Saturday, June 25, 2011

KUADIMIKA KWA MUDA KWA BLOG YA MAISHA NA MAFANIKIO/KAPULYA!!!

Blog ya MAISHA NA MAFANIKIO inapenda kuwataarifu wasomaji wake kwamba haitakuwa hewani kwa muda.
Sababu kubwa ya kutokuwa hewani, nadhani wengi mmeona/soma/sikiliza posti ya 22/6 kuwa KAPULYA atakuwa SAFARINI na posti ya 22/6 ilikuwa kama kionjo tu yaani akifikiri jinsi safari itakavyoanza ....Sio safari nyingine bali ya NYUMBANI-TANZANIA.

Nitajitahidi kuwataafu mawili matatu. TUKUTANE TENA WAKATI MWINGINE PAMOJA DAIMA. NAWATAKIENI WOTE KILA JEMA. TUTAONANA.
NGOJA DR. Remmy amalizie kwa wimbo huu......

KARIBUNI SANA SONGEA-RUHUWIKO:-(-----:-)

Thursday, June 23, 2011

MIAKA NANE YA NDOA, LAKINI HAYA MAUZA UZA NINAYOYASHUHUDIA NABAKI KUJIULIZA, TATIZO NI MALEZI AU NI WAPAMBE?

Ndio, leo hii natimiza miaka nane ya ndoa, lakini nikiwa peke yangu.
Sio kwamba mwenzangu katangulia mbele ya haki, au amesafiri, la hasha,
yupo, tena hapa hapa mjini, yu buheri wa afya kabisa.
Siku kama ya leo, ilikuwa ni furaha isiyo kifani mimi na mume wangu
tulikuwa tumesimama madhabahuni tukila kiapo cha ndoa mbele ya wazazi
wetu, ndugu, jamaa na marafiki. Nakumbuka nilikuwa nimemuangalia mume
wangu usoni wakati alipokuwa akitamka yale maneno ya mwisho ya kiapo
yasemayo, “mpaka kifo kitakapotutenganisha” Alikuwa akionekana dhahiri yale maneno yalitoka katika moyo wake ambao
ulijaa upendo wa hali ya juu, upendo ambao kwangu mimi niliuona
dhahiri ni maalum kwa ajili yangu. Nilimuamini sana mume wangu tangu
aliponitamkia miezi kumi na nane iliyopita kwamba ananipenda na
angependa tuoane.
Naikumbuka vizuri sana siku nilipokutana na mume wangu, ni siku ambayo
kamwe sitakuja kuisahau katika maisha yangu, sijui nisemeje lakini
ninachoweza kukushirikisha wewe msomaji ni kwamba, huyu alikuwa ndiye
mwanaume wa kwanza kukutana naye na moyo wangu kulipuka katika penzi
zito lisilo na mfano.
Mwanzoni mwa maisha yetu ya ndoa, nilianza kuhisi jambo, kwani
nilianza kushuhudia ndugu wa mume wangu wakiwa ndio washauri wakuu wa
mume wangu. Nilijikuta kila mara nikiwa nimeachwa nje kwa kila jambo,
yaani nilikuwa sishirikishwi kabisa katika mambo muhimu ya kifamilia
jambo ambalo lilikuwa linaniuma sana.
Kwa kuwa mume wangu ana uwezo kifedha kwa kiasi fulani, amejikuta
akiwa amezungukwa na ndugu kiasi kwamba wao ndio wamekuwa wakimtegemea
kwa kila kitu mpaka kusomeshewa watoto, na wanahisi labda ndugu yao
angeweza kuwasaidia zaidi, kama sio uwepo wangu yaani kuolewa kwangu.
Nadhani hapo nyuma alikuwa akiwapa misaada mingi sana na huenda tangu
anioe kumetokea upungufu wa misaada tofauti na zamani kwa sababu ya
majukumu ya kifamilia ambayo hakuwa nayo hapo nyuma.
Katika kila ndoa kama mnavyojua kuna kutofautiana kimitizamo na
kukwaruzana kwa hapa na pale kitu ambacho hakiepukiki. Ila kitu
kilichokua kina ni sikitisha ni pale tu mwenzangu anapokua hajali
ushauri wangu na kufata ule wa ndugu zake.
Nilipokuwa najaribu kumshauri mwenzangu, anakuwa ni mkali kupindukia,
ilifika mahali nikajiona kama mtumishi wa ndani.
JUU YA KIDONDA UKAWEKWA MSUMARI WA MOTO
Nikiwa bado nasakamwa na yeye mwenyewe pamoja
na ndugu zake, na kama hiyo haitoshi mnamo Januari mwaka
huu nikampoteza baba yangu.
Ulikuwa ni msiba mzito sana kwangu, kwani, baba yangu alikua kama
ndiye baba wa mume wangu, ametusaidia sana walau kufikia hapa
tulipofika. Alikuwa ni baba mwenye busara sana na mwenye upeo wa hali
ya juu katika masuala ya kifamilia. Alikua akitatua matatizo yetu
mengi sana pale tunapokwaruzana na kutaka kusawazishwa ili maisha
yapate kuendelea.
wakati tunajiandaa na kumaliza 40 tangu baba yangu afariki, siku moja
akaja dada yangu kwa baba mkubwa ambaye ameolewa na mjomba wa
mume wangu. Dada yangu ambaye nilitarajia angekuwa upande wangu, alinitamkia bila kutafuna maneno kuwa wanafamilia ya mume wangu wamefurahi sana na pia
kufanya sherehe baada ya Baba yangu kufariki kwani sasa matakwa yao ya
mimi kuachika yatatimia, hakuishia hapo alitoa maneno mengi ya
kashfa dhidi yangu. Wakati wote mie nilibaki kimya nikiwa siamini kile
kinachotokea mbele yangu.
Baada kusema yale aliyosema na roho yake kuridhika aliondoka huku
akiendelea kunipiga vijembe. Nilibaki pale kwenye kiti kama
walivyonikuta nikitafakari juu ya kadhia ile….. Naam baada a
kutafakari mtiririko wa matukio yaliyopita kati yangu na mume wangu
tangu baba yangu afariki nilianza kuamini maneno ya ndugu zake. Kwani
tangu baba yangu afariki nilianza kuona mwenzangu anabadilika,
hanijali tena na alikuwa na majibu ya ovyo ovyo hata kama namuuliza
jambo la msingi. Nadhani alikuwa ananiheshimu japo kwa kiasi kidogo
kwa sababu ya kumuogopa baba, na kwa kuwa baba ameshafariki, sasa ni
nani nitamkimbilia ili kutaka kusawazishwa pale tutakapokuwa
tunatofautiana………..Nikajua sasa nimekwisha, nilijikuta nikitamka
maneno hayo kwa sauti, nilishtuliwa na sauti yake akinijibu, “ni bora
umelifahamu hilo mapema” hata sikujua aliingia pale ndani saa ngapi?
Hata sikumjibu, nilibaki kumwangalia tu kisha nikaguna, niliingia
chumbani na kujitupa kitandani, ambapo nilipitiwa na usingizi mzito.
Nilishtuliwa na mwenetu pekee wa kiume ambaye ndio alikuwa ametimiza
miaka 6, alikuwa amerudi kutoka shule. Niliamka na kumkumbatia
mwanangu huku machozi yakinitoka. Mwananu alishtuka na kuniuliza,
“mama unalia?” Nilimdanganya kuwa nimemkumbuka babu yake, yaani baba
yangu, mwanangu aliniambia pole na nilimuona dhahiri na yeye akiwa
amegubikwa na uso wa huzuni.
Sikujua kwamba ule ulikuwa ndio mwanzo wa Segere, kwani baada ya
kumaliza 40 ya baba siku kama ya 5 hivi, nakumbuka ilikuwa ni Februari
18, 2011, ulizuka ubishani kati yangu na mume wangu ambao ulizua mzozo
mkubwa tu. Nilijikuta nikapandwa na hasira na kumbwatukia yale maneno
yote niliyoambiwa na ndugu zake.
Mwenzangu katika hali ya taharuki alikasirika sana na nilishangaa
kumuona akichukua baadhi ya nguo zake chache na vyeti vyake akatia
kwenye gari na kuondoka zake, kwa kuwa ilikua usiku wa manane
nikampigia mama mkwe simu kumueleza, maana lolote laweza tokea. Kwa
ufupi mama hakuchukua hatua yeyote ile, na wala hakuja kwangu kujua
sababu ya mume wangu kuondoka katika mazingira ya kutatanisha.
Hata hivyo nililala nikijipa moyo kuwa huenda atarudi kwani alikuwa
amekunywa pombe kidogo, na labda kutokana na hasira na ndio maana
akaamua kuondoka, ingawa jambo lile kwa kweli lilinishtua kwa sababu
tangu tumeoana haijawahi kutokea tukatofautiana kiasi cha mume wangu
kuikimbia nyumba yake. Ndugu msomaji labda unaweza ukashangaa
nikikueleza kwamba mpaka leo hii ambapo ndoa yetu inatimiza miaka 8
sijamtia machoni mume wangu.
Juhudi za kumsihi mama mkwe atusuluhishe zimegonga mwamba kwani
alinitamkia waziwazi kwamba amemchukua mtoto wake na anaishi naye
nyumbani kwake mpaka hasira zitakapo muisha! Alienda mbali zaidi na
kudai kwamba haoni sababu ya kukaa kikao maana hakuna mtu katika ukoo
wangu ambaye wanaweza kumuita na kuongea naye!
Kauli hiyo iliniuma sana. Nilijiuliza, hivi ina maana mimi kufiwa na
wazazi wangu hakuna ndugu yangu anayestahili kuthaminiwa na ndugu wa
mume wangu? Je ina maana hata yale maneno waliyonieleza kuwa
wamefurahia baba yangu kufariki ni kweli?
NAJIULIZA!
Je nifanyaje? Nianze mchakato wa kudai talaka ili niwe huru? Kwa kweli
sina uhakika hata kama tukisuluhishwa sidhani kama tutaweza kuishi kwa
amani, maana kuishi na mtu huku ukiwa unajiuliza je tukigombana
ataondoka tena? na hiyo kama ataondoka nitakuwa na hali gani? mgonjwa?
sina kazi? sina uwezo wa kutunza mtoto? Maswali ni mengi kwa kweli.
Jambo hili linaniumiza sana maana nilijua nimekwisha pata asilimia
kubwa ya vitu ambavyo nilikua navihitaji katika maisha kwa mfano
tayari nimeshapata mume, mtoto, kazi nzuri kwa hiyo nilichokua nawaza
ni maisha ya kiroho, lakini sasa imenilazimu nirudi tena kujipanga
upya.
Dada Yasinta nimeona nikutumie mkasa wangu huu ili kuwashirikisha
wadau wa kibaraza chako cha MAISHA NA MAFANIKIO, kibaraza ambacho mimi
ni msomaji mzuri na nimekuwa nikifuatilia mijadala mingi unayoiweka
hapo ambayo inawavutia wasomaji wengi ambapo maoni na michango
inayotolewa ni darasa tosha.
Ni imani yangu wasomaji wa kibaraza hiki watatumia busara zao na kutoa
maoni na mitizamo yao kwa uhuru na haki bila kupendelea upande wowote.
Sikueleza hayo hapo juu ili kujidhalilisha, bali kutaka kupata
suluhisho ya kile ambacho nakabiliana nacho nikiamini kwamba sisi kama
binaadamu kuna wakati tunahitahi ushauri kutoka kwa wenzetu ili tumudu
kukabiliana na changamoto za maisha.
Natanguliza shukrani zangu za pekee kwako na kwa wadau wote wa Blog
popote pale Duniani.

Ni mimi msomaji wako.
Dada Gly

Saturday, June 18, 2011

Erik Klaesson; kinda wa Tanzania aliyeko Sweden

Erik akiwa uwanjani na mpira


“Soka letu linaumwa. Kwahiyo vijana wadogo kama hawa ni tiba kubwa ya soka letu, tuwekeze kwao.” Haya ni maneno ya Waziri wa Habari na Michezo, Dk Emmanuel Nchimbi wakati akizindua michuano ya Copa Cocacola mwaka huu katika uwanja wa Karume jijini Dar es salaam.
Wakati akizungumzia vijana hao ambao walidhihirisha kwamba nchi yetu imejaliwa vipaji vingi sana vya soka, ndipo upesi nilimkumbuka kijana mdogo kabisa Erik Klaesson, ambaye amejaliwa vipaji vingi maishani mwake, ikiwemo soka.
Ukimtazama umbile lake unaweza kumfananisha na aliyekuwa kiungo mahiri wa Pamba ya Mwanza, Simba ya Dar es salaam na Taifa Stars, Hussein Amani Masha.
Lakini sura yake inakuvuta na kumfananisha na beki mahiri David Luiz wa Chelsea ya England. Erik Kalesson anafanana na beki huyo Mbrazil kutokana na kuwa na nywele nyingi (Afro) ambapo mwandishi wa makala haya anamwita jina la utani, Ras Erik (kwa lugha ya Kiswidi, tamka Irik).
Bila kujali umri wake, anachokuambia kijana huyu utabaini kuwa amejengwa katika misingi imara ya soka. Nilimuuliza juu ya wanasoka mahiri wa Sweden, alisema, “nilipenda kumwangalia Henrik Larsson akicheza hapa Sweden, lakini amezeeka na sasa tunamtazama Zlatan Ibrahimovich, nami nimfikie.”
Anaongeza kwa kusema, “nawapenda Robinho, Cristiano Ronaldo, Lionel Messi na Zlatan. Nataka kuwapiku”
Erik Klaesson mapema Jumanne katikati ya wiki alikuwa kwenye mechi za watoto kati ya timu yake ya IFK Skoghall dhidi ya timu ya Norrstrands IF Rod, zote za Sweden.
Uwezo wake kumiliki mpira ni mkubwa kulingana na umri wake. Anaweza kucheza kwa ufasaha beki wa kushoto na kiungo nambari 10. Hii ni kutokana na kasi, chenga na ujuzi wake unaojitokeza tangu akiwa kinda.
Harakati zake za kucheza soka zinamfanya kuwa na ndoto za kuchezea klabu mashuhuri AC Milan ya Italia. Kinda huyu anaeleza wazi hisia zake kwamba hapendi kucheza soka la kulipwa nchini Sweden anakoishi sasa, kwani amepania kucheza nje ya nchi hiyo. Na mawazo yake yanaelekea kucheza ligi kuu ya Italia maarufu kama Serie A, pindi umri wake utakaporuhusu.
“napenda kucheza je ya Sweden hasa Milan. Kama nitaanzia hapa Sweden basi nitachezea timu ya Malmo, naipenda sana,” anasema Erik.
Mwandishi wa makala haya alimuuliza Mama yake, Yasinta Ngonyani juu ya kinda huyo kuchagua timu ya taifa kati ya Sweden au Tanzania.
Naye bila kusita alisema, “Binafsi napenda miaka ijayo achezee Tanzania. Lakini ni ngumu kwa sasa kuzungumzia kwani ana vipaji vingi. Kwa mfano ana kipaji cha kucheza Floorball na Fiddle.”
Hata hivyo aliongeza kwa kusema, “Yeye (Erik) atachagua ni timu gani anataka kuchezea kati ya Tanzania na Sweden, akitaka ushauri wetu atapata, nadhani unajua nipo upande gani hapo.”
Suala hili na wimbi la makinda wengi kukumbwa na tatizo la kuchagua nchi za kuchezea linaendelea kushamiri huku baadhi yao wakiwa na mabadiliko ya uamuzi kulingana na hali halisi inayowatokea wanapochezea nchi fulani.
Kwa mfano mshambuliaji wa klabu ya Sevilla ya Hispania Frederick Kanoute aliichezea timu ya taifa ya vijana ya Ufaransa, lakini aliamua kuacha kisha kuchezea timu ya taifa ya wakubwa Mali, ambako ni asili ya wazazi wake.
Mwingine ni Danny Wellbeck ambaye anachezea timu ya taifa ya vijana ya England na ameshachezea timu ya wakubwa ya nchi hiyo kwenye pambano la kirafiki dhidi ya Denmark. Hata hivyo anaweza kuchagua kuchezea England au Ghana.
Wengine ni Kevin-Prince Boateng ambaye alizaliwa Ujerumani na kuamua kuchezea Ghana ambako wametokea wazazi wake, pia nduguye Jerome Boateng aliamua kuchezea timu ya taifa ya Ujerumani badala ya Ghana.
Lakini kwa upande wa kinda huyu Erik Klaesson moja kwa moja anaweza kuiwakilisha Sweden kutokana na uraia wa kuzaliwa na baba yake, lakini anaweza kufanya uamuzi wa kuchezea Tanzania kutokana na asili ya mama hivyo kuukana uraia wa Sweden.
Uwezekano wa hili la pili ni mkubwa kwakuwa Erik Klaesson amekuwa akiwasili nchini mara kwa mara ndipo ndoto ya kuanzisha timu yake pindi akistaafu soka, ilipoanza kumea. Na vilevile msukumo wa baba yake ambaye ni mpenzi mkubwa wa Tanzania na amekuwa akimweleza kijana huyo umuhimu wa nchi hii.

Akizungumzia, mawazo ya mwanaye miaka ijayo alisema, “huwa anasema anataka kuanzisha timu yake Tanzania pale atakapokuwa mkubwa na ana ndoto nyingi nasi tunazifuata.”
“kuna kipindi alikuwa akienda sana kwenye mazoezi ya Fiddle, lakini akatuambia akili yake inafikiria mpira wa miguu 100% na anahitaji msukumo wetu.”
“nina hamu sana kumwona (Erik) akicheza mpira wa miguu hata kama hatavaa jezi za AC Milan kama anavyoazimia, muhimu ni kucheza mpira wa kulipwa nje ya Sweden, nasi tunakubali hilo.” Anasema Torbjorn Klaesson, baba wa Erik.
Akaongeza kusema, “nikimtazama mtoto huyu (Erk) naamini atakuwa moto wa kuotea mbali, kwanza anabidii, utulivu wake na uwezo wake anapokuwa na mpira. Walimu wake wananiambia subiri matunda kwa kijana wako muda si mrefu.”
“napenda mpira kupita kiasi, na Sweden unajua tunavyompenda Henrik (Larsson) tangu akicheza Glasgow Rangers kule Uskochi (Scotland) na baadaye Barcelona kule Hispania na kidogo Manchester United. Alikuwa na uwezo mkubwa na anajituma, nami sikujua kama nitapaja kijana mwenye kipaji cha soka, lakini naambiwa nivute subira, namuunga mkono,” anasema Torbjorn Klaesson
Alipotokea Erik Klaesson
Kinda huyu kwa sasa ana miaka 11. Alizaliwa tarehe 3/6/2000 nchini Sweden. Ana kipaji kikubwa cha kucheza soka, na michezo mingine kama floorball /innebandy.
Kama tulivyoona hapo mwanzo, baba yake ni Torbjorn Klaesson, raia wa Sweden na mama yake ni Yasinta Ngonyani, ambaye ni Mtanzania na mzaliwa wa Songea mkoani Ruvuma.
Jambo moja kubwa ni kwamba baba wa kijana huyu anapenda mila na desturi za Mtanzania, na hana shaka juu ya mwanaye endapo atachagua kuwakilisha Taifa Stars miaka ijayo.
Kutokana na yeye kuishi na kufanya kazi kwa muda mrefu hapa nchini, suala ambalo anatoa kipaumbele kwa kijana wake ni kumhimiza kutimiza ndoto zake.
Kwa sasa kinda huyu analelewa kwenye kikosi cha timu ya IFK Skoghall ya Sweden ambako anajifunza mambo mengi kuhusu soka. Ni umri huu ndiyo unakuwa tiba kwa wanasoka mahiri ulimwenguni, hivyo kauli ya Waziri wa Habari na Michezo, Dk Emmanuel Nchimbi kuhusu kuwalea vijana inatakiwa kuungwa na mkono.
Kwani tayari tunaye kinda Erik Klaesson mwenye asili ya Tanzania anayekuja juu kisoka aliyeko nchini Sweden. Kazi kwao TFF.
Na Markus Mpangala, shukrani nyingi zikufikie.Gonga hapa kumsoma habari zake nyingie Nyasa na hapa .

Friday, June 17, 2011

NIMEUKUMBUKA MKAO HUU:- KUKAA PAMOJA FAMILIA NZIMA KWA KUJUMUIKA KULA!!

Picha hii imenikumbusha enzi zile miaka arobaini na saba familia nzima inajumuika pamoja na kushika chakula iwe cha asubuhi, mchana au jioni. Hakika hii ilikuwa safi sana. Ila hapa naona watatu wanatumia vijiko na mmoja anatumia mkono... Halafu unajua kitu kimoja ukishazoea kula chakula mkiwa wengi huwa kinanoga sana kuliko kula peke yako...je wewe nawe umekumbuka nin? IJUMAA NJEMA NA UKIPATA NAFASI KULA NA JIRANI YAKO AU RAFIKI.

Thursday, June 16, 2011

Thankfulne​ss

Be thankful my dear,
Always learn to thank them.

People will ignore you,
Be happy when thanking them.

When people do hurt you,
Make sure you thank them.

They'll then satisfy you,
Don't forget to thank them.

Love has to disappoint you,
Be happy and thank it.

And when people do admire you,
It's when you always thank them.

Then, after reading this poem,
Happily say, THANK YOU!
SHAIRI HILI NIMETUMIWA NA MTANI WANGU MSHAIRI MTANGA nikaona si vibaya kama nikiweka hapa ili nanyi mpate chochote. AHSANTE!!

Leo tuangalie Historia ya nchi yetu ya Tanzania!!!


TUKUTANE TENA MUUMBA AKITUJALIA!!!

Wednesday, June 15, 2011

NDOA YA MALAIKA HAIJAWAHI KUWEPO DUNIANI!!!

Kama kawaida leo ni jumatano ambayo ni siku ya kile KIPENGELE CHETU CHA MARUDIO haya karibuni tujumuike nami!!!!!





Wakati mwingine misukosuko ya ndoa huwaliza wanawake,


lakini hizo zote ni changamoto !


Kuna kudanganyana kwingi kuhusu ndoa pale mtu anaposhindwa kuwa mwangalifu sana kwa kauli za wengine walio kwenye ndoa. Hii hutokana na ukweli kwamba kuna kujumuisha kwingi sana. Kuna wakati huwa tunasikia au kuambiwa kwamba ndoa ni sawa na jehenamu. Baadhi ya watu walio kwenye ndoa kuna wakati huzungumza kwa njia ambayo hutufanya tuamini kwamba kuoa au kuolewa ni jinai. Ndoa ni ujinga mtupu haina maana, mtu anaweza kusema. Wasemaji hawa wanaweza kuwa ni watu tunaowaamini sana kama wazazi wetu na wengine wa aina hiyo.
Baadhi ya watu badala ya kuponda na kubeza kuizungumzia kama kitu kizuri sana kisicho na doa wala chembe ya usumbufu. Inawezekena kabisa nasi tukawaamini wazungumzaji hao, hivyo kuamini kwamba, ndoa hazina usumbufu.
Inawezekana dhana hii ikaingizwa vichwani mwetu wakati tukiwa wadogo au hata tukiwa watu wazima. Hebu fikiria juu ya mtu ambaye anajisifu kwamba ndoa yake haina hata chembe ya mkwaruzo. Ambaye anaieleza ndoa yake kwa njia yenye kushawishi kuwa, kumbe ndoa zenye matatizo siyo ndoa bali kisirani kitupu. Kama nawe uko kwenye ndoa na ndoa hiyo ina matatizo hata madogo unaweza kudhani kwamba ulikosa kuoana na huyo mwenzako. Dhana hiyoinaweza kuchipuka kutokana na kauli kama hiyo inayoelezea ndoa kama kitu kisicho na mikwaruzo hata kidogo.
Kama usipokuwa mwangalifu unaweza kuacha kuchukua hatua za kujaribu kuondoa tofauti zilizo kwenye ndoa yenu. Utaacha kufanya hivyo kwa sababu mtu fulani atakuwa tayari ameingiza kichwani mwako uongo kwamba ndoa ni “asali” na “maziwa” matupu. Ni uongo kwa sababu hakuna ndoa isiyo na mikwaruzo.
Tunatakiwa kujua kwamba lengo la ndoa siyo kuepuka kukorofishana , hapana . Ukweli ni kwamba kukorofishana kunapotumiwa vema huweza kujenga uhusiano mzuri na imara sana. Kwa sababu kukorofishana hakuwezi kuepukika kwenye ndoa kunatakiwa kutumika kama shule na dawa ya kuimarisha ndoa.
Bila kukwaruzana kwenye ndoa zetu inaweza ikawa vigumu sana kwetu kubandua tabaka la uongo lililotufunika ambalo humfanya kila mmoja kati yetu kushindwa kuona na kumfahamu mwenzake katika tabia yake halisi.
Bila kukwaruzana, kila mmoja wetu atajidanganya kwamba anamfahamu mwenzake kama alivyo wakati siyo kweli. Tunapokwaruzana tunapata nafasi ya kufahamiana vizuri katika hali halisi.
Mwanamke mmoja maarufu aliwahi kuulizwa kama huwa anakwaruzana na mumewe. Alikiri kwamba huwa wanakwaruzana kwa kusema , “ndiyo tunakwaruzana, vinginevyo tungekuwa hatuna tofauti, na hapo bila shaka ndoa na maisha vingekuwa vimepooza sana”. Huo ndiyo ukweli wenyewe, kwamba bila kukwaruzana hatuwezi kufahamiana vema na kujua kwa undani tofauti kati yetu na wenzetu.
Inabidi tujue kwamba hakuna binadamu aliyekamili, yaani asiyekosea, kama ilivyo dunia yenyewe. Kwa hali hiyo hakuna ndoa ambayo haina makosa, kwa sababu ndoa ni binadamu hao ambao siyo kamili. Kwa hiyo, mtu anapotarajia kuwa au kuishi kwenye ndoa isiyo na kukwaruzana, ni sawa na mtu huyo kutarajia kukutana na binadamu ambaye ni kamili, yaani asiyekosea.
Kutarajia kuwa na ndoa ambayo haina kukwaruzana kunaelezwa kuwa ni chanzo kizuri sana kwa ndoa nyingi kulegelege au kuanguka kabisa. Mtu anapoingia kwenye ndoa akitarajia kwamba huko hatapambana na maudhi au kero za aina fulani, ni lazima ajue kwamba, hatadumu kwenye ndoa yake kwa sababu ndoa hiyo anayoitarajia haipo.
Mtu ambaye hakubali au angalau hataki kuelewa kwamba, ndoa ni lazima iwe na mikwaruzo anaweza kukabiliwa na tatizo lingine baya zaidi kwenye ndoa yake. Kwa kutokujua au kuepuka kukwaruzana, hawezi kuwa tayari kukubali kujadili migogoro ya kindoa ili kupata ufumbuzi. Hawezi kulikubali hilo kwa sababu haamini kwamba ndoa yenye kukwaruzana ni ndoa.
Wakati mwingine rafiki, ndugu au jamaa zetu hutusimulia jinsi ndoa zao zisivyo na kukwaruzana kama kwamba ni za malaika watupu. Bila kujua, huwa tunajikuta tumewaamini. Tunapowaamini huwa tunachukulia kukwaruzana kuliko kwenye ndoa zetu kama jambo au kitu ambacho hakikutakiwa kuwepo. Hapo hujikuta tukitamani kuondoka kwenye ndoa hizo kwa matarajio kwamba tunaweza kukutana na “malaika” ambao tutajenga nao ndoa zisizo na doa.
Hata pale ambapo tunasema wanandoa wanapendana sana, bado ndoa yao ni lazima itakuwa na kukwaruzana. Lakini wanachofanya hawa na ambacho huenda wengine hawafanyi ni kujadili tofauti hizo sawia na kuamua kuzisahau na hapo wote kukubali kujifunza kutokana na tofauti hizo.
Wale walio tayari kujadili tofauti zao sawia ndiyo ambao ndoa zao huwa na afya sana hadi wengine kushangaa kama siyo pamoja na kuona wivu. Wale wanaodhani ndoa ni mahali pa kila jambo kwenda kama mtu atakavyo, ndoa zao hupogoka vibaya na kufa kwa kishindo........

Makala hii nimeitoa katika Gazeti la Jitambue la hayati Munga Tehenan.

TUONANE TENA JUMATANO IJAYO PANAPO MAJALIWA!!!

Tuesday, June 14, 2011

CHANGAMOTO YA LEO:-PICHA ZA MICHORO! JE? UNAWAFAHAMU/UNAMFAHAMU KATI YA MMOJA WAO AU WOTE?




Je hii/huu mchoro wa kwanza ni nani hapa?


Na je? katika mchoro huu ni nani?
Katika michoro hii miwili kuna kitu ambacho kinaleta uhusiano fulani. Je? unajua ni nini au ni kipi? karibuni tutafakari pamoja.

Monday, June 13, 2011

SHUKRANI ZANGU KWA WALEZI/WALIMU

Leo napenda kutoa shukrani zangu za dhati kwa WALEZI/WALIMU kwa kazi kubwa waifanyayo. Sijui kama wewe mwenzangu umewahi siku moja kufikiria ya kuwa hakuna mlezi/walezi wazuri kama walimu. Fikiria mtoto aanzapo chekechea, unampeleka huko chekechea/”shule ya Vidudu” na wewe mwenyewe unaenda kazini na baadaya ukishamaliza kazi unaenda kumchukua.
Na unakutana mtoto mwenye furaha tele kabisa. Na pia inawezekana baada ya muda mtoto atakuwa kamzoea zaidi mwalimu kuliko hata wewe na mwalimu atamfahamu zaidi mwanao kuliko wewe/mimi mwenyewe.
Nimejaribu kufikiria sana, sisi wazazi jinsi tulivyo na muda mchace sana kuwa na watoto wetu. Je? wewe pia umefikiria hili? Yaani hapa unaweza kusema walimu wa chekechea wao ndio wazazi kamili. NA INAWEZEKANA HATA KUANZA KUTEMBEA NA HATA KUSEMA MANENO YA KWANZA ANAANZIA HUKOHUKO CHEKECHEA.
Kwa kweli mnastahili PONGEZI WALIMU.
Na baada ya miaka ya kuanza shule ifikapo, hapo ndio inakuwa pia mtoto anaondoka asubuhi kwenda shule. Muda wote anakuwa na MWALIMU/WALIMU. Na mwalimu/walimu ndiye/ndio wamleao kwa asilimia kubwa. Kwani anakuwa muda mwingi san ana mtoto /watoto wako/wetu kuliko sisi WAZAZI. Nimejaribu kufikiria kwa mfano mimi mwenyewe binafsi, mara nyingi tunaagana asubuhi na halafu tutaonana tena kesho alasiri nirudipo katika mihangaiko yangu . Na kwa wengine huwa hawakutani kabisa na watoto asubuhi. Kwa vile labda baba au mama anahitajika kuwahi sana kazini, na anaporudi jioni watoto wanakuwa wamelala na kesho yako hivyo hivyo huondoka kabla watoto hawajaamka.


Kwa hiyo mimi kama mzazi napenda kutoa shukrani zangu kwa WALEZI/WALIMU WOTE KWA KAZI NZURI MUIFANYAYO. MAANA MNASTAHILI KWA KWELI. AHSANTENI SANA!!!!

Sunday, June 12, 2011

JUMAPILI NJEMA NDUGU ZANGUNI!!!!!!!


Nawatakieni jumapili njema kwa wimbo huu maana umenikuna kweli kweli na nimeusikiliza mara elfu na elfu...
IMANI NA UPENDO WA MWENYEZI MUNGU UTAWALE NYUMBANI MWENU !!

Saturday, June 11, 2011

UJUMBE WA JUMAMOSI YA LEO !!!

Upendo/Mapenzi unaponya/yanaponya watu , wote wnaotoa na wanaopokea.
NAWATAKIENI JUMAMOSI NJEMA!!!!

Friday, June 10, 2011

Picha ya Ijumaa ya hii-: Huyu ndiye ombaomba Maarufu MATONYA

Picha hii imenikumbusha kila Ijumaa mjini Songea kuna kuna mtindo huu watu kuja kuomba...sijui kama wewe umewahi kuwaona? HAYA IJUMAA NJEMA NA MWANZO MWEMA WA MWISHO WA JUMA!!!!

Thursday, June 9, 2011

Swali la leo:- CHANZO CHA UKOO NI NINI?

Swali langu la leo nimeenda hadi Upareni na kurudi...Nikimaanisha litawalenga hasa ndugu zetu WAPARE. Ila nitaanza na mifano miwili ambayo ni zoefu kwangu:-
Nilipokuwa msichana mdogo nakumbuka niliwauliza wazazi wangu kwa nini twaitwa NGONYANI na ni nana alianzisha na pia kwa nini karibu majina mengi ni ya wanyama? Sikumbuki kama nilipata jibu.
Baadaye nikawa msichana mkubwa na nikaanza maisha na nikaanzia maisha yangu kuishi na WABENA. Kwa kweli walibifanya UDADISI/UKAPULYA wangu uzidi. Kwa vile wao U-KOO wao unaanza na M, mfano:- Mwageni, Mgaya, Mbilinyi, Mgina nk.
Lakini hata hivi si WABENA tu ambao wanaanza na M. Na hili ndilo ambalo lilikuwa kiini cha swali langu zaidi ndugu zetu WAPARE... Yaani koo kama za KIPARE:- Kwanini zinaanza na M?. Mfano MSUYA, MMBAGA, MZIRAYI, MFINANGA, MSHANA,MCHOMVU ......NK. Nina uhakika hapa nitasaidiwa. TUKUTANE TENA WAKATI MWINGINE:-

Wednesday, June 8, 2011

MSAADA: RENATHA BENEDICTO ANATAFUTWA NA FAMILIA YA MUBELWA BANDIO!!!

Hapa ni bibi na bwana Bandio


Ndugu. Kwa mara nyingine nawakilisha ombi la kunisaidia kutangaza (wakati wowote upatapo nafasi) kuhusu Dada mdogo RENATHA BENEDICTO ambaye tumepoteana kwa takriban miaka 12 sasa.

Renatha alikuwa mwanafunzi wa shule ya Sekondari Kibasila jijini Dar kati ya mwaka 1998 - 2001 na baada ya hapo alienda Songea TTC kujiunga na masomo ya ualimu. Pia alikuwa kati ya wahanga wa ajali mbaya ya Tawfiq iliyotokea tarehe kama ya leo mwaka 1999 ambapo alikuwa msaada mkubwa saana kuokoa maisha yangu. (Maelezo kamili yako http://changamotoyetu.blogspot.com/2009/04/namtafuta-renatha-benedicto.html)

Niliwasiliana naye kwa miaka miwili iliyofuata mpaka alipoenda chuoni Songea nami nikaondoka nchini mwaka 2003 na kwa miaka mingi sasa nimekuwa nikijitahidi saana kumtafuta bila mafanikio. Naomba kama anaweza kusoma ama kuna anayesoma na kumfahamu anisaidie kuwasiliana naye.
Email yangu ni changamoto@gmail.com

NATANGULIZA SHUKRANI

http://www.changamotoyetu.blogspot.com/
http://www.youtube.com/user/mutwiba

USAFIRI WA NDEGE TOKA DAR ES SALAAM KWENDA SONGEA UMEANZA LEO

Habari hii imenipa furaha sana kwa kweli. Na nikaona si mbaya kama ikiwa katika kipengele chetu cha MARUDIO YA JUMATANO. Katika utembezi wangu pia kama wengine waniitavyo KAPULYA basi nimeipata habari hii JIFUNZE KUSINI.


Ndege ndogo zinatua katika kiwanja hiki cha Ruhuwiko Songea Ruvuma

Na ndege kubwa pia zinatua katika uwanja huu,Songea ina uwanja mzuri wa ndege,ila bahati mbaya ni ndege za viongozi ndizo zinazo tua hapo,sasa imekuwa bahati kampuni hii imeamua kuanzisha huduma hiyo ya usafiri.


Maneja wa uwanja wa ndege Songea Bwana Valentine Fasha mwenye tai nyeusi akiwa na mfanyakazi mwenzake wakati Rais Kikwete akiwasili uwanjani hapo juzi.
KAMPUNI ya ndege ya Air Indigo imeanza safari zake Leo,toka Dar es salaam kwenda Songea,ambapo toka juzi abiria kutoka Dar es salaam kwenda Songea walikwisha jaza ndege inayoweza kuchukua abiria 25.
Meneja wa uwanja wa ndege wa Songea Bwana Valentine Fasha aliiambia blog hii uwanajani hapo kuwa nauli ya kwenda na kurudi ni Tanzania shilingi 400,000/=,pia alisema usafiri wa ndege utakuwa wa siku mbili Juma tatu na Ijumaa.
Alisema kuwa booking ya safari inafanyika hapo hapo Air port kwani kwa muda huu hawana na ofisi ya kukatia tiketi mjini Songea.Hizo ndizo habari njema kwa wakazi wa Songe,na wilaya zake.

Monday, June 6, 2011

Mungu wa Kimasai adhaniwaye kuwa na nyuso mbili


NI pembezoni mwa jiji la Nairobi, Kenya, watu wa kabila hili wametengeneza duara, mmoja anaimba kwa sauti ya mtetemo mfano wa zeze na wengine wanaitika kwa sauti mchanganyiko nyembamba na nzito, kisha mmoja mmoja anaingia kati na kuruka juu akiwa amenyooka mithili ya nguzo.

Shuka zao zenye mchanganyiko wa rangi zinasalimu amri kwa kupepea kila warukapo juu, hali kadhalika vito vyao miguuni na mikononi hata shingani vinatoa sauti na kutengeneza mapigo kama ya ala za muziki. Hao ni Wamasai, watu wanaosifika ulimwenguni kote kwa kutunza tamaduni zao.
Zimekuwepo dhana na hadithi mbalimbali kuhusu mila na taratibu zao, baadhi zimesifiwa, nyingine zimekuwa zikipigwa vita na baadhi yake zinashtusha na kuacha simulizi la kushangaza.

Lakini, ukweli unabaki palepale kuwa kabila hili ni kivutio kwa wengi na ni miongoni mwa machache yaliyoweza kuhifadhi na kuheshimu mila zao, licha ya maendeleo ya sayansi ya teknolojia.
‘Enkai’ au Mungu wa Kimasai
Wao huabudu, wanamwabudu mungu mmoja, ‘Enkai’ au Engai ambaye si mwanamke wala si mwanaume. Lakini, mungu huyu amegawanyika katika sura mbili tofauti, upande mweusi(engai narok) na mwekundu(engai nanyokie). Upande mweusi ni mwema na wenye upendo na mwekundu ni wa kishetani na usio na chembe ya huruma.

Wanaamini kuwa, sauti ya radi ni dalili ya pande mbili za ‘Enkai’zikigombana, ambapo upande mweusi unataka kutoa mvua kwa ajili ya mifugo na watu, na upande mwekundu unataka mvua isinyeshe na wamasai pamoja na mifugo yao wapoteze maisha.

Wanaume husuka, wanawake hunyoa vipara
Kimila, wanawake kunyoa vipara na wanaume kusuka rasta ni baadhi ya taratibu za kipekee kwa kabila hili, si hivyo tu, bali wanawake ndiyo hujenga nyumba ya familia, tofauti na makabila mengi ya Afrika Mashariki ambapo wanaume wanawajibika katika ujenzi wa nyumba na wanawake wakiwa na jukumu la ulezi na si ujenzi.

Dhana ya kuchomeka mkuki
Imekuwepo hadithi ya kwamba, mwanamke wa Kimasai anamilikiwa na ukoo wote, kwa hilo, kila mwanaume hushiriki kitanda na wanaume wengine.
Anachofanya ni kuchomeka mkuki mbele ya nyumba (boma) na kisha kuendelea na shughuli iliyomfikisha mahali pale.
Hivyo basi, yeyote atakayekuja na kukuta mkuki huo mbele ya nyumba, hatakiwi kuingia ndani, bali kusubiri, na kuwa mvumilivu. Wivu hautakiwi kwao.

Kwa mujibu wa Simeon ole Serere, dhana hiyo ipo mbali na ukweli, kwani, mkuki huo unamaanisha kujisalimisha na hana nia ya kudhuru, hivyo mwenyeji atakaporejea asiwe na shaka kwani silaha ipo nje.

Laana ya kukata misitu
Hadi leo, Wamasai wamezungukwa na mimea katika mazingira yao, kwa mfano kuna msitu karibu na kijiji cha Mau unaoitwa Medung’i, ukimaanisha ‘Maa’ yaani ‘ usikate’. Inaaminika kwamba, ukikata miti katika eneo hilo, damu itatiririka kutoka humo na kukulaani.
“Mila hizi ndizo zilizowezesha uoto asilia kustawi katika mazingira yetu, tumeweza kuhifadhi Masai Mara, Amboseli na hifadhi za wanyama za Serengeti kwa kuwa hatuli wanyama pori,” anasema ole Kulet, mwandishi wa riwaya nane kuhusu mila za Wamasai.

Hakuna kilio, wala hisia za maumivu
Vijana wa Kimasai wanapofikia umri wa kubalehe, hutakiwa kupitia hatua ya tohara, hii huwajumuisha vijana wote wenye umri wa miaka 12 hadi 25. Kitendo hicho hufanyikaa bila ganzi na inasemekana kuwa wakati wa tendo hilo hutakiwi kulia au hata kukunja sura kuonyesha unahisi maumivu, kwani kufanya hivyo kunaonyesha udhaifu na ni aibu kwa ukoo wako.

Lakini pia, kutikisika au kukunja sura kunaweza kusababisha makosa katika ukataji wa ngozi ya uume na kusababisha kovu la kudumu au kilema cha aina yoyote ile.
“kupona kunachukua miezi mitatu hadi minne, kipindi ambacho vijana hupata shida kujisadia haja ndogo huku kukiambatana na maumivu makali. Vijana hao hutakiwa kuvaa mavazi meusi kwa kipindi cha miezi minne hadi minane,” anasema Laizer Selelii, mlinzi katika ghala moja la mazao jijini Nairobi.

Wanawake pia hufanyiwa tohara au emorata tendo hilo limekuwa likipingwa vikali na wanaharakati na wanawake ambao wamefanyiwa, kama Agnes Pareiyo.
“Usipofanyiwa tohara unaweza kukosa mume, ni kitendo kinachochukuliwa kama cha thamani na sifa kwa mwanamke, wakati mwingine, mahari yako huweza kuwa ni ng’ombe wachache kama usipopitia hatua hii,” anasema Pareiyo. “Lakini, madhara yake ni makubwa wakati wa kujifungua.”

Uchumba wa mimba
Inasemekana kuwa, wanaume wa kimasai huchumbia mimba na kuitolea mahari endapo mtoto atazaliwa wa kiume mahari ile hurudishwa.
Mila hii ndiyo inayosababisha mabinti wa kabila hili kuolewa wakiwa na umri mdogo wengine hata miaka kumi hadi kumi na mbili.
Ole Serere, anasema, suala la wao kuchumbia mimba lilikuwepo zamani ingawa sasa halifanyiki sana.Anakiri kuwa, mabinti wa Kimasai huchumbiwa wakiwa na umri mdogo kwa sababu hawaendi shule.

Ung’oaji wa jino la chini
Utafiti uliofanywa mwaka 1991/92 na kuhusisha watoto tisini na tano wenye umri wa kati ya miezi sita na miaka miwili uligundua kuwa wameng’olewa meno ya chini.

Wakati wale wenye umri wa miaka mitatu hadi saba, asilimia 72 ya watoto 111 walionekana hawana jino moja au mawili ya chini.
Utafiti huo uligundua kuwa, meno hayo hutolewa kwa ajili ya kupitisha maziwa endapo mtu amekunywa sumu au anaumwa mahututi.
Baadhi yao wanasema, kitendo hicho hufanywa wakati wa utoto ili kuondoa meno hayo ya plastiki yenye minyoo ambao husababisha watoto kuharisha na kutapika.

Kutowazika maiti
Wamasai wanaamini kuwa kila binadamu ana malaika wake mlinzi ambaye mtu akifariki humbeba na kumpleka sehemu mbili kati ya hizi, aidha jangwani kama mtu huyo alitenda maovu au katika rdhi ya utajiri wa ng’ombe kama alitenda mema.

Hata hivyo, hawatamki hata siku moja kuwa mtu amefariki, kama ni mtoto husema amepotea na kama ni mtu mzima hutajwa kuwa, amelala.
Hawawaziki wafu, bali baada tu ya kifo,mwili hutupwa porini ili uliwe na fisi. Katu hawachimbi kaburi, kwani wanaamini ardhi imebarikiwa kwa ajili yao, endapo wataichimba watalaaniwa.

“wakati mwingine tunahama kabisa makazi ambapo mtu amefariki, kwani nyumba hiyo yote huwa na mizimu,” anaeleza Serere.
Katika miaka ya hivi karibuni, wameanza kubadilika, kwani sasa hivi hulima, hufanya biashara na wapo wasomi, wake kwa waume.
Hata hivyo, hiyo si sababu ya wao kuacha baadhi ya mila zao muhimu na zenye manufaa kwao. Bado wangali wamebeba fimbo na sime, kama alama ya ushujaa wao.
Na Florence Majani wa Gazeti la Mwananchi

Saturday, June 4, 2011

NAPENDA KUWATAKIENI JUMAMOSI PIA JUMAPILI NJEMA WOTE!! MUNGU WANGU WEWE WAJUA SABABU KWANINI NIYAPITIE HAYA....



Mungu ndiye muweza: Nawatakieni wote Jumamosi njema na pia jumapili njema na tuonane tena Mwanzo wa wiki:- UPENDO WA MWENYEZI MUNGU NA UWE NANYI WOTE.

Friday, June 3, 2011

HONGERA KWA SIKU YA KUZALIWA KWAKO ERIK !!!/Grattis på Födelsedagen Erik!!!

Hapa nilitaka kupiga mpira kwa kichwa....
...na hapa najaribu kumtia chenga huyu adui yangu..


Leo ni siku /tarehe ambayo kijana huyu alianza maisha yake. Yaani alizaliwa ni miaka kumi na moja iliyopita tarehe 3/6/2000 alizaliwa kijana Erik. Na leo anatimiza miaka 11. Kama mumuonavyo Erik anapenda sana mpira wa miguu, floorball /innebandy. Pia mziki pia. HONGERA KWA SIKU YAKO YA KUZALIWA ERIK NA UWE NA SIKU NZURI. PIA KILA LA KHERI KATIKA MASOMO YAKO, NA KATIKA MAISHA YAKO.!!!!!!!

Wednesday, June 1, 2011

TUONDOE SEHEMU ZA MIILI YETU ZILIZOKUFA.

Kupitia Jongoo huyu alijifunza kitu muhimu maishani


Mzee mmoja, Salim Keni wa Makongorosi huko Chunya mkoani Mbeya, anasema kuwa siku moja alishangazwa sana na kauli ya mtoto wake wa miaka kumi. Anasema alikuwa amekaa nje ya nyumba yake jioni. Hapo alipokuwa amekaa alikuwa akiangalia jongoo. Jongoo huyo alikuwa ameumia sehemu yake ya nyuma, ambayo sasa ilikuwa imekauka, yaani imekufa.

Sehemu ya mbele ambayo ilikuwa ni nzima iliunganishwa na sehemu hiyo ya nyuma au ya mkia kwa kiuzi kidogo sana. Tunaweza kusema kwamba sehemu hiyo ya mkia ilikuwa inakokotwa na ile ya mbele. Hali hiyo ilimfanya jongoo yule kupata shida sana ya kusogea. Ukweli ni kwamba, hata kama sehemu ile ya nyuma ya jongoo yule ingeondolewa wala asingebaini, kwani ilikuwa sio sehemu ya mwili wake tena-ilishapoteza uhai.

Lakini aliendelea kuikokota kama vile bado alikuwa akiihitaji. Wakati Mzee Salim akimshangaa jongoo yule, mtoto wake huyo ambaye ni mtundu sana alifika hapo, ambapo naye alimuona jongoo huyo.
Alikaa chini karibu na baba yake na kumkodolea macho kabla hajatoa kauli hiyo ya kushangaza. ‘Sasa baba, huyu mdudu si anapata shida bure, kwa nini asiache hii sehemu ya nyuma ili atembee vizuri, kwa sababu yenyewe imekauka…..’

Kabla baba yake hajajibu, mtoto yule alichukua kijiti na kutenganisha sehemu ya mbele na ile ya nyuma ya jongoo yule. Baada ya kufanya hivyo, jongoo yule aliweza kuongeza kasi ya kutembea na alionekana wazi kwamba amekuwa huru.

Mzee Salim alishikwa na butwa kwani hakuwa amepata muda wa kufikiri hivyo wakati akimtazama yule jongoo. Ni kweli kabisa, mtoto wake alikuwa amemfunulia kitendawili kikubwa sana cha maisha. Ya nini kutembea na sehemu ya mwili ambayo haina kazi, ambayo imekufa, ambayo angeweza kuiacha na kuwa huru zaidi?

Mtoto yule aliona wazi kabisa pamoja na akili yake ya kitoto kwamba, kama mdudu yule angemudu kuiacha sehemu ya mwili wake ambayo ilikuwa tayari imekufa angeweza kuishi katika uhalisia.

Uvumbuzi wa mtoto yule ni uzumbuzi wetu sote. Ni lini nasi tutaamua kuacha sehemu zetu ambazo zimekufa ili tuweze kuishi katika uhalisia? Sehemu zetu za miili zilizokufa ni zipi? Ni maumivu ya kimaisha yaliyopita. Ni mizigo ya mashtaka ya dhamira zetu na haja yetu ya kutaka kulipiza visasi. Ni masikitiko na majuto ya mambo yaliyopita, ambayo bado yanatuumiza hadi leo, mambo ambayo hayana maana yoyote tena kwetu.

Wengi wetu tunatembea au kuishi na mizigo mizito sana ya mambo yaliyopita, mambo ambayo ukweli ni kwamba hayana maana yoyote kwetu. Lakini kwa sababu tumeamua kutembea nayo, hutuzuia kwenda kama tunavyotaka, hutuzuia kufurahia maisha na hutuzuia kuwa huru katika mambo yetu mengi kimaisha.

Bila shaka tukiwa jasiri kama mtoto yule na kubaini sisi wenyewe kwamba tunatembea na sehemu zetu ambazo zimekufa, tutakuwa tayari kuziondoa na kuwa huru. Ni vizuri kujiuliza kama kuna mambo yaliyopita ambayo yanatuzuia katika kufanya na kufikia malengo yetu, ambayo yanatunyima furaha na kutufanya tujione kama watumwa. Je mambo hayo yana maana gani kwetu wakati yameshapita? Ni wazi yamekua, tunayabeba bure.

Kuna ambao wanalia hadi leo kufuatia vifo vya wapenzi wao vilivyotokea mika kumi iliyopita. Kuna wanaohangaika kutaka kulipa visasi vya yale mabaya waliyotendewa miaka kadhaa nyuma. Kuna wale ambao wanasumbuliwa na mawazo ya jinsi walivyofilisika au kusalitiwa na jamaa au wapenzi wao. Hii yote ni mizigo ya bure, ni sehemu za miili au maisha yao ambazo zimekufa, lakini wanaziburuza.

Nimekuwa nikiandika hapa mara kwa mara kwamba mambo yaliyopita hayapaswi kutuumiza, kutuondolea furaha na kutufanya tujihisi wanyonge na tusio na thamani, kwa sababu mambo haya hayana maana yoyote tena kwetu. Hata kama utafikiri kwa miaka mia kuhusu jambo Fulani ambalo tayari limekutokea, huwezi kulibadili hata kwa chembe ndogo sana, sanasana unalipa uzito ili likutese zaidi.

Ili uishi hasa, uishi kwa kadiri ya utashi wa kanuni za kimaumbile, inakupasa uondoe sehemu ya mwili wako ambayo imeshakufa. Bila kuiondoa sehemu hiyo, ni lazima utaelemewa sana.
Habari hii iliwahi kuandikwa katika Gazeti la Jitambue.


Kama kawaida leo ni Jumatano ambayo ni siku ya kipengele chetu cha marudio ya mada/makala /picha nk mbalimbali na leo mada hii inatoka kwa mzee wa Utambuzi na Kujitambua .