwenye arusi, kwenye msiba, nk. Kanga si nguo tu. Matumizi ya kanga ni mengi. 
Kama kanga hii isemavyo TUSISAHAU KWETU...!!

Sunday, February 23, 2014

BLOG YA MAISHA NA MAFANIKIO YATIMIZA MIAKA SITA LEO!!!

Hapa ni mwenyewe dada/mama Maisha na Mafanikio Leo!!!

Mmmmhh! Miaka sita leo imefika kama mchezo!!!!
Blog ya Maisha na Mafanikio kama mchezo leo yatimiza miaka sita (6) kamili. Napenda kuchukua nafasi hii na kusema:- Hii yote ni kutokana na uwepo wenu ulioambatana na upendo pia ushirikiano mzuri mlio nao. Na kubwa zaidi ni kwa familia yangu kwa kuwa bega kwa bega nami. Pia napenda kusema kwa kupitia michango ya wasomaji na wanablog wenzangu nimeweza kijifunza mambo mengi sana. Na ndiyo kwa sababa hii napenda kusema:- AHSANTENI SANA KWA USHIRIKIANO WENU NASEMA TENA KWANI NAAMINI BILA NINYI, NISINGEFIKA HAPA NILIPO LEO. KWA KWELI NAAMINI KUWA SISI SOTE NI NDUGU NA NI WATOTO WA BABA MMOJA. UPENDO NA UMOJA WETU UDUMU DAIMA NA PIA MILELE!!!!!......Halafu la kufurahisha siku niliyoanza kublog ilikuwa ni JUMAMOSI na leo ni JUMAPILI.... HAYA JUMAPILI IWE NJEMA SANA KWA WOTE MTAKAOPITA HAPA NA WENGINE WOTE.

Friday, February 21, 2014

HONGERA KWA SIKU YA KUZALIWA BINTI YETU CAMILLA:- MIAKA 16 LEO!!!

 Mwaka 1998 tarehe 21/2 alizaliwa binti huyu. Ni siku ambayo familia hii haitaweza kusahau. Twamshukuru Mwenyezi Mungu kwa yote. Na twazidi kumwomba amwongoze binti Camilla katika kila akifanyacho ili kiwe vema. Pia twamshukuru Mungu kwa kutuongoza sisi wazazi/walezi katika malezi ya binti Camilla.
Katika maisha ukiwa na marafiki  basi nao hawakosi kuwa nawe katika kila litokealo. Asubuhi hii marafiki wawili kabala ya kwenda shule nao walijumuika na Camilla kwa siku hii. Walikuaja kumpongeza na kula chakula cha asubuhi pamoja. Hivi ndivyo siku ya dada Camilla ilivyoanza .....
....kaenda shule sasa...TWAMTAKIA SIKU YAKE IWE NJEMA SANA. HONGERA Binti, dada, rafiki, mjukuu nk.

Thursday, February 20, 2014

PICHA YA WIKI...UBUNIFU MWINGINE BWANA!!!

Ndiyo ni ubunifu mzuri....ila binafsi ningetumia mkaa au kuni maana hapa...itakuwaje. Swali linakuja je? kama hakuna umeme utafanyaje?... Na je? kutaliwa nyama tu?..:-) SIKU IWE NJEMA SANA KWA WOTE NA IKIWEZEKANA JARIBU UBUNIFU HUU ILA USIMWACHE MTOTO AJARIBU:-)

Tuesday, February 18, 2014

HAPA NI MOJA YA VYAKULA BORA KATIKA MIILI YETU PAPAI...NIMETAMANI KWELI LEO!!



TUNAAMBIWA kuwa kuishi vizuri ni pamoja na kula chakula bora na sahihi. Pia, mtu anayeishi vizuri ni yule ambaye hasumbuliwi na maradhi hatari na njia pekee ya kuulinda mwili dhidi ya maradhi hatari ni kujua ipasavyo na kuvitumia vyakula bora pamoja na kufanya mazoezi. Ila duh hapa nilipo vipapai vyenyewe kama ngumu yangu...wakati wengine wanalisha nguruwe haya mapapai pia maembe....na papai ni moja kati ya hivyo vyakula...TUSISAHAU KULA PALE TUKUMBUKAPO:-)

Monday, February 17, 2014

JUMATATU HII NIMEONA TURUDI NYUMA MPAKA MIAKA ILE TULIYOSOMA SHULE YA MSINGI "DARASA LA NNE" NA HADITHI HII YA SADIKI NA SIKIRI!!!

Sadiki ni mtoto anayeishi karibu na Ujiji. Anaye ndugu yake aitwaye Sikiri. Sadiki na Sikiri husoma katika shule ya Businde. Sadiki anafanya kazi zote kwa bidii. Lakini Sikiri ni mtoto mbaya kwa sababu ni mvivu, kaidi, tena hana adabu.
Siku moja wakati wa livu baba yao aliwaamsha mapema sana. Akasema, "Sadiki, chuukua hii shilingi. Nenda sokoni ukanunue samaki. Na wewe Sikiri, nenda kisimani ukateke maji." Wote wawili wakaenda. Sadiki alinunua samaki, akarudi nyumbani haraka. Lakini Sikiri alichelewa. Baba yake akamngoja mpaka akachoka.
Baba akatoka kwa hasira kumfuata Sikiri kule kisimani. Alipofika alimkuta anachezea maji. Anayateka na kuyamwaga juu ya jiwe. Baba yake akamwuliza, "Unafanya nini Sikiri? Mbona unacheza tu? Teka maji, twende nyumbani." Sikiri akateka maji, wakarudi nyumbani.
Walipofika nyumbani walimkuta mama amekwisha tayarisha uji. Wakanywa. Walipomaliza, baba yao akawaambia, "Twendeni tukapalilie bustani ya mboga. Mama atabaki hapa nyumbani. Atalisha kuku na kusafisha nyumba. Baadaye atatayarisha chakula."
Kule katika bustani kulipandwa mchicha, maharagwe, vitunguu na nyanya. Magugu na manyasi yaliota kwa wingi. Sadiki, Sikiri na baba yao walipalilia kwa uangalifu ili wasiharibu mimea ya mazao.
Sikiri hakupenda kazi. Kwa hiyo alitoroka akaenda kichakani. Kule kichakani alitafuta matunda mwitu. Sikiri alikuwa mtoto mvivu kweli. Hakutaka kufanya kazi kwa bidii. Sadiki na baba yake waliporudi nyumbani, akawafuata.
Walipofika nyumbani chakula kilikuwa tayari. Sikiri alikuwa wa kwanza kunawa mikono na kuanza kula. Siku ile mama alipika ugali na samaki alionunua Sadiki. Walipokwisha kula, baba alimwita Sikiri akamwuliza, "kwa nini leo alitoroka?" Sikiri alinyamaza tu. Sakiri alikuwa mtoto mkaidi. Baba akamwambia, "Kesho utakwenda kupalilia bustani. Usipokwenda hutapata chakula."
Siku iliyofuata Sikiri alikataa kwenda bustanini, alitoroka. Sadiki na baba yake walikwenda kupalilia peke yao. Jioni waliporudi, baba alimwuliza mama, "Sikiri amekwenda wapi?" Mama akajibu, "Mimi leo sijamwona nyumbani. Sijui amekwenda wapi." Kumbe, siku ile asubuhi Sikiri alipanda basi kwenda mjini Kigoma. Huko njiani aliulizawa nauli. Sikiri hakuwa na pesa hata kidogo. Dereva akamtelemsha pale pale. Akaachwa peke yake. Sikiri alilia sana . Mwisho akaanza kusema kwa uchungu:-
Sikiri mimi maskini,
Uvivu wangu nyumbani,
Ukiwa huu njiani,
Nakufa hapa kwa nini?

Sadiki sasa ashiba,
Chakula kingi kwa baba,
Nirudi tena kwa baba,
Nakufa hapa kwa nini?
Sikiri alirudi nyumbani. Alikuwa amechoka sana. Alipofika nyumbani aliomba radhi. akamwambia baba na mama.
Naomba radhi nimekosa,
Nitakuwa mtoto mwema sasa,
Shambani tena sitakosa,
Baba na mama nisameheni.

Nitalima kama Sadiki,
Nitalima wala sichoki,
Na nyumbani tena sitoki
Baba na mama nisameheni.
Baba hakumpiga Sikiri. Alimsamehe. Sikiri akabadili tabia yake, akawa anawasaidia wazee wake. Kila alipotumwa alikwenda upesi. Mama yake alifurahi, akamwambia, "Siku hizi wewe ni mtoto mwema kama Sadiki. Mtoto mtii hupendwa na wazazi wake. Tena hupendwa na watu wote kijijini. Endelea kuwa mtoto mwema na mtii.......MWISHO......
HADITHI HII KILA NINAPOISOMA INANIKUMBUSHA SANA NA ILE HADITHI YA MWANA MPOTEVU EBU MSIKILIZA HAPA WIMBO HUU WA EMACHICHI

NAWATAKIENI JUMATATU NJENA NA KILA LA KHERI KWA KILA MTAKACHOFANYA!!! UJUMBE WA LEO YULE AWEKAYE AKIBA BASI HUFAIDI...maana yake ukitunza ulichonacho kitawafaa wengi..Elimu ni kugawana.

Sunday, February 16, 2014

HILI NI CHAGUA LA MAOMBI/SALA YA JUMAPILI YA LEO NA MAISHA NA MAIFANIKIO KWA WATU WOTE!!!

Eh, Mungu uliye Mtakatifu, sisi ni watenda dhambi, hatuwezi kujiokoa twakuomba Bwana Yesu uingie katika mioyo yetu na utusamehe dhambi zetu. Amina.

Naona si mbaya kama tukimalizia na kumsikiliza dada Rose Muhando na wimbo huu UNASHANGAZA

JUMAPILI IWE NJEMA KWENU NA AMANI PIA UPENDO VITAWALE DAIMA.

Friday, February 14, 2014

IJUMAA YA LEO NI IJUMAA/SIKU YA WAPENDANAO NA MAISHA NA MAFANIKIO INA UJUMBE HUU KATIKA SIKU HII KWA WATU WOTE KWA SIKU HII!!!

Katika maisha furaha kubwa ni kupenda na kupendwa
Basi kwa ujumbe huu usipoteze furaha uliyo nayo. NAWATAKIENI IJUMAA /MWISHO WA JUMA HII UISHE VIZURI!!!

Wednesday, February 12, 2014

MAISHA NA MAFANIKIO ILIVYOWAANDALIA JIKONI JANA JIONI: SUPU YA VIAZI!!!!

 Hapa ni maandalizi yz upikaji wa supu ya viazi, ambayo Kapulya mwenyewe kaivumbua. Na katika supu hii kuna:- Viazi 8, kitunguu 1, vipande viwili vya kitunguu saumu, tangawizi kiasi utakacho mimi natumia kama cm 2 hivi, pilipi kidogo hasa kama hupendi ukali sana na kama una watoto wadodo, Chumvi kijiko kimoja cha sukari (msk), binzari kijiko kimoja cha sukari (msk), mafuta vijiko viwili vya mezani, Paketi moja ya nyanya au nyanya freshi 3, maji lita moja na bila kusahau sufuria kubwa na mwiko wa kukorogea.
Ni  hivi: Menya viazi, kisha menya kitunguu na kitunguu saumu...Katakata viazi vipande vidogovidogo, na halafu vichemshe kwa dakika 5, weka pembeni. Katakata kitunguu, unaweza kutakata kitunguu saumu na tangawizi pia vipande vidogovidogo sana lakini safi zaidi kama una kakinu basi ponda ponda pamoja na pilipili pia chumvi kidogo kwa kurahisisha. Weka sufuria katika jiko na moto mkali kidogo na weka mafuta. Kaanga vitunguu, kitunguu saumu, tangawizi na pilipili mpaka vinakuwa laini ila visiungue. Weka binzari pia nyanya,  kama unatumia pakati weka nusu, ache vitokote dakika kama 5 hivi. Baada ya hapo chukua viazi na uchanganye kwenye chachandu na yale maji ulochemshia  na acha vichemke tena dakika 5 zaidi ila kwa moto kidogo sana. Na mwisho wake chakula tayari imechukua dakika 15 kupika na maandalizi kama nusu saa.

Na hapa unaona matokeo yake ...Ni Supu tamu na kama una haraka ni chapuchapu na ninauhakika watoto wako watapenda pia kwani wangu wanapenda sana. Kama katika picha unaweza kula kama ilivyo au na kipande cha mkate kama nilivyofanya mimi jana na pia ni kama mpenzi wa mikate. Kinywaji hapa ni maji ...ila ni chagua la mtu. Nakutakia MAJARIBIO MEMA..KWANI NAJUA kuna wadada na wakaka watajaribu tu:-) KILA LA KHERI NA NAJUA MTAIPENDA HII SUPU.

Tuesday, February 11, 2014

MKE ANAPOMJALI NA KUMKUBALI MUME HUMUONGEZEA KUJIAMINI…

Mke anapomjali na kumkubali mume humuongezea kujiamini…
Mahusiano kati ya mume na mke nyumbani huweza kumfanya mume afanikiwe kwenye shughuli zake au aanguke. Kwa nini? Ni kwamba, mtu ambaye anakataliwa na mtu au watu wanaomhusu huwa anakosa kujiamini, huwa anafikia mahali ambapo hujichukia hata yeye mwenyewe.
Mke anapomkosoa mume, anapomlalamikia kila mara na kuwa na ghubu, bila kujali kama mume huyo amekosa au hapana, mume hufikia mahali huanza kujitilia mashaka kama kweli ana uwezo wa kufanya mambo, kama kweli ana thamani anayodhani kuwa anayo. Kujiuliza huku mara nyingi kuna maana ya mwanaume kuanza kupoteza kujiamini na hata kuanza kuwa na uhusiano mbaya na watu anaohusiana nao mahali pengine kama kazini. Unaweza kumgundua mtu ambaye ana mke mlalamikaji, mkosoaji na mwenye ghubu kwa kuangalia jinsi anavyojitathmini. Kama mke ni mkosoaji na mwenye ghubu kwa mumewe ni lazima mume atakosa kujiamini katika kufanya mambo yake mengi, ni lazima ataanza kuwa na uhusiano mmbaya na watu wengine kutokana na hukohuko kutojiamini kwake ambako kumesababishwa na ghubu na kukosoa kwengi kwa mkewe. Mwanaume ambaye ana mke mkosoaji na mwenye ghubu hutokea kutowapenda watu wengine na kukosoa wengine inatokea kuwa sehemu muhimu kwa maisha yake, anatokea kuwa na hasira za karibukaribu na ni vigumu sana kwa mtu wa aina hii kuelewana na watu.
Baadhi ya makampuni huko Marekani, kabla hayajampandisha mtumishi wake cheo, humchunguza mke wa mtumishi. Hawachunguzi kama ni mzuri wa sura au kama anajua mapenzi au kupika vizuri. Mara zote huchunguza kama mwanamke huwa anampa mumewe moyo, kama hamkosoi na kumlalamikia na kama hana ghubu. Wanapogundua kwamba mke wa mtumishi siyo mkosoaji
wala mwenye kulalamika-lalamika humpa cheo mtumshi kwa imani kwamba atakuwa ni mtu mwenye kujiamini. Lakini wanapogundua kwamba mke ni mwenye kukosoa, mwenye ghubu na
mlalamikaji, kamwe hawampi mtumishi cheo, kwa sababu wanaamini kwamba, mtumishi huyo hawezi kuwa makini, atakuwa hajiamini.
.......................................................................................................................................................
Swali langu hapa je hii ni pale tu mwanamke anapomjali mume na ndio iwe hivi? Je? mwanamke astahili kujaliwa na kukubaliwa ili kuongeza kujiamini?..au ndo kusema mwanamke anajiamini sana kuliko mwanamume?..swali kutoka kwa KAPULYA...
Habari/mada hii nimetumiwa na mkereketwa/msomaji wa Maisha na Mafanikio kwa kutaka tu mimi nisome lakini mimi nimeona ina mafundisho ndani yake nikaona ni bora niiweke hapa ili wengine wafaidike na ELIMU hii.

Sunday, February 9, 2014

MAOMBI YA JUMAPILI YA LEO NI KAMA IFUATAVYO:- SHUKRANI!!

Mungu wetu tunakushukuru kwamba unatupenda. Yesu Kristo ingia ndani ya mioyo yetu na uchukue dhambi zetu, huzuni, maumivu na hali yetu ya kutamamauka. Tupe tumaini, twaomba tupe maisha mapya. Ahsante sana Bwana tumeamini mioyoni kila mmoja anayekuja kwako ataokoka na kuanza maisha yake upya. Twasema AHSANTE kutukubali leo . Tupe moyo mpya na maisha mapya Bwana katika jina la Yesu Kristo.
AMINA.

Friday, February 7, 2014

UJUMBE WA IJUMAA YA LEO KUTOKA KWA KIBARAZA CHA MAISHA NA MAFANIKIO NI KAMA UFUATAVYO!!!!

Bila ubishi wala maswali mengi katika maisha ya Taifa letu tunategemea sana  uwepo wa wanawake.
NAWATAKIENI WOTE MWANZA MWEMA WA JUMA HILI MAANA LEO NI IJUMAA WENGI WANAANZA MAPUMZIKO  BAADA YA KAZI YA JUMA NZIMA.


Thursday, February 6, 2014

HII KWA KWELI ITAKUWA PICHA YA WIKI...UGALI KWA NYAMA PANYA !!!MMMMHHH KAZI IPO!!!

Ni muda mrefu nimekuwa nikisikia ya kwamba nyama ya panya na nyoka ni tamu kama ya kuku. Na pia nimesikia katika habari ya kwamba baaada ya miaka wadudu wote watakuwa kitowoe kizuri sana kwa binaadamu. Swali moja kutoka kwa kijana wangu linaulizwa hivi:- Iweje tule panya wakati anatuletea magonjwa? Na je nyoka si adui yetu na pia ana sumu?

Wednesday, February 5, 2014

INAHUZUNISHA LAKINI KUNA FUNDISHO KUU KWA WOTE!!

Katika mizunguko yako nimekutana na habari hii ambayo ni kusikitisha lakini pia ni kumpa mtu mafunzo mazuri sana. Ungana nami ….

---------------------------------------------------------------------------------------



Ndugu zangu wapendwa!
Inahuzunisha lakini kuna fundisho kuu kwetu sote. “Nilipofika nyumbani usiku ule, mke wangu aliponitayarishia chakula, nilimshika mkono na kumwambia, kuna kitu nataka nikwambie. Mke wangu alikaa chini na kula chakula kimya akiwa tayari kunisikiliza. Tena nikagundua macho yake yalionyesha ana umizwa. Nilishindwa hata namna ya kuanza kufumbua kinywa changu. Lakini ilibidi nimwambie ili ajue nilikuwa nikifikiri nini juu yake. Nataka kukupa talaka. Nilianza kusema kwa utulivu. Alionekana kutokereka na maneno yangu badala yake aliniuliza kwa sauté ya upole ‘kwa nini?’ Sikumjibu Sali lake. Kutojibu kulimfanya akasirike. Akatupa kijiko na akanikaripia, ‘wewe si mwanamume!’ Usiku ule, hakukuwa na maongezi kati yetu. Alikuwa akilia kwa kwikwi. Nilifahamu kwamba alitaka kujua ni nini kimetokea kwenye ndoa yetu?. Lakini kwa hakika nisingeweza kumpa Jibu wala sababu ya kuridhisha; alionekana si mali, kitu kwangu penzi langu lilihamia kwa Mary. Sikumpenda tena mke wangu mawazo yote yalikuwa kwaMary. Kwa kweli nilimdharau mke wangu! Huku moyo wangu ukijua wazi kwamba nafanya kosa, niliandika talaka ambayo ilionyesha kwamba yeye (mke wangu) angepata nyumba yetu, gari na atakuwa na hisa 30% ya kampuni yetu. Aliangalia talaka ile na kuichana vipande vipande. Mke ambaye tumeishi nami kwa miaka 10 alionekana mgeni machoni mwangu. Nilimuonea huruma kwa muda, rasilimali na nguvu alizopoteza lakini sikuweza kurudi nyuma kwa sababu Mary aliuteka moyo wangu kisawasawa. Hatimaye mke wangu alilia kwa sauti mbele yangu, jambo ambalo kwa hakika nilitarajia. Kwangu mimi kilio chake kilinipa nafuu. Wazo la kuachana na mke wangu limenisumbua kwa majuma kadhaa na sasa limeendelea kuimarika nakuwa jambo la hakika zaidi. Siku iliyofuata nilikuja nyumbani kwa kuchelewa sana nikakuta mke wangu akiandika jambo mezani. Sikutamani hata kula chakula alichonipikia nilikwenda moja kwa moja chumbani na usingizi ulinichukua mara moja kwa sababu nilikuwa nimechoka baada ya kula raha za kufa mtu na Mary. Usiku nilishtuka usingizini mke wangu alikuwa bado akiandika. Sikujali Kabila nikajifunika vyema shuka na kulala tena. Asubuhi yake alinikabidhi masharti ya talaka yake: hakutaka kitu chochote kutoka kwangu lakini alihitaji apate angalau mwezi mmoja wa kujiandaa
kabla hajaachika. Akaomba kwamba katika kipindi hicho cha mwezi mmoja sote mimi na yeye tujitahidi kuishi maisha ya upendo au kawaida kwa kadiri itakavyowezekana. Sababu yake ilikuwa ndogo lakini muhimu: mwanetu wa kiume alikuwa akikaribia kufanya mtihani katika mwezi uliofuata kwa hiyo hakupenda mtoto aathirike kisaikolojia kwa sababu ya kuachana kwetu. Hili halikuwatatizo kwangu,nilikubali mango wake. Lakini alikuwa na sharti la ziada, aliniomba nikumbuke jinsi nilivyombeba siku za fungate yetu hasa siku ya harusi yetu. Akaniomba na kunisihi kwamba katika kipindi hicho cha mwezi mmoja niwe nambeba kutoka kitandani kwetu mpaka mlango wa kutokea kila asubuhi. Nilidhani anakaribia kuwa kichaa. Ili kufanya siku zetu za mwisho zisiwe na migogoro nilikubaliana na masharti yake ya ajabu. Nilimsimulia Mary kuhusu masharti ya kuachana na mke wangu. Mary alicheka sana, aliona ni ujinga. ‘Hata akitumia ujanja wa namna gani talaka ni lazima’, alisema Mary tena kwa dharau. Mimi na mke wangu hatukuwahi kugusana tangu nilipomweleza dhamira ya kumtaliki. Kwa hiyo nilipombeba kwa mara ya kwanza sote tulinuniana. Mwanetu alifurahi sana nakupiga makofi nyuma yetu, ‘aah baba kambeba mama mikononi mwake’. Maneno yake yalinichoma moyoni moja kwa moja. Kutoka chumbani kwetu hadi sebuleni, halafu tena mpaka mlangoni, ni zaidi ya mita kumi nimembeba mke wangu. Alifumba macho na kusema kwa sauti laini na ya upole; usimwambie mwanetu juu ya talaka. Nilikubali kwa kichwa, ingawa nilijisikia vibaya. Nilimuweka chini nje ya nyumba. Alienda kituoni kusubiri basi la kazini kwake nami nikaendesha gari kwenda ofisini kwangu. Siku ya pili, zoezi lilikuwa rahisi kwetu sote. Aliegemea kifuani pangu. Nilisikia harufu nzuri ya utur aliofukiza kwenye blauzi yake. Nikagundua kwamba sijamuangalia kwa makini mkewangu kwa kipindi kirefu sana. Nikagundua hakuwa binti tena. Kulikuwa na mikunjo usoni na nywele zake zilianza kuwa nyeupe!Ndoa yetu imekula urembo wake. Kwa dakika moja nikafikiri kwa nini namfanyia hivi. Siku ya nne nilipombeba hisia za mapenzi kati yetu zilirejea. Huyu ni mwanamke aliyejitoa kuishi nami na tumeishi kwa miaka kumi sasa. Siku ya tano na ya sita ilikuwa wazi kwamba mapenzi yetu yalikuwa yakimea upya. Sikumwambia Mary kuhusu jambo hili. Kadiri mwezi ulivyokaribia kwisha niliona raha kumbeba mke wangu na zoezi likawa rahisi zaidi. Pengine kufanya kazi hii kila siku kuliniimarisha zaidi. Alikuwa akichagua nini cha kuvaa asubuhi. Alichagua mavazi kadhaa hakupata linalomfaa. Kisha akaguna, ‘nguo zangu zote zimekuwa kubwa’. Nikagundua kwamba mke wangu amepungua sana, nadhani ndiyo maana niliweza kumbeba kirahisi. Ghafla jambo likanichoma... Mke wangu ana uchungu na maumivu makuu moyoni mwake. Bila kujitambua nikamgusa kichwa chake. Mara mtoto wetu akatokeza na kusema ‘baba ni wakati wa kumbeba mama muende kazini’. Kwake kumuona baba akimbeba mama likawa ni jambo la furaha sana. Mkewangu alimuonyesha ishara mwanetu asogee karibu na akamkumbatia kwa upendo mkuu. Niligeuza uso wangu nisije nikabadili mawazo katika dakika ya mwisho. Kisha nikambeba mikononi mwangu kutoka chumbani, sebuleni halafu mpaka mlangoni. Mkono Wake laini ulikuwa umeizunguka shingo yangu kwa upendo. Nilimkumbatia Mwili wake; ilikuwa ni mithili ya siku ya ndoa yetu. Lakini wepesi wake ulinitia mashaka. Siku ya mwisho nilipombeba nilipata shida hata kupiga hatua moja. Mtoto wetu alishakwenda shuleni. Nilimshika kwa karibu nakumwambia sikubaini kwamba maisha yetu yalikosa upendo. Nikaenda zangu ofisini…. Nikashuka garini hata bila kufunga mlango. Maana nilihisi nikichelewa tu ninaweza kubadili nilichoamua....nikapanda ngazi. Mary alifungua mango nikamwambia, ‘Samahani, Mary, sihitaji tena kumtaliki mke wangu’.Akaniangalia kwa kustaajabu, halafu akagusa kichwa changu. Akaniuliza‘Unaumwa?’ Nikaondoa mkono wake kichwani kwangu. ‘Samahani, kumtaliki mke wangu. Nadhani ndoa yangu haikuwa na furaha kwa sababu sikuthamini undani wa maisha yetu, mimi na mke wangu, si kwamba hatupendani. Nimetambua hilo tangu nilipombeba siku ya ndoa yetu nilitakiwa kumbeba siku zote za maisha yetu, nampenda mke wangu
sitamuacha mpaka kifo kitakapotutenganisha.’Ikawa kama Mary alizinduka usingizini. Akanizaba kibao cha nguvu, akajiegemeza mlangoni na kuanza kulia. Nikashuka ngazi na kuondoka zangu. Nikaingia kwenye duka la maua nikaagiza maua mengi mazuri kwa ajili ya mkewangu. Muuzaji akaniuliza aandike nini kwenye kadi. Nikatabasamu nakuandika “Nitakubeba kila asubuhi mke wangu mpaka kilo kitakapotutenganisha”. Jioni ile nilifika nyumbani na maua mikononi mwangu, tabasamu Kuba usoni nikakimbia mpaka chumbani, nikapokelewa na maiti ya mke wangu kitandani. Kumbe mke wangu alikuwa akisumbuliwa na saratani kwa miezi kadhaa nami nilishindwa kubaini kwa sababu nilihamishia akili yangu kwa Mary. Alijua kwamba angekufa karibuni na alitaka asiniingize katika chuki na mwanetu kama ningelazimisha talaka mapema. Angalau machoni mwa mwanangu naonekana ni mume mwema….Jamani vitu vidogo vidogo vizuri ni vya msingi sana katika mahusiano yetu... Siyo majumba au magari au fedha zilizoko kwenye benki. Hivi vitakupa tu mazingira ya kufurahi lakini vyenyewe siyo furaha. Kwa hiyo jitahidi kuwa na muda mzuri na mazingira rafiki ya kuwa na mwenzi wako, kuwa rafiki wa mwenzi wako. Fanya vitu mlivyofanya wakati wa uchumba na wa ndoa yenu ambavyo vitawaweka karibu siku zote. Muwe na ndoa yenye furaha. Mara nyingi watu hushindwa katika ndoa kwa kutotambua ni kwa kiasi gani walikuwa karibu wakati wa kujenga uhusiano wao Mungu awabariki na awe nanyi nyote mliosoma nakujifunza hapa
NAWATAKIENI JUMATANO NJEMA SANA…

Tuesday, February 4, 2014

USIJE UKADHANI NI MJI KASORO BAHARI:- NI MOROGORO YETU YA SONGEA/PERAMIHO!!

Ndiyo:- najua wengi mtashangaa, lakini msishangae sana. Tulio wengi tunafahamu Morogoro hii kutokana na HOSPITAL maalumu/MAARUFU ya  wagonjwa wa ukoma.  Si mbali kutoka Peramiho kama sikosei ni km 5-8 hivi.

Monday, February 3, 2014

MSAADA WA VITENDAWILI NA MAANA ZAKE!!

Nimetumiwa ujumbe huu lakini kwa bahati mbaya hivi vitandawili kwangu vimekuwa vigumu kidogo kwa hiyo naomba ndugu zangu tusaidiane maana palipona wengi hapaharibiki kitu..Natunguliza shukrani zangu za dhati kwenu. Na ujumbe wenyewe unasema hivi:- karibuni!!
--------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------
Dada Yasinta, habari za leo? Samahani naomba msaada wako kwa vitendawili vifuatavyo:
1) Wanastarehe darini.
2) Sina dada wala kaka, lakini baba wa huyu jamaa ni mtoto wa baba yangu.
3) Nguo ivaliwayo kila siku isiyoingiwa na chawa.
4) Ini la ng'ombe huliwa hata na walio mbali.
5) Chatembea na hakijapata kupumzika hata nukta moja.
6) Mvua kidogo ng'ombe kaoga kichwa.
7) Njoo hapa nije hapo.
8) Msitu ambao haulii hondohondo.
9) Aliwa, yuala, ala, aliwa.
10) Ajenga ingawa hana mikono.
JUMATATU IWE NJEMA KWA WOTE!

Saturday, February 1, 2014

HUYU NDIYE MWANAMTINDO ATAKAYEFUNGUA MWEZI HUU WA PILI/FEBRUARI

Ebu angalia hapa alivyopendeza nimependa ile mbaya. Rangi zote zimekaa safi sana.
Hapa akaona abadili mtindo  amekaa na kofia nyingine hakika nimependa mno vazi hili. Na huyu binti si mwingine tena bali  ni shangazi yangu Paulina Mubelwa. Binti Bandio Mubelwa /Mzee wa Changamoto.
JUMAMOSI NJEMA.