Thursday, September 30, 2010

Picha ya wiki na ya mwisho kwa mwezi huu:- HAPA VIPI JAMANI????

Nimeipenda hii picha nimecheka kweli na nimeona iwe picha ya wiki na pia sikupenda kucheka peke yangu nimeona na wenzengu tucheke pamoja na tunenepe pamoja. Kaazi kweli kweli!!! Sijui huko tuendako itakuaje?

Wednesday, September 29, 2010

Utamaduni na Utandawazi


Habari hii ameichapisha Profesa Joseph L.Mbele kwenye blogu yake , nami imenigusa kiasi cha kuamua kuiweka Maisha na Mafanikio, ili habari ienee zaidi kadiri iwezekanavyo

---------------------------------------------------------------------------------------

Tangu mwaka jana, nimekuwa naendesha warsha hapa Tanzania kuhusu utamaduni na utandawazi. Mwaka jana nilifanya hivyo Arusha, na mwaka huu nimeendesha warsha Tanga na Dar es Salaam. Warsha hizi zimehudhuriwa na watu kutoka Tanzania, Kenya, Cameroon, Uingereza, Sweden, na Marekani. Hao wa nchi za nje ni watu waliokuwepo Tanzania kwa shughuli mbali mbali.

Niliamua kuanza kuendesha warsha hizi hapa Tanzania kutokana na kutambua kuwa ni muhimu katika dunia ya leo inayozidi kuwa kijiji. Watu wa tamaduni mbali mbali wanazidi kukutana kwa sababu mbali mbali, kama vile biashara, masomo, utalii, na uwekezaji. Watu wa tamaduni mbali mbali wanajikuta wakifanya kazi pamoja viwandani, maofisini, na kadhalika. Wanafunzi, watafiti, na walimu, wanajikuta wakishughulika na watu wa tamaduni mbali mbali.

Hali hii inaweza kusababisha migogoro ya aina aina, kwani kila mtu ana namna yake ya kuongea, kufikiri, kufanya mambo, ambayo inatokana na utamaduni wake. Bila kuelewa utamaduni wa wengine, matatizo lazima yatatokea, kama vile kutoelewana na kugombana.

Kwa miaka mingi katika kufundisha Marekani, nimehusika pia katika kutoa ushauri kwa waMarekani kuhusu utamaduni wa waAfrika. Wamarekani hao ni wale wanaokuja Afrika, iwe ni kwa masomo, utalii, shughuli za kidini, au za kujitolea. Nimehusika pia katika kutoa ushauri kwa waAfrika waishio Marekani, kuwasaidia kuulewa utamaduni wa Mmarekani.

Uzoefu huu umenifungua macho kuhusu umuhimu wa suala hili la kuelewa tamaduni mbali mbali, hasa kwa kuwa dunia inabadilika na kuwa kijiji. Hatutaweza kukwepa maingiliano baina ya tamaduni mbali mbali. Wafanya biashara watahitaji kutafuta masoko katika nchi za mbali, au watahitaji kutafuta washiriki kutoka nchi za mbali, au watahitaji kutafuta malighafi kutoka nchi za mbali. Makampuni yatahitaji kuwaajiri watu kufanya shughuli zake sehemu mbali mbali duniani, na katika kufanya hivyo, yatawajibika kuwaajiri watu wa tamaduni mbali mbali.

Kutokana na uzoefu huu nilioupata Marekani, niliona niko tayari kufanya warsha Tanzania. Nilikuwa na hamu ya kukutana na waTanzania na kuona nitafanikiwa vipi kuleta ujumbe wangu.

Jambo la kwanza nililofanya katika warsha hizi ni kuelezea maana ya utamaduni na maana ya utandawazi. Utamaduni, kama nilivyogusia, ni dhana inayojumlisha tabia, mwenendo, hisia na taratibu za maisha. Hata namna ya kuzungumza hutofautisha utamaduni mmoja na mwingine, kiasi kwamba, kwa mfano Mmarekani akisema jambo, linaweza kuonekana kuwa ni maudhi kwa Mwafrika au utovu wa heshima, wakati kwa utamaduni wa Mmarekani, ni usemi wa kawaida au wa heshima. Kadhalika, Mwafrika anaweza kusema jambo ambalo ni la kawaida au la heshima katika utamaduni wake, lakini likawa kero kwa Mmarekani.

Kuhusu utandawazi, dhana yangu ni kuwa utandawazi haukuanza miaka yetu hii, kama wengi wanavyofikiri. Ni jambo lililoanza zamani sana, tangu enzi za binadamu wa mwanzo kabisa. Utandawazi ulianza pale binadamu waliposambaa kutoka Afrika, ambako ndiko walikoanzia, na kuenea duniani. Kuenea huku kwa binadamu kuliandamana na kuenea kwa ujuzi, maarifa, lugha, na mambo mengine mengi.

Utandawazi ulichukua sura mbali mbali kadiri historia ilivyosonga mbele. Katika enzi zetu, utandawazi umetawaliwa na kuenea kwa ubepari, ambao umeathiri uchumi, siasa, utamaduni, na mambo mengine mengi.

Pamoja na hayo, bado tunazo tofauti za tamaduni ambazo zinaweza kuwa kipingamizi tunapokutana na watu wa nchi mbali mbali. Hapo ndipo ulipo umuhimu wa kujielimisha kuhusu tofauti hizi.

Baada ya kuongelea masuala haya ya jumla na kinadharia katika warsha hizi, niliingia katika kutoa mifano ya matatizo ambazo makampuni yamekumbana nayo wakati wa kujaribu kupeleka shughuli zao katika nchi za mbali, kwenye utamaduni tofauti. Makampuni ya Marekani, kwa mfano, yamewahi kupata matatizo katika nchi za Ulaya na Asia. Hata namna ya kutangaza biashara inaweza kuwa chanzo cha matatizo. Tangazo ambalo linavutia wateja katika utamaduni fulani linaweza kuwa kero kwa watu wa utamaduni tofauti. Hata rangi zinazotumika katika tangazo zinaweza kuwa na maana tofauti au kuleta hisia tofauti katika tamaduni mbali mbali.

Kwa bahati nzuri, washiriki wa warsha hizi wamevutiwa na wamesisitiza kuwa ni muhimu warsha hizi ziendelee siku za usoni, kwenye mashirika, vyuo, na taasisi mbali mbali. Kwa upande wangu, nimefurahi kupata fursa ya kuongea kwa undani na waTanzania ambao tulikuwa hatufahamiani. Nimefurahi kuanza kuamsha fikra za masuala haya muhimu miongoni mwa waTanzania. Nimefurahi kuanza kujenga mtandao wa watu ambao tutaweza kuchangia kwa namna fulani maendeleo katika jamii yetu.

Katika kuthibitisha zaidi hoja hizi, nimekuwa nikiongelea mifano hai ya jinsi utamaduni wa Mmarekani unavyotofautiana na utamaduni wa Mwafrika, kama nilivyojionea mimi mwenyewe katika kuishi kwangu na waMarekani. Katika kufanya hivyo, nimekuwa nikitumia kitabu ambacho nimeandika, na ambacho kinatumika na waMarekani wanaofika Afrika, na pia waAfrika wanaoishi Marekani. Ninaandika muda wote, na hii ni njia ya kuendelea kujifunza mimi mwenyewe na kuendelea kutoa mchango wangu katika masuala haya muhimu.

Kitu kimoja ambacho nimekuwa nikisisitiza ni kuwa hili ni suala la elimu, na elimu haina mwisho. Tunawajibika kuanza kujielimisha na kuendelea hivyo bila kuchoka. Warsha moja au mbili haitoshi, bali ni mwanzo. Ni mwanzo mzuri, na nangojea kuendelea kuendesha warsha hizi siku zijazo. Zaidi Hapa kwetu

Tuesday, September 28, 2010

HONGERA KWA SIKU YA KUZALIWA KAKA YANGU SHABAN KALUSE


Kaka Shaban Kaluse
Napenda kukutakia HONGERA kwa siku yako ya kuzaliwa, na nakutakia kila la kheri kwa kila jambo utakalotenda liwe jema na pia nakutakia maisha mema, upendo na amani itawale katika familia yako. Na halafu uwe na mafanikio kwa kila utakalo tenda. Halafu najiuliza hivi siku hizi sijui upo wapi wewe kaka wa utambuzi ? HAYA HONGERA SANA KWA SIKU HII MUHIMU KATIKA MAISHA YAKO. HONGERA KAKA SHABAN!!!!!. Kwa kutaka kujua mambo ya mwanautambuzi huyo gonga hapa.

Monday, September 27, 2010

LAITI KAMA NINGEKUFAHAMU KABLA.........HADITHI YA KUFIKIRIKA


Miaka mitano iliyopita nilikuwa natafuta mke wa kumuoa ambaye angekuwa na sifa nizitakazo. Nilikuwa natafuta msichana mzuri wa wastani maana sikutaka kuoa mke mzuri kupindukia asije niua bure kwa presha na jakamoyo. Nilikuwa natafuta binti atakanikubali kama nilivyo na mapungufu yangu na mimi niliahidi kumkubali na mapungufu yake ili mradi asiwe ni mwenye tamaa ya kupenda sana pesa na mfujaji.
Awe na staha na anayeweza kukabiliana na hali yoyote, niwe nacho, nisiwe nacho au kwa kifupi tupendane kwa shida na raha.

Pamoja na sifa nyingine ndogo ndogo, lakini muhimu ni upendo na amani vitawale nyumbani kwangu.
Hatimaye nilimpata Binti Yasinaty, na kukutana kwetu kulikuwa ni kama muujiza, nakumbuka siku hiyo nilipanda daladala nikielekea kazini na kwa bahati kiti nilichokalia kilikuwa ni cha mwisho upande wa dirishani. Wakati nakaa nikahisi kukalia kitu kigumu, nilipopapasa ilikuwa ni simu mpya kabisa tena ya bei mbaya kama sikosei wakati huo ilikuwa inauzwa shilingi laki nne kwa wakati huo, kumbuka kwamba hapa nazungumzia habari ya miaka mitano iliyopita.

Kwa bahati mbaya simu ile ilikuwa imezimwa, na nilipojaribu kuiwasha iliwaka na kuzima kuashiria kwamba betri yake iliisha chaji. Niliiweka mfukoni na kujiuliza kuwa ile simu ilikuwa ni ya nani, sikusikia mtu kulalamika kwamba amepoteza simu na niliogopa kuuliza maana nilichelea mtu kujitokeza na kusema kwamba ni yake ilihali sio ya kwake.

Nilifika ofisini na kuanza kazi, baadae nilimuita katibu muhtasi wangu na kumwomba anisaidie kutafuta chaji ya ile simu kwa kuwauliza wafanyakazi pale ofisini, nilikuwa na shauku ya kumfahamu mwenye simu ile ili nimrudishie, kwani nilikuwa namuoana dhahiri akisikitika kwa kupotelewa na simu yake, kwa jinsi ilivyoonekana ilikuwa bado ilikuwa ni mpya kabisa na ilikuwa haijatumika zaidi ya wiki.

Katibu wangu muhtasi hakufanikiwa kuipata ile chaja ya ile simu. Niliweka ile simu kwenye droo ya ofisini kwangu ili jioni nikitoka nipitie nayo kariakoo ninunue chaja yake.
Ilipofika jioni alikuja mchumba wangu ambaye tulitofautiana wiki iliyopita na kuamua kutengana naye. Sikutaka kuonana naye na nilimwambia katibu wangu muhtasi amwambie kuwa niko bize na sitaki afike tena pale ofisini kwangu.

Ukweli ni kwamba nilimpenda sana lakini kitendo chake cha kukuta mwanaume mwingine chumbani kwake tena akiwa amelala kitandani kwake halafu anajidai kunidanganya kuwa eti ni binamu yake hakikunifurahisha kabisa. Nakumbuka nilisafiri kikazi kwenda Mbeya, na ilikuwa nikae kule kwa wiki moja, lakini ilitokea dharura huku Makao makuu Dar ikabidi nirudi baada ya siku mbili tu na nilipofika kwa kuwa ilikuwa ni usiku kama saa mbili niliamua kupitia kwa mchumba wangu ambaye alikuwa akiishi Mwengeili kupata chakula cha jioni kabla sijaenda kwangu Maeneo ya Sinza. Nilipofika nilimkuta akiwa nje akipika, lakini aliponiona alishtuka sana akabaki kinywa wazi, hakunipokea alibaki ameduwaa, nikahisi kuna jambo. Nilimsalimia alijibu kwa wasiwasi nilipotaka kuingia ndani, alinizuia, na huku akiongea kwa sauti yenye kutetemeka aliniambia eti ndani kuna binamu yake kaja na amejipumzisha kitandani kwake, nilishtuka. Niliiingia ndani moja kwa moja na kumkuta kijana amelala kitandani nilipomuhoji kuwa yeye ni nani na anafanya nini pale akaniambia kuwa yuko pale kwa girlfriend wake na alitaka kujua eti mimi ni nani..Sikutaka kuzua ugomvi, nilimwambia kuwa pale ni kwa dada yangu na nilifika kumsalimia, nilimuomba radhi kwa kuingia bila hodi, ila nilimshauri aharakishe kulipa mahari ili tujue kuwa dada yetu anaye mtu, ili wakati mwingine tubishe hodi, niliongea kwa utani, yule kijana alimsifia sana mchumba wangu kuwa ni mzuri hasa na anajua kupenda, alibwabwaja mambo mengi na upuuzi wao wanaofanya nikiwa sipo, niliongea naye kwa utani mwingi na kuaga na kuondoka, lakini moyoni roho ilikuwa ikiniuma kweli. Nilikuwa nampa yule binti karibu kila kitu alichohitaji, lakini kumbe hakuridhika bado akawa na mwanaume mwingine.

Nilitoka na nilimkuta kajiinamia pale nje, sikumuaga nikaondoka zangu. Nilipofika nyumbani nilimtumia ujumbe mfupi wa simu ya kiganjani nikimwambia kuwa kuanzia siku hiyo ilikuwa ni mwisho wa uhusiano wetu. Hakijibu na siku iliyofuata alipiga simu lakini sikupokea, alibadilisha namba na nilipopokea na kugundua kuwa ni yeye nilikata simu, baadae zilifuata ujumbe kadhaa wa simu yake ya kiganjani akitaka tuonane ili tuyamalize. Sikumjibu. Na ndio akaamua kuja ofisini.

Nilimpigia simu katibu muhtasi wangu na kumuamuru amwambie yule binti aondoke pale ofisini. Niliambiwa kuwa amekataa, nilimpigia simu dereva wangu na kumuuliza kama gari limeshatoka gereji, akanijibu kuwa gari litatoka baadae kidogo, nikamwambia akitoka gereji aende nalo nyumbani kisha kesho asubuhi anifuate. Gari langu liliharibika siku mbili zilizopita, hivyo nililazimika kupanda daladala au taxi kama nikiwa na dharura. Niliondoka pale ofisini nikimuacha akiongea na katibu wangu muhtasi na kuondoka zangu. Nilikodi taxi na wakati niko njiani nikakumbuka kuhusu ile simu, lakini niliisahau ofisini, kwa hiyo sikupitia kariakoo tena. Nilikwenda moja kwa moja hadi kwa rafiki yangu anayeishi maeneo ya Kijitonyama na kupoteza muda huko hadi usiku ndio nikarudi nyumbani.

Siku iliyofuata dereva alinifuata na kunipeleka ofisini, nilipofika nilimpa ile simu na kumtuma akanitafutie chaja ya ile simu. Baadae alirudi akiwa na chaja ya simu ile na kunikabidhi. Niliichaji na ilipojaa niliiwasha ziliingia ujumbe kadhaa kutoka kwa watu waliokuwa wakimtafuta mwenye simu ile, nilipozisoma niligundua mwenye simu ile alikuwa anaitwa Yasinaty, nilikata shauri nimpigie mmoja wa watu waliokuwa wametuma ujumbe ambaye alionekana kuwa ni mama yake. Nilipompigia simu na kuuliza kama anamjua mwenye simu kwanza alitaka kujua mimi ni nani na kwa nini simu ya mwanaye ninayo mimi. Nilimsimulia kila kitu na nilimuomba ampe mwanae namba yangu ya simu na kumuomba amwambie awasiliane na mimi ili nimpe simu yake. Yule mama alifurahi sana na kunishukuru sana, kumbe ile simu Yasinaty alitumiwa na kaka yake aishie Ughaibuni.

Mchana nilipigiwa simu na Yasinaty na tuliongea mengi na alionekana ni binti mchangamfu kweli, alinimbia kuwa anafanya kazi kwenye Hoteli moja ya kitalii maarufu iliyoko katikati ya jiji, nilimuahidi kumpitia kazini kwake jioni nikitoka ofisini.
Nilimpitia jioni na kama alivyonielekeza kuwa yuko reception nilimkuta pale akimalizia kazi na aliniomba nimsubiri kweye kijimgahawa kilichopo pale ndani, kwa kuwa mimi sio mnywaji wa pombe niliagiza juisi ili kumsubiri. Baadae alinipitia pale nilipokaa na kunimbia kuwa anatoka hivyo tukutane nje kwani anakwenda kubadili sare za kazini. Alitoka na kunikuta nje nikimsubiri, alipanda kwenye gari na nilimuomba dereva wangu atupeleke Hoteli nyingine ya kitalii maarufu pale hapa jijini ili tupate kahawa na Yasinaty. Tulifika pale tuliagiza vinywaji. Nilitumia wasaa ule kumtazama vizuri Yasinaty, alikuwa ni binti mrembo sana, na mchangamfu hasa, naamini alistahili kufanya kazi reception.

Nilimkabidhi simu yake na yakafuata maongezi mengine ya kujuana na simulizi za hapa na pale. Huo ndio ukawa mwanzo wa kujuana na Yasinaty, ambaye baadae alikuja kuwa mke wangu mpenzi.

Laiti kama ningekufahamu kabla Yasinaty………………….

Habari hii nimetumiwa na msomaji wa blog hii ya MAISHA ambaye anasheherekea ndoa yake kutimiza miaka mitano leo. Na nimeona si vibaya kama nikiweka hapa.

Sunday, September 26, 2010

Jumapili njema ndugu zanguni!!!



MUNGU AW E NANYI WOTE POPOTE MTAKAPOKUWA NA AWE NANYI KWA LOLOTE MTAKALOFANYA NA MFANYALO!!!! JUMAPILI NJEMA !!!!!

Elimu

Habari yako mdau

Naomba uweke kwenye site yako nipate maoni ya wadau tafadhali.

Nimeanzisha MAKULILO SCHOLARSHIP SHOW kwenye mtandao wa YOU TUBE ambapo nitakua nafanya recording ya "vipindi" kila wiki kuhusu mambo ya scholarships. Hii namini itasaidia kwa watu wengi kujibu maswali yao na kurahisisha mbinu za upatikanaji wa scholarships. Show hiyo inapatikana hapa kwenye account hii http://www.youtube.com/makulilofoundation Tembelea link hiyo upate video clips za Show sasahivi.

Naomba maoni ya wadau nini nifanye kuboresha show hii. Kwa sasa show hii ina lugha ya Kiswahili na Kiingereza kwani huduma yangu inasaidia watu wote wa Nchi Zinazoendelea japo msisitizo upo kwa Watanzania wapate nafasi hizi kwa wingi.

Kwa maswali au maoni, niandikie hapa makulilo@makulilofoundation.org

MAKULILO, Jr.

http://www.makulilo.blogspot.com/
http://www.scholarshipnetwork.ning.com/
http://www.makulilofoundation.org/
www.facebook.com/makulilo.scholarships

Friday, September 24, 2010

IJUMAA NJEMA NA WIMBO HUU WA MATATIZO NA DADA NAKAAYA SUMARI

WIMBO HUU NIKIWA NAUSIKILIZA KILA MARA NA UNANIFANYA MAFIKIRISHO SANA-:) SIJUI WENZANGU NANYI ITAKUWA KAMA MIMI!! IJUMAA NJEMA NDUGU ZANGU !!!!!

Thursday, September 23, 2010

SHUKRANI KWA WOTE!!!


Kwa ajili yenu wote kutoka kwa Yasinta Ngonyani!!!

Wanablog wenzani leo napenda kutoa shukrani zangu nyingi sana na za dhat kwa UWEPO wenu na pia UPENDO wenu kwangu, kwa familia yangu na kwa blog ya MAISHA NA MAFANIKIO.

Kwanza kabisa napenda kuwashukuruni kwa UWAZI wenu kwangu, hapa nina maanisha kwa kuniambia yale niliyokuwa nayajua kuhusu mimi na yale ambayo sikuyajua kuhusu mimi. Ni jambo la kujivunia sana pia kufurahisha kuona unaambiwa mambo kama haya kabla hujaiacha dunia hii. Kama tunavyojua wengi wameiacha dunia hii bila kuja wametenda nini hapa duniani na wao ni akina nani? Na siku ile ya safari ya mwisho ndo watu wanapotamka yale yote mazuri na mabaya. Na mimi naweza kusema nina bahati kwani nimebahatika kuyajua na pia wengine kunijua. AHSANTENI SANA.

Kwa kujikumbusha unaweza kusoma hapa kwa mdogo wangu wa hiari Koero Mkundi na hapa kwa Mzee wa lundunyasa Markus Mpangala, pia hapa kwa Diwani ya Fadhili kwa mtani wangu Fadhy Mtanga na halafu hapa.

Pia kwa wengine wengi walioniandika na ambao sijawataja hapa, nawashukuruni sana wote wote kwa ujumla kwa UPENDO wenu.

Swali la leo Neno mpenzi lina maana gani?

Nimekuwa muda mrefu nikijiuliza hivi hili neno MPENZI lina maana gani? na leo
nimeona ni afadhali nipate msaada. Maana palipo na wengi pana mengi pia.

SWALI :- kuitana mpenzi, nakupenda nk unaweza kumwita nani, yoyote, umpendaye au mumeo/mpenzi, mkeo/mpenzi rafiki/mpenzi wako?

Tuesday, September 21, 2010

CHAKULA CHA USIKU: WAHANGA SASA NI WANAWAKE!

Mwambie, usione haya
Zamani ilikuwa ni wanaume waliokuwa wakilalamika, kwamba wake zao hawataki kuwapa chakula cha usiku kama wanavyotaka. Lakini baadae yaani siku hizi ni zamu ya wanawake kulalamika.

Katika nyumba nyingi siku hizi hasa mijini wanawake ndio wanolalamika zaidi kukosa chakula cha usiku kama wanavyotaka kutoka kwa waume zao.

Kwa nini hali hii?

Ukweli ni kwamba maisha yamebadilika sana na kila mtu anajitahidi sana kutaka kuhahakisha kwamba anafanya kazi hadi anaishiwa nguvu kabisa, akili na mwili vinachoka. Wanaume wengi wanaolalamikiwa na wake zao kuhusu kupata uhaba wa chakula cha usiku ni wale wanaofanya kazi sana.

Ningependa kuwashauri wanaume kwamba wakati wanafanya kazi zao mchana wakumbuke kwamba kuna wake zao wapendwa ambao wanawasubiri jioni kuzungumza nao na zaidi ya hapo. Wakumbuke hawajaoa kazi bali wameoa wake. Pamoja na kwamba ni muhimu kwao kufanya kazi, lakini wakumbuke kwamba kazi hazina mwisho.

Kuna jambo ambalo wanaume na hata wanawake hawalijui vizuri, hili ni lile linalohusu mazoezi. Mtu anapofanya mazoezi anawezesha damu kuzunguka na kufikia sehemu zote za mwili kwa kiwango kinachotakiwa. Kukaa ofisini kutwa na kurudi nyumbani na kukaa kwenye kochi na kuangalia TV siyo aina ya maisha inayoshauriwa tuishi. Mwili unapochangamka kwa damu kufika kila mahali kwa kiwango kinachotakiwa hamu ya kutoa chakula cha usiku na kukipokea huwa kubwa.

Lakini mbaya zaidi ni kwa wanawake wenyewe pia. Kuna wanawake ambao bado wanaishi kwa miiko ya karne moja nyuma. Hawa wanangoja wanaume zao wawachokoze, wasipofanya hivyo, basi hata mwaka watakaa wakilalamika kwamba hawapati chakula cha usiku. Tukumbuke kwamba hata wanaume nao ni binadamu pia, huhitaji wakati mwingine kushtuliwa, kwani wakishtua wao tu kila siku, kuna wakati hukinai.
Habari hii nimeipata toka blog ya kaka Shaban Kalus fungua hapa kumsoma zaidi. Naamini kila mara kurudia kusoam jambo/somo ndo tunazidi kujifunza maishani.

Monday, September 20, 2010

NILIDHANI KUWA NI KAPULYA MDADISI TU KUMBE KUNA:- KIMWAGA MDADISI PIA!!!

Raha ya kujua kusoma


Nimekisoma mimi na sasa watoto wangu wanasoma ama kweli raha
Nilikuwa nimeishau hii hadithi, nilidhani kuna Kapulya mdadisi tu kumbe! Nadhani kuna wengi tunakumbuka darasa la tatu tulipokuwa tukisoma hadithi hizi :-haya hebu fuatana nami pia mtoto Erik katika hadithi hii ya KIMWAGA MDADISI.


Hapo zamani palikuwa na motto moja aliitwa Kimwaga. Mtoto Hugo alimpenda sana babu yrke Lukindo. Kimwaga na babu yrke waliishi katika kijiji cha Kwemasafi, Wilayani Korogwe. Jioni, baada ya jua kuzama, Kimwaga alikuwa akikoka moto kwenye Kilanda chao cha mazungumzo. Babu yrke alikuwa akipenda sana kuota moto na kuzungumza na mjukuu Wake.

Siku moja jioni, Mzee Lukindo na Kimwaga walikuwa wakiota moto. Kimwaga alikuwa motto mdadis sana. Alimsimulia babu yrke habari moja iliyomshangaza. Alisema, “Babu, leo tulikuwa tukilima katika samba letu la shule. Mimi niliinua jembe kwa Nguru ili nichimbue magugu. Jembe likagonga jiwe, nikaona cheche za moto zinamulika. Hivi babu moto ulitoka wap?”

Babau yrke akamuuliza, “Hivi mjukuu wangu hujui hadithi ya moto?” Kimwaga akamjibu, “Sijui,” Babu yrke akamwambia, “Basi nikueleze kidogo, Hapo zamani za kale binadamu hawakuwa na moto. Waliishi katika mapango yenye giza. Walikula matunda na Nyala mbichi. Maisha yao yalikuwa ya tabu sana.

“Kwa Bahai, siku moja mzee moja akachukua mawe, akayagongagonga ili yavunjike apate jiwe la kuchimbia viazi mwitu. Alipoyagonga aliona yakitoka cheche za moto. Akafikiri sana. Halafu akaweka manyasi makavu karibu na ylle mawe, na akaendelea kuyagongagonga. Mara ylle manyasi yakawaka moto. Kumbe alikuwa amegundua moto kama ulivyoona wewe leo wakati ulipolima huko shuleni.”

Kimwaga akamwambia babu yrke, “Kumbe hata mimik nimegundua moto.” Kisha akaendelea, “Babu, juzi tulipokuwa tunatoka shule tulinyeshewa na mua tukalowa. Tulipofika kwenye samba moja tulijificha chini ya Kilanda kimoja kidogo. Mwenzetu Kimweri akapekechapekecha vijiti viwili vikavu. Mara tukapata moto, tukautumia kwa kukaushia nguo zetu. Je, babu moto ule ulitoka wapi?”

Mzee Lukindo akasema , “Aaa, wewe Kimwaga unadadisi sana. Basi nitakueleza hadithi nyingine. Hapo zamani sana, kabla mimi sijazaliwa, palikuwa na motto moja mtundu sana. Siku moja alitaka kutoboa kigogo kikavu ili atengeneze kidude cha kuchezea. Akachukua kijiti akaanza kupekecha. Kile kigogo kikatoa unga mweusi. Akaendelea kupekecha kwa nguvu sana. Akaona Moshe. Mwisho ule unga mweusi ukashika moto. Akachukua nyasi kavu na kuziweka karibu na ule unga. Nyasi zikawaka moto. Kumbe naye alikuwa amegundua moto.”

Siku nyingine tena, Kimwaga akamweleza babu yrke namna alivyomtazama buibui. Akamuuliza babu yrke, “Je, babu, ule uti ambao buibui hujengea nyumba unatoka wap?” Mzee Lukindo akajibu, “Buibui ni mdudu wa ajabu. Anapotaka kujenga nyumba yrke, hutoa maji kutoka tumboni make. Maji haya yanapotoka nje tu huganda, na anapokwenda huonekana kama uti.”

Babu yrke Kimwaga alipomaliza kusimulia habari za buibui, Kimwaga alikuwa anasinzia kwa sababu siku ile alichelewa sana kwenda kulala. Mzee Lukindo akamwambia, “Sasa mjukuu wangu, Nena ukalale. Nitakueleza hadithi nyingine kesho.” Kimwaga akaenda zake kulala.

Sunday, September 19, 2010

HESHIMA YA MWANAMKE NA WITO WAKE!!!!

"Mwnamke kama Mama na mlezi wa kwanza wa mwanadamu ana haki ya pekee kabla ya mwanaume. Umama kwa upande wa utu na maadili unaonyesha uwezo wa mwanamke wa kuumba ulivyo muhimu sana ambao unadhihirisha wito wa pekee na ni changamoto ya pekee inayomchochea mwanmume na ubaba wake"


"Heshima ya mwanamke hutegemea utaratibu wa upendo, nao ni hasa utaratibu wa haki na wa kupendana.."



"Hongera kwa mwanamke aliyekuzaa na kukunyonyesha!" Yesu akajibu, "Barabara; lakini heri yake zaidi yule anayelisikia neno la Mungu na kulishika" (Lk 11:27-28). NAWATAKIENI JUMAPILI NJEMA KWA WOTE !!!!!!

Friday, September 17, 2010

Imetutoa jasho orodha ya 9!... Au?

Kwa kweli orodha hii mimi ilinitoa jasho kidogo na wala sikuwaza kufanya hivyo kama inavyoonyeshwa hapo juu. Je ? kuna mtu alijua njia hii?

Ijumaa njema na ujumbe huu wa Mama ntilie!!!



Haya tusikilize na tutafakari kwa pamoja ujumbe huu!! IJUMAA NJEMA SANA NA TUONANE WAKATI MWINGINE !!!

Thursday, September 16, 2010

NANI KASEMA TANZANIA HAKUNA WAREMBO? HII NI MADE IN TZ!!

Hapa ni mrembo/mwanamtindo dada Nuru
Hapa ni mwnadada mwingine tena Yasinta au wengine wanamwita Kapulya.

Ukiangalia vizuri katika picha hizi kuna mfananisho fulani kati ya wanadada hawa. Je ni nini ambacho kinawafanya kufanana au sio kufanana?





Wednesday, September 15, 2010

NIMEUPENDA MSEMO HUU!!

"HAKUNA ANAYEJUA UPWEKE UNAOSABABISHWA NA YEYE KUTOKUWEPO MAHALI FULANI"

MTU AKIONDOKA MAHALA HUACHA UPWEKE, NA UPWEKE HUO HAUSIMULIKI. INA MAANA NI LAZIMA UWEPO ILI KUUHISI.
NA UPWEKE HAUWEZI KUWEPO KAMA WEWE UPO

INA MAANA:- NI LAZIMA WEWE USIWEPO ILI UPWEKE UWEPO NA HAKUNA NAMNA YA KUUSIMULIA UPWEKE, HIVYO NI LAZIMA UWEPO ILI KUUJUA
KWA HIYO, HAKUNA AJUAYE UPWEKE USABABISHWAO NA YEYE KUTOKUWA MAHALA FULANI KWANI NI LAZIMA ASIWEPO ILI UPWEKE UWEPO NA HAKUNA NAMNA YA KUUSIMULIA MPAKA UWEPO."
Hii ni nukuu nzuri sana na mimi napenda sana:- Ukitaka kujua nimeipata wapi basi sikiliza kwa kakangu Mubelwa.

Tuesday, September 14, 2010

Hii nimeipenda sana!!!


Nadhani wote mnajua huyu ni nani na ukiangalia kwa makini utaona anafanya nini na anaangalia nini au labda anasoma . Sijui ilikuaje hapa?

Monday, September 13, 2010

Wanaume wajaribiwa katika kazi ya ukunga!!


Kazi hii yaweza kufanywa na wakunga wa jadi wa kiume kama wakifundishwa.
HENRY Teh anasogeza taratibu shuka la rangi ya bluu hospitalini kuonyesha tumbo la mama mjamzito.
Wakati akisikiliza mapigo ya kichanga tumboni, mkunga huyo aliyepo kwenye mafunzo anajua anavunja jadi
na kubadili sura ya huduma za uzazi nchini Liberia.

"Katika mazingira yetu, kuna baadhi ya wanawake ambao hawapendi wanaume kuwaangalia... kwa sababu
ya maeneo yao ya siri," anasema, huku akichezea chezea 'stetoskopu' yake.

Mwaka 2009, Teh alikuwa mmoja wa wanaume ambao waliandikishwa katika mpango wa kutoa mafunzo kwa
wakunga wa jadi kusini mashariki mwa Liberia. Shule ya wakunga wa jadi ya kijijini, iliyofungwa miaka 20
iliyopita kutokana na vita, ilifunguliwa upya na shirika la msaada wa dawa la Uingereza la Merlin na Wizara ya
Afya na Ustawi wa Jamii ya Liberia.

Uhaba wa wanafunzi wanaohitimu

Viongozi wa shule wanagundua kwa haraka kuwa kuna uhaba wa wanafunzi wa kike wanaohitimu katika
maeneo ya vijijini. Vijana wachache wa kike nchini Liberia walihitimu kutoka shule za sekondari katika miongo
michache iliyopita kutokana na wazazi kupendelea kupeleka watoto wa kiume shule.

Uamuzi wa kuchukua wanaume ulionekana kuwa na mantiki, alisema mkufunzi wa ukunga Sawah
Shaffa. "Liberia ina madaktari wanaume. Ina manesi wanaume. Hivyo, hata wakunga wa jadi hawapaswi
kuwa wanawake tu."

Katika hospitali ya kutoa mafunzo ya Martha Tubman huko Zwedru, Teh anamkaribisha mwanamke
mwingine kulala juu ya meza na kumfanyia uchunguzi. Kijana huyo anaelezea jinsi gani aliruka na kuingia
katika fursa hiyo na kuwa mkunga kutokana na uzoefu binafsi ambapo dada yake mwenye umri wa miaka 19
alifariki wakati akijifungua msituni.

"Alikuwa akijaribu kutembea kutoka mji wa karibu kwenda Kanweaken, ambako tuna kliniki. Alianza kutokwa
na damu nyingi na kulikuwa hakuna gari."

Wanakijiji walimbeba mwanamke huyo kwenye mkokoteni kwenda mji uliopo karibu, lakini alifariki dunia kabla
ya kufika kwa gari la kubebea wagonjwa.

Huduma bora za uzazi zinahitajika

Ripoti ya mwaka 2009 ya Shirika la Kuhudumia Watoto la Umoja wa Mataifa (Unicef) inasema kuwa
wanawake wa Liberia wana uwaino wa hatari. Mmoja katika kila 12 ya hufariki dunia wakati wa ujauzito au
kujifungua mara nyingi kutokana na kuziba kwa kizazi, kutokwa damu au maambukizi na kusababisha kuwa
taifa la nane lenye vifo vingi vya uzazi duniani. Unicef inasema asilimia 80 ya vifo vya uzazi vinaweza
kuzuilika kwa kuwa na wafanyakazi wa afya wenye mafunzo.

Liberia ina watu milioni 3.8 lakini ina wakunga wa jadi 400 tu wenye mafunzo. Maofisa wa afya wanasema
wakunga wengine 1,200 wanahitajika.

Kuondokana na vikwazo vya kitamaduni

Mpango wa wakunga wa kiume utakuwa na mafanikio? Hilo ni suala linalohojiwa. Katika chumba cha
kusubiria chenye watu wengi kwenye Hospitali ya Zwedru, mwanamke mdogo mwenye mimba anaugulia
maumivu huku akiminya tumbo lake. Aletha Cherley (22), anaogopa kwa sababu ni ya mimba yake ya
kwanza lakini pamoja na kukamatwa na misuli na kuumwa na mgongo, anasita kuchunguzwa na Teh.

"Kwangu, mwanaume tofauti ambaye siyo rafiki wangu wa kiume anaona sehemu zangu za siri, najisikia aibu
mno ... Ni aibu kubwa kwangu. Hii ndiyo sababu wanawake hapa wanapaswa kufanya kazi hiyo," anasema
Cherley.

"Unajua, ukunga una maana kuwa mtu anapaswa kukaa na mwanamke kwa muda mrefu. Wanawake wengi

watajisikia wenye furaha kwa kuwa na mwanamke mwingine hadi wanajifungua," anasema mkunga kutoka
Kenya, Zeena Abdalla Ramadhan, ambaye ni mratibu wa Merlin.

"Ukunga ni jambo binafsi... ni mwanamke kwa mwanamke."

Abdalla (56), anayejulikana kama "Mama Zeena," ametumia karibu nusu ya maisha yake akiwa anafundisha
wakunga nchini Sudan, Chad na Kambi ya Wakimbizi ya Kakuma, Kenya. Anatambua kuna vikwazo vya
kitamaduni kuanza kutumia wanaume katika fani ya ukunga ambayo kwa jadi ni ya wanawake.

"Katika Sudan Kusini, wanaweza kumwita mwanaume wakati mwanamke anaposhindwa. Wanaume
watakuja na mkuki kumtoa mtoto, mtoto aliyenasa. Hata hivyo bado, mwanamke anapaswa kuwepo."

Je, wanaume waliopatiwa mafunzo wanaweza kujaza pengo?

Mama Zeena alifundishwa kuwa mkunga wa jadi baada ya kupoteza mtoto wake aliyemaliza muda wake
tumboni mwaka 1987. Leo hii, amekuwa mtetezi mkuu wa kutoa mafunzo kwa wakunga wa jadi katika
mataifa masikini yaliyokuwa na vita.

Anaonya kuwa Lengo la Maendeleo la Milenia (MDG) la kupunguza kiwango cha vifo vya mama wajawazito
duniani kwa tatu ya nne ifikapo mwaka 2015 na kutoa huduma ya afya ya umma kwa wote, halitaweza
kufikiwa bila kuwekeza kwa kiasi kikubwa.

Nchini Liberia, amekabiliwa na maswali kama mafunzo ya ukunga kwa wanawake yanafaa kama masuala ya
jinsia yanazuia wanawake wenye mimba kupata ushauri kutoka kwa wanaume. Uamuzi unakuwa mgumu
zaidi kwa sababu wanaume wanapata alama za juu zaidi katika mtihani wa kujiunga na mafunzo.

"Kama tungekwenda na alama, tungeishia na wanaume tu... Lakini (wanajumuiya) walionyesha shaka.
Hatuwezi kutoa mafunzo kwa watu ambao hawatakuwa na maana. Hivyo, tuliamua tusichukue wanaume
zaidi."

Shule ilipunguza idadi ya wanafunzi wakunga wanaume mwaka 2010 hadi wawili tu. Mama Zeena hajui nini
kitatokea mwaka ujao.

Ukirejea katika chumba cha upimaji cha Teh, kijana mdogo anaweka sikio lake kwenye kipimo na
anakibonyeza dhidi ya tumbo la mwanamke mwenye mimba ili kusikiliza mapigo ya mtoto. Teh, ambaye
alikuwa akichaji simu za kiganjani ili kuingiza fedha katika kijiji chao kidogo mwaka jana, anapiga kelele kwa
furaha anapoelezea ni kwa kiasi gani anapenda mafunzo hayo ya kuwa mkunga.

Tofauti na uongozi wa shule, yeye ana imani kuwa wanawake wajawazito wataondokana na aibu yao na
miiko ya kitamaduni kupata huduma za afya kutoka kwake kijijini humo.

"Napenda mno fani hii... na unapaswa kuwakaribia wanawake kwa njia ambayo unadhani watahisi vizuri."

Darasa la kwanza la wakunga 32, ambao watamaliza masomo yao Desemba 2010, limesaini mikataba na
Wizara ya Afya ambayo inawahakikishia ajira kamili kwa miaka mitatu, kwa kuhudumia majimbo sita ya vijijini kusini mashariki mwa Liberia.
kusini mashariki mwa Liberia.

Habari hii nimeipata kutoka gazeti la mwananchi na Bonnie Allen, IPS-Liberia

Friday, September 10, 2010

Jamani sisi kama watoto safari zetu huanzia mbali sana!

Tumetoka mbali jamani!!

Basi ngoja tumsikilize Dada Lady Jay Dee na wimbo wake natamani kuwa malaika, natamani tena kurudi nyuma, natamani kuwa kama zamani na natamani kuwa kama mtoto.!!!!!!!!!!!!!!

Basi ngoja niwatakieni IJUMAA NJEMA pia EID MUBARAK!!! AKIPENDA TUTAONANA !!

Thursday, September 9, 2010

HUU NI UJUMBE WA WIKI HII!!!






" Uongozi unaweza ukawa mzuri au mbaya, au usiojali, lakini kama watu wameamka na wanajitambua wenyewe, kutoshirikishwa kwa mawazo na tabia ya jamii hakutaendelea kwa muda mrefu"


Chanzo: kutoka katika kitabu cha kipindi cha ujamaa na kujitegemea yakisemwa na mwal. Julius K. Nyerere.

Wednesday, September 8, 2010

NIMEMALIZA SHULE!!!

BAADHI ya watahiniwa katika shule ya Msingi, Miburani, Temeke, Dar es Salaam wakishangilia baada ya mtihani wa mwisho wa kuhitimu Elimu ya Msingi. (photo: Bashir Nkoromo).

Vijana hawa wananikumbusha siku tuliyokuwa tukiisubiri kwa hamu kubwa sana, 'kumaliza shule' tukiamini ati baada ya kuondokana na adha ya kudamka alfajiri, kushikana mashati na 'konda', kuwahi 'namba' na 'mstarini'... yaani ndoto za kila aina alimradi kujiaminisha usumbufu utakuwa umekwisha kabisa.

Tulijiona sisi ndiyo 'top' hakuna mwingine duniani kama sisi. Hisia za 'kumaliza shule' na kubaki nyumbani wakati wengine wanaamka asubuhi wakiwa na heka heka za ama kwenda shuleni au kazini, zilitutawala.

Siku hizi, tofauti na zamani nilipomwona 'madha mnoko', huwa najivuna sana kuwa na Mama asiye na longolongo wala 'kukopesha maneno' kwani, aliponisikia nikijitapa eti 'nimemaliza shule' siku moja aliniambia,

"...wewe, umemaliza shule ipi? Subi, hujamaliza shule. Umehitimu Elimu ya Msingi tu. Umeimalizaje shule wakati hujafika hata Sekondari? Umesahau methali mlizofundishwa, Elimu ni bahari; Elimu haina mwisho? au ulidhani ukishakariri na kuandika kwenye daftari ukafunga na ulichofundishwa kimefungwa kwenye mkoba? Yaani mwalimu akishafuta ubao na kwenye akili yako vinafutika? (kichwani mwangu nawaza, 'kwani si ndiyo kazi ya shule? unaandika, mnakusanya madaftari, mwalimu anatia 'pata' kama hesabu umekosea fanya masahihisho tu, basi').

Umevuka madarasa ya shule ya awali, sababu ya kuitwa 'msingi' ni kwa kuwa umeweka msingi wa elimu na maisha yako. Ni sawa na kujenga nyumba. Ili iweze kusimama imara, lazima msingi uwepo, tena uwe ni msingi ulio imara. Msingi ndiyo kigezo cha uimara wa nyumba. Umeweka msingi, bado kuta, madirisha, paa, na fenicha na vifaa vingine vya ndani. Lakini la muhimu ni msingi. Ikiwa uliweka msingi imara, nyumba yako itakuwa imara, utaweza kujenga nyumba kuuuubwa au hata orofa, inategemea na uimara wa msingi wake."

Ni baada ya kwenda kwa Bibi na kuwatembelea ndugu, ninarejelewa kauli ya Mama, 'hujamaliza shule' nhe he, ndipo nilipotia akilini, kumbe tulichokuwa tukifurahia 'standadi seven kumaliza shule' ilikuwa ni furaha ya muda tu, tena ya kitoto, bado ilikuwepo kazi kubwa mbele yetu; Kuna kusaidia kazi za nyumbani sasa zaidi ya wengine na; Kuna kuchukua fomu za shule za "private" tena kujaza zaidi ya moja, na kwa ambaye matokeo ya maendeleo yake shuleni kila mhula hayakuwa mazuri, hali kwake ilikuwa ni mbaya, yaani atazijaza fomu za 'private school' hata tano ili walao abahatishe moja ikiwa atakataliwa kwingineko. Nakumbuka nilizijaza mbili, Majengo Secondary na Uru Seminary. Kisha kuna kufanya tena mtihani wa kuomba kujiunga na shule hizo na, ni lazima ufaulu, la sivyo uaibike kwa kuzurura mtaani na kufanya kazi nyumbani wakati wenzio wanaongozana kwenda na kutoka shuleni! Shabash! Hakuna kumaliza shule!

Naam, huo ndiyo wakati nilipoanza kufahamu kuwa ninayahama maisha ya utoto na kuingia ujanani.

Hongereni vijana mliohitimu elimu ya msingi, shule bado hamjaimaliza. Elimu haina mwisho!


Nimeipenda sana simulizi hii kwani imenikumbusha pia enzi zile namaliza darasa la saba. Ni kweli yaani ile asubuhi kuwahi namba ukichelewa tu viboko hivyo. Halafu kukimbia mchaka mchaka, nakumbuka baada ya mchaka kchaka kulikuwa hakuna tena kuoga maji ni kuaa hivyohivyo darasani na mijasho inakutiririka. Mweeh kwa kweli tunatoka mbali na kweli elimu haina mwiho. Na ukitaka kujua nilipoipata basi unaweza kubonyeza hapa

Upweke, Je wewe umewahi kujisikia mpweke??


Katika maisha haya ya kublog tumekuwa kama vile ndugu, mmoja akiadimika bila taarifa basi twapata wasiwasi. Nimewaza na kuwazua hawa binadamu wamepatwa na nini?. Na mwisho najisikia UPWEKE. Na katika pita pita zangu kama kawaida nikakutana na shairi hili nikaona si mbaya hata kama tumesoma lakini kusoma tena na tena ndio kukumbuka mambo, haya karibu !!. Na shairi hili lina toka kwa mtani wangu Fadhy Mtanga.

Pale unapojikuta u-mpweke, je? ufanyeje?

Upweke jama adhabu, upweke unasumbua,
Upweke ni maghilibu, kukufanya kuugua,
Watamani wa karibu, nenolo taelijua,
Upweke.

Upweke hutesa sana, umpendaye awe mbali,
Utamuwazia sana, hata mara alfu mbili,
Kwa usiku na mchana, maumivu ni makali,
Upweke.

Upweke unakondesha, chakula hukitamani,
Upweke unahenyesha, simanzi tele moyoni,
Homa pia hupandisha, na mwokozi humuoni,
Upweke.

Upweke tele mateso, hata machozi kulia,
Moyoni ni manyanyaso, nao moyo kuumia,
Wala si kimasomaso, kwani huleta udhia,
Upweke.

Upweke ni kama jela, huleta nyingi simanzi,
Huwezi hata kulala, maisha tele majonzi,
Utapiga hata sala, uruke vyote viunzi,
Upweke.

Upweke sawa na shimo, mtu ukatumbukia,
Nako shimoni uwamo, wateswa nayo dunia,
Kwani hauna makamo, kuweza kuvumilia,
Upweke.

Tuesday, September 7, 2010

HONGERA BLOG YA LUNDUNYASA KWA KUTIMIZA MIAKA MINNE!!!

Markus Mpangala wa lundunyasa


Miaka yaenda kasi mno tarehe 31/8/2007 blog hii ya LUNDUNYASA ilitimiza miaka 4. Blog ya MAISHA NA MAFANIKIO yakutakia yote utakayotenda yawe na mafanikio mema. Hongera sana na uwepo wako unathaminiwa sana. Ingia hapa utakuta mengi

Monday, September 6, 2010

‘Housigeli’ anataka kuniharibia ndoa

Mama mkwe
habari yako. Nategemea mzima wa afya na hutasita kunisaidia kunipa ushauri unaonifaa. Mimi ni mwanamke mwenye watoto wawili. Tangu nimeolewa miaka sita iliyopita, nimekuwa na msichana wangu wa kazi mmoja ambaye nimempenda sana hasa kwa kuwalea vizuri watoto wangu na kuwa mwepesi wa kazi. Kutokana na kuishi vizuri na ‘housigeli’ huyu, amekuwa kama mtoto wa nyumbani na hata ndugu zangu na wa mume wangu wanampenda sana na wamemzoea kupita kiasi.
Tatizo hili la kuwazoea ndugu wa mume wangu sasa naona linataka kuharibu ndoa yangu kwani huyu msichana ameanza tabia mbaya na amemweleza mkwe wangu kuwa mimi situlii nyumbani na sina muda wa kumshughulikia mume wangu kwani kazi zote anafanya yeye, mimi kazi yangu kusafiri na kushinda kazini. Huyu mama mkwe wangu kusikia hayo, amekuja juu na sasa anamshinikiza mume wangu aniache eti nashindwa kuhudumia nyumba na badala yake amuoe ‘housigeli’. Mume wangu ameshtuka na amenieleza kila kitu hali iliyonikasirisha sana.
Sasa naomba ushauri wako kwani mama mkwe bado yupo kwangu, je, nifanyeje kabla hajaondoka kurudi kwake? Mama Kelvin Tabata, Dar es Salaam. Mama Kelvin pole sana kwani inaonekana huyo mama mkwe wako hajaelimika vya kutosha. Uzuri wa mwanamke haupimwi kwa kazi za nyumbani pekee, bali kuna mambo mengi na mkwe wako anapaswa kutambua kuwa wewe unafanya kazi hivyo huwezi kukaa nyumbani muda wote na ndiyo sababu ukatafuta msaidizi.
Lakini pia ni vyema ukiwa nyumbani ufanye kazi zilizopo ikiwamo kumpikia mumeo na kumhudumia ipasavyo. Usiwe na hasira za haraka kwa msichana wako wa kazi kwani inawezekana aliulizwa kimtego naye akajibu vizuri tu lakini mkweo akawasilisha kwa mumeo vibaya. Nadhani mumeo pia anapaswa amweleze mama yake kwa upole kuwa wewe unafanya kazi na huwezi kufanya kazi zote za nyumbani. Pia amweleze kuwa huyo msichana wa kazi kamwe hawezi kuwa mke wa mtoto wake.
Naamini mtoto wake akimwelimisha na akawa na msimamo, mama mkwe wako ataelewa au hata kama hataelewa, atashindwa kuendelea kusisitiza anachotaka. Ni vyema pia ukakaa na mshichana wako na kumhoji ilikuwaje hata wakazungumza hayo na mkweo na ukiona kama alichokonolewa basi mtahadharishe akae mbali na mama mkwe na asiwe mwepesi kueleza mambo ya ndani ya nyumba kwa mkweo.
Hata hivyo fanya uchunguzi wako kwa siri na ukiona msichana wako anapalilia ili aolewe yeye, basi ni vyema ukatafuta msichana mwingine wa kazi na huyo kumwondoa ili asije kuharibu ndoa yako. Haina haja kugombana na mtu yoyote kwani naamini huyo mkweo ataondoka na nyinyi mtaendelea na maisha yenu. Pia jifunze kuvumilia kwani wakwe wengine uelewa wao ni mdogo.

Habari hii nimeipata jamii forum na nimeona si vibaya kama nikiweka hapa Maisha na Mafanikio.

Sunday, September 5, 2010

Mtu, Kinywa chake hunena yale yaujazayo moyo wake!-TAFAKARI

Mathayo 7:15-20
Jihadharini na manabii wa uongo, watu wanaowajia wamevaa mavazi ya kondoo, walakini kwa ndani ni mbwa-mwitu wakali. Mtawatambua kwa matunda yao. Je! Watu huchuma zabibu katika miiba, au tini katika mibaruti? Vivyo hivyo kila mti mwema huzaa matunda mazuri; na mti mwovu huzaa matunda mabaya.Mti mwema hauwezi kuzaa matunda mabaya, wala mti mwovu kuzaa matunda mazuri. Kila mti usiozaa tunda zuri hukatwa ukatupwa motoni. Ndiposa kwa matunda yao mtawatambua.

Luka 6:43-45
Kwa maana hakuna mti mzuri uzaao matunda mabaya, wala mti mbaya uzaao matunda mazuri; kwa kuwa kila mti hutambulikana kwa matunda yake; maana, katika miiba hawachumi tini, wala katika michongoma hawachumi zabibu. Mtu mwema katika hazina njema ya moyo wake hutoa yaliyo mema, na mtu mwovu katika hazina mbovu ya moyo wake hutoa yaliyo maovu; kwa kuwa mtu, kinywa chake hunena yale yaujazayo moyo Wave
Habari hii nimeipata nimeipata hapa http://strictlygospel.wordpress.com/ na nikaona si mbaya kama nikiweka katika kibaraba cha Maisha na Mafanikio. JUMAPILI NJEMA KWA WOTE

Saturday, September 4, 2010

Likonde: Jubilei ya miaka 50 ya Seminary ya Likonde

Seminari ya Likonde



Ama kweli miaka inakimbia kweli leo hii ni jubilei ya hii Seminary!!


Friday, September 3, 2010

KIBAO CHA CCM CHA MARLOW NA VUVUZELA!!



Mungu ibariki Tanzania na Mungu mbariki Rais mtarajiwa na bila kusahau utubaribi sisi wananchi tuweza kumchagua rais mchapakazi!!!

Huyu ni mrembo wa wiki hii, Je? unamfahamu huyu??

Napenda kuwatakieni wote Ijumaa njema. Picha hii nimeipenda na nimeona iwe ni picha ya wiki hii. Jipende kwanza mwenyewe na wengine watakupenda!!! Juma ndio linaisha sasa, kwa wengi ni wakati wa kumpumzika, na wengine kazi kama kawaida. Basi nasema tena nawatakieni wote muwe na wakati mzuri. IJUMAA NJEMA!!

Thursday, September 2, 2010

Tunaomba msaada wenu:- Ni vipi mchezo huu wa Bao/nchua uunachezwa?


Bao/nchua!!
Wakati nipo likizo na mpaka sasa kuna mvua kila siku na hata kunasababisha mafuliko sehemu fulani fulani. Sasa mimi na familia yangu baada ya kuona hatuwezi kufanya michezo mingine ya kuwafurahisha watoto tukakumbuka tuna bao/nchua ambayo tuliinunua Tanzania. Tukachukua kila tukijaribu kucheza ubongo haukumbuki kanuni inakuwa vipi. Nikaona mmmhhh! kuuliza si ujinga aulizaye anataka kujua na umoja ni uwingi. Kwa hiyo nimeona niwaulize je ni vipi kanuni inakuwa? Tutashukuru sana kama mkitusaidia.

Wednesday, September 1, 2010

Sheria, Mila na Desturi pia Tamaduni pale Zinapotofautiana!!

Mama, baba na watoto, maisha ya ndoa!!

Mama na watoto wake peke yake!!
(Ensamstående )

Fuatana nami kwa habari hii fupi kuhusu maisha yalivyo tofauti:- Kwa miaka kadhaa iliyopita nchini Sweden kulikuwa na uhaba wa watoto. Yaani maisha yalikuwa magumu na watu walipunguza "waliacha" kuzaa watoto wengi. Baada ya Serikali kuona hivyo ikaja na sharia kuwa kila mtoto atayezaliwa basi wazazi watalipwa kiasi fulani kila mwezi mpaka mtoto atakapotimiza miaka 18. Pia ni kwamba kiasi cha malipo kitaongezeka mtoto wa pili atapozaliwa kama mtaliwa 2000SEK na sasa mtalipwa 4000SEK na mtoto wa tatu wa tatu mtalipwa 7000SEK huu ni mfano tu

Sasa tatizo jingine limeibuka sasa hivi tu, nilikuwa nasikiliza habari na nikasikia kitu ambacho sikuweza kuamini. Naweza kusema nilishangaa ama kweli TEMBEA UONE YA DUNIA. Ni hivi kama mmefunga ndoa na baadaye mnapata mtoto hapo kuna utaratibu kwamba wazazi mnapewa siku 480 kwa mwaka kuwa nyumbani na mtoto. Ni hiari yenu kama mnataka kugawana hizo siku au mzazi mmoja atabaki nyumbani na mtoto. Inaitwa (föräldraledighet) au kwa lugha ya kitaalamu ni (Maternity live) na hizo siku mnalipwa kwa kuwa nyumbani na mtoto wenu.

Ila sasa kama mnaishi bila kufunga ndoa (Sambo) hizo haki zote zitaenda kwa mama. Na halafu baba atakuwa hana haki hata ya kuwa na mwanae, kwa maana hiyo anakosa kile kipindi cha mtoto awapo mchanga kipindi ambacho kila mzazi/mlezi angependa kukishuhudia.

Mwisho, ni kwamba Sweden mume na mke wakiachana mtoto au watoto watakuwa wanafuatana na mama. Pia ni ruksa kuitwa ubini wa mama. Nimetoa mfano huu kwa vile Tanzania kama wazazi wanaachana watoto wanabaki na baba. Najua Tanzania ni Lazima kuitwa ubini wa baba au NIMEKOSEA tusaidiane .