Tuesday, January 31, 2012

ULIKUWA UNAJUA MATUNDA HAYA YANAITWA MABUNGO?.....

......na yanapatikana ZANZIBAR. Je? kuna anayejua kama yanapatikana sehmu nyingine? kuna dada mmoja alikuwa huko na alionja na akayapenda. Binafsi sijawahi kuonja. Natumaini nitapata jibu kwani nimeulizwa swali hilo na nimeshindwa kujibu na nikaona hapa nitapata tu jibu..Natanguliza shukrani....

Monday, January 30, 2012

WANAUME NA KAULI HIZI: 'HUYO SIO WA KUOA, NI WA KUCHEZEA TU'

Bila shaka wewe msomaji unayesoma hapa utakubaliana na mimi kuwa umeshawahi kuzisikia kauli hizi kutoka kwa wanaume pale anapozungumziwa mwanamke mzuri kwa sura na umbo.

Kwa kawaida vipimo vya uzuri wa mwanamke kwa wanaume vimegawanyika. Wanaume wengi hupima uzuri wa mwanamke kwa sura au umbo, lakini linapokuja swala la kuoa, suala la tabia na mwenendo hupewa nafasi kubwa.
Na ndio maana wakati mwingine unaweza kushangaa kukuta mwanaume ambaye ni hodari wa kuchagua wanawake wazuri, lakini ukija kumuona mke aliyemuoa, utakuta ni mbaya kwa sura na umbo, lakini kwa upande mwingine utakuta mke huyo ni mzuri katika maeneo mengine kama vile, tabia nzuri,upendo, wema, na anayemudu malezi ya watoto katika familia.

Sifa nyingine ni zile za kumkubali mwingine kirahisi, kuwa tayari kusaidia yanapojitokeza matatizo katika familia, mpenda amani na kumfanya mume wake aone kuwa hakukosea kumchagua yeye kuwa mke wake. Kwa kifupi wanawake wa aina hii hata kama wangekuwa ni wabaya kwa sura na umbo bado wako kwenye nafasi ya kuonekana kuwa ni wazuri, na huolewa kirahisi zaidi.

Wanawake wazuri kwa sura na umbo ambao tabia na mienendo yao hairidhishi wako kwenye nafasi kubwa ya kuishi bila kuolewa, na kwa bahati mbaya zaidi wanawake wengi wanaohesabika kuwa ni wazuri, tabia na mienendo yao ni ya kutilia mashaka. Wanaume wengi huvutiwa na wanawake hao kujenga uhusiano nao hasa wa kimwili tu na si vinginevyo, na ndio maana wanawake wazuri kwa sura na umbo wanalo soko kubwa sana kwa wanaume, lakini huishia kuchezewa zaidi kuliko kuolewa.

Wanaume nao kwa upande wao wamejenga dhana kwamba wanawake wazuri sana sio wa kuoa na hivyo kuwaogopa. Wanaamini kwamba wanawake wazuri sana ni wasumbufu, kitu ambacho kina ukweli kwa kiasi fulani. Wanaume wanaamini kwamba wanawake wazuri sana kwa sura na umbo huwasababishia waume zao maradhi ya moyo,shinikizo la damu na wakati mwingine hata kuwafanya kupata matatizo fulani ya kiakili, na hiyo inatokana na waume hao kuwa katika mashaka ya wake zao kuchukuliwa na wanaume wengine wakati wowote kutokana na uzuri wao. Hata hivyo wanawake wazuri nao huwaendesha waume zao wakijua kuwa ni wazuri na soko lao liko juu na waume zao nao huwanyenyekea wakihofia kuachwa.

Na ndio maana usishangae kuona kuwa wale wanawake ambao watu wamekuwa wakiamini kuwa ndio wabaya kwa sura au umbo lakini tabia na mienendo yao ni mizuri ndio wanaoolewa na hata ndoa zao zinadumu, tofauti na za wale wanaoonekana kuwa ni wazuri sana kwa sura na umbo na ambao tabia na mienendo yao si mizuri, ndoa zao hazina umri mrefu

Sunday, January 29, 2012

WIMBO HUU NIMEUIMBA TANGU NILIPOKUWA MDOGO ILA ULINIPOTEA LEO NIMEUPATA:-SISI WANA WA DUNIA...


Yaani najisikia raha, roho yangu imekuwa kama vile ni mpya kwa jinsi utamu wa wimbo huu unavyopendeza. Kaka Baraka upo maana wewe najua unaupenda sana wimbo huu:-)MNAPENDWA WOTE..KWA MARA NYINGINE TENA JUMAPILI NJEMA!!!

SWALI LA JUMAPILI YA LEO:- Msamaa ni nini?


Nisamehe

Je utaratibu sahihi wa kumsamehe /kusamehewa kwa mtu aliyekosa ni upi?
1. Mtu aombae msamaha kwanza/atubu ndipo asamehewe?
2. Asamehewe hata pasipo kuomba msamaha au?
3. Vyote viwili ni sawa?


Friday, January 27, 2012

PICHA YA WIKI ILIYOPENDWA NA PIA KUCHAGULIWA NA KIBARAZA HIKI !!

Inapendeza kuona watoto wanashika vitabu na kujifunza/kusoma. Sijui hapa anauliza mama/baba hii ni nini au wenzangu mnasemaje?

UJUMBE WA IJUMAA YA LEO:- KUJIJUA!!!

Leo nimeamka nikiwaza neno hili: Kujijua: Ni mojawapo ya stadi kuu za maisha ni kwamba mtu unapaswa kufahamu jinsi ya kutumia akili yako ili kunufaisha maisha yako. Mahali popote pale ulipo. Uwe mtendaji, siyo mtendewa, ili ujielewe zaidi, ujiamini zaidi, ufanye mambo makubwa na udhibiti mwelekeo wa maisha yako.....unapaswa kujijua!!!!!!!
NAWATAKIENI MWISHO WA JUMA MWEMA WOTE NA WOTE MNAPENDWA SANA!!!!

Thursday, January 26, 2012

JE? KUNA NAFASI YA KUKIMBA HAPA?

Kaaaazi kwelikweli hilo panga hilo, kweli siku ya fumanizi ni fumanizi au niseme za mwizi orobaini!! Sijua hapo mwenye kosa ni nani? Maana inaonekana kama huyo mume mwenye panga hapo ndIo nyumbani kwake na ameibiwa. Mmmmmhhh!

Wednesday, January 25, 2012

Madaktari watangaza mgomo nchi nzima

MADAKTARI wametangaza rasmi kuanza mgomo katika hospitali zote za rufaa na vituo mbalimbali vya afya nchini kote hadi hapo madai yao yatakaposhughulikiwa na Serikali.
Pia wamepitisha azimio la kumtaka Rais Jakaya Kikwete kuifumua na kuiunda upya Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii kwa kuwaondoa kwenye nyadhifa zao Waziri Dk Haji Mponda na Naibu wake, Dk Lucy Nkya kutokana na kile wanachodai kuwa ni kudhalilisha taaluma yao.Dk Uliomboka pia aliwataja Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Blandina Nyoni na Mganga Mkuu wa Serikali, Dk Deo Mtasiwa kwamba wanapaswa kuwajibishwa na Rais.
Akitangaza mgomo huo, Dar es Salaam jana Mwenyekiti wa Kamati ya Muda ya Jumuiya ya Madaktari hao, Dk Stephene Ulimboka alisema hatua hiyo inalenga kupata ufumbuzi wa madai waliyotoa kwa muda mrefu na kuongeza kwamba, leo wanatarajia kukutana na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda.
Dk Ulimboka alitaja baadhi ya madai yao kuwa ni kuwawekea mazingira bora ya kazi madaktari kwa kupeleka vifaa vya kazi hospitalini na kwenye vituo vya afya, kuboresha malipo ya posho na kuwapatia sitahili zote wanataalamu hao.
Hata hivyo, tafauti na ilivyokuwa awali, kikao cha jana ambacho kilikuwa cha majumuisho, kilitumika pia kupokea ripoti ya mikutano iliyokuwa ikiongozwa na Chama cha Madaktari Tanzania (MAT) na kupokea majukumu ya kuongoza harakati hizo.
“Kuanzia leo tunatangaza kuwa madaktari wote wanaoguswa na hili kote nchini kuacha kufanya kazi hadi hapo Serikali itakapotekeleza madai yetu, tunataka Serikali iboreshe mazingira ya kutolea huduma za afya, ili kumwezesha daktari kumpatia huduma mgonjwa katika kiwango kinachostahili,” alisema Dk Ulimboka.
Alitaja madai mengine matatu ambayo kamati anayoiongoza inasimamia kuhakikisha yanatekelezwa kuwa ni pamoja na madaktari kurejeshewa nyumba za kuishi kama inavyoelekezwa kwenye ‘Standard order’ ya Serikali, ambayo inasema daktari atapatiwa nyumba ya kuishi na Serikali na kama sivyo atapatiwa asimilia 30 ya mshahara.
Alisema kipengele hicho kiliondolewa kinyemela bila wao kushirikisha wala kuelezwa sababu za kuondolewa kwake, jambo linalowaongezea ugumu wa maisha na kuwafanya wadharaulike.
Madai mengine yalihusu nyongeza za mishahara, ambayo alisema kumekuwa na ugumu wa kutekeleza suala hilo kila mara hadi wanapofanya mgomo.
“Mwaka 2005 wakati tunaanza kazi, mshahara wa daktari ulikuwa unafikia Sh124, 000, lakini baada ya mgomo ndipo ukapandishwa hadi kufikia karibu ya laki 700,000 sisi tunataka suala hili lirekebishwe na nyongeza yake isisubiri shinikizo,” alisema.
Madai mengine ni malipo kwa madaktari pindi wanapofanya kazi katika mazingira hatarishi na kupendekeza walipwe asimilia 30 ya mshahara wao, posho wakati wa kazi ya ziada ambayo kwa sasa wanalipwa asimilia 10 ya mshahara wao.
Kuhusu mshahara, alisema yapo mapendekezo ambayo alisema wataitaarifu Serikali watakapokutana na viongozi wake.
Madaktari hao leo wanatarajia kuendelea na mkutano wao katika ukumbi wa Don Bosco.Rais wa MAT, Dk Namala Mkopi alisema alikabidhi majukumu kwa kamati iliyoundwa na wanachama baada ya kuonekana kuwa hadi sasa Serikali imekuwa ikiwazungusha.
“Wanachama wamesema hapo mlipofikia tunashukuru mmejitahidi vya kutosha na sasa tunaomba mtukabidhi majukumu ili shughuli hii iweze kusimamiwa na kamati ya madaktari,” alisema Dk Mkopi.
Hatua hiyo imelenga kuongeza wigo wa washiriki ambao watawahusisha madaktari wasio wanachama wa MAT na wafanyakazi wengine katika sekta hiyo ya afya.
Chanzo: Gazeti la Mwananchi.....kupitia http://simulizi.blogspot.com/.

MTOTO AVUNJA MLANGO NA KUMBAKA MAMA YAKE MZAZI AKIWA AMELALA

NI JUMATANO NA NI SIKU ILE YA KIPENGELE CHETU CHA MARUDIO NA LEO NIMEFIKA NYUMBANI RUVUMA NA HABARI HII YA KUSIKITISHA... EBU SOMENI..NIMEKUTANA NAYO Na Mwandishi Wetu, Songea
-------------------------------------------------------------------------------------------------
JESHI la polisi Mkoani Ruvuma linamshikilia Frank Jota (26) mkazi wa kijiji cha Litisha Wilayani Songea kwa tuhuma za kumbaka mama yake mzazi mwenye umri miaka 54 ambaye jina lake limehifadhiwa wakati amelala nyumbani kwake majira ya saa za usiku.
Kamanda wa Polisi Koa wa Ruvuma Michael Kamuhanda amesema kuwa tukio hilo limetokea januari mosi mwaka huu huko katika kijiji cha Litisha kilichopo nje ya mji mdogo wa Peramiho.
Amesema kuwa siku hiyo ya tukio majira ya saa za usiku Jota alikwenda nyumbani kwao ambako alimkuta mama yake mzazi akiwa amelala na baadaye alianza kutafuta namna ya kuingia kwenye nyumba hiyo ambayo mlango wake ulifungwa na komeo kwa ndani.
Amefafanua zaidi kuwa Jota baada ya kuona mlango umefungwa kwa komeo kwa ndani aliamua kuuvunja mlango wa nyumba hiyo kisha aliingia ndani na kwenda moja kwa moja kwenye chumba alicholala mama yake mzazi ambaye jina lake limehifadhiwa.
Amesema kuwa Jota akiwa kwenye chumba ambacho mama yake alikuwa amelala alianza kumtishia kwa kisu alichokuwa ameshika mkononi na baadaye alimkaba shingo na kufanikiwa kumvua nguo ya ndani aliyokuwa amevaa kisha alianza kufanya naye mapenzi.
Amebainisha zaidi kuwa wakati Jota akiendelea kufanya mapenzi na mama yake watu waliokuwa jilani na tukio walisikia kelele za mtu akipiga mayowe na walipofika kwenye eneo hilo la tukio waliingia ndani ya nyumba hiyo na kumkuta Jota akitokea kwenye chumba alicholala mama yake na baadaye alipowaona watu alijalibu kukimbia lakini majirani hao walifanikiwa kumkamata na kumpeleka kituo kidogo cha polisi cha peramiho.
Hata hivyo kamanda wa polisi Mkoa wa Ruvuma Kamuhanda ameeleza kuwa polisi baada ya kumuhoji mtuhumiwa amekili kutenda kosa hilo na anatarajiwa kufikishwa mahakamani mara tu upelelezi utakapo kamilika.
Mwisho.
TUKUTANE JUMATANO IJAYO !!!!!!

Monday, January 23, 2012

TUANZE JUMATUTA KIHIVI:-JE? NI PICHA GANI AMBAYO IMEVUNJA REKODI MWAKA 2011 KATIKA BLOG YA MAISHA NA MAFANIKIO?

Ni ombi kutoka kwa dada Mija:-"Ombi..tuongezee ile juu kwenye page yako ya blogu, ulovaa tisheti ya njano, sketi nyeupe na mkanda wa kipepeo.."


mwaka 1992 Wilima (Matetere) Madaba



Picha hii nilipiga mwaka 2008 mwezi wa sita



Na hii nilipiga mwa jana 2011 mwezi wa kumi....




...............hii pia mwaka jana mwezi wa kumi na mbili kijapani:-)



Hii ni ya mwaka huu 4/1 2012




Sunday, January 22, 2012

JUMAPILI NJEMA WAPENDWA!!


Napenda kuwatakieni wote mtakaopita hapa JUMAPILI njema sana . Nineona niwatakieni jumapili hii kwa wimbo huu ingawa sielewi nini kinasemwa ila nimeupenda tu...naamini wanaimba kumsifu Mungu.....

Saturday, January 21, 2012

MWANAMKE NA NYUSO ZAKE!!!

NIMEIPENDA NUKUU HII EBU SOMA!! "Mwanamke kama dutu la udongo wa mfinyanzi huubwa na kuumbuliwa na jamii kwa namna mbalimbali. Kama kinyonga, uso wake unabeba rangi tofauti kulingana na mikondo ya maisha na mapigo ya wakati. Itakuwaje mwanamke awe wa wa kuuzwa kama mwenye ugaga wa hisia za kujichagulia mwenyewe; au awe wa kuuzwa kama pakacha la maemba katika soko la umma? Uso wa mwanamke ni njia mbilimbili; ikiwa hazai analea, isipokuwa akirembesha anarembeshwa, kama hatumbuizi anatumbuizwa, ikiwa hajengi anabomoa; na kila mtu anamtazama na kumtarajia aonyehe uongofu wa malaika kama kwamba yeye si mtu. Haya yanapokolea ndipo mwanamke anaonyesha nyuso zake." kutoka kwenye kitabu kiitwacho NYUSO ZA MWANAMKE.

Friday, January 20, 2012

EBU ANGALIA TEKNOLOGIA HII!!...NJOMBE......


Binafsi nimeipenda ...KILA LA KHERI KWA WOTE !!

PICHA ZILIZOCHAGULIWA NA BLOG YA MAISHA NA MAFANIKIO KUWA PICHA ZA WIKI!!

Nadhani hapa ni maandalizi....
Na hapa naona safari inaanza . Raha jipe mwenyewe:-) au nisema fanya vitu ambavyo hujafanya kabla muda haujakukimbia.
NAPENDA KUWATAKIENI WOTE MTAOPITA HAPA MWISHO WA JUMA MWEMA!!!!.

Thursday, January 19, 2012

NI MSIMU WA MAEMBE/NINA HAMU YA KULA EMBE!!

Nimekaa hapa nikawa nawaza kuwa sasa ni msimu wa maembe, mmhhh nikapata hamu. Natamani kweli embe. Maana msimu huu huwa maembe yanakuwa mengi mpaka wengine wanalisha nguruwe...Je wewe una tamani matunda gani? au chakula gani?


WAZO LA KUFUKIRISHA KWA ALHAMISI YA LEO KUTOKA KWA KAPULYA!!

Hivi ni mimi tu au nawe mwenzangu umewahi kufikiria ya kwamba:- Ni ajabu watu wengi wanajua vipi komputa au gari vinafanya kazi. Lakini HAWAJUI/HAWAJIJUI WENYEWE WAPOJE/WANAFANYA KAZI VIPI.
NAWATAKIENI ALHAMISI NJEMA NA FIKRA NJEMA!!!

Wednesday, January 18, 2012

HUYU NDIYE YASINTA NGONYANI!!!

Kama kawaida ni JUMATANO NYINGINE TENA NA NI KILE KIPENGELE CHA MARUDIO YA MATUKIO MBALIMBALI. Na Makala hii nimeshawahi kuiweka hapa. Lakini nimeshindwa kuvumilia kutoiweka hapa tena. Ni ZAWADI AMBAYO SITAWEZA KUISAHAU MILELE.

Yasinta Ngonyani, Picha kwa hisani ya Maisha Blog
Ni binti halisi wa kitanzania, ingawa anaishi ughaibuni lakini hujivunia asili yake na utaifa wake, ni binti pekee aliyejitolea muda wake kuwaelemisha watu wa rika zote bila kujali rangi, kabila, itikadi, taifa wala jinsia.


Binti huyu si mjivuni na hupenda kubadilishana mawazo na watu mbali mbali, na pia hupenda kufuatilia habari za nyumbani kwao alikotoka na haoni tahayari kuongea lugha ya kwao. Daima hujitambulisha kwa jina la asili ya kwao na huona fahari kutumia jina hilo.


Binti huyu hakuona ajizi kuwajuza wanae asili ya kwao japo wamezaliwa ughaibuni, amekuwa msitari wa mbele katika malezi ya wanae ili kuhakikisha wanae hao hawajitengi na asili ya aliotoka yeye.


Si mchoyo wa ushauri na kupitia makala zake aziwekazo kibarazani kwake amekuwa ni msaada kwa wengi, amekuwa mstari wa mbele katika kuilemisha jamii bila kujali rika. Amejitolea kufundisha kile akijuacho juu ya malezi na matatizo mbali mbali yanayowakabili wanandoa na malezi ya watoto.


Kibaraza chake kimekuwa ni kitovu chenye kukutanisha wadau mbali mbali wenye fikra pevu, na kuibua mijadala yenye kuelimisha, kufundisha, kuburudisha na kuhuzunisha pia.


Binafsi napenda kumuita dada na kwangu mimi ni zaidi ya dada, kwani amekuwa ni mwalimu mzuri kwangu nikijifunza mambo mengi kupitia kibaraza chake nimekuwa nikijifunza mengi, na sisiti kukiri kwamba chimbuko la kibaraza cha VUKANI ni kutokana na kile nilichojifuza kwake.


Ni mkweli na muwazi, na hasiti kusema wazi hisia zake, lakini huwa makini sana ili kuepuka kumuumiza mtu mwingine kihisia, na kama kwa kusema huko kutamkera mtu mwingine, ni mwepesi kuweka sawa maelezo yake ili kuondoa msigishano wa mawazo.


Nakumbuka wakati fulani nlipopata msongo wa mawazo kutokana na tofauti zangu na wazazi wangu, alikuwa ni mtu wa kwanza kunitumia email binafsi akijaribu kuniliwaza na kunitaka nisichukue hatua yoyote kujidhuru, naomba nikiri kwamba email ile ilinisaidia sana kurudi katika hali yangu ya kawaida na nilijisikia fahari kuona kwamba kuna mtu ananipenda na kunijali japo sijawahi kuonana naye uso kwa uso.


Huu kwangu ulikuwa kama muujiza, inakuwaje, mtu kusoma mawazo yangu kupitia blog tu halafu awe karibu nami kiasi hiki, ni kitu gani kimemvuta? Kusema kweli tangu siku hiyo niliamni kuwa maandishi yana nguvu sana na kupitia maandishi yawezekana mtu mwingine kukufahamu vizuri sana.


Nimekuwa karibu sana na binti huyu, na amekuwa ni mwema sana kwangu na mshauri wangu pia, na kupitia vibaraza vyetu, tumekuwa tukibadilishana mawazo na kupeana ushauri mbali mbali ili kuboresha ustawi wetu na wa familia zetu.


Huyu ndiye Yasinta Ngonyani, kwa kumsoma zaidi bofya hapa.


-------------------------------------------------------------------------------------------------Makala hii iliandikwa na mdogo wangu wa hiari Koero Mkundi mwaka 2009/08/14 bado nimevutiwa sana na hii makala na nimeona niiweke hapa kwangu pia kama kumbukumbu na pia kujikumbusha yaliyopita kwani si vibaya. Pia nachukua nafasi hii kwa kumshukuru sana mdogo wangu huyu wa hiari Koero Mkundi kwa kazi nzuri anazozifanya kwa kumsoma zaidi kazi zake ingia hapa. Pia nauthamini sana uwepo wake Mwenyezi Mungu na akulinde na akuongoze na yote utendayo yawe mema. Kwani yeye ndiye mwezeshaji wa yote na yeye ndiye ajua anavyotuwazia maana mawazo atuwaziayo ni mema. Ni hayo tu kwa leo...Halafu sijui upo wapo Koero?
TUKUTANE TENA JUMATANO IJAYO AU WAKATI MWINGINE....


Tuesday, January 17, 2012

TAREHE 17 YA MWEZI WOWOTE ULE INANIFANYA NIMKUMBUKE SANA MAMA YANGU!!


Sijui nina nini kila mwezi ifikapo tarehe 17 huwa ninakosa raha sana. Kwa hiyo leo mtaniwia radhi kama sitakuwa mtembezi katika vibaraza vingine pia kama nitamjibu mtu ovyo, Yasinta/kapulya

Monday, January 16, 2012

KUTHUBUTU KUONYESHA MAPENZI/UPENDO=MAISHA

Kuthubutu kuonyesha upendo wako,

sio tu maneno mazuri,

Na sio tu upendo wa matendo

Au maua na chokleti.

Ni kuonyeshana heshima,

uaminifu na imani.

Kuonyesha wepesi wa kuona huruma wakati mwanzako anapokuwa na

msongo/matatizo.

Kuwa msaidizi mwema na mwenye kusema ukweli.

Kuthubutu kuonyesha masikitiko yako,

Sio kila wakati kujifanya mwenye nguvu (mvumilivu),

Tukae/kaeni pamoja, tuthubutu kuwa watoto ndani yetu.

Tuwe sisi (Kuweni ninyi) kwa dakika chache.

Tuwe na dakika chache za furaha.

Tuwe na dakika chache za huzuni.

Tufanye siku iwe ya shangwe.

Tushirikiane katika raha na taabu katika maisha.

Tuwe waaminifu, tukaribiane na tupeane joto.

Sunday, January 15, 2012

KAPULYA ANAWATAKIENI JUMAPILI NJEMA WOTE MTAKAOPITA HAPA!!

Ni Jumapili ya tatu ya mwaka huu 2012 na blog ya Maisha na Mafanikio inapenda kuwatakieni wote mtakaopita hapa afya njema pia baraka nyingi sana. JUAMAPILI NJEMA WAPENDWA WANGU.

Saturday, January 14, 2012

NAPENDA KUWATAKIA WOTE MWISHO WA JUMA NA MUSIKI HUU HAYA TUFURAHI PAMOJA


NA UJUMBE WA LEO NI :- UKITAKA KUJUA MENGI BASI NI KUULIZA NDIO DAWA YAKE. MWISHO WA JUMA MWEMA NDUGU ZANGUNI. TUSISAHAU KUWAKUMBUKA TUWAPENDAO PIA HATA WALE TUWACHUKIAO KAMA WAPO.!!!

Friday, January 13, 2012

JE? KUNA TOFOUTI KATIKA PICHA HIZI MBILI?

Akina dada wamekaa mduara na nadhani wapo katika shindano fulani...maana inaonyesha katika mavazi yao..


........................na hapa ni kundi la watoto wamekaa kwa macho yangu mimi ni kama vile wamekaa na wanasikiliza hadithi?....wewe je unaonaje? IJUMAA NJEMA KWA WOTE!!!

Thursday, January 12, 2012

DAGAA WAPANDA BEI IRINGA!!!

Duh! kilo moja ya dagaa sasa ni shilingi ELFU TANO! Tutapona kweli? Mmmhh..naona tuanze kulima bustani za mbogamboga.....kaaaazi kwelikweli!! picha kutoka blog ya Mjengwa.
Ngoja Blad Key amalizie na wimbo huu.....

Muwe Salama wote tutaonana tena wakati ujao!!

MAJI YA KWENYE MTUNGI NI MATAMU JAMANI!

Maji ya mtu ni matamu sana hasa kama unatumia kata au kikombe cha bati kama uonavyo hapo kwenye picha. Mtungi huu una historia yake:- Ni Hivi mwaka jana nilipokuwa Matema beach, pale kuna soko kubwa la vyombo vya aina mbalimbali vya udongo wa mfinyanzi. Nami nikaona ngoja niende nikasafishe macho. Kwa bahati nzuri nikaona mtungi huu nikaununua. Nakuambieni penye nia pana njia. Niliupakata mtungi huu kuanzia Matema Beach mpaka Songea/Ruhuwiko. Halafu kabla hatujafika nyumbani Ruhuwiko tukasimamishwa na Polisi pale Bombambili kwa wale wanaojua umbali wa kutoka Bombambili mpaka Songea mjini /Ruhuwiko. Tukamsalimu, mnajua alitaka nini, baada ya kuangalia ndani ya gari? MTUNGI HUU! Duh! hapo nikasema simpi ngó, naye akasema nitawatoza kwa spidi ila mkinipa mtungi nitawaacha nami nikamjibu, sawa tu..kwa vile nilijua hatukuwa katika mwendo wa spidi. Akashindwa na tukaendelea na safari. Hii ni historia fupi ya MTUNGI HUU.
Hapo juu nimesema maji ya mtungi ni matamu kwa kunywa kwa kutumia KATA. Kwa wale wasiojua kata ni nini . Katika picha hii hapa mnamwona Stella Manyanya akijaribu kunywa maji kwa kutumia KATA. Hivi ndivyo ilivyokuwa hapo zamani ni utamaduni wetu.

Wednesday, January 11, 2012

Ndoa ni ninyi wenyewe, Siyo watu wa nje

TULIKUWA TUMEPUMZIKA KIDOGO NA KIPENGELE CHETU CHA MARUDIO KILA SIKU KAMA HII YA JUMATANO. NA LEO KATIKA UPEKUZI WA KAPULYA AMEKUTANA NA MAKALA HII NA AMEONA SI MBAYA KAMA WENGI TUKIJUA KWANI KAMA NISEMAVYO KURUDIA SOMA NDIO MTU UNAPOELEWA ZAIDI. MAKALA HII NIMEIKUTA HAPA. KARIBUNI.
---------------------------------------------------------------------------------------------
SIRI moja kubwa ya kuwa na ndoa nzuri ni wanandoa wenyewe kujitambua kuwa wao ndiyo wenye deni la kuimarisha uhusiano walionao.

Ndiyo kusema kuwa kila siku katika maisha yako, unapaswa kutafuta mbinu za kufanya ili uhusiano wenu uendelee kuwa mzuri.
Siku moja nilikuwa napita Sinza (Dar es Salaam), nikamsikia dada mmoja akijibizana na mwenzi wake kwenye simu; Aah! kwani wewe unataka muda huu niwe wapi? Haya basi niko chooni.

Hayakuwa majibu mazuri, kiasi dada mwingine aliyekuwa karibu, akamsihi mwenzake asizungumze vile.Watu wengi wanapenda kuwa na ndoa nzuri, lakini wao hawajui kuwafanyia mazuri wenzao. Utakuwaje na ndoa nzuri wakati kauli zako ni chafu?

Jitahidi kuwa na kauli nzuri kwa mwenzi wako. Hata pale mwenziyo anapokukosea, zungumza naye kwa njia ya kuondoa kasoro, si kutukanana. Siku zote waza namna ya kuujenga uhusiano wenu. Usidhani ndoa nzuri za wenzio ni jambo linaloshindikana kwako, hapana. Ndoa haijengwi kwa matofali, bali kauli njema na matendo mema.

Kumbuka hakuna mtu aliyezaliwa aje kuiimarisha ndoa yako, ni wewe mwenyewe unapaswa kufanya kazi hiyo. Anza leo kuchukua hatua kama ndoa yako ina walakini huo, utashangaa utakavyokuwa na ndoa nzuri. Katika maisha hakuna lisilowezekana. Kwanza weka lengo, kisha chukua hatua, utafanikiwa.

Ni muhimu kujifunza masuala haya kwani elimu haina mwisho. Wengi wakishaingia kwenye ndoa, basi hudhani wameshamaliza kila kitu. Ni makosa makubwa, unapaswa kuendelea kutafuta mbinu mpya kila siku ili mfaidi raha za ndoa.

Kuna mengi ya kujifunza:
Katika ndoa kuna mengi ya kujifunza, mojawapo ni kujua mwenzi wako anapenda nini. Kwa mfano wanaume wengi wanapenda wake zao wawe na utayari katika mahusiano.Unaweza kushangaa, lakini ni ukweli. Tafiti zinaonyesha watu wasio kwenye ndoa hukutana kimwili mara nyingi zaidi kuliko walio kwenye ndoa, licha ya kuwa wanalala kitanda kimoja.

Watu wakishaingia kwenye ndoa, hufanya tendo hilo kwa muda mfupi zaidi kuliko ilivyokuwa kabla hawajaoana, unajua ni kwa nini? Utayari huwa matatizoni. Sababu ziko nyingi, lakini mojawapo ni wanaume wengi kurudi majumbani wamelewa chakari, wananuka pombe na wake zao wanalazimika tu, wafanyeje.

Lakini wakati wa uchumba, wanaume hao huenda kwa wapenzi wao wakiwa hawajalewa.
Ndiyo ukweli. Kimsingi wanandoa kila mmoja anatarajia kuona mwenzi wake anamjali na anamsikiliza. Kufanikiwa hili, lazima kutumia akili.

Kuna ambao licha ya kuwa tayari kaingia kwenye ndoa, lakini kwa upumbavu, anazungumzia habari za mpenzi wa zamani.

Pia kuna walio kwenye ndoa, lakini wanajali zaidi watu wengine wa nje au kuwasikiliza zaidi wazazi ambao mara kadhaa wamekuwa chanzo cha ndoa kuvunjika.
Jamani hata Biblia imeandika;
Mtu atawaacha wazazi wake na kuandamana na mkewe, hao wawili watakuwa mwili mmoja.

Wengine wako katika ndoa lakini wana lundo la wapenzi nje. Hapo ndoa yako ikiyumba utamlaumu nani? Fanya jitihada kuipa uhai ndoa yako, iwe paradiso ya kweli.Kuna ambao badala ya kutamani kurudi nyumbani, wao hutamani kuchelewa, maana nyumbani hakukaliki.Yaani hakuna mapenzi, hakuna kinachovutia. Mume au mke hapendi kujifunza mambo zaidi.
Ndugu yangu rekebisha ndoa yako, uishi kwa furaha.

Dismas Lyassa ni mtaalam wa mahusiano, wasiliana naye kwa simu 0754 498972 au 0786 148105.
TUKUTANE TENA WAKATI UJAO AU NISEME JUMATANO IJAYO.

Tuesday, January 10, 2012

LEO TUANGALIE VITENDAWILI VYA KISWAHILI:- KITENDAWILI…..

1. Haukamatika wala haushikiki.........
2. Anataga huku akitambaa...................
3. Ninapompiga mwanangu watu hucheza...................
4. Ubwabwa wa mwana mtamu........................
5. Kuku wangu katagia mayai mibani.................

Monday, January 9, 2012

HUU NI MLO WANGU WA MCHANA WA LEO KARIBUNI NI SUPU YA KAROTI!!


HAPA NI KAROTI AMBAZO TAYARI ZIMEMENYWA KWA AJILI YA SUPU
Karoti 6-8 kubwa,
Vitunguu 2
Vitunguu swaumu/saumu vipande 3,
Kijiko 1 cha siagi,
Vijiko 2 vya tangawizi iliyokunwa.
Lita 1 ya maji.
Vikombe 2 vya cream,
Vikombe 2 vya maziwa,
Kijiko1 chumvi
Pilipili kidogo/kadili upendavyo.
Jinsi ya kufanya:-
Menya karoti, vitunguu na vitunguu saumu/swaumu. Kisha kata vipande vipande. Yeyusha siagi na kaanga kwa dakika 3-5 kwenye sufuria kubwa. Weka tangawizi , kisha tia maji. Pika supu kwa joto la chini huku umefunika hadi karoti ziwe laini. Weka cream, maziwa na pilipili. Kisha unamixa na blender ya mkono mpaka kuwa laini. unawezawa kuongeza maji au maziwa kama unaona supu ni nzito. KILA LA KHERI NA UPISHI HUU:-)


HABARI ILIYONISIKITISHA...MICHEZO NI YA WATOTO AU WAZAZI?

Jana jini nikiwa nasikiliza taarifa ya habari. Kukawa na habari ya michezo ya watoto. Ni mchezo wa innebandy/floorball, mtoto huyo mwenye miaka 10 jina halikutajwa baada ya mchezo timu yake ilishindwa. Na hapo baba yake mzazi alikasirika, na kumwacha mtoto huyo nje akiwa na jezi tu na wakati nje kulikuwa na baridi. Baada ya muda mzazi mwingine alikuwa akipita akamwona yule mtoto akamchukua na kumpeleka kwao. Usiku wote nikawa nafikiria na kujiuliza hivi hii michezo ni kwa ajili ya watoto au wazazi?

Sunday, January 8, 2012

NAWATAKIENI JUMAPILI NJEMA NDUGU ZANGU!!


SIKU ZINAKIMBIA KWELI LEO TAYARI NI JUMAPILI YA PILI KWA MWAKA HUU....KILA LA KHERI AU KAMA WIMBO USEMAVYO SONGA MBELE......

Saturday, January 7, 2012

NIMEULIZWA SWALI HILI NA BINTI YANGU....

Ilikuwa mwaka jana siku ya Noeli ...Binti yangu Camilla akaniuliza:- Mama, hivi kwa nini Yesu alizaliwa tarehe 25/12..Lakini, kipindi cha Pasaka huwa tuna sema kuwa Yesu anakufa, kwa nini ile tarehe ya kufa huwa haiwi ileile kila mara? Je kuna Yesu wangapi?...Mmmhhh!! hapa nikawa natafakari na sijapata jibu na leo nimeona niombe msaada hapa kibarazani kwani palipo na wengi huwa hakiharibiki kitu....

Friday, January 6, 2012

TANZANIA YETU NA UZURI WAKE....


Nawatakieni IJUMAA HII YA KWANZA YA MWAKA HUU 2012 IWE NJEMA PIA USIKU, MCHANA AU JIONI AU LABDA ASUBHI NJEMA Mie hapa ni saa kumi na mbili jioni.

Thursday, January 5, 2012

LEO NI SIKU YANGU YA KUZALIWA!!!

Napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu, kwa kunilinda salama mpaka kufika siku hii ya leo na kuongeza limwaka limoja zaidi. "AU uzee". Namshukuru kwa kuniepusha na mambo mabaya, magonjwa na pia vishawishi. Pia nawshukuru sana wazazi/walezi wangu kwa kunilea na kuwa kama nilivyo. Na halafu napenda kuwapa HERI YA KUZALIWA wote waliozaliwa mwezi huu walitimiza tayari miaka na watakaotimiza siku zijazo.
NAPENDA PIA KUSHEHEREKEA SIKU HII KWA WIMBO HUU:-)

NAMSHUKURU MUNGU KWA YOTE, FAMILIA YANGU PIA NINYI NDUGU ZANGU NA MARAFIKI WOTE NA NASEMA NAWAPENDENI SANA:-)

Wednesday, January 4, 2012

Nafasi ya Kazi...

Blogger Mwenza.
Ninatafuta blogger mwenza kwa ajili ya kushirikiana kuiandikia na kuiendeleza Kona Ya Waungwana.Sifa zifuatazo zahitajika:
1. Awe ni msomaji na mfuatiliaji wa blog mbalimbali hapa nchini Tanzania
2. Awe ni mkazi wa jijini Dar
3. Awe na background ya uandishi wa habari (si lazima sana)
4. Anaweza kuwa mwanafunzi katika chuo chochote Dar na hasa chuo cha Uandishi wa habari
5. Awe na ujuzi katika kublog na ufahamu wa blogger.com
6. Awe na nafasi ya angalau masaa matatu kwa siku kwa ajili ya kutafiti habari na kupost
7. Awe ni mmiliki wa Laptop yenye uwezo wa kuunganisha internet, na digital camera
8. Awe na uwezo wa kuongea kwa ufasaha lugha ya Kiswahili na Kiingereza
Mafao ni maelewano. Kama una sifa hizo hapo juu niandikie lacford.media@gmail.com au SMS +1301 222 7739 Ahsante, Mfalme MropeJe Huu Ni Uungwana

Monday, January 2, 2012

NIMEONA TUUANZA MWAKA MPYA 2012! KWA MTINDO HUU!!!!!!

Mwaka mpya huwa ni wakati wa malengo mapya na mwelekeo mpya. Kila binadamu ana malengo yake hapa duniani. Mimi nina malengo yangu na wewe pia una yako. Kila kukicha huwa tunajitahidi kuyatimiza. Tunapasua vichwa kujaribu kuyatimiza malengo yetu . Ndio maisha.

Bila shaka na wewe umeshaketi chini na kujiuliza swali hili:- ninataka kutimiza malengo gani mwaka huu? Je? ni kurudi shule kuongeza ujuzi? Je? ni kuoa au kuolewa? Je? ni kujitolea zaidi katika jamii yako/yangu? Je? ni kutunza na kulinda mazingira? Msururu wa malengo unaweza kuwa mkubwa. Kama kutimiza malengo fulani fulani ndio mkakati wako wa mwaka huu basi zingatia ushauri ufuatao:-

Weka malengo yanayotimizika au yenye uhalisia-Jiangalie ulipo, angalia vitendea kazi ulivyonavyo, tazama kwa makini ujuzi ulionao kisha yapime vizuri malengo yako.

Jiulize swali au maswali:- Nitayatimizaje malengo yangu? ukishafanya hivyo jiwekee utaratibu wa jinsi ya kutimiza malengo yako. Yaani mpango wa utekelezaji wako.

Nenda utaratibu -Mwaka ndio kwanza umeanza, yakaribiribie malengo yako kwa mwendo wa taratibu. Usiwe na haraka wala pupa. Si unakumbuka kwamba mambo mazuri hayataki haraka?

Usiogope kurekebisha malengo-Kadri mwaka unavyoanza kusonga mbele, unaweza kugundua kwamba huenda kutimiza malengo fulani. Hiyo inawezekana kutokea kwa sababu mbalimbali zikiwemo za kiuchumi, kiafya au kibinafsi. Usihofu kurekebisha malengo yako.

Usiogope kushindwa-Yawezekana kabisa ukashindwa kutimiza malengo fulani fulani. Kwa sababu zaweza kuwa kama hizo nilizozitaja hapo juu, usiogope. Cha muhimu ni kujaribu na kujaribu na kujaribu. Jitahidi kadri unavyoweza, nina uhakika ukijaribu utafanikiwa kwa hiyo mwisho wa siku hadithi ya kushindwa wala haitokuwepo.

La muhimu ni kuomba msaada inapobidi yapo mambo mengine ambayo hutaweza kuyatekeleza peke yako. Hilo linapotokea, usiwe mgumu kuomba msaada.
Kwa mara nyingine tena nawatakieni wasomaji wa blogya MAISHA NA MAFANIKIO kila la kheri katika mwaka huu wa 2012.